STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, July 15, 2014

'Shujaa' waa Ujerumani haamini kama wametwaa ndoo

KIkosi cha Ujerumani na kocha wao wakishangilia ubingwa
Mario Gotze akiwa na famnilia yake akishangilia ubingwa
 MUUAJI aliyeizamisha Argentina na kuipata timu yake ya Ujerumani ubingwa wa Kombe la Dunia Mario Gotze amesema ilikuwa ni ndoto iliyokua kweli baada ya kuisaidia Ujerumani kutwaa Kombe la Dunia kwa kufunga goli pekee la mechi ya fainali dhidi ya Argentina kwenye Uwanja wa Maracana juzi.
Kiungo huyo wa Bayern Munich alianzia benchi katika mechi hiyo hiyo, lakini aliingizwa mwishoni mwa kipindi cha pili kuchukua nafasi ya Miroslav Klose.
Gotze hakumuangusha kocha Joachim Low na akafunga goli katika dakika ya 113 kufuatia krosi ya Andre Schurrle na kuwapa Ujerumani ubingwa wa nne wa Kombe la Dunia.
"Ni hisia za aina yake, sijui nizielezee vipi. Nilipiga shuti tu na sikujua nini kitatokea. Ni ngumu kuamini," alisema nyota huyo mwenye umri wa miaka 21.
"Kwetu sisi,ndoto imekua kweli. Najivunia timu na nina furaha ya kupindukia kwa kila kilichotokea Brazil.
"Kila mchezaji katika timu yetu anastahili kutajwa hapa na tunajivunia kutwaa kombe hili."
Gotze amecheza mechi sita za Kombe la Dunia 2014 na amefunga magoli mawili.

MAYWEATHER KURUDIANA NA MAIDANA SEPTEMBA.

BINGWA wa masumbwi wa uzito wa welter ambaye hajapigwa mpaka sasa, Floyd Mayweather anatarajiwa kucheza pambano la marudiano na Marcos Maidana wa Argentina. 
Mayweather mwenye umri wa miaka 37 raia wa Marekani anatarajiwa kutetea mikanda yake ya ubingwa inayotambuliwa na Baraza la Ngumi Duniani-WBC na Chama cha Ngumi Duniani-WBA dhidi ya maidana aliyemdunda katika pambano lililofanyika Mei 3 mwaka huu. 
Wawili hao wanatarajiwa kupambana tena jijini Las Vegas, Septemba mwaka huu. 
Akihojiwa Mayweather ametamba kuwa ana uhakika wa kushinda pambano hilo pamoja na kukiri kuwa utakuwa mpambano na mgumu. 
Katika pambano lililofanyika Mei, jaji wa kwanza alitoa alama 114-114, wakati majaji wawili waliobakia walitoa alama 116-112 na 117-111 ambapo alama zote za juu zilikwenda kwa Mayweather. 
Mayweather anakaribia kufikisha rekodi ya kucheza mapambano 49 bila kupigwa iliyowekwa na bingwa wa zamani wa uzito wa juu Rocky Marciano, ambapo mpaka sasa ameshashinda mapambano 46 bila kupigwa.

Mnigeria, Wema, Sir Nature kupamba Usiku wa Matumaini

Wema Sepetu
TAMASHA la Usiku wa Matumaini la mwaka 2014 linatarajiwa kufanyika  Agosti 8 na litapambwa na wasanii mbalimbali nyota nchini pamoja na mwanadada mkali toka Nigeria Yemi Alade anayetamba na wimbo wa 'Johnny'
Kawaida ya tamasha hilo hufanyika Julai 7, lakini kutokana na mwaka huu tarehe hiyo kuangukia kwenye mfungo wa mwezi wa Ramadhani, waandaaji wake wameamua kupeleka hadi Nanenane kwa heshima ya waumini wa Kiislam.
Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha hilo, Abdallah Mrisho alisema kuwa 'Usiku wa Matumaini' safari hii umeboreshwa kwa upande wa burudani ambapo Mnigeria Yami Alade anatarajia kutua kutumbuiza.
Mrisho alisema kwa upande wa wasanii wa nyumbani 'ujazo'umeongezwa kwa kuwakusanya wakali watupu kuanzia waigizaji, wasanii wa muziki wa kizazi kipya hadi wanamiochezo.
Wasanii wanaoatarajiwa kupanda jukwaani siku hiyo ni pamoja na Ali Kiba, Roma Mkatoliki, Madee, Juma Nature na wengineo kibao akiwamo Wema Sepetu atakayeimba na kucheza nyimbo za 'baby' wake, Diamond Platnumz.
"Upande wa masumbwi kutakuwa na pambano kati ya Mada Maugo na Thiomas Mashali, huku Khaleed Chokoraa aliyehamia kwenye ngumi atazipiga siku hiyo na Saim Memba, " alisema Mrisho kutoka kampuni ya Global Publishers ambao ndiyo waandaaji wa tamasha hilo la kila mwaka.
Aliongeza kuwa, Naibu Waziri wa Fedha na Mbunge, Mwingulu Nchemba atapanda ulingoni kuzipiga na Dk Hamis Kigwangala, huku wana Bongo Movie JB atazipiga na Cloud 112 na Irene Uwoya atappetana na Jackyline Wiolper.
"Pia kutakuwa na pambano la soka la Bongo Movie dhidi ya wapinzani wao Bongofleva na mechi ya wabunge wa Simba na Yanga ambao safari hii watakuwa na nyota wapya, Yanga wana Ridhiwani Kikwete na Simba wanaye Godfrey Mgimwa," alisema Mrisho.
Mwaka jana pambano la wabunge lilianzishwa na Rais Jakaya Kikwete kabla ya kupokewa na mwamuzi wa zamani wa kimataifa nchini, Othman Kazi 'Collina'.


KAJALA ampa UJUMBE mzito MWANAE akisherehekea miaka 12 ya kuzaliwa kwake

Paula
Kajala na mwanae Kajala
SIKU kama ya leo miaka 12 iliyopitaq  mwanadada Kajala Masanja alifanikiwa kujifungua mtoto wake aliyezaa na P Funk Majani aitwaye Paula.
Katika kuikumbuka siku hiyo muhimu kwa mwanae, Kajala kupitia ukursa wake wa INSTAGRAM ameandika ujumbe maalu kwa mtoto wake kueleza magumu yao yote waliopitia tangu siku ya kwanza Paula alipokuja duniani kwa kuzaliwa mpaka sasa...Kiukweli Kajala amefunguka mengi sana.....

Fainali za Usomaji wa Qur'an Julai 25

FAINALI za kumtafuta bingwa wa kuhifadhi Q'uran kwa njia ya kughani (Tajuweed) mwaka huu zitafanyika kwenye Msikiti wa Manyema jijini Dar es Salaam, Ijumaa ya mwisho ya mfungo mtukufu wa Ramadhani Julai 25 mwezi huu.
Aidha, siku hiyo itakuwa ni sawa na funga ya 27 ya mwezi huu mtukufu wa Ramadhani, hivyo waumini wa dini ya Kiislamu watakuwa ndani ya maombi maalum maarufu kama “Lailatul Qadir” ambayo huyatumia kuomba msamaha na kufutiwa madhambi maradufu na Mwenyezi Mungu.
Hayo yalisemwa na Katibu wa Taasisi ya Kuhifadhi na Usomaji wa Kuran ya Sheikh Yahya Hussein (Sheikh Yahya Hussein Tahfidh Q’uran and Tajweed Foundation), Maalim Hassan Yahya katika taarifa aliyotuma kwenye vyombo vya habari mwishoni mwa wiki.
 Maalim alisema  fainali hizo zitawakutanisha washindi wote wa michuano ya kusoma Koran watakaokuwa wameshinda kwenye michuano ya taasisi mbalimbali inayoendelea hivi sasa Afrika Mashariki na Kati.
“Tutakuwa na washindanaji walioshinda kutoka nchi zote za Afrika Mashariki na Kati ambazo ni Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, Congo DRC, Sudan Kusini na Tanzania,”alisema Maalim
Aidha alisema kuwa kutakuwa na majaji kutoka nchi hizo na wengine kutoka Saudi Arabia na Iran.
Alisema kuwa ni  washindi watatu wa mwanzo watapata nafasi ya kwenda Hijjah kwa gharama za taasisi yake pia watazawadiwa vyeti na fedha taslimu.

Brazili yamtimua 'Big Phil' ni baada ya aibu aliyowapa nyumbani


Scolari katika picha tofauti kabla ya kutimuliwa kocha wa Brazil
BRAZIL imemtimua kocha Luiz Felipe Scolari saa chache tu baada ya kumalizika kwa fainali za Kombe la Dunia ambalo walikumbana na vipigo vyao viwili vibaya zaidi katika historia yao ya michuano hiyo, moja ya magazeti yanayoongoza Brazil liliripoti jana.
Kikosi cha kocha Scolari cha Brazil kilikuwa kikipewa nafasi ya kutwaa ubingwa wa michuano hiyo lakini kilikumbana na kipigo cha aibu cha magoli 7-1 katika nusu fainali dhidi ya waliokuja kuwa mabingwa Ujerumani. Katika kukamilisha mwisho wao mbaya, walikumbana na kipigo kingine cha 3-0 dhidi ya Uholanzi katika mechi ya kusaka mshindi wa tatu.
Scolari, ambaye aliiongoza Brazil kutwaa taji lao la tano na la mwisho la Kombe la Dunia 2002, alisema baada ya mechi hiyo kwamba atawasilisha ripoti kwa mabosi wake katika Shirikisho la Soka la Brazil (CBF) na ni wakati huo tu hatima yake itaamuliwa.
Lakini gazeti la O Globo liliripoti jana kwamba Scolari alitimuliwa Jumapili usiku. Gazeti hilo lilisema taarifa rasmi ingetoka baadaye jana.
Hapakuwa na uthibitisho kutoka CBF, wala mshauri wa habari wa Scolari.
Scolari aliichukua timu hiyo Novemba 2012 na amepoteza mechi tano tu kati ya 29 alizokuwa madarakani. Aliiongoza Brazil kutwaa Kombe la Mabingwa wa Mabara mwaka jana kwa ushindi wa kukumbukwa wa 3-0 dhidi ya mabingwa wa dunia wa wakati huo Hispania katika mechi ya fainali.
Alikuwa ni mtu anayependwa sana Brazil kwa ucheshi wake na pia kwa wachezaji ambao humchukulia kama baba yao.
Alikuwa na sapoti ya taifa kuelekea kwenye Kombe la Dunia na kulikuwa na upinzani mdogo kwa kikosi alichoteua, jambo ambalo ni nadra sana nchini Brazil, kunakofahamika kama "taifa la makocha milioni 200."
Kama kuondoka kwake kutathibitishwa, makocha wanaopewa nafasi ya mapema kama warithi wake watakuwa ni Tite, kocha ambaye aliiongoza Corinthians kutwaa Kombe la Ligi ya Klabu Bingwa Amerika Kusini (Copa Libertadores) na Kombe la Dunia la Klabu 2012, na Muricy Ramalho, ambaye ni kocha wa sasa wa klabu ya Sao Paulo.