STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, December 30, 2011

PICHA KALI YA MWAKA 2011


UTAJAZA MWENYEWE!

NENO LA KUUAGA MWAKA 2011




MUNGU AMETUWEZESHA KUVUKA MILIMA NA MABONDE YA MWAKA 2011 NA HUENDA AKATUJALIA KUMALIZA KILICHOBAKIA NDANI YA MWAKA HUU NA KUKARIBISHA MWAKA MPYA WA 2012. KITU CHA MUHIMU NI KUJIULIZA KIPI TUNACHOWEZA KUMLIPA MUNGU KWA WEMA NA UKARIMU ALIOTUFANYIA KIPINDI CHOTE CHA MAISHA YETU. NADHANI KIKUBWA TUNACHOPASWA KUFANYA NI KUMSHUKURU NA KUZIDI KUMTII NA KUMNYENYEKEA KUSUDI AZIDI KUTUPA MEMA ZAIDI. MICHARAZO MITUPU INAWATAKIA KILA LA HERI KATIKA KUUAGA MWAKA 2011 NA KUUKARIBISHA MWAKA MPYA WA 2012.

Fella aahidi makubwa 2012



MENEJA wa kundi la TMK Wanaume Family, Said Fella amesema mwaka 2011 kwake umekuwa wa mafanikio, ikiwemo kuwakusanya vijana chipukizi 37 aliwatoa mmoja baada ya mwingine katika anga la muziki Tanzania.
Pia, alisema kumiliki studio binafsi na kuliendeleza kundi la TMK Wanaume Family linalokaribia umri wa miaka 10 tangu kuanzishwa kwake na kufyatua albamu katika miondoko ya taarabu ni vitu vingine vinavyomfanya atembee kifua mbele.
Akizungumza na MICHARAZO, Fella alisema kama kuna mwaka uliokuwa wa neema kwake na kujivunia ni huu unaomalizika leo usiku, kutokana na kufanya mambo makubwa yanayomfanya aufurahie.
Alisema kuunda kundi lenye vijana 37 wenye vipaji mbalimbali na kuwasaidia kuwatoa mmoja baada ya mwingine kama alivyofanya kwa Aslay Is'haka 'Dogo Asley', Mugogo anayetamba na kibao cha 'Jicho Chongo' na wengineo.
"Nadhani kwa mwaka 2012 kwa uwezo wa Allah, nitaendelea kuwatoa vijana chipukizi kama nilivyoweza kufanya ndani ya mwaka huu," alisema.
Fella, alisema pamoja na kuendelea kuwatoa chipukizi, mipango yake ni kuona TMK linatamba nchini, huku akifyatua vitu vikali zaidi kupitia studio yake ya Poteza Records na kuupeleka mbele muziki wa kizazi kipya na sanaa kwa ujumla.
"Kuna mengi niliyoyapanga kuyafanya mwaka ujao, lakini cha muhimu ni Mungu kuniwezesha na kunipa afya njema kuyafanikisha, ila lazima nishukuru kwamba 2011 ulikuwa ni mwaka mzuri kwangu," alisema Fella.
Mwisho

Msondo kuuona mwaka Dar



WAKATI wapinzani wao wa jadi wakilikimbia jiji na kwenda kuukaribisha mwaka mpya jijini Mwanza, bendi ya Msondo Ngoma, yenyewe imejichimbia Dar ikiendelea kutambulisha nyimbo mpya zinazoandaliwa kwa albamu ijayo.
Msemaji wa Msondo Ngoma, Rajabu Mhamila 'Super D', alisema bendi yao imeamua kuwapa burudani mashabiki wa Dar kwa kufanya maonyesho yao ya mwishoni mwa wiki katika kumbi zao zilizozoeleka.
Alisema leo bendi yao itafanya mambo yake kwenye ukumbi wa Leaders Club, kabla ya kesho kutambulisha vibao vyao na kuukaribisha mwaka 2012 na mashabiki wao ukumbi wa TCC-Chang'ombe, wilayani Temeke.
"Sie tumeamua kukomaa Dar ambapo kama kawaida leo Ijumaa tupo Leaders Club wilayani Kinondoni, Jumamosi tutakuwa TCC- Chang'ombe kwa mashabiki wa wilaya ya Temeke na Jumapili tunamalizia hasira zetu kwa watu wa Ilala pale DDC Kariakoo," alisema.
Alisema katika maonyesho yote, Msondo watapiga nyimbo zao zote zilizowasambaratisha wapinzani wao, Sikinde katika mpambano wao usio rasmi uliofanyika siku ya Krismasi.
"Tutatumia silaha zetu zote zilizowasambaratisha wapinzani wetu wiki iliyopita, kuanzia Suluhu, Dawa ya Deni, Baba Kibene, Nadhiri ya Mapenzi, hadi nyimbo za albamu zetu za zamani kuanzia enzi za NUTA, JUWATA na OTTU," alisema Super D.

Jinamizi la Talaka lipo Mwanza



BENDI kongwe ya muziki wa dansi ya Mlimani Park 'Sikinde' wanatarajia kuvitambulisha vibao vyao vipya kikiwemo 'Jinamizi la Talaka' kwa mashabiki wao wa jijini Mwanza.
Bendi hiyo iliyoondoka jana jijini Dar es Salaam ikiwa na kikosi chake kamili imeenda kuuaga mwaka 2011 na kuukaribisha mwaka mpya jijini Mwanza kwa kufanya maonyesho mawili.
Katibu Mipango wa bendi hiyo, Hamis Milambo alisema onyesho la kwanza litafanyika kesho kwenye ukumbi wa Villa Park, kabla ya kumalizia burudani yao keshokutwa kwa onyesho jingine ambalo litafanyika CCM Kirumba.
Milambo, alisema katika maonyesho yote watatambulisha nyimbo zao zinazoandaliwa kwa ajili ya albamu yao mpya iliyoanza kurekodiwa itakayokuwa na nyimbo sita.
"Tunaelekea Mwanza kufanya maonyesho mawili kwa ajili ya kuuaga na kuukaribisha mwaka 2012 na mashabiki wetu wa jijini humo, ambapo tutafanya onyesho la kwanza Villa Park na kumalizia CCM Kirumba," alisema Milambo.
Milambo alisema hata hivyo hakuwa na hakika ya onyesho la CCm Kirumba, akidai huenda wakafanya onyesho ukumbi wa ndani ambao watapangiwa na wenyeji wao waliowaalika jijini humo.
Katibu huyo alivitaja vibao vipya vitakavyotambulishwa ni Jinamizi la Talaka, 'Kilio cha Kazi', 'Kinyonga', 'Bundi', 'Samahani' na 'Deni Nitalipa'.
"Hivyo ni baadhi tu, lakini pia tutakumbushia nyimbo zetu za zamani zilizoifanya Sikinde kuwa Mabingwa wa Dansi Tanzania," alisema Milambo.

Big Daddy yafunga mwaka wa Kanumba



MSANII nyota wa fani ya filamu nchini, Steven Kanumba 'The Great', amedai filamu yake mpya ya 'Big Daddy' ndiyo ya kufungua mwaka.
Hata hivyo, Kanumba alisema tayari ameshaandaa kazi nyingine mpya kwa ajili ya kufungua mwaka mpya wa 2012 unaoatarajiwa kusherehekewa keshokutwa.
Kanumba, alisema kama ilivyokuwa filamu za 'This is It', 'Uncle JJ', filamu ya Big Daddy imejaa vunja mbavu, sambamba na kuibua wasanii chipukizi aliowatabiria kutamba baadaye.
"Niliuanza mwaka kwa kutoka na Deception na ninaufunga na Big Daddy, ni moja ya kazi iliyojaa vichekesho na iliyowaibua wasanii chipukizi kama nilivyofanya kazi zangu za nyuma," alisema.
Aliwataja baadhi ya wasanii walioibuliwa ndani ya filamu hiyo ni Jamila Jaylawi na Jalilah Jaylawi, mbali na Cathy Rupia, Abdul Ahmed, Patchou Mwamba na yeye walioishiriki kazi hiyo.
Kanumba alisema, kazi yake mpya inatarajiwa kufahamika mara baada ya mwaka 2012 kuingia, ila alitamba kuwa ni kama kazi zake nyingine ambazo huwafanya mashabiki wa fani hiyo kuumwa wazikosapo kwa namna zinavyoambiliwa.

Villa Squad yajitapa haishuki daraja ng'o!

UONGOZI wa klabu ya soka ya Villa Squad, umesema utajitahidi kadri ya uwezo wao kuhakikisha timu yao haishuki daraja kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara.
Villa iliyorejea ligi kuu msimu huu tangu iliposhuka msimu wa 2008, ndiyo inayoburuza mkia kwenye msimamo wa ligi hiyo ikizibeba timu nyingine 13 na ni moja ya klabu iliyo na hali mbaya kiuchumi kiasi cha kutishia ushiriki wao wa ligi hiyo.
Hata hivyo Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Ramadhani Uledi, alisema licha ya kumaliza duru la kwanza wakiwa hoi, uongozi wao umejipanga kuhakikisha timu hiyo haishuki daraja.
Uledi, alisema kitu cha kwanza walichofanya kuhakikisha Villa haiteremki daraja ni kukipangua kikosi chao cha awali kwa kusajili wachezaji wapya kulingana na mapendekezo ya kocha wao, Habib Kondo na wasaidizi wake.
"Cha pili tunachopanga kwa sasa ni kuhakikisha timu inaandaliwa mapema nma kucheza mechi nyingi za kujipima nguvu, ili kutoa fursa kwa wachezaji kupata uzoefu na kumpa nafasi mwalimu kuona na kurekebisha makosa mapema," alisema.
Uledi alisema kwa namna hiyo wanaamini ni vigumu kwa Villa kuendelea kuwa 'mdebwedo' katika duru la pili la ligi hiyo itakayoanza Januari 21.
"Tunawaahidi wanachama na wadau wa soka wa Kinondoni kwamba Villa Squad haitashuka daraja na tunaomba tuungwe mkono kwa kuisaidia kwa hali na mali, viongozi tupo makini na tumerekebisha mambo yote yaliyotukwaza duru lililopita," alisema.
Timu hiyo yenye maskani yake Magomeni Mapipa, imesajili wachezaji wapya 11 wakiwemo sita waliopata kwa mkopo toka Azam Fc na kuwaondosha kikosi baadhi ya wachezaji walioonekana hawastahiki kuichezea timu hiyo.

Snake Jr apania kulinda rekodi, heshima ya baba yake



BONDIA chipukizi 'asiyepigika', Mohammed Matumla 'Snake Boy Jr', amesema amepania kumsambaratisha mpinzani wake, Cosmas Cheka atakayepigana nae kesho mjini Morogoro ili kulinda heshima ya baba yake, Rashid Matumla 'Snake Man.
Matumla na Cheka wanatarajiwa kuzichapa kesho kwenye uwanja wa Jamhuri, katika pambano lisilo la ubingwa la kumaliza ubishi baina yao, ambapo Mkuu wa Mkoa wa Morogoro, Joel Bendera anatarajiwa kuwa mgeni rasmi.
Akizungumza na MICHARAZO, Matumla alisema kwa namna alivyojiandaa ni wazi atamsambaratisha mpinzani wao licha ya kucheza uwanja wa nyumbani, lengo likiwa ni kulinda hadhi ya baba yake, Rashid Matumla mbele ya ukoo wa akina Cheka.
Matumla, alisema mbali na kutaka kulinda heshima ya baba yake aliyewahi kupigwa na kumpiga Francis Cheka katika mipambano yao, pia anataka kulinda rekodi yake ya kutopigwa na bondia yeyote nchini.
"Naenda Morogoro kuhakikisha namchakaza Cheka ili kulinda heshima ya mdingi (baba), na kulinda rekodi yangu ya kutopigwa katika michezo 10 niliyokwishacheza hadi sasa," alisema Matumla.
Hata hivyo wakati Matumla akijiapiza hivyo, mpinzani wake amenukuliwa na vyombo vya habari kwamba hana hofu dhidi ya pambano hilo kwa kuamini ataibuka na ushindi kuendeleza ubabe wa ukoo wao mbele ya ukoo wa akina Matumla.
Kwa mujibu wa rekodi zilizopo baina ya mabondia hao wawili ni kwamba Matumla ambaye ni mtoto wa bingwa wa zamani wa WBU, amecheza michezo 10 na kushinda saba, huku Cosmas Cheka mdogo wa Francis Cheka amecheza mechi saba na kushinda manne, akipoteza moja na kupata sare mbili.
Kwa mujibu wa waratibu wa pambano hilo, kabla ya Cheka na Matumla kupanda ulingoni mabondia wa kike wenye upinzani wa jadi, Salma Kiogwa wa Morogoro na Asha Ngedere wa Dar watapigana sambamba na mapambano mengine ya utangulizi.

Mwisho

Super D ajivunia mafanikio mwaka 2011



NYOTA wa zamani wa ngumi za kulipwa nchini ambaye kwa sasa ni kocha wa klabu ya mchezo huo ya Ashanti na timu ya mkoa wa Ilala, Rajabu Mhamila 'Super D' amesema anajivunia mafanikio makubwa aliyoyapata ndani ya mwaka 2011.
Akizungumza na MICHARAZO, Super D, ambaye pia ni Msemaji wa bendi kongwe ya Msondo Ngoma, alisema moja ya mafanikio anayojivunia ni kuwaandaa vijana wengi wanaochipukia katika mchezo sambamba na kuwaelimisha wengine kwa njia ya DVD.
Super D, alisema mbali na hilo pia ameweza kushirikiana vema na wadau wa ngumi
pamoja na mapromota mbalimbali wanaoandaa mapambano makubwa kwa kutoa
mchango wake wa vifaa vya ngumi kufanikisha mapambano hayo ndani ya 2011.
"Nashukuru mwaka 2011 umekuwa ni mwaka wa mafanikio kwangu kwa kuridhika namna nilivyojitahidi kuusaidia mchezo wa ngumi kwa kuwaibua vijana wengi sambamba na kuwasaidia wengine kupitia njia ya DVD ninazoandaa," alisema.
DVD hizo zenye mafunzo ya ngumi pamoja na michezo mikubwa iliyowahi kuchezwa na magwiji wa mchezo huo duniani zimekuwa zikiuzwa na kocha huyo kama njia ya kufika kwa haraka mafunzo ya ngumi kwa wadau wengi.
Ndani ya DVD hizo zinawajumuisha wakali kama Floyd Mayweather, Manny Paquaio, Amir Khan, Muhammed Ali, Mike 'Iron' Tyson, David Haye na wengine ikiwemo na matukio ya mazoezi yao kabla ya mapambano waliyocheza.
Super D, alisema kwa mwaka 2012 panapo majaliwa amepania kuendeleza aliyoyafanya mwaka huu katika kuwainua na kuwaendeleza chipukizi aliowaibua kama akina Shomar Mirundi, Ibrahim Class na Salum Ubwa ili watambe kimataifa.
Chipukizi hao wa klabu ya Ashanti wamekuwa wakifanya vema katika michezo yao, ikiwemo wiki iliyopita Ubwa kumtwanga kwa pointi 60-57 Mustapha Dotto katika pambano lililosindikiza mpambano wa Maneno Oswald na Rashid Matumla.

Mwisho

Kazimoto atajwa mrithi wa Gagarino





KIUNGO mahiri wa klabu ya soka ya Simba, Mwinyi Kazimoto ametajwa kuwa ndiye mrithi wa kiungo nyota wa zamani aliyewahi kutamba nchini na timu za Simba na Yanga, Hamis Gaga 'Gagarino' kwa namna ya uchezaji wake.
Beki wa zamani wa kimataifa wa Tanzania, Willy Martin 'Gari Kubwa', ndiye aliyemtawaza Kazimoto kurithi mikoba ya Gagarino ambaye kwa sasa ni marehemu.
Martin, alisema kwa namna ya uchezaji wake kuanzia umiliki wa mipira, kugawa vyumba na kuburudisha uwanjani, Kazimoto ndiye haswa anayeonekana kufuata nyayo za Gagarino.
Hata hivyo Martin, aliyewaji kuzichezea timu za Simba, Yanga na Taifa Stars, alisema Kazimoto, amekuwa akishindwa kuonyesha makali yake kutokana na kuwa majeruhi mara kwa mara.
"Ukitaka nikuambie ni mchezaji gani ambaye anafuata nyayo za nyota wa zamani ambao walikuwa wakiwatendea haki watazamaji uwanjani, basi ni Mwinyi Kazimto kwani kwa uchezaji wake hana tofauti kabisa na Gagarino," alisema Martin.
Beki huyo aliyewahi kuzichezea pia timu za Majimaji-Songea na Bandari-Mtwara, alisema kwa yeyote anayependa burudani na ufundi dimbani basi kwa Kazimoto kila kitu kipo kama alivyokuwa marehemu Gagarino kiungo mahiri kuwahi kutokea nchini.
Martin, alisema anaamini Kazimoto asingekuwa akisumbuliwa na majeraha huenda angeibeba Tanzania katika kikosi cha timu ya taifa, Taifa Stars na klabu anazochezea.
Mwinyi Kazimoto alitua Simba msimu huu akitokea JKT Ruvu, ambapo amekuwa akitajwa kuwa mmoja wa viungo bora kwa namna ya 'ufundi' aliokuwa nao na amewahi kuitwa Stars mara kadhaa kabla ya kuenguliwa kutokana na kuwa majeruhi.

Mwisho

Moro Utd waanza kujifua, kuanza kambi Jan 10

WAKATI uongozi wa Moro United ulitangaza kuwa, kambi rasmi ya timu hiyo kujiandaa na duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara itaanza rasmi Janauri 10, jumla ya wachezaji 20 wa timu hiyo wakijitokeza siku ya kwanza ya mazoezi ya klabu hiyo.
Mazoezi hayo ya Moro United yalianza jana asubuhi eneo la Tabata Segerea, jijini Dar es Salaam, tayari kwa maandalizi hayo ya ligi kuu itakayoendelea tena Januari 21.
Katika mazoezi hayo ni wachezaji sita tu ndio waliokosekana kutokana na sababu mbalimbali na kuufanya uongozi wa klabu hiyo kufurahia mahudhurio ya nyota wake hao waliojitoeza kuanza kujifua hiyo jana.
Katibu Mkuu wa Moro United, Hamza Abdallah 'Mido' aliiambia MICHARAZO kuwa, kujitokeza kwa wachezaji 20 katika siku ya kwanza ya mazoezi yao ni muitikio mzuri na imani nyota wao sita waliokosekana watajumuika kadri siku zinazoendelea.
Wachezaji waliokosekana kwenye mazoezi hayo ni pamoja na kipa Jackson Chove, George Mkoba, Steohen Marashi, Sadick Gawaza na Gideon Sepo.
Katibu huyo aliongeza kuwa mazoezi ya timu hiyo yataendelea kila siku asubuhi hadi Januari 10 wakati timu hiyo itapoingia rasmi kambini sambamba na kuanza kucheza mechi za kirafiki za kujipima nguvu na timu watakazokubaliana nazo.
"Kambi rasmi ya timu yetu itaanza Januari 10, kwa sasa wachezaji watakuwa wakitokea majumbani kuja mazoezini kila siku jioni, wiki mbili baadae ndipo kikosi chetu kitaanza kucheza mechi za kirafiki za kujiweka tayari kwa ligi hiyo," alisema Abdallah.
Abdallah alisema wanatarajia kucheza mechi tatu za kujipima nguvu na timu za Ligi Kuu Tanzania Bara, ingawa hakuweza kuzitaja majina yake kwa madai ni mapema mno.
Moro United ni miongoni mwa timu nne zilizopanda daraja msimu huu zikitokea Ligi Daraja la Kwanza. Nyingine ni Villa Squad, Coastal Union na JKT Oljoro.

Mwisho

Matumla alilia ushindi kwa Maneno, mratibu ampuuza




BINGWA wa zamani wa Dunia wa Ngumi za Kulipwa, Rashid Matumla 'Snake Man', ameibuka na kudai alistahili kuwa mshindi wa pambano lake dhidi ya Maneno Oswald 'Mtambo wa Gongo' lililofanyika Desemba 25 jijini Dar es Salaam.
Pia bondia huyo amewalalamikia waandaaji wa mchezo huo kwa madai ulingo ulikuwa una utelezi, kiasi cha kumfanya aanguke mara kadhaa na kupelekea kuumia mkono na mguu.
Katika pambano hilo lililofanyika kwenye ukumbi wa Heinkein Pub, Mtoni Kijichi, Matumla na Maneno walishindwa kutambiana baada ya kutangazwa wametoka sare kwa kupata pointi 99-99, kitu ambacho Maneno alikipinga akidai alistahili yeye ushindi.
Hata hivyo, Matumla naye ameibuka na kudai yeye alistahili kutangazwa mshindi kwa namna alivyocheza na kumdhibiti mpinzani wake aliyekiri ni mmoja wa mabondia wazuri nchini.
"Kwa kweli licha ya kwamba mwamuzi na majaji ndio watu wa mwisho katika maamuzi na kukubaliana na maamuzi ya kutangaza droo baina yangu na Maneno, lakini naamini nilistahili kuwa mshindi kwa jinsi nilivyocheza," alisema Matumla.
Matumla, alisema hata baadhi ya mashabiki waliofurika kwenye ukumbi huo walikuwa wakilalamikia droo iliyotangazwa kitu kinachoonyesha mechi ile haikustahili kuwa hivyo.
Pia, alisema kuanguka kwake mara kwa mara ulingoni kulitokana na ulingo kuwa na utelezi na kutoa ushauri wa waandaaji wa ngumi wawe wakiepuka vitu kama hivyo ili kusaidia kufanya mabondia waonyeshe uwezo wao na kuwapa burudani mashabiki.
"Waandaaji wawe makini na maandalizi ya michezo yao, wajaribu kuandaa ulingo wenye ubora sio kama ilivyotokea katika pambano letu ambapo kulikuwa na utelezi na kusababisha niumie mkono na miguu kwa kuanguka wakati wa mchezo,"alisema.
Muandaaji wa pambano hilo, Shaaban Adios 'Mwayamwaya' ameyapinga madai ya Matumla kwa ulingoni ulikuwa na utelezi kwa kudai kuwa ulingo huo kwa miaka mingi ndio 'Snake Man' amekuwa akiutumia kuwapiga wapinzani wake.
Adios alisema ulingo huo uliletwa na DJB Promotion, ambao ndio waliowakodisha na juu ya kuanguka kwa Matumla, alisema alimueleza viatu vyake vilikuwa vimelika 'kashata'.
"Kama ulingo ulikuwa unateleza mbona Maneno hakuwa akianguka, pia ndio ulingoni mkubwa na wenye ubora wa hali ya juu kati ya ulingo zote nchini na ambao Matumla amekuwa akiutumia kuwapiga wapinzani wake," alisema Adios.

Mwisho

Tuesday, December 27, 2011

Kingwande 'aitabiria' mema Lyon duru la pili

KIUNGO Mshambuliaji nyota wa timu ya African Lyon, Adam Kingwande, amesema ana matumaini makubwa kwa timu yake kufanya vema katika duru lijalo la Ligi Kuu Tanzania Bara kutokana na kusajiliwa kwa wchezaji kadhaa wapya katika kikosi chao.
Akizungumza na MICHARAZO, Kingwande, aliyewahi kuzichezea timu za Ashanti Utd na Simba, alisema usajili uliofanywa kupitia dirisha dogo lililomalizika mwezi uliopita kwa namna moja utaisaidia timu yao kufanye vema kwenye duru hilo lijalo.
Kingwande, alisema awali kikosi chao kilikuwa na mapungufu makubwa ambayo yaliifanya Lyon iyumbe kwenye duru la kwanza, jambo ambalo lilionwa na kufanyiwa kazi na uongozi na benchi la ufundi lao la ufundi kwa kusajiliwa wachezaji hao wapya.
Alisema kwa namna usajili huo uliofanyika kwa kuchanganya wachezaji wa ndani na nje ya nchi ni wazi Lyon, itakuwa moto wa kuotea mbali katika duru lijalo, kitu alichotaka timu pinzani zikae chonjo dhidi yao.
"Binafsi naamini Lyon itakuwa moto duru lijalo kutokana na kuongezwa wachezaji wapya kupitia dirisha dogo, pia, nashukuru kwamba kwa sasa nipo fiti tukianza maandalizi ya duru hilo," alisema.
Lyon inayoshiriki Ligi Kuu Tanzania Bara kwa msimu wa tatu sasa, ilianza vema duru la kwanza kabla ya kutetereka ikimaliza duru hilo ikiwa nafasi ya tisa katika msimamo wa ligi hiyo kwa kujikusanyia jumla ya pointi 14.
Msimamo wa ligi hiyo unaongozwa na Simba yenye pointi 28 ikifuatiwa na Yanga yenye piinti 27 na Azam waliona pointi 23 sawa na JKT Oljoro wanaoshika nafasi ya nne.

Mwisho

Kocha Papic 'aivua' nguo Yanga, Niyonzima mh!




KOCHA Kostadian Papic wa Yanga amefichua ubabaishaji mkubwa uliopo katika klabu yake na kuonya kuwa kamwe asitafutwe mchawi pindi watakapoboronga kwani hadi sasa hakuna maandalizi yoyote ya maana waliyoanza kuyafanya kwa ajili ya mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Bara na pia kwa mechi yao ya kwanza ya Ligi ya Klabu Bingwa Afrika dhidi ya Zamalek ya Misri.
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam, Papic maarufu kama 'Clinton' alisema, hali ngumu ya maisha klabuni hapo ni tatizo kwani wachezaji wake hawahakikishiwi maslahi yao kwa wakati na hadi sasa wanashindwa hata kupata chakula cha uhakika.
Papic alisema kuwa kukosa fedha kumeifanya timu hiyo kushindwa kufanya mazoezi kwa siku saba sasa kwavile hawana hata fedha za kukodisha uwanja wa kufanyia mazoezi.
"Kwa hali hii ya ukata, siwezi kuahidi matokeo mazuri kwa mashabiki wetu... ukweli ni kwamba hivi sasa wachezaji wamepoteza morari ya mazoezi kwa kukosa fedha zao na chakula. Hali hii inasikitisha kwa sababu hivi sasa tunashindwa hata kwenda gym kwa kukosa fedha," alisema Papic.
"Wanayanga wasije wakawalaumu wachezaji au kocha wakati watakapoona timu inafanya vibaya. Pengine si habari nzuri, lakini hiyo ndio hali halisi klabuni," aliongeza Papic.
Papic alisema kuwa kutokana na hali mbaya waliyo nayo kifedha, sasa anakosa nguvu ya kuwabana wachezaji wake kufanya mazoezi kwa kuwa anafahamu hali ngumu wanayokabiliana nayo.
Ppic alianika zaidi udhaifu mwingine klabuni kwao kuwa ni wamawasiliano duni kati ya benchi la ufundi na uongozi wa klabu hiyo.
Kuhusiana na maslahi yake, Papic alisema kuwa mambo mengi waliyokubaliana awali na uongozi kwenye mkataba wao hayajatekelezwa na hivyo hata yeye anakabiliwa na wakati mgumu.
Katika hatua nyingine, Papic alisema kuwa pamoja na timu hiyo kuwa mbioni kushiriki mashindano ya Kombe la Mapinduzi (visiwani Zanzibar), hadi sasa bado hajapewa taarifa rasmi za kuandaa timu yake kwa ajili ya mashindano hayo.
"Sifahamu chochote kuhusu mashindano hayo... nasikia juu juu tu," alisema Papic.
Papic alisema kuwa wametuma majina ya wachezaji 28 kwa Shirikisho la Soka la Afrika (CAF) kwa ajili ya klabu bingwa Afrika, lakini amemtema kiungo Rashidi Gumbo kwa maelezo mafupi kuwa mchezaji huyo hayupo tayari kwa mashindano hayo.
Papic alisema vilevile kuwa baada ya ratiba iliyotolewa na CAF kuonyesha kuwa watacheza dhidi ya Zamalek, aliomba kupatiwa mikanda ya video ya timu hiyo ili iwasaidie katika maandalizi yao lakini hadi sasa hawajaipata kutokanan na sababu ileile ya uklata inayokwamisha pia harakati nyingine za maandalizi ya kikosi chake.
"Inatakiwa dola za Marekani 10,000 ili kuipata mikanda niliyokuwa nikiitaka... jambo hili hadi sasa limeshindikana," alisema Papic.
Kuhusiana na kiungo wao wa kimataifa kutoka Rwanda, Haruna Niyonzima, ambaye hajaripoti hadi sasa tangu alipomaliza mapumziko waliyopewa baada ya kumalizika kwa michuano ya Kombe la Chalenji, Papic alisema kuwa atamuadhibu ili fundisho kwa wengine.
"Mara kwa mara amekuwa akitoa visingizio kuwa ana matatizo ya hati yake ya kusafiria.. nitamwadhibu na kumkata mshahara wake ili iwe fundisho kwa wachezaji wengine," alisema Papic.
Hata hivyo uongozi wa Yanga ulipoulizwa juu ya madai hayo ya Papic, Afisa Habari wa klabu hiyo, Louis Sendeu, alisema kuwa hawezi kuzungumzia chochote kuhusiana na suala hilo kwa kuwa ni la kiutendaji.
“Hilo suala ni kubwa kwangu. Ni la kiutawala zaidi na hivyo naomba mumtafute katibu au mwenyekiti. Wao ndio wanaoweza kuwajibu,’ alisema Sendeu.
Pia Sendeu alidai kushangazwa na kocha wao kukimbilia kwenye vyombo vya habari wakati angeweza kutoa malalamiko yake kwa uongozi ili kumaliza tatizo.
Naye Katibu wa Yanga, Celestine Mwesigwa, alijibu kwa kifupi kuwa watatoa ufafanuzi juu ya taarifa za kocha wao, ambazo ni kama kuwavua nguo mbele ya wadau wa soka.

Villa kuchagua mwenyekiti Februari

UCHAGUZI mdogo wa klabu ya soka ya Villa Squad ya jijini Dar es Salaam kuziba nafasi ya Mwenyekiti na wajumbe wa Kamati ya Utendaji unatarajiwa kufanyika mwezi Februari.
Makamu Mwenyekiti wa Villa, Ramadhan Uledi, aliiambia MICHARAZO kuwa, uchaguzi huo mdogo utafanyika mwanzoni mwa Februari mara baada ya duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara kuchanganya kasi.
Uledi, alisema mwezi ujao kupitia kamati yao ya uchaguzi itatangaza taratibu za uchaguzi huo, ili kufanyika kwake na kuikamilisha safu ya uongozi wa klabu yao.
"Uchaguzi mdogo wa kumpata mwenyekiti na wajumbe wawili wa kamati ya utendaji utafanyika mara baada ya duru la pili la ligi kuu kuanza, nadhani itakuwa mapema Februari mwakani," alisema Uledi.
Aliongeza, kwamba wangeweza kuitisha mapema uchaguzi huo hata sasa, lakini hali mbaya ya ukata waliyonayo na maandalizi ya ligi inayowakabili ndio maana wameona wavute muda hadi baadae huku akisisitiza ni lazima ufanyike katika muda huo.
Mbali na kuwahimiza wanachama wa klabu hiyo kuanza kukaa mkao wa kula kujitokeza kuwania nafasi hizo, ambazo zilishindwa kuwapata washindi wake kwenye uchaguzi mkuu uliofanyika Juni, mwaka huu pia aliwataka wajitokeza kuichangia Villa.
"Wanachama na wadau wa Villa wasaidie kuichangia timu yao kwa ajili ya ushiriki wa duru lijalo, sambamba na kujiweka tayari kuziba nafasi hizo zilizo wazi kwenye uchaguzi huo mdogo," alisema.
Villa ilishindwa kumpata Mwenyekiti wakati wa uchaguzi wake mkuu, kufuatia Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, kumuengua aliyekuwa mgombea pekee wa nafasi hiyo, Abdallah Majura Bulembo kwa kilichoelezwa kukosa sifa stahiki.

Mwisho

Toto Afrika kuwavaa Wanigeria Mwanza na Shinyanga

TIMU ya soka ya Toto Afrika ya Mwanza jioni ya leo inatarajiwa kushuka dimba la CCM Kirumba, jijini humo kupepetana na wageni wao Abuja FC ya Nigeria katika pambano la kirafiki la kimataifa la kujiandaa na duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara.
Pambano hilo la Mwanza ni kati ya mechi mbili zitakazochezwa baina ya timu hizo mbili ambazo zimeanzisha ushirikiano wa pamoja.
Kwa mujibu wa Katibu Mipango wa Toto, Hassani Kiraka, pambano jingine la timu hizo mbili litachezwa kesho kwenye dimba la Kambarage, mkoani Shinyanga.
Kiraka alisema, mbali na mechi hizo mbili kutumiwa na timu yao kukiandaa kikosi chao kwa ajili ya duru la pili litakaloanza Januari 21, pia zitatumiwa kukusanya fedha kwa za kuiwezesha Toto kushiriki vema ligi hiyo kutokana na kuwa na hali mbaya kiuchumi.
"Tunawahimiza mashabiki wa soka wa jijini Mwanza na Shinyanga ambao kwa muda mrefu hawajapata burudani ya kimataifa kujitokeza kwa wingi katika mechi hizo ikiwa sehemu yao ya kuichangia timu yetu, ili ishiriki vema katika duru lijalo," alisema Kiraka.
Alisema, uongozi wao umepania kuona Toto Afrika katika duru la pili, ikifanya vema tofauti na ilivyokuwa duru lililopita kwa nia ya kuiokoa timu yao isishuke daraja, ndio maana wameialika Abuja Fc ambayo wameanzisha ushirikiano wa pamoja baina yao.
Aliongeza, katika mechi hizo mbili benchi la ufundi la Toto lililopo chini ya John Tegete na msaidizi wake, Choki Abeid, watatafuta wachezaji wanne kutoka kikosi cha Abuja Fc, ili ikiwezekana mwakani wawasajili katika timu yao.
Toto iliyoanza duru la kwanza kwa makeke kabla ya kutetereka na kumaliza mzunguko huo ikiwa nafasi ya 11 katika msimamo wa ligi, katika kikosi chake inao nyota wawili wa Kinigeria, akiwemo kinara wao wa mabao, Enyima Darlington na Chika Chimaobi Chukwu.

Mwisho

Simba, Yanga zaumwa sikio



BEKI wa zamani wa timu za Ushirika-Moshi, Simba na Yanga, Willy Martin 'Gari Kubwa', amezitaka klabu za Simba na Yanga na kufanya maandalizi kwa vitendo badala ya maneno ili kujiandaa na mechi za kimataifa mwakani.
Aidha amelitaka Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, kumsaidia kocha Jan Poulsen wa Taifa Stars kuitafutia timu mechi za kutosha za kimataifa kabla ya kushiriki wa mechi za kuwania Fainali za Afrika za 2013 na Kombe la Dunia la 2014.
Akizungumza kwenye mahojiano maalum, Gari Kubwa, alisema ili Simba na Yanga ziweze kufanya vema katika mechi zake za Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho ni lazima zijipange vya kutosha badala ya kupiga 'blabla' huku muda ukienda.
Gari Kubwa, aliyewahi kuzichezea pia timu ya Majimaji-Songea, Bandari-Mtwara na Taifa Stars kwa nyakati tofauti, alisema maandalizi ya kutosha na kupata mechi nyingi za kirafiki za kimataifa zinaweza kuzibeba Simba na Yanga mwakani.
Alisema kinyume cha hapo ni kwamba timu hizo zisubiri kung'olewa mapema kama ilivyozoeleka na kuishia kutoa visingizio visivyo na maana.
"Naamini Simba na Yanga zikijipanga vema zinaweza kufanya vizuri katika uwakilishi wao, lakini zikiendelea kupiga blabla wakati muda ukizidi kwenda basi watarajie kuendelea kuwasononesha mashabiki wao kwa kung'olewa mapema," alisema.
Aidha, alilishauri Shirikisho la Soka nchini, TFF, kuanza maandalizi ya kuitafutia mechi za kirafiki za kimataifa, timu ya taifa, Taifa Stars, ili ijiweke vema kabla ya kukabiliana na wapinzani wao katika kuwania Fainali za Afrika na zile za Dunia.
Alisema amegundua Kocha Mkuu, Jan Poulsen amekuwa na wakati mgumu kwa matokeo mabaya ya timu yake kwa makosa yanayofanywa na TFF kwa kutoitafutia Stars mechi za kutosha kumpa nafasi kocha kurekebisha makosa.
"TFF lazima ibadilike na kuitafutia Stars mechi nyingi za kimataifa mapema, ili kumsaidia Poulsen, ni vigumu timu kufanya vema kama haipati mechi za maana za kujipima nguvu kabla ya kuingia kwenye ushindani," alisema.
Stars imepangwa kundi C katika makundi ya kuwania Fainali za Dunia zitakazofanyika Brazil, huku pia ikiwa na kibarua cha kuumana na Msumbiji katika mechi za mchujo za kuingia makundi ya kufuzu Fainali za Afrika 2013 zitakazochezwa nchini Afrika Kusini.

mwisho

Mchaki 'aula' VIlla Squad

KLABU ya soka ya Villa Squad, imemteua aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama cha Soka wilaya ya Kinondoni, KIFA, Frank Mchaki kuwa Kaimu Katibu Mkuu baada ya Katibu Mkuu wao, Idd Godigodi kuwa mgonjwa.
Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Ramadhani Uledi, aliiambia MICHARAZO kuwa, wamelazimika kumuomba Mchaki awashikie nafasi hiyo ya Ukatibu kuitokana na Katibu wao kuwa mgonjwa na huku wakikabiliwa na majukumu kabla ya kuanza kwa ligi.
Uledi, alisema kamati yao ya utendaji ililazimika kuhitisha kikao cha dharura na kufanya maamuzi hayo, kwa nia ya kuifanya Villa isitetereke wakati ikijiandaa na duru la pili la Ligi Kuu Tanzania bara litakaloanza Januari 21.
"Tumemundikia barua kumuomba akaimu ukatibu mkuu, kutokana na uzoefu alionao na ametukubalia kwani kabla ya uteuzi alikuwa ndiye Katibu wa Kamati ya Usajili ya klabu yetu ambayo alifanya kazi nzuri kwa kuimarisha kikosi," alisema Uledi.
MICHARAZO iliwasiliana na Mchaki, ambaye alikiri kuombwa na uongozi wa klabu hiyo kushikilia cheo hicho na kudai haoni sababu ya kuikataa ilihali ni mmoja wa wadau wakubwa wa klabu hiyo.
"Ni kweli kuhusu jambo hilo na nimeshawajibu kuafiki uteuzi huo na kuwahidi wana Villa wanipe ushirikiano kuiwezesha timu yetu ifanye vema kwenye ligi hiyo na kuondokanan na janga la kushuka daraja pamoja na ukata uliopitiliza," alisema.
Villa Squad iliyorejea Ligi Kuu msimu huu, ndiyo inayoshikilia mkia katika msimamo wa ligi hiyo yenye timu 14.

Mwisho

Maneno, Matumla washindwa kutambiana





MABONDIA wakongwe wa ngumi za kulipwa nchini, Maneno Oswald 'Mtambo wa Gongo' na Rashid Matumla 'Snake Man' juzi walishindwa kutambiana baada ya pambano lao la kumaliza ubishi kuisha kwa kutoka sare.
Hata hivyo Oswald, ameyakubali matokeo hayo kwa ushingo upande, akidai kwamba alistahili kutangazwa mshindi kutokana na kumzidi maarifa mpinzani wake aliyeteleza na kuanguka ulingoni mara sita na kujikuta akiumia mguu.
Pambano hilo lisilo la ubingwa lililokuwa na raundi 10 na uzani wa kati lililosimamiwa na Shirikisho la Ngumi za Kulipwa Nchini, PST, lilifanyika kwenye ukumbi wa Heinken Pub, Mtoni Kijichi nje kidogo ya jiji la Dar es Salaam.
Katika pambano hilo lililochezeshwa na mwamuzi wa kimataifa wa mchezo huo nchini, Anthony Rutta, mabondia wote wawili walipewa pointi 99-99, kitu ambacho Maneno Oswald aliiambia MICHARAZO kuwa ni kama mpinzani wake 'alibebwa' tu.
"Kwa kweli nimeyakubali matokeo hayo kwa shingo upande kwa vile nilistahili kabisa ushindi, ila mpinzani wangu amelindwa, Matumla kaanguka mara sita ulingoni, utetezi wake ulingo ulikuwa unateleza mbona mie sikuteleza," alisema Maneno.
Aliongeza kuwa, licha ya kuambiwa kuna mipango inafanywa ili warudiane tena, yeye binafsi hana mpango wa kufanya hivyo na kudai anataka kupigana na Mada Maugo, aliyedai ndiye anayemuona mpinzani wake wa ukweli.
"Sitarudiana na Matumla hata iweje, nataka kupigana na Maugo kwani namuona ndiye bondia wa kweli kwa sasa nchini katika uzito wetu.," alisema.
MICHARAZO lilijaribu kumsaka Matumla kusikia kauli yake juu ya matokeo ya mchezo huo, lakini simu yake haikuwa hewani.
Hilo lilikuwa ni pambano la nne kwa Maneno na Matumla kuzipiga, kwani walishacheza mechi tatu na mara mbili Matumla aliibuka na ushindi dhidi ya moja la mpinzani wake.
Katika mechi nyingine za utangulizi zilizochezwa kabla ya pambano la wawili, Ubwa
Kabla ya pambano hilo kuchezwa kulifanyika mechi kadhaa za utangulizi, ambapo moja wao lilimkutanisha bondia Ubwa Salum aliyempiga kwa pointi Mustafa Dotto.

Friday, December 2, 2011

Zanzibar mguu ndani mguu nje Kombe la Chalenji 2011



HATMA ya timu ya taifa ya Zanzibar, Zanzibar Heroes kuendelea na michuano ya Kombe la Chalenji, inasubiri majaliwa ya sheria ya kumpata best losser, kufuatia goli la Amissi Cedric lililo wapa ushindi Burundi wa goli 1-0 pala walipowakabili Uganda jana.
Zanzibar ilipata ushindi wake wa kwanza kwenye michuano hiyo inayoendelea jijini jana katika pambano lililochezwa mapema kwenye uwanja wa Taifa kwa kuilazaq Somalia mabao 3-0 na kufikisha pointi nne.
Mabao ya mshambuliaji wao hatari Suleiman Kassim 'Selembe', Ally Badru na nahodha Aggrey Morris yaliisaidia Zanzibar kujiweka katika nafasi nzuri ya kusonga mbele kutegemeana na matokeo ya makundi mengine yanayochezwa leo na kesho.
Kama mambo yatajipa Zanzibar waliopo nafasi ya tatu katika kundi lao la B nyuma ya Burundi wanaoongoza kwa pointi 7 na Uganda wenye pointi sita itafuzu hatua ya robo fainali.
Kwani kama sio ushindi wa bao 1-0 iliyopata Burundi mbele ya Uganda, Zanzibar isingekuwa na wakati mgumu wa kusubiri kapu la hisani kusonga mbele.
Zanzibar itabidi wangoje hekima za CECAFA kama watapata nafasi katika best loser ingawa kwa kuangalia matokeo ya makundi mengine yalivyo moja ya nafasi ya mshindwa bora kwa 'mashujaa' hao wa Zanzibar ni kubwa, ingawa soka halipo hivyo.
Ndugu zao Tanzania kesho nao watakuwa vitani kupigana kutinga robo fainali, kwa kuumana na Zimbabwe wanaolingana nao pointi tatu, huku Rwanda amabyo itacheza leo dhidi ya Djibout ikiwa imeshajihakikishia nafasi mojawapo ya kucheza hatua hiyo ya mtoani itakayoanza Jumatatu.

TMK kuumwa Kichwa Dar mpaka Mwanza



BAADA ya kimya cha miaka mitatu, kundi la muziki wa kizazi kipya la TMK Wanaume Family, limefyatua wimbo na video mpya iitwayo 'Kichwa Kinauma' itakayotambulishwa katika maonyesho maalum jijini Dar na Mwanza.
Kibao hicho kipya kilichorekodiwa 'audio' yake katika studio za MJ Records na video kutolewa na kampuni ya Visual Lab, inatarajiwa kusambazwa kwenye vituo vya redio na runinga wiki hii na kufuatiwa na maonyesho katika majiji hayo.
Meneja wa kundi hilo, Said Fella 'Mkubwa Fella' aliliambia MICHARAZO kuwa, kazi hiyo mpya itatambulishwa kwa wakazi wa Dar katika onyesho litakalofanyika Jumapili ya Desemba 4 kwenye ukumbi wa Maisha Club na kisha kuvaamia Mwanza Desemba 9.
Fella alisema wakiwa jijini Mwanza, kudni lao litakitambulisha kibao hicho na nyimbo nyingine binafsi za wasanii wa TMK Wanaume Family, kwenye ukumbi wa Villa Park.
"Mkubwa tumefyatua kibao kipya na video yake iitwayo Kichwa Kinauma ikiwa ni baada ya ukimya wa miaka mitatu tangu tutoe kazi ya mwisho na tutaitambulisha rasmi kwa mashabiki wetu katika miji ya Dar na Mwanza," alisema.
Fella aliongeza katika maonyesho hayo mawili ya jijini Dar na Mwanza, pia wataonyesha 'trela' la filamu ya kundi hilo ili kuwapa kionjo tu mashabiki wao kabla ya filamu hiyo kuingizwa sokoni katikati ya mwezi ujao.
"Unajua tumefyatua filamu inayohusiana na kundi letu, hivyo katika maonyesho hayo mawili ya utambulisho wa 'Kichwa Kinauma', pia tutaonyesha trela la filamu hiyo ambayo tutaitoa hadharani katikati ya Desemba," alisema Fella.
Kundi hilo la TMK Wanaume Family, linaundwa na wasanii kadhaa nyota wakiwemo Mhe Temba, Said Chegge, Dogo Aslay anayetamba na wimbo wa 'Nakusemea' na wengineo.

Sikinde yajiandaa kukamilisha albmu mpya

BENDI kongwe ya Mlimani Park 'Sikinde' ipo katika maandalizi ya mwisho ya kufyatua albamu yao mpya itakayozinduliwa mwishoni mwa mwezi ujao.
Katibu wa bendi hiyo, Hamis Milambo, alisema kuwa tayari wameshafyatua vibao kadhaa kwa ajili ya albamu hiyo itakayokuwa na nyimbo sita na watamalizia nyimbo zilizosalia kabla ya katikati ya Desemba.
Milambo, alisema katika harakati za kuitambulisha albamu hiyo wamefyatua video ya kibao chao cha 'Jinamizi la Talaka' ambao unatesa kwenye vituo kadhaa vya redio nchini.
"Sikinde tupo katika maandalizi ya kukamilisha kurekodi albamu yetu mpya itakayokuwa na nyimbo sita, ambayo tutaitoa hadharani mwishoni mwa Desemba," alisema.
Katibu huyo alivitaja baadhi ya vibao vitakavyokuwa katika albamu hiyo itakayochukua nafasi ya 'Supu Imetiwa Nazi' kuwa ni; 'Jinamizi la Talaka', 'Bundi', 'Mihangaiko ya Kazi' na 'Asali na Shubiri'.
Sikinde, kwa muda wa miaka miwili sasa haijatoa albamu yoyote tangu ilipotamba na Supu Imetiwa Nazi ambayo ilifyatuliwa wakati ikiwa chini ya Shirika na Maendeleo Dar es Salaam, DDC iliyowatema rasmi mapema mwaka uliopita.

Poulsen bado hajaniamini-Jabu




BEKI mahiri wa Simba anayezichezea pia timu za taifa, Juma Jabu, amekiri kwamba kocha wa sasa wa timu ya taifa (Taifa Stars), Jan Poulsen hajamuamini ndiyo maana amekuwa haitwi mara kwa mara katika kikosi hicho.
Hata hivyo, alisema kutoaminiwa huko kunatokana na kuwepo majeruhi kwa muda mrefu tangu Mdenmark huyo alipoitwaa timu hiyo toka kwa Mbrazil, Marcio Maximo.
Jabu maarufu kama 'JJ', alisema amekuwa akipata nafasi ndogo ndani ya kikosi cha Stars kwa vile Poulsen hajaridhika naye, tofauti na ilivyo kwa Maximo ambapo panga pangua hakukosekana kikosini.
"Sio siri sijapata nafasi kubwa ndani ya kikosi cha Stars tangu iwe chini ya Poulsen, hii inatokana na kocha kutoniamini pengine kwa vile nilikuwa majeruhi na hivyo kutoonekana dimbani, ila naamini michuano ya Chalenji itanirejesha Stars," alisema.
Alisema kuitwa kwake katika kikosi cha Kilimanjaro Stars ambayo leo inamaliza mechi zake za makundi dhidi ya Zimbambwe, ni fursa nzuri ya kumshawishi Poulsen ampe nafasi ya kudumu katika Stars inayokabiliwa na mechi za kuwania kufuzu CAN 2013 na WC 2014.
Katika hatua nyingine beki huyo alisema mipango yake ya kwenda kucheza soka la kulipwa nchini Afrika Kusini inaendelea vema, ingawa hakupenda kuweka bayana kwa madai suala lake linasimamiwa na wakala wake.
"Mipango yangu ya kwenda Afrika Kusini ipo pazuri, ila mwenye nafasi ya kuliongelea kwa undani ni wakala wangu," alisema Jabu.

Mkenya Kariuki kutua nchini Kesho kupiogana na Nassib Ramadhan



MPINZANI wa Bingwa wa Dunia anayetambuliwa na World Boxing Forum, Nassib Ramadhan 'Manny Pacquiao', Mkenya Anthony Kariuki, anatarajia kutua nchini kesho kwa pambano lao litakalofanyika Desemba 9 jijini Dar es Salaam.
Kariuki na Nassib watapigana katika pambano lisilo la ubingwa la raundi 10 uzani wa Fly kwenye ukumbi wa DDC Keko, ambapo watasindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi.
Akizungumza na MICHARAZO, mratibu wa pambano hilo, Pius Agathon, alisema Kariuki atatua nchini leo mchana akiambatana na kocha wake tayari kwa pambano lake ambalo litaenda sambamba na maadhimisho ya Miaka 50 ya Uhuru.Agathon, alisema kambi ya Mkenya huyo itakuwa eneo la Keko, wakati mpinzani wake ipo eneo la Mabibo chini ya kocha wake, Christopher Mzazi.
"Mkenya atakayepigana na Nassib Ramadhan atatua nchini Jumamosi (kesho)na moja kwa moja ataingia kambini eneo la Keko, tayari kuvaana na mpinzani wake aliyejichimbia Mabibo," alisema Agathon.
Agathon aliongeza kuwa maandalizi kwa ujumla ya pambano hilo litakalohudhuriwa pia na nyota wa zamani wa mchezo huo walioliletea sifa Tanzania katika miaka 50 ya Uhuru yamekamilika na inasubiriwa siku ya kufanyika kwa mchezo huo.
Alisema siku hiyo kutakuwa na michezo mitano ya utangulizi kabla ya Nassib Ramadhan kupeperusha bendera ya Tanzania mbele ya Mkenya.

BREAKING NEWS: Mr Ebbo hatunaye



Taarifa zilizotufikia muda huu zinasema kwamba aliyekuwa msanii wa muziki wa kizazi kipya, Abel Loshilaa Motika 'Mr Ebbo' amefariki alfajiri ya leo na anatarajiwa kuzikwa huko kwao Arusha siku ya Jumapili.
Mr Ebbo aliyetamba na staili yake ya kuimba 'kiswahili cha kimasai', arakumbukwa kwa nyimbo matata kama Mi Mmasai Bana, Maneno Mbofu Mbofu, 'Pombe' na nyinginezo.
Kwa taarifa za awali zinasema alikuwa akiugua kitambo, ingawa haikuwahi kuripotiwa mapema hadi leo tulipopenyezewa taarifa hizi.
Mungu Aiweke Roho ya Mr Ebbo Mahali Pema. Amin