STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, January 31, 2013

BREAKING NEWS: DIZUMBA WA MAJIMAJI AFARIKI

HABARI zilizotufikia muda huu zinasema kuwa aliyekuwa Makamu Mwenyekiti wa klabu ya Majimaji Songea inayojiandaa na duru la pili la Ligi Daraja la Kwanza Tanzania Bara, Ahmed Dizumba amefariki dunia.
Taarifa zilizopatikana asubuhi hii ambazo MICHARAZO inaendelea kuzifuatilia kwa ukaribu zinasema Dizumba amefariki usiku wa kuamkia leo na anatarajiwa kuzikwa leo mjini Songea.
Kwa yeyote mwenye taarifa zaidi anaweza kutupenyezea, juu ya msiba huu ulioikumba Majimaji ikiwa katika harakati za kuanza duru la pili la ligi daraja la kwanza kuwania kurejea ligi kuu.
Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na TFF, Majimaji imepangwa kuanza utepe wa duru hilo kwenye uwanja wake wa Majimaji Songea kuvaana na Kurugenzi mechi ya kundi A.

Mtibwa Sugar ipo tayari kuivaa Yanga, Mgosi majaribuni...!

Kocha wa Mtibwa Mecky Mexime

TIMU ya soka ya Mtibwa Sugar imesema imejiandaa vya kutosha kuweza kuwakabili vinara wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga watakaovaana nao keshokutwa jijini Dar es Salaam.
Mtibwa inatarajiwa kuvaana na Yanga katika mfululizo wa mechi za ligi hiyo duru la pili ikiwa na kumbukumbu ya kipigo cha bao 1-0 walichopewa nyumbani kwao na Polisi Morogoro.
Katika pambano lao la awali Mtibwa iliisasambua Yanga mjini Morogoro kwa mabao 3-0, hali inayofanya pambano hilo la marudiano kuwa la aina yake, ndio maana benchi la ufundi la timu hiyo limedai kuwa limepania kurekebisha makosa mbele ya wapinzani wao wanaoongoza msimamo wa ligi hiyo kwa sasa.
Kocha wa Mtibwa, Mecky Mexime, amesema kuwa kikosi chao kipo katika hali nzuri kuweza kuikabili Yanga na kuendeleza ubabe wao, licha ya kukiri wanatarajia upinzani mkali.
Mexime, alisema hana shaka na pambano hilo kwa namna alivyoweza kurekebisha makosa yaliyowagharimu katika pambano lao lililopita walilopoteza nyumbani.
"Tumejiandaa na tupo tayari kuivaa Yanga na hatuna hofu yoyote, vijana wangu wapo kamili kuweza kurekebisha makosa yaliyotuponza kwa Polisi Moro," alisema Mexime.
Mexime, alisema ushindi pekee ndiyo kitu kinachohitajika kwa Mtibwa ili kuweza kujipanga kwa ajili ya kumaliza nafasi za juu mwishoni mwa msimu.
Mbali na mechi hiyo ya Yanga na Mtibwa, siku hiyo ya jumamosi kutakuwa na mechi nyingine kadhaa kabla ya Jumapili Mabingwa watetezi, Simba kuvaana na JKT Ruvu ambayo .inatarajiwa kumtumia nyota wqa zamani za Msimbani Mussa Hassani Mgosi kuweza kuwasimamisha Simba walioilaza Africans Lyon katika mechi yao iliyopita.

Manchester United yazidi kujichimbia kileleni Ligi ya England

Rooney akipachika mpira wavuni


MABAO mawili yaliyopachikwa wavuni na mshambuliaji Wayne Rooney imeiwezesha Manchester United kuendelea kujikita kileleni mwea msimamo wa Ligi Kuu ya England baada ya kuilaza Southampton kwa mabao 2-1 katika mfululizo wa ligi hiyo.
Mashetani hao Wekundu waliokuwa uwanja wao wa nyumbani wa Old Trafoord, walijikuta wakishtukizwa kwa kufungwa bao la mapema na wageni wao lililofungwa na Jay  Rodriguez dakika ya tatu tu ya mchezo huo, hata hivyo dakika tano baadae Rooney aliwatuliza mashabiki wa timu yake kwa kusawazisha bao.
Rooney aliendelea kung'ara kwa kuongeza bao la pili dakika ya 27 akimalizia kazi nzuri ya Patric Evra na kufanya hadi mapumziko timu hizo ziwe zimefungana mabao 2-1 yaliyomudu hadi zilipomalizika dakika 90 za pambano hilo.
Kwa ushindi huo Manchester imeongeza pengo la pointi saba kati yao na wapinzani wao, Manchester City ambayo juzi ililazimishwa sare na kusalia na pointi zao 52 huku timu zote zikiwa zimecheza mechi 24 kila mmoja.
Katika mapambano mengine yaliyochezwa usiku wa jana, Liverpool iliwabana wenyeji wao Arsenal na kufungana nao mabao 2-2, huku Norwich City ilijikuta ikibanwa mbavu nyumbani kwa kulazimishwa sare ya bao 1-1.
Nayo Reading iliing'ang'ania waliokuwa mabingwa watetezi wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, Chelsea kwa kufungana nao magoli 2-2 na Fulham iliicharaza West Ham United mabao 3-1 na Everton iliendeleza maajabu wake msimu huu kwa kupata ushindi wa mabao 2-1 mbele ya West Bromwich.
Ligi hiyo inatarajiwa kuingia mzunguko wa 25  mwishoni mwa wiki kwa mechi katika viwanja mbalimbali nchini humo.
Rooney akishangilia moja ya mabao yake ya jana



Balotelli ilibidi tu aondoke - Mancini


Kocha Mancini akiwa na Balotelli wakipeana majukumu wakati walipokuwa pamoja Manchester City

KOCHA wa Manchester City, Roberto Mancini amesema kuondoka kwa Mario Balotelli kwenda AC Milan kunaifanya timu yake ipungukiwe wachezaji.
Sare yao ya 0-0 dhidi ya QPR usiku wa kuamkia jana iliwaacha mabingwa wakiwa hatarini kupitwa zaidi na vinara Manchester United, ambao usiku wa kuamkia leo walitarajiwa kucheza dhidi ya Southampton.
"Ni ngumu kwa sababu nimempoteza mchezaji mmoja muhimu na ambaye angekuwa muhimu katika mechi 14 zijazo," alisema Mancini.
"Lakini ilikuwa ni muhimu kwa Mario kurejea Italia, kurejea kwenye familia yake na kuchezea Milan."
Mancini anaamini kwamba Balotelli amefanya kazi "nzuri sana" katika miaka yake miwili na nusu akiwa na Man City, ingawa amekubali kwamba msimu huu ulikuwa mgumu zaidi kwa mshambuliaji huyo.
Mancini pia haraka alikanusha mtazamo kwamba kuondoka kwa Balotelli kumetokana na ugumu wa kumdhibiti mshambuliaji huyo mtata.
"Hapana, hapana, hapana, siyo kwangu," alisema. "Kwangu mimi, Mario alikuwa kama mwanangu mwingine.
"Mario yuko hivyo lakini anaweza kukufadhaisha wakati mwingine.
"Klabu imeniambia kwamba imepokea ofa kutoka Milan. Nilizungumza na Mario na nadhani alitaka uhamisho huu.
"Nadhani kwake kucheza miaka mitatu England na kisha kurejea Italia itakuwa ni jambo zuri kwake."
Balotelli alitambulishwa rasmi jana na klabu yake mpya ya AC Milan akikabidhiwa jezi yenye namba kama alivyokuwa akiitumia alipokuwa City, 45.

AZAM, JKT OLJORO ZAZIDI KUPAA LIGI KUU BARA

 
TIMU za soka za Azam na JKT Oljoro zimezidi kupeta katika mfululizo wa Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya jana kuendeleza wimbi la ushindi katika mechi zao zilizochezwa katika miji tofauti ya Dar na Arusha.
Azam iliibuka na ushindi wa mabao 3-1 dhidi ya Toto Africans ya Mwanza katika mchezo uliochezwa kwenye uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
Mabao ya Azam katika mchezo huo yametiwa kimiani na Kipre Michael Balou wa Ivory Coast, dakika ya tisa, Mganda, Brian Umony dakika ya 20 na Mkenya Humphrey Mieno dakika ya 46.
Bao la kufutia machozi la Toto lilitumbukizwa kimiani katika dakika ya 77 na Selemani Kibuta, ambalo hata hivyo halikuwaongezea lolote na kuifanya timu hiyo kupioteza mechi ya pili mfululizo kwa idadi ya mabao hayo 3-1.
Toto ililazwa idadi hiyo na Oljoro JKT katika mechi iliyochezwa mjini Arusha Jumamosi iliyopita, ambapo jana timu hiyo ya maafande wa JKT waliendeleza wimbi la ushindi kwa kuilaza Kagera Sugar kwa mabao 2-0.

TAIFA STARS KUIVAA CAMEROON WIKI IJAYO


Na Boniface Wambura
TANZANIA (Taifa Stars) itacheza na Cameroon katika moja ya mechi za kirafiki za Kalenda ya Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA)- FIFA Date zitakazofanyika duniani kote Februari 6 mwaka huu.
Mechi hiyo itafanyika kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 11 kamili jioni. Kikosi cha Cameroon kinachoundwa na wachezaji wengi wa kulipwa wanaocheza katika nchi mbalimbali duniani kitaanza kuwasili nchini Februari 3 mwaka huu.
Nchi kadhaa ziliomba kucheza na Taifa Stars katika tarehe hiyo ya FIFA, lakini Kocha wa Stars, Kim Poulsen ameamua kucheza mechi hiyo dhidi ya Cameroon ambayo nahodha wake ni mchezaji nyota wa kimataifa, Samuel Etoo Fils.
Congo Brazzaville, Equatorial Guinea, Rwanda na Swaziland nazo zilikuwa zimeomba kucheza dhidi ya Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager. Ukiondoa Swaziland iliyotaka mechi hiyo ichezwe Dar es Salaam, nyingine zilitaka kucheza nyumbani kwao.
Wakati huo huo, Kocha Kim Poulsen atakutana na Waandishi wa Habari kuzungumzia maandalizi ya mechi hiyo ikiwemo kutaja kikosi ambacho atakitumia. Mkutano huo utafanyika saa 5 kamili asubuhi kwenye ukumbi wa mikutano wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).

Madrid yaidindia Barca Kombe la Mfalme

Cesc Febregas akishangilia bao katika pambano la jana la El Clasico
MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu ya Hispania, Real Madrid usiku wa kuamkia leo iliikomalia vinara wa ligi hiyo, Barcelona kwa kulazimishwa sare ya bao 1-1 katika pambano la nusu fainali ya kwanza ya Kombe la Mfalme katika pambano lililochezwa kwenye uwanja wake wa nyumbani, mjini Madrid.
Ikicheza bila baadhi ya nyota wake kutokana na kutumikia adhabu na kuwa majeruhi, Real Madrid iliibana Barca na kwenda nao mapumziko wakiwa nguvu sawa bila kufungana.
Kipindi cha pili kilianza kwa kasi na Barcelona kuwashtua wenyeji wao kwa kujipatia bao la kuongoza lililofungwa dakika ya 50 na kiungo Cesc Fabregas akimalizia kazi nzuri ya Lionel Messi.
Timu hizo zilizoenda kushambuliana na kufanya kosa kosa kadhaa na kwenye dakika ya 81, wenyeji walifanikiwa kusawazisha bao hilo kupitia kwa Raphael Varane aliyemaliza kazi murua ilioyofanywa na Mjerumani Mesut Ozil.
Wapinzani hao wa jadi wa nchini Hispania wanatarajiwa kurudiana mwishoni mwa mwezi Februari, ambapo ndiyo itaamua hatma ya timu ipi itinge fainali za michuano hiyo kuungana na mshindi kati ya Sevilla na Atletico Madrid ambazo nufa fainali yao ya kwanza inatarajiwa kuchezwa kesho mjini Madrid kabla ya kwenda kurudiana nyumbani kwa Sevilla.
Katika pambano hilo la El Clasico lililoshuhudia Barcelona ikiwatumia wachezaji wake waliokuwa nje kwa muda mrefu kwa majereha, wachezaji sita, watatu kila upande wakionyeshwa kadi za njano kwa makosa mbalimbali.