STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, June 21, 2013

Japhet Kaseba, Mada Maugo kumaliza ubishi Septemba 7

http://3.bp.blogspot.com/-ZeBz1lzEUVM/TauLfXKMzfI/AAAAAAAADnA/v3G_eDWihmI/s1600/7.JPG
Mada Maugo (kushoto) akichuana na Kaseba katika pambano lao la kwanza April 16, 2011
MABONDIA machachari wa ngumi za kulipwa wenye upinzani mkubwa nchini, Japhet Kaseba 'Champion' na Mada Maugo 'King maugo Jr' wanatarajiwa kuvaana Septemba 7 mwaka huu katika pambano la kumaliza ubishi baina yao litakalofanyika jijini Dar es Salaam.
Wanamasumbwi hao walipambana mara ya mwisho April 16, 2011 na Maugo kuibuka kidedea kwa TKO  ya raundi ya saba baada ya wapambe wa Kaseba kuingia ulingoni na kumvua bondia wao glovu ikiwa bado raundi moja kabla ya pambano hilo kumalizika.
Akizungumza na MICHARAZO hivi punde, Kaseba alisema pambano hilo litakuwa la kuwania taji lililo wazi la WBF kwenye ukumbi kati ya Diamond Jubilee au PTA na litasimamiwa na Shirikisho la Ngumi za Kulipwa Tanzania (PST).
Kaseba alisema anaamini pambano hilo ndilo litakalomaliza ubishi kati yake na Maugo baada ya kutoridhishwa na ushindi aliopewa walipoumana mara ya mwisho.
Bondia huyo aliyetoka kumnyuka Mmalawi, Rasco Simwanza kwa KO ametamba kuibuka na ushindi mbele ya Maugo ambaye kwa sasa yupo katika maandalizi ya kwenda Russia kuzipiga na mwenyeji wake Movsur Yusupov Julai 27 kwa sababu amebaini ili kumaliza ubishi ni lazima ashinde kwa KO kitu alichoanza kutumia sasa katika mapambano yake.
"Nimebaini ukimpiga mtu kwa KO hakuna malalamiko tofauti na kumaliza pambano na kushinda kwa pointi, hivuo Maugo ajiandae kukumbana na KO ya hatari kwa vile kiu yangu ni kutwaa ubingwa wa dunia kama nilivyofanya kwenye Kick Boxing," alisema Kaseba.
Maugo mwenyewe hakupatikana kueleza tambo hizo za mpinzani wake, ingawa imefahamika kuwa tayari kila kitu juu ya pambano hilo ikiwemo kusainishwa kwa mikataba kumeshafanyika.

Mbunge wa NCCR-Mageuzi ashambuliwa, wawili washikiliwa na Polisi

Mbunge wa Kasulu Mjini (NCCR), Moses Machali akiwa amelazwa wodini.
Akisiendelea kupata nafuu baada kushambuliwa.

Kamanda wa Polisi mkoani Dodoma,David Misime akizungumza na waandishi wa habari mjini humo jana kuhusu tukio la  Mbunge wa Kasulu Mjini (NCCR) Moses Machali kuvamiwa na vibaka eneo la Area E juzi usiku. 
 

Na. Jeshi la Polisi Dodoma.
DODOMA IJUMAA JUNI 21, 2013.  Jeshi la Polisi Mkoa Dodoma linawashikilia watu wawili kwa tuhuma za kumvamia na kumshambulia Mheshimiwa MOSES S/O MACHALI, miaka 31, Muha, Mbunge wa Kasulu Mjini kupitia NCCR – Mageuzi wakati anaelekea nyumbani kwake
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Jeshi la Polisi Bw. David. A. Misime  alisema Tukio hilo limetokea tarehe 20/06/2013 majira ya 19.00 hrs  katika eneo la Area ‘E’ katika Manispaa ya Dodoma
alikutana na vijana wanne (4) walikouwa amesimama katikati ya barabara akapiga honi lakini hawakupisha. Aliamua kuwauliza “Jamani mnasimama katikati ya barabara si nitawagonga?” Nao wakamjibu: “Wewe si unajifanya mtto wa Mbunge, tutakupiga sasa”. Alisisitiza Kamanda Misime
Kamanda Misime alisema Mheshimiwa alipojaribu kupita vijana hao walipiga gari lake. kitu ambacho kilimfanya  ashuke ili atazame kama gari hilo limepata uharibifu.wowote, ndipo vijana hao wakaanza kumshambulia kwa ngumi na mateke huku naye akijitahidi kujihami.
Hata hivyo Bw.Misime alisema,  walitokea vijana wawili (2) na kumsaidia. Mheshimiwa mbunge ambapo kijana mmoja kati ya waliokuwa wanamshambulia Mheshimiwa Machali ‘alimng’ata’ mgongoni kijana aliyekuwa anamsaidia Mheshimiwa Mbunge.
Bw. Misime alisema Watuhumiwa baada ya kuona wamezidiwa nguvu walitimua mbio. Ambapo pia Mheshimiwa Machali aligundua kuwa simu yake ya mkononi wameondoka nayo vijana hao.
Kamanda David. A. Misime alisema jeshi la Polisi mkoani Dodoma lilifanya  Msako mkali ulifanyika  usiku wa manane ambapo watuhumiwa wawili (2) walikamatwa ambao aliwataja kuwa ni JEREMIA  LAWRENT MKUDE@ JERRY, Miaka 18, Mkaguru Mkazi wa Chaduru, Manispaa ya Dodoma. aliyekutwa akiwa na jeraha usoni alilopata wakati anapambana na Mheshimiwa Mbunge na vijana waliokuwa wanamsaidia.
Kamanda huyo wa Polisi Mkoa wa Dododoma alimtaja mtuhumiwa mwingine anayeshikiliwa na jeshi la polisi kuwa  ni CHARLES  CHIKUMBILI, Miaka 22, Mkulima, Mkazi wa Swaswa, katika Manispaa ya Dodoma.
Kamishna Msaidizi  wa Jeshi la Polisi, Bw. David Misime alisema   askari walipowafanyia upekuzi wa mwili watuhumiwa usiku huo wa manane wamekutwa na misokoto miwili (2) ya bhangi.
MWISHO:
CONTACT:
POLISI MKOA WA DODOMA
DAWATI LA HABARI, ELIMU NA MAHUSIANO,
Phone:  0715 006523, Luppy Kung’alo – Mrakibu msaidizi wa Polisi (ASP)

Wanasoka Bora wa Mwaka SPUTANZA kufahamika kesho

CHAMA cha Wanasoka Tanzania (Sputanza), kesho kinatarajia kuwapatia tuzo wanasoka bora wa mwaka maarufu kama Sputanza Football Players Award katika hafla itakayofanyika kwenye Ukumbi wa Diamond Jubillee, jijini Dar es Salaam.

Katibu Mkuu wa chama hicho, Abeid Kasabalala alisema tuzo hizo zitatolewa kwa mwanasoka bora wa mwaka, mwanasoka bora chipukizi, kocha bora wa msimu na kipa bora.

Alisema tuzo hizo zinazodhaminiwa na Kampuni ya Kishen Enterprises Ltd zitakuwa zikitolewa kila mwaka kuwaongezea wachezaji ari uwanjani wakati wa mashindano mbalimbali ya ndani na nje ya nchi.

“Makocha na viongozi kutoka mikoa mbalimbali wanatarajia kuwasili kesho (leo) ambao kwa kushirikiana na Kamati ya Utendaji ya Sputanza, watafanya uteuzi wa washindi kwa kutumia vigezo vilivyopo,” alisema Kasabalala.

Aliongeza kuwa katika tuzo hizo, pia watatoa vyeti vya kuwakumbuka na kuwapongeza wachezaji wa zamani waliochezea timu ya taifa miaka ya nyuma ambapo alisema kiingilio kitakuwa sh 10,000 na sh 50,000.

Golden Bush kupimana ubavu wenyewe mbele ya wakala wa kimataifa

Baadhi ya wachezaji wa timu ya Golden Bush Veterani
TIMU za soka za Golden Bush Fc inayoshiriki Ligi Daraja la Nne wilaya ya Kinondoni na Golden Bush Veterani asubuhi ya kesho zinatarajiwa kumenyana katika pambano la kirafiki huku wakishuhudiwa na wakala wa soka kutoka Msumbiji, Ashraf ambaye atakuwa na kazi ya kuangalia vijana wa kuondoka nao.
Kwa mujibu wa msemaji na mlezi wa timu hizo Onesmo Waziri 'Ticotico' pambano hilo litachezwa saa 1:30 asubuhi kwenye uwanja wa Kinesi maarufu kama St James Park, huku wakala huyo aliyekuwa kusaka wachezaji wa kwenda kucheza soka la kulipwa nchini kwao atakuwa na akishuhudia pambano hilo.
Ticotico alisema tayari mmoja wa wachezaji wa kikosi cha vijana wanaoongoza kwenye msimamo wa kundi lao katika ligi wanayoshiriki wakiwa na pointi 12 kwa michezo minne bila kupoteza wala kutoa sare mechi yoyote, lakini alikuwa akipenda kuwaangalia vijana vizuri kabla ya kuondoka na vijana watakaomkuna kisoka.
"Kesho uwanja wa Kinesi (st James park) utakuwa moto ambapo timu hizo mbili zitaumana kuanzia saa moja na robo asubuhi. Game hii itakuwa kipimo tosha kwa wazee ambao watakuwa wanafanya maandilizi ya mwisho kabla ya bonanza la Pugu siku ya jumapili week hii ambapo Golden Bush tumepata mwaliko maalum na Mbunge wa Ukonga Mama Mwaiposa," alisema.
Ticotico alisema pambano hilo litachezeshwa na mwamuzi Fred Mazuni badala ya waamuzi waliozoeleka katika mechi za timu hizo, Madaraka Seleman 'Mzee wa Kiminyio' au Ally Mayay.
Katika mechi mbili baina ya timu hizo Wazee walinyanyaswa kwa vipigo mfululizo, jambo ambalo ndilo limefanya abadilishwe  mwamuzi kwa hisia kwamba Babu Mada na Mayay wamekuwa wakiibeba timu ya vijana ambao ni viongozi na makocha wao.

Uhuru Seleman athibitishia kutua Coastal Union


KIUNGO mchezeshaji wa aliyekuwa akiichezea Azam kwa mkopo kutoka Simba, Uhuru Seleman ametua Coastal Union ya Tanga pia kwa mkopo kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Uhuru aliithibitishia MICHARAZO kwamba ametua Coastal kwa ajili ya ligi ijayo na kwamba anajifua vilivyo ili kuwapa raha mashabiki wa klabu hiyo aliyowahi kuichezea msimu wa 2007-2008 na kufikia kuzigombanisha Simba na Coastal wakimgombea kila mmoja alipodai ni mchezaji wake.
Kiungo huyo ambaye amewahi pia kutamba na Mtibwa Sugar, alisema amefurahi kutua Coastal kwa kuamini atapata nafasi nzuri ya kuonyesha kipaji chake baada ya kushindwa kupata fursa hiyo ndani ya Simba na hata Azam walipomchukua msimu uliopita.
"Ni kweli nimetua Coastal kwa mkopo na najiandaa kuichezea kwa msimu ujao, nimefurahi kwa sababu naamini nitarejesha makali yangu," alisema Uhuru.
Uongozi wa Coastal kupitia Mkurugenzi wake wa Ufundi, Nassor Binslum amethibitisha suala la kumnyakua kiungo huyo akidai wamezungumza na Simba ili wamchukue kwa mkopo na watasaidiana nao kulipa mshahara wa mchezaji huyo wakati akiichezea timu yao ambayo ilimaliza msimu wa ligi iliyopita katika nafasi ya 6.
Mabingwa hao wa zamani wa kandanda nchini mbali na kumnyakua Uhuru pia imewanasa wachezaji wengine wapya katika kukiimarisha kikosi chao baadhi yao ni beki Juma Nyosso na Haruna Moshi (wote Simba), Kenneth Masumbuko toka Polisi-Moro, Marcus Ndeheli na Said Lubawa (JKT Oljoro) na Abdallah Ally kutoka visiwani Zanzibar.

Juma Seif Kijiko atua Ruvu Shooting, wa5 watupiwa virago

Juma Seif Kijiko aliyesajiliwa Ruvu Shooting Stars
KIUNGO wa zamani wa Yanga aliyekuwa akiichezea African Lyon katika Ligi Kuu iliyoisha hivi karibuni, Juma Seif Dion 'Kijiko' ametua Ruvu Shooting kwa mkataba wa miaka miwili.
Kwa mujibu wa Msemaji wa Ruvu Shooting, Masau Bwire, Kijiko alisaini mkataba huo jana tayari kuichezea timu yao kwa msimu ujao.
Bwire alisema Kijiko anakuwa mchezaji wa tano kusajiliwa na timu yao baada ya kuwanyakua Cosmas Ader kutoka Azam, Elias Maguli (Prisons-Mbeya), Juma Nade (Kagera Sugar) na Jerome Lembeli toka Ashanti United.
Aidha Bwire alisema klabu yao imewatema kikosini wachezaji watano kwa sababu mbalimbali ikiwemo kushuka viwango na kuwataja kuwa ni Paul Ndauka,  Charles Nobert, Gido Chawala, Frank Mabande na Liberatus  Manyasi.
"Tumemsajili kiungo wa zamani wa Yanga, Juma Kijiko aliyeichezea Lyon msimu uliopita na pia tumewaacha wachezaji wetu watano kwa sababu mbalimbali na kikosi chertu kitaanza kujifua kwa msimu ujao kuanzia Juni 24," alisema Bwire.
Bwire aliwataka wachezaji wote wa timu hiyo kuhudhuria mazoezi hayo yatakayokuwa chini ya kocha wao Charles Boniface Mkwasa.

Nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa wa Mkoa kutimkia wikiendi hii


Na Boniface Wambura
TIMU nne zimefuzu kucheza hatua ya nne (nusu fainali) ya Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL) baada ya kushinda mechi zao za hatua ya tatu ya michuano hiyo itakayotoa washindi watatu watakaocheza Ligi Daraja la Kwanza (FDL) msimu ujao.

Katika hatua hiyo Polisi Jamii ya Mara itaikaribisha Kimondo SC ya Mbeya kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume mjini Musoma wakati Stand United FC ya Shinyanga itakuwa mgeni wa Friends Rangers ya Dar es Salaam kwenye Uwanja wa Azam Chamazi.

Mechi za kwanza zitachezwa Juni 23 mwaka huu wakati zile za marudiano zitafanyika kwenye viwanja vya Sokoine jijini Mbeya na Kambarage mjini Shinyanga, Juni 30 mwaka huu.

Kwenye hatua ya tatu ya RCL, Friends Rangers iliing’oa Kariakoo ya Lindi kwa jumla ya mabao 2-0, Stand United FC ikaitoa Machava FC ya Kilimanjaro kwa mabao 2-1, Kimondo SC ikaishinda Njombe Mji mabao 6-5 wakati Polisi Jamii iliitambia Katavi Warriors kwa mabao 7-6.

Hatua ya mwisho ya ligi hiyo itachezwa Julai 3 mwaka huu kwa mechi za kwanza wakati zile za marudiano zitakuwa Julai 7 mwaka huu.

Kim Poulsen amtema Pazi, amuita Luhende Stars

Kocha wa Taifa Stars, Kimm Poulsen
Na Boniface Wambura
BEKI wa Yanga, David Luhende ameongezwa kwenye kikosi cha Taifa Stars kwa ajili ya mechi dhidi ya Uganda (The Cranes) kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa Wachezaji wa Ligi za Ndani (CHAN) zitakazofanyika mwakani nchini Afrika Kusini.

Kocha Kim Poulsen amesema kutokana na uamuzi huo wa kumuongeza beki huyo wa kushoto amemuondoa mchezaji mmoja kwenye kikosi chake. Mchezaji huyo ni mshambuliaji Zahoro Pazi wa JKT Ruvu.

Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager sasa itaingia kambini kwenye hoteli ya Tansoma jijini Dar es Salaam, Julai 3 mwaka huu badala ya Julai 4 mwaka huu kama ilivyokuwa imepangwa awali.

Mechi ya Uganda itachezwa Julai 13 mwaka huu, saa 9 kamili alasiri kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati ile ya marudiano itachezwa wiki mbili baadaye jijini Kampala, Uganda.

Wachezaji wanaotakiwa kambini ni Aggrey Morris (Azam), Aishi Manula (Azam), Ally Mustafa (Yanga), Amri Kiemba (Simba), Athuman Idd (Yanga), Frank Domayo (Yanga), Haruni Chanongo (Simba), John Bocco (Azam), Juma Kaseja (Simba), Juma Liuzio (Mtibwa Sugar) na Kelvin Yondani (Yanga).

Wengine ni Khamis Mcha (Azam), Mrisho Ngasa (Simba), Mudathiri Yahya (Azam), Mwadini Ali (Azam), Mwinyi Kazimoto (Simba), Nadir Haroub (Yanga), Salum Abubakar (Azam), Shomari Kapombe (Simba), Simon Msuva (Yanga) na Vincent Barnabas (Mtibwa Sugar).

Chid Benz kushiriki miaka 13 ya Kikosi leo New Msasani Club

 https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEgsRmvXwbSJaHszeaIBlQllQfjJ7Zmu0z3OF6Tw9tQQzPJDPSzOZCFLwHxcHfXfoKxRPCsvzqnvRsKNHB5kzFNa0y595Ct7WWWKOJBuzZNNjd1eyOTfa00aYb4X-axVtADtpB7ybdvnw5M/s400/KIKOSI.jpg
WAKATI maadhimisho ya miaka 13 ya Kikosi cha Mizinga inatarajiwa kufanyika leo kwenye ukumbi wa New Msasani Club, kiongozi wa kundi hilo, Karama Masoud 'Kalapina' amefichua kumaliza 'bifu' lake na Chid Benz na kumtangaza kwamba ni miongoni mwa wasanii watakaonegesha onyesho hilo kabambe.
Aidha Kalapina amesema kuwa makundi na msanii yeyote ambaye angependa kujitokeza kushiriki katika show yao hata kama siyo kwa kupanda jukwaani anawakaribisha kwa nia ya kufanikisha maadhimisho hayo na pia kutangaza Amani na Upendo Tanzania.
Akizungumza mapema asubuhi hii, Kalapina alisema Chid Benz naye atakuwepo katika show yao, licha ya kwamba mapema mwezi uliiopita walitibuana baada ya Benz kuvamia shoo ya Kikosi na kulazimika kutimuliwa jukwaani kitemi na kuibua hisia kwamba 'vita' ya wawili hao imeanza.
Hata hivyo, Kalapina alisema kwa sasa kikosi wamekuwa na hivuo wamezika tofauti zao za zamani na kuamua kufanya kazi baada ya kutumia muda mwingi kufanya harakati za kuisimamisha hop hop Bongo ambapo ilikuwa ikipata vikwazo vingi kiasi cha kutotangazika licha ya msaada mkubwa kwa jamii.
"Tumeshakuwa, mambo ya ubabe na kila lililokuwa likiwaudhi watu kwa sasa bhaaas, ndiyo maana Chid mdogo weangu nimemualika na pia naruhusu makundi yote yanayotuunga mkono na wasanii wengine waje ukumbini kutuopa sapoti kwa nia ya kutangaza amani na upendo kupitia tamasha hili la leo," alisema.
Kikosi cha Mizinga kitafanya onyesho hili likisindikizwa na wasanii kibao nyota nchini akiwemo 'Dume la Simba' Afande Sele, Manzese Crew, gangwe Mob, Mansu-Lee, Stereo, Nikki Mbishi, Young Killer na wengine huku kukiwa na maonyesho mbalimbali yenye utamaduni wa hip hop kama uchoraji kudance n.k.

Kocha Patrick Liewig aipa Simba siku 4

http://in2eastafrica.net/wp-content/uploads/2012/12/Patrick-Liewig.jpg
Kocha wa zamani wa Simba, Patrick Liewig
ALIYEKUWA kocha mkuu wa klabu ya Simba, Patrick Liewig, ameipa klabu hiyo siku nne kuhakikisha kuwa wanamlipa madai yake kabla hajamtaka mwanasheria wake kuwashtaki ifikapo Jumatatu.
Liewig aliyechukua mikoba ya kuifundisha Simba baada ya Mserbia Milovan Cirkovic, aliliambia gazeti hili kuwa anadai kiasi cha dola za Marekani 26,000 (Sh. milioni 42).
Akizungumza na NIPASHE jana, Liewig, alisema kwamba amemueleza Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili, Hanspoppe Zacharia, kuwa anahitaji kupewa haki yake hiyo ili arejee kwao na hapendi kuona anabaki nchini wakati hana kazi.
Liewig alisema kuwa anashangazwa kuona Simba wakishindwa kumpa taarifa za kusitishwa kwa mkataba wake kwa maandishi na kumuacha arejee nchini.
"Nilianza kusikia kwamba Simba hainihitaji mapema, hata waandishi walipenda kuniuliza hatma yangu kila mara Simba ilipokuwa inapoteza mechi... kumbe walitaka niamke na kujua kuwa nafasi yangu ndani ya klabu ni ndogo," alisema kocha huyo.
Aliongeza kuwa hivi sasa anasubiri kukutana na Hanspoppe ili ajue malipo yake yatakavyokuwa na haamini hata kidogo kuwa klabu hiyo itatekeleza madai yake baada ya kuondoka nchini.
"Napenda haki zangu nizipate sasa ili tumalizane kwa amani. Si tabia njema kufikisha malalamiko CAF (Shirikisho la Soka la Afrika) au FIFA (Shirikisho la Soka la Kimataifa)," aliongeza kocha huyo.
Simba iliamua kuachana na Liewig baada ya timu yake kushindwa kutetea ubingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara na mwishowe kumrejesha kocha na mchezaji wao wa zamani, Abdallah Kibaden 'King'.
Hata hivyo, ni uongozi wa Simba ndiyo uliokuwa ukiunga mkono uamuzi wa kutowachezesha baadhi ya nyota wao wenye majina makubwa kama Haruna Moshi 'Boban' na Juma Nyosso na kuwachezesha zaidi yosso wao kuelekea mwishoni mwa msimu na mwishowe kujikuta wakipoteza ubingwa mapema.
Liewig anaidai Simba fedha za mshahara wake wa mwezi Aprili na Mei mwaka huu ambao ni dola za Marekani 14,000 (Sh. milioni 14) na kingine kilichobakia kinatokana na makubaliano ya kuvunja mkataba wao uliopaswa kumalizika mwishoni mwa mwezi huu.
Hanspoppe alikiri kuwa Simba inadaiwa na kocha huyo na kueleza kwamba klabu inasaka fedha kutoka kwa wadau wake ili kuhakikisha wanalipa madeni yote kabla ya kuanza kwa msimu mpya .
Mapema mwaka hii mmoja wa wanachama wa Simba, Rahma Al Kharoos, aliokoa jahazi kwa kumlipa Milovan madai yake baada ya kutimuliwa kama ilivyo sasa kwa Liewig.

Chanzo:NIPASHE

Mabondia wa Tanzania wafungwa Mauritius kwa dawa za kulevya



Mabondia waliohukumiwa

Mabondia wanne wa Tanzania wafungwa miaka 15 jela nchini Mauritius kwa makosa ya kuingiza dawa za kulevya aina ya heroin.

Mabondia hao ni Case Ramadhani Fills, Nathanael Elia Charles, Ally Rajabu Msengwa na Petro Charles Mtagwa.

Wakati kesi hiyo ilipoanza kusikilizwa, wote walikiri makosa ya kuingiza mihadarati hiyo nchini Mauritius wakati walipokwenda kushiriki mashindano ya ndondi barani Afrika mwaka 2008.
Wakiwa mbele ya Jaji, waliiambia mahakama kuwa walilazimika kuingia katika biashara hiyo haramu kutokana na hali zao za maisha kuwa maskini.
"Tunaomba radhi kwa taifa la Mauritius", waliiambia mahakama.
"Tu watu maskini na tunategemewa na familia, watoto na wazee wetu wanaotugemea."
"Kwa dawa hizi tungepata kiasi cha Pauni £4,000". walisema
Jaji Benjamin Marie Joseph alisema katika kutoa adhabu hiyo yote hayo ameyafikiria, kwani walitoa ushirikiano mzuri wakati wote wa uchunguzi wa kesi hiyo, kulikowezesha hata wafanyabiashara hiyo, raia wa Mauritius kukamatwa.
Wamekuwa mahabusu kwa siku 1,722, sawa na miaka miatano, hivyo watatumikia miaka kumi iliyobakia jela. Pia watatakiwa kulipa faini ya pauni £1,600 na gharama nyingine za uendeshaji wa kesi hiyo.
Kwa mujibu wa mwandishi wa habari wa BBC nchini Mauritius Yasine Mohabuth in Mauritius, Jaji aliwashutumu kwa kuukosea umma wa Mauritius kwa kuingiza dawa hizo za kulevya aina ya heroin.
Mabondia hao waliwasili Mauritius tarehe 10 Juni 2008 na kuweza kupita uwanja wa ndege bila kunaswa hadi walipokamatwa katika hoteli waliyofikia ya Quatre Bornes.
Kwa pamoja walimeza gram 4639.04 za heroin zikiwa katika vifuko 358 vijulikavyo kama pipi.

BBC