STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, September 21, 2011

Kaseba amwinda Oswald


BONDIA mchachari nchini, Japhet Kaseba yupo katika maandalizi makali kwa ajili ya pambano lake dhidi ya mzoefu, Maneno Oswald 'Mtambo wa Gongo', akitamba kuwa anafanya hivyo ili kumzima mpinzani wake.
Kaseba na Oswald wanatarajiwa kupanda ulingoni kuzipiga katika pambano lisilo la ubingwa la raundi 10 la uzani wa kati, litakalofanyika kwenye ukumbi wa Travertine, jijini Dar es Salaam.
Kila bondia amekuwa kwenye maandalizi ya pambano hilo, ambapo Kaseba, bingwa wa zamani wa dunia wa kick boxing, alikutwa na Micharazo kambini kwake, Mwananyamala Komakoma akijifua, huku akiapa kumshinda mpinzani wake.
"Kaka kama unavyoniona, nia yangu ni kutaka kurejesha heshima yangu katika ngumi kwa kutaka kumchakaza Oswald, siku tukikutana kwenye pambano hilo ambalo litasimamiwa na PST," alisema Kaseba.
Kaseba, alisema anaamini mazoezi anayofanya yatamwezesha kumnyuka Oswald ambaye kambi yake ipo Keko, ambapo amekuwa akisisitiza anataka kumshikisha adabu, muhimu mwamuzi amchunge Kaseba asirushe mateke yake.
Bondia huyo, alisema pambano lao na Oswald limeratibiwa na Gervas Muganda, litasindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi ambapo aliyataja baadhi kuwa ni kati ya
Kaseba, alisema kabla ya pambano lake na Oswald ambaye amenukuliwa akitamba kumpiga akitaka waamuzi kumchunga asirushe mateke kwa kudhani yupo kwenye kick boxing, watasindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi.
Michezo hiyo ni pamoja na pigano la bingwa wa zamani wa ngumi za kulipwa nchini, Ernest Bujiku dhidi ya Mbukile Chuwa.
Mapambano mengine ambayo yote yameandaliwa na mratibu, Gervas Muganda wa kampuni ya Babyface ni, Chaurembo Palasa dhidi ya Sweet Kalulu, Venance Mponji atapanda ulingoni kuzipiga na Jafar Majiha 'Mr Nice' na michezo miwili ya kick boxing.
Moja ya pambano hilo la Kick Boxing ni kati ya Ramadhani Mshana atapigana na Hamed Said na Kaseba alisema maandalizi yote kwa ajili ya michezo hiyo inaendelea vema.

Mwisho