STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, April 14, 2014

Idadi ya waliokufa kwa mafuriko yaongezeka

Baadhi ya nyumba zilizozungukwa na maji


IDADI ya waliokufa kutokana na mafuriko jijini Dar es Salaam imefikia watu 13 kufikia Jumatatu.
Mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam, Sadiq Meck Sadiq amesema idadi hiyo huenda ikaongezeka baada ya kupata taarifa za matukio ya mafuriko kutoka maeneo yote ya mkoa wa Dar es Salaam.
Kwa siku tatu mfululizo tangu Ijumaa iliyopita, mvua kubwa ziliendelea kunyesha na kusababisha madhara makubwa vikiwemo vifo, uharibifu wa miundombinu ya barabara na madaraja, hivyo kukata mawasiliano na mikoa ya jirani ya Pwani na Morogoro na hata ndani ya mkoa wenyewe. Karibu maeneo yote ya mkoa wa Dar es Salaam yameathirika kutokana na mvua kubwa zilizonyesha na kusababisha mafuriko, huku wakaazi wa maeneo ya mabondeni wakiathirika zaidi baada ya nyumba zao kujaa maji. Miundombinu ya barabara na madaraja mbalimbali yanayounganisha jiji la Dar es Salaam na vitongoji vyake pia imeharibiwa.
Picha ya Anga ya mafuriko jijini Dar
Mradi mwingine muhimu wa mabasi yaendayo kasi, DART unaolenga kutatua tatizo la usafiri jijini Dar es Salaam, nao umeathiriwa na mafuriko hayo ambapo magari, mashine na mifuko ya saruji imechukuliwa na maji hivyo kusitisha shughuli zake za ujenzi zilizo katika hatua za mwisho za kukamilisha mradi huo.
Shughuli za urejeshaji wa miundombinu zimekuwa zikiendelea ikiwa ni pamoja na matengenezo katika daraja la Mpiji linaloiunganisha mikoa ya Dar es Salaam na Pwani.
Hata hivyo Mamlaka ya Utabiri wa Hali ya Hewa Tanzania, TMA, yametahadharisha kuhusu kuendelea kunyesha kwa mvua na kuwataka watu wanaoishi katika maeneo hatarishi kuhama ili kusalimisha maisha na mali yao.
BBC

Kocha Azam kicheko kitupu baada ya ubingwa

Kocha Joseph Omog (kushoto) toka Cameroon akiwa na msaidizi wake
KOCHA Mcameroon, Joseph Marius Omog amefurahia ushindi wa jana wa mabao 2-1 dhidi ya wenyeji Mbeya City Uwanja wa Sokoine ulioihakikishia ubingwa wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara timu yake, Azam FC, lakini amewaambia wachezaji wake, pati ni baada ya mechi ya mwisho Aprili 19, mwaka huu.

“Ni furaha sana, tumepambana sana, haikuwa kazi nyepesi, tumepitia mechi ngumu tangu naanza kazi hapa, lakini tulibaki kwenye dhamira yetu na tukaendelea kupambana hatimaye tumetimiza malengo. Sote tuna furaha sasa, kila mtu ana sababu ya kufurahia kazi yake kati yetu,”alisema Omog.

Omog amewataka wachezaji wake kutobweteka na matokeo ya jana, na badala yake waelekeze nguvu zao katika mchezo wa Aprili 19, ili washinde na kukabidhiwa Kombe kwa furaha. 

“Nasikia Yanga walikata rufaa, hata kama haina maana, lakini lazima tushinde mechi ya mwisho, wachezaji wangu wanajua hilo, nimewaambia,”alisema.

Mabao ya Gaudence Mwaikimba na John Bocco ‘Adebayor’ kila kipindi jana yalitosha kuihakikishia Azam FC ubingwa wa Ligi Kuu Uwanja wa Sokoine mjini Mbeya dhidi ya bao la Mwagane Yeya.

Ushindi huo, umeifanya Azam ifikishe pointi 59 ikiwa na mchezo mmoja mkononi ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote baada ya mechi za mwisho Aprili 19, mwaka huu.

Nafasi ya pili tayari ni Yanga SC yenye pointi 55 sasa baada ya jana kuifunga JKT Oljoro 2-1 Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mjini Arusha ambayo kama itawafunga pia na Simba SC wiki ijayo itafikisha pointi 58, ambazo haziwezi pia kufikiwa na timu za chini
yake.

Azam FC itacheza mechi ya mwisho nyumbani, Uwanja wa Azam Complex, Chamazi nje kidogo ya Jiji la Dar es Salaam Jumamosi wiki hii, dhidi ya JKT Ruvu ikiwa na dhamira ya kushinda ili kuweka rekodi ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu bila kupoteza mechi.

Kikosi cha Azam kinaondoka leo Saa 10:00 mjini Mbeya kwa ndege kurejea Dar es Salaam na wachezaji watapewa mapumziko ya siku moja kabla ya kukutana kwa maandalizi ya mchezo wa kufungia pazia la msimu. 

LIWAZO ZITO

Rais JK naye amlilia Mzee Gurumo

Rais Jakaya Kikwete akimpongeza Mzee Gurumo enzi za uhai wake baada ya kumkabidhi tuzo maalum ya mchango wake kwa taifa kupitimia muziki
RAIS Jakaya Kikwete amemtumia salamu za rambirambi Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, Dk. Fenella Mukangara kutokana na kifo cha mwanamuziki maarufu na wa siku nyingi, Muhidini Gurumo kilichotokea juzi mjini Dar es Salaam.

Gurumo alifariki dunia jana katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH) alikokuwa amelazwa kwa matibabu ya ugonjwa wa moyo uliomsumbua kwa muda mrefu.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu, Rais Kikwete alisema mchango wa marehemu Gurumo kwa Taifa ni mkubwa na wa kupigiwa mfano kupitia kipaji alichojaaliwa na Mwenyezi Mungu ambacho alikitumia kikamilifu kwa manufaa ya wananchi na taifa kwa ujumla.

“Nimesikitishwa na kuhuzunishwa na taarifa za kifo cha Gurumo ambaye alikuwa mmoja wa wasanii wa muziki wa dansi nchini waliolitumikia Taifa hili kwa bidii tangu miaka ya sitini kupitia sanaa ya muziki,

Katika bendi mbalimbali za muziki wa dansi kuanzia Bendi ya NUTA Jazz, Mlimani Park Orchestra, Orchestra Safari Sound (OSS) na Msondo Ngoma ambayo ameitumikia hadi alipostaafu mwaka 2013,”alisema Rais Kikwete.

Rais Kikwete alimuomba Waziri wa Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo kumfikishia salamu zake za rambirambi na pole nyingi kwa familia ya marehemu Gurumo kwa kumpoteza kiongozi na mhimili wa familia yao.

Alisema anaungana na familia ya marehemu kuomboleza msiba huo mkubwa kwa kutambua kuwa msiba wao ni wa wote, na anamuomba Mwenyezi Mungu.

Aliwaomba wanafamilia ya marehemu kuwa na moyo wa uvumilivu na subira katika kipindi hiki kigumu cha kuomboleza msiba wa mpendwa wao kwa kutambua kwamba yote ni mapenzi ya mola.

Man City yapata pigo kwa Yaya Toure

KLABU ya Manchester City imepata pigo baada ya kufahamika kuwa huenda kiungo wake mahiri Yaya Toure asicheze tena msimu huu baada ya kuumia katika mchezo dhidi ya Liverpool uliochezwa mwishoni mwa wiki katika Uwanja wa Anfield. 
Nyota huyo wa kimataifa wa Ivory Coast alitolewa nje wakati wa kipindi kwanza na kusababisha hali kuwa mbaya kwa kikosi chake na kupelekea kufungwa mabao 3-2 na mahasimu wao hao katika mbio za ubingwa wa Ligi Kuu. 
Akihojiwa kuhusiana na hali ya nyota huyo, kocha wa City Manuel Pellegrini amesema itakuwa ngumu kwa mchezaji huyo kumaliza msimu huu. 
Toure alijiumiza mwenyewe baada ya kupiga shuti lililopaa katika mchezo huo wakati City wakijaribu kurejea baada ya kufungwa bao la kuongoza na Raheem Sterling.

Lyon yaidonyoa PSG kimoja Ufaransa

Mfungaji wa bao pekee la Lyon, Ferri (12) akipambana uwanjani dhidi ya PSG jana
MABINGWA watetezi wa Ligi ya Ufaransa, PSG jana ilionja kipigo chake cha kwanza baada ya mfululizo wa ushindi katika ligi hiyo kwa kudonyolewa goli 1-0 dhidi ya Olympique Lyon.
Ikicheza ugenini, PSG ilishindwa kufuruka kwa Lyon waliopata bao lao katika dakika ya 31 kupitia kwa Jordan Ferri.
Pamoja na kwamba kipigo hicho hakijaiteteresha matajiri hao wa Paris, lakini imefanya pengo la pointi baina ya wapinzani wanaowafukuzia kileleni, Monaco kuwa pointi 10 badala ya 13 ya awali baada ya Monaco kupata ushindi ugenini siku ya Jumamosi dhidi ya Rennes.
PSG imeendelea kusaliwa na pointi zake 79, huku Monaco wakiwa nafasi ya pili na pointi zao 69 huku timu zote zikiwa zimecheza michezo 33 na kusaliwa na mechi tano kabla ya kufungia msimu wa 2013-2014.

BASATA waomboleza kifo cha Gurumo


Mzee Gurumo enzi za uhai wake
BARAZA la Sanaa la Taifa (BASATA) limepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za msiba wa msanii nguli wa tasnia ya muziki wa Dansi nchini Muhidini Mwalimu Gurumo


“ Baraza limestushwa na kuhuzunishwa sana kutokana na taarifa ya kifo hiki cha Muhidini Maalimu Ngurumo ambaye mchango wake katika muziki wa dansi ni mkubwa mno na  unahitajika sana, pengo aliloliacha ni kubwa kwani ubunifu wake bado unahitajika katika tasnia hii.” 
Baraza linatoa pole kwa familia ya marehemu na wasanii wote nchini, aidha tunawatakia moyo wa subira katika wakati huu wa majonzi ya kuondokewa na mpendwa wetu.
Mwenyezi Mungu aipumzishe mahala pema peponi roho ya marehemu. Baraza liko pamoja na familia ya marehemu katika kipindi hiki kigumu cha majonzi.

Imetolewa na
Godfrey Mngereza
Kaimu Katibu Mtendaji

Baraza la Sanaa la taifa

Katibu Mkuu wa FIFA kutua Dar Mei 1

KATIBU MKUU WA FIFA KUFUNGUA SEMINA DAR
Katibu Mkuu wa FIFA

KATIBU Mkuu wa Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Jerome Valcke atawasili nchini Mei 1 mwaka huu ambapo atafungua semina ya mawasiliano itakayoshirikisha viongozi wa vyama wanachama wa Baraza la Vyama vya Mpira wa Miguu Afrika Mashariki na Kati (CECAFA).
 
Akizungumza Dar es Salaam leo (Aprili 14 mwaka huu), Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi amesema Valcke ambaye hii ni mara yake ya kwanza kuja Tanzania atafuatana na maofisa wengine wa saba wa FIFA.

Amesema semina hiyo iliyoandaliwa na FIFA itafanyika kwa siku mbili (Mei 1 na 2 mwaka huu) ambapo vilevile Valcke atapata fursa ya kuzungumza na waandishi wa habari wa ndani na wa kimataifa.

Rais Malinzi amesema washiriki wa semina hiyo ni marais, makatibu wakuu na wakuu wa mawasiliano wa wanachama 12 wa CECAFA ambao ni Burundi, Djibouti, Eritrea, Ethiopia, Kenya, Rwanda, Somali, Sudan, Sudan Kusini, Tanzania na Uganda.

Naye Mwenyekiti wa CECAFA, Leodegar Tenga ambaye alifuatana na Katibu Mkuu wake Nicholas Musonye amemshukuru Rais wa TFF kwa kukubali kuwa mwenyeji wa semina hiyo kwani itasaidia katika maendeleo ya mpira wa miguu katika ukanda huu

Bomu jingine lalipuka jijini Arusha

Kijana ambaye hakufahamika jina lake baada ya kupata majeraha makubwa mguuni.

Hali ya sintofahamu iliyowakumba wakazi wa jiji la Arusha baada ya bomu kulipuka jana.
Majeruhi baada ya bomu kulipuka.
Mmoja wa majeruhi akiwa hoi baada ya mlipuko.
Taarifa kutoka mjini Arusha zinasema bomu la kutengenezwa kwa mkono lililipuliwa jana usiku April 13 kwenye Baada iitwayo Arusha Night Park, iliyopo eneo la Mianzini jijin i Arusha na kusababisha watu kadhaa kujeruhiwa, huku taarifa zingine zikisema watu wawili wamepoteza maisha katika mlipuko huo kwamba ni watu 15 wamejeruhiwa kwenye mlipuko huo.
Inaelezwa watu 15 walithibitishwa kuumia katika mlipuko huo wa tatu kutokea mkoani humo kwa kipindi cha mwaka mmoja baada ya tukio la mlipuko kanisani na kwenye mkutano wa CHADEMA na kupelekea vifo vya watu kadhaa.
Inaelezwa wengi wa majeruhi katika mlipuko huo wa jana ni wahudumu wa baa hiyo pamoja na waliojitokeza kuangalia mpira kqwenye truninga na kwamba walikimbizwa hospitali za Mount Meru, Seliani na St. Elizabeth kwa ajili ya matibabu zaidi.

Mzee Gurumo kuagwa na kuzikwa kesho

Mzee Gurumo enzi za uhai wake akiwa na mkewe kipenzi, Pili bint Said Kitwana

Waombolezaji wakiwa wamekusanyika nyumbani kwa marehemu Muhidin Gurumo maeneo ya Mabibo Makuburi, Dar es Salaam.
Mke wa marehemu Gurumo (kulia) akifarijiwa na baadhi ya jamaa zake kwenye msiba wa mumewe nyumbani kwake Makuburi.
MWILI wa gwiji wa muziki wa dansi nchini, marehemu Muhidin Gurumo 'Mjomba' unatarajiwa kuagwa rasmi kesho kuanzia saa 2 asubuhi kabla ya kusafirishwa kijijini kwao Masaki kwa ajili ya maziko yatakayofanyika mchana.
Awali ilipangwa marehemu Gurumo aliyefariki jana katika hospitali ya Muhimbili azikwe leo, ila kwa kuzingatia wosia ulioachwa na kusisitizwa na gwiji huyo enzi za uhai kuwa,  asiharakishwe kuzikwa mapema familia imeamua kutii wosia huo.
Akizungumza na MICHARAZO nyumbani kwa marehemu Gurumo, Mabibo External, Msemaji wa familia, Yahya Mikole alisema mara kadha Mzee Gurumo alikuwa akiwasisitiza kuwa atakapokufa asizikwe kwa haraka.
Mikole ambaye ni mdogo binamu wa marehemu alisema, Mzee Gurumo alikuwa akimwambia kwa kuwa yeye ni mwanamuziki mkubwa na maarufu kuharakishwa kuzikwa kwake kunaweza kuwanyima wengine kumuaga au kuhudhuria maziko yake.
"Kwa kuzingatia hilo na ombo toka serikali, tumeamua kusogeza shughuli za mazishi ya merehemu kutoka leo mpaka kesho kwa utaratibu wa kuagwa kuanzia saa 2-4 asubuhi kabla ya kuondoka kwenda kumpumzisha kijijini kwao majira ya saa 7 mchana," alisema Mikole.
Msemaji huyo alieleza marehemu alikuwa akisumbuliwa na tatizo la mapafu na uigonjwa wa moyo na juzi kabla ya kifo chake alipatwa na tatizo la ukosefu wa damu ambapo alipofikishwa Muhimbili aliwekewa chupa tatu za damu.
"Tatizo la ukosefu wa damu lilijitokeza juzi na aliwekewa chupa tatu zilizoisha asubuhi ya jana kabla ya alasiri kupoteza maisha, huku akionekana mwenye afya yake ya kawaida kabisa," alisema Mikole.
Mikole alisema taratibu za mazishi ya marehemu zinaendelea kama kawaida nyumbani kwa marehemu.
Kwenye msiba huo watu mbalimbali wakiwamo wanamuziki wa zamani na walio wahi kufanya kazi na marehemu walihudhuria kama akina Juma Ubao, Mjusi Shemboza, Karama Regesu na wengine.
Marehemu Gurumo aliyezaliwa mwaka 1940 ameacha mjane mmoja na watoto sita, watatu wa kiume ambao ni Abdallah, Omar na Mwalimu na wa kike pia wakiwa watatu ambao ni Mariam, ambaye ndiye mtoto mkubwa wa marehemu, Mwazani na Kibibi aliye wa mwisho kuzaliwa.
Hata hivyo wakati wa uhai wake alipozungumza na Mmiliki wa blogu hii alisema ana watoto wanne, lakini Msemaji huyo wa familia alifafanua mzee Gurumo 'alichepuka' ila hakupenda kuzungumzia suala la watoto wake hao wengine japo wanafamilia wanawatambua na wameshajulishwa msiba huo.

Julio amlilia Mzee Gurumo

Jamhuri Kihwelu 'Julio'
KOCHA maarufu wa soka na mdau mkubwa wa bendi ya Msondo Ngoma, Jamhuri Kihwelu 'Julio' amemlilia nguli wa bendi hiyo, Muhidini Gurumo akidai kifo chake ni pigo kwa familia, wadau wa muziki na michezo nchini.
Julio aliyewahi kuichezea na kuinoa Simba kabla ya kutua Mwadui-Shinyanga na kukaribia kuipandisha Ligi Kuu, alisema kifo cha Gurumo kwake ni pigo kubwa kwani alikuwa ni mjomba wake mbali na unazi wao wa Simba na Msondo.
Alisema yeye binafsi ameumia sana kwa msiba wa mwanamuziki na mwanachama huyo wa Simba kama ambavyo wadau wa fani za muziki na michezo walivyoumizwa na kudai ni vigumu kupatikana wa kuziba pengo lake.
"Kwa hakika nimeumia kama walivyoumia wadau wa michezo na muziki kwani enzi za uhai wake, Gurumo alikuwa mwanachama wa Simba na pia ni gwiji wa muziki ambaye hakuwa na mfano wake katika kizazi chake," alisema Julio.
Julio, alisema marehemu Gurumo alikuwa mmoja wa watu wa mfano kwa kule kuipenda fani yake na kujali masilahi ya wanamuziki, mbali na kufanya kazi kwa umri mkubwa mpaka miezi michache alipotangaza kustaafu.
Alisema kustaafu na mwisho kufa kwake, kumeifanya krimu na safu ya mbele ya Msongo imetoweka baada ya kuondoka kwa Tx Moshi, Joseph Maina, Athuman Momba na Suleiman Mbwembwe.
"Itatuchukua muda mrefu kumsahau Mzee Gurumo, nakumbuka wakati anaumwa mara kwa mara nilikuwa namtembelea kumjulia hali na kutaniana naye sijui nitamtania nani tena, kwa kweli naumia..Mungu Amrehemu," alisema Julio.
Enzi za uhai wake Mzee Gurumo alikuwa mwanachama wa Simba na shabiki mkubwa wa Mabingwa watetezi wa England, Manchester United.
Chini ya uongozi wa akina Hassan Dalali, Mzee Gurumo aliwahi kuwapelekea wachezaji wa Simba wakiwa mazoezi matunda mbalimbali kutoka shambani mwake kwa nia ya kuboresha siha na afya zao kuonyesha unazi wake wa Simba.
Mzee Gurumo (74) alifariki Alasiri ya jana Muhimbili baada ya kuugua kwa muda mrefu maradhi ya Mapafu na ugonjwa wa Moyo na anatarajiwa kuzika leo kijijini kwao, Masaki wilaya ya Kisarawe, Pwani.

TFF yamlilia Josephat Magazi

SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limepokea kwa masikitiko kifo cha Mwenyekiti wa Chama cha Waamuzi wa Mpira wa Miguu (FRAT) Mkoa wa Singida, Josephat Magazi kilichotokea jana mkoani Kilimanjaro.
Magazi ambaye pia aliwahi kuwa mwamuzi na kamishna wa mechi za Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) na Ligi Daraja la Kwanza (FDL) alikuwa amelazwa katika Hospitali ya KCMC. Mazishi yatafanyika kesho (Aprili 15 mwaka huu) saa 5 asubuhi kwao Ushirombo mkoani Shinyanga.
Msiba huo ni mkubwa katika fani ya mpira wa miguu kwani kwa nyakati tofauti Magazi alishirikiana na TFF na wadau wengine wa mpira wa miguu katika masuala ya uamuzi na uongozi, hivyo mchango wake tutaukumbuka daima.
TFF tunatoa pole kwa familia ya marehemu Magazi, FRAT na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Singida (SHIREFA) na kuwataka kuwa na subira na uvumilivu katika kipindi hiki kigumu cha msiba huo mzito.
 
Bwana alitoa, Bwana ametwaa jina lake lihimidiwe. Amina