STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, April 15, 2014

Azam yawekwa rekodi saba Tanzania Bara

Mabingwa wa Tanzania Bara, Azam Fc
TIMU ya Azam ambayo juzi ilitwaa ubingwa wa Tanzania Bara kwa msimu wa 2013/14, imeweka rekodi saba kwenye medani ya soka nchini.
Azam iliifunga Mbeya City mabao 2-1 kwenye uwanja wa Sokoine na kuweka rekodi ya kuwa timu pekee iliyoifunga timu hiyo kwenye uwanja wake wa nyumbani.
Awali, Mbeya City ilikuwa haijawahi kufungwa kwenye uwanja wake wa nyumbani kabla ya rekodi yake kuvunjwa na Azam.
Mabingwa hao wameifikia pia rekodi ya Simba ya kutwaa ubingwa bila ya kupoteza mechi ya msimu wa 2009/10 na sasa wanafukuzia rekodi nyingine ya 'Wekundu wa Msimbazi' ya kumaliza msimu bila ya kupoteza mechi wakati watakapowakabili JKT Ruvu katika mechi yao ya mwisho ya msimu.
Mbali na hilo, pia wameweka rekodi ya kuwa timu ya tisa kutwaa ubingwa wa Tanzania Bara tangu ligi hiyo ilipoanza.
Azam pia imekuwa ni timu ya saba kutwaa ubingwa huo nje ya miamba wawili wa soka nchini ambao wamekuwa wakipokezana ubingwa huo, Simba na Yanga.
Timu nyingine ambazo zimeshawahi kufanya hivyo, nazo ni Cosmopolitan ya Dar es salaam mwaka 1967, Mseto Sports ya Morogoro (1975), Pan African (1982), Tukuyu Stars (1986), Coastal Union (1988) na Mtibwa Sugar mwaka 1999 na 2000.
Rekodi nyingine ni kuwa timu ya tano kutoka jijini Dar es Salaam kutwaa ubingwa wa Bara, ikizifuata timu za Simba, Yanga, Cosmopolitan na Pan African.
Lakini vile vile Azam imekuwa ni timu ya kwanza kutoka nje ya Manispaa ya Ilala kutwaa ubingwa kwani timu za Simba, Yanga, Cosmopolitan na Pan African zinatoka Ilala, huku yenyewe ikitokea Temeke.
Vile vile imekuwa ni timu ya pili ya kampuni kutwaa ubingwa nchini baada ya Mtibwa Sugar kufanya hivyo mwaka 1999 na 2000.
Timu hiyo imetwaa ubingwa kwa pointi 59 ambazo hazitafikiwa na timu yoyote kwenye mechi ya kuhitimisha Ligi Kuu Jumamosi.
Wakati huo huo, Sanula Athanas, anaripoti kuwa wadhamini wakuu wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL), Kampuni ya Mawasiliano ya Vodacom Tanzania, wameipongeza Azam FC kwa kutwaa ubingwa wa ligi hiyo msimu huu msimu ikiwa ni mara ya kwanza tangu ipande miaka saba iliyopita.
Azam inayonolewa na Mcameroon Joseph Omog ilitwaa ubingwa huo juzi baada ya kuifunga Mbeya City 2-1 katika raundi ya 25 ya ligi hiyo na kufikisha pointi 59 ambazo haziwezi kufikiwa na timu yoyote msimu huu.
Mara tu baada ya kumalizika kwa mechi hiyo kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Sokoine mjini Mbeya juzi, Meneja Uhusiano wa Nje wa kampumi hiyo, Salum Mwalim alisema wameridhishwa na kiwango cha Azam FC pamoja na timu zote zinazoshiriki katika ligi na hivyo wanawapongeza kwa dhati timu hiyo kutwaa taji.
"Tunawapongeza Azam kwa kuwa bingwa mpya wa VPL kwa sababu wamekabiliana vema na mikikimikiki ya ligi, hivyo ubingwa wao haukuwa mwepesi kuupata kutokana na ushindani uliokuwapo kwa timu zote shiriki," alisema Mwalim.
"Tunaamini ubingwa huu wa Azam utaifanya ligi msimu ujao kuwa ngumu zaidi kwani timu za Yanga na Simba ambazo zimekuwa zikipokezana ubingwa tangu 2001 zitataka kurudisha heshima yao na nyingine zikipata nguvu kwa kuwa yoyote inaweza kuwa bingwa, na hilo likitokea ubora wa ligi yetu utazidi kupaa," alisema zaidi Mwalim.
Alisema Azam watakabidhiwa kombe lao la ubingwa Jumamosi kwenye uwanja wao wa nyumbani, Chamazi jijini Dar es Salaam wakati wa mechi yao ya mwisho dhidi ya JKT Ruvu.
Aidha Mwalim amezipongeza timu zote 14 zilizoshiriki ligi hiyo kwa kujituma na kutoa changamoto katika kila mechi jambo lililofanya bingwa kutopatikana kwa urahisi na mapema.

Taswira katika msiba wa Gurumo