STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, July 31, 2011

Uongozi wakana kumpa Nyagawa umeneja Simba



UONGOZI wa klabu ya soka ya Simba umekanusha taarifa kwamba umempa cheo cha umeneja kiungo wake iliyomtema kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania, Nico Nyagawa.
Nyagawa, aliyekuwa nahodha wa klabu hiyo ametemwa kwenye usajili wa kikosi kipya kitakachoitumikia timu hiyo msimu ujao, huku kukiwepo na taarifa kwamba kiungo huyo amekula shavu la kuteuliwa kuwa meneja wa timu hiyo.
Klabu ya Simba kupitria Afisa Habari wake, Ezekiel Kamwaga, alikanusha madai hayo ya kumpa Nyagawa umeneja, akisema cheo hicho bado kipo kwa King Abdallah Kibadeni, licha ya kukiri ni kweli wamemuacha mchezaji huyo kwa msimu ujao.
"Nyagawa hajapewa umeneja, ingawa ni kweli ametemwa kwenye orodha mpya ya kikosi cha Simba kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara," alisema Kamwaga.
Alisema kwa sasa uongozi wao unaangalia namna ya kumpa kazi nahodha wao huyo, kwa vile bado anaye mkataba na klabu hiyo hadi mwakani.
Alipoulizwa madai kwamba mchezaji huyo amekuwa akitaka kulipwa haki zake ili atimke zake kimoja Msimbazi, Kamwaga alisema hizo ni taarifa za uzushi kwa vile Nyagawa mwenyewe hajawahi kuueleza chochote uongozi juu ya jambo hilo hadi alipoongea na Sema Usikike.
"Hizo ni taarifa za uzushi tu, tulishazungumza na Nyagawa na ndio maana tunasema tupo katika mipango ya kumpa majukumu ndani ya Simba, " alisema.
Nyagawa aliyesajiliwa na Simba msimu wa 2005-2006 akitokea Mtibwa Sugar anatajwa kama mmoja wa wachezaji wenye nidhamu ya hali ya juu wa soka nchini, ingawa amekuwa na bahati mbaya ya kutoitwa mara kwa mara katika kikosi cha timu ya taifa, Taifa Stars.


Mwisho

Yanga yawatoa hofu mashabiki *Ni juu ya kutoweka kwa 'Diego'




UONGOZI wa klabu ya soka ya Yanga umewatoa hofu wanachama na mashabiki wake juu ya taarifa kwamba mshambuliaji wao nyota kutoka Uganda, Hamis Kizza 'Diego' ametoweka.
Kiza aliyeng'ara kwenye michuano ya Kombe la Kagame na kuibebesha taji mabingwa hao wa Tanzania Bara, ndiye aliyekuwa hajaripoti katika kambi ya timu hiyo inayojiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara pamoja na mechi ya Ngao ya Hisani dhidi ya Simba.
Afisa Habari wa Yanga, Louis Sendeu, alisema hakuna ukweli kuwa Kizza 'amepeperuka' Jangwani kama inavyovumishwa, ila nyota huyo alikuwa na matatizo ya kifamilia na kwamba angewasili mwishoni mwa wiki.
Sendeu, alisema kama mshambuliaji huyo asingekuwa mali yao jina lake lisingekuwa kwenyue orodha ya wachezaji wapya wa kikosi chao, pamoja na kuitumikia Yanga kwenye michuano ya Kombe la Kagame ambapo walifanikiwa kutwaa taji ikiwa ni mara yao ya nne tangu 1974.
"Ni kweli Kizza amechelewa kuja, lakini haina maana ndio kaingia mitini kama baadhi ya vyombo vya habari vinavyotaka kupotosha, tunadhani atawasili kabla ya Jumapili," alisema.
Aidha, Sendeu, alisema wameamua kukacha kucheza mechi mbili za kirafiki dhidi ya timu za Coastal Union na Azam kutokana na walioziratibu kushindwa kufanya mawasiliano na uongozi wao kulingana na programu za benchi lao la ufundi.
"Hizo mechi tulikuwa tukizisikia tu redio na kwenye vyombo vingine vya habari, lakini uongozi haukuwa na taarifa nazo na ndio maana tumeamua kuachana nazo, kwani tunahisi kuna ujanja ujanja uliokuwa ukifanyika hasa mechi ya Coastal," alisema Sendeu.
Yanga wanaoendelea kujinoa jijini Dar chini ya makocha wake, Sam Timbe na Fred Felix 'Minziro' walitangaza kufuta mechi hizo zilizokuwa zichezwe mwishoni mwa wiki katika miji ya Tanga na Dar es Salaam.

Tamasha la Simba Day usipime!




BURUDANI mbalimbali za muziki na pambano la kirafiki la kimataifa litakaloihusisha wawakilishi wa Uganda kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika zinatarajiwa kupamba tamasha la soka la klabu ya Simba, 'Simba Day' litakalofanyika Agosti 8 jijini Dar es Salaam.
Wawakilishi hao wa Uganda, Simba Fc inayomilikiwa na Jeshi la nchi hiyo ndiyo watakaokuja kupamba tamasha hilo, ambalo pia litashuhudia timu ya Simba U23, ikikwaruzana na Azam katika kunogesha shamrashamra hizo.
Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, aliiambia MICHARAZO kuwa, tamasha lao litapambwa na burudani za muziki toka kwa bendi mbalimbali za muziki wa dansi na wasanii wa muziki wa kizazi kipya ambao hata hivyo hakuwataja.
Kamwaga alisema shamrashamra hizo za burudani ya muziki zitafuatiwa siku hiyo na utoaji wa tuzo za heshima kwa wadau wa Simba wakiwemo wachezaji, makocha na viongozi wa zamani walioisaidia klabu yao tangu ilipoanzishwa pamoja na wale wanaoisaidia sasa klabu hiyo.
"Karibu kila kitu kimekaa vema kwa sasa ikiwemo kuthibitishwa kwa Simba ya Uganda kuja nchini kucheza nasi katika tamasha hilo, ambalo kabla ya pambano hilo kutakuwa na burudani za muziki na pambano la timu za vijana za Simba na Azam," alisema Kamwaga.
"Mbali na burudani hizo pia tutatoa tuzo za heshima kwa wadau wetu katika namna ya kukumbuka na kushukuru mchango wao," alisema Kamwaga.
Kuhusu maandalizi yao ya mechi yao ya Ngao ya Hisani iliyoapngwa kucheza Agosti 17, Kamwaga alisema yanaendelea vema ikiwemo kikosi chao kuendelea kujifua kwa mazoezi pamoja na kucheza kadhaa za kirafiki visiwani Zanzibar.
Alisema wana imani kubwa ya kufanya vema kwenye pambano hilo dhidi ya Yanga pamoja na kwenye msimu mpya wa ligi kuu utakaoanza wiki moja baada ya pambano hilo la Ngao ya Hisani.
Simba ina deni la kulipa kisasi kwa Yanga iliyowafunga kwenye mechi kama hiyo msimu uliopita kwa mikwaju ya penati na kipigo ilichopata kwenye fainali za Kombe la Kagame lililochezwa hivi karibuni jijini Dar es Salaam ambapo Mghana Kenneth Asamoah waliwaliza.
"Hatuna shaka na mechi zetu zijazo kutokana na maandalizi tuliyofanya huko Zanzibar," alisema Kamwaga aliyechukua nafasi hiyo hivi karibuni akimrithi, Clifford Ndimbo.

Mwisho

Kalapina ahubiri Uzalendo nchini

MSANII nyota wa muziki wa hip hop nchini, Karama Masoud 'Kalapina' ametaka somo la uzalendo lifunzwe rasmi shuleni kwa nia ya kuwapika viongozi na wananchi watakaokuwa na uchungu wa kweli dhidi ya nchi yao kitu kinachoweza kupunguza ufisadi.
Kalapina, alisema somo hilo la uzalendo mbali na kusaidia kuondoa ufisadi, pia itawafanya hata wasanii kujipenda na kujithamini kwa kutanguliza utanzania kwanza tofauti na sasa kukosa kujiamini na kuendelea kuwatukuza wasanii wa kigeni na kushindwa kuwika kimataifa.
Akizungumza na blog hii mwishoni mwa wiki, Kalapina alisema mambo yanayoendelea nchini kuanzia kwa wananchi wa kawaida hadi viongozi na wanasiasa kuwa wabinafsi, wenye uchu na kutokuwa na uchungu wa nchi yao imetokana na kukosekana kwa somo la uzalendo.
"Nadhani watanzania tangu utotoni wakianza kufunzwa uzalendo na kujithamini wenyewe, vitendo vya ufisadi, uharamia na wasanii kupenda kuwaiga wasanii wa kimataifa badala ya kubuni kazi zao litaondoka na nchi itaenda vema," alisema.
Kalapina, alisema hata vitendo vya wanajamii kuwaibia kazi wasanii unatokana na ukosefu wa uzalendo na kuzidi kuwafanya wasanii kuendelea kuishi maisha ya dhiki kinyume na wenzao wa kimataifa wanaoongoza kwa utajiri kuliko hata viongozi wao wa serikali.
Kiongozi huyo wa kundi la muziki wa hip hop la Kikosi cha Mizinga, alisema hapendi hali ya mambo inayoendelea nchini kwa watanzania kuwa maskini wakati inafahamika nchi ina rasilimali zinazoweza kuwafanya waishi maisha ya kitajiri kuliko taifa lolote barani Afrika

Coastal 'yamrudisha' Mwalala kwao

MSHAMBULIAJI mpya wa timu ya Coastal Union ya Tanga, Ben Mwalala 'amerejeshwa' kwa nchini Kenya, baada ya timu yake iliyorejea Ligi Kuu Tanzania Bara, kuamua kupiga kambi ya kudumu nchini humo.
Coastal iliyowahi kuwa mabingwa wa soka nchini mwaka 1988, imeamua kuweka kambi ya kudumu mjini Mombasa, kujiandaa na msimu mpya wa ligi utakaoanza mwezi ujao hali inayowafanya nyota wao wapya Mwalala na mkenya mwenzie Abubakar Husseni kurejea kwao.
Afisa Habari wa timu hiyo, Eddo Kumwembe, alisema uongozi wao umeamua kuweka kambi ya kudumu Kenya, ikicheza mechi kadhaa za kirafiki za kujipima nguvu kujiweka fiti kabla ya kuanza kwa mikikimikiki ya ligi iliyokuwa ianze rasmi Agosti 20.
Kumwembe, alisema awali walikuwa wamepanga kurejea kwa muda Tanzania kwa ajili ya kuja kucheza pambano la kirafiki na Yanga lililokuwa lichezwe jana, lakini kutokana na uongozi wa Jangwani 'kuchomoa' kucheza nao wameamua kusalia Kenya hadi msimu utakapoanza.
"Kutokana na Yanga kuchomoa kucheza na sisi, tumeamua kubaki Kenya kujiandaa na msimu mpya wa ligi kwa kujipima nguvu na timu za huko," alisema.
Coastal inayonolewa na kocha Hafidh Badru, imefanya usajili unaoonekena wa kutisha kwa kuwajaza nyota wa kigeni kama Mwalala, Husseni na wanigeria wawili, Felix Amechi na Samuel Temi huku ikiwa na nyota wengine wa Tanzania akiwemo Aziz Salum Gilla aliyetoka Simba.

Mwisho

Super D aachia DVD nyingine za kufunzia ngumi




KOCHA maarufu wa mchezo wa ngumi nchini, Rajab Mhamila 'Super D' aliyeamua kutumia njia ya DVD kuwafunza watu ngumi, ameachia kazi nyingne tatu mpya.
Kazi hizo tatu zinahusisha mapambano kadhaa ya nyota na mabingwa wa ngumi za kulipwa duniani, ziachiwa sokoni zaidi ya wiki moja sasa.
Akizungumza na MICHARAZO, Super D, alisema tofauti na kanda yake ya awali, DVD za sasa zimeandaliwa kisasa na zikiwa na mchanganyiko wa 'clips' za michezo ya nyota wa dunia katika kuwafunza watu namna ya kupigana ngumi.
Super D, alisema mbali na michezo ya nyota hao wa dunia akiwemo Manny Pacquiao, Floyd Maywather, Roy Jones na wakali wengine DVD hizo pia zina michezo ya tamasha lao la ngumi wanaloendesha kwa kushirikiana na kocha Habib Kinyogoli.
"Katika muendelezo wa kuwafunza watu ngumi kwa njia rahisi, nimetoa dvd pamoja na cd nyingine tatu tofauti zilizokusanya michezo ya mabingwa wa dunia na mafunzo ya ngumi tunayoendesha kupitia tamasha letu na Kinyogoli Foundation," alisema.
Super D, ambaye ni kocha wa klabu ya ngumi ya Ashanti, alisema anaamini kupitia njia hiyo watu wengi wenye kupenda kujifunza mchezo wa ngumi kwa kuangalia mbinu na ufundi katika mchezo huo kupitia michezo ya mabondia waliopo kwenye dvd hizo.
Aliongeza kuwa, mbali na dvd hizo bado vijana wenye vipaji vya ngumi wanaweza kujiunga na klabu zao za Ashanti na Amana kujifunza 'live' chini ya makocha Habib Kinyogoli, Kondo Nassor, yeye Super D na wengine wanaowanoa vijana mbalimbali.

Mwisho

Siujasaini kokote-Nsa Job





MSHAMBULIAJI nyota wa zamani wa Yanga, Nsa Job, amedai hajasaini kokote hadi sasa licha ya jina lake kuwepo kwenye orodha ya wachezaji wa klabu ya Villa Squad.
Hata hivyo mchezaji huyo, alisema kama uongozi wa Villa utakaa nae mezani na kukubaliana juu ya masilahi atakubali kuichezea kwa vile imeonyesha nia ya kumhitaji.
Akizungumza na MICHARAZO, Job, aliyeachwa na Yanga msimu huu baada ya kuitumikia msimu uliopita akitokea Azam, alisema hakuna mazungumzo yoyote aliyofanya na Villa waka kusaini kuichezea klabu hiyo.
Alisema, mara alipoachwa na Yanga alikuwa kwenye mipango ya kwenda Sweden kucheza soka la kulipwa, hivyo hakuwahi kufanya mazungumzo na klabu yoyote, ila kama ni kweli Villa inamhitaji ataweza kuwasaidia wakielewana juu ya suala la masilahi.
"Sijasaini kokote ndugu yangu, sio Villa wala klabu nyingine niliyofanya nao mazungumzo, ila kama klabu hiyo inanitaka sioni tatizo kuichezea kama tutaelewana juu ya masilahi, si unajua soka ni ajira bwana," alisema Job.
Mshambuliaji huyo aliyewahi kuzichezea Moro United na Simba, alisema hata kama atakubaliana na Villa kuichezea, bado mipango yake ya kwenda kucheza soka la kulipwa ipo pale pale kwani anaendelea kuwasiliana na wakala wake Nyupi Mwakitosa.
Job, alisema wakala huyo ambaye ni mchezaji wa zamani wa soka Tanzania mwenye uraia wa Sweden kwa sasa, amemhakikishia kumhangaikia kupata timu ya kwenda kufanya nanyo majaribio baada ya ile ya awali kushindwa kukubaliana nao baadhi ya mambo.

Mwisho

Pondamali awachanganya Villa Squad

UONGOZI wa klabu ya soka ya Villa Squad, umedai kuchanganywa na kitendo cha aliyekuwa kocha wao, Juma Pondamali kujiondoa kikosi, huku wakikanusha kumteua Rachel Mwiligwa kuwa msemaji mpya wa klabu yao.
Makamu Mwenyekiti wa Villa, Ramadhani Uledi, aliambia MICHARAZO juzi kuwa, kujiondoa kwa Pondamali kumewapa wakati mgumu kutokana na ukweli alikuwa sehemu ya mipango yao ya kuisaidia timu hiyo kwenye msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Uledi alisema kinachowachanganya zaidi ni hatua ya kocha huyo aliyekuwa pia Mkurugenzi wa Ufundi, kuondoka kimyakimya bila kuwaambia zaidi ya kusoma taarifa zake kwenye vyombo vya habari.
"Tumeshtushwa na kuchanganywa na Pondamali kujiondoa tukielekea kwenye mikikimikiki ya Ligi Kuu Tanzania Bara tuliyoirejea msimu huu, hatujui kitu gani kilichomkimbiza, ila kutakutana kujadili tuone tunafanyaje," alisema.
Uledi anayekaimu pia nafasi ya Mwenyekiti, ambayo ipo wazi baada ya TFF kusitisha kuwaniwa kwenye uchaguzi mkuu wa klabu hiyo uliofanyika Juni, mwaka huu, alisema pia sio kweli kama klabu yao imemteua Mwandishi Rachel Mwiligwa kuwa Msemaji wao, akisisitiza nafasi hiyo bado inashikiliwa na Idd Godigodi aliyetangaza kujiuzulu.
"Hatutateua msemaji mpya kwa kuwa nafasi hiyo na zile zinazotakiwa zitolewe kwa ajira rasmi, zitatangazwa baada ya kikao chetu, kwa maana hiyo Godigodi aliyetangaza kujiondoa baada ya kusoma taarifa za uteuzi wa Mwiligwa ataendelea na nafasi yake," alisema Uledi.
Mwenyekiti huyo aliongeza katika kikao chao watajadili suala la ushiriki wa timu yao katika msimu mpya wa ligi waliorejea baada ya kushuka msimu wa 2008-2009.
Villa Squad ni miongoni mwa timu nne 'mpya' zitakazocheza ligi ya msimu ujao iliyopangwa kuanza Agosti 20, zingine zikiwa ni JKT Oljoro, Coastal Union na Moro United.

Mwisho

Waumini Answar Sunna wacharuka, watulizwa na RITA

WAUMINI wa Jumuiya ya Answar Sunna Tanzania wanaoshinikiza uongozi wa juu ya jumuiya hiyo hung'oke madarakani kwa kukiuka katiba, wametulizwa wakitakiwa kuwa na subira wakati ofisi wa Wakala wa Usajili, Ufilisi na Udhamini, RITA ukisubiri kutoa maamuzi juu ya mgogoro huo.
Wito huo umetolewa jana kwenye maazimio ya mkutano wa pamoja kati ya waumini hao na kamati yao maalum inayofuatilia mgogoro huo, uliofanyika kwenye msikiti uliopo makao makuu ya Answar Sunna, Kinondoni jijini Dar es Salaam.
Kadhalika wito kama huo umetolewa na Meneja wa Ufilisi na Udhamini wa Rita, Linna Msanga Katema, alipozungumza na MICHARAZO akithibitisha ofisi yao imeomba ipewe muda wa mwezi mmoja kutoa majibu juu ya sakata linaloendelea kwenye jumuiya hiyo.
Meneja huyo alikiri kuwepo kwa mgogoro huo na kueleza tofauti na awali walipokuwa wakikosa ushirikiano toka kwa viongozi wanaolalamikiwa wakiwemo Baraza la Wadhamini na Amiri wa Jumuiya hiyo, Sheikh Juma Poli, sasa mambo ni shwari.
"Tumeshawaandikia barua kuomba watupe muda wa mwezi mmoja toka Julai 26 tuliowaandikia barua ili RITA tutoe maamuzi juu ya kinachoendelea baina ya pande hizo mbili, hivyo tunaomba waumini watulie haki itatendeka," alisema Katema.
Katika mkutano wao wa jana, waumini hao walionyesha kuwa na hasira ya kutaka viongozi wang'oke kwa kukiuka katika na kushindwa kuipeleka mbele jumuiya yao, kabla ya Mwenyekiti wa Kamati yao, Hamis Buguza kuwasihi wavute subira.
"Vuteni subira tusubiri maamuzi ya RITA ili kuona nini kitaamuliwa, ila lolote litakalotolewa tunawaahidi kuyaleta kwenu mjue kitu cha kufanya, ila kwa sasa ni mapema mno na Uislam unatufundisha kuwa na subira," alisema mwenyekiti huyo.
Kutokana na kauli ya Mwenyekiti pamoja na Katibu wao, Abdulhafidh Nahoda, waumini hao katika kutoa maazimio waliafiki kuvuta subira hadi maamuzi ya RITA yanayotarajiwa kutolewa Agosti 26, ili wajue la kufanya.
Hata hivyo walitoa angalizo kwa kudai kama kutakuwa na aina fulani ya upendeleo basi, watakachoamua wasije wakaamuliwa kwa madai wamechoka kuvumilia.
Mzozo wa waumini wa jumuiya hiyo na uongozi wao umeanza tangu mwaka juzi kutokana na madai viongozi wamekiuka katiba kwa kutoitisha mikutano kwa muda wa miaka 10, huku wakifanya maamuzi bila kuwashirikisha kama wanavyoelekezwa kwenye katika mama ya mwaka 1992.

Mwisho

Wednesday, July 27, 2011

Banka aishtaki Simba kwa TFF




KIUNGO Mohammed Banka ameishtaki klabu yake ya Simba kwa Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, juu ya sakata lake la kutaka kupelekwa kucheza kwa mkopo katika timu ya Villa Squad bila ridhaa yake.
Banka, aliyeichezea Simba kwa mafanikio tangu ilipomsajili baada ya kutemwa na Yanga, msimu wa 2008-2009, alisema ameamua kuchukua maamuzi huo kutokana na kuona viongozi wa Simba wanamzungusha kuhusu suala la uhamisho wake.
Mwanasheria aliyepewa kazi ya kumpigania Banka, John Mallya, aliiambia MICHARAZO jana kuwa, wameandika barua Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, ili kuingilia kazi suala la mteja wao kabla ya hatua zingine za kisheria kufuata.
Mallya, alisema wameamua kuandika barua hiyo, TFF kutokana na kuona viongozi wa Simba wanakwepa kukutana kulimaliza suala la Banka, kutokana na wenyewe kukiuka mkabata baina yao na mchezaji huyo kama sheria zinavyoelekeza.
Alisema walikuwa katika mazungumzo mazuri na viongozi wa klabu hiyo, lakini juzi walipopanga kukutana ili kulimaliza suala hilo, wenzao walishindwa kutokea na kuona ni vema waombe msaada TFF, kabla ya kuangalia cha kufanya kumsaidia mteja wao.
Afisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alikiri kupokewa kwa barua hiyo ya ombi la Banka kutaka shirikisho lao kuingilia kati na kudai itapelekwa kunakohusika kufanyiwa kazi.
"Ni kweli barua hiyo imefika kwetu, Banka akiomba TFF iingilie kati sakata lake la Simba," alisema Wambura.
Naye Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, alikiri kuwepo kwa mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea baina ya pande hizo mbili, ingawa alisema alikuwa hajaipata nakala ya barua hiyo ya malalamiko ya Banka iliyopelekwa TFF.
"Hilo la kushtakiwa TFF, silijui kwani sijapata barua, pia siwezi kuliongelea kwa undani kwa vile lilikuwa linashughulikiwa na viongozi wa juu, ambao kwa bahati karibu wote wameenda Uturuki kushughulikia suala la ujenzi wa uwanja," alisema.
Banka, amekuwa akisisitiza kuwa kama Simba haimhitaji ni bora mlipe chake aangalie ustaarabu wake kuliko kumlazimisha kwenda Villa Sqaud iliyorejea ligi kuu msimu huu.

Mwisho

Bingwa wa Kick Boxing Kenya atua Bongo kuzipiga




BINGWA wa Kick Boxing kutoka Kenya, Rukia Kaselete ametua nchini tayari kwa ajili ya pambano lake dhidi ya Mtanzania Jamhuri Said, watakaosindikiza pambano la nani mkali kati ya Amour Zungu wa Zanzibar na Mchumia Tumbo wa Tanzania Bara.
Michezo hiyo iliyoandaliwa na Bingwa wa Dunia wa Kick Boxing anayeshikilia mikanda ya WKL na WKC, Japhet Kaseba inatarajiwa kucheza siku ya Jumamosi kwenye ukumbi wa DDC Keko, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na MICHARAZO jana, Kaseba, alisema maandalizi ya michezo hiyo kwa wastani inaendelea vema ikiwemo mabondia wote kuwasili jijini akiwemo mkenya huyo atakayepigana na Jamhuri kusindikiza pambano la Zungu na mwenzake.
Kaseba alisema mabondia wote watakaoshiriki michezo hiyo ya Kick Boxing na Ngumi za Kulipwa wanatarajiwa kupimwa afya zao siku ya Ijumaa kwenye gym yake, iliyopo eneo la Mwananyamala jijini Dar es Salaam.
"Kwa kweli kila kitu kinaenda vema ikiwemo mabondia wote kuwasili Dar tayari kwa ajili ya michezo hiyo ya Jumamosi, ambapo Amour Zungu atazipiga na Mchumia Tumbo katika pambano la kusaka mkali kati yao," alisema Kaseba.
Kaseba alisema mbali na pamoja ya pambano la Kaseleta na Jamhuri, siku hiyo pia kutakuwa na michezo mingine ya utangulizi ambapo wanadada Asha Abubakar wa Kisarawe na Fadhila Adam wa Dar wataonyeshana kazi kwenye kick boxing.
"Wengine watakaopigana siku hiyo ni kati ya Dragon Kaizum dhisi ya Faza Boy, Idd na Dragon Boy na Lion Heart ataonyeshana kazi na Begeje," alisema.
Aliongeza pambano la ngumi za kulipwa zitawakutanisha wakongwe wa mchezo huo, Ernest Bujiku dhidi ya Maneno Osward 'Mtambo wa Gongo'.

Mwisho

Viongozi Simba waenda kumalizana na Waturuki



VIONGOZI wa klabu ya soka ya Simba wameondoka nchini juzi kuelekea Uturuki kwa ajili ya kwenda kumalizia taratibu za ujenzi wa uwanja wao mpya wa kisasa utakaojengwa eneo la Bunju, nje kidogo ya jijini la Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Afisa Habari wa klabu hiyo, Ezekiel Kamwaga, viongozi walioondoka ni Mwenyekiti Ismail Aden Rage na Katibu wake, Evodius Mtawala.
Kamwaga alisema Rage na Mtawala waliondoka juzi kuelekea nchini humo kufanya mazungumzo ya mwisho na uongozi wa kampuni ya Petroland, ambayo ndiyo itakayoujenga uwanja huo utakaoingiza watazamaji wasiopungua 60,000.
"Viongozi wetu wawili wa juu wameondoka nchini jana, kwenda Uturuki kwa ajili ya kumalizana na watakaotujengea uwanja wetu wa kisasa utakaokuwa eneo la Bunju," alisema Kamwaga.
Afisa Habari huyo, alisema viongozi wao wameenda kuweka mambo sawa kabla ya wakandarasi hao kuja kuanza kazi yao na kuifanya Simba kufuata nyayo za klabu kubwa barani Afrika kama ASEC Memosa au Kaizer Chief zenye viwanja vikubwa vya kisasa.
Uwanja huo utakaokuwa wa kisasa na mkubwa kama ule wa Taifa, utaigharimu Simba kiasi cha Shilingi Bilioni 75 hadi utakapomalizika ukihusisha uwanja wa kuchezea, maduka, kumbi za mikutano na burudani, mbali na hoteli na kituo cha michezo.
Kwa hapa nchini ukiondoa Yanga yenye kuumiliki uwanja wa Kaunda, klabu nyingine yenye uwanja wake mwenyewe ni Azam iliyoujenga eneo la Chamanzi, Mbande nje kidogo ya jijini la Dar es Salaam ambao utaanza kutumika msimu mpya wa Ligi Kuu.

Mwisho

Simba yawaita DCMP Da kumjadili Mgosi




UONGOZI wa klabu ya soka ya Simba, umeutaka uongozi wa timu ya DC Motema Pembe ya DR Congo, kuja jijini Dar es Salaam kuzungumza nao ili waachiwe kiungo mshambuliaji, Mussa Hassani Mgosi vinginevyo imsahau kumpata.
Motema Pembe imeonyesha nia ya kumsajili Mgosi, isipokuwa inamtaka kama mchezaji huru, kitu kinachopingwa na uongozi wa Simba wenye mkataba bao ikidai kama ina ya dhati ya kumnasa mchezaji huyo wake wazungumze mezani waafikiane.
Akizungumza na MICHARAZO jana, Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, alisema klabu yao ipo tayari kumuacha Mgosi aende DCMP, ila kama uongozi wa klabu hiyo utakuja kuzungumza nao ili kumhamisha kwani ni mchezaji wao halali.
Kamwaga alisema Simba haina nia ya kumbania Mgosi, ila kwa hali ilivyo ni vigumu kwao kumtoa winga huyo bure wakati wana mkataba naye.
Kamwaga, alisema Simba itaona raha iwapo mchezaji huyo atajiunga na DCMP kama ilivyokuwa kwa akina Mbwana Samatta na Patrick Ochan walisajiliwa TP Mazembe, ila wenzake wanamtaka bure kitu kinachowafanya wamzuie hadi kieleweke.
"Kama kweli wana nia na Mgosi waje wazungumze nasi, Mgosi ana mkataba Simba na hivyo hatuwezi kumuachia bure," alisema.
Kamwaga, alisema tayari wameshaifahamisha TFF juu ya msimamo wao na wanasubiri kuona uongozi wa DCMP utafanya nini kuamua hatma ya Mgosi, ambaye jina lake lipo kwenye orodha ya usajili wa klabu ya Simba kwa msimu ujao wa ligi kuu Tanzania Bara.
Alisema kama mipango yake ya kwenda Congo itakwama, Mgosi ataendelea kuichezea timu yao kwa msimu ujao hadi atakapomaliza mkataba utakaoisha mwakani.
Katika hatua nyingine, Kamwaga alisema klabu yao inatarajiwa kuianika timu watakaocheza nao kwenye Tamasha la Siku ya Simba 'Simba Day' litakalofanyika Agosti 8 mwaka huu.
Kamwaga alisema klabu yao ilipeleka maombi kwa klabu tatu za nje ya nchi na leo wanatarajia kutangaza timu watakayocheza nao katika tamasha hilo
"Timu itakayotusindikiza kwenye Simba Day tutaitangaza kesho (leo) pia tutaanika kila kitu juu ya maandalizi ya tamasha hilo," alisema Kamwaga.

Mwisho

Talent Band kutambulisha mpya Sinza

BENDI ya muziki wa dansi ya Talent 'Wazee wa Kuchechemea' inatarajiwa kuvamia kitongoji cha Sinza ili kuitambulisha albamu yao mpya ya 'Shoka la Bucha'.
Mkurugenzi wa bendi hiyo, Husseni Jumbe, aliambia MICHARAZO jana kuwa, onyesho hilo litafanyika kesho kwenye ukumbi wa Nouvel Social Centre (zamani Rufita) ambapo watatambulisha nyimbo zote zilizopo kwenye albamu hiyo mpya.
Jumbe, alisema onyesho hilo limeratibiwa na Mkurugenzi wa ukumbi huyo aliyemtaja kwa jina la Mamaa Joyce.
"Baada ya kuikamilisha albamu yetu mpya ya Shoka la Bucha, Talent Band, inatarajiwa kuitambulisha albamu hiyo katika onyesho maalum litakaloofanyika siku ya Alhamis kwenye ukumbi wa Nouvel Social Centre," alisema Jumbe.
Jumbe alizitaja nyimbo zitakazotambulishwa kwenye onyesho hilo kuwa ni Shoka la Bucha, Kiapo Mara Tatu, Kilio cha Swahiba na zile za albamu yao ya kwanza ya Subiri Kidogo.
Naye mratibu wa onyesho hilo, Joyce alisema kila kitu kipo sawa na wanachosubiri ni kupata burudani toka kwa Talent.

Mwisho

Tamasha kubwa la sanaa kufanyika Moro

WASANII zaidi ya 100 wa mkoani Morogoro wanatarajia kufanya tamasha kubwa litakaloshirikisha sanaa za aina mbalimbali.
Mratibu wa tamasha hilo lililopewa jina la 'Wakali Concert', Athuman Mswagala 'Mahita' aliiambia Micharazokwa njia ya simu kutoka Morogoro kuwa tamasha hilo litafanyika Julai 30 katika ukumbi wa Vijana Social ulioko mjini hapa.
Mswagala, alisema lengo la tamasha hilo litakalowahusisha wasanii wa mkoa huo wa fani mbalimbali ni kufahamiana na kuibua vipaji vipya.
Alisema maandalizi kwa ajili ya tamasha hilo yanakwenda vizuri na kwamba kinachosubiriwa ni kufanyika kwa tamasha hilo.
Alisema katika tamasha hilo litakalokuwa likifanyika kila mwaka, wasanii watakaofanya vizuri watazawadiwa zawadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na fedha taslimu.
"Kimsingi, maandaalizi yanakwenda vizuri na wasanii wengi wamethibitisha kushiriki hali ambayo naamini itakuwa burudani tosha kwa wakazi wa Morogoro" alisema.
Naye, mkurugenzi wa kampuni ya Katundu, wanaodhamini tamasha hilo, Mohamed Katundu, alisema kampuni yake imeamua kudhamini tamasha hilo kwa lengo la kusapoti wasanii wa Morogoro.
Katundu alisema hiyo ni moja ya mipango ya kampuni yake kuhakikisha wasanii mkoani hapa wanapata mafanikio makubwa kupitia sanaa mbalimbali.

Saturday, July 16, 2011

Sunzu asaini mkataba wa miaka miwili



MSHAMBULIAJI wa Kimataifa kutoka Zambia, Felix Mumba Sunzu amesaini mkataba wa miaka miwili ya kuichezea klabu ya soka ya Simba kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya kimataifa.
Makamu Mwenyekiti wa Simba, Godfrey Nyange Kaburu, aliuambia mtandao wa MICHARAZO jana usiku kwamba wameshamalizana na Sunzu na kwamba mchezaji huyo atarejea kwao wakati wakifanya taratibu za uhamisho wake wa kimataifa toka Al Hilal.
"Kila kitu kipo ok, baada ya mkutano mrefu baina yenu amekubali kusaini mkataba wa miaka miwili kuwepo Simba," alisema Kaburu.
Kaburu hakupenda kueleza kwa undani mambo mengine waliyokubaliana na mchezaji huyo.
Kadhalika, Kaburu alikanusha taarifa kwamba wamemnyakua mshambuliaji wa Yanga, Jerry Tegete akidai wanaheshimu mkataba uliopo baina ya Yanga na mchezaji huyo.
"Hizo ni taarifa za mtaani, ila si kweli, mtu ambaye tumemalizana nae ni Sunzu, huyo Tegete wala hatuna mpango nae," alisema.
Pia alisema sio kweli kama beki wao king'ang'anizi, Kelvin Yondan, amewakacha na kwenda Yanga kwa maelezo bado wana mkataba naye, pia kisheria Yanga wanapaswa waonane nao kama ni kweli walimtaka mchezaji huyo.
"taratibu zipo wazi, pia Yondan ana mkataba wa kuichezea Simba sasa ataendaje Yanga, hizi ni nyepesi nyepesi tu ila mchezaji huyo bado yupo Simba, alisema Kaburu.
Katiak hatua nyingine ni kwamba wachezaji wawili, Mohammed Banka na Athuman Idd 'Chuji' huenda wakaichezea Villa Squad kwa mkopo baada ya kuridhiana na Simba juu ya wachezaji hao wanaomudu nafasi ya kiungo.
Viongozi wa Villa waliuambia mtandao huu walikuwa wakimalizana na Simba, lakini hawakuweka kila kitu bayana wakidai watazungumza leo.

Friday, July 15, 2011

Twiga Stars kuanza na Ghana All African Games

SHIRIKISHO la Soka Afrika, CAF, imetangaza ratiba ya michuano ya soka kwa timu za wanawake zinazoshiriki michuano ya Afrika (All African Games) ambapo timu ya taifa ya Tanzania, Twiga Stars itaanza kibarua chake kwa kuumana na Ghana.
Michuano hiyo ya Afrika inatarajiwa kuanza kufanyika Septemba 3-18 kwenye mji wa Maputo, Msuimbiji, ambapo kwa mujibu wa ratiba hiyo ya CAF ni kwamba Twiga iliyopo kundi B itafungua dimba kwa kuumana na Ghana siku ya Septemba 5.
Timu zingine zilizopo katika kundi hilo ni Afrika Kusini na mabingwa wapya wa Kombe la COSAFA, Zimbabwe.
Ratiba hiyo ya CAF inaonyesha kuwa Twiga itashuka dimbani tena Septemba 8 kucheza na Afrika Kusini kabla ya kumaliza mechi zake, Septemba 11 kwa kucheza na Zimbabwe.
Twiga imejikuta kundi moja na timu hizo mbili ambazo ziliichachafya katika michuano ya Kombe la COSAFA, ambapo Afrika Kusini waliokuwa nao kundi moja waliwalaza bao 1-0 kabla ya Zimbabwe kuifunga kwenye mechi ya nusu fainali kwa mikwaju ya penati 4-2.
Timu zingine zitakazoshiriki michuano hiyo na zilizopangwa kundi A ni wenyeji Msumbiji, Cameroon, Algeria na Guinea, ambapo washindi wawili wa kwanza wa kila kundi ndizo zitakazosonga mbele kwa hatua ya nusu fainali.
Nigeria ndiyo waliokuwa mabingwa wa mwaka 2007, lakini hawakufanikiwa kufuzu
kwa michuano hiyo mwaka huu ambayo hufanyika kila baada ya miaka minne.
Wakati huo huo mikoa mitatu ya Dodoma, Mwanza na Ruvuma imeteuliwa kuwa vituo vya kuendeshea semina na mitihani ya utimamu wa mwili (physical fitness test) kwa waamuzi wa daraja la pili na tatu inayotarajiwa kufanyika mapema mwezi ujao.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, kupitia Afisa Habari wake, Boniface Wambura, ni kwamba semina na mitihani hiyo itafanyika kwa muda wa siku tatu kuanzia Agosti 2-5 katika vituo hivyo.
Taarifa hiyo inasema washiriki wa semina na mitihani hiyo watajitegemea kila kitu kuanzia gharama za usafiri, chakula na malazi, huku vyama vya soka vya mikoa ya Tanzania Bara vikihimizwa kuwakumbusha washiriki kuhudhuria semina na mafunzo hayo kwa faida yao.
Iliongeza kuwa semina na mitihani hiyo itatumika kuwapandisha daraja washiriki hao.
Hiyo ni semina ya pili kuandaliwa na TFF ndani ya kipindi kifupi ikiwa ni maandalizi na msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara, kwani karibu wiki moja sasa ilikuwa ikiendesha semina kama hiyo inayowahusisha waamuzi wa daraja la IA na IB iliyokuwa ikifanyika katika miji ya Mwanza na Dar es Salaam.
Semina na mitihani hiyo ilianza Julai 13 na inatarajiwa kufungwa leo Julai 16.

Stars kukipiga ughaibuni na Palestina, Jordan

KATIKA kujiweka fiti kabla ya kumaliza viporo vya michezo yake miwili iliyosalia ya kuwania kufuzu Fainali za Afrika za mwaka 2012, timu ya soka ya taifa ya Tanzania, Taifa Stars inatarajiwa kwenda Mashariki na Kati kucheza mechi mbili za kirafiki za kimataifa.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, kuopitia Afisa Habari wake, Boniface Wambura inasema, Stars itaumana na timu za mataifa ya Palestina na Jordan mapema mwezi ujao.
Wambura alisema mechi ya kwanza ya timu hiyo inayoshikilia nafasi ya tatu katika kundi D lenye timu za Morocco, Afrika ya Kati na Algeria, itachezwa siku ya Agosti 10 katika mji wa Ramallah dhidi ya wenyeji wao Palestina.
Mechi ya Tanzania na Palestina itakuwa ni kama marudiano, kwani mapema mwaka huu timu hizo zilipepetana hapa nchini katika pambano jingine la kirafiki la kimataifa.
Katika mechi hiyo ilichezwa Februari 9 kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam, Stars iliitambia Palestina kwa kuilaza bao 1-0, bado lililofungwa na winga mahiri, Mrisho Ngassa ambaye kwa sasa yupo Marekani kufanya majaribio ya kucheza soka la kulipwa katika klabu ya Seattle Sounders inayoshiriki ligi ya Marekani, MLS.
Wambura aliongeza Stars itashuka tena dimbani Agosti 13 kupepetana na Jordan katika pambano litakalochezwa kwenye mji mkuu wa nchi hiyo ya Jordan, Amani.
Wambura alisema Stars itaondoka nchini Agosti 7 na kikosi cha timu hiyo kinatarajiwa kutajwa mara baada ya kocha mkuu wa timu hiyo, Jan Poulsen kurejea kutoka mapumziko nchini Denmark, mapema mwezi ujao.
Stars inahitaji ushindi katika mechi zake zilizosalia dhidi ya Algeria itakayochezwa nyumbani na ile ya mwisho dhidi ya Morocco, iwapo inataka kufuzu fainali hizo za Afrika zitakazofanyika mwakani katika nchi za Guinea ya Ikweta na Gabon.

Hatimaye Sunzu atua Bongo


MSHAMBULIAJI nyota wa kimataifa wa timu ya Al Hilal ya Sudan, Felex Sunzu ametua nchini mapema leo tayari kufanya mazungumzo na klabu ya Simba ili kuichezea tyimu hiyo kwa msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara 2011-2012.
Sunzu alitua leo asubuhi akiambatana na mkewe na hadi wakati huu alikuwa akiendelea kufanya mazungumzo na uongozi wa Simba ili kuweza kumwaga wino wa kuichezea klabu hiyo.
Makamu Mwenyekiti wa Simba, Geofrey Nyange Kaburu aliyempokea mshambuliaji huyo aliyeng'ara kwenye mihuano ya Kombe la Chalenji iliyofanyika mwishoni mwa mwaka jana akiichezea Zambia, iliyoalikwa amesema wakati wowote wataweka taarifa juu ya kumnasa rasmi mkali huyo.
Kwenye uwanja wa ndege, Sunzu ambaye alikuwa akitokea mapumzikoni nchini Nigeria, alisema amekuja nchini na kama atapata fursa ya kumalizana na Simba basi mashabiki wa timu hiyo watarajie makubwa kutoka kwake muhimu apewe ushirikiano.
Nyota huyo ambaye ameshindwa kuitumikia Al Hilal kwa kiwango stahiki kiasi cha klabu yake kutaka kumtoa kwa mkopo, alisema anazifahamu Simba na Yanga na anaimani atang'ara nchini kama ilivyo kwa mzambia mwenzake Davis Mwape aliyepo Yanga.
Simba inahaha kusaka mshambuliaji wa kuziba nafasi ya Mbwana Samatta aliyenunuliwa na TP Mazembe, ambayo Sunzu anaonekana kama 'muarubaini'wa tatizo la safu butu ya ushambuliaji ya timu hiyo iliyoshindwa kutwaa taji la Kagame kwa kulazwa na Yanga bao 1-0 katika mechi ya fainali baina yao iliyochezwa Jumapili iliyopita.

Rostam Aziz alipobwaga manyanga Igunga



UTANGULIZI

WAZEE wangu, kwanza kabisa kabla ya kueleza kile ambacho kimenisukuma kuzungumza nanyi leo, napenda kuanza kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu, mwingi wa rehema kwa kutuwezesha kufikia siku hii ambayo inatukutanisha waja wake.

Wazee wangu wa Igunga, baada ya kufanya hivyo napenda pia kutumia fursa hii kuwashukuru ninyi nyote mmoja mmoja na katika umoja wenu kwa kuitikia wito wangu, kijana wenu, niliyewaomba nije nizungumze nanyi siku hii ya leo.

Nafanya hivyo nikitambua vyema kwamba, kama si nyinyi wazee wangu na wengine wengi ambao hatuko nao hapa leo kwa sababu mbalimbali, ambao mmekuwa na imani kubwa nami nisingeweza kufikia hapa nilipofika sasa.

Wazee wangu, waasisi wa taifa letu walitufundisha kutambua na kuheshimu ukweli kwamba; ‘Uongozi ni Dhamana’ dhana ambayo kila ninapokaa na kutafakari huwa inanirejesha nyuma na kukumbuka jinsi nyinyi mlivyokaa katika umoja wenu na kuniteua mimi, miongoni mwa vijana wenu wengi, kuwa mwakilishi wa Jimbo la Igunga tangu mwaka 1994.

Katika kipindi hicho chote cha utumishi wangu, nyinyi wazee wangu mmekuwa mhimili muhimu ambao umeniwezesha kutimiza wajibu wangu kwa bidii kubwa, maarifa na nidhamu ya hali ya juu nikitambua namna ambavyo mmekuwa na imani kubwa juu yangu.

Ari na moyo wa imani, ushirikiano na mshikamano ambao wazee wangu mmekuwa nao kwangu ndiyo ambao kwa kiwango kikubwa umetuwezesha kufanya kazi kwa pamoja, tukishinda changamoto mbalimbali ambazo zimekuwa zikilikabili jimbo letu katika kipindi chote ambacho mmeendelea kuniamini kuwa mbunge wenu kwa miaka 18 sasa.

Wakati nikitambua na kuheshimu ukweli kwamba katika kipindi chote cha ubunge wangu mmekuwa na imani kubwa nami na kuniunga mkono kwa dhati, naamini kwamba kwa upande wangu pia nimejitahidi kwa kadiri nilivyoweza, kutimiza matarajio ya wananchi wa Igunga.

Miongoni mwa mafanikio makubwa tuliyoyafikia kupitia ushirikiano wetu na uongozi wa pamoja ni kwamba, mwaka 1994 Igunga ilikuwa ni wilaya ya mwisho kwa maendeleo mkoani Tabora lakini leo ndiyo ya kwanza, taa za barabarani, bima ya afya kwa kila kaya, zahanati kila kijiji na shule nyingi kuliko idadi ya kata zilizomo kwenye wilaya.

Wazee wangu, nayasema haya nikitambua kwamba, kama ilivyo katika maeneo mbalimbali hapa nchini, mafanikio makubwa tuliyoyapata katika nyanja za elimu, afya, makaazi bora na kilimo katika kipindi chote ambacho mmendelea kuniamini kuwa mbunge wenu kwa miaka 18 sasa.

Wakati nikitambua na kuheshimu ukweli kwamba katika kipindi chote cha ubunge wangu mmekuwa na imani kubwa nami na kuniunga mkono kwa dhati, naamini kwamba kwa upande wangu pia nimejitahidi kwa kadiri nilivyoweza, kutimiza matarajio ya wananchi wa Igunga.

Wazee wangu, nayasema haya nikitambua kwamba, kama ilivyo katika maeneo mbalimbali hapa nchini, mafanikio makubwa tuliyoyapata katika nyanja za elimu, afya, makaazi bora na kilimo katika kipindi hicho chote hayajaweza kumaliza changamoto zote za maendeleo ambazo zinatukabili.

Wazee wangu, ingawa nimekuwa na kawaida ya kukutana na kuzungumza nanyi mara kwa mara, mmoja mmoja na wakati mwingine katika umoja wenu, wito wangu wa leo una makusudi ambayo kwa kiwango kikubwa ni tofauti na yale ambayo tumeyazoea.

Japokuwa ujumbe ninaotaka kuzungumza nanyi wazee wangu, si mgeni sana masikioni mwenu, tofauti ya leo na mikutano yetu mingine iliyopita ni uamuzi ambao nimekusudia kuufanya na ambao nitayatangaza muda mfupi ujao.

YATOKANAYO

Wazee wangu, naamini mmekuwa mkifuatilia kwa karibu hali ya siasa nchini na hususani afya ya kisiasa na matukio mengine ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) ambacho mimi ni mwanachama wake na Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) nikiuwakilisha Mkoa wetu wa Tabora.

Naamini kwamba katika kufuatilia kwenu mtakuwa mmebaini kuwapo kwa matukio ambayo kwa namna moja au nyingine yamekuwa yakitokea huku yakiligusa jina langu na wakati fulani nafasi yangu kama kiongozi wa chama hicho.

Wazee wangu, nayasema hayo kwa sababu mara kwa mara ninapokutana nanyi nikiwa katika ziara zangu jimboni na wakati mwingine mnapowasiliana nami kwa njia mbalimbali mmekuwa mkionesha kuguswa kushitushwa na kutaka kujua kulikoni kuhusu mambo hayo yanayotokea.

Mimi, kama mnavyonijua nyote, ni mtu muwazi na mkweli. Siku zote nimekuwa mwepesi sana wa kuwaeleza kuhusu kila kinachotokea ili kuwaondoa hofu na wakati huo huo kuwahakikishia kwamba masuala yasiyo na msingi hususani yale yanayogusa siasa za kitaifa hayawezi kutuondoa katika mstari sahihi wa kuwahudumia wananchi wa Igunga, mkiwamo nyinyi wazee wangu ambao mmeniamini na kunituma kuwawakilisha.

Nyinyi wenyewe ni mashahidi wazuri kwamba tangu matukio yanayogusa jina langu yaanze kutokea miezi michache tu baada ya Serikali ya Awamu ya Nne inayoongozwa na Rais Jakaya Kikweti kuingia madarakani kwa mara ya kwanza mwaka 2005, tumekuwa tukiyapuuza na tukaendelea kufanya kazi pamoja kwa bidii.

Bado naamini na nitaendelea kuamini kwamba tulifanya uamuzi sahihi wa kuyapuuza matukio hayo kwani mbali ya kuendelea kutimiza malengo mbalimbali yaliyokuwamo katika Ilani yetu ya Uchaguzi ya CCM, pia mliendelea kuniamini kwa nafasi yangu ya kuwa mwakilishi wenu bungeni na hata mkaniruhusu nibebe jukumu jingine kubwa la kuwa Mjumbe wa NEC ninayewakilisha mkoa wetu wa kihistoria wa Tabora.

Wazee wangu, nyinyi ndiyo watu mnaolifahamu vyema jimbo letu la Igunga na hakika nyinyi ni sehemu muhimu ya watu wanaojua historia ya kisiasa ya Mkoa wa Tabora kwa miaka mingi hata kabla ya kuja kwa mfumo wa vyama vingi hapa nchini.

Hakuna shaka hata kidogo kwamba, Tabora ni kitovu hasa cha uasisi wa siasa za vyama vingi hapa nchini. Ni wazi kwamba huwezi ukazungumzia chimbuko la vyama vya upinzani tunavyoviona hapa nchini leo pasipo kugusa mkoa huu ambao umekuwa chimbuko la wanasiasa wenye mizizi hapa na nchini kwa ujumla.

Majina ya wanasiasa wa aina ya wazee wetu, hayati Chifu Said Abdallah Fundikira na Christopher Kassanga Tumbo, Kasela Bantu (Mungu awalaze mahala pema peponi), James Mapalala, Profesa Ibrahim Lipumba na mengi mengine yana mizizi yao katika Mkoa wetu wa Tabora.

Kutokana na ukweli huo basi ni wazi kwamba, nikiwa Mbunge wa Igunga kwa vipindi vinne mfululizo na wakati huo huo nikiwa Mjumbe wa NEC kwa vipindi vitatu mfululizo, moja ya kazi ambazo nimezifanya kwa uaminifu na kwa bidii kubwa huku nikiungwa mkono na kushirikiana nanyi ni ile ya kuhakikisha kwamba mkoa huu pamoja na kuwa kitovu cha upinzani unaendelea kubakia kuwa ngome muhimu ya kisiasa ya CCM.

Si vibaya tukakumbushana kwamba, wakati nachaguliwa kuwa mjumbe wa NEC wa Mkoa mwaka 1997, jimbo moja katika mkoa wetu lilikuwa likishikiliwa na upinzani. Leo hii Tabora ni mkoa pekee miongoni mwa mikoa iliyotuzunguka ambao haukupoteza jimbo hata moja kwenda upinzani katika Uchaguzi Mkuu wa 2010. Mafanikio haya tuliyafikia kwa pamoja kutokana na ushirikiano wenu wazee wangu.

Wazee wangu, Waswahili wanasema usione vyaelea, vimeundwa. Kazi ya kuijenga CCM katika mazingira yenye mizizi hasa ya upinzani nikiwa mbunge na hususani M-NEC kutoka Mkoa wa Tabora haijapata kuwa rahisi na itaendelea kuwa ngumu na ambayo mapambano yake ni makali sana.

Wazee wangu, kwa namna ya pekee kabisa napenda kuchukua fursa hii kuwashukuru nyinyi wazee wangu wa Igunga na wananchi wenzangu wote wa Mkoa wa Tabora kwa kushikamana na kuifanya kazi hiyo kwa bidii, uaminifu na mafanikio makubwa.

Matunda ya kazi hiyo kubwa yanaonekana. Pamoja na kuwa kitovu cha kihistoria cha siasa za upinzani, Tabora ndiyo mkoa pekee katika eneo hili ambao unaongozwa na wabunge wote kutoka CCM baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana na hata kabla ya hapo.Kwa sababu hiyo basi, wazee wangu, sote katika umoja wetu ukiacha mafanikio makubwa tuliyopata katika jimbo na Wilaya yetu ya Igunga, tunayo mambo mengine ya msingi ya kujivunia. Kwa moyo wa dhati na kwa unyenyekevu mkubwa napenda kuwapongeza kwa namna mlivyojitoa kukipigania na kukitetea chama chetu kwa ari na nguvu ya kipekee.KUJIVUA GAMBAWazee wangu, chama chetu chini ya uongozi wa Mwenyekiti wake, Rais Jakaya Kikwete kimeamua kwa kauli na nia moja kujitathmini na kufanya mabadiliko makubwa ya kimfumo yenye lengo la kukiwezesha kiendelee kubakia chama kinachoaminiwa na kuungwa mkono na Watanzania walio wengi.Dhamira ya mwelekeo huo wa kufanya mabadiliko ya ndani ya chama chetu ilitangazwa rasmi na Mwenyekiti wetu Rais Kikwete wakati wa kilele cha maadhimisho ya miaka 34 ya kuzaliwa kwa CCM, mjini Dodoma.Katika hotuba yake hiyo, Rais Kikwete aliyafananisha mabadiliko hayo na tabia ya kawaida na ya asili ya nyoka na wanyama wengine kadhaa ya ‘Kujivua Gamba’.Wazee wangu hatua ya kwanza ya utekelezaji wa azimio hilo na mwelekeo huo sahihi ilifanyika mjini Dodoma wakati wa kikao cha Kamati Kuu ya Taifa ya CCM ambacho mimi nilikuwa mjumbe wake.Wakati wa kikao hicho, wajumbe wote wa Kamati Kuu na wale wa Sekretarieti ya chama chetu wa wakati huo kwa kauli moja tulikubaliana kujiuzulu, lengo likiwa ni kumpa Mwenyekiti wetu fursa nzuri ya kufanya mabadiliko ya uongozi yatakayotoa nafasi ya kupata mwelekeo mpya wa Chama.Wazee wangu, tulifanya hivyo tukionesha kuunga mkono kwa asilimia 100 kile ambacho bado naendelea kuamini kuwa ni mawazo sahihi na yenye mwelekeo thabiti ya Mwenyekiti wetu ambayo kwa kiwango kikubwa yalikuwa yakiakisi matokeo ya Uchaguzi Mkuu wa urais, ubunge na udiwani wa Oktoba mwaka jana.Niliseme kwa maneno machache tu hili. Ingawa ni kweli kwamba Uchaguzi Mkuu wa mwaka jana umekirudisha madarakani chama chetu kwa kukipa ushindi mkubwa katika uchaguzi wa urais, ubunge na udiwani kwa Tanzania Bara na Zanzibar, kiwango cha ushindi tulichopata kimeonyesha waziwazi dalili za wananchi kupunguza imani yao kwetu kuilinganisha na ilivyokuwa mwaka 2005.Tungekuwa ni chama cha siasa cha ovyo iwapo tungepuuza kupungua kwa kura za rais kutoka zaidi ya asilimia 80 tulizopata mwaka 2005 hadi kufikia aislimia 61 mwaka jana kiwango ambacho ni pungufu kwa asilimia 20 ya kura katika kipindi cha miaka mitano tu, hasa ikizingatia ukweli kwamba mgombea urais ni mtu yule yule.Tungekuwa ni chama cha siasa kilichokosa umakini iwapo tungekaa pasipo kuchukua hatua zozote za kujiimarisha baada ya matokeo ya Uchaguzi Mkuu kuonesha wazi kukua kwa upinzani ambao umeongeza idadi ya wabunge na madiwani katika pande zote mbili za muungano.Matokeo hayo ya uchaguzi ambayo hapana shaka yamekitikisa chama chetu yalitukumbusha wasia ambao tuliachiwa na Baba wa Taifa aliyesema; ‘Bila ya CCM Madhubuti Nchi Yetu Itayumba’.Wazee wangu, kwa sababu ya kutambua ukweli kwamba hakuna haki isiyo na wajibu kama nilivyosema awali, mimi na wenzangu tuliokuwa katika Kamati Kuu tuliona ulazima, haja na umuhimu wa kukubali kwa kauli moja wito wa kututaka tujiuzulu ikiwa ni hatua moja ya kujipanga na kukijenga upya chama chetu.KUJIVUA GAMBA KWAPOTOSHWAWazee wangu, kilichotokea baada ya kujiuzulu kwetu kila aliye ndani na nje ya chama chetu amekisikia na anakifahamu. Chama kilipata safu mpya ya uongozi iliyotokana na kuundwa kwa Sekretarieti inayoongozwa na Katibu Mkuu wetu mpya, Mhe. Wilson Mukama, na Kamati Kuu iliyokuwa na sura tofauti na ile ya awali.Wakati tukitafakari na kuangalia mustakabali mpya wa kisiasa ndani ya chama chetu, ghafla yalianza kutokea mambo ambayo chokochoko zake zilianza kusikika tangu tukiwa ndani ya Kamati Kuu ambayo ilijiuzulu baadaye.Mara tu baada ya kumalizika kwa kikao cha Halmashauri Kuu ya Taifa ambacho kilichagua wajumbe wapya wa Kamati Kuu na kuidhinisha uundwaji wa Sekretarieti mpya, dhana ya kujivua gamba ambayo naamini Mwenyekiti wetu aliianzisha kwa nia njema ilianza kuenezwa ikichukua tafsiri na mwelekeo tofauti na ule wa awali.Wajumbe wawili wa Sekretarieti, Naibu Katibu Mkuu (Tanzania Bara), Mhe. John Chiligati, na Katibu wa Idara ya Itikadi na Uenezi, Mhe. Nape Nnauye, walisikika wakitangaza kwamba Halmashauri Kuu ya Taifa ilikuwa imefikia uamuzi wa kuwapa siku tisini wale walioitwa watuhumiwa wanaokabiliwa na tuhuma za ufisadi ndani ya chama kujitoa katika nafasi zao za uongozi vinginevyo watafukuzwa na chama.Wazee wangu, baada ya kushinikizwa sana na vyombo vya habari wawataje kwa majina wanasiasa waliokuwa wakituhumiwa kwa ufisadi ambao ni wajumbe wa NEC na ambao wanapaswa kujiuzulu nyadhifa zao, wajumbe hao wa Sekretarieti walikwenda mbele zaidi.Baada ya awali kuwaeleza waandishi wa habari kwamba majina ya watuhumiwa hao yalikuwa yakifahamika kutokana na kuhusishwa katika kashfa tofauti kama zile za Richmond, EPA na ununuzi wa rada, mwishoni viongozi hao walikaririwa wakiyataja majina ya wanasiasa watatu kuwa ndiyo ambao walikuwa wakilengwa na maamuzi hayo.

Wazee wangu, nilishangazwa na kushitushwa na namna porojo na fitina za kisiasa zilivyofinyangwa kwa mara nyingine tena baada ya kusikia jina la mbunge wenu ambaye ni mimi, likitajwa kuwa miongoni mwa yale matatu ya viongozi waliokuwa wakitakiwa eti kupima wenyewe na kisha kuchukua uamuzi wa kujiuzulu nafasi zao za uongozi ndani ya NEC katika kipindi cha siku tisini.Niliseme hili mapema. Mshangao na mshituko wangu haukusababishwa na kutajwa kwa jina langu, la hasha, bali namna uamuzi halisi wa NEC na hususani dhana nzima ya ‘kujivua gamba’ ilivyoweza kupindishwa na wajanja wachache na kisha kuendeshwa kwa maslahi binafsi ya kikundi fulani cha watu.Pili, nilishangazwa na kushitushwa na hatua ya viongozi wa chama changu ambacho nimekitumikia kwa bidii na uaminifu mkubwa kufanya juhudi kubwa hata kukivisha kikao kitukufu cha NEC uamuzi ambao msingi wa hoja zake ni vita vya kimakundi ya kisiasa yaliyo ndani ya CCM kwa upande mmoja na propaganda za vyama vya siasa vya upinzani na vyombo vya habari kwa upande mwingine.Tatu, nilishangazwa na kushitushwa na ujasiri ambao umekuwa ukioneshwa na baadhi ya viongozi wetu wapya wa Sekretarieti wanaolitaja jina langu na kulihusisha na kile wanachokiita ufisadi ambao hata ukweli wa kimazingira na kihistoria ukiachilia mbali ushahidi wa wazi umeshathibitisha kwamba ni porojo za kisiasa zilizotokana na makovu na matarajio ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2005 na ule ujao wa 2015.Wazee wangu, nyinyi ni mashahidi kwamba, mbali ya mimi mwenyewe kujitokeza kupitia vyombo vya habari na kueleza wazi kwamba sijapata kujihusisha katika vitendo vyovyote vya ukiukwaji wa maadili ya uongozi au vya rushwa, hakuna ushahidi wowote uliotolewa unaonihusisha na kashfa yoyote miongoni mwa zile zilizotajwa.Wazee wangu, ni wazi kwamba kama chama chenye siasa chenye dhamana ya kuwaoongoza Watanzania kutoka katika lindi la ufukara, maradhi, matatizo ya makaazi na mengineyo siku zote tunapaswa kuwa makini katika kuhakikisha kwamba changamoto za kuwaongoza na kuwakomboa wananchi waliotupa dhamana hazitikiswi na mawimbi ya matakwa ya nyakati ama ya vyombo vya habari au wapinzani wetu wa kisiasa walio nje ya CCM.Ni kwa sababu ya kulitambua hilo na hasa kuyatambua madhara yanayoweza kukipata chama chetu na nchi yetu iwapo tutaendekeza siasa za kupakana matope pasipo na sababu za msingi, kuchafuana kusikokoma na kulipizana kisasi ndiyo maana nimeona nitumie fursa hii kuzungumza nanyi wazee wangu ili kuweka kumbukumbu sahihi.MAAMUZI YANGUWazee wangu, nimetafakari sana na kimsingi nimefikia hatua ya kupima yale ambayo yamekuwa yakisemwa na kuandikwa juu yangu na ambayo kwa mtazamo wangu unaoungwa mkono na wanafamilia yangu, marafiki zangu na washirika wangu wa kibiashara walio ndani na nje ya nchi, naona umefika wakati muafaka wa kuchukua hatua.Kwa sababu ya kutambua uzito wa hatua ninazokusudia kuzichukua, niliona halitakuwa jambo la hekima hata kidogo iwapo ningefanya hivyo pahala pengine popote bali hapa Igunga mbele ya nyie wazee wangu.Baada ya kukaa na wanafamilia yangu, marafiki na washirika wangu wa kibiashara niliona halitakuwa jambo la busara hata kidogo kuendelea kuvutana na viongozi wa chama changu na wanachama wenzangu wa CCM katika mambo ambayo yanaweza kumalizwa kwa njia muafaka.Wazee wangu, sina budi niwaeleze kwamba, mbali ya athari za kisiasa na kifamilia, vita vya ovyo vya kisiasa kama hivi tunavyoviendesha na kuviendeleza ndani ya CCM na ndani ya nchi yetu huwa vina athari kubwa katika ulimwengu wa kibiashara. Athari kama hizo za kibiashara huingia ndani zaidi kuliko vichwa vya habari vya magazeti vinavyolenga kuchafuana, na athari hizo huwa kubwa zaidi kwa mtu kama mimi kwa sababu tofauti na wengine wengi hapa nchini, mimi ni mfanyabiashara wa kimataifa.

Katika ulimwengu wa kibiashara wa leo, vita hivi ambavyo vinaweza kuonekana kuwa ni vidogo tu vyenye malengo ya kuchafuana kisiasa, vinakuwa na athari kubwa katika uhusiano wa kibiashara kuliko hata wale wasioelewa wanavyoweza kukadiria. Ndiyo maana nimeona ni afadhali sasa niwape nafasi wale wanaoendesha siasa hizi uchwara na zisizo na tija waendelee na siasa zao hizo ambazo kwa bahati mbaya kwao, mimi sina muda nazo na siwezi kuwa sehemu yake. Na mimi kwa upande wangu niendelee na maisha yangu.Kutokana na ukweli huo na sababu zote hizo basi, kwa moyo wa dhati na kwa nia thabiti, hatua ya kwanza niliyoiona kuwa ninapaswa kuichukua ilikuwa ni hii ya kuitikia wito unaotokana na msukumo wa ndani ya nafsi yangu wa kuamua kukomesha kabisa malumbano na mivutano isiyo na manufaa kwangu binafsi, kwa viongozi wa chama changu na chama chenyewe.Msukumo huo si mwingine bali ni ule wa kuamua kuachia nafasi zangu zote za uongozi ndani ya chama, nikianzia na ile ya ujumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa nikiuwakilisha Mkoa wa Tabora na hii ya ubunge wa Igunga ambazo kama si kwa baraka za chama changu nisingelikuwa nazo.Napenda kuliweka hili sawa sawa. Uamuzi wangu wa kuachia nafasi zangu zote za uongozi nilizopata kwa tiketi ya CCM haukutokana na wala haumaanishi kukubaliana na shinikizo lililopotoshwa kuhusu azma ya utekelezaji wa dhana ya kujivua gamba, la hasha, bali dhamira ya dhati ya kuachana na siasa hizi uchwara (gutter politics) na kutumia muda wangu kushughulika na biashara zangu.Aidha, nimefikia uamuzi huo lengo likiwa ni kuwajengea heshima na imani machoni mwa wanachama na wananchi wengine, viongozi wangu ambao naamini baada ya mimi kujitoa watapata fursa ya kutafakari upya changamoto nyingine mbadala zinazowakabili ambazo msingi wake ni dhamana kubwa walizo nazo za kukiongoza chama chetu na nchi yetu kupitia Serikali yake.Wakati nachukua uamuzi huu, natambua vyema kwamba, watatokea watu ndani ya chama chetu na nje ambao watafanya kila juhudi kupotosha au kupindisha ukweli kuhusu hatima yangu ya kisiasa baada ya kujiweka kando na kujipa mimi mwenyewe na chama changu fursa ya kutafakari kwa kina majaaliwa yangu na ya nchi yangu katika siku zijazo.Nafanya hivyo nikiwa na imani thabiti kwamba, uamuzi wangu huu, hususani ule wa kuachia nafasi yangu ya ubunge, yatakipa fursa nyingine CCM ya kuendelea kuliongoza jimbo letu la Igunga katika kipindi cha miaka minne ijayo kabla ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2015.

Kwa upande mwingine, uamuzi wangu huu naona ni fursa kwa viongozi wa Chama changu cha CCM kutafakari na kuamua njia wanayoiona wao ni sahihi kuichukua kwa hatima na mustakabali wa chama chetu na ambayo wanaamini itakipa nguvu mpya ya kisiasa dhidi ya vyama vya upinzani.Sambamba na hilo, ninayo imani thabiti kwamba, uamuzi wangu wa kubakia kuwa mwanachama wa kawaida na mtiifu wa CCM utakuwa chachu kwa chama changu na kwa Serikali yake kuwatumikia wananchi kwa Ari Zaidi, Kasi Zaidi na Nguvu Zaidi.Mwisho kabisa, nikimalizia naomba nitumie fursa hii kutoa heshima za pekee kwa Rais Jakaya Kikwete kwa kazi kubwa aliyoifanyia na anayoendelea kuifanyia nchi yetu. Amefanya mengi na makubwa kuiendeleza nchi yetu na watu wake kuliko inavyothaminiwa na kufahamika. Kazi yake kubwa inashindwa kuthaminiwa na kufahamika kutokana na siasa chafu tunazoziendesha Tanzania. Wasia wangu kwa wanasiasa wenzangu, waandishi wa habari na Watanzania wenzangu kwa ujumla ni kuwa tunahitaji kuisaidia nchi yetu kwa kufanya siasa zenye mwelekeo wa kujenga ambazo ndiyo hasa zinapaswa kuwa siasa kwa maana halisi ya neno hilo.

Wazee wangu, baada ya maelezo hayo, nawashukuru sana kwa kunisikiliza na kunielewa.Ahsanteni sana.
Mwisho…

Ndolo, Fabriges wagonganisha vichwa Yanga


PANGA pangua ya nani abaki na yupo atoke kati ya Tonny Ndolo na Haruna Niyonzima 'Iniesta' ndani ya usajili mpya wa mabingwa wapya wa Kombe la Kagame, Yanga, imeibua mzozo ndani ya klabu hiyo.
Ndolo, Mganda aliyesajiliwa toka Kagara Sugar na Iniesta aliyetoka APR ya Rwanda, mmoja kati yao anapaswa kuachwa kwenye usajili ili kutekelezwa kwa kanuni ya idadi ya wachezaji wa kigeni wanaopaswa kusajiliwa na klabu za soka nchini.
Yanga tayari imetimiza idadi ya wachezaji sita wa kigeni, mmoja zaidi ya idadi inayotakiwa na TFF na kwa maana hiyo kuilazimisha klabu hiyo kupunguza jina moja na mzozo unakuja juu ya nani aachwe kati ya wachezaji hao wawili kutokana umuhimu wao katika kikosi hicho.
Awali ilikuwa ikitajwa kwamba mshambuliaji Hamis Kiza 'Diego' ndiye aliyekuwa katika hatihati ya kubakishwa Yanga, lakini kwa kiwango alichokionyesha kwenye michuano ya Kagame akiifungia mabao muhimu akishirikiana na 'mapro' wengine wawili, Davis Mwape wa Zambia na Kenneth Asamoah aliyewapa ubingwa mbele ya Simba, hali imekuwa kizungumkuti.
Mchezaji mwingine wa kigeni aliyepo Yanga ni kipa Yew Berko kutoka Ghana ambaye msimu uliopita wa Ligi Kuu Tanzania Bara alichaguliwa kuwa Kipa Bora akimfunika Juma Kaseja.
Habari za ndani za klabu hiyo zinasema mapendekezo ya kocha Sam Timbe tangu awali ni kuachana na Iniesta, lakini kamati ya usajili imekuwa ikimkumbatia kiungo huyo, ikitaka wa kuachwa awe Ndolo, kitu ambacho kocha hataki kusikia kutokana na kumhitaji nyota huyo.
Hali hiyo imefanya hata Msemaji wa klabu hiyo, Louis Sendeu kushindwa kujua ukweli yupi kati ya wachezaji hao wawili ndiye atakayeachwa wakati dirisha la uhamisho wa wachezaji likifungwa Alhamisi iliyopita.
"Kwa kweli mie sijui nani ataachwa, ila hatma yao itafahamika wakati wowote kwa vile tunajua tunatakiwa kupunguza jina la mchezaji mmoja kutokana na kuzidisha idadi ya wachezaji wa kigeni inayotakiwa na kanuni za usajili nchini," alisema Sendeu.

Msiwaite wafanyakazi wenu wa ndani majina mabaya


WAAJIRI wa wafanyakazi wa majumbani nchini, wameombwa kuachwa kuwaita majina
mabaya watumishi wao, kwa madai kufanya hivyo ni kushusha hadhi na utu wa wafanyakazi hao ambao ni watu muhimu kwao na familia zao kwa ujumla.
Kadhalika wametahadhariwa kuepuka tabia ya kuwaajiri wafanyakazi wenye umri chini ya
miaka 17 kutokana na ukweli umri huo ni mdogo kwa ajira na pia ni kosa kulingana na sheria za kimataifa kuhusu ajira za watoto.
Hayo yalisemwa na wawezeshaji wa semina ya siku moja ya 'Waajiri Makini' iliyoandaliwa na Shirika la kuhudumia Afya na Maendeleo ya Wanawake na Watoto ya Kiota, (KIWOHEDE), walipokuwa wakitoa mafunzo ya kujenga mauhusiano bora kati ya waajiri na wafanyakazi wa majumbani, iliyofanyika katikati ya wiki iliyopita.
Edda Kawala na Stella Mwambenja wote kutoka KIWOHEDE, walisema tabia ya waajiri
kuwaita majina mabaya watumishi wao na kuwanyanyasa au kuwabagua ni jambo baya kwani
linashusha hadhi na utu wa wafanyakazi hao kinyume na sheria na mikataba wa kazi kimataifa.
Wawezeshaji hao walisema ni wajibu waajiri kuishi kwa wema na watumishi wao kwa
kuwafanya kama sehemu ya familia zao badala ya kuwabagua na kunyanyapaa, kitu ambacho sio ubinadamu na kinachochangia uhasama usio na maana baina ya wawili hao.
Pia waliwataka waajiri kuchungua kuajiri wafanyakazi wenye umri mdogo ili wasiweze kunasa kwenye mikono ya sheria inayokataza ajira kwa watoto.
"Mbali na kuchunga umri, pia msiwe mnawabagua wafanyakazi wenu wakati wamekuwa
msaada mkubwa katika majumba yenu kwa kazi wanazowafanyia, muwalipe vema na kwa
wakati kwa vile nao ni wanastahili mahitaji kama watu wengine," alisema Stella.

Wafanyakazi wa Majumbani sasa wapata 'Rungu'

KUPITISHWA kwa Mkataba wa Kimataifa wa 189 wa Shirika la Kazi Duniani, ILO,
kumeelezwa kuwa kama ni 'rungu' kwa wafanyakazi wa majumbani kuwashughulikia waajiri
wao watakaokiuka sheria na mikataba ya kazi kama ilivyo kwa wafanyakazi wengine nchini.
Mkataba huo wa kuwatambua wafanyakazi hao wa majumbani ulipitishwa Juni 16 mwaka huu
katika mkutano wa 100 wa ILO uliofanyika nchini Uswisi, ambapo siku moja kabla ya
kupitishwa kwake, Rais wa Tanzania, Jakaya Kikwete alihutubia mkutano huo kuuridhia,
Akizungumza na MICHARAZO, Mratibu wa Shirika la Wafanyakazi wa Majumbani Kanda ya
Afrika, IUF, Bi Vick Kanyoka, alisema kuridhiwa kwa mkataba huo kumetoa fursa na nafuu kwa watumishi hao wa majumbani ambao kwa miaka mingi walikuwa hawathaminiwi nchini.
Bi Kanyoka, alisema kulingana na mkataba huo ni kwamba wafanyakazi wa majumbani kwa
sasa wanatambuliwa kama wafanyakazi wengine wakihitajiwa kulindwa na kupewa haki zao
ikiwemo kusainishwa mikataba na makubaliano kabla ya kuanza kazi kwa muajiriwa.
Mratibu huyo alisema kitu cha muhimu baada ya kupitishwa kwa mkataba huo ni serikali ya Tanzania na wananchi wake kuutekeleza kwa vitendo mkataba huo ili kuhakikisha wafanyakazi wanajivunia kazi yao tofauti na siku za nyuma walipokuwa wakijificha.
"Kwa hakika kupitishwa kwa mkataba huo wa 189 ni kama rungu kwa wafanyakazi wa
majumbani kuweza kuwabana waajiri wao, ambao kwa miaka mingi walikuwa wakiwabagua,
kuwanyanyasa na kuwadharau wakiwachukulia kama 'vijakazi'," alisema.
Aliongeza kwa kuwataka watumishi hao kuwa mstari wa mbele katika utekelezaji wa mkataba huo kwa kutokubali kuajiriwa kabla ya kuingia mkataba na kuridhia haki zake stahiki katika ajira yake, ili inapotokea tatizo mbele ya safari iwe rahisi kusaidiwa.
Bi Kanyoka, aliwasihi pia waajiri kuridhia na kuutekeleza mkataba huo kwa kuamini watumishi hao ni kama sehemu za familia zao na hivyo kuwapa huduma na stahiki zote ikiwemo kuwalipa fedha kulingana na kima wanachokubaliana na kwa muda muafaka.
"Pia wawajali na kuwathamini kwa sababu wao ni watu tegemeo kwao na familia zao, hivyo kukaa nao kwa ubaya ni kusababisha matatizo ambayo tumekuwa tukishuhudia katika jamii yetu," alisema.
Mratibu huyo alisema mkataba huo ulipitishwa kwa kupigiwa kura 396 za ndio huku kura 16 zikiukataa miongoni mwa nchi zilizougomea ikiwa ni taifa la Uingereza, huku mataifa ya Afrika ikiwemo Tanzania na yale ya Amerika Kusini na Kaskazini yakiongoza kwa kuupitisha.

Thursday, July 14, 2011

Banka yu tayari wa lolote Simba



KIUNGO nyota wa timu ya Simba na timu ya taifa, Taifa Stars, Mohammed Banka, amesema ingawa hajapata taarifa rasmi ya kutemwa ndani ya kikosi hicho, lakini yupo tayari kwa lolote mradi alipwe chake kwa kuvunjwa mkataba alionao na klabu hiyo.
Aidha amedai kusikitishwa na lawama anazotupiwa kwa kushindwa kung'ara kwenye pambano la fainali za Kombe la Kagame dhidi yao na Yanga, wakati ilifahamika kuwa ametoka majeruhi kitu ambacho hata kocha Moses Basena alikuwa akifahamu.
Akizungumza na MICHARAZO mapema leo, Banka alisema hana taarifa za kuachwa na Simba kama baadhi ya vyombo vya habari vilivyoripoti jana, lakini kama jambo hilo ni kweli hana jinsi zaidi ya kukubaliana na mapendekezo ya viongozi wake.
Banka alisema kitu cha msingi ni klabu ya Simba imlipe chake kwa kuvunja mkataba wao, ili akatafute maisha pengine, ingawa alisema amesikitishwa na kushutumiwa kwa kuwa miongoni mwa walioikosesha Simba taji la saba la michuano ya Kagame.
"Kwa kweli sijapewa taarifa yoyote rasmi zaidi ya kusoma kwenye vyomvo vya habari, lakini kama uongozi umeazimia hivyo, sitakuwa na jinsi zaidi ya kusubiri kulipwa changu kwa kuvunjwa mkataba nitafute mahali pa kwenda," alisema.
Aliongeza, kucheza kwake chini ya kiwango katika mechi ya Simba na Yanga katika fainali za Kagame ilitokana na kutoka kuwa majeruhi, kitu ambacho hata mwenyewe alishtuka alipoagizwa na kocha Basena kuingia dimbani.
"Kocha aliniambia kabla ya mechi atanichezesha kipindi cha pili ili kuangalia maendeleo yangu ya kupona majeraha, hivyo alivyoniambia niingie nilishangaa, lakini kama mchezaji ninayezingatia nidhamu sikuweza kumbishia, ila Simba wasinielewe vibaya," alisema Banka.
Kiungo huyo alisema anaamini mchango wake ndani ya Simba ni mkubwa kuliko lawama anazopewa sasa, lakini kwa kuwa soka ndivyo lilivyo anajiandaa kutafuta maisha mahali pengine kwa kuamini 'riziki' yake imeisha ndani ya klabu hiyo.
Banka, pamoja na Mussa Hassani Mgosi na Athumani Idd 'Chuji' walitajwa kuwa miongoni mwa waliopendekezwa kutemwa ndani ya Simba kwa ajili ya msimu ujao wa Ligi Kuu Tanzania Bara na michuano ya kimataifa kutokana na kuonyesha kiwango duni kwenye Kombe la Kagame, ambapo Simba ilifungwa na Yanga bao 1-0.

Mwisho

Bujibu kuchapana na Mtambo wa Gongo


WAKATI michuano ya Ligi ya Kick Boxing iliyotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu ikiahirishwa hadi Desemba, mabondia wakongwe wa ngumi za kulipwa nchini, Maneno Osward na Ernest Bujiku wanatarajiwa kupamba ulingoni kupigana.
Maneno Osward maarufu kama Mtambo wa Gongo atapigana na Bujiku katika moja ya mapambano ya ngumi yatakayoshindikiza pambano la Kick Boxing kati ya Amour Zungu wa Zanzibar dhidi ya Mchumia Tumbo litakalofanyika Julai 30 kwenye ukumbi wa DDC Keko, Dar es Salaam.
Kaseba alisema, mbalio na pambano la Osward na Bujiku siku hiyo pia mabondia wa kike, Jamhuri Said wa Tanzania atapimana ubavu na Rukia Kaselete wa Kenya katika pambano jingine la Kick Boxing.
Alisema michezo mingine itakayosindikiza mipambano hiyo ni kati ya Fadhila dhidi Demu wa Kisarawe, Dragon Kaizum atakayepigana na Faza Boy, Idd dhidi ya Dragon Boy, Lion Heart dhidi ya Begeje na michezo mingine ya ngumi za kulipwa.
Kaseba alisema michezo hiyo inafanyika ili kuwapa burudani wakazi wa Dar es Salaam ambao walikuwa wakijiandaa kushuhudia ligi ya Kick Boxing ambayo imeahirishwa hadi Desemba kwa ajili ya kufanya maandalizi ya kutosha.
"Tumeamua kuahirisha ligi ya Kick Boxing hadi Desemba kutoa muda kwa mabondia kujiandaa na kufanya katika kiwango cha kimataifa, hivyo ili kutowanyima raha wadau wa mchezo huo tumeandaa michezo kadhaa ya Kick Boxing na ngumi za kulipwa siku ya Julai 30 itakayofanyika kwenye ukumbi wa DDC Keko," alisema Kaseba.
Alisema Bujiku na Osward kila mmoja kwa sasa yupo katika maandalizi makali ya kuonyeshana umwamba wakikumbushia enzi zao wakitamba kwenye mchezo huo.

Mwisho

Waajiri wapigwa msasa kuishi na wafanyakazi wa majumbani



WAAJIRI wa wafanyakazi wa ndani watakiwa kutowabagua na kuwanyanyasa watumishi wao wa ndani na badala yake kuishi nao kwa wema kutokana na ukweli wao ni watu wa karibu na wasiri wakubwa wa familia zao.
Wito huo umetolewa kwenye semina ya siku moja iliyoandaliwa na Asasi ya kiraia ya KIWOHEDE kwa lengo la kujenga mauhusiano mema baina ya waajiri na watumishi wa kazi za ndani ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakichukuliwa kama vijakazi.
Mgeni rasmi wa semina hiyo, Sheikh Shughuli Sheikh, ambaye ni Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Malapa Kata ya Buguruni na Mwezeshaji wa semina hiyo Edda Kawala, walisema kuna umuhimu wa waajiri kuwaona wafanyakazi wa majumbani kama sehemu ya familia zao.
Sheikh, alisema kutokana na mchango na umuhimu wa wafanyakazi wa ndani ambao ni tegemeo la waajiri katika kusaidiwa kazi za nyumbani ni vema watumishi hao wakapewa heshima na kuthaminiwa kama wanafamilia.
"Wao ndio wanaowapikieni, kuwafulieni na kazi nyingine za ndani, hivyo ni wasiri na watu muhimu katika familia zenu hivyo ni vema kukaa nao kwa wema mkiwajali na kuwathamini tofauti na baadhi yenu mnavyowafanyia," alisema Sheikh.
Naye Mwezeshaji alisema lengo la semina hiyo ni kuona waajiri na wafanyakazi hao wa ndani wanakuwa na mauhisiano mema, pamoja na kila mmoja kuhakikisha wanakuwa na mikataba au makubaliano yanayolinda haki na hadhi ya kila mmoja.
Alisema KIWOHEDE, imebaini zipo baadhi ya nyumba au waajiri wamekuwa wakiwabagua watumishi wao na kuwanyima haki zao stahiki na kuchangia kuwepo kwa uhasama na kuifanya kazi hiyo kudharaulika mbele ya jamii.
Washiriki wa semina hiyo wengi wao wakiwa ni akinamama, walisema kuna mambo mengine hawakuwa wanayajua juu ya haki za msingi za watumishi hao na semina hiyo imewafungua macho na kuahidi kuwa 'mabalozi' mema warejeapo makwao.
Semina hiyo ilielekeza umri stahiki wa wafanyakazi wanaopaswa kuajiriwa kwa kazi za majumbani, haki za msingi stahiki za watumishi hao na namna ya uwajibikaji wa kila mmoja kati ya waajiri na wafanyakazi hao.

Mwisho

Tanzania yapongezwa kuridhia mkataba wa ILO


SERIKALI ya Tanzania imepongezwa kwa kuwa miongoni mwa nchi zilizopitisha Mkataba wa Kimataifa wa Kutambuliwa kwa Wafanyakazi wa Majumbani, iliuyopitishwa kwenye Mkutano wa 100 wa Shirika la Kazi Duniani (ILO).
Kadhalika Rais Jakaya Kikwete amepongezwa kwa hutuba aliyoisoma kwenye mkutano huo juu ya serikali ya Tanzania kuwatambua wafanyakazi hao kama watumishi halali wanaoostahiki hakio zote wa waajiriwa, akiombwa kuhakikisha utekezaji unafanyika.
Mratibu wa Shirika la Wafanyakazi wa Majumbani Kanda ya Afrika (IUF), Vick Kanyoka, akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam alieleza maazimio ya mkutano wa ILO uliofanyika mwezi uliopita mjini Geneva, Uswisi.
Kanyoka, alisema kitendo cha Tanzania kuwa miongoni mwa nchi zilizopigia kura ya kupitisha mkataba huo wa 189 wa kuwatambua wafanyakazi wa majumbani ni ushindi kwa wafanyakazi wote ambao kabla ya hapo walikuwa wakichukuliwa kama watumwa.
Aliongeza IUF, inaipongeza Tanzania na Rais Jakaya Kikwete aliyehutubia kwenye mkutano huo Juni 15 mwaka huu na kuiomba serikali hiyo itekeleze kwa vitendo mkataba huo ili wafanyakazi wa majumbani kupata haki na kuthaminiwa kama wafanyakazi wengine.
Alisema ingawa sheria ya kuwalinda na kuwatetea wafanyakazi majumbani ipo, lakin i utekelezaji wake umekuwa ni tatizo na ndio maana IUF inaiomba Tanzania kuhakikisha jambo hilo linapata ufanisi ili kuleta usawa miongoni mwa watumishi hao.
"IUF tunaipongeza Tanzania na Rais wake kwa kuridhika kupitishwa kwa mkataba wa 189 wa kutambulika kwa wafanyakazi wa majumbani, uliopitioshwa Juni 16 mwaka huu ambapo ulipitishwa kwa kura 396, huku 16 zikiukataa miongoni mwa mataifa yaliyoukataa likiwa ni Uingereza," alisema Kanyoka.
Mratibu huyo alisema ni kutekelezwa kwa vitendo kwa mkataba huo kutatoa fursa ya waajiri kuwathamini na kuwajali watumishi hao kwa kuingia nao mkataba na kuwalipa haki zao stahiki kma ilivyo kwa watumishi wengine.
Alisisitiza ni muhimu wafanyakazi hao kusaidia kufanikisha uitekelezaji huo kwa kuwa wa kwanza kuhakikisha wanaingia mikataba na makubalino na waajiri wao kabla ya kuanza kazi ili watakapofanyiwa kinyume iwe rahisi kutetewa na kupata haki zao.

Mwisho

Saturday, July 9, 2011

Ligi ya Kick Boxing yaiva

MICHUANO ya Ligi ya Kick Boxing inatarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwezi huu jijini Dar es Salaam kwa mabondia wa kike na wa kiume kuumana kuwania ushiriki wa fainali za taifa zitakazofanyika baadaye mwaka huu.
Kwa mujibu wa mratibu wa michuano hiyo, Japhet Kaseba, alisema michuano hiyo itafanyika Julai 31 kwenye ukumbi wa DDC Mlimani, Mwenge jijini Dar es Salaam.
Kaseba, alisema kabla ya kufanyika kwa michuano hiyo anatarajiwa kukutana na mabondia washiriki kwa lengo la kuwapa darasa dhidi ya mchezo huo ambao safari hii utashirikisha wakongwe na chipukizi ikiwa ni mikakati ya kuendeleza mchezo huo.
"Michuano yetu ya ligi ya Kick Boxing itafanyika mwishoni mwa mwezi huu kwenye ukumbi wa DDC Mlimani, ambapo mabondia mbalimbali wake wa waume chipukizi na wakongwe wataonyesha kazi safari hii," alisema.
Kaseba alisema kwa sasa anaendelea na mipango ya kusaka wadhamini kwa ajili yua kulipiga tafu shindano lao ambalo limekuwa kikifanyika kwa mwaka wa tatu sasa katika njia ya kurejesha msisimko wa michuano hiyo iliyompa mataji ya Afrika na Dunia.
Katika hatua nyingine bingwa wa Kick Boxing wa Uganda, Moses Golola, alifanikiwa kumchakaza bondia toka Sudan, Abdul Quadir Rahim mwishoni mwa wiki jijini Kampala, akisisitiza ana hasira ya kutaka kupigana na Kanda Kabongo wa Tanzania.
Golola aliyepigwa na Kabongo katika pambano la kuwania ubingwa wa Afrika, alisema ushindi wake wa KO ya raundi ya pili dhidi ya Msudan ni salamu kwa Kabongo kuwa ajiandae kwa ajili ya kisasi siku wakikutana ambapo huenda ikawa ndani ya mwaka huu.

Klabu za ngumi kupepetana Ilala

KLABU za ngumi za ridhaa za Amana na Matimbwa ni miongoni mwa klabu zaidi ya tano zinazotarajiwa kuonyeshana kazi katika mfululizo wa michuano maalum ya mchezo huo inayoendelea wilayani Ilala jijini Dar es Salaam.
Klabu zingine zitakazopambana katika michezo itakayofanyika mwishoni mwa wiki hii ikiratibiwa na taasisi ya Kinyogoli Foundation ni Ashanti, Big Right na zingine ambazo hazikuweza kufahamika mapema.
Mratibu wa michuano hiyo, Rajab Mhamila 'Super D' alisema michezo hio itafanyika Jumamosi kwenye ukumbi wa Panandipanandi, Ilala Bungoni.
Super D, alisema maandalizi ya michezo hiyo yamekamilika ikiwemo vikosi vya timu zote kuendelea kujifua.
Aliwataja baadhi ya mabondia watakaoziwakilisha klabu zao kuwa ni Ibrahim Class, Khalfan Othman, Kassim Sambo na Saidi Ally kwa upande wa Amana, wakati Matimbwa itawakilishwa na Mohamed Matimbwa, Mohamed Muhani, Edson Joviki na Mohamed Kumbilambali.
Kwa upande wa Ashanti, Super D alisema itawakilishwa na mabondia kama Uwesu Manyota, Ramadhani Kimangale, Mark Edson na wengine na mipambano yao itachezwa kwa raundi nne nne kila mmoja.
Aliongeza kwa kutoa wito kwa wadau wa ngumi kujitokeza kuzisaidia klabu shiriki na mabondia vifaa vya michezo na mahitaji yao mengine ili kuwatia moyo wa kuupenda mchezo huo.