STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, December 19, 2012

Pacha wa Dotnata aja na mpya

Dometria Alphonce 'DD' katika pozi


MUIGIZAJI wa filamu ambaye ni pacha wa nyota wa fani hiyo na muziki, Husna Posh 'Dotnata', Dometria Alphonce 'DD', amepakua filamu mpya iitwayo 'Kua Uyaone' ambayo inasimulia mkasa wa kweli uliowahi kumpata katika maisha yake ya ndoa.
DD, aliiambia MICHARAZO juzi kuwa filamu hiyo imeshakamilika na wakati wowote itaachiwa hadharani, ikiwa imemshirikisha yeye mwenyewe na wasanii wengine waliopo katika kikundi chake cha sanaa cha DD Films kilichopo Ukonga.
Msanii huyo ambaye pia anajihusisha na nyimbo za Injili akishirikiana na pacha wake wakiandaa albamu kwa sasa, alisema hiyo itakuwa filamu yake ya kwanza kuitunga na kuiandaa mwenyewe baada ya kushirikishwa kazi kadhaa siku za nyuma.
'Nimekamilisha filamu yangu mpya iliyojikita kwenye simulizi la kweli ambao limewahi kunitokea katika maisha yangu ya ndoa, nimecheza na wasanii mbalimbali baadhi wakiwa ni askari waliopo katika kikundi changu cha sanaa cha DD Films," alisema.
Alisema filamu hiyo ni maalum kwa wanawake wote waliowahi kukutwa na misukosuko katika maisha ya ndoa zao, kwani mbali na mikasa ya kusisimua, lakini pia inatoa suluhu ya nini kifanyike mtu anapokumbwa na misukosuko kama hiyo.
Msanii huyo ambaye kama pacha wake naye ni mjasiriamali, alisema filamu hiyo ni yenye kuwatia nguvu na ujasiri wanawake wote wanaoteseka katika ndoa zao.
Aliongeza kuwa, wakati filamu hiyo ikiwa katika harakati ya kutolewa hadharani pia tayari anaendelea kuandaa kazi nyingine ambayo hakupenda kuitaja, ingawa alidai imeshaanza kufanyiwa 'shutingi'.

Mwisho

After Death sasa Kanumba Day

Jacklyne Wolper na 'watoto wa Kanumba'
Leah Richard 'Lamata'



FILAMU mpya ya kumuenzi aliyekuwa nyota wa zamani wa filamu nchini, marehemu Steven Kanumba iitwayo 'After Death', inatarajiwa kuzinduliwa rasmi siku ya kumbukumbu ya mwaka mmoja tangu msanii huyo alipofariki dunia Aprili 7.
Mmoja wa waratibu wa filamu hiyo, Leah Richard 'Lamata' alisema wameamua kuupeleka uzinduzi huo Aprili 7 mwakani, ili kuleta maana halisi ya kumuenzi nyota huyo aliyefariki ghafla nyumbani baada ya kutokea mzozo na mpenziwe.
Lamata, ambaye ndiye muongozaji wa filamu hiyo iliyotungwa na Jacklyne Wolper, alisema awali walipanga wafanye uzinduzi huo Februari, lakini wakaona isingeleta maana ilihali Kanumba alifariki mwezi Aprili na hivyo wamepeleka hadi tarehe hiyo.
"Uzinduzi wa filamu maalum ya kumuenzi Kanumba, iitwayo 'After Death' ambayo tulipanga kuizindua Februari sasa itazinduliwa Aprili 7, ambayo itakuwa siku ya kumbukumbu ya mwaka mmoja tangu msanii huyo alipofariki," alisema Lamata.
Lamata mmoja wa waongozaji mahiri wa filamu nchini, alisema anaamini siku hiyo itawapa fursa nzuri mashabiki wa filamu hasa waliomzimia Kanumba kumuenzi na kushuhudia baadhi ya kazi za mkali huyo.
Alisema After Death, iliyoigizwa na karibu wasanii wote waliowahi kufanya kazi na Kanumba, itawarejeshea kumbukumbu mashabiki wa filamu kutokana na msanii Philemon Lutwaza 'Uncle D' kucheza nafasi ya nyota huyo aliyefanana naye.
Wengine walioshiriki filamu hiyo ni Mayasa Mrisho, Jacklyne Wolper, Patcho Mwamba, Ben Blanco, Irene Paul, Ruth Suka 'Mainda' na watoto walioibuliwa na marehemu Kanumba kupitia 'This is It' na 'Uncle JJ' Patrick na Jennifa.

Mabingwa wa Afrika, Zambia kutua ncnhini leo




Kikosi cha timu ya taifa ya Zambia
MABINGWA wa kandanda barani Afrika, Zambia ‘Chipolopolo’ wakiwa na msafara wa watu 32 wanatarajiwa kuwasili nchini leo tayari kwa pambano lao la kujipima nguvu dhidi ya Tanzania, Taifa Stars.
Timu hiyo itatua Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) saa 11 kamili jioni kwa ndege ya PrecisionAir ikitokea Lusaka.
Mbali ya wachezaji 24, msafara wa Zambia ambayo inakuja nchini kwa ajili ya mechi dhidi ya Taifa Stars utakuwa na maofisa wengine wanane wakiwemo wa benchi la ufundi linaloongozwa na Kocha Herve Renard aliyeipa timu hiyo ubingwa wa Afrika mwaka jana nchini Gabon.
Wachezaji kwenye msafara huo ni Chintu Kampamba, Chisamba Lungu, Christopher Katongo, Danny Munyau, Davy Kaumbwa, Derrick Mwansa, Evans Kangwa, Felix Katongo na Francis Kasonde.
Given Singuluma, Hichani Himonde, Isaac Chansa, James Chamanga, Jimmy Chisenga, Jonas Sakuwaha, Joshua Titima, Kalililo Kakonje, Moses Phiri, Mukuka Mulenga, Rainford Kalaba, Rodrick Kabwe, Salulani Phiri, Shadrack Malambo na Stoppila Sunzu.
Mechi dhidi ya Taifa Stars itafanyika Jumamosi (Desemba 22 mwaka huu) kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 10 kamili jioni. Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager iko kambini jijini Dar es Salaam tangu Desemba 12 mwaka huu chini ya Kocha Kim Poulsen kujiandaa kwa mechi hiyo.
Viingilio katika mechi hiyo vitakuwa sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya bluu na kijani, sh. 7,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, sh. 10,000 kwa VIP C, sh. 20,000 kwa VIP B wakati VIP A itakuwa sh. 30,000.
Tiketi zinatarajiwa kuanza kuuzwa siku moja kabla ya mechi katika vituo vya Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, Uwanja wa Uhuru, Mgahawa wa Steers ulioko Mtaa wa Ohio na Samora, Sokoni Kariakoo, kituo cha mafuta cha Ubungo OilCom na Dar Live Mbagala.
Pia tiketi zitauzwa Ijumaa (Desemba 21 mwaka huu) kwenye tamasha la Kilimanjaro Premium Lager kuhamasisha washabiki wa Taifa Stars litakalofanyika kwenye viwanja vya Sigara, Chang’ombe.

Kikosi cha Zambia kilipokuwa kikishiriki michuano ya AFCON 2012

Maugo, Mbwana wawapania waganda


Kocha wa ngumi Pascal Mhagama kushoto anaemfua bondia Mbwana Matumla kwa ajili ya mpambano wake na David Chalanga wa kenya mpambano utakaochezwa Desemba 25 katika ukumbi wa Dar Live picha na www.superdboxingcoach.blogspot.com
Bondia Mbwana Matumla kushoto akionesha ufundi wa kutupa masumbwi mbele ya kocha wake Pascal Mhagama kwa ajili ya mpambano wake na David Chalanga wa kenya mpambano utakaochezwa Desemba 25 katika ukumbi wa Dar Live picha na www.superdboxingcoach.blogspot.com
Bondia Mada MAUGO AKILUKA KAMBA KWA AJILI YA MAANDALIZI YA MPAMBANO WAKE NAbondia Yiga Juma wa Uganda mpambano utakaofanyika Desemba 25 katika ukumbi wa Dar Live jijini Dar es salaam picha na www.superdboxingcoach.blogspot.com
Kocha wa Mchezo wa Masumbwi Said Chaku kushoto akimwelekeza bondia Mada Maugo jinsi ya kutupa Ngumi wakati wa mazoezi yake ya mwisho kwa ajili ya kumkabili bondia Yiga Juma wa Uganda mpambano utakaofanyika Desemba 25 katika ukumbi wa Dar Live jijini Dar es salaam picha na www.superdboxingcoach.blogspot.com
Bondia Mada Maugo kushoto akionesha umaili wa kutupa makonde na kocha wake Said Chaku wakati wa mazoezi yake ya mwisho kabla ya kupambana na bondia Yiga Juma wa Uganda Desemba 25 katika ukumbi wa Dar Live jijini Dar es salaam Picha na www.superdboxingcoach.blogspot.com

Kamote kurudiana na Mmalawi Des 29

Kamote akiwa na mataji anayoyashikilia kwa sasa

BONDIA mtanzania ambaye ni bingwa wa Dunia anayetambuliwa na World Boxing Forum, Allan Kamote anatarajiwa kwenda nchini Malawi ili kuzichapa na mwenyeji wake, Osgood Kayuni katika pambano litakalofanyika wiki ijayo.
Kamote aliyetwaa taji hilo la WBF Septemba 28 mwaka huu kwa kumpiga kwa TKO, Mmalawi Wellington Balakasi, atazichapa na Kayuni katika pambano la uzani wa Light raundi 10 litakalofanyika mjini Blantyre siku ya Desemba 29.
Hilo litakuwa pambano la marudiano baina ya mabondia hao kwani Februari mwaka huu walizichapa nchini huo na Kamote kupigwa kwa pointi, kitu "Natarajia kuondoka nchini siku ya Alhamisi kwenda Malawi kupigana na bondia aitwae Osgood Kayuni, ambayo nilipigana naye Februari mwaka huu na kunishinda kwa pointi, sidhani kama nitarudia tena makosa," alisema.
Kamote anayetokea mkoa wa Tanga, alisema anaendelea vema kujiandaa na pambano hilo na ana imani kubwa kurudia kile alichokifanya kwa Balakasi aliyempiga kwa TKO ya raundi ya nne na kutwaa ubingwa huo wa WBF.

Mwisho

Nusu fainali Kawambwa Cup kuanza kesho


NUSU fainali za michuano ya Kombe la Kawambwa inayoshirikisha timu za soka za Jimbo la Bagamoyo, inatarajiwa kuanza kutimua vumbi keshokuwa ambao timu nne zilizotiunga hatua hiyo zitachuana kuwania kucheza fainali.
Kwa mujibu wa msemaji wa michuano hiyo inayodhaminia na Mbunge wa Jimbo la Bagamoyo ambaye pia ni Waziri wa Elimu na Ufundi Stadi, Dk Shukuru Kawambwa, Masau Bwire, timu zilizofuzu hatua hiyo ni pamoja na Beach Boys, Mataya Fc, Chaulu na Matimbwa.
Masau alisema timu hizo zilizofua hatua ya roboi fainali iliyochezwa katika vituo viwili, zitaanza kupepetana katika  nusu fainali zitakazoanza kesho Alhamis kwa pambamo kati ya Chaulu Fc dhidi ya Mataya Fc.
"Nusu fainali ya pili itachezwa siku inayofuata yaani Ijumaa Desemba 21 kwa kuzikutanisha Beach Boys dhidi ya Matimbwa Fc, mechi zote zitachezwa katika uwanja wa Mwanakalenge na fainali itakuwa Jumapili," alisema Bwire.
Bwire alisema katika fainali hiyo, mgeni rasmi anatarajiwa kuwa Waziri Dk. Kawambwa ambaye atakabidhi kombe na zawadi nyingine kwea bingwa na washindi wengine wa michuano hiyo.
Msemaji huyo alisema michuano hiyo iliyoanza Septemba 25 mwaka huu ikishirikisha jumla ya timu 84 kutoka kata saba zilizopo jimbo la Bagamyoto za Dunda, Magomeni, Kiromo, Zinga, Kerege, Yombo na Vigwaza iliandaliwa na Waziri huyo kwa lengo la kuibua na kuendeleza vipaji vya soka ndani ya jimbo hilo na mkoa mzima wa Pwani.

Mwisho

Cheka, Mmalawi kuzipiga Boxing Day

Bondia Francis Cheka 'SMG'


BONDIA Francis Cheka 'SMG' ametamba kuwa yupo fiti tayari kwa pambano lake la kimataifa dhidi ya Mmalawi, Chiotcha Chimwemwe watakaovaana naye siku ya Boxing Day kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid, jijini Arusha.
Cheka atakayevaana na Chimwemwe katika pambano hilo la raundi 12 uzani wa Super Middle, alisema maandalizi aliyofanya kwa ajili ya mchezo huo yanampa imani ya kufanya vema kwa kumnyuka mpinzani wake.
"Nimejiandaa vya kutosha kuweza kufanya vema katika pambano lao dhidi ya Mmalawi litakalochezwa jijini Arusha, nawaahidi mashabiki wangu sintawangusha kwani kocha wangu Abdallah Saleh 'Komando' amenifua vya kutosha," alisema Cheka.
Naye mraribu wa pambano hilo litakalokuwa la kwanza kufanyika Arusha tangu mji uwe uwe jiji, Andrew George, alisema maandalizi ya mchezo huo utakaosindikizwa na mapambano ya mabondia wa miji ya Arusha na Moshi yamekamilika.
"Maandalizi yote ya pambano hilo yamekamilia kwa asilimia zote ikiwa ni pamoja na kumtumia tiketi bondia huyo wa Malawi," alisema George.
George alisema aliamua kulipeleka pambano hilo jijini humo kwa lengo la kuwapa burudani mashabiki wa mchezo wa ngumi wa mji huo sambamba na kuwapa fursa wakazi wa Arusha kuisherehekea vema sikukuu ya Krismasi.
Mratibu huyo alisema Cheka na Chimwemwe pamoja na mabondia watakaosindikiza pambano hilo watapimwa uzitoi na afya zao siku ya Krismasi tayari kupanda ulingoni Desemba 26.

Mwisho

Msondo, Sikinde kupambana Krismasi Equator Grill

Waimbaji wa Msondo Ngoma Eddo Sanga na Juma Katundu wakiwajibika jukwaani

Baadhi ya wanamuziki wa Mlimani Park 'Sikinde'
 
BAADA ya kila moja kupewa vyombo vipya na Konyagi, bendi pinzani za Msondo Ngoma 'Baba ya Muziki'  na  Mlimani Park Orchestra 'Sikinde Ngoma ya Ukae' zitapambana siku ya Krismasi katika ukumbi wa Equator Grill, Temeke.
Mpambano huo umeandaliwa na kampuni za Bob Entertainment na Keen Arts na kudhaminiwa na kinywaji cha Konyagi.
Mratibu wa mchuano huo Joseph Kapinga amesema pambano hilo litakuwa la kusherekea sikukuu ya Krismasi na kufunga mwaka 2012.
Kapinga alisema kuwa pia pambano hilo litaamua ni bendi gani bora kati ya magwiji hao wawili wa muziki wa dansi nchini kwa mwaka 2012.
Mratibu huyo alisema bendi hizo zitapiga jukuwaa moja lakini kila moja atatumia vyombo vyake ili kuondoa malamiko ya kuhujumiwa. Kila bendi itatumia muda wa saa moja kabla ya nyingine kupanda jukwani.
“Litakuwa pambano la aina yake ukizingatia kuwa hii itakuwa ni mara ya pili kwa bendi hizo kupambana siku ya Krismasi tangu zianzishwe. Mwaka jana zilipambana katika TCC Club Chang’ombe,” alisema Kapinga.
Alisema mchuano huo itaanza saa tisa alasiri hadi liamba.