STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, March 2, 2014

TASWA yapata viongozi wapya, Pinto, Mgosi warudi, FK aula


Baadhi ya wajumbe wa TASWA wakipiga kura kuwachagua viongozi mbalimbali wa kukiongoza chama hicho. Mroki Mroki FK, Mwani Nyangasa na Amiri Mhando ni miongoni mwa wateule wapya.
Safu mpya ya Viongozi wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA) waliochaguliwa hii leo.
***
JUMA Abbas Pinto amefanikiwa kutetea nafasi yake ya Uenyekiti wa Chama cha Waandishi wa Habari za Michezo Tanzania (TASWA)  baada ya mpinzani wake George John Ishabairu kujitoa katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika leo kwenye ukumbi wa NSSF Water Front, Dar es Salaam. 

George alitangaza kujitoa baada ya kufika ukumbini, akisema kwamba Mwajiri wake, Wizara ya Maji amemwambia ajitoe. 
Pinto alipata kura 82 wakati 13 zilimkataa, na Egbert Mkoko ameshinda nafasi ya Makamu Mwenyekiti kwa kura 67 dhidi ya 32 za Mohammed Omary Masenga.

Akitangaza matokeo ya uchaguzi huo, Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi, Boniface Wambura Mgoyo alimtaja Amir Mhando kushinda tena nafasi ya Ukatibu Mkuu baada ya kupata kura 93. Mhando hakuwa na mpinzani na kura mbili tu zilimkataa.

Nafasi ya Katibu Msaidizi imekwenda kwa Grace Aloyce Hoka aliyepata kura 65 dhidi ya 31 za Alfred Lucas Mapunda.
  Mweka Hazina Msaidizi Zena Suleiman Chande amepata kura 55 dhidi ya 40 za Elius John Kambili, Mweka Hazina Shija Richard Shija amepata kura 57 dhidi ya 38 za Mohamed Salim Mkangara.

Walioshinda nafasi za Ujumbe ni Ibrahim Mkomwa Bakari, Mroki Timothy Mroki 'Father Kidevu', Mussa Juma, Mwani Omary Nyangassa, Rehure Richard Nyaulawa na Urick Chacha Maginga.
FK

Spurs, Aston Villa zashinda England

Roberto Soldado
Wachezaji wa Spurs wakipongezana baada ya kupata bao pekee dhidi ya Cardiff  City

Leandro Bacuna
TOTTENHAM Hotspur muda mfupi uliopita imepata ushindi kiduchu nyumbani dhidi ya Cardiff City, huku Aston Villa kupata ushindi wa kishindo nyumbani kwa kuifumua Norwich City kwa kuilaza mabao 4-1 katika mfululizo wa Ligi Kuu ya England.
Roberto Saldado aliifungia Spurs bao pekee katika dakika ya 28 baada ya kutengenezewa pande zuri na Emmanuel Adebayor na kuifanya Spurs kujiimarisha kwenye nafasi ya tano ikiwa na pointi 53.
Aston Villa ikiwa uwanja wake wa nyumbani iliifumua Norwich City kwa mabao 4-1, ambapo wageni walitangulia kupata bao dakika ya tatu tu ya mchezo iliyofungwa na Hoolahan kabla ya Christian Benteke akiisawazishia bao dakika ya 25 na kuongeza jingine dakika moja baadaye na Bacuna aliionheza bao la tatu na Sebastian Bassong alijifunga bao katika dakika ya 41 na kuifanya wenyeji kupata ushindi huo mnono.
Katika mechi nyingine, Swansea City ilishindwa kutamba nyumbani baada ya kulazimishwa sare ya 1-1 na Crystal Palace.















Ronaldo aiokoa Real Madrid isife kwa Atletico

Cristiano Ronaldo
Ronaldo akishangilia bao lao la kusawazisha dhidi ya mahasimu wao Atletico Madrid leo
BAO la dakika ya 82 lililofungwa na nyota wa Real Madrid Cristiano Ronaldo kwa pasi ya Gareth Bale imeiokoa vinara hao wa Ligi Kuu ya Hispania kufa mbele ya mahasimu wao wa jiji la Madrid, Atletico Madrid na kulazimisha sare ya mabao 2-2.
Karim Benzema alitangulia kuifungia Real iliyokuwa uwanja wa ugenini dhidi ya Atletico baada ya kumalizia mpira wa Angel di Maria, lakini wenyeji walisawazisha dakika ya 28 kupitia kwa Koke kabla ya Gabi kuongeza la pili sekundu chache timu hazijaenda mapumziko.
Dakika nane kabla ya pambano hilo lililokuwa kali kumalizika Ronaldo aliifungia timu yake bao la kusawazisha na kuifanya iendelea kusalia kileleni ikiwa na pointi 64 huku wapinzani wao wakikwea hadi nafasi ya pili ila watakaa kwa muda iwao Barcelona itashinda mechi yake itakayochezwa baadaye dhidi ya Almeria.
Katika mechi nyingine zilizochezwa leo Villarreal ikiwa nyumbani ililazimishwa sare ya 1-1 dhidi ya Real Betis.

Ashanti Utd, Kagera Sugar zatakata, Prisons yabanwa na Mgambo JKT

Ashanti United iliyoifumua Rhino Rangers
Kagera Sugar iliyoitandika JKT Ruvu
WAUZA Mitumba wa Ilala, Ashanti United imepata ushindi mwembamba wa bao 1-0 dhidi ya 'vibonde' wenzao Rhino Rangers ya Tabora, ushindi kama iliyopata Kagera Sugar nyumbani kwao mjini Bukoba dhidi ya JKT Ruvu, huku Prisons na Mgambo zikigawana pointi Mbeya.
Mechi hizo tatu ni kati ya nne zilizochezwa leo Jumapili, ambapo kwenye uwanja wa Chamazi, Ashanti ilipata ushindi wake wa pili kwenye duru ili la pili baada ya nyota wa zamani wa Yanga, Abubakar Mtiro kufunga bao hilo pekee lililoipa Ashanti pointi tatu na kuzidi kuiweka pabaya Rhino katika janga lake la kushuka daraja.
Nayo timu ya Kagera Sugar kwenye uwanja wake wa Kaitaba, iliizima JKT Ruvu iliyoshuka dimbani hapo ikiwa na kumbukumbu ya ushindi wa kushtukiza dhidi ya Simba wiki iliyopita kwa kuilaza bao 1-0.
Bao hilo pekee la mchezo huo lilifungwa kwa mkwaju wa penati na Themi Felix katika dakika ya 43 na kuifanya Kagera kujizatiti kwenye nafasi ya tano nyuma ya Simba, huku JKT ikisaliwa na pointi zao 22.
Katika pambano jingine la ligi hiyo leo lililochezwa uwanja wa Sokoine, Mbeya baada ya Mgambo JKT kuwabana wenyeji wao Prisons na kutoka sare ya 1-1.
Mgambo walitangulia kufunga bao lililodumu hadi wakati wa mapumziko kabla ya wenyeji kuchomoa kupitia kwa Laurian Mpalile katika kipindi cha pili na kuendeleza rekodi ya kutopoteza mchezo wowote kwenye duru la pili na wiki ijayo itakabiliwa na Simba.

Simba yazinduka, Tambwe hashikiki kwa mabao


WAKATI Simba ikizinduka kwenye Ligi Kuu Tanzania Bara kwa kuicharaza Ruvu Shooting 'Wazee wa Wiki' kwa mabao 3-2,  Mshambuliaji kutoka Burundi, Amissi Tambwe 'Amissi Magoli' akiendelea kujihakikishia kiatu cha dhahabu katika ligi hiyo kwa msimu huu.
Tambwe aliyefunga mabao mawili katika mchezo huo wa leo uliochezwa kwenye uwanja wa Taifa, amefikisha mabao 19 na kufikia rekodi iliyowahi kuwekwa na John Bocco 'Adebayor' misimu miwili iliyopita.
Mrundi huyo alifunga bao la kwanza dakika ya 23 na kuongeza la pili dakika 33 na kuifanya Simba kwenda mapumziko ikiongoza kwa mabao 2-0.
Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote kufanya mabadiliko yaliyoonekana kuinufaisha zaidi Ruvu walioongeza kazi ya mashambulizi na kujipatia bao la kwanza lililofungwa na Said Dilunga kabla ya Haruna Chanongo kuifungia Simba bao la tatu.
Bao la pili la Ruvu lilifungwa kwa mkwaju wa penati na Lambele Jarime baada ya mmoja wa wachezaji wa Simba kunawa mpira katika harakati za kuokoa mpira langoni mwake.
Kwa ushindi huo Simba imefikisha pointi 35 na kuendelea kusalia nafasi ya nne nyuma ya Mbeya City yenye pointi 36 ambayo jana ililazimishwa suluhu na Oljoro JKT.
Kwa upande wa mbio za kuwania kiatu cha dhahabu, Amissi Tambwe amezdi kuwaacha mbali wapinzani wake baada ya kufikisha jumla ya mabao 19, huku anayemfuata Kipre Tchetche akiwa na mabao 10.
Mwanzoni mwa msimu huu Tambwe alinukuliwa na MICHARAZO akisema amepania kufunga jumla ya mabao 20 msimu huu ili kunyakua kiatu cha dhahabu kitu kinachoonekana kuwa kweli kwani mechi zikiwa bado kama sita kabla ya ligi kufikia tamati ameshafikisha idadi hiyo bao moja zaidi ya lengo lake je atyaifikia rekodi ya Abdallah Juma nyota wa zamani wa Mtibwa aliyefunga mabao 25 katika msimu mmoja? Tusubiri tuone.

Manchester City yatwaa taji la Capital One


KLABU ya Manchester City jioni hii imenyakua taji lake la kwanza kati ya manne ambayo kocha wae, Manuel Pellegrini alitangaza kuyawinda kwa msimu huu baada yta kuifumua Sunderland katika Fainali ya Kombe la Ligi (Captital One).
Pellegrini aliahidi mwezi uliopita kwamba timu yake itanyakua mataji manne likiwemo hilo la Ligi, FA, Ligi ya Mabingwa Afrika na Ligi Kuu ya England.
Pambano hilo lililochezwa kwenye uwanja wa Wembley ilishuhudiwa Sunderland ikitangulia kupata bao kupitia kwa 
Fabio Borini katika dakika ya 10 na kudumu hadi mapumziko.
hata hivyo kipindi cha pili Man City ilicharuka na kusawazisha bao dakika ya 55 kupitia kwa Mchezaji Bora wa Afrika, Yaya Toure kabla ya Samir Nasir kuongeza la pili dakika ya moja baadaye na Jesus Navas kuongeza la tatu dakika ya 90.






Hiki ndicho kikosi cha Ruvu Shooting dhidi ya Simba

HIKI ndicho kikosi cha Ruvu Shooting dhidi ya Simba kwa mujibu wa Msemaji wa timu hiyo, Masau Bwire aliyeitumia MICHRAZO MITUPU mapema kabla ya kuelekea uwanjani.
Ni kikosi kile kile kilichobugizwa mabao 7-0 na Yanga wiki iliyopita, japo kina mabadiliko yaliyotajwa na Bwire cha kuishikisha adabu Simba kama walivyofanya kaka zao JKT Ruvu Jumapili iliyopita.

1. Abdallah Rashid-1
2.Michael Aidan-20
3.Mau Boffu-23
4.Baraka Jafar-2
5.Gideon Sepo-22
6. Ally Kani-14
7.Hamis Kisuke-17
8.Juma Nade-5
9.Elias Maguli-10
10.Said Dilunga-25
11.Raphael Kyala-8
Benchi:
Abdul Juma-30
Said Madega-19
Renatus Kisake-6
Frank Msesa-16
Ayoub Kitala-7Lambele Jerome-11
Juma Seif Kijiko-13
Tayari maafande hao wameshalimwa goli mopja dakika ya 23 lililofungwa na Amissi Tambwe na kumfanya Mrundi huyo kufikisha bao lake la 18 msimu huu, mechi inaendelea.

MAUAJI YA KUTISHA NCHINI CHINA


KUNDI moja la watu waliojihami kwa visu limewauawa takriban watu 28 katika kituo kimoja cha treni kusini magharibi mwa mji wa Kunming, nchini China.
Kituo cha habari cha Xhinua kimesema kuwa zaidi ya watu mia moja walijeruhiwa.
Baadhi ya majeruhi katika shambulio hilo wakiwa hospitali. 
Mashahidi wamesema kuwa washambuliaji hao waliovalia nguo nyeusi,waliwavamia abiria waliokuwa wakingojea kuabiri treni na kuwakatakata huku wengine wakiwadunga visu wale walioshindwa kukimbia kwa kasi.
Miili ya watu waliouawa katika shambulio hilo.
Kulikuwa na takriban washambuliaji 10..Polisi waliwapiga risasi na kuwaua washambuliaji 5 huku wakiwasaka waliosalia. Shirika la habari la Xhinua limewalaumu watu wanaopigania kujitenga katika mkoa wa Shinjiang kwa tukio hilo.
Baadhi ya mizigo iliyoachwa eneo la tukio.

Jide waing'arisha Sikinde kizamani

Lady Jaydee a.k.a 'Anaconda'
Baadhi ya wanamuziki wa Sikinde, wakiwajibika jukwaani
BENDI kongwe ya muziki wa dansi ya Mlimani Park 'Wana Sikinde' imeanza kurekodi nyimbo za zamani ikishirikisha baadhi ya wasanii wa muziki wa kizazi kipya ili kuzipa vionjo tofauti.
Sikinde imeanza na wimbo wa 'Duniani Kuna Mambo', ambao imeurekodi kwa kumshirikisha mkongwe Muhidini Gurumo 'Kamanda' na nyota wa muziki wa kizazi kipya, Lady Jay Dee.
Katibu wa bendi hiyo, Hamis Milambo alisema wimbo huo tayari umeshasambazwa kwenye vituo vya redio na kuanza kurushwa hewani wakijipanga kurekodi nyimbo nyingine hapo baadaye.
Milambo alisema wanataka kurekodi nyimbo zao zote za zamani kwa lengo la kukumbusha kizazi cha sasa kazi kubwa iliyofanywa na bendi hiyo katika kuendeleza muziki wa Tanzania.
Alisema nyimbo hizo baadhi zimeshasahaulika kutokana na mfumo wa zamani wa kurekodi na utunzaji ulivyokuwapo na hivyo wanataka kuzirudia na kuziweka kisasa ili kusaidia kudumisha muziki wao.
"Tumeanza na wimbo wa Duniani Kuna Mambo ambao tumeimba na Lady Jay Dee na Mzee Gurumo na umeanza kuruka hewani, baada ya hapo zitafuata nyingine tukishirikisha wasanii mbalimbali," alisema.
Milambo alisema pia bendi yao iliyoasisiwa mwaka Agosti 1978 inaendelea kurekodi nyimbo mpya kwa ajili ya albamu yao ijayo waliyopanga kuizinduliwa maadhimisho yao ya miaka 36.

Lambele: 'Bunduki' ya Ruvu Shooting iliyoweka rekodi FDL

Jerome Lambele
KIPAJI kikubwa alichonacho katika soka, hasa katika kufumania nyavu kimemwezesha mara kadhaa, mchezaji Jerome Lambele kunyakua tuzo mbalimbali za Mchezaji Bora na Mfungaji Bora.
Akicheza soka kwao Kigoma katika timu ya Kayengeyenge aliwahi kunyakua tuzo ya Mchezaji Bora wa Mkoa, na mwaka jana tena alitwaa tuzo ya Mfungaji Bora wa Ligi Daraja la Kwanza (FDL).
Tuzo hiyo aliipata kwa kufunga jumla ya mabao 16 yaliyoisaidia Ashanti United kurejea Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya misimu sita kupita tangu ilipoteremka mwaka 2007.
Mshambuliaji huyo anayeichezea Ruvu Shooting kwa sasa, anasema tuzo hizo na nyingine alizowahi kunyakua kupitia klabu na michuano mbalimbali zimekuwa zikimpa faraja kubwa kama mwanasoka.
"Kwa kweli najisikia faraja kunyakua tuzo mara kadhaa kwa kipaji nilichojaliwa, ila furaha kubwa zaidi kwangu ni  kuiwezesha timu ya taifa ya Coca Coca kunyakua taji la dunia nchini Brazili mwaka 2008," anasema.
Lambele, mwenye mabao matatu kwa sasa katika ligi ya msimu huu anasema tukio la Brazili la kunyakua taji bila kupoteza mchezo wowote limebaki kichwani mwake.
"Hili ndilo tukio la furaha lisilofutika kichwani mwangu, kwa sababu hakuna aliyetegemea kama Tanzania tungeweza kunyakua ubingwa huo, lakini tulifanikiwa," anasema.
Lambele anakumbuka katika michuano hiyo ya vijana U17 waliifunga Chile kwa mabao 2-1 katika mchezo wa fainali baada ya awali kutoa visago kwa Peru kwa kuilaza 5-0, ikatoka suluhu na Chile kabla ya kuilaza Argentina mabao 2-0 katika mechi za kundi. Hatua ya Robo fainali waliilaza Argentina 2-0 kisha kuifumua Paraguay kwa mabap 3-1 hatua ya Nusu Fainali.
Shabiki huyo wa klabu ya Manchester United anayemzimia nyota wa timu hiyo, Wayne Rooney, anasema kunyakua taji hilo kwa timu yao ilikuwa ni uthibitisho kuwa Tanzania imejaliwa vipaji vingi vya soka.
Anasema vipaji vya soka nchini vipo ila vinashindwa kuendelezwa hasa kutokana na kukosekana kwa mashindano mengi ya vijana.
"Lazima TFF na wadau wa soka wawekeze katika soka la vijana kwa kusaidia kuwe na mashindano mengi kuendeleza vipaji kwa faida ya taifa, pia klabu zitoe kipaumbele kwa timu zao za vijana," anasema.
Lambele anayependa kula ugali kwa samaki na kunywa juisi ya matunda mchanganyiko, anasema bila uwekezaji mkubwa katika soka la vijana ni vigumu taifa kuzifikia nchi nyingine zinazotamba duniani.
Lambele akichuana na Niyonzima
AJABU
Lambele anayejishughulisha na biashara na anayeshukuru soka kumsaidia kwa mambo mengi ikiwamo kupata elimu yake ya sekondari kwa sababu ya kipaji chake, anasema licha ya kucheza mechi nyingi halisahau pambano la Ligi Kuu msimu 2011-2012.
Anasema anaikumbuka mechi hiyo iliyochezwa uwanja wa Chamazi Novemba 5, 2011 wakati akiichezea Moro United walipoumana na Simba na kutoka nao sare ya 'miujiza' ya mabao 3-3.
Anasema hakuna aliyetarajia mechi hiyo ingeisha kwa sare hiyo kwani Moro Utd waliwatangulia Simba kwa kuwafunga mabao 3-1 hadi mapumziko, bao la Simba likifungwa 'jioni' ya kipindi hicho.
"Kwangu niliona kama miujiza kwa sababu tuliamini tumeshaimaliza Simba baada ya kwenda mapumziko tukiongoza 3-1," anasema.
"Hata hivyo kipindi cha pili mambo yalibadilika na Simba kurejesha mabao hayo na kulazimika tugawane pointi kutokana na sare ya 3-3."
Mkali huyo anasema mbali na mechi hiyo pia anakumbuka mechi ya Moro Utd msimu huo dhidi ya Yanga lililochezwa uwanja wa Jamhuri, Morogoro alipoifungia timu yake bao la kusawazisha.
"Bao hilo ndilo goli tamu na bomba kwangu, kwani nililifunga kiufundi na kuisaidia Moro Utd kupata sare ya 1-1," anasema.
Juu ya huzuni, Lambele ambaye hajaoa wala kuwa na mtoto mwenye kiu ya kutaka kurejea darasani ili ajiendeleze kielimu, anasema ni kipigo walichopewa na Mbeya City katika mechi ya duru la kwanza.
"Kwa kweli kipigo kile cha mabao 2-1 tulichopewa ugenini jijini Mbeya katika duru la kwanza ndiyo huzuni yangu kwani hatukutegemea kwa namna tulivyocheza vyema," anasema.
Akiwa mbele ya gari lake
KIPAJI
Lambele aliyezaliwa Juni 23, 1993 Ujiji Kigoma na kusoma Shule yua Msingi Buzebazeba kabla ya kufaulu na kuendelea Kichangachui Ujiji na kuja kumalizia elimu yake Shule ya Kanali Idd Kipingu.
Tangu akiwa kinda Lambele alianza kuonyesha kipaji chake cha soka kwa kucheza mtaani kabla ya kutamba shuleni na kupewa Uwaziri wa Michezo akimudu nafasi zote za ushambuliaji.
Baadhi ya timu alizozichezea kabla ya kuja kutamba kwenye ligi ni  True Lies, Kayengeyenge, Fire Stone na Kigoma United kabla ya kutua Dar na kutamba kwenye michuano ya Copa Coca Cola-2008.
Michuano hiyo ndiyo iliyomfungulia nyota huyo baraka za kuonwa na timu za Ligi Kuu akidakwa na Moro Utd kabla ya kutua Ashanti Utd ikiwa daraja la kwanza na kuipandisha Ligi Kuu msimu huu.
Lambele aliweka rekodi ya kufunga mabao 6 pekee yake katika mchezo mmoja walipoisulubu Moro Utd kwa mabao 10-1 pia alifunga mabao pekee yake walipoilaza Transit Camp 4-0 na kufunga hat trick nyingine mbili na kuipadisha Ashanti Utd Ligi Kuu.
Hiyo ni rekodi ya aina yake kwa vile katika mechi za ligi ni Edibily Lunyamila na Nsa Job waliokuwa wameweza kufunga idadi kubwa ya mabao katika mechi moja. Kila mmoja alifunga mabao matano.
Pia haikuwahi kushuhudiwa mchezaji mmoja kufunga hat-trick nne mfululizo katika mechi yoyote ya ligi kama alivyofanya mchezaji huyo katika FDL akiwa na Ashanti kabla ya kuihama msimu huu.
Lambele aliihama Ashanti na kutua Ruvu Shooting aliyoisaidia timu hiyo kushika nafasi ya tano kwenye msimamo nyuma ya Simba, Mbeya City, Yanga na Azam.
Matarajio yake ni kufika mbali katika soka na kimaisha na kutoa shukrani zake kwa wazazi wake, Kanali Kipingu kwa kumsomesha na makocha Kim Poulsen aliyemnoa U17 mpaka sasa na Tom Olaba.
Lambele anayedaiu kusumbuliwa dimbani na beki wa timu yake aliyemtaja kwa jina la Chogo, anawataka wachezaji wenzake kuwa na nidhamu, kufanya mazoezi na kusikiliza makocha na kuwa na kiu ya maendeleo hasa ya kucheza soka la kulipwa nje ya nchi.
"Wachezaji wakizingatia nidhamu, kujituma mazoezini na uwanjani kutasaidia kuinua kiwango cha soka letu, pia wadau na viongozi wathamini mchango wa wachezaji kwani wanavuja jasho," anasema.
===============

Simba katika mtihani mwingine mgumu leo Taifa

* Inaivaa Ruvu Shooting iliyopigwa 7-0 na Yanga
* Ashanti Utd kujiuliza kwa Rhino Rangers
* Tambwe kuendelea kucheka na nyavu
Mshambuliaji nyota wa Simba na kinara wa mabao katika ligi kuu, Amissi Tambwe atawanyamazisha Ruvu Shooting leo
BAADA ya Jumapili iliyopita kuangukia pua mbele ya 'maafande' wa JKT Ruvu kwa kutandikwa mabao 3-2, Wekundu wa Msimbazi, Simba leo wanatarajiwa kuwa na kibarua kingine kigumu pale watakapovaana na maafande wengine wa Ruvu Shooting katika mfululizo wa Ligi Kuu.
Pambano hilo litakalochezwa kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam ni kati ya mechi nne za ligi hiyo iliyopo raundi ya  ya 20 zitakazochezwa leo katika viwanja tofauti na mashabiki wana hamu kubwa ya kutaka kuona Simba itavuna nini kwa maafande hao waliobugizwa mabao 7-0 na Yanga.
Simba inayokamata nafasi ya nne ikiwa na pointi 32 inahitaji ushindi ili kutuliza hasira za mashabiki wao ambao wamekosa amani baada ya timu yao kupata matokeo yasiyoridhisha katika mechi zao nne zilizopita walizoambulia pointi mbili tu huku ikipoteza michezo miwili na kuambulia sare mbili.
Wanachama na mashabiki wa Simba wanaoushutumu uongozi wa Ismail Aden Rage kwa madai ya kuitelekeza timu, huku baadhi wakihisi kuna hujuma zinazofanywa ili timu ifanye vibaya, kitu ambacho kinaweza kutulizwa iwapo Simba itashinda tu leo vinginevyo moto utawaka Msimbazi.
Kocha Zdrakov Logarusic anayeshutumiwa kwa kuchangia kufanya vibaya kwa timu hiyo kitendo chake cha kuwafokea na kuwatulea maneno machafu wachezaji anaweza kukiweka kibarua chake rehani, iwapo Simba itapoteza mechi yao leo kwa Ruvu Shooting inayonolewa na Tom Olaba.
Logarusic amedaiwa amekuwa mkali kupita kiasi hali inayowafanya wachezaji wasijiamini uwanjani na kufanya timu ipate matokeo mabaya, hali inayoweza kuwa mbaya zaidi kama Ruvu itafuata nyayo za 'kaka' zao wa JKT Ruvu kwa kuisulubu vijana wa Msimbazi.
Wachezaji wa Simba chini ya manahodha wao, Nassor Masoud 'Chollo' na Amri Kiemba wameapa kupigana kiume ili kurekebisha makosa, huku wakijaribu kuficha 'siri' juu ya tatizo ambalo linawakabilia wachezaji kwa kudai hawadai wala kucheza chini ya kiwango kwa kudai posho zao.
"Hali hii inatuhuzunisha hata sisi, lakini ni ugumu wa ligi na tutapigana kiume kuona tunashinda mechi zetu zilizosalia za ligi kuu," alisema Chollo alipozungumza na wanahabari wiki hii.
Hata hivyo Msemaji wa Ruvu, Masau Bwire ametamba kuwa, baada ya kuotewa na Yanga jumamosi iliyopita na kubugizwa mabao 7-0 wasingekubali kuona wakifungwa pia na Simba leo.
Bwire alisema kochao kutoka Kenya, Tom Olaba na wachezaji wameuhakikishia uongozi kuwa leo watakufa na Simba ili kunyakua pointi tatu na kujiweka pazuri kwenye msimamo baada ya wiki iliyopita kuteleza kwa mabingwa watetezi na kudai Simba leo hawaponi Taifa.
"Hawaponi. Hatukubali kufungwa kwa mara nyingine tena. Yanga wametudhalilisha vya kutosha na sasa ni zamu ya kurekebisha makosa kwa kuichabanga Simba kwenye uwanja wa Taifa," alisema.
Ukiondoa mechi hiyo ya Simba na Ruvu, leo pia kutakuwa na mechi nyingine nne zitazikutanisha timu nane ambapo Kagera Sugar itakuwa nyumbani kuikaribisha JKT Ruvu  uwanja wa Kaitaba, Kagera huku Rhino Rangers itakakuwa wageni wa Ashanti United kwenye uwanja wa Chamazi, Dar es Salaam na Prisons Mbeya itaikaribisha Mgambo JKT kwenye uwanja wa Sokoine, Mbeya.

Msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara 2013-2014     
                                  P    W     D     L    F     A   GD  PTS
01.Azam                    18   11    07   00   35   12   23  40
02.Yanga                   17   11    05   01   41   12   29  38
03.Mbeya City           20   09    09   02   24   16   08  36
04.Simba                   19   08    08   03   35   19   16  32
05.Kagera Sugar        19   06    08   05   16  15   01  26
06.Coastal Union        19   05    10    04  14  09   05  25
07.Mtibwa Sugar       19   06    07    06   23  23   00  25
08.Ruvu Shooting       19  06    07   06    20  26  -06  25
09.JKT Ruvu             19   07    01    11   16  29  -13  22
10.Prisons                  18   04    08    05   17  18  -01  20
11.Mgambo               19   05    05    09   12  27  -15  20
12.Oljoro                   21   02    10    09   15  30  -15  16
13.Ashanti                 19   03    05    11   15  34  -19  14
14.Rhino Rangers      19   02    07    10   12  23  -11  13
 
Wafungaji:

17- Tambwe Amisi (Simba)
10- Kipre Tchetche (Azam)
09- Elias Maguri (Ruvu Shooting) Hamis Kiiza, Didier Kavumbagu (Yanga)
08-Juma Luizio (Mtibwa Sugar), Mrisho Ngassa (Yanga)
07- Peter Michael (Prisons)
06- Themi Felix (Kagera Sugar), Mwegani Yeya (Mbeya City)
05- Tumba Sued (Ashanti Utd), Jerry Santo (Coastal Union)
04- Jerry Tegete (Yanga), Jonas Mkude, Betram Mombeki (Simba), Bakar Kondo, Salum Machaku (JKT Ruvu), Jerome Lambele (Ruvu Shooting), Abdallah Juma (Mtibwa Sugar)

Titina: Dansa Extra Bongo anayetamani kuwa kama Mbilia Bel

Titina katika pozi
BAADA ya miaka 14 ya kunengua jukwaani katika bendi mbalimbali, dansa Titi Mwinyiamiri maarufu kama 'Titina' anasema anatamani kwa sasa kuwa muimbaji ili kuupumzisha mwili wake.
Mnenguaji huyo wa bendi ya Extra  Bongo anasema tayari ameanza kujifunza kuimba ili kutimiza ndoto zake kama baadhi ya madansa wa zamani ambao walikuja kutamba kimataifa katika fani ya uimbaji.
"Natamani kuwa muimbaji mkubwa, nataka kuupumzisha mwili baada ya kunengua kwa miaka karibu 14 tangu mwaka 2000 nilipojitosa rasmi katika fani hii," anasema.
Mwanadada huyo anasema kipaji cha uimbaji na sauti nzuri anayo japo hakuitilia maanani kipindi akiwa shuleni wakati alipokuwa akiimba kwaya na bendi ya shule.
Titina anasema kwa miaka ya sasa waimbaji wa kike wapo wachache jambo ambalo linamhamasisha kutamani kuwa muimbaji ili kupunguza pengo lililopo baina ya wanamuziki wa kike na kiume.
"Siku za nyuma asilimia kubwa ya bendi za muziki wa dansi zilizokuwa na waimbaji wa kike, siku hizi ni bendi chache pengine kutokana na uchache wa waimbaji hao, hivyo nataka kupunguza pengo hilo."
Anasema anaamini kwa kipaji alichonacho katika sanaa kitamfikisha mbali kama ilivyokuwa kwa Mbilia Bell, Tshalla Mwana na hata Luiza Mbutu walioanzia katika uneguaji kabla ya kugeuka waimbaji mahiri.
"Naamini bidii yangu itanifikisha kule ilipowafikisha waimbaji kadhaa nyota waliokuja kutamba kimataifa wakitokea kwenye unenguaji kama ilivyokuwa kwa akina Tshalla Mwana au Yondo Kusala," anasema.

MAFANIKIO
Titina anayependa kula wali kwa kuku wa kienyeji na kunywa soda ya Novida, anasema licha ya watu wengi kuidharau fani ya sanaa hasa unenguaji, yeye anaiheshimu kwa mafanikio makubwa aliyoyapata.
KImwana huyo anasema sanaa hiyo imemwezesha kumiliki saluni za kike na ya kiume, kumjengea nyumba mama yake ambaye hata hivyo ameshafariki na pia kumiliki viwanja viwili kitu anachojivunia.
"Kwa kweli nashukuru Mungu kazi hii imenisaidia kwa mengi kiasi kwamba naiheshimu na hata ninapoona watu wanaibeza nashindwa kuwaelewa kwa sababu ni kazi kama kazi nyingine," anasema.
Titina anasema pamoja na mafanikio hayo, lakini bado hajaridhika na badala yake anatamani afike mbali zaidi ili hapo baadaye aje kujikita kwenye biashara wakati umri utakapokuwa umetupa mkono.
"Sijaridhika kabisa, japo nashukuru kwa mafanikio haya ila napenda Mungu anisaidie nifike mbali zaidi," anasema.
nilipofikia,"  kwa vile wapo watu wengine hawana mafanikio kama haya niliyonayo," anasema.
HUZUNI
Titina ambaye pia ni msusi wa nywele na mfumaji wa vitambaa vya uzi, anasema hakuna tukio linalomsikitisha mpaka sasa kama tukio la kufiwa na mama yake wakati akiwa ughaibuni.
"Tukio lenyewe limenitokea mwaka jana baada ya kupata safari ya kwenda kutumbuiza Dubai, Falme za Kiarabu ambapo wiki chache baada ya kupata visa nilifahamishwa mama yangu kadondoka."
"Wiki moja baadaye nikafahamishwa kuwa mama yangu amefariki dunia kwa kweli roho iliniuma, inaniuma na itaendelea kuniuma kwa vile mwanae nilikuwa natafuta riziki kwa ajili yake," anaongeza.
Titina anasema tukio hilo linamliza kila akilikumbuka, huku akisema furaha yake ni jinsi mpenzi wake anavyopenda, kumheshimu na kumjali kama mkewe na huchukia kumsaidia mtu kisha asiwe na shukrani kwa kumsema vibaya mitaani.
Mnenguaji huyo anawataka wasanii wenzake kujiheshimu, kupendana na kusaidiana, anasema sanaa ya muziki Tanzania bado ipo chini kwa kukosa sapoti kubwa toka serikali na hata kwa wadau wake.
"Kwa Bongofleva na taarab kuna nafuu fulani, siyo muziki wa dansi hivyo ni vyema serikali na wadau wakaupiga tafu muziki huo ufike mbali zaidi," anasema.
"Wapo baadhi ya watu hukosa shukrani pale unapowasaidia kwa kukusema vibaya, wananiudhi sana watu wa hivi na kukatisha tamaa kutoa msaada kwa wengine," anasema.

WATOTO WA MBWA

Titina anayewakubali waimbaji Nyoshi el Saadat na Ally Choki, pia anaiangukia serikali juu ya vitendo vya uhalifu vinavyofanywa na kundi la Watoto wa Mbwa wanaowanyima raha wakazi za maeneo ya Ilala.
"Hili kundi linalojiita 'Watoto wa Mbwa' wanatunyima raha kwa vitendo vyao vya ukabaji na uporaji wakati mwingine mchana kweupe kiasi cha kushindwa kuishi kwa amani, serikali itusaidie," anasema.
Anasema anaamini serikali kwa kutumia jeshi la Polisi wakiwavalia njuga 'wahuni' hao wanaweza kuwafanya waishi kwa uhuru na amani kama wakazi wa maeneo mengine.
"Wanatukosesha raha, yaani kila unapokuwa unatoka kibaruani unakuwa na hofu kurejea nyumbani kwa kuwafikiria vijana hao waliotawala eneo la Kiwalani na wilaya ya Ilala kwa ujumla," anasema.
KIPAJI
Titi Mwinyiamiri, alizaliwa Oktoba 10, 1980 mjini Bagamoyo akiwa ni mtoto wa 10 kati ya 11 wa familia yao. Alisoma Shule ya Msingi Magomeni Makuti ambapo alianza kuonyesha kipaji cha sanaa.
Hata hivyo alijitosa rasmi kwenye fani hiyo mwaka 2000 akianzia bendi ya Double M Sound ya Mwinjuma Muumin, kisha akatua African Stars 'Twanga Pepeta' na baadaye akaenda FM Academia.
Baada ya kutamba FM alihama bendi hiyo na kutumia Extra Bongo alikonako mpaka sasa na kudai ni mahali anapofurahia maisha yake ya sanaa kwa namna wasanii wanavyothaminiwa na 'mabosi' wao.

Yanga yaweka rekodi EAC kama Flambeau de l'Est na AS Kigali

Yanga
USHINDI wa bao 1-0 iliyopata dhidi ya watetezi wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Al Ahly ya Misri imeifanya klabu ya Yanga kuwa moja ya timu tatu pekee za Jumuiya ya Afrika Mashariki zilizopata ushindi barani Afrika mwishoni mwa wiki.
Yanga walipata ushindi huo kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam ikiwa ni mara yao ya kwanza kuifunga timu kutoka Misri na ukanda wa Afrika Kaskazini baada ya zaidi ya miaka 30 iliyopita.
Timu nyingine za ukanda huo iliyotakata Afrika ni; Flambeau de l'Est ya Burundi iliyoiduwaza Cotonsport ya Cameroon katika Ligi ya Mabingwa Afrika kwa kuilaza bao 1-0 mjini Bunjumbura, huku AS Kigali ya Rwanda ikishinda pia nyumbani kwa bao 1-0 katika michuano ya Kombe la Shirikisho dhidi ya Al Ahly Shendi ya Sudan Kusini.
Timu hizo tatu Yanga, Flambeau de l'Est na AS Kigali zinahitaji sare yoyote ugenini kuweza kusonga mbele kwenye hatua inayofuata ya michuano wanayoishiriki baadaye wiki hii.
Wawakilishi wengine wa jumuiya hiyo, Gor Mahia na AFC Leopards za Kenya zenyewe zilichezea vichapo katika michuano hiyo ya Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho.
Gor Mahia ilifungwa nyumbani na Esperance ya Tunisia katika Ligi ya Mabingwa Afrika kwa mabao
3-2, huku Leopards wakinyukwa ugenini mabao 2-0 na Supersport ya Afrika Kusini.
Mabingwa wa Kombe la Mapinduzi, KCCA ya Uganda, walilazimisha sare ya mabao 2-2 ugenini dhidi
ya Nkana Red Devil's ya Zambia na kujiweka katika nafasi nzuri ya kusonga mbele katika mechi ya
marudiano mjini Kampala.
Timu za ukanda wa Afrika Mashariki, zimekuwa haina matokeo mazuri kwenye michuano mikubwa
barani Afrika, lakini ushindi iliyopata Yanga, Flambeau de l'Est na As Kigali na sare ya KCCA ni dalili njema, ingawa Gor Mahia na AFC Leopards bado nazo zina nafasi ya kujiuliza wikiendi hii.

Liverpool yazidi kung'ara England, yaing'oa Arsenal nafasi ya pili

Luis Suarez akishangiulia bao lake

LIVERPOOL imeiengua Arsenal kwenye nafasi ya pili na kuikamata wenyewe baada ya jana usiku kuizabua Southampton ikiwa kwao kwa mabao 3-0.
Mapema jana Arsenal ilikumbana na kipigo cha kushtukiza cha bao 1-0 toka kwa Stoke City na kuwafanya wasalie na pointi zao 59 ambazo zimefikiwa na Liverpool kwa ushindi wake wakitofautiana idadi ya mabao ya kufunga na kufungwa.
Luis Suarez alitangulia kufunga bao la mapema dakika ya 16  bao lililodumu hadi mapumziko kabla ya kipindi cha pili wenyeji kuonekana kucharuka kutaka kusawazisha bao hilo.
Hata hivyo, Raheem Sterling alifunga bao la pili dakika ya 56 akimalizia pande safi la Suarez kabla ya nahodha Steven Gerrard kumalizia udhia dakika za nyongeza kwa mkwaju wa penati na kuiweka timu yake katika mbio za ubingwa ikiipumulia Chelsea iliyopo kileleni waliowazidi pointi nne tu.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea tena leo kwa michezo mitatu, Aston Villa itavaana na Norwich City, Swansea iliyong'olewa kwenye michuano ya Europa Lague itaumana na Crystal Palace na Tottenham Hotspur itakuwa nyumbani kuwakaribisha Cardiff City.