STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 30, 2011

Msondo yaingia studio kurekodi albamu mpya



BENDI kongwe ya Msondo Ngoma, mapema leo asubuhi imeingia studio kurekodi kibao kipya kiitwacho 'Suluhu', ikiwa ni maandalizi ya upakuaji wa albamu yao mpya.
Mmoja wa viongozi wa bendi hiyo, Shaaban Dede, aliiambia MICHARAZO kuwa, nyimbo zao mpya zitarekodiwa katika studio za Fabreas Records na kwa kuanza leo anarekodi kibao cha 'Suluhu', ambacho amekitunga yeye.
Dede, alisema mara baada ya kibao hicho kurekodiwa kitasambazwa kwenye vituo vya redio kwa nia ya kukitambulisha huku, bendi yao ikiendelea kumalizia nyimbo nyingine tano zilizosalia.
"Tumeingia leo studio kwa Fabreas kwa lengo la kufyatua kibao cha Suluhu na vingine kwa ajili ya albamu yetu mpya ijayo," alisema Dede.
Alisema nyimbo nyingine za albamu hiyo ambazo zimeshakamilika ni 'Dawa ya Deni', 'Lipi Jema', 'Kwa Mjomba Hakuna Urithi', 'Baba Kibene' na 'Nadhiri ya Mapenzi'.
"Nadhani muda si mrefu mashabiki wetu na wale wa muziki kwa ujumla wataipata albamu yetu, kwani tutakuwa tukidondosha wimbo mmoja mmoja, kabla ya kuikamilisha na kuiachia mtaani, kabla ya kumalizika mwaka huu," alisema.
Msondo Ngoma imekuwa na desturi ya kutoa albamu kila mwaka, ila kwa mwaka jana haikuachia kazi yoyote, albamu yao ya mwisho ni ile ya mwaka juzi iitwayo 'Huna Shukrani'.

Siwezi kuchojoa nguo nicheze X-Skyner



MSANII wa filamu anayekuja juu nchini, Skyner Ally, amesema hata apewe kiasi gani cha fedha hawezi kucheza picha za watu wazima 'X' kwa madai kufanya hivyo mbali na kujidhalilisha, pia ni kwenda kinyume na mafundisho ya Mungu.
Akizungumza na MICHARAZO, Skyner, alisema ingawa yupo ndani ya fani ya uigizaji kwa nia ya kusaka fedha, lakini hayupo tayari kujivua utu wake, ili akubali kuchojoa nguo na kuigiza filamu za X.
Skyner, alisema anaamini kucheza filamu za namna hiyo ni kwenda kinyume na maadili na kukiuka mafundisho ya dini, mbali na yeye mwenyewe kujidhalilisha mbele ya jamii.
"Ingawa nasaka fedha kupitia kipaji cha uigizaji nilichonacho, lakini siwezi kukubali kucheza filamu za X hata nikiahidiwa kiasi gani cha fedha," alisema.
Kisura huyo, anayetamba kwenye filamu kama 'The Second Wife', 'Unpredictable', 'What is It', 'I hate My Birthday', 'Why I Did Love', 'Kizungumkuti' na nyinginezo, alisema kuwa msanii hakuna maana kujirahisisha na kufanya mtendo machafu, jambo alilolata wasanii wenzake kuepukana nayo ili kulinda heshima zao na fani zao kwa ujumla.
"Wasanii lazima tujiheshimu na kujithamini, kujiingiza kwenye skendo na matendo machafu ndiyo yanayotufanya tusiheshimike na kuichafua fani nzima ya sanaa, wakati imekuwa ikitusaidia baadhi yetu kumudu maisha na kuzisaidia familia zetu," alisema.
Skyner, anayetarajiwa kuolewa wiki ijayo, alisema wasanii wakijiheshimu na kuepuka skendo ni wazi jamii itawapenda na kuwathamini, hasa kama watajibidiisha kuboresha kazi zao.

Yanga sasa roho kwatu!


USHINDI mnono wa mabao 5-0 iliyopata kwa Coastal Union, umewafanya wadau wa klabu ya Yanga kuchekelea wakisisitiza kuwa hawana hofu ya kutetea taji lao msimu huu.
Yanga iliyokuwa ikichechemea katika ligi hiyo, iliishindilia Coastal mabao hayo katika pambano lilkilochezwa uwanja wa Taifa, na kuipandisha mabingwa watetezi hao hadi kwenye nafasi ya nne nyuma ya timu za Simba, Azam na JKT Oljoro zilizoitangulia.
Afisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu, alisema wanaamini ushindi waliopata kwa Wagosi wa Kaya ni salamu kwa watani zao na timu nyingine zilizokuwa zikiikejeli timu yao ilipoanza kwa kusuasua katika ligi hiyo.
Sendeu, alisema tangu awali walikuwa wakisisitiza kuwa, ligi bado mbichi na vigumu watu kuitabiria Yanga kwamba haiwezi kufurukuta msimu huu, bahati nzuri imethibitika kwa ushindi mfululizo ambao umewafanya wapinzani wao kuanza 'kuhema'.
Alisema anaamini mapumziko ya ligi kupisha pambano la Stars na Morocco itatumiwa vema na benchi lao la ufundi pamoja na wachezaji wao kuhakikisha wakirejea dimbani wanakuwa moto zaidi, ili kumaliza duru la kwanza katika nafasi stahiki.
"Nadhani waliokuwa wakitukejeli kwamba tumefulia, salama wamezipata na ninajua huko walipo presha zimeshaanza kuwapata, tunaombea tuendelee na mwendo huu huu ili tumalize duru la kwanza katika nafasi mbili za juu na kujiweka vema kulitetea taji letu," alisema.
Nao baadhi ya wadau wa klabu hiyo, wamedai pamoja na kuanza kuonyesha mwanga kwa timu yao, bado wachezaji hawapaswi kubweteka na badala yake waongeze juhudi ili kumaliza meechi tano zilizosalia kwa mafanikio.
"Tumefurahi mafanikio ya timu yetu, lakini naomba wachezaji na viuongozi wasibweteke, tuendelee kushinda mechi zijazo ikiwemo ile ya Simba Oktoba 29, ili turejeshe heshima yetu iliyopotea kwa matokeo mabaya ya mechi za awali," alisema Ramadhani Kampira.
Yanga kabla ya kuvaana na Simba katika pambano linalosubiriwa kwa hamu, itacheza na timu za Kagera Sugar, Toto Afrika na JKT Oljoro kabla ya kufunga dimba la duru la pili kwa kuumana na Polisi Dodoma mjini Dodoma Novemba 5.

Stewart ruksa kuinoa Zanzibar Heroes


UONGOZI wa klabu ya soka ya Azam, umekubali kwa moyo mmoja uteuzi wa kocha wao mkuu, Stewart Hall, kuinoa timu ya taifa ya Zanzibar, Zanzibar Heroes kwa ajili ya michuano ya Kombe la Chalanji itakayofanyika Novemba, jijini Dar es Salaam.
Chama cha Soka Visiwani Zanzibar, ZFA, kilimtangaza Stewart kuwa ndiye atakayeinoa timu hiyo katika michuano hiyo, ikiwa ni mara ya pili kwa kocha huyo kupewa kibarua hicho cha kuinoa Zanzibar Heroes.
Katibu Mkuu wa Azam, Nassor Idrissa 'Father', alisema uongozi wao, hauna tatizo la kocha wao kwenda kuinoa Zanzibar Heroes, kutokana na ukweli kwa namna moja ni faida kwa Azam ambayo hutoa wachezaji wengi katika kikosi cha timu hiyo.
Idrissa, alisema pia kocha huyo ataenda kuinoa timu hiyo wakati klabu yao itakuwa imeshawapa likizo wachezaji wao kwa ajili ya mapumziko marefu kabla ya kuanza kwa duru la pili la ligi hiyo mapema mwakani.
Katibu huyo alisema pia ni vigumu kwa Azam kumzuia kocha huyo kwenda kutekeleza jukumu lake kwa timu ya taifa, ambayo ni sehemu ya Muungano wa Tanzania, labda kama angeteuliwa kwenda kuinoa Kenya au Uganda ndio wangweka pingamizi.
"Angekuwa ameteuliwa kuinoa Kenya au Uganda, hapo ingekuwa vigumu kumruhusu lakini kama ni Zanzibar au hata kama ingekuwa Tanzania Bara, tungemruhusu kwa vile ni faida kwa maendeleo ya soka letu, kwani Stewart ni kocha mzuri," alisema.
ZFA, ilisema kocha huyo angeungana na timu hiyo ya taifa, Novemba 10, siku tano baada ya duru la kwanza la ligi kuu kumalizika.
Kabla ya kutua Azam, Stewart anayetokea Uingereza aliletwa nchini kuinoa timu hiyo ya Zanzibar kupitia kampuni ya Future Century.

Skyner: Kisura anayetishia mastaa wa kike Bongo Movie





NI muda mfupi tangu Skyner Ally Seif, ajiingize kwenye fani ya uigizaji, ila tayari amekuwa na jina kubwa kutokana na umahiri aliouonyesha kupitia kazi alizoshiriki.
Mbali nba umahiri wa kisanii, pia mvuto wa sura na umbile vimemfanya msanii huyo, awe miongoni mwa wasanii wa kike wanaotamba nchini kwa sasa.
Sykner alikiri, licha ya kuwa na kipaji cha sanaa tangu utotoni, hakupata fursa ya kukionyesha hadi mwaka jana alipoibuliwa na Vincent Kigosi 'Ray' kupitia filamu ya 'The Second Wife'.
Alisema kabla ya 'shavu' la Ray, alishacheza kazi nyingine kama 'Mtumwa wa Mapenzi' na 'Johnson' ambazo hazikumtangaza sana.
Kazi nyingine alizoshiriki mara alipoibuliwa na Ray, ni 'What is It', 'Why I Did Love', 'I Hate My Birthday', 'Kizungumkuti', 'Unpredictable' na nyingine.
Skyner anayejiandaa kuolewa Ijumaa ijayo, alizaliwa mwaka 1992 jijini Dar, akiwa mtoto wa pili wa familia ya watoto watatu, alihitimu masomo ya sekondari Shule ya Cambridge, ya jijini Dar.
Nyota huyo, anayependa biriani na kunywa fanta, alisema licha ya kuwepo kwenye sanaa kwa muda mfupi, fani hiyo imemnufaisha mengi, akiota kuja kutamba kimataifa na mtayarishaji na muongozaji bora, akimiliki kampuni yake binafsi.
Kisura huyo, hutumia muda wake wa ziada kumuomba Mungu na kulala, pia ni shabiki wa
muziki akihusudu miondoko ya Arabian.
Juu ya madai ya rushwa na ngono katika sanaa, Skyner alikiri ni kweli amewahi kusikia, ila yeye hajawahi kukumbana nayo.
Ila, alisema wasanii wanaoombwa rushwa hiyo wana uhuru wa kukataa kwa kuringia vipaji vyao badala ya kujirahisisha na kudhalilika.
Skyner aliyewafiwa na wazazi wote mwaka 2006 wakipishana miezi mitano, akitangulia mama yake aliyefariki mwezi Aprili, kisha Septemba kufuata baba'ake, alisema licha ya kuwepo kwenye sanaa kusaka fedha, hayupo tayari kuchojoa nguo, ili acheze filamu za X.
Kimwana huyo, anayewazimia Irene Uwoya na Ray, alidai hawezi kucheza X hata akiahidiwa kiasi gani cha donge la fedha, kwa vile anajiheshimu na kujithamini kama mwanamke.
Aliwaasa wenzake, kujiheshimu na kuepukana na matendo machafu, aliyodai huwavunjia hadhi mbele ya jamii, na kusababisha sanaa yao kuonekana kama kazi ya wahuni wakati sio kweli.
Alisema, umaarufu wa msanii hupatikana kupitia ubora wa kazi zake na sio skendo chafu.
Skyner aliiomba serikali iwasaidie wasanii nchini kuweza kupambana na maharamia wanaowaibia kazi zao na kuwafanya wasanii wafe maskini tofauti na wenzao wa mataifa mengine.
Kadhalika, aliiasa jamii kuwa bega kwa bega na wasanii kwa kununua kazi zao halisi mara zitokapo, badala ya kukubali kuuziwa kazi feki, kitu kinachochangia wasanii kunyonywa na kuwafanya washindwe kusimama kimaisha na kiuchumi.

Mwisho

Azam yagomea nyota wake kwenda likizo, kisa...!

WAKATI nyota wa Simba na Yanga wakipewa likizo fupi ya kupisha mchezo wa timu ya taifa, Taifa Stars dhidi ya Morocco utakaochezwa ugenini mwezi ujao, uongozi wa Azam umewagomea mastaa wake, ukisisitiza kuwa timu yao itaendelea kujifua kama kawaida.
Simba kupitia Afisa Habari wake, Ezekiel Kamwaga, imetangaza kuwapa likizo ya wiki moja wachezaji wao, ili kupumzika kabla ya kurejea tena kujiandaa na pambano dhidi ya African Lyon litakalochezwa Oktoba 16, jijini Dar es Salaam.
Klabu hiyo imewapa likizo wachezaji hao baada ya kazi nzuri waliyofanya kwa kuiweka kileleni mwa msimamo timu yao ikiwa na pointi 18 kutokana na kucheza mechi nane bila kupoteza hata moja, ikishinda mechi tano na kutoka sare mechi tatu, .
"Wachezaji wetu tumewapa likizo ya muda mfupi, kabla ya kurejea tena kuanza maandalizi dhidi ya mechi yetu ijayo na zile zilizosalia katika ligi hiyo," alisema Kamwaga.
Hata hivyo timu inayoifukuzia Simba katika msimamo wa ligi hiyo, Azam imesema hawaendi mapumziko kama timu nyingine, bali wataendelea kujifua kujiandaa zaidi kwa mechi zao zijazo kabla ya kumaliza duru la kwanza mnamo Novemba 5.
Katibu wa Azam, Nassor Idrissa, alisema nyota wa timu yao wataendelea kufanya mazoezi kama kawaida, licha ya kwamba hawatakuwa na mchezo wowote hadi Oktoba 15 dhidi ya 'maafande' wa JKT Ruvu.
"Nyota wetu hawataenda likizo, wataendelea kujifua mazoezi kulingana na programu za kocha kwa nia ya kuwaweka sawa wachezaji kwa mechi zilizosalia za kumalizia duru la kwanza," alisema.
Idrissa maarufu kama 'Father' alisema yapo makosa ambayo yalikuwa yakifanyika katika kikosi chao, hivyo muda uliopo utatumiwa na benchi lao la ufundi kuweka mambo sawa kabla ya kurejea tena dimbani wakiwa moto kuliko hivi sasa.
Azam iliyopanda Ligi Kuu msimu wa 2008-2009, ndiyo inayoshikilia nafasi ya pili katika msimamo wa ligi ikiwa na pointi 15, tatu zaidi ya vinara Simba.

'Vijana wa Kova' wamsajili Mnigeria Ligi Daraja la Kwanza

MABINGWA wa Ligi ya TFF-Taifa, Central Stars (Polisi-Dar es Salaam), imetangaza kuwaongeza wachezaji sita wapya akiwemo Mnigeria kwa ajili ya Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara inayotarajiwa kuanza Oktoba 15 katika vituo vitatu tofauti.
Uongozi wa timu hiyo umedai, umewaongeza wachezaji hao kwa lengo la kuipa nguvu timu yao inayoendelea kujifua kwenye uwanja wa Chuo cha Polisi, Kurasini kuhakikisha inakuwa miongoni mwa klabu zitakazopanda Ligi Kuu msimu ujao.
Katibu wa timu hiyo, Ngello Nyanjaba, aliiambia MICHARAZO kuwa, wachezaji hao wapya waliongezwa ni Mnigeria, Felix Ameche, Msiba Joto, Paul Skazwe, Juma Sedege na Awadh ambao tayari wameorodheshwa kwenye usajili wa timu yao.
Nyanjaba, ambaye pia ni kocha wa timu hiyo ya Polisi, alisema wachezaji hao wapya wataungana na nyota 22 wa kikosi hicho waliopandisha daraja timu hiyo kwa ajili ya ligi hiyo, akisema walitarajia kuwasilisha usajili wao wakati wowote kuanzia leo.
"Tunaendelea vema na maandalizi ya ligi daraja la kwanza, ambapo tangu turejee toka Tanga tunaendelea kujifua kwa mazoezi, lakini kubwa ni kuongeza wachezaji wapya sita akiwemo Mnigeria kwa lengo la kufanya vema kwenye michuano hiyo," alisema.
Michuano hiyo itakayochezwa kwa mtindo wa nyumbani na ugenini itashirikisha timu timu 18 zilizopangwa katika makundi matatu, ambapo Polisi-Dar, imepangwa kundi A na timu za Mgambo-Tanga, Morani-Manyara, TMK United na Transit Camp za Dar na Burkina Faso ya Morogoro.
Kundi B lina timu za Majimaji-Songea, Mbeya City Council, Mlale JKT-Ruvuma, Polisi- Iringa, Small Kids-Rukwa na Tanzania Prisons ya Mbeya.
Timu nyingine zitakazoshiriki ligi hiyo ni pamoja na 94 KJ ya Dar, AFC-Arusha, Polisi-Morogoro, Polisi-Tabora, Rhino Rangers-Tabora na Samaria-Singida, zilizopangwa katika kundi C.

Mwisho

Kaseba, Oswald kumaliza ubishi kesho Dar


MABONDIA Japhet Kaseba na Maneno Oswald 'Mtambo wa Gongo', leo wamepima uzito tayari kumaliza ubishi katika pambano lao linalofanyika kesho jijini Dar es Salaam.
Kaseba na Oswald watapigana kwenye pambano lisilo la ubingwa la raundi 10 la uzani wa Middle, litakalofanyika kwenye ukumbi wa Travertine Hoteli, Magomeni.
Pambano hilo lililoandaliwa na mratibu Gervas Muganda chini ya usimamizi wa Shirikisho la Ngumi za Kulipwa Tanzania, PST, litasindikizwa na mapambano kadhaa ya utangulizi yakiwemo yale ya mchezo wa kick boxing.
Mabondia hao kwa nyakati tofauti wametambiana kila mmoja akitamba ni lazima aibuke mshindi katika pambano hilo kutokana na anavyomchukulia mpinzani wake, sambamba na maandalizi wanayofanya.
Oswald, alisema kwa uzoefu alionao ni wazi atammaliza Kaseba raundi za awali, huku Kaseba, licha ya kukiri mpinzani wake ni 'ngangari', ila anaamini atampiga.
"Ni kweli Oswald ni mzuri na mzoefu wa ngumi, ndio maana amesaini mapambano mawili dhidi yangu na la Rashidi Matumla, lakini kwa nilivyojiandaa nitamshinda tu," alisema Kaseba.
Oswald nae alisema anachotaka ni mashabiki wa ngumi kufurika ukumbini kuona namna Kaseba anavyorejeshwa kwenye kick boxing, kwa jinsi atakavyompiga.
Alisema anajiamini uwezo alionao katika ngumi ni vigumu kuzuiwa na Kaseba, akisisitiza kuwa atawathibitishia wadau wa ngumi kwa nini aliitwa 'Mtambo wa Gongo' na watu wa Malawi.
Michezo ya utangulizi itakayolisindikiza pambano la Kaseba na Oswald ni la bingwa wa zamani wa ngumi za kulipwa nchini, Ernest Bujiku dhidi ya Mbukile Chuwa, Sweet Kalulu atakayepigana na Chaurembo Palasa na Venance Mponji kuzipiga na Jafar Majiha.

Villa kukutana J'pili, yamnyakua Habib Kondo

WAKATI wanachama wa Villa Squad wakitarajia kufanya mkutano wao mkuu keshokutwa, uongozi wa klabu hiyo umemnyakua kocha wa zamani wa Azam, Habib Kondo, ili kuokoa jahazi la timu yao linaloendelea kuzama katika Ligi Kuu Tanzania.
Makamu Mwenyekiti wa Villa, Ramadhani Uledi, aliiambia MICHARAZO kwamba klabu yao inatarajia kufanya mkutano wa wanachama kwa ajili ya kujadili mustakabali wa timu yao pamoja na mipango mingine ya kimaendeleo.
Uledi, alisema mkutano huo utafanyika Jumapili na kuwahimiza wanachama wake kuhudhuria kwa wingi kwa ajili ya kuisaidia klabu yao kuweka mikakati ya kuinusuru isishuke daraja.
"Tunatarajia kufanya mkutano wa wanachama siku ya Jumapili, kwa nia ya kujadili mustakabali wa timu yetu pamoja na mambo mengine ya maendeleo ya klabu yetu ikiwemo suala la uchaguzi mdogo wa kuziba nafasi zilizo wazi," alisema.
Aidha uongozi wa klabu hiyo umemnyakua aliyekuwa kocha wa timu ya Azam, Habib Kondo baada ya aliyekuwa kocha wao, Said Chamosi, kurejea kwao Kenya.
Kondo, alithibitisha kunyakuliwa kwake, akisema ameombwa na uongozi wa Villa kuisaidia timu yao, hadi atakapopatikana kwa kocha mpya mkuu wa kuinoa timu hiyo.
"Aisee ni kweli bwana, baada ya kufuatwa na viongozi wa Villa ili kuisaidia timu yao, nimekubali kuinoa kwa muda, wakati wakiendelea kusaka kocha mkuu wa kudumu, kwa wanamichezo kama sisi ni vigumu kukataa ombi kama hilo," alisema.
Kondo, alisema licha ya kuanza kuinoa timu hiyo kwa kupata sare ya 0-0 dhidi ya JKT Ruvu, bado itabidi afanye kazi ya ziada kuisaidia timu hiyo kutokana na ukweli nafasi iliyopo sio nzuri, ingawa ligi bado ipo katika duru la kwanza.
Nyota huyo wa zamani wa Reli-Morogoro na Sigara, ndiye aliyeipandisha daraja hadi ligi kuu timu ya Azam msimu wa 2008-2009 kabla ya kuwa msaidizi wa makocha wa kigeni walioinoa timu hiyo kwa vipindi tofauti akiwemo kocha wa sasa Stewart Hall.

Timu za 'Maafande' zaitisha Azam Ligi Kuu T'Bara


TIMU ya soka ya Azam, imedai inakoseshwa usingizi ndani ya Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu na kasi ya timu za jeshi, kuliko na vigogo vya Simba na Yanga.
Aidha klabu hiyo imeisifia safu yao ya ulinzi ambayo hadi sasa imeruhusu mabao mawili, ikiwa ndio timu pekee iliyofungwa mabao machache katika ligi hiyo.
Uongozi wa klabu hiyo, umesema mwenendo wa timu hizo za majeshi zilizopo katika ligi hiyo, umeifanya ligi ya msimu huu, kiasi cha kuwanyima raha wakizifikiria.
Katibu Mkuu wa klabu hiyo, Nassor Idrissa 'Father', aliiambia MICHARAZO juzi kuwa, licha ya Simba na Yanga kuonekana tishio kwa klabu nyingine, wao Azam wanazihofu timu za JKT Oljoro, JKT Ruvu na Ruvu Shooting kwa jinsi zilivyo na upinzani mkali.
Idrissa, alisema timu hizo zimekuwa na upinzani mkali na kucheza soka la kusisimua na kutofungika kirahisi kitu kinachoifanya Azam zikiangalie kwa umakini timu hizo kuliko Simba na Yanga.
"Kwa kweli ligi ya msimu huu ni ngumu na yenye kusisimua na kati ya timu zinazotunyima raha ni timu za maafande ambazo zimekuwa na upinzania mkali na zenye kucheza soka la kusisimua," alisema Idrissa.
Alisema, timu hizo zimekuwa na matokeo bora zikiwa dimba la nyumbani au ugenini, na kudai uthibitisho wa ukali wao hata ukiziangalia kwenye msimamo zinafuata zikitofautiana kwa pointi chache na timu zilizopo juu.
Aidha Idrissa, aliipongeza safu ya ulinzi ya timu yake kwa kuruhusu kufungwa idadi ndogo ya mabao,ikiifanya iongoze kwa kuwa na ukuta mgumu hadi sasa nchini.
Azam katika mechi nane ilizokwishacheza hadi sasa imeruhusu mabao mawili, huku ikifuatiwa na Simba iliyoruhusu kufungwa mabao manne hadi hivi sasa.
"Kwa kweli tunaipongeza timu yetu na hasa safu ya ulinzi kwa kasi nzuri iliyofanya kwa kuruhusu mabao machache, naamini kwa mwenendo huu tunaweza kutimiza ndoto za kutwaa ubingwa au kuwa wawakilishi wa nchi kimataifa mwakani," alisema Idrissa.

Mwandido kuja nchini kuzindua kibao cha Assosa


MWANAMUZIKI nyota wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Ny'boma Mwandido anatarajiwa kuja nchini kutumbuiza kwenye uzinduzi wa kitabu cha gwiji la muziki wa dansi nchini, Tshimanga Kalala Assosa kiitwacho 'Jifunze Lingala'.
Uzinduzi wa kitabu hicho unatarajiwa kufanyika jijini Dar es Salaam, ingawa tarehe na jina la ukumbi, bado hazijawekwa bayana.
Akizungumza na MICHARAZO juzi, Assosa, alisema mipango ya uzinduzi wa kitabu chake yanaendelea vema ikiwemo kufanya mpango wa kumleta Ny'boma, aliyewahi kufanya naye kazi katika bendi mbalimbali nchini Congo, ili kushiriki uzinduzi huo.
Assosa alisema tayari wameshakubaliana na gwiji hilo linalotamba na nyimbo kama 'Double Double', 'Masua' na 'Abisina' kuja katika uzinduzi huo, kinachoendelea kwa sasa ni kumtafutia tiketi ya ndege ya kumleta na kumrejeshwa baada ya shughuli hiyo.
"Maandalizi ya uzinduzi wa kitabu changu yanaendelea vema, ambapo natarajia kuja

kushindikizwa na Ny'boma Mwandido, ambaye ameafiki mualiko wetu na kuhitaji tumtumie tiketi ya ndege," alisema Assosa.
Assosa, anayemiliki bendi ya Bana Marquiz, alisema umoja wao wa Wana 'Dar Kavasha Club', unafanya mipango ya kuisaka tiketi hiyo pamoja na ufadhili kwa ajili ya shughuli nzima ya uzinduzi wa kitabu hicho ambacho tayari kipo mtaani karibu miezi sita sasa.
"Kwa sasa tunasubiri majibu ya maombi yetu ya udhamini tuliotuma katika makampuni ya masharika mbalimbali ili kufanikisha uzinduzi huo utakaoenda sambamba na burudani ya muziki," alisema.
Aliongeza mbali na kitabu hicho cha 'Jifunze Lingala-Toleo la Kwanza', pia tayari ameanza maandalizi ya toleo la pili la kitabu hicho na na kile kinachohusu maisha yake binafsi.
Vitabu vyote vinafadhiliwa Klabu ya Dar Kavasha, umoja ambao Assosa ameomba mashabiki wa miondoko hiyo mikoani kuanzisha matawi yao, ili kuupanua zaidi.

Mwisho