STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, March 12, 2011

Kanumba atambia 'The Shock'



MUIGIZAJI Nyota wa Filamu Tanzania, Steven Kanumba, ametamba kuwa kazi yake mpya ya 'The Shock' ambayo ipo kwenye foleni kabla ya kuachiwa mitaani ni 'funika bovu' ya mwaka 2011.
Kanumba, mshindi wa tuzo ya Muigizaji Bora wa Kiume 2010, alisema filamu hiyo iliyoandaliwa na kampuni yake ya Kanumba The Great Films ni moja ya kazi itakayokimbiza kwenye soko la filamu kutokana na namna iliyoandaliwa pamoja na washiriki wake walivyofanya kweli.
Akizungumza na Micharazo, Kanumba, alisema sio kawaida yake kujisifu, ila kazi hiyo ni moja ya kazi nzuri iliyouanza mwaka 2011.
Alisema wakati kazi hiyo ambayo inamuibua muigizaji mpya wa kike nchini Shez Sadry, ikiwa kwenye foleni kabla ya kuingia mitaani, kampuni yake inaendelea na maandalizi ya kazi nyingine.
"Sio siri kama kuna kazi itakayokimbiza mwaka huu, basi ni The Shock, kutokana na jinsi nilivyoiandaa na namna washiriki walivyofanya kazi ya ziada kudhihirisha kuwa fani yetu inazidi kupaa nchini," alisema.
Washiriki wengine waliopo ndani ya filamu hiyo ni mwanamuziki mahiri wa bendi ya FM Academia, Patcho Mwamba na wengine wengi.
Katika hatua nyingine, kampuni ya kusambaza filamu ya Kapico, imeamua kuibeba filamu mpya ya kusisimua ya Bangkok Deal inayohusisha majoka makubwa kama ilivyokuwa 'Anaconda'.
Filamu hiyo iliyoandaliwa na kampuni ya Huba Production, imewashirikisha wasanii wakali kama Charles Magali, Bambucha na wengine, wakati wowote itakuwa hewani kupitia Kapico moja ya wasambazaji wakubwa wa filamua za Kibongo nchini.
Mwisho

Sikinde wavamia ngome ya Msondo

BENDI kongwe ya muziki wa dansi ya Mlimani Park 'Sikinde' imevamia ngome ya wapinzani wao, Msondo Ngoma kwa kuanzisha bonanza linalofanyika kila Jumapili kwenye ukumbi wa TCC Club-Chang'ombe.
Msondo kwa muda mrefu imekuwa ikifanya bonanza kila Jumamosi kwenye klabu hiyo, hivyo kutua kwa Sikinde ni kama kuwachokoza ikiwa ni wiki kadhaa tangu pambano lao kuahirishwa.
Katibu wa bendi ya Sikinde, Hamis Milambo, alisema bendi yao imelianza bonanza hilo tangu wiki iliyopita kwa kutumbuiza kuanzia saa 8 mchana hadi saa 12 kabla ya kumalizia burudani zao kwenye ukumbi wa SUWATA.
Milambo, alisema hilo ni bonanza la pili kwa bendi yao, baada ya kufanya pia bonanza jingine linalifahamika kama Konyagi Bonanza kila Jumamosi kwenye ukumbi wa DDC Kariakoo.
"Tangu wiki iliyopita tumekuwa tukifanya bonanza jipya kwenye ukumbi wa TCC Chang'ombe majira ya saa 8-12 kisha kuendelea na ratiba yetu pale SUWATA kuanzia saa 1-5 usiku," alisema.
Aliongeza kwa leo bendi yao itakamua kwenye bonanza lao la Konyagi ikitambulisha nyimbo zao mpya na zile za zamani zilizoifanya bendi hiyo kuwa Mabingwa wa Muziki Tanzania.
Baadhi ya nyimbo mpya za bendi hiyo ni Tunu ya Huba, Wanawake Wakiwezeshwa, Urithi, sambamba na zile za albamu yao ya Supu Imetiwa Nazi.
Mwisho

Filamu ya ngumi hadharani leo



FILAMU mpya inayozungumzia maisha ya bondia wa zamani na kocha wa sasa wa klabu ya Ashanti, Rajabu Mhamila 'Super D' iitwayo 'Super D:Boxing Coach', inatarajiwa kutolewa rasmi leo.
Filamu hiyo ambayo inahusisha pia mapambano kadhaa ya mabondia nyota duniani, itatolewa rasmi leo katika sherehe maalum itakayofanyika kwenye klabu ya ngumi ya Ashanti inayoadhimisha mwaka mmoja tangu kuanzishwa kwake.
Akizungumza na micharazao, Super D, aliyewahi kuzichezea klabu za Simba, Reli na Amana na kupigana na mabondia kama Mbwana Ally na wengineo, alisema filamu hiyo ni maalum kwa ajili ya kuhamasisha mchezo wa ngumi ambao umeshuka kiwango kwa sasa.
"Pamoja na kusimulia na kuonyesha michezo yangu tangu wakati nikipigana mwaka 1984, pia kuna mapambano ya wakali wa dunia katika mchezo wa ngumi za kulipwa," alisema Super D.
Super D, alisema filamu hiyo itazinduliwa leo na kuachiwa hadharani ili mashabiki wa ngumi na filamu kwa ujumla kuipata na kwenda kuishuhudia uhondo wake.
Aliyataja mapambano yaliyopo ndani ya filamu hiyo kuwa ni, ya Muhammad Ally, Iron Mike Tyson, Manu Pacquiao, Michael Moore, Llyod Mayweather, Oscar de La Hoya na wengineo.
"Kazi yangu itakuwa mitaani kuanzia Machi 12, wakati tukiadhimisha mwaka mmoja tangu Ashanti Boxing ianzishwe mie nikiwa miongoni mwa makocha wake," alisema.
Hiyo itakuwa ni filamu ya pili inayozungumzia mabondia wa zamani na mafunzo ya ngumi, awali bingwa wa dunia, Francis Cheka 'SMG' akifanya hivyo mwaka juzi kwa kutoa filamu kama hiyo ikiwa na jina na Francis Cheka na Historia Yake.

Talent wasubiri kidogo videoni



BENDI ya Talent 'Wazee wa Kuchechemea' imekamilisha kurekodi video ya nyimbo za albamu yao mpya ya 'Subiri Kidogo', huku ikiendelea kuandaa albamu ya pili.
Mkurugenzi wa bendi hiyo, Husseni Jumbe, alisema video ya albamu hiyo imekamilika mapema wiki hii na kwa sasa inafanyiwa uhariri kabla ya kusambazwa sokoni na kwenye vituo vya runinga.
Jumbe, alisema video ya albamu hiyo yenye nyimbo sita imetayarishwa na kampuni moja ya jijini na ina mandhari ya kuvutia ikirekodiwa kwa kiwango cha hali ya juu.
"Tumekamilisha kuiweka kwenye video albamu yetu mpya ya Subiri Kidogo, kwa sasa inahaririwa kabla ya kuanza kusambazwa ili mashabiki wetu wapate uhondo," alisema Jumbe.
Alizitaja nyimbo zilizorekodiwa kwenye video hiyo ni 'Subiri Kidogo', 'Dillema', 'Nyuma ya Pazia', 'Songombingo' na 'Nimeamua Kunyamaza'.
Jumbe alisema video hiyo ikikamilika, tayari bendi yake yenye wanamuziki 10, imeshaanza kuandaa albamu mpya ijayo.
Alisema nyimbo nne kati ya sita za albamu hiyo zimeshakamilika na kuanza kutambulishwa kwenye maonyesho yao ambazo ni pamoja na 'Shoka la Bucha', 'Jipu la Moyo' na 'Kilio cha Swahiba' ambao awali ulipangwa kuwepo kwenye albamu yao ya kwanza.
"Kibao cha Kilio cha Swahiba tuliamua kukiweka kwa ajili ya albamu hii ya pili, ambayo tayari ina nyimbo zingine tatu," alisema Jumbe.
Jumbe, alisema kabla ya Juni, albamu hiyo aliyopanga kuiitwa kwa jina la Shoka la Bucha huenda ikakamilika rasmi.

Riyama Ally: Kisura mkali anayewagusa wengi







AKIIGIZA mwenye majonzi utamuonea huruma kwa jinsi atakavyolia kwa kumwaga machozi kama yupo msibani, akicheza kama mwendawazimu utamsikitikia kwa jinsi atakavyokuwa akila jalalani na kufanya vituko vyote wafanyavyo watu wenye kuugua kichaa.
Wengi hudhani yale anayoyafanya kwenye filamu ni mambo ya kweli kutokana na kucheza uhalisia asilimia 100, kitu kinachomfanya Riyama Ally kuwa mvuto wa pekee katika filamu anazoziigiza.
Mwanadada huyo mmoja wa waigizaji wa kike wakali nchini,alianza kufahamika mwishoni mwa miaka ya 1990 alipokuwa na kundi la Taswira na hasa igizo la Jabari lililokuwa likionyeshwa kwenye kituo cha ITV mwaka 2000.Katika igizo hilo lililokuwa gumzo nchini miaka hiyo, Riyama aliigiza kama mtoto aliyegeuzwa kichaa na mama yake mzazi aliyekosea masharti ya dawa za mganga ili kumdhibiti mumewe, ndilo lilothibitisha kuwa kisura huyo ni mkali.
Miaka mitatu baadae, yaani mwaka 2003 Riyama aliachana na Taswira na kutua kundi la Tamba Art, lililowahi kutamba na filamu kama Nsyuka na kuzidi kuonyesha makali yake.
Akiwa na kundi hilo linalomilikiwa na mganga maarufu wa tiba asilia, Dk Maneno Tamba, Riyama, alishiriki filamu mbalimbali zilizozidi kumjengea jina kutokana na staili yake ya uigizaji kama anayefanya kweli.
Baadhi ya filamu alizofyatua akiwa na kundi hilo ni pamoja na 'Miwani ya Maisha', 'Mzee wa Busara', Fungu la Kukosa na nyinginezo kabla ya kupata bahati ya kushiriki kazi nyingine nje ya kundi hilo.
Filamu kama 'My Darling','Simu ya Kifo', 'Darkness Night', 'Mwana Pango', 'Kolelo','Segito', Fake Promise na nyinginezo ni baadhi ya kazi hizo za nje zilizompaisha mrembo huyo mwenye asili ya mkoa wa Tanga.
Akiwa mmoja wa waigizaji wa kike wanaojiheshimu akiwa hana kashfa yoyote kama mastaa wengine wa aina yake, Riyama mbali na uigizaji, pia ni mtunzi wa filamu na mtayarishaji moja ya kazi yake binafsi ikiwa ni Mwasu iliyofanya vema sokoni kwa kitambo kirefu.
Riyama, mshindi wa tuzo ya Uigizaji Bora ya Risasi 2005-2006, kwa sasa yupo mbioni kuibuka na filamu mpya ya Second Wife, aliyoigiza na Vincent Kigosi 'Ray', Aisha Bui, Colleta Raymond na wengine.
Filamu hiyo inatarajiwa kuachiwa hadharani keshokutwa, ambapo kama kawaida yake, Riyama 'chozi' linamtoka kutokana na kutendwa sivyo ndivyo na 'mumewe' ndani ya filamu hiyo.
Riyama anayependa kusafiri, kupika na kulala anapokuwa nje ya fani yake ya uigizaji, ni shabiki mkubwa wa muziki wa taarab, kundi la Mambo Jambo na pia kusoma vitabu mbalimbali.

Mwisho

Benita: Kimwana aliyekacha 'utawa' aigize







TAMTHILIA ya 'Beyond Our Dreams'iliyokuwa ikirushwa kupitia kituo cha runinga cha NTA miaka ya katikati ya 1996 ndiyo iliyomtangaza Benita Nzeribe, mmoja wa waigizaji nyota wa Nigeria.
Mwaka 1998 alijitumbukiza kwenye fani ya uchezaji filamu na kazi mbili za awali za 'Notorious Virgin' na 'Gold Diggers' zilizomtangaza vema kwenye ulingwengu wa fani hiyo.
Filamu hizo ilitoka mwaka 1999-2000 na tangu hapo ameshiriki kazi mbalimbali zilizomjengea jina katika ukanda wa Nollywood na kufahamika kimataifa.
Mzaliwa huyo wa Jimbo la Anambra aliyewahi kunusurika kufa kwenye ajali ya gari, alisema pamoja na kipaji cha sanaa kuwa cha kuzaliwa, lakini kuvutiwa kwake na waigizaji Liz Benson wa Nigeria, Angeline Jolie na Cameroon Diaz wa Marekani ndiko kulikomtumbukiza huko.
Alisema, hata alipojiunga na Chuo Kikuu cha Abia, lengo lake lilikuwa kusomea masomo ya sanaa, lakini chuo hicho hakikuwa na kozi hizo na hivyo kuchukua masomo ya Lugha ya Kiingereza aliyohitimu kabla ya kuanza kuuza sura kwenye runinga.
Aliongeza kuwa bahati nzuri ni kwamba alipoanza kuigiza wazazi wake hawakumuangusha, ingawa baadhi ya wahitimu wenzake walimshangaa kwa kuichagua kazi hiyo ya uigizaji.
Benita, mtoto wa tatu kati ya wanne wa mfanyabiashara maarufu Mr Nzeribe na mama muuguzi mstaafu, tangu alipoanza kushiriki uigizaji wa filamu amecheza zaidi ya kazi 100 kati ya hizo akishirikiana na wakali kama mkongwe Olu Jacobs, Ejike Asiegbu, Ken Okonkwo, Fred Amata, Juliet Ibe na wengineo.
Moja ya filamu anayojivunia ni ile ya Peace of Mind, aliyocheza kama mke anayenyanyaswa na kupigwa na mumewe, kitu alichodai kimewahi kumtokea katika maisha yake ya kimapenzi.
Mwanadada huyo, ambaye pia ni mwanamitindo na mpambaji, majina yake kamili ni Benita Nnenna Adaeze Nzeribe, aliyezaliwa Uzoakwa, Ihiala, Jimbo la Anambra, elimu yake ya msingi na sekondari aliisoma katika miji ya Aba na Umuahia.
Pia alipitia mafunzo ya kiroho akiwa na lengfo la kuja kuwa mtawa, kabla ya kufuta wazo hilo na kati ya vitu anavyokumbuka katika makuzi yake ni tukio la baba yake kumnunulia gari lake la kwanza akiwa na miaka 14 tu.
"Tukio hili la baba kuninunulia gari nikiwa na miaka 14 siwezi kulisahau maishani mwangu kwani lililonyesha alivyonijali na kunithamini," alinukuliwa.
Kuhusu uigizaji wake wa filamu za kimapenzi, alisema ni jambo la kawaida kulingana na nafasia anayopangiwa na muongozaji wake, ila ni mtu anayejiheshimu na kuithamini kazi yake.
Alipoulizwa kama yupo tayari kuchojoa ili aigize utupu, Benita alisema katu hawezi kufanya upuuzi huo hata kwa kisi gani cha fedha hasa kutokana na hadhi ya familia yake nchini kwao.
Baadhi ya kazi alizoshiriki kisura huyo, mbali na zile zilizomtambulisha Nollywood ni Cross My Heart, Cross & Tinapa,Endless Madness,Tears of a Saint, Treasure Hunt,Breath Again,Buried Emotion,Enemies in Love, Games Men Play, Girls Cot,King of the Town na Life Abroad.
Pia ameshiriki Peace Talk, The Final Days, Christian Girls, Fools in Love, Hold Me Down, Paradise to Hell, Secret Affairs, The Scorpion, Under Arrest, Beyond Reason, My Desire,Stand by Me, A Night to Remember, Arrows, Great Change, Lagos Babes, Mission to Africa, Saved by Grace, Street Life, The One I Trust, Agony of a Mother, Fire on the Mountain na kadhalika.

Tuesday, March 8, 2011

Msamba 'ajitoa' Villa Squad *Ni baada ya kuirejesha Ligi Kuu

KOCHA aliyeipandisha daraja klabu ya Villa Squad hadi Ligi Kuu Tanzania Bara, Abdallah Msamba, ametangaza 'kuitema' timu hiyo akiutaka uongozi usake kocha mwingine wa kuiongoza kwenye ligi hiyo msimu wa 2011-2012.
Akizungumza na Micharazo, Msamba, alisema baada ya kutimiza jukumu la kuirejesha Ligi Kuu, Villa Squad anaona ni vema kupisha kocha mwingine wa kuendelea kuinoa timu hiyo katika ligi hiyo msimu ujao.
Msamba, alisema kujiondoa kwake kuinoa timu hiyo haina maana kuwa kajitoa kabisa Villa Squad, ila alisema kwa hadhi ya ligi ilivyo inapaswa timu iwe na mtu mwingine kukabiliana na mshikemshike wake.
"Nimeashautaarifu uongozi utafute kocha mwingine wa kuiandaa timu kwa ligi kuu ijayo, mie naishia hapa baada ya kuipandisha daraja, ila nitakuwa kocha msaidizi au mshauri kwa lengo la kuona Villa inafanya vema," alisema.
Winga huyo wa zamani wa Sigara, Simba na Kajumulo World Soccer, alisema ili kuweza kufanya vema kwenye ligi hiyo, Villa inahitaji kufanya marekebisho kidogo katika kikosi chake, chini ya kocha mwenye hadhi stahiki.
Alisema ana imani kama marekebisho hayo yatafanyika mapema na timu kuandaliwa mapema ikipata michezo mingi ya kujipima nguvu inaweza kutisha katika ligi hiyo iliyowahi kuicheza kabla ya kushuka msimu wa 2008-2009.
Villa Squad ni miongoni mwa timu nne zilizopanda Ligi Kuu msimu ujao baada ya kufanya vema kwenye Ligi Daraja la Kwanza iliyochezwa mjini Tanga.
Timu zingine zilizoungana na klabu hiyo yenye maskani yake Magomeni Mapipa ni JKT Oljoro waliokuwa mabingwa wa ligi hiyo ya daraja la kwanza, Coasta Union na Moro United zinazorejea tena kwenye Ligi Kuu ya Tanzania.

Mwisho

Mtambo wa Gongo, kuzigonga na Cobra Machi 12

BONDIA mkongwe wa ngumi za kulipwa nchini, Maneno Osward 'Mtambo wa Gongo' anatarajiwa kuvaana na Robert Mrossy 'Cobra' katika pambano la Middleweight, litakalofanyika Machi 20 mwaka huu.
Osward mwenye miaka 41 atapigana na Cobra katika pambano lililoandaliwa na Rais wa Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBO, Yassin Abdalla 'Ustaadh' litafanyika kwenye ukumbi wa Amana Club, Ilala jijini Dar.
Ustaadh aliiambia Micharazo kuwa, pambano hilo lisilo la ubingwa la raundi 12 ni maalum kwa ajili ya kupima viwango vya mabondia husika, pia kutoa fursa kwa mabondia wa mikoani kujitangaza kwenye mchezo huo.
Rais huyo wa TPBO, alisema Cobra ni bondia kutoka Arusha na hivyo kupata fursa ya kupigana na mkongwe Osward, kutampa nafasi ya kujitangaza katiuka mchezo huo.
Ustaadh alisema awali pambano hilo lilipangwa kufanyika Jumapili ijayo, ila kutokana na kuahirishwa kwa lingine la ngumi hizo za kulipwa kati ya Ashraf Suleiman na Awadh Tamim kutoka Machi 5 hadi Machi 12 imewafanya walisogeze mbele hadi Machi 20.
"Tumeona isingekuwa vema pambano letu lifanyika kama tulivyopanga Machi 13, wakati siku moja kungekuwa na pigano jingine la Ashraf na Tamim ambalo awali lilipangwa kufanyika Machi 5, lakini likasogezwa hadi Machi 12," alisema Rais huyo wa TPBO.

Kaseba, Maugo kutambulishwa rasmi leo

MABONDIA Mada Maugo na Japhet Kaseba wanaotarajiwa kupigana Aprili 16, pamoja na watakaowasindikiza pambano hilo wanatarajiwa kutambulishwa rasmi leo mbele ya waandishi wa habari.
Mratibu wa pambano hilo, Kaike Siraju aliiambia Micharazo jana kuwa leo watafanya mkutano na vyombo vya habari kulitambulisha rasmi pambano hilo ambalo litafanyika kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es Salaam.
"Nitawatambulisha rasmi mabondia wote watakaopigana Aprili 16 katika mkutano na vyombo vya habari utakaofanyika kesho (leo) kwenye ukumbi wa Habari-Maelezo majira ya saa 5," alisema Siraju.
Alisema katika mkutano huo, Maugo na Kaseba kila mmoja atapata fursa ya kuongea machache kuhusiana na pambano lao hilo la raundi nane uzito wa kilo 72 litakalokuwa la kusaka mkali baina yao wa kuzipiga na Francis Cheka.
Ingawa Siraju amekuwa akificha majina ya mabondia watakaoshindikiza pambano hilo, lakini uchunguzi wa Micharazo umebaini kuwa nahodha wa zamani wa timu ya taifa ya ngumi ya ridhaa, Joseph Martin ni miongoni mwao.
Martin aliyeachana na ngumi za ridhaa na kuingia za kulipwa atapigana na Sweet Kalulu, pia Francis Miyeyusho na Afande Juma nao watakuwepo katika usindikizaji.
Kwa mujibu wa Siraju, mgeni rasmi wa pambano hilo anatarajiwa kuwa Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova ambaye atamualika IGP Said Mwema kuhudhuria kwenye ngumi hizo.

Friday, March 4, 2011

Mwanza yaenguliwa Tamasha la Pasaka

MKOA wa Mwanza uliokuwa kwenye ratiba ya Tamasha la Pasaka, umeenguliwa na kufanya kwa sasa isalie mikoa mitatu tu itakayoshuhudia maonyesho hayo ya muziki wa Injili.
Mwenyekiti wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha hilo, Alex Msama, alisema mikoa iliyosalia katika maonyesho hayo ni Dar es Salaam, Dodoma na Shinyanga.
Mkurugenzi Mtendaji huyo wa Msama Promotions, alisema onyesho la kwanza la tamasha hilo litafanyika jijini Dar es Salaam siku ya April 24 kisha siku inayofuata litafanyikia mjini Dodoma kisha kumalizika Shinyanga Aprili 26.
Msama alisema onyesho la jiji la Mwanza limefutwa kutokana na sababu zilizo nje ya uwezo wao na kuwaomba radhi mashabiki wa muziki wa Injili kwa jambo lililotokea.
"Kwa sababu zilizo nje ya uwezo wetu, tumefuta onyesho la jijini Mwanza na tunatanguliza kuomba radhi kwa lililotokea ambalo lilikuwa nje ya uwezo wetu, ila tunawahidi wale wa mikoa mingine watarajie burudani kabambe," alisema Msama.
Msama alisema onyesho la jijini litakalofanyika siku ya Sikukuu ya Pasaka litafanyikia kwenye ukumbi wa Diamond Jubilee ambapo waimbaji nhyota wa muziki huo akiwemo Upendo Nkone na waimbaji toka mataifa mbalimbali ya Kiafrika watakuwepo ukumbini kutumbuiza.
"Onyesho la Dar na mengineyo yatapambwa na waimbaji nyota wa Tanzania na nchi jirani kama za Kenya, Uganda, Rwanda, DR Congo, Afrika Kusini na Zambia, lengo likiwa ni kukusanya fedha za kuwasaidia yatima na wajane," alisema Msama.
Aliongeza mbali na fedha hizo kuwanufaisha yatima na wajane kwa nia ya kujikumu na kupata mitaji ya kujiendeshea shughuli za biashara, pia sehemu ya mapato ya maonyesho hayo yatatolewa kwa waathirika wa mabomu yaliyotokea katika kambi ya jeshi Gongo la Mboto.
"Sehemu ya fedha zitakazopatikana kwenye maoanyesho hayo itatolewa kama pole kwa waathirika wa Mabomu ya Gongo la Mboto kama nilivyoahidi awali," alisema Msama.
Tamasha la Pasaka limekuwa likifanyika kila mwaka zaidi ya mwaka wa tatu sasa, ambapo waimbaji na makundi mbalimbali ya muziki wa Injili wa ndani ya nje hujumuika pamoja kutumbuiza sambamba na kuhamasisha upatikanaji wa fedha za kuwasaidia wenye matatizo nchini.

Jokha Kassim akwama kushebeduka

MWIMBAJI nyota wa muziki wa taarab, Jokha Kassim, amesema bado anaendelea kuhangaikia uzinduzi wa albamu yake binafsi ya 'Wacha Nijishebedue' iliyokwamba kuzinduliwa mwaka jana.
Uzinduzi wa albamu hiyo ulikwama katikati ya mwaka jana kutokana na sababu mbalimbali kubwa kukosa wafadhili na wadhamini wa kumpiga tafu.
Jokha, alisema bado hajakata tamaa kwa vile anaendelea kuwasiliana na wafadhili ili kufanikisha uzinduzi huo ndani ya mwaka huu.
"Najipanga kufanikisha uzinduzi wangu ndani ya mwaka huu, naamini Mungu atanisaidia nipata wadhamini wa kunipiga tafu," alisema.
Mwimbaji huyo alizitaja nyimbo zinazounda albamu yake hiyo 'Yamekushinda', 'Meseji za Nini', 'Kinyang'anyiro Hukiwezi', 'Kelele za Mlango' na Wacha Nijishebedue' uliobeba jina la albamu.
"Niliporekodi na kushuti video ya nyimbo zangu nilipata mfadhili na sasa anatafuta wengine watakaonisaidia kwenye uzinduzi wa albamu yangu, hivyo mashabiki wangu wajue kuwa bado ninahangaikia fedha," alisema.
Alisema, baadhi ya nyimbo zake ukiwemo uliobeba jina la albamu zimekuwa zikisikika kwenye vitu mbalimbali vya redio na televisheni na kumpa matumaini kwamba huenda akapata soko atapozindua.

Mtenda Akitendewa videoni

WIMBO mpya wa bendi ya Extra Bongo unatarajiwa kutambulishwa rasmi leo kwa mashabiki sambamba na vibao vingine na wanamuziki wapya uitwao, Mtenda Akitendewa umefyatuliwa video yake.
Video ya kibao hicho ambacho awali lilipangwa kufahamika kama 'Under 18' kimefyatuliwa na wanamuziki wa bendi hiyo wakiwa kambini kupitia kampuni ya Sophia Records ya jijini Dar es Salaam na utaanza kuonekana hewani wakati wowote kuanzia sasa.
Mkurugenzi wa Extra Bongo, Ally Choki 'Kamarade' aliiambia micharazo kuwa, waliamua kurekodi video ya wimbo huo wakiwa kambini kama njia ya kuwapa burudani mashabiki wao kuwaonyesha hawakuwa bure kambini bali walikuwa wakiwaandalia mambo mapya.
"Pamoja na kuandaa kazi mpya, lakini pia tumefyatua video ya moja ya vibao hivyo kiitwacho Mtenda Akitendewa ambacho kitaanza kuonekana wakati wowote,tumeshasambaza, kibao hicho na vingine pamoja na wanamuziki wapya tutawatambulisha rasmi Ijumaa (leo)," alisema.
Choki alisema onyesho la utambulisho kwa bendi yao utafanyika kwenye ukumbi wa New Msasani Club, ambapo kesho litafuatiwa na onyesho jingine TCC-Chang'ombe na kabla ya Jumapili kutambulishwa Mango Garden na kwenda kuvunja kambi yao ili kujiandaa kwenda Zanzibar.
Mtunzi na muimbaji huyo alizitaja nyimbo nyingine zitakazotambulishwa sambana na wanamuziki sita waliowanyakua wakienda kambini kutoka Twanga Pepeta ni Neema, Nguvu na Akili na Fisadi wa Mapenzi vinavyoandaliwa kwa ajili ya albamu mpya na ya pili.
Wanamuziki watakaotambulishwa kwenye maonyesho hayo ya mwishoni mwa wiki ni mtunzi na muimbaji nyota nchini, Rogert Hegga 'Caterpillar', Rapa Saulo John 'Ferguson', mpiga besi, Hoseah Mgohachi na wanenguaji Hassani Mohammed 'Super Nyamwela', Isaac Burhan 'Super Danger' na Otilia Boniface waliotoka African Stars 'Twanga Pepeta'.

Thursday, March 3, 2011

Maugo atamba atatumia siku 16 kumchapa Kaseba




WAKATI Japhet Kaseba akiwa ameshaanza mazoezi kujiandaa na pambano lao itakalochezwa mwezi ujao, bondia Mada Maugo, amesema hana haraka ya kufanya hivyo badala yake ataanza rasmi April Mosi, akidai siku 16 zitamtosha kujiandaa kumchakaza mpinzani wake huyo.
Kaseba na Maugo watapigana kwenye pambano maalum la 'Nani Zaidi' litakalofanyika April 16, kwenye ukumbi wa PTA, Dar es Salaam kwa ajili ya kusaka mshindi atakayepigana na bingwa wa dunia, Francis Cheka.
Kaseba ameshatangaza ameshaanza maandalizi ili kujiweka sawa kumpiga Maugo, ambaye kama yeye ameshawahi kujeruhiwa na Cheka siku za nyuma, lakini Maugo akizungumza na Micharazo alisema yeye bado hajaanza.
Maugo alisema yeye bao yupo yupo kwa sasa na ataanza rasmi April Mosi na kutumia siku 16 kabla ya kuvaana na Kaseba kujiweka fiti na kutamba siku hizo zinatosha kumchakaza bingwa huko wa dunia wa Kick Boxing.
"Sijaanza na wala sitarajii kuanza kwa sasa kwa vile pambano lenyewe ni jepesi sana kwangu, nitatumia siku 16 kabla ya pambano hilo kuanza mazoezi na nina uhakika wa kumchakaza Kaseba bila tatizo," alisema Maugo.
Maugo alisema pamoja na kwamba mpinzani wake kuanza kujinadi kuwa atampiga, yeye hataki kupiga domo na badala yake kuwaomba mashabiki wa ngumi kujitokeza ukumbini siku ya April 16 kushuhudia ukweli huo.
"Sitaki kujibishana maneno na Kaseba, sio kawaida yangu, mie ni mtu wa vitendo zaidi na hivyo nawasihi mashabiki waje ukumbi kuona kama Kaseba atamaliza raundi nane la pambano hilo ni hayo tu," alisema Maugo.
Mabondia hao wenye majina makubwa nchini watapambana katika pambano la raundi nane la uzani wa Kilo 72 lililoandaliwa na mratibu Kaike Siraju kupitia kampuni ya Kaike Promotion chini ya usimamizi wa Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBO.

Mwisho

Nyilawila awafunika Cheka, Maugo



BINGWA wa Dunia wa Ngumi za Kulipwa anayeshikilia taji la WBF, Karama Nyalawila, ndiye Mtanzania anayeongoza kwa ubora miongoni mwa mabondia wa uzani wa Middle akiwafunika wakali kama Francis Cheka na Mada Maugo.
Kwa mujibu wa takwimu za ubora wa mabondia wa uzani huo duniani, kupitia mtandao wa Box Rec, Nyalawila anashikilia nafasi ya 74, wakati Cheka, Bingwa wa Dunia wa UBO, ICB na WBC yupo nafasi ya 142.
Maugo yeye anashika nafasi ya 196 akimzidi wakongwe Rashid Matumla 'Snake Man' na Maneno Osward 'Mtambo wa Gongo' wanashika nafasi ya 327 na 370.
Nyalawila aliyetwaa taji hilo Desemba 3 mwaka jana huko Jamhuri ya Czech, ni miongoni mwa mabondia wanne wa kiafrika waliopo kwenye orodha wa mabondia 100 Bora Duniani wa uzani huo wa Middle.
Wengine waliopo kwenye orodha hiyo ni Mganda, Kassim Ouma anayeshika nafasi ya 32 akiwa ndiye kinara kwa mabondia wa Kiafrika, Assie Duran na Osumanu Adama wa Ghana waliopo nafasi ya 34 na 35 na Mnigeria, Eromosele Albert aliyepo anayeshikilia nafasi ya 38.
Bondia anayeongoza kwenye orodha ya wapiganaji wa uzani huo ni Sergio Gabriel Martinez wa Argentina anayefuatiwa na Felix Sturm wa Ujerumani na anmayeshikilia nafasi ya tatu duniani ni Danile Geale wa Australia.
Mabondia wa Kitanzania wanatengeneza 10 Bora yao wakiwafuata Nyalawila na Cheka ni, Mada Maugo (196), Thomas Mashali (212), George Dimoso (289), Maisha Samson (302), Rashid Matumla (327), Bagaza Mwambene (342), Stan Kessy (350) na Maneno Oswald 'Mtando wa Gongo' akiishika nafasi ya 370.

Kanumba ana 'shock', Ray atamba





BAADA ya kuanza mwaka na filamu ya 'Deception', muigizaji nyota wa filamu nchini, Steven Kanumba 'The Great' ameibuka na filamu mpya iitwayo 'The Shock'.
Filamu hiyo ambayo imekamilika hivi karibuni na sasa ipo katika maandalizi ya kuachiwa mitaani, ni ya pili kwa msanii huyo kwa mwaka huu wa 2011.
Akizungumza na Micharazo, Kanumba alisema kama ulivyo utaratibu wake wa kuibua wasanii wapya katika fani hiyo, ndani ya 'The Shock' amemtambulisha muigizaji mpya mwanadada mrembo Shez Sadry ambaye amedai amefanya mambo makubwa kama mzoefu.
Kanumba alisema mbali na mwanadada huyo ambaye ndiye mhusika mkuu, pia kuna kuna muimbaji wa FM Academia Patcho Mwamba, Ben Braco, yeye mwenyewe na wengineo.
"Baada ya Deception sasa The Shock inakuja ambayo na kifaa kipya lakini kikali katika muigizaji, Shaz Sadry," alisema Kanumba.
Alisema filamu hiyo inatarajiwa kuachiwa mitaani ndani ya mwezi huu na itasambazwa na kampuni ya Steps Entertainment.
Katika hatua nyingine, mpinzani mkubwa wa Kanumba, Vincent Kigosi 'Ray' amesema filamu yake mpya ya 'Second Wife' inatarajiwa kuingia mitaani wiki ijayo na kuwataka mashabiki wa fani hiyo kukaa mkao wa kula kupata uhondo.
Katika filamu hiyo mpya, Ray ameigiza na wakali kama Riyama Ally, Coleta Raymond, Aisha Bui, muigizaji mpya mwanadada Skyner Ally na mtoto Aisha.
Ray amesema filamu hiyo ni 'funika bovu' kutokana na jinsi alivyoigiza kwa kushirikiana na wenzake na kusisitiza kuwa, hizo ni salamu kwa wapinzani wao kuwa RJ Production imekuja kivingine ndani ya mwaka 2011.

Madee asikitika Dogo Janja kuzinguliwa shuleni

MSANII nyota wa muziki wa kizazi kipya, Hamad Ally 'Madee' amedai kusikitishwa na kitendo ambacho amekuwa akifanyiwa msanii chipukizi anayemfadhili, Abdul-Aziz Chende 'Dogo Janja' na mmoja wa walimu wa Shule ya Sekondari ya Makongo anayosoma kwa sasa.
Akizungumza na Micharazo, Madee alisema kuwa, amesikitishwa na taarifa kwamba mmoja wa walimu wa shule hiyo amekuwa akimpa wakati mgumu Dogo Janja, jambo analohofia linaweza kushuka kiwango chake cha elimu darasani.
Hata hivyo Madee alisema tayari suala la mwalimu huyo ambaye hakumtaja jina, limeshafikishwa kwa mkuu wa shule hiyo, na Dogo Janja anaendelea kusoma kwa vile hana mpango wa kuhama.
"Kwa walimu wa namna hii wanaharibu viwango vya wanafunzi darasani, ila nashukuru mambo yameshamalizwa kwa Dogo kwenda kwa Mkuu na kulalamika na ticha huyo kuonywa," alisema.
Aliongeza ni vema walimu wakatambua kuwa wao ni walezi kwa wanafunzi na hivyo waishi
kama watoto wao na wanapokosea wawaelekeze hata kama kwa bakora, lakini wakizingatia
miiko na taaluma zao za kazi.
Dogo Janja, alinukuliwa na kituo kimoja akisema kuwa alikung'utwa na mwalimu wake huyo baada ya kutofautiana nae kiswahili, huku akidai mara kwa mara amekuwa akimzingua akimuita 'Dogo Jinga' badala ya jina lake la Dogo Janja, kitu kilichokuwa kikimnyima raha shuleni.
Madee, aliamua kumsaidia Dogo Janja mwenyeji wa Arusha kutokanan na kuvutiwa na kipaji chake na tayari ameshamkamilishia albamu mpya iitwayo Ngarenaro, akiwa pia ndiye anayemlipia ada shuleni hapo akijiandaa kumfyatulia video ya albamu hiyo yenye nyimbo 10.

Mtenda Akitendewa ya Extra Bongo videoni



WIMBO mpya wa bendi ya Extra Bongo unaotarajiwa kutambulishwa rasmi leo kwa mashabiki sambamba na vibao vingine na wanamuziki wapya uitwao, Mtenda Akitendewa umefyatuliwa video yake.
Video ya kibao hicho ambacho awali lilipangwa kufahamika kama 'Under 18' kimefyatuliwa na wanamuziki wa bendi hiyo wakiwa kambini kupitia kampuni ya Sophia Records ya jijini Dar es Salaam na utaanza kuonekana hewani wakati wowote kuanzia sasa.
Mkurugenzi wa Extra Bongo, Ally Choki 'Kamarade' aliiambia Micharazo kuwa, waliamua
kurekodi video ya wimbo huo wakiwa kambini kama njia ya kuwapa burudani mashabiki wao kuwaonyesha hawakuwa bure kambini bali walikuwa wakiwaandalia mambo mapya.
"Pamoja na kuandaa kazi mpya, lakini pia tumefyatua video ya moja ya vibao hivyo kiitwacho Mtenda Akitendewa ambacho kitaanza kuonekana wakati wowote,tumeshasambaza, kibao hicho na vingine pamoja na wanamuziki wapya tutawatambulisha rasmi Ijumaa," alisema.
Choki alisema onyesho la utambulisho kwa bendi yao litafanyika leo kwenye ukumbi wa New Msasani Club kabla ya kufuatiwa na maonyesho mawili ya TTC Chang'ombe litakalofanyika Jumamosi kisha Jumapili pale Mango Garden kabla ya kujiandaa kwenda Zanzibar.
Mtunzi na muimbaji huyo alizitaja nyimbo nyingine zitakazotambulishwa sambana na
wanamuziki sita waliowanyakua wakienda kambini kutoka Twanga Pepeta ni Neema, Nguvu
na Akili na Fisadi wa Mapenzi vinavyoandaliwa kwa ajili ya albamu mpya na ya pili.
Alipoulizwa kama kibao hicho ni 'dongo' mahasimu wao, African Stars 'Twanga Pepeta', Choki alisema sio kweli kibao cha Mtenda Akitendewa ni kijembe, ila alisema kama kuna mtu atakayeguswa nao na kulalamika ujue ndiye mhusika.
"Staili yetu ni kama ile ya zamani ya kurusha jiwe kwenye kiza, atakasema mmh, hujue limempata, ila sio kweli kama nimetunga mahususi kwa ajili ya mtu yeyote," alisema Choki.
Mkurugenzi huyo aliwataja wanamuziki watakaotambulishwa kwenye maonyesho hayo ya mwishoni mwa wiki ni mtunzi na muimbaji nyota nchini, Rogert Hegga 'Caterpillar', Rapa Saulo John 'Ferguson', mpiga besi, Hoseah Mgohachi na wanenguaji Hassani Mohammed 'Super Nyamwela', Isaac Burhan 'Super Danger' na Otilia Boniface waliotoka African Stars 'Twanga Pepeta'.

Akudo Impact yanyakua wanenguaji wapya





BENDI ya Akudo Impact imeongeza nguvu kwenye safu ya ushambuliaji wa jukwaa baada ya
kuwanasa wanenguaji watatu kutoka Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo.
Kwa mujibu wa meneja wa bendi hiyo George Kyatika, wanenguaji hao ni Mariam Sangwa,
Francine Bozi na Mary Sheli ambao tayari wameshatambulishwa kwenye maonyesho mbalimbali ya Akudo.
Meneja huyo alisema ujio wa wanenguaji hao unaifanya Akudo kuwa na jumla ya madansa sita wengine wakiwa ni Fanny Bosawa, Raissa Sangwa na Nadine Issala.
"Tumeongeza wanenguaji wakati huu ambao tuko kwenye maandalizi ya uzinduzi wa albamu
yetu ya History no Change ambayo itazinduliwa mwezi wa ujao," alisema Kyatika.
Alisema kuwa awali safu yao ya ushambuliaji wa jukwaa ilikuwa inapwaya hasa baada kupunguza baadhi ya wanenguaji ambao makali yao ya kufanya kazi yalikuwa yamepungua lakini sasa wamepata wapya.
Kyatika alizitaja baadhi ya nyimbo za albamu hiyo wanayojiandaa kuzindua kuwa ni 'Ubinafsi', 'Umefulia', 'Pongezi kwa Wanandoa' na 'Umejificha Wapi'.
Aliongeza kusema kuwa sasa Akudo imejipanga upya kuanzia kwenye uongozi wa bendi na
hivyo ana uhakika itaendelea kufanya vizuri kwa kuwaburudisha mashabiki na wapenzi wake.
Akudo imekuwa ikitamba na albamu yake ya kwanza ya Impact ambayo ilichangia kuipandisha chati bendi hiyo inayojiita Vijana wa Masauri ikiwa chini ya rais wake Christian Bella.

Wednesday, March 2, 2011

PAMBANO LA WATANI J'MOSI Furaha kubwa inasubiriwa *Ni Msimbazi au Jangwani?

VIGOGO wa soka nchini Simba na Yanga zinakutana Jumamosi katika 'big match' ya pekee kwa aina yake msimu huu wa Ligi Kuu ya Vodacom, huku Wekundu wa Msimbazi wakipania kulipa kisasi cha kufungwa katika mechi ya kwanza, na Yanga wakitamba kuendeleza ubabe.
Pambano hili la marudiano baada ya lile kwanza mwishoni mwa mwaka jana kwenye uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza na Simba kuloa bao 1-0, linafanyika kwenye uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Vita ya mechi hii ambayo tayari imeteka hisia za mashabiki wengi wa soka inatokana na namna timu hizo zinavyopokezana kukalia kiti cha uongozi wa ligi hiyo pamoja na Azam FC.
Kigogo kitakachoshinda katika mechi hiyo, kitakuwa kimejiweka kwenye mazingira mazuri ya kutwaa ubingwa wa soka ambao kwa sasa uko mikononi mwa Simba.
Yanga ndio inayoongoza ligi hiyo kufuatia ushindi wake wa bao 1-0 dhidi ya Ruvu Shooting na kuiengua Simba waliokuwa kileleni kwa masaa tangu walipoichabanga Mtibwa Sugar mabao 4-1.
Jerry Tegete ndiye aliyekuwa shujaa kwa kufunga bao zuri wakati Simba ikilala 1-0 kwenye mechi ya kwanza, na amepania kurejesha tena huzuni kwa Simba kwenye mechi ya kesho.
Hata hivyo Yanga pia watashuka uwanjani kesho wakiwa na machungu ya kipigo cha mabao 2-0 ilichopewa na watani zao hao katika pambano la fainali la Kombe la Mapinduzi mapema mwaka huu visiwani Zanzibar.
Kipigo hicho hakikuonekana kuwauma sana Yanga, kwani walijitetea kwa kusema wachezaji wake wengi walikuwa na timu ya taifa iliyokuwa ikishiriki michuano ya Mto Nile nchini Misri.
Simba itashuka dimbani ikitokea chimbo lake la kawaida mjini Zanzibar, na Yanga wakiingia kusaka pointi mbili wakitoka Bagamoyo.
Simba kupitia nyota wake kadhaa kama Juma Jabu, Rashid Gumbo na Mohammed Banka wamesema hawana hofu ya pambano hilo.
Wamesema wamejiandaa kushinda mechi hiyo, na hakuna shaka matarajio yao yatatimia ili iwe sehemu nzuri ya maandalizi dhidi ya pambano lao la Klabu bingwa dhidi ya Mazembe.
"Hatuna hofu na Yanga, tutawafunga ili tukienda Lubumbashi kuvaana na TP Mazembe tukiwa na ari ya ushindi kama tunavyowakabili Yanga kufuatia kuilaza Mtibwa mabao 4-1," alisema Banka.
Hata hivyo Yanga kupitia Afisa Habari wao, Louis Sendeu alisema wachezaji wake watacheza kufa na kupona na kuifunga Simba ili kujiweka kwenye mazingira mazuri ya kutwaa ubingwa.
"Kama tulivyofanya Mwanza ndivyo tutakavyorejea tena Jumamosi, timu ipo katika hali nzuri na tuna uhakika wa kuilaza tena Simba," alisema Sendeu.
Kama Yanga itashinda itazidi kujikita kileleni, lakini kama itakubali kipigo kwa watani zao maana yake wataporomoka na kuwapisha Simba warejee kileleni.
Timu hizo zinakutana Yanga ikiwa na kocha mpya, Sam Timbe kutoka Uganda, huku ikiwa na wachezaji wawili wapya ambao kwenye fainali za Kombe la Mapinduzi hawakuonyesha makali yoyote nao ni Davies Mwape na Juma Seif 'Kijiko'.
Simba kwa upande wao, itashuka dimbani ikiwa na mshambuliaji mwenye uchu Mbwana Samatta na Ally Ahmed 'Shiboli' ambao katika mechi ya Mwanza hawakuwepo.
Nani atakayeibuka na ushindi katika pambano la kesho na kuzima ngebe za wenzake? Bila shaka ni suala la kusubiri dakika 90 za mchezo huo.

INAFRIKA WAREJEA NA MBELEKO TOKA ULAYA




BAADA ya ziara ya miezi miwili na nusu ya maonyesho ya burudani katika nchi mbalimbali za Ulaya, bendi ya InAfrika imerejea nchini, ikijinadi kuwa, ziara yao ilikuwa ya mafanikio makubwa.
Bendi hiyo iliwasili jana majira ya saa 4 asubuhi, kupitia mmoja wa viongozi
na wanamuziki wake, Bob Rudala imesema itatumia siku chache kupumzika
kabla ya kuanza kuitambulisha albamu yao mpya mikoani.
Akizungumza na Micharazo mara baada ya kuwasili kwenye uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam, alisema albamu hiyo ya pili kwao baada ya ile ya 'Indege', inaitwa 'Mbeleko'.
Rudala aliyewahi kutamba na nyimbo binafsi kama 'Nimekuchagua Wewe', alisema albamu hiyo ina nyimbo 10 zilizopigwa katika miondoko mbalimbali ya ngoma asilia za Tanzania.
Rudala alisema utambulisho wa albamu hiyo utaanzia mkoa wa Arusha wiki ijayo, kabla ya uongozi wa bendi hiyo kupanga mahali pengine pa kufanya hivyo.
Kuhusu ziara hiyo, Rudala alisema ilikuwa ya mafanikio makubwa na kwamba watatumia utambulisho wa albamu hiyo kuudhibitishia umma wa Tanzania kuwa walienda kujifunza mambo mengi kuendeleza muziki nchini.
"Tunashukuru tumerejea salama, ila kwa kifupi tumefarijika na mafanikio makubwa tuliyopata katika ziara hiyo na tunapumzika kwa siku kadhaa kabla ya kabla ya kuanza kuitambulisha albamu yetu ya Mbeleko," alisema.
Alizitaja baadhi ya nyimbo zilizopo kwenye albamu hiyo kuwa ni Mbeleko, Hatushangai, Jamila, Kitchen Party, Mimi Muafrika, Amina, Jua Limetua na kadhalika.
Aliongeza kuwa ziara yao waliyoifanya kuanzia Desemba mwaka jana, ilihusisha nchi tano za Uholanzi, Ujerumani, Uswisi, Austria na Romania ambapo mbali na bendi, pia InAfrika iliambatana na kikundi chao cha wanenguaji na wacheza sarakasi.
InAfrika ilianzishwa mwaka 1992 ikiwa na albamu ya kwanza ya 'Indege' ambayo pia hufahamika kama 'Omunwa'ambayo ilisaidia kuipandisha chati kwa nyimbo zake mchanganyiko zikiwemo zenye miondoko ya asili.