STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, October 8, 2013

Cheka kwenda kuhamasisha ngumi Muheza


BINGWA wa Dunia wa mchezo wa ngumibza kulipwa anayetambuliwa na WBF, Francis Cheka 'SMG' anatarajiwa kwenda kuhamasisha mchezo huo wilayani Muheza, Tanga kwa mwaliko wa kocha maarufu Charles Mhilu 'Spinks'.
Spinks aliiambia MICHARAZO kuwa Cheka ataenda kuhamamisha mchezo huo siku ya Eid El Hajj itakayoadhimishwa wiki ijayo wakati wa michezo kadhaa ya ngumi itakayofanyika kwenye viwanja vya Jitegemee, mjini humo.
Kocha huyo ambaye amekuwa akimnoa Cheka kwa nyakati tofauti alisema lengo la kumualika Cheka ni kutaka kuwahamasisha vijana wa wilaya hiyo na mkoa mzima wa Tanga katika mchezo huo.
"Sifa alizonazo katika mchezo huo ikizingatiwa ni hivi karibuni ametoka kumpiga Mmarekani na kunyakua ubingwa wa Dunia itasaidia kuwatia hamasa vijana wenye vipaji vya ngumi kujibidiisha kuwa kama yeye," alisema.
Spinks, alitoa wito kwa wadau wa ngumi kujitokeza kusaidia mchezo huo kwa lengo la kuufanya uwe na tija na kuwasaidia vijana wanaoucheza kuutumia kama ajira yao sambamba na kuliletea sifa taifa kama ilivyo kwa Cheka na wenzake.
Cheka hakuweza kupatikana kuthibitisha juu ya mualiko huo, kwa vile siku yake kutopatikana hewani pengine alikuwa darasani baada ya hivi karibuni kuanza masomo katika Shule ya St Joseph ya mjini Morogoro.


Cannavaro atamba Yanga kwenda kupata ushindi Kaitaba

Cannavaro (kushoto) akichuana na mchezaji wa Kagera Sugar ligi ya marudiano msimu uliopita
NAHODHA wa mabingwa watetezi wa Ligi Kuu Tanzania Bara ,Yanga Nadir  Haroub 'Cannavaro', amesema licha ya kutambua ugumu wa pambano lao lijalo dhidi ya Kagera Sugar, bado anaamini timu yake itaibuka na ushindi ugenini.
Yanga itasafiri hadi mjini Bukoba, mkoani Kagera kuvaana na Kagera Sugar siku ya Jumamosi kwenye uwanja wa Kaitaba katika moja ya mfululizo wa mechi za Ligi Kuu mwishoni mwa wiki hii.
Mabingwa hao watetezi wanaokamata nafasi ya pili kwa sasa katika msimamo huo, walichezea kichapo cha bao 1-0 katika mechi kama hiyo kwa msimu uliopita iliyochezwa Oktoba 8 na kuwa pambano pekee kupoteza kipindi chote hadi hivi karibuni walipolazwa na Azam katika ligi ya msimu huu.
Cannavaro, beki wa kati wa kutumianiwa wa Yanga anafahamu usumbufu wa wapinzani wao wanapokuwa uwanja wao wa Kaitaba, lakini alisema kwa namna kikosi chao kilichojipanga anaamini wanaenda Kagera kuvuna pointi tatu.
"Tunajua litakuwa pambano gumu na lenye upinzani mkali, lakini Yanga tutapigana kiume ili kushinda kuendeleza wimbi la ushindi tulilolianza," alisema.
Cannavaro anayeichezea pia timu ya taifa, alisema wachezaji wote wa Yanga wana ari kubwa ya kuisaidia timu yao kuendeleza ushindi baada ya awali kuchechemea kwa sare na kupoteza mchezo wao na Azam.
Yanga imepata ushindi mara mbili mfululizo dhidi ya timu za Ruvu Shooting na Mtibwa Sugar na kuwafanya wawasogelee watani zao, Simba wanaoongoza wakiwa na pointi 15, tatu pungufu na ilizonazo Yanga na JKT Ruvu.
Kivumbi cha ligi hiyo kinatarajiwa kuendelea tena kesho kwa michezo minne katika viwanja vinne tofauti ambapo Rhino Rangers itakuwa nyumbani mjini Tabora kuikaribisha Mbeya City kwenye uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, huku Oljoro JKT itaialika Ruvu Shooting kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid , Arusha.
Pambano jingine litazikutanisha Azam na Mgambo JKT zitakazoumana kwenye uwanja wa Chamazi na Mtibwa Sugar itakuwa nyumbani Manungu kuikaribisha JKT Ruvu.