STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 30, 2011

Msondo yaingia studio kurekodi albamu mpya



BENDI kongwe ya Msondo Ngoma, mapema leo asubuhi imeingia studio kurekodi kibao kipya kiitwacho 'Suluhu', ikiwa ni maandalizi ya upakuaji wa albamu yao mpya.
Mmoja wa viongozi wa bendi hiyo, Shaaban Dede, aliiambia MICHARAZO kuwa, nyimbo zao mpya zitarekodiwa katika studio za Fabreas Records na kwa kuanza leo anarekodi kibao cha 'Suluhu', ambacho amekitunga yeye.
Dede, alisema mara baada ya kibao hicho kurekodiwa kitasambazwa kwenye vituo vya redio kwa nia ya kukitambulisha huku, bendi yao ikiendelea kumalizia nyimbo nyingine tano zilizosalia.
"Tumeingia leo studio kwa Fabreas kwa lengo la kufyatua kibao cha Suluhu na vingine kwa ajili ya albamu yetu mpya ijayo," alisema Dede.
Alisema nyimbo nyingine za albamu hiyo ambazo zimeshakamilika ni 'Dawa ya Deni', 'Lipi Jema', 'Kwa Mjomba Hakuna Urithi', 'Baba Kibene' na 'Nadhiri ya Mapenzi'.
"Nadhani muda si mrefu mashabiki wetu na wale wa muziki kwa ujumla wataipata albamu yetu, kwani tutakuwa tukidondosha wimbo mmoja mmoja, kabla ya kuikamilisha na kuiachia mtaani, kabla ya kumalizika mwaka huu," alisema.
Msondo Ngoma imekuwa na desturi ya kutoa albamu kila mwaka, ila kwa mwaka jana haikuachia kazi yoyote, albamu yao ya mwisho ni ile ya mwaka juzi iitwayo 'Huna Shukrani'.

No comments:

Post a Comment