STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Thursday, August 29, 2013

Frank Ribery ndiye Mchezaji Bora Barani Ulaya awabwaga Messi na Ronaldo

Frank Ribery ambaye kiimani ni Muislam akiomba dua kabla ya kuanza pambano la soka la timu yake ya Bayern Munich

NYOTA wa Kifaransa anayeichezea klabu ya Bayern Munich, Frank Ribery amewagaragaza wakali wa Hispania, Lionel Messi wa Barcelona na Cristiano Ronaldo kwa kunyakua tuzo ya Mchezaji Bora wa Ulaya 2012-2013.
Mkali huyo aliyeisaidia Bayern Munich kunyakua taji la Ligi ya Mabingwa ya Ulaya na mengine mawili ya Ligi ya Ujerumani alitangazwa kunyakua tuzo hiyo leo barani humo.
Ribery amenyakua tuzo hiyo akimpokea Iniesta wa Barcelona aliyenyakua msimu uliopita akitanguliwa na Messi aliyetwaa mwaka 2010-2011.
Nafasi ya pili katika kimyang'anyiro hicho ilienda kwa Messim kisha Ronaldo aliyeshina nafasi ya tatu, ingawa hjakuweza kuhudhuria sherehe hizo zilizoenda sambamba na kutangazwa kwa makundi ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu wa 2013-2014.

Rais Kikwete amteua Kamishna Mkuu Idara ya Uhamiaji

Rais Jakaya Kikwete
RAIS wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete amemteua Ndugu Sylvester Ambokile Mwakinyule kuwa Kamishna Mkuu, Idara ya Uhamiaji.
 
Taarifa iliyotolewa leo, Alhamisi, 29 Agosti, 2013 mjini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Y. Sefue inasema kuwa uteuzi huo umeanza jana, Agosti 28, mwaka huu, 2013.
Ndugu Mwakinyule anachukua nafasi ya Ndugu Magnus Ulungi ambaye atapangiwa kazi nyingine.
 
Kabla ya uteuzi wake, Ndugu Sylvester Ambokile Mwakinyule, alikuwa Naibu Kamishna wa Uhamiaji na Mwambata wa Uhamiaji katika Ubalozi wa Tanzania, London, Uingereza
 
Rais pia amemteua Dkt. Nyamajeje Calleb Weggoro kuwa Msaidizi wa Rais, Masuala ya Ushirikiano wa Kikanda.
 
Taarifa iliyotolewa leo, Alhamisi, 29 Agosti, 2013 mjini Dar es Salaam na Katibu Mkuu Kiongozi Balozi Ombeni Y. Sefue inasema kuwa uteuzi huo umeanza jana Agosti 28, mwaka huu, 2013.
 
Kabla ya uteuzi huu, Dkt. Nyamajeje Calleb Weggoro alikuwa Mkurugenzi wa Sekta za Uzalishaji (Productive Sectors) katika Sekretarieti ya Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC).
 
 
 

Makundi UEFA League yatoka, Barca, Milan, Ajax chungu kimoja

MAKUNDI ya Ligi ya Mabingwa Ulaya yametangazwa leo ambapo mabingwa wa Hispania, Barcelona wametupwa kundi moja na AC Milan na Ajax, wakati Chelsea wameweka kundi moja na 'wasumbufu' Basel.
Makundi kamili ya ligi hiyo ambapo mabingwa wake watetezi ni Wajerumani Bayern Munich, ni kama yafuatayo;
 
Group A
Man. United (ENG)
Shakhtar Donetsk(UKR)
Leverkusen(GER)
Real Sociedad(ESP)
Group B
Real Madrid(ESP)
Juventus(ITA)
Galatasaray(TUR)
København(DEN)
Group C
Benfica(POR)
PSG(FRA)
Olympiacos(GRE)
Anderlecht(BEL)
Group D
Bayern(GER)
CSKA Moskva(RUS)
Man. City(ENG)
Plzeň(CZE)
Group E
Chelsea(ENG)
Schalke(GER)
Basel(SUI)
Steaua(ROU)
Group F
Arsenal(ENG)
Marseille(FRA)
Dortmund(GER)
Napoli(ITA)
Group G
Porto(POR)
Atlético(ESP)
Zenit(RUS)
Austria Wien(AUT)
Group H
Barcelona(ESP)
Milan(ITA)
Ajax(NED)
Celtic(SCO)

'Bondia Ibrahim Maokola hajakamatwa, katelekezwa Italia'

https://fbcdn-sphotos-f-a.akamaihd.net/hphotos-ak-ash3/944257_379837705469127_1264255997_n.jpg
Bondia Ibrahim Maokola
 KOCHA wa bondia machachari wa ngumi za kulipwa nchini, Ibrahim Maokola, Chaurembo Palasa amekanusha taarifa kwamba bondia huyo amekatwa nchini Italia kwa tuhuma za dawa za kulevya.
Badala yake Palasa alisema Maokola, aliyechukuliwa na promota maarufu nchini Shomari Kimbau ametelekezwa na promta huyo akiwa hana tiketi ya kurejea nchini.
Palasa alisema bondia wake alichukuliwa kinyemela na Kimbau kwenda kupigana na mipango ikaenda hovyo na Kimbau kumtoroka na kumuacha akiwa hana msaada wowote mpaka sasa na siyo kweli kama katiwa mbaroni kwa tuhuma za dawa za kulevya kama ilivyoelezwa na gazeti moja la kila wiki.
"Bondia Ibrahim Maokola, hajakamatwa Italia kama ilivyoripoti gazeti la ....la wiki iliyopita. Bondia Maokola alichukuliwa na Shomari Kimbau kwenda kupigana ngumi Italia mpaka muda huu bondia huyo ametelekezwa ghetto akiwa hana tiketi ya kurudi Tanzania," Palasa aliiambia MICHARAZO.
Awali ilielezwa kuwa bondia huyo na promota huyo walinaswa Italia kwa tuhuma kwamba walipeleka dawa za kulevya, ingawa hakuna uthibitisho wowote uliowahi kutolewa kuthibitisha taarifa hizo na hivyo meneja huyo wa Maokola ameamua kuweka sawa ili kusafisha hali ya hewa ambayo ilianza kumchafukia bondia wake wakati yupo kwenye matatizo, yeye akijaribu kuwasiliana na familia yake ili kumsaidia arejee nchini..

Yanga, Coastal Union wavuna Sh . Mil. 152

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEj404PkGb7SiEVuMydJgAD5SUi1Dn7qkqZ-XJCGqQF3h-FdUmM4SqgP3xdez_ThTpx8JPnrFmD3GbEKygqyxzrpvY7SJWe6UDXkWzwSGti0PPt1pVV8_19cFA9PBY88prvEcTXFt_7qkmc/s640/IMG_3331.JPG
Na Boniface Wambura
PAMBANO la Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) kati ya Yanga na Coastal Union lililochezwa jana (Agosti 28 mwaka huu) katika Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam limeingiza sh. 152,296,000.

Watazamaji 26,137 walikata tiketi kushuhudia mechi hiyo namba 14 ya VPL msimu wa 2013/2014 iliyomalizika kwa sare ya bao 1-1.

Viingilio katika mechi hiyo vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 36,947,427.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 23,231,593.22.

Mgawo mwingine ni asilimia 15 ya uwanja sh. 18,786,827.52, tiketi sh. 3,818,890, gharama za mechi sh. 11,272,096.51, Kamati ya Ligi sh. 11,272,096.51, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 5,636,048.26 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 4,383,593.09.

Golden Bush kukipiga Pugu, yamnyatia George Masatu

http://thumbp4-ne1.thumb.mail.yahoo.com/tn?sid=2126005954&mid=AH1bimIAABNxUh7nBQAAAM7weWo&midoffset=2_0_0_1_1255535&partid=2&f=1215&fid=Inbox&w=480&h=331
BAADA ya kushindwa kutambiana na Mwanza United Veterani kwa kutoka sare ya mabao 4-4, wakali wa soka jijini Dar es Salaam, Golden Bush Veterani Jumamosi inatarajiwa kuwafuata Pugu Veterani kwao kwa ajili ya pambano la kirafiki litakalofanyika Pugu Kajiungeni, nje kidogo ya jiji la Dar.

Kwa mujibu wa Msemaji wa Golden Bush, Onesmo Waziri 'Ticotico' ni kwamba pambano hilo litachezwa majira ya asubuhi na kuna uwezekano kikosi chao kikamtumia kwa mara ya kwanza nyota wa zamani wa Pamba, Simba na Taifa Stars, George Masatu.

Ticotico alisema Golden Bush imevutiwa na Masatu baada ya kuonyesha kiwango kikubwa katika mechi ya kirafiki baina yao na kwamba walikuwa katika 'mazungumzo' ya kumsajili rasmi katika kikosi chao ili aweze kuanza kuitumikia Golden Bush dhidi ya Pugu Veterani.

Msemaji huyo ambaye pia ni mmoja wa washambuliaji tegemeo wa timu hiyo, alisema mazungumzo ya kumnyakua Masatu ili kumahamisha kutoka Mwanza United yanafanywa na mwanasheria wa timu ya Golden Bush Godfrey Chambua  a.k.a Zacharia Hans Poppe.

"Bwana Poppe aliyeshikana mkono na Athumani Machuppa pichani ndiye aliyewezesha usajili wa akina Athuman Machuppa na Sadik Muhimbo ambao wote wametolewa kwa mkopo timu za Sweden na DRC," alisema Ticotico.

Kabla ya pambano hilo kulikuwa na mipango Golden Bush iumane na TASWA, lakini kwa mujibu wa maelezo ya Ticotico, wanahabari hao wamechomoa kiaina na wao kulazimika kusafiri hadi Pugu Kajiungeni ili kugawa dozi kwa wapinzani wao kama inavyofanywa kwa viklosi vingine jijini Dar es Salaam.

Copa Cola Cola Kanda kuanza Septemba 2

Na Boniface Wambura
MICHUANO ya Copa Coca-Cola kwa vijana wenye umri chini ya miaka 15 inayoshirikisha mikoa yote ya Tanzania Bara na Visiwani inaanza kutimua vumbi Septemba 2 mwaka huu katika vituo sita tofauti.

Kwa mujibu wa ratiba iliyopangwa leo (Agosti 29 mwaka huu), kituo cha Mwanza mechi zake zitachezwa katika viwanja vya Alliance ambapo timu zitakazofungua dimba ni Kagera vs Kigoma, Mara vs Tabora, Simiyu vs Geita na Mwanza vs Shinyanga.

Kituo cha Mbeya ambapo mechi zitachezwa viwanja vya Iyunga ni Katavi vs Njombe, na Ruvuma vs Mbeya. Kituo cha Pwani ni Ilala vs Kaskazini Unguja, na Lindi vs Pwani.

Ufunguzi katika kituo cha Arusha ambapo mechi zake zitachezwa Uwanja wa Kumbukumbu ya Sheikh Kaluta Amri Abeid ni Manyara vs Kilimanjaro, na Arusha vs Singida.

Uwanja wa Jamhuri ambapo utatumika kwa mechi za kituo cha Morogoro, Tanga itacheza na Dodoma wakati Morogoro itaumana na Temeke. Mjini Zanibar kwenye Uwanja wa Chuo cha Amaan ni kati ya Kaskazini Pemba na Mjini Magharibi, na Kusini Pemba dhidi ya Kusini Unguja.

USAILI WAGOMBEA TFF, TPL BOARD KUANZA KESHO


Na Boniface Wambura
USAILI kwa wanaoomba kuteuliwa kuwa wagombea uongozi katika uchaguzi wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na ule wa Bodi wa Ligi Kuu (TPL Board) unaanza kesho (Agosti 30 mwaka huu).

Kwa mujibu wa ratiba iliyotolewa na Kamati ya Uchaguzi ya TFF, Agosti 30 mwaka huu ni usaili kwa waombaji uongozi wote katika Bodi ya Ligi Kuu pamoja na waombaji uongozi wa TFF kwa kanda namba 11 (Morogoro na Pwani), kanda namba 12 (Kilimanjaro na Tanga) na kanda namba 13 (Dar es Salaam).

Agosti 31 mwaka huu ni kanda namba sita (Rukwa na Katavi), kanda namba saba (Mbeya na Iringa), kanda namba nane (Njombe na Ruvuma), kanda namba tisa (Lindi na Mtwara) na kanda namba kumi (Dodoma na Singida).

Usaili kwa kanda namba moja (Geita na Kagera), kanda namba mbili (Mara na Mwanza), kanda namba tatu (Simiyu na Shinyanga), kanda namba nne (Arusha na Manyara) kanda namba tano (Kigoma na Tabora), na nafasi za Rais na Makamu wa Rais wa TFF utafanyika Septemba Mosi mwaka huu.

Waombaji wote wamepangiwa muda wao wa usaili. Kwa mujibu wa ratiba usaili ufanyika kuanzia saa 3 kamili asubuhi hadi saa 2 usiku. Wasailiwa wote wanatakiwa kuzingatia muda waliopangiwa.

Duniani kuna Mambo! Wanaume China wanakodisha wanawake kunyonya maziwa yao kama vichanga



GAZETI la Morning Post la China Kusini limeripoti kwamba watu wazima nchini humo wanawalipa wanawake fedha ili wawanyonyeshe maziwa yao ya kifuani !.
Wanawake wanaojitolea kutoa maziwa yao hulipwa kiasi cha dola 2,700 za Marekani  (kama sh. Milioni 4) kwa mwezi ambapo watu wazima hao huweza kuyanyonya maz
iwa hayo moja kwa moja kutoka vifuani mwa kinamama hao kama watoto wadogo !.

Watu wengi wanaona jambo hilo ni la ajabu kwa mwanamme au mwanamke mzima kunyonya matiti ya mwanamke mwenzake.  Hata hivyo, nyuma ya kituko hicho kuna habari kwamba watu wanaofanya hivyo ni wale wenye magonjwa sugu na ambao wanashindwa kupata chakula kizuri chenye rutuba ya asili, badala ya vyakula vingi nchini humo ambavyo vimechakachuliwa.

Hivyo katika mazingira ya uchakachuaji huo ambayo yameenea nchini humo, watu wanakimbilia kwenye maziwa ya kinamama ambayo wanaona ndicho chakula halisi na cha asilia na chenye viini vingi vyenye kuimarisha afya ya binadamu.

Pamoja na hivyo, maoni ya watu ni kwamba iwapo watu wengine wanawakodisha kina mama hao kwa ajili tu ya kufanya kitu hicho kama burudani, basi kitendo hicho si cha kiungwana, lakini kama kweli wanafanya hivyo kwa ajili ya kuokoa maisha yao, hatua hiyo ni jambo jema.

Mwanajeshi wa Tanzania afa Goma- DR Congo


JESHI LA ULINZI LA WANANCHI WA TANZANIA
Simu ya Upepo  : “N G O M E”                                             Makao Makuu ya Jeshi,
Simu ya Mdomo  : DSM  22150463                                         Sanduku la Posta 9203,
Telex                     : 41051                                       DAR ES SALAAM,   29  Agosti, 2013.
Tele Fax                : 2153426
Barua pepe         : ulinzimagazine@yahoo.co.uk
Tovuti                   : www.tpdf.mil.tz
                  
TAARIFA KUHUSU TUKIO LA KUFARIKI KWA AFISA WA JWTZ KATIKA JUKUMU LA KULINDA AMANI-DRC,GOMA

1.       Kama mnavyofahamu, JWTZ linashiriki katika operesheni za Umoja wa Mataifa huko Goma DRC. Kikosi chetu kimeendelea kutekeleza majukumu yake ya kulinda amani kama kinavyopangiwa na Jeshi la Umoja wa Mataifa nchini DRC lijulikanalo kama MONUSCO.

2.       Tarehe 28 Agosti 2013 Wanajeshi wetu wakiwa katika eneo lao la Ulinzi waliangukiwa na bomu katika eneo hilo na kusababisha Majeruhi. Wakati wanapelekwa hospitali kwa matibabu, kwa bahati mbaya mwanajeshi wetu mmoja, Meja Khatibu Mshindo alifariki dunia. Majeruhi wengine wanaendelea na matibabu, na hali zao zinaendelea vizuri.
3.       MONUSCO inaandaa utaratibu wa kuleta mwili wa Marehemu.
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Habari na Uhusiano
Makao Makuu ya Jeshi.
Dar es Salaam.

Msiba! Askofu Mosses Kulola katutoka duniani

ASKOFU Mkuu wa Kanisa la Evangelistic Assemblies of God hapa nchini Dk.Moses Kulola (pichani), amefariki dunia baada ya kuugua kwa muda mrefu.
Taarifa za kifo cha askofu huyu maarufu zimetolewa na mtoto wake Mwiinjilisti Daniel Kulola ambaye ameitoa kupitia mtandao wa face book ambapo ameueleza umma wa watanzania kuwa baba yake mzazi amefariki dunia katika hospitari ya Aga Khan ambako alikuwa amelazwa.
Hajaeleza marehemu alikua anaumwa nini lakini taarifa zinasema amekuwa mgonjwa siku nyingi ambapo aliwahi kulazwa nje ya nchi na baadae akarudishwa nchini na hatimae kufariki Dunia.
Hadi hivi sasa haijajulikana askofu kulola atazikwa lini lakini pia taarifa zimethibitishwa rasmi kutoka kwa wachungaji mbalimbali ambao wako chini ya kanisa lake ambalo lina mtandao nchi nzima na lenye waumini zaidi ya milioni 5 nchini kote.
 Moses Kulola, alizaliwa mwezi Juni 1928, katika familia ya watoto kumi, na watano kati yao bado ni hai. alisajiliwa katika shule  ya kwanza mwaka 1939 iitwayo Ligsha Sukuma shule ya misheni baada ya Ligsha, alijiunga na taasisi ya usanifu mwaka 1949. Alibatizwa mwaka 1950 katika Kanisa la AIC Makongoro.
Alimwoa Elizabeth na wamezaa  watoto 10 ambapo saba bado hai.
Alianza kazi za kimisionari mwaka1950 japokuwa aliitwa mwaka 1949 mara tu baada ya kubatizwa. Mwaka 1959 alianza kufanya kazi serikalini, wakati huo huo akihubiri Injili katika miji na vijiji. 
Utumishi wake mkubwa kwa nchi ulifika mwisho mwaka 1962, ambapo aliamua kujitolea moja kwa moja nguvu zake zote, mwili na nafsi. Mwaka 1964 alijiunga na chuo cha kiteolojia na 1966 alitunukiwa stashahada.
Hakuacha elimu pale tu, aliendelea na masomo mbalimbali ambapo alitunukiwa vyeti mbalimbali katika mataifa mbalimbali.
Alihudumu kikazi kwa miaka miwili kama Mchungaji kabla ya kuwa mpentekoste mnamo 1961-1962, alifanya kazi katika kanisa la TAG 1966 mpaka 1991 ambapo aliamua kuanzishaa makanisa Evangelistic Assemblies God (EAGT), ambapo yalifanikiwa kukua kwa kasi kubwa katika nchi za Tanzania, Zambia , Malawi na kwa ujumla kuan makanisa yapatayo 4000 katika nchi mbalimbali yakiwemo makubwa na madogo.
Askofu Moses Kulola anayeongoza makanisa elfu nne, Askofu Msaidizi wake ni Mwaisabila. Mchakato wa kuongoza makanisa elfu nne si rahisi na kwamba kumefanyika mgawanyiko wa majimbo yasiyopungua 34 ya kazi na kanda tano kwa ajili ya kurahisisha kazi na kila kanda na jimbo lina mwangalizi wake. 
Nampenda sana Askofu Moses Kulola maana anafanya kazi ya MUNGU kwa moyo na kwa mujibu wa kitabu cha historia yake Askofu Kulola amezunguka Tanzania nzima tena wakati mwingine kwa kutembea kwa miguu na kwenye mazingira magumu sana kiasi kwamba ni wito mkuu wa MUNGU mkuu alionao Askofu Kulola na kwa miaka zaidi ya 60 amekuwa akihubiri neno la MUNGU na hadi sasa MUNGU anamtumia sana, katika mkutano uliopita wa askofu Kulola pale viwanja vya jangwani jijini Dar es salaam maelfu ya watu walihudhulia na wengi sana kufunguliwa na injili anayohubiri askofu Kulola na injili iliyonyooka na akiwataka wanadamu kumpa YESU KRISTO maisha yao ili wapate uzima wa milele bure.MUNGU ambariki sana mtumishi wake huyu ni mfano hai kwa watumishi wa MUNGU wa sasa.
BWANA Ametoa na BWANA pia Ametwaa Jina Lake Lihimidiwe.

Ajali tena! Kipanya chaua watu 13 Shinyanga

Kamanda Kihenya Kihenya.
ABIRIA 13 wamekufa katika ajali baada ya gari aina ya Toyota Hiace kugonga gari la mizigo lililokuwa limeharibika barabarani katika kijiji cha Ngogwa wilayani hapa.
Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Shinyanga, Kihenya Kihenya alisema jana kuwa ajali hiyo ilitokea juzi saa 2 usiku ambapo Hiace hiyo namba T 756 CHX inayofanya safari zake Kahama na Ushirombo iligonga lori hilo namba T 999 AMS.
Alisema katika ajali hiyo, watu 11 walikufa papo hapo na wawili katika hospitali ya wilaya ya Kahama wakati wakitibiwa. Kamanda alisema majina ya waliokufa hadi jana hayakuwa yamepatikana. Hata hivyo, alisema baadhi ya ndugu na jamaa walijitokeza jana jioni kutambua miili ya ndugu zao.
Kaimu Kihenya alishukuru wakazi wa kijiji cha Ngongwa kwa kutoa ushirikiano kwa Jeshi hilo baada ya ajali kutokea.  Kamanda alitaka madereva kuwa makini wanapoendesha magari hasa usiku na wawe makini wakiwa na abiria.
Kaimu Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Wilaya ya Kahama, Joseph Fwoma alithibitisha kupokea maiti 11 akiwamo dereva wa Hiace, Ezekiel Werema ambaye pia ndiye mmiliki wake. Alikiri majeruhi wawili pia kufia hospitalini hapo.
Katika hatua nyingine, Chama cha Wamiliki wa Mabasi ya Mikoani (TABOA) kimesema ajali nyingi za mabasi zinazotokea nchini, zinasababishwa na mamlaka husika, kutoa leseni kwa kampuni au wafanyabiashara bila utafiti wa kina na wao kutoshirikishwa.
Barua iliyoandikwa na chama hicho ikisainiwa na Katibu wake, Enea Mrutu kwenda wa Waziri wa Uchukuzi, Dk Harrison Mwakyembe na nakala kusambazwa kwa vyombo vya habari, ikisema pamoja na uzembe wa madereva pia kwa kiasi fulani linachangiwa na utoaji wa leseni usiofuata utaratibu, ikiwamo kupewa leseni watu wasio na sifa.
“Uwepo wa ajali nyingi barabarani ni changamoto sugu katika sekta  ya usafirishaji kwani tumejaribu mara nyingi kulikabili tatizo hili, lakini bado ajali zinaendelea kuwepo na hii inatokana na  kampuni nyingi au watu wengi kupewa leseni bila utafiti wa kina,” alisema Mrutu.
Aliendelea kushauri kupitia barua hiyo: “Tunaomba  uwepo utafiti wa kina wa kampuni  mpya kabla ya utoaji wa  leseni ya usafirishaji na Taboa  makao makuu na matawi yake mikoani washirikishwe na ipewe nguvu kama wanavyofanya Chama cha Wasafirishaji wa Malori (TATOA) kwani  hupewi leseni bila kupita kwao.”
Alisema Tatoa wameweza kusimamia ubora wa malori yanayoingizwa nchini, mwendo na kupunguza ajali za malori barabarani. 
Aidha, chama hicho kilisema kilibaini uwepo wa mabasi mengi yaendayo mikoani na ndani ya mikoa yasiyo na leseni za usafirishaji, jambo alilosema kuwa ni hatari katika sekta ya  usafirishaji hasa katika suala zima la kupunguza ajali za barabarani.
Alisema uwepo wa kampuni nyingi zinazomilikiwa na watu kutoka nje ya Afrika Mashariki zinazoingiza mabasi nchini na kupewa leseni ya biashara bila hata Taboa kupewa taarifa, unachangia kudhoofisha chama katika kusimamia taratibu za usafirishaji nchini.

Mwigulu Nchemba aanza 'chokochoko' kwa CHADEMA

 MBUNGE wa Iramba Magharibi, Mwigulu Nchemba (CCM), amechafua hali ya hewa bungeni kwa kuitaka Serikali kuwachukuliwa hatua viongozi wa juu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Mbunge huyo alisema mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe pamoja na Katibu Mkuu wake, Dk. Wilbroad Slaa, wanapaswa kuchukuliwa hatua kwa madai ya kusababisha mauaji ya raia.

Mwigulu, ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Bara, alisema katika kipindi cha miaka miwili tangu nchi ilipotoka kwenye uchaguzi, viongozi hao wamekuwa wakihamasisha maandamano na kusababisha umwagaji wa damu za Watanzania.

“Mheshimiwa Naibu Spika, katika kipindi cha miaka miwili tangu nchi yetu ilipomaliza Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2010, Mbowe na Dk. Slaa wamekuwa wakitoa kauli za wazi na hata kusababisha mauaji ya watu bila hatia.

“Kutokana na hali hii, sijui Serikali inafanya nini katika kuwachukulia hatua, kwani viongozi hawa wamekuwa wakitafuta umaarufu wa kisiasa kwa kuchochea chuki na mauaji dhidi ya raia.

“Kwa hali hiyo, tangu kipindi hicho hadi leo hii wanasubiri nini badala ya kwenda kuwaweka jela, kwani huko ndiko wanatakiwa kuwa,” alisema.

Mwigulu, alisema kukosekana kwa maadili kwa baadhi ya viongozi wa siasa, ambao wamekuwa wakitumia majukwaa na kuhubiri umwagaji damu ni hatari kwa taifa.

Alisema viongozi hao wamekuwa wakitumia majukwaa hayo na kusababisha vifo vya wananchi, huku akitaja vurugu zilizotokea katika mikoa ya Morogoro, Iringa, Arusha na Singida.

Akijibu swali hilo, Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika, alisema Serikali inafanya kazi kwa mujibu wa sheria, ikiwa ni pamoja na kukusanya ushahidi na kwamba mahakama ndicho chombo chenye uamuzi wa mwisho dhidi ya adhabu kwa raia au kiongozi yeyote wa kisiasa.

Kauli hiyo ya Mwigulu ilionekana kuchafua hali ya hewa ndani ya Bunge, ambapo Mbunge wa Nyamagana, Ezekiel Wenje (Chadema), alisimama na kuomba mwongozo wa Spika, huku akimtaka Mwigulu kuthibitisha kauli yake, vinginevyo aombe radhi.

Wenje alisema hoja ya Mwigulu imekosa mashiko na ina lengo la kuwadhalilisha viongozi wa Chadema, huku akisahau kuwa baada ya uchaguzi wa Arumeru Mashariki, aliyekuwa Mwenyetiki wa Chadema tawi la Usa River, Omari Mbwambo, aliuawa na watu anaodaiwa kuwa ni wafuasi wa CCM.

Awali katika swali la msingi, Mbunge wa Same Mashariki, Anne Kilango (CCM), alitaka kujua Serikali inachukua hatua gani kwa wanasiasa wanaokiuka maadili na kusababisha uvunjifu wa amani.

“Wanataaluma kama vile madaktari, wahandisi, wahasibu na hata wakandarasi pindi wanapokiuka maadili ya kazi zao huchukuliwa hatua kwa kufutiwa leseni zao.

“Vile vile viongozi wa kisiasa wanayo maadili yanayowaongoza, kwanini pale wanapokiuka maadili ya kazi zao hawachukuliwi hatua kama ilivyo katika makundi hayo? (taaluma),” alisema Kilango.


-Mtanzania