STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, July 9, 2011

Ligi ya Kick Boxing yaiva

MICHUANO ya Ligi ya Kick Boxing inatarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu jijini Dar es Salaam kwa mabondia wa kike na wa kiume kuumana kuwania ushiriki wa fainali za taifa zitakazofanyika baadaye mwaka huu.
Kwa mujibu wa mratibu wa michuano hiyo, Japhet Kaseba, alisema michuano hiyo itafanyika Julai 31 kwenye ukumbi wa DDC Mlimani, Mwenge jijini Dar es Salaam.
Kaseba, alisema kabla ya kufanyika kwa michuano hiyo anatarajiwa kukutana na mabondia washiriki kwa lengo la kuwapa darasa dhidi ya mchezo huo ambao safari hii utashirikisha wakongwe na chipukizi ikiwa ni mikakati ya kuendeleza mchezo huo.
"Michuano yetu ya ligi ya Kick Boxing itafanyika mwishoni mwa mwezi huu kwenye ukumbi wa DDC Mlimani, ambapo mabondia mbalimbali wake wa waume chipukizi na wakongwe wataonyesha kazi safari hii," alisema.
Kaseba alisema kwa sasa anaendelea na mipango ya kusaka wadhamini kwa ajili yua kulipiga tafu shindano lao ambalo limekuwa kikifanyika kwa mwaka wa tatu sasa katika njia ya kurejesha msisimko wa michuano hiyo iliyompa mataji ya Afrika na Dunia.
Katika hatua nyingine bingwa wa Kick Boxing wa Uganda, Moses Golola, alifanikiwa kumchakaza bondia toka Sudan, Abdul Quadir Rahim mwishoni mwa wiki jijini Kampala, akisisitiza ana hasira ya kutaka kupigana na Kanda Kabongo wa Tanzania.
Golola aliyepigwa na Kabongo katika pambano la kuwania ubingwa wa Afrika, alisema ushindi wake wa KO ya raundi ya pili dhidi ya Msudan ni salamu kwa Kabongo kuwa ajiandae kwa ajili ya kisasi siku wakikutana ambapo huenda ikawa ndani ya mwaka huu.

Klabu za ngumi kupepetana Ilala

KLABU za ngumi za ridhaa za Amana na Matimbwa ni miongoni mwa klabu zaidi ya tano zinazotarajiwa kuonyeshana kazi katika mfululizo wa michuano maalum ya mchezo huo inayoendelea wilayani Ilala jijini Dar es Salaam.
Klabu zingine zitakazopambana katika michezo itakayofanyika mwishoni mwa wiki hii ikiratibiwa na taasisi ya Kinyogoli Foundation ni Ashanti, Big Right na zingine ambazo hazikuweza kufahamika mapema.
Mratibu wa michuano hiyo, Rajab Mhamila 'Super D' alisema michezo hio itafanyika Jumamosi kwenye ukumbi wa Panandipanandi, Ilala Bungoni.
Super D, alisema maandalizi ya michezo hiyo yamekamilika ikiwemo vikosi vya timu zote kuendelea kujifua.
Aliwataja baadhi ya mabondia watakaoziwakilisha klabu zao kuwa ni Ibrahim Class, Khalfan Othman, Kassim Sambo na Saidi Ally kwa upande wa Amana, wakati Matimbwa itawakilishwa na Mohamed Matimbwa, Mohamed Muhani, Edson Joviki na Mohamed Kumbilambali.
Kwa upande wa Ashanti, Super D alisema itawakilishwa na mabondia kama Uwesu Manyota, Ramadhani Kimangale, Mark Edson na wengine na mipambano yao itachezwa kwa raundi nne nne kila mmoja.
Aliongeza kwa kutoa wito kwa wadau wa ngumi kujitokeza kuzisaidia klabu shiriki na mabondia vifaa vya michezo na mahitaji yao mengine ili kuwatia moyo wa kuupenda mchezo huo.