STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, September 30, 2011

Villa kukutana J'pili, yamnyakua Habib Kondo

WAKATI wanachama wa Villa Squad wakitarajia kufanya mkutano wao mkuu keshokutwa, uongozi wa klabu hiyo umemnyakua kocha wa zamani wa Azam, Habib Kondo, ili kuokoa jahazi la timu yao linaloendelea kuzama katika Ligi Kuu Tanzania.
Makamu Mwenyekiti wa Villa, Ramadhani Uledi, aliiambia MICHARAZO kwamba klabu yao inatarajia kufanya mkutano wa wanachama kwa ajili ya kujadili mustakabali wa timu yao pamoja na mipango mingine ya kimaendeleo.
Uledi, alisema mkutano huo utafanyika Jumapili na kuwahimiza wanachama wake kuhudhuria kwa wingi kwa ajili ya kuisaidia klabu yao kuweka mikakati ya kuinusuru isishuke daraja.
"Tunatarajia kufanya mkutano wa wanachama siku ya Jumapili, kwa nia ya kujadili mustakabali wa timu yetu pamoja na mambo mengine ya maendeleo ya klabu yetu ikiwemo suala la uchaguzi mdogo wa kuziba nafasi zilizo wazi," alisema.
Aidha uongozi wa klabu hiyo umemnyakua aliyekuwa kocha wa timu ya Azam, Habib Kondo baada ya aliyekuwa kocha wao, Said Chamosi, kurejea kwao Kenya.
Kondo, alithibitisha kunyakuliwa kwake, akisema ameombwa na uongozi wa Villa kuisaidia timu yao, hadi atakapopatikana kwa kocha mpya mkuu wa kuinoa timu hiyo.
"Aisee ni kweli bwana, baada ya kufuatwa na viongozi wa Villa ili kuisaidia timu yao, nimekubali kuinoa kwa muda, wakati wakiendelea kusaka kocha mkuu wa kudumu, kwa wanamichezo kama sisi ni vigumu kukataa ombi kama hilo," alisema.
Kondo, alisema licha ya kuanza kuinoa timu hiyo kwa kupata sare ya 0-0 dhidi ya JKT Ruvu, bado itabidi afanye kazi ya ziada kuisaidia timu hiyo kutokana na ukweli nafasi iliyopo sio nzuri, ingawa ligi bado ipo katika duru la kwanza.
Nyota huyo wa zamani wa Reli-Morogoro na Sigara, ndiye aliyeipandisha daraja hadi ligi kuu timu ya Azam msimu wa 2008-2009 kabla ya kuwa msaidizi wa makocha wa kigeni walioinoa timu hiyo kwa vipindi tofauti akiwemo kocha wa sasa Stewart Hall.

No comments:

Post a Comment