STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, January 19, 2012

'Ajuza' afyatua kibao na Mhe Temba




UNAWEZA kudhani ni utani, ila ukweli ni kwamba msanii chipukizi lakini mwenye umri mkubwa wa zaidi ya miaka 50, Mwanahija Cheka 'Bi Cheka' amefyatua kibao kipya cha miondoko ya kizazi kipya akishirikiana na nyota wa miondoko hiyo nchini, Mheshimiwa Temba.
Meneja wa msanii huyo, Said Fella, alisema kibao cha Bi Cheka kiitwacho 'Ni Wewe', kimerekodiwa katika studio za Poteza Records, chini ya utayarishaji wa Suleiman Daud 'Sulesh' au 'Mr India'.
Fella, alisema tofauti na umri wake wa miaka 51, Bi Cheka 'amechana' mno katika kibao hicho, kiasi kwamba hata Mheshimiwa Temba alimvulia kofia wakati wakirekodi.
"Huwezi amini, hajawahi kuimba kokote zaidi ya kuimba kaswida alipokuwa chuo, akimtaja mkongwe wa muziki wa dansi nchini, Maalim Muhidin Gurumo ndiye aliyekuwa mwalimu wake, lakini kazi kubwa aliyofanya kwenye wimbo huo mpya inashangaza," alisema Fella.
Aliongeza, ndani ya kibao hicho Bi Cheka anamlilia Temba awe wake kimapenzi, huku Temba akijaribu kumtolea nje kitu kilichoufanya wimbo huo kuwa wa kusisimua ambapo wanatarajia kuusambaza katika vituo vya redio kwa ajili ya kurushwa hewani.
Fella alisema mbali na kujipanga kuusambaza wimbo huo, pia wameanza maandalizi ya kufyatua video yake, huku wakiendelea kumrekodiwa nyimbo nyimbo kwa ajili ya albamu yake ambayo alisema huenda ikawa na nyimbo nane au kumi.
"Video ya kibao hicho ambacho Bi Cheka ameimba hip hop na kuchana mistari kama Da Brat (msanii nyota wa miondoko hiyo wa nchi ya Marekani), tunatarajia kuanza kurekodi wakati wowote kuanzia sasa," alisema Fella.
Fella, alisema msanii huyo aliwasiliana nae kumuomba amsaidie kumtolea kazi baada ya kusikia ana kituo cha kukuza na kuendeleza vipaji, ingawa alisitiza awali kwa umri alionao, lakini alimsihi ampe nafasi na mwenyewe ameridhika nae kwa uwezo mkubwa wa kuimba na upangiliaji wa sauti alionao.

Dar Modern kuzindua tatu kwa mpigo



KUNDI linalokimbiza kwenye miondoko ya mwambao nchini, Dar Modern Taarab 'Wana wa Jiji' wanatarajia kuzindua kwa mpigo albamu zao tatu mpya katika onyesho litakalofanyika mwezi ujao jijini Dar es Salaam.
Albamu hizo tatu za kundi hilo ni 'Sikukuchagua kwa Mapesa', 'Ndugu wa Mume Mna Hila' na 'Toto la Kiafrika' ambazo kila moja ina nyimbo nne.
Akizungumza na MICHARAZO jana, Mkurugenzi wa kundi hilo, Mridu Ally Mridu 'Tx', alisema uzinduzi huo utafanyika mwishoni mwa Februari, mara baada ya kuwasili kwa kanda za kaseti za albamu hizo ambazo zinatengezwa kwa sasa nchini Kenya.
Mridu, alisema uzinduzi wao wamepanga kuufanya katika ukumbi wa Hoteli ya Travertine-Magomeni ama Diamond Jubilee yote ya jijini Dar es Salaam.
"Tupo katika mipango ya kufanya uzinduzi wa albamu zetu tatu kwa mpigo utakaofanyika ama Travertine au Diamond. Kwa sasa tunasubiri kaseti za albamu hizo zinazotengenezwa Kenya, kuwasili nchini ili tupange tarehe rasmi ya kufanyika kwa uzinduzi huo, ila utafanyika mwishoni mwa Februari," alisema.
Mridu alisema katika onyesho hilo la uzinduzi watawatambulisha wasanii wao wapya waliowanyakua hivi karibuni katika kuliimarisha kundi lao ambalo liliondokewa na mastaa wao kadhaa akiwemo Hammer Q, Hashim Said 'Big Sound' na wengineo.
Pia alisema mbali na kuzindua albamu mpya kwa kupiga nyimbo 12 za albamu hizo, pia watakumbushia nyimbo za albamu zao za zamani kama 'Ni Vijimambo Tu', 'Sote Twasaka Riziki', 'Kitu Mapenzi' na 'Gharika ya Moyo' maarufu kama 'Pembe la Ng'ombe'.
"Yaani itakuwa full burudani kwa namna tukavyowapa mashabiki wetu vitu mchanganyiko, kuanzia vile vya awali hadi hivyo vipya pamoja na kuutambulisha mtindo wetu mpya wa kunengua," alisema Mridui.
Kundi hilo la Dar Modern lilianzishwa rasmi mwaka 2006 likiundwa na wasanii mchanganyiko waliotoka kundi la Babloom Modern Taarab na mengine ya jijini Dar es Salaam.

Asilimia 80 ya waandishi wa habari hawajaajiriwa

RAIS wa Umoja wa Vilabu vya Waandishi wa Habari (UTPC), Kenneth Simbaya, amesema zaidi ya asilimia 80 ya waandishi wa habari nchini hawajaajiriwa na hawana mikataba ya aina yoyote ya kazi na wamiliki wa vyombo vya habari, licha ya kwamba wanafanya kazi katika mazingira magumu .
Simbaya aliyasema hayo jana, baada ya kutembelea Klabu ya Waandishi wa Habari Mkoani Kilimanjaro (MECKI) na kuzungumza na wajumbe wa kamati ya utendaji ya klabu hiyo iliyopo mjini Moshi.
Alisema utafiti uliofanywa na UTPC, umebaini zaidi ya asilimia 80 ya waandishi wa habari hapa nchini wanajitegemea kutafuta habari katika maeneo ya mjini na vijijini na hata kwenye maeneo ya hatari bila kuajiriwa ama kuwa na mikataba na wamiliki wa vyombo wanavyovifanyia kazi.
Alisema mwandishi pia amekuwa akilipwa ujira mdogo wa Sh. 5,000 na 3,000 hadi Sh. 1,500 kwa habari moja inayotoka gazetini, licha ya gharama kubwa anazotumia kutafuta habari hizo na kuwafikishia wenye vyombo vya habari.
Alisema kutokana na tatizo hilo kuwa kubwa, UTPC inafanya jitihada za makusudi kuwasiliana na wamiliki wa vyombo vya habari ili kuangalia namna waandishi wa habari wanakuwa na mikataba ya ajira kazini na hata kuendelezwa kitaaluma pindi wanapokuwa kazini kwa muda mrefu.
Alisema UTPC pia inakusudia kuanzisha vyombo huru vya habari yakiwemo magazeti, redio na televisheni, vitakavyowawezesha waandishi wa habari kuwa na vyombo vyao vinavyotumia habari sahihi na zilizofanyiwa utafiti na uchunguzi wa kina bila upendeleo.
Alitoa wito kwa waandishi wa habari pamoja na kufanyakazi katika mazingira magumu nay a hatari, kuzingatia maadili ya kazi zao na kuepuka kutumiwa na baadhi ya wamiliki wa vyombo vya habari kwa malengo yao binfsi.
Hivi karibuni Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Leonidas Gama, alisema waandishi wengi wa habari wamekuwa wakifanya kazi kubwa na hata kuhatarisha usalama wa maisha yao, lakini hawalipwi mishahara kulingana na kazi wanazozifanya na badala yake wamegeuka kuwa ombaomba .
Mkuu huyo wa mkoa alisema waandishi wengi wamekuwa wakiishi kwa njia za kiujanja ujanja ili kusukuma maisha yao.

NB:Imeandikwa na Jackson Kimambo, NIPASHE-Moshi