STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, July 14, 2011

Waajiri wapigwa msasa kuishi na wafanyakazi wa majumbani



WAAJIRI wa wafanyakazi wa ndani watakiwa kutowabagua na kuwanyanyasa watumishi wao wa ndani na badala yake kuishi nao kwa wema kutokana na ukweli wao ni watu wa karibu na wasiri wakubwa wa familia zao.
Wito huo umetolewa kwenye semina ya siku moja iliyoandaliwa na Asasi ya kiraia ya KIWOHEDE kwa lengo la kujenga mauhusiano mema baina ya waajiri na watumishi wa kazi za ndani ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakichukuliwa kama vijakazi.
Mgeni rasmi wa semina hiyo, Sheikh Shughuli Sheikh, ambaye ni Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa Malapa Kata ya Buguruni na Mwezeshaji wa semina hiyo Edda Kawala, walisema kuna umuhimu wa waajiri kuwaona wafanyakazi wa majumbani kama sehemu ya familia zao.
Sheikh, alisema kutokana na mchango na umuhimu wa wafanyakazi wa ndani ambao ni tegemeo la waajiri katika kusaidiwa kazi za nyumbani ni vema watumishi hao wakapewa heshima na kuthaminiwa kama wanafamilia.
"Wao ndio wanaowapikieni, kuwafulieni na kazi nyingine za ndani, hivyo ni wasiri na watu muhimu katika familia zenu hivyo ni vema kukaa nao kwa wema mkiwajali na kuwathamini tofauti na baadhi yenu mnavyowafanyia," alisema Sheikh.
Naye Mwezeshaji alisema lengo la semina hiyo ni kuona waajiri na wafanyakazi hao wa ndani wanakuwa na mauhisiano mema, pamoja na kila mmoja kuhakikisha wanakuwa na mikataba au makubaliano yanayolinda haki na hadhi ya kila mmoja.
Alisema KIWOHEDE, imebaini zipo baadhi ya nyumba au waajiri wamekuwa wakiwabagua watumishi wao na kuwanyima haki zao stahiki na kuchangia kuwepo kwa uhasama na kuifanya kazi hiyo kudharaulika mbele ya jamii.
Washiriki wa semina hiyo wengi wao wakiwa ni akinamama, walisema kuna mambo mengine hawakuwa wanayajua juu ya haki za msingi za watumishi hao na semina hiyo imewafungua macho na kuahidi kuwa 'mabalozi' mema warejeapo makwao.
Semina hiyo ilielekeza umri stahiki wa wafanyakazi wanaopaswa kuajiriwa kwa kazi za majumbani, haki za msingi stahiki za watumishi hao na namna ya uwajibikaji wa kila mmoja kati ya waajiri na wafanyakazi hao.

Mwisho

No comments:

Post a Comment