STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, May 30, 2013

Mwili wa Ngwair kuwasili nchini J'mosi, kuagwa J'2 kabla ya kuzikwa Moro J3

http://blog.greatlakesmix.com/wp-content/uploads/2013/02/ngwair-400x600.jpg
Ngwair enzi za uhai wake
MWILI wa marehemu Albert Mwangwea 'Ngwair' unatarajiwa kutua nchini siku ya Jumamosi jioni na kuagwa rasmi Jumapili kutwa nzima kabla ya kusafrishwa kwenye Morogoro kwa ajili ya mazishi yatakayofanyika Jumatatu.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kamati ya Mazishi ya msanii huyo aliyefariki juzi nchini Afrika Kusini taratibu zote za kurejeshwa kwa mwili wa Ngwair zinaendelea vyema na kwamba kamati hiyo inaomba watu wajitokeza kuichangia kamati hiyo kutokana na ukweli kuna gharama kubwa zinazohitajika kufanikisha mambo.
Msemaji wa kamati hiyo Adam Juma, alisema mchana huu kuwa kila kitu kinaenda sawa na kwamba mwili ya marehemu Ngwair utawasili nchini jioni ya Jumamosi na Jumapili kuanzia saa 2 mpaka saa 10 wananchi watauaga mwili huo kabla ya kusafirishwa kwenda Morogoro kwa mazishi.
Juma alisema mazishi ya Ngwair yafanyika Jumatatu na kwamba kamati yao inayoongozwa na Kaka wa Marehemu Kenneth Mangwair inaratibu kila kitu kwa sasa kwa ufanisi mkubwa, ila aliwaomba mashabiki wa muziki na watanzania kwa ujumla kujitolea kwa hali na mali kuwezesha mipango ya mazishi ya Ngwair.
Mkali huyo wa miondoko ya hip hip aliyetamba na vibao mbalimbalio vikali, alifariki nchini humo alipoenda kufanya maonyesho ya muziki akiwa na msanii mwenzake, M to the P ambaye alikuwa amezimika chumbani walimokuwa wanakaa na kwa sasa inaelezwa hali yake inaendelea vyema jambo linalotoa matumaini.

Balozi Biswaro awapa changamoto Stars

Balozi Biswaro

Kikosi cha Stars
Na Boniface Wambura, Addis Ababa
BALOZIi wa Tanzania nchini Ethiopia, Joram Biswaro amewataka wachezaji wa Taifa Stars kuhakikisha wanaipeleka timu hiyo kwenye fainali za Kombe la Dunia zitakazofanyika mwakani nchini Brazil.

Ametoa changamoto hiyo wakati alipotembelea mazoezi ya timu hiyo jana (Mei 29 mwaka huu). Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager imepiga kambi nchini Ethiopia na inafanya mazoezi kwenye Uwanja wa Addis Ababa.

“Watanzania tunafurahi kutokana na uwezo mnaouonyesha, hasa baada ya kuifunga Morocco mabao 3-1. Kama mliwafunga nyumbani hata kwao mnaweza kuwafunga. Tunataka kuwaona Maracana (Brazil) mwakani, mimi tayari ninayo tiketi mtanikuta kule,” amesema Balozi Biswaro ambaye enzi zake aliwahi kuichezea timu ya Yanga.

Taifa Stars ambayo iko Addis Ababa tangu Jumatatu (Mei 27 mwaka huu) imeweka kambi katika hoteli ya Hilton ambapo Jumapili (Juni 2 mwaka huu) itacheza mechi ya kirafiki na Sudan (Nile Crocodile) kwenye Uwanja wa Addis Ababa.

Balozi Biswaro ameikaribisha Taifa Stars ubalozini Addis Ababa mara baada ya mechi dhidi ya Sudan ambapo itakutana na baadhi ya Watanzania wanaoishi Ethiopia kabla ya kuondoka alfajiri kwenda Marrakech, Morocco kwa kupitia Cairo, Misri.

Kocha Kim Poulsen amesema kikosi chake kinaendelea na mazoezi vizuri na kitaimarika zaidi baada ya wachezaji Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu wanaochezea timu ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC) kujiunga nacho Juni 3 mwaka huu jijini Marrakech kwa ajili ya mechi dhidi ya Morocco itakayochezwa Juni 8 mwaka huu.

Wachezaji walioko katika kikosi cha Stars jijini Addis Ababa ni Juma Kaseja, Aggrey Morris, Mwadini Ally, Ally Mustafa, Shomari Kapombe, Kevin Yondani, Erasto Nyoni, Haroub Nadir, Mwinyi Kazimoto, Frank Domayo, Mrisho Ngasa, Khamis Mchana, Amri Kiemba, Salum Abubakar, Simon Msuva, John Bocco, Vicent Barnabas, Mudathiri Yahya, Athuman Idd, Haruni Chanongo na Zahoro Pazi.

Wednesday, May 29, 2013

Yathibitika M2P hajafa, ila bado yu mahututi

ASUBUHI zilizagaa taarifa nchini kwamba msanii aliyekuwa na marehemu Albert Mangwea 'Ngweair', M to the P aliyekutwa amezimia kwamba naye alikuwa amefariki dunia, ukweli ni kwamba msanii huyo bado yu hai ingawa hali yake inaelezwa kuwa bado si nzuri kwani anaendelea kupumulia gesi.
Kwa mujibu wa Mtangazaji wa kituo cha radio cha Clouds Fm, Millard Ayo, aliyekuwa akizungumza moja kwa moja kutoka Afrika Kusini alipoenda, alisema kuwa M2P bado yu hai, ingawa bado amelazwa na anapumua kwa kutumia mashine maalum.
Ayo alisema M2P aliyekuwa sambamba na Ngweair katika chumba kimoja, alionekana na baadhi ya marafiki zake akiwamo msanii Bushoke akinyanyuka mara aalipowaona wameenda kumjulia hali na kuthibitisha kuwa yu hai tofauti na taarifa za mapema asubuhi kwamba msanii huyo naye aliaga dunia.
Aidha mtangazaji huyo anayeendesha kipindi cha Amplifaya, alisema mwili wa marehemu Ngweair ulihamishw atoka hospitali ya Helen Joseph na kupelekwa hospitali ya serikali ukisubiri taratibu za kuusafirisha kuurejesha Tanzania kwa ajili ya mazishi.

Jide, aungana na MwanaFA, Kalapina kufuta onyesho


 
Judith Wambura Mbibo 'Jide' a.k.a Anaconda
MWANADADA mkali wa miondoko ya muziki wa kizazi kipya nchini, Lady Jaydee ameamua kufuta onyesho lake la miaka 13 tangu awe katika fani hiyo lililokuwa lifanyike Ijumaa kupisha msiba wa Albert Mwangwea 'Ngwair'.
Hatua ya Jide imekuja huku wakali wengine wa muziki huo nchini MwanaFA na Karama Masoud 'Kalapina' ambao nao walikuwa wafanye maonyesho yao Mei 31 jijini dar katika kundi tofauyti.
Jide, ambaye hivi karibuni aliingia kwenye mzozo na kituo cha radio cha Clouds, kiasi cha kufikishwa mahakamani, alinukuliwa akisema kuwa onyesho hilo halitafanyika tena kesho mpaka msiba wa Ngwair utakapomalizika.
Akihojiwa na kipindi cha Super Mix kinachorushwa na kituo cha EA Radio, Jide maarufu kama Komandoo a.k.a Binti Machozi au ukipenda Anaconda, mkongwe alikuwa na wakati mgumu alipoulizwa unamuelezeaje msanii Mangwear.
Jide aliyekuwa mwenye huzuni akijibu huku akilia kuwa, Tanzania imempoteza nyota. Juu ya shoo yake Jide alisema imebidi aisogeze mbele kidogo mpaka msiba huu upite kwanza ndipo atasema tarehe rasmi.
Ngwair alifariki jana nchini Afrika Kusini kwa kile kilichoelezwa kuwa kala kitu chenye sumu, taarifa nyingine zikidai alijidunga dawa na kuzimika yeye na rafikie M to the P aliyeripotiwa kulazwa hospitalini akiwa hoi mjini  Johannesburg.

Familia ya Ngwair watoa taarifa ya mazishi na jinsi mwili utakavyoletwa Bongo

http://3.bp.blogspot.com/-WhLAsO1Z0Cg/TftKo0GeYeI/AAAAAAAAAkY/Z6SKc0_7gz0/s1600/NgweaWEB.jpg
Ngwair enzi za uhai wake
BABA Mdogo wa 'Membaz' wa kundi la Chember Squad, Albert Mangwea 'Ngwair', Mzee Mangweha ambaye yuko Mbinga Songea kikazi, amesema kuwa wamekubaliana na kaka yake mkubwa yaani baba mkubwa wa Ngwair, David Mangweha ambaye naye yuko Songea kuwa watu watakutanika Mbezi kwa msiba na pia mapokezi yatafanyika hapa Dar es salaam Mbezi Beach. 
  

Baba huyo mdogo alisema kuwa kesho ndo watarudi Dar es Salaam pamoja na kaka yake yaani baba mkubwa wa marehemu. 
 
Kuhusu mwili kuletwa hapa Tanzania kutoka Afrika Kusini baba mdogo amesema kuwa mpaka sasa hawajajua jinsi gani mwili huo utafika hapa lakini kuna ndugu zao ambao tayari washaanza kufanya taratibu za kuwasiliana na ubalozi wa Afrika Kusini ili kujua ni jinsi gani mwili huo utafika hapa.

Kama kutakuwa na mabadiliko yeyote watakapowasili kesho baba mdogo na baba mkubwa baada ya kikao cha familia watatoa taarifa.
Lakini asuibuhi mmoja wa ndugu wa marehemu kutoka mkoa wa Mara alisema kuwa mwili wa msanii huyo aliyekuwa mkali wa Hip hop utakapowasili nchini utazikwa mjini Morogoro ambapo tayari kuna msiba umewekwa na mama yake.
Ndugu huyo alikuwa akihojiwa moja kwa moja na kituo kimoja cha redio na kusema wana ndugu wamekubaliana Ngwair akazikwe Morogoro alipohifadhiwa baba yake.
Ngwair, aliyefahamika baada ya kutoa kibao cha Ghetto Langu mwaka 2003 kabla ya kupakua albamu ya Mimi na kisha kufuatiwa na Nge, alifariki jana nchini Afrika Kusini kwa kile kilichoelezwa kujidunga dawa za kulevya, ingawa bado haijathibitishwa kidaktari alipoenda kufanya shoo na msanii mwenzake M2P. 

WASIFU WA MAREHEMU NGWAIR


 MAREHEMU Albert Kenneth Mangwea alizaliwa Novemba 16, 1982 mjini Mbeya akiwa ni mtoto wa mwisho kati ya watoto 10 wa baba yake na wa sita kwa mama.
Kiasili Ngwair alikuwa mwenyeji wa mkoa wa Ruvuma kabila la Kingoni, ingawa amekuwa mjini Morogoro na mkoa wa Dodoma.
Shule ya Msingi aliisoma Shule ya Bungo mjini Morogoro alikohamia akiwa na miaka mitano kabla ya kuhamia Dodoma kulamizia darasa la saba toka la tano alilohama nalo Shule ya Mlimwa.
Sekondari aliisoma Mazengo Sec kabla ya kuendelea Chuo cha Ufundi cha Mazengo pia mjini Dodoma alipoanza kujihusisha na muziki kabla ya kutua kundi la Chamber Squad lililoundwa na Jafarah, Jay Mo, Noorah, Mez B, Mchizi Mox na Dark Master.
Amewahi kunyakua tuzo ya Kili Music Award kupitia kipengele cha muziki bora wa Hiphop, huku nyimbo kadhaa zilimtambulisha vyema kwa mashabiki baadhi ikiwa ni  Ghetto Langu, Mikasi na nyingine za kushirikishwa na wasanii mbalimbali.
Katika maisha yake ya muziki aliwahi kutoa albamu mbili za Mimi ya mwaka 2005 na Nge ya mwaka juzi ambayo hata hivyo haikufanya vyema sokoni kama ile ya awali.

Tuesday, May 28, 2013

Breaking Newssss:Albert Mangwea afariki Afrika Kusini, inadaiwa kalishwa sumu

Albert Mangwea enzi za uhai wake
NYOTA wa nyimbo za Ghetto Langu, Mikasi, Nipe Deal na nyinginezo, Albert Mangwea 'Ngwair' amefariki dunia leo saa 9 alasiri akiwa nchini Afrika Kusini kwa kile kilichoelezwa huenda alilishwa sumu.
Taarifa zilizotufikia hivi punde zinasema kuwa Ngwair tangu alipolala usiku wa jana hakuweza kuamka na wenzake waliokuwa wameambatana nchini humo waliamua kumgongea na walipoingia ndani walimkuta katulia na kumkimbiza hospitali moja mjini Pretoria na kugundulika kuwa amefariki baada ya kupimwa na daktari aliyempokea hospitalini hapo.
Japo taarifa zingine zinasema kuwa Ngwair na msanii mwenzake alioenda nchini humo kufanya Show M to the P walijidunga 'unga' na kusababisha mkali huyo wa hip hop kuaga dunia na mwenzake kuwa taaban.
Tayari inaelezwa msiba wa msanii huyo umewekwa mjini Morogoro baada ya taarifa hizo kufika kwa mama yake anayeishi huko.
Mungu aiweze roho yake mahali pema na MICHARAZO inafuatilia zaidi taarifa hizo kujua ukweli.

Dekula Band kufanya makamuzi Little Nairobi




Dekula Kahanga 'Vumbi'

MKALI wa zamani wa bendi ya Orchestra Marquiz Original 'Wana Sendema', Alain Dekula Kahanga 'Vumbi' pamoja na kundi lake la Dekula Band wakiwa na wakali kama Lady Neema, Bobo Sukari na Yaya Sella wikiendi hii wataendelea na makamuzi yake nchini Sweden wanapoendelea na shughuli zao za muziki.
Vumbi aliiambia MICHARAZO kuwa Dekula Band 'Ngoma ya Kilo' watakamua burudani katika ukum,bi wa Lila Wien, maarufu kama Little Nairobi, wakiangusha ngoma mpya na za zamani mwanzo mwisho.
Maonyesho hayo yatafanyika kwa siku mbili mfululizo Mei 31 na Juni Mosi na kusema mashabiki wa bendi hiyo na waliozoea ukumbi huo hawapaswi kuikosa burudani hiyo itakayoambatana na show kabambe pamoja na kukumbushiwa vibao vya zamani vilivyomfanya yeye wenzake kuwatamba nchini enzi zao.
Vumbi alisema wamepania kufanya mambo makubwa zaidi ya yaliyozoeleka kufanywa na bendi yake.

Tangazo lao linasomeka hivi;
"Wazee Wapewe" present's;
Lady Neema,Bobo Sukari & Yaya Sella
Dekula Band"Ngoma Ya Kilo"
Place: Lilla Wien"Little Nairobi"
Date: 31/may & 01/june/2013
Time: 21.00-01.00
Addr: Swedenborgsg.20
Pendel: Södra station
http://www.youtube.com/watch?v=T3KIYgRlyR0

Real Madrid wasisitiza Ronaldo hauzwi


http://img.thesun.co.uk/multimedia/archive/01623/ronni_1623771a.jpg
Cristiano Ronaldo

KLABU ya Real Madrid ya Hispania imesisitiza kuwa nyota wake, Cristiano Ronaldo hauzwi kwa vile bado  wanamtegemea mchezaji huyo kwa msimu ujao.
Nyota huyo wa Ureno mwenye miaka 28 amekuwa akitajwa kuwa yu mbioni kurejea klabu yake ya zamani wa Manchester United ya England pia akitajwa kunyatiwa na mabingwa wa Ufaransa, PSG.
Ronadlo alinukuliwa mwaka uliopita kuwa anajisikia huzuni kuwepo Bernabeu na kudai alikuwa anafikiria kuachana na klabu hiyo.
Lakini Rais wa Real, Florentino Perez alisema wanatumaini mshambuliaji huyo atasalia katika klabu yao na wana imani atakuwa miongoni mwa wachezaji wao kwa miaka kadhaa ijayo.
Perez alisema: Aliniambia katika kipindi cha majira ya joto alikuwa na huzuni na tulimueleza jinsi tukavyofanya kila linalowezekana kwa ajili yake mradi ajisikie poa.
"Sijui kama kuna ofa yoyote aliyopewa kutoka PSG. Nafikiri Cristiano ni mwansoka bora kabisa duniani," alisema Perez na kuongeza wangependa kuijenga Madrid kwa misimu kadhaa ikiwa na ubora wa hali ya juu sambamba na Ronaldo aliyedai wangependa kuendelea kuwa mchezaji anayelipwa vyema duniani.
Duru za soka zinasema kuwa Ronaldo yupo kwenye mipango ya kurejeshwa Old Trafford, kwa kile kinachoelezwa hafurahii maisha ya Madrid kwa namna mashabiki wanavyomchukulia licha ya kufanya kazi kubwa tangu atue katika klabu hiyo akitokea Manchester United.

Stars watua salama Ethiopia waanza kujifua

Wachezaji wa Stars katika suti kabla ya kwenda Ethiopia
Na Boniface Wambura, Addis Ababa
Taifa Stars imetua jijini Addis Ababa, Ethiopia leo (Mei 28 mwaka huu) alfajiri kwa ndege ya EgyptAir ambapo itaweka kambi ya wiki moja kujiandaa kwa mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia dhidi ya Morocco (Lions of the Atlas) itakayochezwa Juni 8 mwaka huu jijini Marrakech.

Stars iliyotua na kikosi cha wachezaji 21 imefikia hoteli ya Hilton, na imeanza mazoezi leo (Mei 28 mwaka huu) saa 12 jioni kwenye Uwanja wa Addis.

Kwa mujibu wa Kocha Kim Poulsen, Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itakuwa na vipindi (sessions) vinne vya mazoezi kabla ya kucheza mechi ya kirafiki na Sudan (Nile Crocodile). Mechi dhidi yan Sudan itachezwa Jumapili kuanzia saa 11 jioni kwenye Uwanja wa Addis.

Sudan ambayo pia imeweka kambi yake Addis Ababa kujiandaa kwa mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia ilicheza mechi yake ya kwanza jana (Mei 27 mwaka huu) dhidi ya wenyeji Ethiopia na kulala mabao 2-0.

Wachezaji wanaounda Stars ni nahodha Juma Kaseja, nahodha msaidizi Aggrey Morris, Mwadini Ally, Ally Mustafa, Shomari Kapombe, Kevin Yondani, Erasto Nyoni, Haroub Nadir, Mwinyi Kazimoto, Frank Domayo, Mrisho Ngasa, Khamis Mchana, Amri Kiemba, Salum Abubakar, Simon Msuva, John Bocco, Vicent Barnabas, Mudathiri Yahya, Athuman Idd, Haruni Chanongo na Zahoro Pazi.

Kikosi hicho kinatarajiwa kuondoka Addis Ababa kwenda Marrakech alfajiri ya Juni 3 mwaka huu kwa ndege ya EgyptAir. Stars itatua siku hiyo hiyo Casabalanca na kuunganisha moja kwa moja kwenda Marrakech.

Wakongo wanne wajitokeza kuomba kazi Msimbazi


Wachezaji wa Simba wakijifua

Tutamvutia tu Kibadeni! Ndivyo wachezaji wapya wanaoomba kazi Mismbazi wakijifua kabla ya kuangaliwa na kocha Kibadeni

Kibadeni akiwahakiki wachezaji wapya walijitokeza kujaribiwa

Andika majina yako kamili: Kibadeni akiwaandikisha majina wachezaji

Add caption

Wachezaji wapya wakijifua

Mtacheza hivi: Kocha msaidizi, Seleman Matola kizungumza na wachezaji wapya waliojitokeza kujaribiwa huku King KIbadeni (wa pili kulia) akisikiliza kwa makini


Wachezaji wa Simba U20 na wapya wakipimana ubavu leo uwanja wa Kinesi

Wachezaji wa Simba wakionyeshana kazi mazoezini leo asubuhi

Matola akitetea jambo na wanahabari

Mimi ndio Matola Bwana! Kocha wa U20 Seleman Matola akimueleza jambo Mahmoud Zubeiry mwenye miwani,  huku Saleh Ally akicheka kando yao

Wachezaji wapya wa Simba wakipashga moto uwanja wa Kinesi
WACHEZAJI wanne kutoka nchi ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo (DR Congo), wakiwamo watatu wanaokipiga AS Vita wamejitokeza kuomba kibarua cha kuichezea Simba kwa msimu ujao ambao asubuhi ya leo walikuwa wakijaribiwa na kocha mpya wa timu hiyo, Abdallah Kibadeni 'King Mputa'.
Pia katika majaribio hayo wapo wachezaji wengine kadhaa akiwamo Mtanzania aliyekuwa akiichezea timu ya Ferreviario de Nampula ya Msumbuji, Miembeni Zanzibar na wachezaji wengine chipukizi kutoka jijini Dar katika klabu za Fc Boom ya Ilala, Buza Sports na Mbagala Scaret Academy.

Wachezaji kutoka Kongo wakiwamo washambuliaji watatu ni pamoja na Joe Fils kutoka Le Verez Club, Fabian Tshayaz, Fabrice Balou na Patrick Milambo wote wa AS Vita.
Wengine waliojitokeza kuomba 'kazi' Msimbazi ni Ramadhani Kipicha kutoka klabu ya Buza, Adeyun Saleh wa Miembeni Zanzibar, Mohammed Abdallah aliyekuwa anacheza Ferreviario De Nampula ya Msumbiji, Shaaban Kondo wa Mbagala Scalet Academy na Shaaban Said wa Fc Boom ya Ilala.
Wachezaji hao walisema wamejitokeza kuomba nafasi ya kufanya kazi Msimbazi kwa kuamini wanaweza licha ya kudai jukumu la kupima uwezo wao lipo mikononi mwa makocha wao, King Kibadeni, Jamhuri Kihwelu 'Julio', Seleman Matola na wote waliopo kwenye benchi la ufundi la timu hiyo.

Wakati wa maharibio hayo wachezaji wao walipewa muongozo na kocha wa timu ya vijana, Seleman Matola kabla ya Kibadeni kuzungumza nao huku wakishuhudiwa na Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Evodius Mtawala aliyefika mapema uwanja wa Kinesi kwa ajili ya kuona kazi zinaendeleaje.

King Kibadeni atua rasmi Msimbazi na mikwara, Julio achekelea


Kocha Abdallah Kibadeni akizungumza na baadhi ya wachezaji wapya walijitokeza kujaribiwa Simba

King Kibadeni (wapili kulia) akiteta na Amri Said wakati walipokuwa wakizungumza na wachezaji waliojitokeza kuwania kusajiliwa Simba ambao jana walipimwa na kocha huyo.

Kocha Abdallah Kibadeni (kulia) akiwa na wasaidizi wake, Jamhuri Kihwelu 'Julio' na Seleman Matola wakiwa kwenye  mazoezi ya timu hiyo asubuhi ya leo katika uwanja wa Kinesi.

Katibu Mkuu wa Simba, Evodius Mtawala akiteta na makocha wa timu yao, Abdallah KIbadeni (kulia) Jamhuri Kihwelu 'Julio' na Seleman Matola.

Kocha msaidizi, Seleman Matola akigawa jezi kwa wachezaji waliojitokeza kutaka kusajiliwa Simba asubuhi ya leo kwenye uwanja wa Kinesi.

Wachezaji wa kikosi cha Simba B wakijifua kabla ya kuwapima wachezaji wapya wanaowania kujiunga na Simba
KOCHA maarufu aliyewahi kuwa nyota wa Simba na Taifa Stars, Abdallah Kibadeni, ameanza rasmi kazi ya kuinoa timu hiyo baada ya kusaini mkataba wa miaka miwili akichukua nafasi ya Mfaransa, Patrick Liewig aliyetimuliwa.
Kibadeni maarufu kama 'King Mputa' ametua Simba ikiwa ni mara yake ya nne akitokea Kagera Sugar aliyoinoa msimu huu kwa mkataba wa mwaka mmoja katika Ligi Kuu Tanzania Bara iliyomalizika hivi karibuni na kuifikisha timu hiyo kwenye 'Nne Bora'
Kocha huyo alianza kazi asubuhi ya leokwenye uwanja wa Kinesi, Ubungo jijini Dar es Salaam kwa kuwajaribu wachezaji wapya waliojitokeza kuwania kusajiliwa Simba wakiwemo Wakongo wanne na mmoja kutoka Msumbiji.
Kibadeni alisema amesaini mkataba wa miaka miwili kuinoa Simba na kwamba malengo yake ni kuhakikisha Simba inafika mbali katika ligi ya nyumbani na kimataifa kama ilivyo desturi yake.
Kocha huyo aliyewahi kuifikisha Simba kwenye fainali za michuano ya CAF mwaka 1993 na kufungwa mabao 2-0 na Stella Abidjan, alisema kitu cha muhimu angependa apewa muda ndani ya kikosi hicho kufanya kazi zake.
"Nimetua rasmi Simba kwa mkataba wa miaka miwili na matarajio yangu ni kuifikisha mbali, ingawa watarajie lolote kwa michuano ya Kagame kwa muda uliopo wa maandalizi, lakini kwa ligi wasiwe na shaka," alisema.
Aliongeza anachopenda kwa uongozi wake ni kumpa nafasi ya kufanya kazi bila kuingiliwa, ili hata mwisho wa  siku iwe rahisi kwao kumbana.
"Hakuna jambo ambalo silipendi kama kuingiliwa kazi, kila mtu atekeleze majukumu yake kwa maana benchi ya ufundi tuachwe tuifanye kazi na wataona nini tutakachokifanya kwani najiamini naweza," alisema Kibadeni.
Kuhusu wachezaji waliosimamishwa na uongozi wa tuhuma za utovu wa nidhamu, Kibadeni alisema hawana nafasi kwake kwa madai siku zote yeye amekuwa muumini wa suala la nidhamu kwa wachezaji.
"Kama viongozi waliwasimamisha kwa utovu wa nidhamu, kwangu pia hawana nafasi ili wasije wakaniharibia kazi, nitafanya kazi na wachezaji wote walio tayari kuitumikia Simba kwa hali na mali ili ifike mbali," alisema.
Kocha huyo anayeanza rasmi kuinoa timu hiyo kwa ajili ya maandalizi ya michuano ya Kombe la Kagame itakayofanyika nchini Sudan, aliusisitizia uongozi umpe ushirikiano katika utekelezaji wa programu zake kama walivyokuwa wakifanya kwa makocha wa kigeni.
"Nikipewa ushirikiano na kutekelezewa kila ambalo nahitaji kwa maandalizi na programu ya timu naamini Simba itatisha msimu ujao, ikizingatiwa nalijua soka la Tanzania na wasaidizi nilionao ni watu wanaojua soka," alisema.
Kwa upande wa makocha wasaidizi waliompokea Kibadeni, Jamhuri Kihwelu 'Julio', Seleman Matola na Amri Said walisema wamefurahi ujio wa mwalimu huyo aliyewahi kuwanoa enzi za uchezaji na kuamini benchi la ufundi sasa limekamilika na Simba itatisha.
"Simba ijayo itatisha, nani asiyemjue Super Coach, King Kibadeni, ebu piga picha huku King, hapa Julio aaah Simba itatakata tuombe Mungu, ila tumefurahi mno kurejeshwa kwa Kibadeni Msimbazi," alisema Julio.

Hussein Javu airuka kimanga Yanga, asisitiza yeye bado wa Mtibwa

Hussein Javu
MSHAMBULIAJI nyota wa timu ya soka ya Mtibwa Sugar, Hussein Javu ameiruka kimanga klabu ya Yanga kuhusu mipango yao ya kutaka kumsajili kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Javu alisema hajawahi kufanya mazungumzo na kiongozi yeyote wa Yanga na kushangazwa na taarifa kwamba yupo njiani kutua Jangwani akitokea Mtibwa.
Akizungumza na MICHARAZO, Javu alisema mpaka sasa yeye ni mchezaji wa Mtibwa Sugar na angependa kuendelea kuichezea klabu hiyo kwa misimu mingine na hajui wanaomzushia kwamba anajiandaa kuhamia Yanga.
"Sijajua hizi taarifa zinatoka wapi, sijazungumza na kiongozi yeyote wa Yanga kuhusu suala la kuhamia Jangwani, lakini naona naandikwa kuhusu mipango hiyo wengine wakidai nimteoa masharti ya kutaka nyumba na gari," alisema.
Alisema anashukuru kupata nafasi ya kuzungumza na MICHARAZOna kuweka bayana suala hilo ili isije akaeleweka vibaya kwa viongozi na wachezaji wenzake.
Alipoulizwa yupo tayari kutoka Mtibwa Sugar, Javu alisema hajafikiria kwa sasa ila alisema kama kweli kuna klabu inayomhitaji ni lazima izungumze naye pamoja na viongozi wake na wakiafikiana atakuwa na maamuzi sahihi.
"Soka ni ajira yangu, pamoja na kwamba napenda kucheza Mtibwa, kama itatokea klabu yoyote itakayokuwa inanihitaji ikazungumza nami au viongozi wangu naweza kuhama, lakini siyo kwa kuzushiwa kama sasa," alisema Javu.
Mshambuliaji huyo ambaye amekuwa na bahati za kuzitungua Simba na Yanga kila timu hizo zikikutana na Mtibwa Sugar, alisema ingekuwa vyema vyombo vya habari zinaposikia fununu zozote hasa kipindi hiki cha usajili kikafanya jitihada za kuzungumza na wahusika badala ya kuandika tu na kuharibiana.
Javu amekuwa akihusishwa na mioango ya kutua Yanga kwa nia ya kuimarisha kikosi cha timu hiyo baada ya washambuliaji waliopo sasa baadhi yao kushindwa kung'ara kwenye msimu uliopita.

Wawakilishi wa Tanzania Big Brother The Chase hawa hapa

Nando

Feza Kessy
MASHINDANO ya Big Brother Africa ‘Big Brother-The Chase’ yamezinduliwa rasmi juzi nchini Afrika Kusini.
Mashindano hayo ambayo yanafanyika kwa mara ya nane mwaka huu, yanashirikisha jumla ya watu 24 kutoka katika nchi 14 za Afrika.
Washiriki hao wanatarajiwa kukaa ndani ya nyumba hiyo kwa muda wa siku 90 ambapo wataanza kuchujwa kuanzia mwishoni mwa wiki hii.
Tanzania inawakilishwa na Feza Kessy pamoja na Ammy Nando ambapo mshindi wa mwaka huu ataondoka na kitita cha dola za Kimarekani 300,000.
Akizungumza Dar es Salaam juzi wakati wa uzinduzi huo, Ofisa Habari wa Dstv Tanzania Barbara Kambogi, alisema kuwa pamoja na kuwa msimu huu Ligi mbalimbali zimeshamalizika hivyo mashabiki wengi watapata burudani kupitia katika shindano hilo.
Alisema kuwa mashindano hayo yanaonyeshwa moja kwa moja na Dstv kupitia chaneli 197 na 198 ambapo mashabiki kutoka nchi 50 watapata fursa ya kuyaangalia.
Pia Mkurugenzi wa Masoko wa Kampuni ya Simu ya Airtel ambao pia ni wadhamini wa mashindano hayo kwa mwaka huu Bw, Levi Nyakundi alisema kuwa mashindano hayo yanazidi kupata umaarufu kutokana na kila mwaka kuwa tofauti.
Aliongeza kuwa wateja wa Airtel wananafasi ya kulipia huduma ya DSTV kwa kupitia huduma ya Airtel kwa kupiga *150*60# kwa urahisi wakiwa nyumbani au sehemu zao za kazi.
“Airtel Money itasaidia sana wateja wetu kuokoa muda wao wa kazi pale wanapolipia huduma ya DSTV wakati wowote wakati wa msimu huu wa Big Brother, mashabiki hawana budi kuwapigia kura washiriki wanaoiwakilisha Tanzania ili kuhakikisha wanaibuka na ushindi,” alisema Nyakundi.
“Mashindano ya mwaka huu yanaonekana kuwa tofauti na yaliyopita hivyo tunatarajia kupata burudani nzuri na hivyo mashabiki wawapigie kura Watanzania ili wafanye vizuri” alisema.
Katika uzinduzi huo kulikuwa na burudani zilizotolewa na wasanii kutoka Afrika Kusini Mafikizolo pamoja na Stela Mwangi wa Kenya.

Monday, May 27, 2013

Coastal Union kusajili kimyakimya


baadhi ya viongozi wa Coastal Union

WAKATI klabu za Simba na Yanga zikipigana vikumbo na kutambiana kwenye vcyombo vya habari juu ya wachezaji inayowanasa kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara, uongozi wa Coastal Union ya Tanga umesema utafanya usajili wao kimyakimya bila makeke kama vigogo hivyo vya soka nchini.
Coastal iliyorejea kwenye Ligi Kuu msimu wa 2011-2012, imesema kitu cha muhimu na watakachozingatia ni kusajili kwa umakini mkubwa na kwa kiwango cha kimataifa, ili kuiwezesha timu yao kufanya vyema kwa ligi ijayo sambamba na kutimiza malengo waliyojiweka mabyo msimu huu wameshindwa kuyafikia.
Mkurugenzi wa Ufundi wa klabu hiyo, Nassor Binslum, aliiambia MICHARAZO kuwa, hawatafanya usajili wa mbwembwe na makeke badala yake ifanya mambo yao kimyakimya bila kuwashtua watu hadi mwishoni watakapokianika kikosi chao.
Binslum, alisema watakachozingatia ni kusajili wachezaji watakaoiwezesha Coastal ifanye vyema katika ligi hiyo tofauti na msimu huu waliomaliza wakiwa kwenye Sita Bora, kinyume na msimu uliopita walipomaliza nafasi ya Tano.
"Coastal Union hatuna mbwembwe tutafanya usajili wetu kimyakimya na kwa umakini mkubwa ili msimu ujao tutishe na tutakitangaza kikosi mara baada ya mambo yote kukamilika," alisema Binslum.
Mabingwa hao wa zamani wa soka nchini, walimaliza katika nafasi ya sita kwa kujikusanyia pointi 35 kutokana na michezo 26 iliyocheza na ilimaliza msimu vibaya kwa kupewa kichapo cha mabao 2-0 na Polisi Morogoro.

Mtoto wa miaka 7 anusurika kuchomwa moto, kisa...!

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEiRYGNK4P0cFIyKRqOFynOrQq3EIcCP4FHCqYF9HopGj2yWE0li5U95QShB5g6C5tyfVNd6rQZix8eewbtSTxRe5-c3My82W5tXZIy2_4U5Ugq8tTUcyyGuAgGc9nDbHRECNaAQ2qXPtLU/s1600/Waalimu.JPG
Mwenyekiti wa Mtaa wa Kimara King'ongo, Bw Mapesi (kushoto) anayedaiwa kumuokoa mtoto na kijana aliyetaka kumchoma moto mtoto huyo kwa tuhuma za kuiba viatu.


VITENDO vya watoto wadogo kufanyiwa vitendo vya kikatili vinazidi kushamiri katika jamii ambapo hivi karibuni mtoto mmoja wa miaka saba anayesoma Shule ya Msingi iliyopo Kimara King'ongo kata ya Saranga alinusurika kuuwawa kwa kuchomwa moto na kijana mmoja mshona viatu akimtuhumu mwizi.
Tukio hilo ambalo MICHARAZO imedokezwa lilitokea wiki mbili zilizopita majira ya mchana katika eneo la Kwa Komba, Kimara King'ongo baada ya mshona viatu huyo anayefahamika kwa jina na Ngosha kumpiga na kisha kumwagia dumu zima la mafuta ya taaa mtoto huyo kisha kumburuta hadi dukani ili anunue kiberiti cha kumwashia moto kabla ya wasamaria wema kuingilia kati na kumgeuzia kibao kijana huyo.
Inaelezwa mtoto huyo (jina linahifadhiwa) siku moja kabla alienda kwa fundi huyo na kuviona viatu ambavyo alimuomba ampe akamuonyeshe baba yake ili aweze kumununu kutokana na kuvipenda na Ngosha alimpa bila hiyana akimtaka arejeshe mara baada ya kumaliza haja zake kwa baba yake.
Hata hivyo mmoja wa mashahuda wa tukio hilo alidai mara baada ya mtoto huyo kwenda na viatu hivyo kwa wazazi wake na kueleza shida na mahali alipovipata, baba yake alimchapa fimboa kimtaja kuvirejesha mahali alipovipata akiamini huenda kijana wake aliviiba.
Kwa kuwa ilishafika usiku, mtoto alilala na viatu na kesho aliamua kuvirejesha kwa Ngosha na kumueleza baba yake alimchapa akidhani ameviiba na ghafla kijana huyo (pengine kwa bhangi, anazoelezwa anavuta katika eneo lake la kazi) alimbadilikia kijana huyo na kuanza kumchapa makofi akidaia anawatafuta watoto wengi kama mtoto huyo.
Mtoto huyo aliamua kupiga kelele akijitetea yeye siyo mwizi, lakini Ngosha kama asiyemjua alimpiga tani yake kisha kuchukua dumu la mafuta ya taa alililokuwa nalo katika eneo lake la kazi na kumwagia kijana huyo mdogo bila huruma kisha kujisachi na kukuta hana kiberiti na kumburuta hadi kwenye duka lililokuwa jirani na eneo hilo la kituo cha mabasi cha Kwa Komba.
Hata hivyo baadhi ya waendesha pikipiki waliokuwa katika eneo hilo walioshuhudia tukio hilo na wasamaria wema wengine waliamua kuingilia kati na kumhoji Ngosha kwa nini anampiga mtoto na kutaka kumtenda alichokuwa amekusudia na bila aibu alisema anataka kumwasha mtoto mtoto huyo kwani mwizi.
Ndipo wasamaria wema na waendesha pikipiki hao waliamua kumgeuzia kibao kwa kumpiga kijana huyo kabla ya kuja kuokolewa na Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa huyo aliyekuwa amembatana na Polisi na kuondoka na kijana huyo na mtoto aliyekuwa anachuruzika mafuta hadi kituo cha Kidogo cha Polisi cha Kimara.
"Huyo jamaa ni kama aliyechanganyikiwa, alimpa mwenyewe mtoto viatu kisha akamgeuzia kibao baada ya kusikia simulizi lake toka kwa wazazi wake, na kumwagia mafuta yaani kama tusingekuwepo mtoto wa watu angeteketea kibaya wazazi wake wote hakuwepo nyumbani," alisema dereva mmoja wa pikipiki Ally aliyeshuhudia tukio hilo mwanzo mwisho.
Ally alimwagia sifa Mwenyekiti huyo wa serikali ya Mitaa aliyemtaja kwa jina la Demetrius Mapesi, ambaye mbali na kumnusuru mtoto, lakini pia alisaidia Ngosha kufikishwa Polisi kwa usalama bila kudhurika kwani wananchi walutaka wamuunguze yeye wakidai wamemchoka kwa mambo yake yasiyoendana na ustaarabu.
"Kama siyo Mapesi, Ngosha angeiva yeye," alisema Ally.
 MICHARAZO ilimpigia simu mwenyekiti huyo baada ya kupewa namba na dereva huyo, ambapo Mwenyekiti huyo alikiri kutokea kwa tukio hilo na kueleza liliishia Polisi Kimara ambapo mtuhumiwa huyo alifikishwa kwa ajili ya taratibu za kushtakiwa kwa kosa alilotaka kulifanya kwa mtoto huyo mdogo.
"Ni kweli tukio hilo lilitokea wiki mbili zilizopita na tulishamfikisha Ngosha mikononi mwa Polisi kwa taratibu za kufikishwa mahakamani, Ila ilitushtusha mno kijana mzima kaka yeye kumwagia mtoto mafuta ya taa na kutaka kumwasha moto kwa sababu ya viatu ambavyo inadaiwa alimpa mwenyewe," alisema Mapesi.
sikijana mmoja ambaye ni mshona viatu, maarufu kwa jina la Ngosha alikaribia kumlipua kwa moto mwanafunzi wa darasa la kwanza (jina kapuni) akimtuhumu alimuibia viatu.

Vyama vya ngumi vya TPBO, TPBC vyalumbana

http://dewjiblog.com/wp-content/uploads/2012/09/OnesmoNgowi.jpg
Rais wa TPBC, Onesmo Ngowi


http://www.ippmedia.com/media/picture/large/tpboyassinpresidaaa.jpg
Rais wa TPBO, Yasin Abdallah 'Ustaadh'



MASHIRIKISHO ya ngumi za kulipwa nchini yenye heshima kubwa katika mchezo huo, TPBO na TPBC vimeingia kwenye malumbano kila kimoja kikishutumu na kuanika udhaifu wa wenzake kisa ikiwa ni mahojiano aliyoyafanya bondia nyota wa zamani George 'Lister' Sabuni na gazeti moja la kila siku.
Katika habari hiyo Sabuni alinukuliwa akiliponda Oganaiziesheni ya Ngumi za Kulipwa, TPBO kwamba inawakimbiza mapromota kutokana na kuendeshwa kibabaishaji na kuwataka mabondia wapitia Kamisheni ya Ngumi Tanzania, TPBC analofanya nayo kazi.
Hata hivyo kauli hizo zilimfanya Rais wa TPBO, Yasin Abdallah 'Ustaadh' kuwaka na kuanika madudu ya uongozi wa TPBC, ikiwamo kuwakata mabondia asilimia 10 ya fedha kwa safari zao za nje ya nchi badala ya asilimia 1 na mengine ambayo yalijibiwa na Rais wa TPBC, Onesmop Ngowi.
Ngowi alifafanua taarifa kwamba wao TPBC ndiyo waliosababisha promota maarufu nchini wa zamani wa ngumi, DJB Promoters chini ya Jamal na Dioniz Malinzi kuachana na mabondia Rashid Matumla na Mbwana Matumla akidai mabondia hao waliandika wenye barua baada ya kuhamia kwa Kajumulo na Don King Promotions na siyo kweli kama kamisheni yao inahusika.
Kifupi ni kwamba malumbano hayo kwa wadau wa ngumi hayawasaidii na muhimu viongozi hao ambao kwa siku za karibuni walikuwa wakifanya kazi kwa pamoja kukaa chini na kumaliza tofauti zao kwa manufaa ya mchezo huo.
Huu ni mtazamo wa MICHARAZO kama mdau wa michezo nchini.

Ajali tena: Treni yaua mtu Ukonga




Muda mfupi uliopita treni imegongana na gari aina ya RAV4 na dereva (mwanaume)amekufa muda huu na abiria(mwanamke) yu mahututi.  

Sunday, May 26, 2013

Kichanga cha siku nne chaokotwa shimoni alikokaa kwa siku 6



UKISHANGAA ya Mussa basi utayaona ya Firauni, usemi huu umethibitika Songea baada ya Mtoto Bahati Upendo mwenye siku 3 toka azaliwe aliyekuwa amewekwa kwenye mfuko wa mbolea kisha kutupwa kwenye shimo kuokolea akiwa hai licha ya kuishi shimoni humo kwa sita sita.
 
Ndani ya shimo hilo amekaa siku 6 bila kula wala kunywa hadi alipo okotwa na wasamaria wema...
Hivi sasa yuko Hospitali ya Mkoa wa Ruvuma akiwa Salama  Salimini .
Yeyote Mwenye nafasi ya kumsaidia mtoto huyu anaweza kwenda moja kwa moja Hospitali au wasiliana na namba zifuatayo,  mchango  utafuatwa 0755061588 au 0755 731 234.
Dawati la Police Wanawake Mkoa wa Ruvuma wakiwa na Wauguzi kuangalia usalama wa Mtoto huyo aliye Tupwa. Kutoka kulia ni Muguzi Rukia Twahili anaye fuata Devota Umbela na aliye mshika mtoto Mwenyekiti wa Mtandao wa Police Wanawake Fadhila Chacha na wa mwisho kushoto ni A nna Chaima

Taifa Stars kwenda Ethiopia leo njiani kuifuata Morocco

 
Kikosi cha Stars
Na Boniface Wambura
KIKOSI cha timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars) inatarajia kuondoka leo (Mei 26 mwaka huu) usiku kwenda Addis Ababa, Ethiopia ambapo itaweka kambi na kucheza mechi moja ya kirafiki kabla ya kwenda Morocco.

Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itaondoka saa 5 usiku kwa ndege ya EgyptAir ikiwa na kikosi cha wachezaji 21 chini ya nahodha wake kipa Juma Kaseja.

Timu hiyo ikiwa Ethiopia, Juni 2 mwaka huu itacheza mechi ya kirafiki dhidi ya Sudan ambapo siku inayofuata itaondoka kwenda Marrakech, Morocco kwa kupitia Cairo, Misri. Mechi hiyo ya mchujo ya Kombe la Dunia dhidi ya wenyeji Morocco itachezwa Juni 8 mwaka huu jijini Marrakech.

Mbali ya nahodha Kaseja, wachezaji wengine wanaoondoka katika kikosi hicho ambacho kina wiki sasa tangu kingie kambini jijini Dar es Salaam ni Mwadini Ally na Ally Mustafa ambao wote ni makipa.

Wengine ni Shomari Kapombe, Kevin Yondani, Aggrey Morris, Haroub Nadir, Mwinyi Kazimoto, Frank Domayo, Mrisho Ngasa, Khamis Mchana, Amri Kiemba, Salum Abubakar, Simon Msuva, John Bocco, Vicent Barnabas, Mudathiri Yahya, Athuman Idd na Haruni Chanongo.

Wachezaji Mbwana Samata na Thomas Ulimwengu ambao wako na timu yao ya TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo watajiunga moja kwa moja na Stars jijini Marrakech, Juni 4 mwaka huu wakitokea Maputo, Msumbiji mara baada ya mechi yao ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Liga Muculumana ya huko.

Katika msafara huo wa Ethiopia benchi la ufundi la Stars linaundwa na Kim Poulsen (Kocha Mkuu), Sylvester Marsh (Kocha Msaidizi),Juma Pondamali (Kocha wa makipa), Leopold Tasso (Meneja wa timu), Dk. Mwanandi Mwankemwa (Daktari), Frank Mhonda (Mtaalamu wa tibamaungo) na Alfred Chimela (Mtunza vifaa).

Ommy Lax aachia mpya akisaka meneja

Ommy Lax katika pozi
MKALI wa wimbo wa 'Kioo Changu' alioimba na Matonya, Imani Omary 'Ommy Lax' ameachia wimbo mwingine mpya uitwao 'Wapotezee' huku akisaka meneja wa kuzisimamia kazi zake.
Akizungumza na MICHARAZO, Ommy Lax, alisema angependa kufanya kazi chini ya meneja ili kumuongoza katika majukumu yake baada ya mtu aliyekuwa akimtegemea ambaye ni mjomba wake, MP kuwa na majukumu mengine mazito binafsi.
"Natamani na ninasaka meneja wa kunisimamia kazi zangu, hivyo yeyote atakayekuwa tayari anaweza kuwasiliana nami tukae chini na kukubaliana, " alisema Ommy Lax.
Juu ya wimbo wake mpya, Ommy lax alisema ameimba na  mkali kutoka Watanashati, PNC na tayari umeanza kurushwa hewani.
Ommy Lax, alisema kazi hiyo mpya aliyorekodia kwa maprodyuza R Pino na The Timing, ni moja ya nyimbo kali kwa mwaka 2013.
Msanii huyo aliyejishughulisha na sanaa tangu akiwa shuleni na kutoa kazi ya kwanza mwaka 2006, alisema kwa sasa anajipanga kwa ajili ya kutoa  video ya wimbo huo.
"Kaka nimepakua wimbo mpya uitwao 'Wapotezee' nilioimba na PNC, ni moja ya kazi bomba siyo mchezo mashabiki wasubiri kuisikia hewani na sasa nafanya mipango ya video yake, lakini muhimu naomba mtu ajitokeze anipige tafu kama meneja," alisema.

Madabida mgeni tamasha la vipaji



MWENYEKITI wa Chama cha Mapinduzi (CCM) mkoa wa Dar es Salaam, Ramadhani Madabida atakuwa mgeni rasmi katika tamasha la Mastaa chipukizi zaidi ya 320 litafanyika leo Jumapili 26, 2013 katika ukumbi wa Starlight Hotel kuanzia saa 4 asubuhi.

 

Peter Mwenda

                             

Mwenyekiti wa Shiwata, Caasim Taalib alisema Madabida ambaye pia ni Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC) atapata nafasi ya kuona vikundi mbalimbali vya sanaa kikiwepo kikundi cha  Kaole, Splendid, Super Shine Taarab pamoja na wasanii mbalimbali wa Bongo Flava, Maigizo,Ngoma, Dansi na Sarakasi nao wamethibitisha kushiriki.
Taalib alisema wasanii wakongwe wa bongo flava walioalikwa ni Stara Thomas, Safi Theatre Group, Ommy G na waigizaji wakongwe wa Kaole na Splendid wataonesha umahiri wao katika fani ya sanaa Kauli Mbiu ikiwa ni Kilio cha Msanii .
Vikundi vingine vitakavyonesha vipaji vyao ni Kepteni  Shaibu, Tanzania Disabled, Uyoga Boga Village, Ndafu Arts Group, CGC, Magengistar Crew, Dodo Arts Group, Culture Arts Group, Wachapa Kazi Academy, Soweto Picture, Shiwata Commedy, Mwavionelachi, Manuari Arts Group, Tandale Morden Taarab na Begeja Wushu,
 Taalib alisema tamasha hilo ambalo limepata kibali cha Baraza la Sanaa la Taifa (BASATA) pia wamealikwa Shirikisho la Sanaa za Maonesho Tanzania,Shirikisho la Filamu Tanzania (TAFF),Shirikisho la Muziki Tanzania na Shirikisho la Sanaa za maonesho Tanzania.
Mwenyekiti aliwaomba viongozi wengine wa bendi za muziki, taarab, vikundi vya sanaa,mapromota,maprodusa na wadau wote kushiriki katika tamasha hilo ili kujenga ushirikiano wa pamoja.
Peter Mwenda 
Ofisa Habari wa SHIWATA
0715/0752-222677

Kampuni ya Issere yatoa msaada wa jezi


Mkurugenzi wa Masoko wa Kampuni ya Isere Sports, Abbas Ally Isere (kulia) akimkabidhi jezi seti moja mwakilishi, Dige Shaaban Nkusa kwa ajili ya timu ya vijana wa kijiji cha Mwembeni wilayani Kondoa ili kuimarisha michezo vijijini.

 

Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Isere Sports imetoa vifaa vya michezo vyenye thamani ya sh. mil. 1.7 kwa ajili ya kuendeleza vijana katika wilaya ya Kondoa.

Akikabidhi vifaa hivyo jana, Mkurugenzi wa Masoko wa Isere Sports, Abbas Isere alisema ametoa vifaa hivyo ili kuwasaidia vijana kupenda michezo ili kujenga afya na kujikinga na vitengo cha kihalifu.


 

Abbas alisema vifaa alivyotoa ni kwa ajili ya vijiji vya Changaa kwa Mafunchi ambako wamepewa jezi, mipira na soksi, katika kijiji cha Mwembeni kata ya Hondomairo wilayani Kondoa wamekabidhiwa vifaa kama hivyo.

Akipokea vifaa hivyo kwa niaba ya vijana wa Changaa, Issa Lubuva alisema umefika wakati kwa wananchi waishio mijini kuwakumbuka vijana waliobaki nyumbani kwa kuwapatia vifaa vya michezo.

Naye Dige Shaaban aliyepokea vifaa kwa niaba ya kijiji cha Mwembeni alisema wachezaji wengi wapo vijijini lakini hawajapata fursa ya kuonesha vipaji vyao hivyo vifaa hivyo vitasaidia kutoa wachezaji kutoka wilaya ya Kondoa.

Abajalo kuonyeshana kazi na Kariakoo Lindi leo RCL







Na Boniface Wambura
Raundi ya pili ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) inaendelea tena leo (Mei 26 mwaka huu) kwa mechi sita za kwanza zitakazochezwa katika miji sita tofauti.

Abajalo ya Dar es Salaam na Kariakoo ya Lindi zitaumana kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume, Dar es Salaam wakati Machava FC ya Kilimanjaro itakuwa mwenyeji wa Mpwapwa Stars ya Dodoma kwenye Uwanja wa Ushirika mjini Moshi.

Nayo Stand United FC ya Shinyanga itakuwa mgeni wa Magic Pressure ya Singida kwenye Uwanja wa Namfua mjini Singida huku Polisi Jamii ya Bunda mkoani Mara ikimenyana na Biharamulo FC ya Kagera kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma.

Mjini Kigoma kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika ni kati ya wenyeji Saigon FC na Katavi Warriors ya Katavi wakati Njombe Mji itaikaribisha Kimondo SC ya Mbeya kwenye Uwanja wa Sabasaba mjini Njombe.

Twiga Stars waingia kambini

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEg9qCbvL7ACfY-W273M78SjNwShyphenhyphento0pGY0jocv4YwPbT2si8HWRgx-R_CH50plR4aAhjyvtlT_RlMM3p55WStyP9sBPLbjbDHdB-_SW_dqsAbqS6oRTd0nBZTJOMDGRyTRgcDxKE7WB-Zm/s1600/Pix-1.jpg
Kikosi cha Twiga Stars

 
Na Boniface Wambura
KOCHA Mkuu wa timu ya Taifa ya wanawake ya mpira wa miguu (Twiga Stars), Rogasian Kaijage amewaita kambini wachezaji 30 ikiwa ni mwendelezo wa kuijenga na kuiimarisha timu hiyo.

Twiga Stars itakuwa na kambi ya siku kumi kuanzia Jumapili (Mei 26 mwaka huu) ambapo baadaye inatarajia kucheza mechi moja ya kirafiki kabla ya wachezaji kurudi kwenye klabu zao.

Kambi hiyo ni mwendelezo wa programu iliyopendekezwa na kocha kuijenga na kuiimarisha timu hiyo kwa vile haina mashindano mwaka huu, na itakuwa kambi ya pili baada ya ile iliyofanyika Machi mwaka huu.

Wachezaji walioitwa na klabu zao kwenye mabano ni Asha Rashid (Mburahati Queens), Aziza Mwadini (Zanzibar), Belina Julius (Lord Barden), Ester Chabruma (Sayari), Ester Mayala (TSC Academy), Eto Mlenzi (JKT), Evelyn Sekikubo (Mburahati Queens) na Fatuma Bushiri (Mburahati Queens).

Fatuma Hassan (Mburahati Queens), Fatuma Omari (Sayari), Flora Kayanda (Tanzanite), Hamisa Athuman (Marsh Academy), Hellen Peter (JKT), Maimuna Said (JKT), Mwajuma Abdallah (Tanzanite), Mwanahamisi Omari (Mburahati Queens), Mwanaidi Tamba (Mburahati Queens) na Mwapewa Mtumwa (Sayari).

Nabila Ahmed (Marsh Academy), Pulkeria Charaji (Sayari), Rehema Abdul (Lord Barden), Rukia Khamis (Uzuri Queens), Semeni Abeid (Tanzanite), Sharida Boniface (Makongo Sekondari), Sophia Mwasikili (Sayari), Therese Yona (TSC Academy), Vumilia Maarifa (Evergreen) na Zena Khamis (Mburahati Queens).

Miss Tabata 2013 waenda Mikumi



WASHIRIKI wa wa Dodoma Wine, Redd’s Miss Tabata 2013 leo wanatarajiwa kwenda kutembelea hifadhi ya taifa ya Mikumi.
Mratibu wa shindano hilo Godfrey Kalinga alisema warembo hao wataondoka na gari ya aina ya Toyota Double Coaster ikiwa na warembo 20 pamoja na walimu na viongozi wao.
Kalinga alisema ziara hiyo ina lengo la kukuza utalii wa ndani na kujenga ushirikiano miongoni mwao.
Alisema kuwa warembo hao pia watapata fursa ya kutembelea vivutio mbalimbali vilivyomo kwenye mbuga hiyo iliyoko mkoani Morogoro.
“Tutarudi Dar es Salaam Jumatatu kujiandaa na shindano letu litakalofanyika Ijumaa ijayo,” alisema Kalinga.
Kadhalika, Kalinga  alisema kuwa ziara hiyo imedhaminiwa na kampuni ya CXC Africa.
Shindano la kumsaka Miss Tabata  litafanyika Ijumaa ya Mei 31 katika ukumbi wa Da’ West Park, Tabata.
Wadhamini wa shindano hilo ni Nipashe, Redds, Dodoma Wine, Nipashe, Vayle Springs, Multichoice, Fredito Entertainment, Integrated Communications Limited, CXC Africa, Brake Point na Saluti5.
Warembo hao ni Madgalena Bhoke (21), Kabula Juma Kibogoti (20), Upendo Dickson Lema (22), Hidaya David Mwenda (22), Aneth Ndumbalo (19),  Dorice Mollel (22), Eunice Nkoha (19), Kazunde Musa Kitereja (19),  Rehema Kihinja (20),  Pasilida Mandali (21), Brath Chambia (23), Joaniter Kabunga (21), Recho Mushi (20),Caroline Sadiki (20) na  Suzan Daniel (18).
Anayeshikilia taji la Miss Tabata kwa sasa ni Noela Michael ambaye pia ni Miss Ilala.
Miss Tabata inaandaliwa na Bob Entertainment na Keen Arts.