STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, August 8, 2011

RITA yaingilia kati mgogoro wa Answar Sunna

WAKALA wa Usajili, Ufilisi na Udhamini nchini, RITA, umewataka waumini wa Jumuiya ya Answar Sunna Tanzania wanaoshinikiza uongozi wa juu ya jumuiya hiyo ung'oke madarakani kutulia hadi watapotoa maamuzi yao mwishoni mwa mwezi huu.
Waumini hao wa Answar Sunna wanataka uongozi wao ung'oke kwa kukiuka katiba na kushindwa kuiendesha kwa mafanikio jumuiya yao inayotajwa ni taasisi kubwa ya pili nchini baada ya Baraza Kuu la Waislam Tanzania, BAKWATA.
Meneja wa Ufilisi na Udhamini wa RITA, Linna Msanga Katema, aliiambia MICHARAZO kuwa, ofisi yao inatambua kuwepo kwa mgogoro ndani ya jumuiya hiyo baina ya waumini na uongozi wao na wanaendelea kuufanyia kazi.
Linna, alisema hatua waliyofikia katika kuutatua mgogoro huo ni vema waumini kupitia kamati yao maalum wakavuta subira ili waweze kutoa maamuzi mwishoni mwa mwezi huu baada ya kukutana na kupitia vielelezo vya pande hizo mbili.
Meneja huyo, alisema tofauti na hapo awali walipokuwa wakikosa ushirikiano toka kwa viongozi wanaolalamikiwa wakiwemo Baraza la Wadhamini na Amiri wa Jumuiya hiyo, Sheikh Juma Poli, sasa mambo ni shwari na ndio maana wanataka waumini watulie.
"Tumeshawaandikia barua kuomba watupe muda wa mwezi mmoja toka Julai 26 hadi Agosti 26, ili RITA tutoe maamuzi juu ya kinachoendelea baina ya pande hizo mbili, hivyo tunaomba waumini watulie haki itatendeka," alisema Linna.
Nao waumini hao waliofanya mkutano wao Jumapili iliyopita walitoa maamuzi ya kuvuta subiri ili kuona RITA itaamua nini, lakini wakisisitiza wanataka haki itendeke kwa manufaa ya jumuiya yao waliyodai inazidi kudumaa kutokana na uongozi uliopo.
Wakizungumza kwenye mkutano huo waumini hao waliutaka uongozi wa kamati yao inayoongozwa na Mwenyekiti wake, Hamis Buguza na Katibu, Abdulhafidh Nahoda, kuendelea kufuatilia kujua RITA itaamua kitu gani na wao wameamua kuvumilia.
Mzozo wa waumini na uongozi wa jumuiya hiyo ulianza tangu mwaka juzi kutokana na madai ya ukiukwaji katiba ikiwemo kutoitishwa kwa mikutano kwa muda wa miaka 10, pamoja na kubinafsishwa mali za jumuiya hiyo bila waumini hao kushirikishwa.
Katibu wa Baraza la Wadhamini wa Jumuiya, Abdalla Lihumbi, alinukuliwa na gazeti hili wiki iliyopita akikiri uongozi wao kwenda kinyume akidai wanafanya mipango ya kupata suluhu kwa manufaa ya jumuiya yao iliyotambuliwa kitaifa mwaka 1992.

Mwisho

Simba Day ni leo Arusha, uhondo wapungua




KUHAMISHWA kwa tamasha la klabu ya Simba, 'Simba Day' kupelekwa jijini Arusha kumevuruga baadhi ya ratiba zilizokuwa zimepangwa, ingawa uongozi umesema kila kitu kipo sawa na kwamba leo watatambulisha rasmi kikosi chao kipya cha msimu huu jijini humo.
Tamasha hilo linalofanyika kwa mwaka wa tatu mfululizo, awali lilipangwa kufanyika jijini Dar es Salaam, lakini limekwama baada ya kukosekana muafaka wa malipo baina ya uongozi wa klabu hiyo na ule unaosimamia uwanja wa Taifa, na kulazimika kupelekwa Sheikh Amri Abeid.
Kutokana na kuhamishwa huko mkoani Arusha, baadhi ya mambo yaliyotarajiwa kufanyika leo kama pambano la timu za vijana za Simba na Azam U20 limefutwa na badala yake itachezwa mechi ya timu ya veterani ya Arusha dhidi ya viongozi wa Simba.
Kadhalika, bendi na vikundi vilivyokuwa vitumbuize katika tamasha hilo, pia vimeshindikana sawa na tukio la utoaji wa tuzo za wadau walioisaidia Simba kwa hali na mali, ambapo kesho watapewa wachache watakaobahatika kwenda jijini Arusha na wengine watatangazwa tu.
Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, aliiambia MICHARAZO, kuwa pamoja na hali iliyotokea iliyowatatiza kidogo, kila kitu kinatarajiwa kufanyika kwa ufanisi leo ambapo timu yao itakitambulisha rasmi kikosi chao kipya chenye wachezaji wapya wa kimataifa.
"Ni kweli kuhamishwa kwa tamasha hili toka Dar hadi Arusha kumevuruga baadhi ya mambo, lakini kila kitu kipo sawa na wakazi wa Arusha watarajie burudani ya kutosha kwani mambo yamerekebishwa, ili kufanikisha tamasha hilo," alisema Kamwaga.
Kamwaga, alisema kikosi chao tayari kipo jijini humo tangu Ijumaa kikijifua kabla ya leo kuvaana na Simba ya Uganda iliyotarajiwa kutua jana na kusafiri kwenda Arusha kwa ajili ya mechi hiyo ya kirafiki ya kimataifa.
Alisema kikosi chao kipo kamili ukiondoa Mwinyi Kazimoto anayeendelea kujiuguza majeraha yake aliyopata siku ya mechi ya fainali ya Kombe la Kagame kati ya Simba na Yanga, huku wachezaji wengine wawili, Ulimboka Mwakingwe na Amri Kiemba wakirejea toka majeruhi.
Kamwaga alisema watatumia tamasha hilo na hasa mechi yao na Simba ya Uganda kupima kikosi chao kabla ya kuvaana na Yanga wiki ijayo katika pambano la Ngao ya Jamii ikiwa ni uzinduzi wa msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Simba na Yanga zinatarajiwa kuvaana Agosti 17 katika pambano litakalofanyika kwenye uwanja wa Taifa, ikiwa ni wiki kadhaa tangu timu hizo kukutana kwenye fainali hizo za kombe la Kagame na Yanga kuibuka mshindi wa bao 1-0 lililofungwa na Mghana Kenneth Asamoah.

Mwisho

Villa Squad yahaha kusaka Mil 7.2 kuianza Ligi Kuu

UONGOZI wa klabu ya soka ya Villa Squad inahaha kusaka kiasi cha Sh. Milioni 7 kwa ajili ya kuiwezesha timu yao kwenda kuianda Ligi Kuu Tanzania Bara 2011-2012 ugenini Kanda ya Ziwa, huku aliyekuwa mlezi wao, Abdalla Bulembo akisisitiza kujiweka kando katika uongozi.
Villa iliyorejea kwenye ligi hiyo baada ya kushuka daraja mwaka 2008, imepangwa kuanza mechi zake kwa kucheza na Toto Afrika siku ya uzinduzi wa ligi hiyo Agosti 20 kabla ya kuivaa Kagera Sugar ndipo irejee Dar es Salaam kucheza mechi za nyumbani.
Habari za ndani za klabu hiyo zilizothibitishwa na uongozi wake zinasema kuwa, kwa bajeti ya haraka inayotakiwa kwa timu hiyo kwenda kucheza mechi hizo mbili za awali za Ligi Kuu inahitajika kiasi cha Sh. Milioni 7.2 ambazo klabu haijui itazipata wapi kwa sasa.
Katibu wa Villa, Masoud Yasin, alisema kinachowachanganya zaidi ni kuchelewa kutolewa kwa fedha toka kwa wadhamini ambazo kwa kawaida hupitia Shirikisho la Soka Tanzania, TFF na kutoa wito kwa wadau wa soka wa Dar es Salaam hasa wakazi wa Kinondoni kuwasaidia.
"Tunaomba wadau wa soka watusaidie ili Villa tuweze kuianza ligi kwa umakini kwani tuna hali mbaya ya kiuchumi, na hasa kuzisaka fedha hizo kwa ajili ya mechi hizo mbili za kanda ya Ziwa ambapo bajeti yake ni zaidi ya Sh. milioni saba," alisema katibu huyo.
Yasin, alisema hali yao kiuchumi ni mbaya na hawajui watafanyaje katika ushiriki wao hasa baada ya mlezi wao, Abdalla Bulembo kujiweka kando akikataa hata kuzishika nafasi ambazo zipo nje ya katiba yao kama pendekezo lililotolewa na Rais wa TFF, Leodger Tenga.
Tenga alitoa pendekezo hilo wakati akitatua sakata la kuenguliwa kwa Bulembo kuwania Uenyekiti wa Villa na kuibua mtafaruku kabla ya kutulizwa kwa uchaguzi huo kufanyika kwa kuachwa wazi nafasi zilizokosa wagombea wake ikiwemo hiyo ya Mwenyekiti.
Bulembo mwenyewe alipotafutwa na gazeti hili, alikiri ni kweli hana haja ya uongozi baada ya TFF kumwekea kauzibe, ingawa alisema anasikitika na hali inayoendelea na viongozi wa soka nchini kushindwa kuonyesha dhamira ya kweli ya kuinua mchezo huo kupitia klabu ndogo.
"Sitaki hata kusikia habari za kuongoza tena, maadam TFF iliamua kunikwamisha basi mie naendelea na shughuli zangu, ila sidhani kama viongozi wa soka nchini wanania ya kuinua mchezo huu," alisema Bulembo.
Villa ni miongoni mwa timu nne zilizopanda ligi kuu toka daraja la kwanza nyingine zikiwa ni JKT Oljoro Arusha, Coastal Union ya Tanga na Moro United ya Dar es Salaam na tayari TFF imeshatangaza ratiba ya kuanza kwa ligi hiyo Agosti 20 ikishirikisha jumla ya timu 14.

Mwisho

Ubalozi wa UAE wafuturisha waislam Dar

UBALOZI wa Nchi ya Falme za Kiarabu, UAE nchini kupitia taasisi ya kutoa huduma za kijamii ya Khalifa Bin Zaayid Al Nahyaan, umeamua kuwafuturisha waumini wa dini ya kiislam wa Msikiti wa Al Rahman wa Dar es Salaam kwa mwezi mzima wa mfungo wa Ramadhani.
Msaada huo wa futari unaoambatana na tende, ulianzwa kutolewa juzi jioni ambao mamia ya waumini wa msikiti huo walipata fursa ya kufuru chakula hicho kabla ya usiku kugawiwa tende zilizotolewa na ubalozi huo wa UAE.
Imamu wa Msikiti huo wa Al Rahman uliopo eneo la Kinondoni, Sheikh Abdullah Salim Bahssany, akiwahutubia waumini wake wakati wakigawiwa futari hiyo, alisema huo ni msaada toka ubalozi wa UAE na utakuwa ukitolewa hapo kila siku hadi mwezi mtukufu wa Ramadhani utakapomalizika mwishoni mwa mwezi huu.
Imamu huyo aliwaambia waumini hao kuwa wale waliokuwa na shaka na kupata futari katika funga zao, waondoe hofu kwani sasa watakuwa wakipata chakula hicho, huku akiushukuru ubalozi huo kwa ukarimu iliyouonyesha kwa waumini hao.
"Jamani futari mnayokula leo imetolewa na ubalozi wa nchi za Falme za Kiarabu na msaada huu utakuwa ukitolewa kwa mwezi mzima katika mfungo huu wa Ramadhani hivyo msiwe na hofu katika funga zenu,"alisema Sheikh Bahssany.
Baadhi ya waumini waliofuturishwa msikiti hapo waliushukuru ubalozi huo na kuomba watu wengine wenye uwezo kuiga mfano huo wakidai mwezi huu ndio wa waumini wa kweli kuonyesha upendo, ukarimu na kuhurumiana katika kutekeleza nguzo ya nne kati ya tano za Imani za Kiislam.

Mwisho

Kondoo mwenye maandishi ya kiarabu azaliwa Kilimanjaro


KONDOO MWENYE MAANDISHI WA KIARABU YANAYOTAFSIRIKA 'YASIN' AKIWA KANDO YA MAMA YAKE PICHA KWA HISANI WA BLOG YA BURUDAN