STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, May 22, 2013

Wanajeshi wanne wafa Nachingwea wakienda Mtwara kutuliza ghasia


https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEgRZcHVZ3CvZsU4ZT-KF1Whe3ITc-0bHzMl3d37SUPMrVc13MZKx6Iyfu8r9S5f6pDFDQCE_88ubI9JuNojGoqUyfGvP_uPOAUTi0P2GDoMRS7hqdPbZejXJaJ4EuGl0SWFwOV1gPFuELQ/s400/3.JPG
Wanajeshi wakipokea mwili ya askari mwenzao. Picha hii haihusiani na habari hapo chini

WANAJESHI wanne wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) waliokuwa wakielekea Mtwara kusaidia kutuliza ghasia zinazoendelea mjini humo wamefariki dunia, huku wengine 20 wakijeruhiwa baada ya gari walilokuwa wakisafiria kupata ajali wilayani Nachingwea mkoani Lindi.
Habari zilizopatikana hivi punde na kuthibitishwa na baadhi ya mashuhuda zinasema kuwa ajali hiyo ilihusisha lori la wanajeshi hao na gari nyingine imetokea eneo la Kilimani Hewa, kilomita mbili toka kambi ya Jeshi hilo ya 41KJ wilayani humo.
Taarifa hizo zinasema kuwa jumla ya wanajeshi 31 walikuwa kwenye msafara huo na kwamba 20 wamejeruhiwa na kukimbizwa hospitali ya wilaya hiyo, huku wengine saba wakitoka salama bila ya kuwa na majeruhi yoyote.
Inaelezwa kuwa mwendo kasi na kona kali iliyopo eneo la tukio ndiyo chanzo cha ajali hiyo, ingawa Polisi bado haijathibitisha taarifa hizo kuhusiana na vifo vya wanajeshi hao wanne walioelezwa wamefariki katika ajali hiyo.
Mmoja wa mashuhuda wa tukio hilo, Viginia Ole Swai, amenukuliwa na kituo cha Radio One Stereo akisema huenda vumbi nalo lilichangia kutokea kwa ajali hiyo baada ya gari hizo kugongana katika ajali hiyo ambayo imepoteza uhai wa wapiganaji hao wa JWTZ wanne na wengine kujeruhiwa ambapo wapo hospitali wakitibiwa.

Azam Marine kuleta meli nyingine kali zaidi


 Muonekano wa Kilimanjaro 4
KAMPUNI ya Azam Marine, inaleta boti mpya ya Kilimanjaro 4, ambayo inatarajiwa kuwasili nchini, kuanzia mwishoni wa mwezi huu, ikiwa na uwezo wa kubeba abiria 700 na kutumia muda wa dakika 70 kwa safari moja ya kati ya Zanzibar na Dar es Salaam. Hii ni boti mpya kabisa katika muendelezo wa boti za Kilimanjaro, ambayo itakidhi mahitaji ya wasafiri wa eneo hili kwa kuwa inabeba sifa zote, ambazo ni Usalama, Kasi zaidi na Unadhifu. Kaa tayari kwa mzigo mpya kutoka Azam Marine.

Pellegrini athibitika kuondoka Malaga, milango i wazi kutua Man City

http://images.gazzetta.it/Media/Foto/2009/10/30/pelle_01.JPG
Kocha Manuel Pellegrini

MENEJA wa timu ya soka ya Malaga ya Hispania, Manuel Pellegrini amethibitisha kuwa ataondoka katika klabu hiyo mwishoni mwa msimu wa Ligi Kuu ya nchi hiyo.
Duru za michezo zinasema kuwa, Pellegrini atajiunga na Manchester City kuchukua nafasi ya kocha aliyetimuliwa katika timu hiyo, Muitaliano Roberto Mancini.
Kocha huyo alithibitisha mapema leo kwamba ataondoka katika benchi la ufundi la timu hiyo aliyokuwa akiinoa tangu mwaka 2010.
Akinukuliwa na mtandao wa Marca.com wa gazeti moja la nchini humo , kocha huyo alisema yeye na klabu hiyo wanaelekea kuachana, lakini umoja wao utaendelea kuwepo hata kama watatenganishwa na miji watakayokuwepo.
"Naondoka," alinukuliwa kocha huyo aliyoifikisha Malaga kwenye Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya kabla ya kutolewa na  Borussia Dortmund ambayo inatarajiwa kuvaana na wapinzani wao wa Ujerumani, Bayern Munich siku ya Jumamosi katika pambano la Fainali za mwaka huu.

Mkutano wa Tenga na wanahabari haupo tena kesho

 
Rais Tenga akiwa na Katibu Mkuu wa TFF, Angetile Osiah
ULE mkutano kati ya Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga na Waandishi wa Habari uliokuwa ufanyike kesho (Mei 23 mwaka huu) umeahirishwa mpaka hapo mtakapoarifiwa tena.
Taarifa iliyotumwa na Msemaji wa TFF, Boniface Wambura imesomeka kwamba mkutano huo wa kesho haupo kama ulivyokuwa umepangwa bila kufafanuliwa kilichosababisha kufutwa ghafla.
 

Mary Naali ashinda mbio za kimataifa za Marathon Romania

http://runners.ru/images/stories/atced.jpg
Mary Naali
MWANARIADHA wa Tanzania, Mary Naali, kutoka Klabu ya African Ambassadors Athletics (AAAC), ya Arusha ameibuka mshindi katika mbio za kimataifa za Bucharest. ‘Bucharest International Half Marathon’ nchini Romania, mwishoni mwa wiki.

Kwa mujibu wa mtandao wa Bucharest International Half Marathon, Naali alishinda akitumia saa 1:16.32 na kufuatiwa na Salome Albere wa Ethiopia 1:18.20, Mromania Nicoleta Petrescu alishika nafasi ya tatu kwa 1:20.24 huku wa nne akiwa ni Rodean Veronica kutoka Ujerumani 1:24.51 na tano bora ikafungwa na Gradinariu Alexandra wa Sweden 1:30.26.

Simba, Yanga zitaanza hivi Kagame Cup 2013

http://www.gushit.com/files/bookmark_photos/542db1350bL.jpg
Hamis Kiiza 'Diego' akiwa na taji la Kagame, Yanga ilipotwaa kwa mara ya pili mwaka jana jijini Dar


MABINGWA watetezi wa mashindano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame), Yanga wataanza kutetea taji lao dhidi ya Express ya Uganda katika mechi ya kundi C Juni 20 kwenye Uwanja wa Elfasher saa nane mchana wakati Simba iliyopangwa kundi A la 'kifo' itashuka dimbani siku inayofuata kuivaa El Mereikh.

Kwa mujibu wa ratiba ya mashindano hayo yatakayoanza Juni 18 hadi Julai 2 mwaka huu iliyotolewa jana na Shirikisho la Soka Afrika Mashariki na Kati (CECAFA), timu nyingine zinazounda kundi C pamoja na Yanga ni Vital'O ya Burundi na Ports ya Djibouti wakati kundia la kundi A la Simba linahusisha pia timu za APR ya Rwanda na Elman ya Somalia.

Ratiba hiyo inaonyesha kuwa kundi B limezoa timu wenyeji zote tatu za Al Hilal, Al Nasri na Al Ahly Shandy pamoja na Tusker ya Kenya na Super Falcon kutoka Zanzibar.

Yanga ambao ni mabingwa wapya wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara watashuka tena dimbani Juni 22 mwaka huu kuikabili Ports na watakamilisha mechi za hatua ya makundi Juni 25 kwa kuvaana na Vital'O.

Wawakilishi wengine wa Bara, Simba watatupa karata yao ya pili Juni 23 kwa kuwavaa APR na watamaliza na Elman Juni 26.

Mechi ya ufunguzi wa mashindano hayo itakayofanyika Juni 18 saa nane mchana itakuwa ni kati ya Tusker dhidi ya Super Falcon na saa 10:00 jioni Al Hilal itachuana na Al Nasri.

Katibu Mkuu wa CECAFA, Nicholas Musonye, alisema jana kuwa timu nane zitakazosonga mbele kucheza hatua ya robo fainali ambapo mbili kutoka makundi ya A na C, tatu kutoka kundi B na moja (best looser) itakayofanya vizuri kutoa kundi lolote.

Musonye alisema kuwa maandalizi ya mashindano hayo yamekamilika na zawadi za mashindano hayo mwaka huu zitaongezeka kufuatia wadau kujitokeza kusaidia michuano hiyo.

Alisema kwamba sasa CECAFA ina jumla ya Dola za Marekani 100,000 za zawadi lakini kiwango cha fedha watakachopata mabingwa, washindi wa pili na watatu kitajulikana baada ya kikao cha Kamati ya Utendaji ya shirikisho hilo itakayokutana kabla ya kuanza kwa mashindano hayo ya kila mwaka.

Mbunge Lema 'akanasa', Vodacom yamsafisha RC Arusha sms za vitisho dhidi yake


Mbunge wa Arusha, Godbless Lema

KAMANDA wa Polisi wa Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, amedai kuwa uchunguzi wa awali kuhusu ujumbe unaodaiwa kutumwa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo, umetumwa na mtandao wa simu wa nje ya nchi.

Kamanda alisema katika ujumbe huo ambao Lema anadai uliandikwa na Mkuu wa Mkoa Mulongo na kutumwa kwenye simu yake Aprili mwaka huu, uchunguzi wa polisi umeonyesha kwamba haukutumwa kupitia kampuni moja wapo ya simu za mikononi ya hapa nchini.

“Katika kipindi cha mwishoni mwa Aprili mwaka huu, vyombo vingi vya habari vikiwemo radio, magazeti na mitandao ya kijamii viliandika na kutangaza habari iliyoelezea shutuma zilizotolewa na Mbunge Lema kuwa aliandikiwa ujumbe wa vitisho kwa njia ya simu na Mkuu wa Mkoa Mulongo na ulisomeka:

“Umeruka kihunzi cha kwanza nitakuonyesha mimi ni serikali, ulikojificha nitakupata na nitakupa kesi inayoitaka mimi.”

Kamanda Sabas alisema ujumbe huo ulidaiwa kutumwa kutoka namba 0752960276 inayotumiwa na Mkuu wa Mkoa Mulongo kwenda kwenye namba 0764150747 inayotumiwa na Lema. Alisema kufuatia tuhuma hizo, polisi walianza uchunguzi kwa kuzingatia kuwa Mulongo alikanusha kutuma ujumbe wa aina yo yote kwa Mh Lema.

Alisema uchunguzi huo ulihusisha kampuni ya simu ambayo mtandao wake ulitumika katika utumaji wa ujumbe husika. Alisema uchunguzi wa awali wa polisi umebaini kuwa chanzo cha ujumbe huo mfupi hakikuwa kampuni ya simu husika (hakuitaja) kwa vile ‘Centre Number’ iliyotumika kutuma ujumbe huo mfupi wa maneno ni 44780200332, ambayo siyo ya mtandao wa kampuni husika bali ni ya mtandao ulio nje ya nchi.

Alisema uchunguzi zaidi unaendelea kubaini chanzo cha ujumbe huo mfupi wa simu na mtu aliyehusika kutuma hatua za kisheria zitaweza kuchukua mkondo wake.


BARUA  TOKA  VODACOM
 

Tenga kutetea na wanahabari kesho

 
Rais wa TFF Leodger Tenga

Na Boniface Wambura
RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Leodegar Tenga anatarajiwa kuteta na waandishi wa habari katika mkutano utakaofanyika kesho asubuhi.
Mkutano huo wa kesho (Mei 23 mwaka huu) uanatarajiwa kufanyika kuanzia saa 5 kamili asubuhi kwenye ukumbi wa mikutano wa TFF, Ilala jijini Dar es Salaam.



Mtwara hali tete, mabomu risasi zatawala

Baadhi ya matukio yanayoendelea Mtwara
HABARI zilizotufikia hivi punde zinasema hali ni tete mjini Mtwara, hakuna amani, mabomu ya machozi yanarindima muda huu na huduma zote za kijamii zimefungwa hakuna usafiri, masoko, maduka na bar zote zimefungwa, daladala, Taxi na Bodaboda hazifanyi kazi.  
 
Kwa ujumla kinachoendelea ni mapambano makali kati ya Jeshi la polisi na wananchi wenye hasira wanaopinga vikali kuendelea kwa mchakato wa gesi ilihali nchi ikiwa haina sera inayosimamia nishati hiyo.
 
Kufuatia Kambi ya Upinzani kuukataa mpango wa serikali wa ujenzi wa bomba la gesi kutoka Mtwara Mpaka Dar es salaam ilihali Waziri wa Nishati akisoma hotuba yake kwa hisia kali na mbwembwe na kusema bomba la gesi linajengwa kutoka Mtwara kwenda Dar es salaam Wananchi wa Mtwara walicharuka!
 
 Daraja la Mikindani limevunjwa hakuna mawasiliano Mtwara na Dar es salaam.
 
Baadhi ya Wananchi wamepora Silaha na wanazitumia kujibu mashambulizi ya Jeshi la Polisi (habari haijathibitishwa rasmi)
 
 Jengo la Ofisi ya CCM saba saba limechomwa moto. 
Lodge/Hotel (Shengena) inayoaminika kwamba ndiyo waliyofikia Askari wa Jeshi la Polisi (FFU) kutoka mikoa ya jirani kwaajili ya operation inayoendelea imechomwa moto.
 
Milio ya risasi na mabomu ndicho kinachosikika. 
Nyumba kadhaa  za watumishi  wa Serikali  zimechomwa  maeneo ya Shangani.

Ni magari ya FFU ndio yaliyopo barabarani nayo yanapata wakati mgumu kupita kwasababu ya mawe na magogo makubwa yaliyowekwa na Wananchi. 
Askari kadhaa wamekufa (habari hii haijathibitishwa rasmi)
Baadhi ya watu kadhaa wamechukuliwa na askari kwakuwa wamepita jirani na gari yao.
 Yadaiwa askari wengi waliokuja si wa Mtwara, wengi wametoka Masasi na Lindi. 
 Ving'ora vinalia hovyo. Watoto wamefungiwa mashuleni walimu wamekimbia. 
 Vituo vya Redio vya Mtwara havizungumzii hali hii ya hatari bali vinapiga Muziki pengine vinakusanya matukio na habari ya majanga haya ili Wananchi wayapate.
 Mabomu yanapigwa mfululizo maeneo ya Magomeni-Mtwara, mpaka sasa takriban mabomu 20 na ushee yameshapigwa.

Msouth kuzihukumu Stars na Morocco, TFF yaanika ratiba ya mazoezi ya Stars


https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEj5ta_2ly1qlzIPEMvk9-7RZw-jUtAQOF_M1x8hzY9FkGokWUR35u8p492S6fv93ojEEaSwnv5Isx0Oqz1sXA0ns71kzAKekOc-WhQCB9ETEs3ExFRGtjo1Zz6_8tQNl1uqOcAqy2IGfwjF/s1600/Daniel_Bennett.jpg
Refa Frasser Daniel Bennett atakayezichezesha Tanzania na Morocco

Na Boniface Wambura
SHIRIKISHO la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA) limemteua mwamuzi kutoka Afrika Kusini kuchezesha mechi ya mchujo ya Kombe la Dunia, Kanda ya Afrika kati ya Tanzania (Taifa Stars) na wenyeji Morocco (Lions of the Atlas).

Mechi hiyo ya kundi C itachezwa Juni 8 mwaka huu jijini Marrakech, Morocco kwenye Uwanja wa Grand kuanzia saa 3 kamili usiku kwa saa za Morocco. Mwamuzi atakayechezesha mechi hiyo ni Fraser Daniel Bennett.

Bennett atasaidiwa na Thusi Zakhele Siwela pia wa Afrika Kusini, wakati mwamuzi msaidizi namba mbili atakuwa ni Marwa Range kutoka Kenya. Mwamuzi wa akiba (fourth official) ni Lwandile Mfiki wa Afrika Kusini.

Kamishna wa mechi hiyo ni Robert Mangollo-M’voulou wa Gabon wakati mtathimini wa waamuzi (referee assessor) ni Charles Masembe kutoka Uganda.

Taifa Stars ambayo iko chini ya Kocha Kim Poulsen, na ikidhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager tayari iko kambini katika hoteli ya Tansoma ikiendelea kujinoa kwa ajili ya mechi hiyo ambapo kabla itajipima na Sudan (Nile Crocodiles) Juni 2 mwaka huu jijini Addis Ababa, Ethiopia.



Ratiba ya mazoezi kwa timu hiyo ni kama ifuatavyo;
Mei 22                 Saa 10 jioni                             Uwanja wa Karume

Mei 23                 Saa 1 asubuhi na Saa 10 jioni   Uwanja wa Karume

Mei 23                 Saa 10 jioni                             Uwanja wa Karume

Mei 25                 Saa 1 asubuhi na Saa 10 jioni     Uwanja wa Karume

Mei 26                 Saa 3 asubuhi                            Uwanja wa Karume