STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, June 25, 2011

Dialo kutoka Bondeni ana tatu mpya




MSANII aliyewahi kufanya shughuli zake nchini Afrika Kusini, Zakaria Kazi Mkombozi maarufu kama Dialo, akishirikiana na bendi yake binafsi ameachia nyimbo tatu mpya ikiwa ni maandalizi ya kupakua albamu yao ya kwanza.
Akizungumza na mtandao huu, Dialo, alizitaja nyimbo hizo ambazo zimeanza kusambazwa kwenye vituo vya redio kuwa ni 'Sudan Risen' unaozungumzia hali ya kisiasa nchini Sudan, 'Madoda Mpela' uliombwa Kizulu na 'Let Do It'.
Dialo alisema nyimbo hizo ni kati ya nyimbo zitakazokuwa kwenye albamu yao ijayo ambayo bado hawajaipa jina, ila alisema itakuwa na nyimbo 10 zilizopo kwenye miondoko ya Reggae, Afro Pop na Ragga.
"Baada ya kuwa kimya tangu niliporejea nchini kutoka Afrika Kusini, nilipokuwa nafanya shughuli zangu za muziki, nimefanikiwa kuunda bendi ambayo tumeachia kazi tatu mpya ikiwa ni maandalizi ya kupakua albamu yetu ya kwanza," alisema.
Dialo alisema mbali na kuendesha bendi ya muziki, lakini pia ameanzisha klabu ya vijana kwa ajili ya kuwapa elimu ya stadi za maisha na kujiepusha na matumizi ya dawa za kulevya na kujikinga na ukimwi.
Alisema bendi yake ina jumla ya wasanii sita ambao ni yeye Dialo, Bob Chuwa, Dk Today, Alex, Katanga Junior (mdogo wa aliyekuwa mpiga dramu maarufu nchini, Gabby Katanga, ambaye kwa sasa ni marehemu, Yuzo na Amani.
Dialo, aliyewahi kufungwa kwa muda wa miaka mitatu nchini Afrika Kusini kwa kile alichodai kufanyiwa hila na watu aliokuwa akifanya nao kazi ya muziki nchini humo, alisema beni yao inatarajiwa kutumbuiza mjini Moshi siku ya Juni 17 mwaka huu.
Alisema onyesho hilo litafanyika kwenye ukumbi wa Glacian Sports Bar, ambapo mbali na kutambulisha nyimbo zao, lakini pia watapiga nyimbo za magwiji wengine wa muziki duniani kwa staili ya kukopi.
"Tumeanza kufanya maonyesho ambapo Juni 17 tulikuwa nyumbani Moshi, Kilimanjaro kwenye ukumbi wa Glacian Sports Bar," alisema.

Nisha: Wasanii tusiridhike mapema


MSANII anayekuja juu kwenye fani ya filamu nchini, Salma Jabu 'Nisha' amewataka wasanii wenzake kutoridhika na mafanikio ya kutamba nyumbani na badala yake kujibidiisha kujitangaza katika anga la kimataifa.
Nisha aliyeng'ara kwenye filamu kama 'Family Disaster', 'Better Day', 'Kimya' na nyinginezo, alisema kulewa sifa na mafanikio ya nyumbani kwa wasanii wengi nchini kunachangia wengi wao wasitambe kimataifa, kitu kinachopaswa wabadilike sasa.
"Wasanii nchini wanapaswa kubadilika na kujitangaza kimataifa, tusiridhike na mafanikio ya nyumbani kwani ndio yanatufanya tusipige hatua kubwa kimaendeleo kama wenzetu wa nje,' alisema Nisha, aliyejitumbukiza kwenye fani hiyo miaka mitatu iliyopita.
Nisha ambaye yupo mbioni kuibuka na filamu iitwayo 'Simu Sikioni' ya msanii nguli, Deo Shija, alisema hata yeye mwenyewe pamoja na nyota ya neema kuanza kumulikia kwa sasa nchini, hataridhika hadi atakaposimama kimataifa akichuana na wakali wa dunia katika fani hiyo.
"Ndoto zangu ni kutamba kimataifa kwa kuwa sitaridhika na mafanikio ya nyumbani, jambo ambalo kila msanii wa ukweli anatakiwa awe hivyo," alisema Nisha.
Mzanzibar huyo, alisema anaamini kama kila msanii atakuwa na kiu ya kutamba kimataifa ni wazi Tanzania itajitangaza na kutoa fursa ya Watanzania kutambulika kama ilivyo kwa Wanigeria, Wamarekani na wasanii wengine wanaotamba ulimwenguni.