Na Suleiman Msuya
SERIKALI kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo imetoa wito kwa Wananchi ambao wanapendelea kuingia uwanja wa Taifa kushughudia michezo na shughuli zingine za kijamii wawe watunzaji wa rasilimali zilizopo katika uwanja huo.
Hayo yamesemwa na Msemaji wa Wizara hiyo Godblease Malisa wakati akizungumza na mwandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam.
Alisema ni vema kila mpenda michezo kuwa sehemu ya kulinda na kutunza uwanja huo kutokana na ukweli kuwa gharama kubwa zilitumika hadi kupatikana kwake.
Malisa alisema serikali inajitahidi kutunza na kuboresha huduma uwanja hapo ili kuhakikisha kuwa unakuwa wa salama na bora kwa muda wote ili vizazi vijavyo viweze kufaidika.
“Napenda kuwaomba wanamichezo na wasio wanamichezo kuutunza uwanja wetu wa Taifa ili uweze kudumu kwa muda mrefu pia ni vema tutambue kuwa uwanja huo ni wa gharama kubwa,” alisema.
Alisema lengo la Serikali ni kuhakikisha kuwa viwanja vya michezo vinakuwa bora na vinatumika wakati ote hali ambayo itakuwa ni sehemu ya kukuza michezo hapa nchini.
Msemaji huyo alisema uwanja mkubwa wa Taifa unahitahiji gharama kubwa za kuutunza hivyo ni vema kwa wadau ambao wanauomba kuutumia katika shughuli mbalimbali za kijamii.
Aidha Malisa aliwataka wananchi kutumia uwanja huo kwa shughuli mbalimbali kama za mikutano na sherehe za harusi kwani una kumbi za kutosha na nzuri kwani ni vigumu kwa uwanja huo kujiendasha kwa mapato ya mechi zinazochezwa.
Malisa alisema pamoja na uwanja wa Taifa pia Serikali inaendelea na maboresho ya uwanja wa Uhuru, ujenzi wa uwanja wa ndani, mabwawa ya kuogolea yenye viwango vya olimpiki na hosteli.