STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, August 28, 2011

Timu ya Ngumi kuondoka leo mchana




TIMU ya taifa ya mchezo wa ngumi itakayoiwakilisha Tanzania kwenye michuano ya Michezo ya Afrika (All African Games) inatarajiwa kuondoka mchana huu kuelekea nchini Msumbiji, ikiwa na mabondia wanne pamoja na viongozi wawili.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Ngumi Tanzania, BFT, Makore Mashaga, aliiambia MICHARAZO kuwa, timu hiyo imelazimika kuwahia mapema kwenda Maputo, kutokana na kuwepo kwa mabadiliko ya kuanza kwa michuano hiyo kutoka Septemba 3 hadi Septemba 1.
Mashaga, alisema kikosi hicho kilitarajiwa kuondoka jana kwa ndege kikiwa na mabondia wanne na makocha wao wawili tayari kwenda kuwahi zoezi la upimaji afya litakalofanyika kesho (Agosti 30).
"Hapa ninapozungumza nawe nipo katika harakati za kukamilisha kuiwahisha timu uwanja wa ndege ili kuondoka kwenda Msumbiji, ambapo timu yetu itawakilisha na mabondia wanne na makocha wao wawili," alisema Mashaga.
Katibu huyo aliwataja mabondia hao kuwa ni Emilian Patrick atakayepigana uzani wa Feather, Martin Joseph (Middle) na Seleman Kidunda na Macmillian Patrick ambao watapigana uzito wa juu (kilo 91).
"Hao ndio mabondia watakaiwakilisha Tanzania baada ya kufanyika mchujo chini ya makocha, Hurtado Pimenter na msaidizi wake, ambao nao wapo kwenye msafara huo wa kwenda Msumbiji," alisema.
Mashaga alisema BFT ina imani kubwa kwa timu hiyo kufanya vema kama mabondia na makocha wao walivyowaahidi Watanzania kwamba wanaenda kushindana na sio kushiriki au kuwa wasindikizaji.
Mara ya mwisho Tanzania kufanya vema kwenye mashindano hayo kwa upande wa ngumi ilikuwa michuano ya mwaka 2007, yaliyofanyika nchini Algeria ambapo bondia Emilian Patrick aliambulia medali ya fedha.
Wakati huohuo timu ya taifa ya michezo ya Walemavu (Paralimpiki) yenye wachezaji watano inatarajiwa kuondoka Jumatano kwa ajili ya kushiriki michuano hiyo ya All African Games.
Timu zingine zitakazowakilisha Tanzania katika michezo hiyo ya 10 ya Afrika itakayofanyikia kwenye dimba la Zimpeto, mjini Maputo ni zile za Riadha, Netiboli na Soka ambazo zitaondoka pia Jumatano.

Mwisho

Villa yaapa kufa na Simba, yadai ushamba umeshawatoka




KLABU ya soka ya Villa Squad umedai 'ushamba' waliokuwa nao katika Ligi Kuu Tanzania Bara umeshawatoka na kuionya Simba isitarajie mteremko kwenye pambano lao lijalo.
Simba waliopo nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi hiyo nyuma ya Toto Afrika, itaikaribisha Villa katika pambano litakalochezwa Septemba 8, uwanja wa Mkwakwani, mjini Tanga.
Licha ya uongozi huo wa Villa, kukiri kuwa Simba ni timu nzuri, bado wanaionya kwamba isitarajie wepesi kutokana na kikosi chao kujipanga kuwakabili ili kushinda mchezo huo.
Makamu Mwenyekiti wa klabu hiyo, Ramadhani Uledi, alisema mapema leo asubuhi kuwa, kipigo cha mabao 3-0 walichopewa na Toto Afrika katika mechi yao ya awali iliwatoa ushamba na kwa sasa kikosi chao kimeanza kuizoea ligi hiyo na kuonyesha ushindani wa kweli.
Uledi, alisema kuthibitisha hilo waliweza kuibana Kagera Sugar nyumbani kwao na kutoka sare ya bao 1-1 , hali inayowafanya kujiamini wanaweza kuikabili timu yoyote ikiwemo Simba na Yanga.
"Aisee tunaendelea kujiandaa kwa ajili ya pambano letu na Simba, kifupi ni kwamba tumeshaanza kuizoea ligi na kwamba wapinzani wetu wasitarajie mteremko Mkwakwani, hiyo Septmba 8," alisema.
Aliongeza, benchi lao la ufundi linatumia mapumziko ya wiki moja ya ligi kuu kurekebisha matatizo yaliyotokea katika mechi za awali ili kuweza kuingia dimbani kuikabili Simba wakiwa fiti.
"Timu inaendelea kujifua na tuna imani mapumziko yaliyopo yatawapa nafasi makocha na wachezaji kuweka mambo sawa," alisema.
Uledi alisema wachezaji wao wawili waliokuwa majeruhi wameanza kupaata nafuu na kwamba hadi siku ya pambano hilo hali yao itakuwa imetengemaa na kurejea dimbani kuisaidia timu yao.
Klabu hiyo ya Villa Squad inayoshikilia mkia kwa sasa katika msimamo wa ligi hiyo ikiwa na pointi moja, ni miongoni mwa timu nne zilizopanda ligi kuu msimu huu, nyimngine zikiwa ni Coastal Union, JKT Oljoro na Moro United.

Mwisho