STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, April 1, 2014

Droo Play-offs Kombe la Shirikisho yatoka

Al Ahly iliyoangushiwa Wamorocco, watavuna nini?

DROO ya mchujo wa kucheza hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika, liemtangazwa leo mjini Cairo, ambapo waliokuwa watetezi wa Ligi ya Mabingwa Afrika, Al Ahly ya Misri imeangukia mikononi mwa Difaa Hassani Jadida ya Morocco.
Al Ahly itakutana na Wamorocco hao wakiwa na kumbukumbu ya kuvuliwa taji la Afrika na Waarabu wenzao wengine wa Libya mwishoni mwa wiki.
Ratiba hiyo pia imeziingiza mbili za Mali, AS Real na Djoliba zimepangwa pamoja katika mechi hizo. Ratiba hiyo ya upangaji wa droo leo makao makuu ya Shirikisho la Soka Afrika (CAF) mjini Cairo, Misri na kuongozwa na Katibu Mkuu wa CAF, Hicham El-Amrani aliyesaidiwa na Hazem El-Hawary, Mjumbe wa Kamati ya Mashindano ya klabu ya shirikisho hilo. Timu zilizotolewa katika Hatua ya 16 Bora ya Ligi ya Mabingwa Afrika zimepangwa na timu zilizofuzu Nane Bora ya Kombe la Shirikisho.
AS Real, waliofungwa katika Fainali ya Klabu Bingwa Afrika mwaka 1966 watamenyana na wapinzani wao wa jadi, Djoliba, waliofungwa kwenye ya Kombe la Shirikisho miaka miwili iliyopita kuwania kuingia Hatua ya makundi.
Medeama ya Ghana itamenyana na mabingwa wa mwaka 2012, AC Leopards ya Kongo wakati Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini itamenyana na vigogo wa Ivory Coast, ASEC Mimosas.
Mabingwa wa Cameroon, Coton Sport watamenyana na Petro Atletico ya Angola wakati Etoile du Sahel ya Tunisia itamenyana na Horoya ya Guinea.
Bayelsa United ya Nigeria itamenyana na Sewe Sport ya Ivory Coast katika pambano la timu za Magharibi mwa Afrika tupu, wakati Nkana ya Zambia itamenyana na Club Athletique Bizertin ya Tunisia.

Ratiba kamili ya mchujo huo kuwania kutinga hatua ya makundi ni kama ifuatavyo:
Al-Ahly (Misri) vs Difaa Hassani Jadida (Morocco)
AS Real (Mali) vs Djoliba (Mali)
AC Leopards (Kongo) vs Medeama (Ghana)
Kaizer Chiefs (Afrika Kusini) vs ASEC Mimosas (Ivory Coast) 
Coton Sport (Cameroon) vs Petro Atletico (Angola)
Horoya (Guinea) vs Etoile du Sahel (Tunisia)
Sewe Sport (Ivory Coast) vs Bayelsa (Nigeria)
Nkana (Zambia) vs Club Athletique Bizertin (Tunisia)
(Mechi za kwanza zitachezwa kati ya Aprili 18, 19 na 20 wakati marudiano itakuwa kati ya Aprili 25, 26 na 27,mwaka 2014

Fully Maganga ashukuru kutimiza ahadi kuitungua Yanga

Fully Maganga akiwajibika uwanjani
MSHAMBULIAJI nyota wa Mgambo JKT, Fully Maganga, amesema amefurahi na kumshukuru Mungu kwa kufanikiwa kutimiza ahadi yake ya kuwatungua Yanga kwenye uwanja wa Mkwakwani kama alivyoahidi.
Maganga alinukuliwa na MICHARAZO mara alipotoka kuwatungua Simba katika  pambano lao lililochezwa Februari 9, akidai ni lazima angeifunga Yanga na kufanikiwa kufanya hivyo Jumapili Mgambo walipoilaza Yanga mabao 2-1.
Mchezaji huyo alisema anajiamini kwa uwezo wake mkubwa kisoka na ndiyo maana alitoa onyo mapema na anashukuru kufanikiwa kutimiza ahadi hiyo kwa kuiwezesha Mgambo kuwanyamazisha watetezi hao kama Simba.
"Namshukuru Mungu kwa kunisaidia kutimiza ahadi yangu, niliitahadharisha Yanga kwamba ni lazima nitawatungua, nadhani walipuuza na wamekiona kilichowakura Jumapili. Nimefurahi sana kuwafunga," alisema.
Alisema anaamini bao lake lililokuwa la mapema katika pambano hilo ndilo lililowachanganya watetezi hao na kujikuta wakipoteza mchezo huo uliokuwa wa pili kwao kwa msimu huu baada ya Azam kuwafanyizia duru la kwanza.
"Nadhani bao langu liliwavuruga Yanga na kushindwa kujipanga na hilo lilitusaidia kuwazima na kuwapotezea mipango yao ya ubingwa, ingawa bado wanayo nafasi kama wakijipanga vyema kwa mechi zilizosalia," alisema.
Yanga iliyokuwa ikihitaji ushindi katika mchezo huo wa Jumapili ilijikuta ikilala 2-1 licha ya wapinzani wao kucheza pungufu kwa muda mrefu baada ya mashambuliaji wao Mohammed Netto kulimwa kadi nyekundu kwa tuhuma za kuwa na kitu kwenye jezi yake.

TFF waahirisha pambano la Azam vs Ruvu Shooting

Ruvu waliokuwa waikaribishe Azam uwanja wa Mabatini
Azam iliyoomba kuahirishiwa mechi yao ya Jumapili
PAMBANO la Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara kati ya Azam FC na wenyeji Ruvu Shooting lililokuwa lichezwe Aprili 6, mwaka huu Uwanja wa Mabatini, Mlandizi mkoani Pwani kusogezwa mbele hadi Aprili 9, imefahamika.
Tovuti ya Azam FC imemnukuu Katibu wa klabu hiyo, Nassor Idrisa ‘Father’ akisema kwamba, sababu za Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kuusogeza mbele mchezo huo ni Azam FC kuwa na wachezaji wengi katika kikosi cha timu ya taifa ya vijana chini ya umri wa miaka 20, Ngorongoro Heroes.
Ngorongoro Heroes inatarajiwa kuondoka keshokutwa nchini kwenda Nairobi, Kenya kwa ajili ya mechi ya kuwania kucheza Fainali za Vijana Afrika, itakayochezwa Jumapili ya Aprili 6 mwaka huu Uwanja wa Machakos ulioko kilometa 80 kutoka jijini Nairobi na Azam ina wachezaji zaidi ya watano kwenye kikosi hicho.
Hao ni Aishi Manula, Bryson Raphael, Gardiel Michael, Kevin Friday, Mudathir Yahya, Farid Mussa na Hamad Juma. Wachezaji waliobaki wa Azam FC wanaendelea na mazoezi Uwanja wa Azam Complex, Chamazi, Dar es Salaam.
Azam FC inaongoza Ligi Kuu kwa pointi zake 53 baada ya kucheza mechi 23, ikifuatiwa na Yanga SC yenye pointi 46 za mechi 22 na Mbeya City yenye pointi 45 za mechi 23.
Yanga SC itacheza na JKT Ruvu Jumapili Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wakati Mbeya City itacheza na Ashanti United Jumamosi Uwanja wa Azam Complex, Dar es Salaam.

Mikoa 10 yawasilisha mabingwa wao RCL

http://arushafc.com/wp-content/uploads/2014/01/AFC-6-640x360.jpg
AFC Arusha miongoni mabingwa wa mikoa ambao majina yao yamewasilishwa TFF
VYAMA vya mpira wa miguu vya mikoa kumi vimewasilisha majina ya mabingwa wao watakaoshiriki Ligi ya Mabingwa wa Mikoa (RCL).
Mabingwa hao ni Arusha (AFC), Kilimanjaro (Panone FC), Lindi (Kariakoo SC), Manyara (Tanzanite SC), Mara (JKT Rwamukoma), Morogoro (Volcano FC), Mtwara (Pachoto Shooting Stars), Pwani (Kiluvya United), Shinyanga (Bulyanhulu FC), Singida (Singida United) na Tanga (African Sports).
Mikoa ambayo haijawasilisha mabingwa wake ni Dar es Salaam, Dodoma, Geita, Iringa, Kagera, Katavi, Kigoma, Mbeya, Morogoro, Njombe, Rukwa, Ruvuma, Simiyu na Tabora wakati mikoa ya Dodoma na Mwanza imeomba kuongezewa muda kutokana na sababu mbalimbali.
Kamati ya Mashindano ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) iliagiza kuwa mikoa yote iwe imemaliza ligi na kuwasilisha jina la bingwa wake Machi 30 mwaka huu.

Ngorongoro Heroes kuwafuata Wakenya kwao

KIKOSI cha watu 27 wakiwemo wachezaji na benchi la ufundi cha timu ya Taifa ya vijana wenye umri chini ya miaka 20 (Ngorongoro Heroes) kinatarajia kuondoka keshokutwa (Aprili 3 mwaka huu) kwenda Nairobi, Kenya.
Ngorongoro Heroes inayofundishwa na John Simkoko ipo kambini tangu Machi 23 mwaka huu kujiandaa kwa mechi dhidi ya Kenya (U20). Mechi hiyo ya michuano ya Afrika kwa vijana wenye umri huo itachezwa Jumapili (Aprili 6 mwaka huu) saa 10 kamili jioni Uwanja wa Machakos ulioko kilometa 80 kutoka jijini Nairobi.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam leo (Aprili 1 mwaka huu), Kocha Simkoko amesema wachezaji wake wapo tayari kwa ajili ya mechi hiyo, na nia ni kupata matokeo mazuri kabla ya mchezo wa marudiano utakaochezwa nchini wiki tatu baadaye.
Kikosi cha Ngorongoro Heroes chenye wachezaji 20 na viongozi saba kitaondoka saa 4.30 asubuhi kwa ndege ya Kenya Airways. Msafara wa timu hiyo utaongozwa na mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Ayoub Nyenzi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Mpira wa Miguu wa Vijana.
Mechi hiyo itachezeshwa na waamuzi Abdoulkarim Twagiramukiza, Ambroise Hakizimana, Raymond Bwiliza na Louis Hakizimana wote kutoka Rwanda wakati Kamishna ni Maxwell Mtonga wa Malawi.
Ngorongoro Heroes itaagwa kesho (Aprili 2 mwaka huu) saa 5 asubuhi kwenye ofisi za TFF.

Abdi Banda: Mtoto wa beki wa zamani Africans Sports anayetesa Coastal

Abdi Banda kazini
Abdi Banda akichuana na Salim Kinje wa Simba katiuka ligi ya msimu uliopita
KAMA ilivyokuwa kwa baba yake, Hassan Banda nyota wa zamani wa Africans Sports ya Tanga na Taifa Stars, ndivyo ilivyo kwa Abdi Banda beki wa kutumainiwa wa Coastal Union.
Beki huyo chipukizi aliyejaliwa umbile refu lenye nguvu na lililojengeka kimichezo, amekuwa gumzo tangu aanze kuonekana kwenye ligi kuu ya Bara msimu uliopita.
Kipaji kikubwa cha soka, uwezo wa kupiga chenga, mbio na umahiri wa kukaba washambuliaji wasumbufu imemfanya beki huyo kutokosekana kwenye kikosi cha kwanza cha timu hiyo kilichosheheni nyota.
Cha ziada alichonacho beki huyo ambaye huenda Simba inaendelea kumuota baada ya kipigo cha  cha 1-0 kutoka kwa Coastal wiki iliyopita, ni kipaji cha kufumania nyavu.
Msimu huu nyota huyo mwenye ndoto za kucheza soka la kulipwa nje ya nchi amefunga bao moja na msimu uliopita alifunga mabao mawili.
Katika pambano dhidi ya Simba, Banda alishirikiana na mabeki wenzake kuwafunika nyota wa Msimbazi walioongozwa na Amissi Tambwe, Haruna Chanongo na Ramadhani Singano 'Messi'.
Licha ya kuwazima Simba, Banda anasema mechi anayoikumbuka ni ile ya duru la kwanza dhidi ya Yanga iliyochezwa Uwanja wa Taifa na Coastal kuchomoa bao 'jioni' kwa penalti, na kuibua vurugu kubwa kutoka kwa mashabiki wa mabingwa watetezi hao.
"Tukio lile la kuchomoa bao na kuwakera mashabiki wa Yanga kiasi cha kulishambulia gari letu na kulivunja kioo linanifanya niikumbuke mechi ile iliyoisha kwa sare ya 1-1," anasema.
Banda, 19, anasema soka la Tanzania linaweza kupanda kama vijana wakipewa nafasi.
Beki huyo aliyekuwa akivutiwa kisoka na marehemu Patrick Mafisango, anasema mfumo wa soka la vijana ukipewa nafasi zaidi utaleta ukombozi na kurejesha heshima kimataifa.
Pia aliwataka viongozi wa soka nchini kuwathamini wachezaji wazawa badala ya kuendekeza tabia za kuwazimia 'mapro' hata kama wana viwango ambavyo havitofautiani na vya wachezaji wa nyumbani.
Banda alipitia katika mfumo wa ukuzaji soka kwa vijana akianzia Kombez Academy na Africans Sports kabla ya kutua Coastal.
Anasema akiwa Africans Sports ndiyo alipopewa misingi imara ya soka, hasa baada ya kuwa chini ya ulezi na umeneja wa Abdul Bosnia.
"Siwezi kumsahau Abdul Bosnia, kocha Khalfan aliyeninoa Kombez na familia yangu ambayo imekuwa ikinipa sapoti; wakinitia moyo katika mbio zangu za kufika mbali kisoka," anasema.
Banda anawataka wachezaji wenzake kuzingatia nidhamu ndani na nje ya uwanja, kupenda kufanya mazoezi na kupigana 'jihad' uwanjani ili kuzisaidia timu na kujitangaza wenyewe sokoni.
Banda anasema Taifa Stars inaweza kufuzu kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika za mwakani kama ikitafutiwa mechi nyingi za kujipima nguvu za ndani na nje ya nchi.
Mchezaji wa kimataifa huyo alikuwemo katika kikosi cha timu ya taifa ya shirikisho la soka, 'TFF Stars', kilichocheza mechi ya kirafiki dhidi ya Namibia na kutoka sare 1-1 jijini Windhoek mapema mwezi huu.
Anasema uteuzi huo wa 'TFF Stars' ndilo tukio la furaha kwake kwani kabla ya hapo hakuwahi kuitwa hata timu za taifa za vijana na kuwashukuru viongozi wa TFF waliotambua kipaji chake na kumpa nafasi hiyo.

Hamad Juma: Beki Coastal aliyeitungua Simba anayemlilia Mafisango

Hamad Juma akichuana na Ramadhani Singano 'Messi' wa Simba katika picha tofauti
KABLA ya kuwatungua Simba katika pambano la Ligi Kuu Tanzania Bara lililochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam wiki iliyopita, jina la Hamad Juma halikuwa maarufu masikioni mwa mashabiki wa soka.
Hata hivyo, mkwaju aliyomtungua kipa mkongwe na mzoefu nchini, Ivo Mapunda na kuipa ushindi timu yake ya Coastal Union, umelifanya jina la beki huyo wa pembeni kuwa gumzo midomoni mwa watu.
Hamad alifunga bao hilo pekee dakika moja kabla ya mapumziko baada ya kuuwahi mpira uliozembewa kuokolewa na Omar Salum, kisha kufumua shuti lililotinga likimuacha Ivo akigaragara mavumbini.
Mbali na kufunga bao hilo pekee, Hamad na wenzake pia walikuwa mwiba mkali kwa nyota wa Simba walioongozwa na Jonas Mkude, Ramadhani Singano 'Messi', Amisi Tambwe na Haruna Chanongo.
Beki huyo na wenzake walicheza 'jihad' wakianua kila aina ya hatari langoni mwao, huku kipa wao Fikirini Seleman akionyesha manjonjo yake na kuisaidia kuipa Coastal ushindi muhimu mbele ya Simba.
Ingawa beki huyo hakumaliza pambano hilo baada ya kutolewa katika dakika ya 60 kutokana na kuumia, lakini bao lake lilidumu hadi mwisho na kuifanya Simba ipoteze mchezo wake wa nne kwa msimu huu.
Hamad miongoni mwa wachezaji chipukizi waliopandishwa na Coastal msimu huu kutoka kikosi cha vijana, anasema anajisikia furaha kubwa kwa kufunga bao hilo pekee katika pambano hilo kali.
"Najisikia faraja kubwa kuweza kuifunga Simba, kwa sababu ni bao langu la kwanza, pia Simba ni timu kubwa iliyosheheni wachezaji nyota wa ndani na nje ya nchi. Ni furaha kubwa kwangu," anasema.
Beki huyo anasema hakutarajia kama angefunga bao hilo, licha ya maamuzi aliyoyafanya ya kufumua shuti baada ya kuuotea mpira langoni mwa wapinzani wao.
"Mpaka sasa siamini kama ni mimi niliyewatungua Simba," anasema.

NDOTO
Hamad kama wachezaji wengine wa rika lake anasema kiu yake ni kuja kucheza soka la kulipwa nje hasa barani Ulaya,  pia kupata nafasi ya kuitumikia timu ya Taifa (Taifa Stars).
"Bado nina safari ndefu katika maisha yangu ya soka, lakini nitafurahi kama nitatimiza ndoto hizo na kufika mbali kisoka," anasema.
Mchezaji huyo anayependa kula ugali kwa samaki na kunywa juisi halisi, anasema anaamini kipaji cha soka na umri alionao utatimiza ndoto hizo za kucheza Ulaya na kuichezea Taifa Stars.
Hamad anayeishabikia timu ya Taifa ya Brazil, aliyekuwa akimzimia kisoka marehemu Patrick Mafisango aliyeichezea Simba, anasema soka la Tanzania linasonga mbele baada ya vijana kupewa nafasi.
Hata hivyo, anataka juhudi zaidi ziongezwe kwa vipaji vinavyoibuliwa kwenye michuano mbalimbali ya vijana kutunzwa na kuendelezwa ili vije kulisaidia taifa hasa kwa michuano ya kimataifa.
"Vipaji visiachwe vipotee, vitunzwe na kuendelezwa kwani ni hazina itakayolisaidia taifa baadaye," anasema.

FURAHA
Beki huyo anayewashukuru wazazi wake na wote waliomsaidia kufika  alipo, anasema hakuna tukio la furaha kwake kama siku alipopewa nafasi ya kucheza pambano lake la kwanza la Ligi Kuu.
"Pambano hilo lilikuwa ni kati ya Oljoro JKT na Coastal jijini Arusha likiwa la fungua dimba na kwa bahati nzuri tuliibuka na ushindi wa mabao 2-0 ugenini," anasema.
Juu ya huzuni mchezaji huyo anayewataka wachezaji wenzake kuzingatia nidhamu ndani na nje ya uwanja, kupenda mazoezi na kuwasilikiza makocha wao, anasema ni lile la kumpoteza baba yake.
"Kumpoteza baba kabla hajaanza kula matunda ya mafanikio yangu kisoka kunaniuma, huzuni hiyo ni sawa na nilipoumia na kukaa nje ya dimba kwa muda kabla ya kupona," anasema.
Hamad anayependa kutumia muda wake wa ziada kusikiliza muziki akimzimia Sir Juma Nature, anasema kama siyo soka huenda angekuwa imamu wa msikiti kutokana na kupenda mambo ya ibada.

CHIMBUKO
Hamad Juma Hamis, alizaliwa Februari 25, 1994 mjini Tanga na alianza kucheza soka tangu akiwa kinda wakati akisoma Shule ya Msingi Darajani na kuendelea Sekondari ya Jumuiya zote za mjini Tanga.
Beki huyo anasema timu yake ya kwanza kuichezea ni Tanga Middle Age kabla ya kuonwa na Coastal iliyomchukua ili kuichezea timu ya vijana hadi msimu huu alipopandishwa timu ya wakubwa.
Kabla ya kupandishwa timu ya wakubwa, Hamad aliisaidia Coastal Union kufika fainali ya Kombe la Uhai na kushika nafasi ya pili kabla ya msimu huu kikosi hicho kutwaa taji kwa kuilaza Yanga.
Hamas anasema hakuna mchezaji anayemuogopa uwanjani kwa kuwa anajiamini kwa kipaji alichojaliwa na Mungu na kukiri mpaka leo bado anamkumbuka marehemu Mafisango kutokana na kumzimia mno.
Anasema Mafisango alikuwa mkali na mwenye kipaji kikubwa cha soka kabla ya kipaji hicho kukatishwa na ajali ya gari iliyotokea Mei mwaka juzi.
"Yule jamaa achana naye, alikuwa anajua soka na alikuwa kivutio kwangu, Mungu amlaze pema," anasema Hamad.
Hamad anawashukuru makocha wake wote waliomnoa tangu shuleni mpaka kufika alipo, kadhalika anaushukuru uongozi wa klabu yake na wachezaji wenzake kwa ushirikiano wanaompa.

Maria Soloma; Kimwana wa Manywele anayetamba Extra Bongo

Maria Soloma

Akiwajibika jukwaani
SHINDANO la Kimwana wa Manywele wa Twanga Pepeta la 2006-2007 ndilo lililomuibua mwanadada Maria Joseph Soloma.
Katika shindano hilo, Maria alifanikiwa kushika nafasi ya pili nyuma ya Lulu Mathias Semagongo maarufu kama Aunty Lulu na kuacha gumzo kubwa kwa umahiri wake wa kuzungusha nyonga jukwaani.
Licha ya kutoibuka kidedea katika shindano hilo, lakini kipaji kikubwa alichokuwa nacho kilimsaidia kupata 'ulaji' mwanadada huyo baada ya  bendi ya African Stars 'Twanga Pepeta' kumpa ajira ya kudumu.
Maria alichukuliwa na Twanga Pepeta kama mnenguaji na kukaa na bendi hiyo mpaka hivi karibuni alipoamua kuhama na kutua Extra Bongo 'Wana Kimbembe'.
Kisura huyo aliyejiwekea malengo ya kuja kuwa muimbaji mara baada ya viungo vyake kuchoka kunengua, anasema masilahi na kutaka kubadilisha hali ya hewa ndicho kilichomhamisha Twanga Pepeta.
"Masilahi na kutaka kubadili hali ya hewa vilinifanya niondoke Twanga na kutua Extra Bongo. Nafurahi maisha ndani ya Extra ni mazuri, kuna ushirikiano wa kutosha na tunaishi kama ndugu," anasema.

DHANA
Maria anayefurahishwa na tukio la kujifungua mwanae kipenzi, Zahra aliyezaa na muimbaji nyota nchini, Mwinjuma Muumin, anasema hujisikia vibaya jinsi jamii inavyojenga dhana mbaya dhidi ya wasanii.
Anasema baadhi ya wanajamii wamekuwa wakiwadharau wasanii wa kike na kuwachukulia kama watu wanaojiuza bila kujua kwamba sanaa ni kazi yao kama kazi nyingine zinazowaingizia watu riziki zao.
"Kwa kweli jambo hilo huwa silifurahii kwani ni sawa na udhalilishaji, hata kama kuna watu wachache kati yetu wanafanya uhuni, hiyo isichukuliwe ni tabia ya watu wote," anasema.
Anasema suala la wahuni kama kwenye maofisi wapo kutokana na hulka ya mtu na kusisitiza sanaa ni kazi kama kazi nyingine na yeye anaiheshimu kwa vile imemsaidia kwa mengi kimaisha.
Maria anayelizwa na vifo mfululizo vya familia yake ikiwamo cha baba yake na dada zake wawili, anasema hata hivyo kuna haja ya wasanii wenzake kujiheshimu na kuepuka mambo ya upuuzi ili waheshimiwe.
"Kama tusipojiheshimu sisi wenyewe ni vigumu kuheshimiwa, baadhi ya matendo ya wenzetu kwa kutojiheshimu imefanya tudharauliwe na kuonekana wote ni wahuni kitu ambacho siyo cha kweli," anasema.
Anasema kutojiheshimu kwa wasanii na kujihusisha na mambo ya hovyo imechangia wazazi na walezi kuwabania watoto wao wenye vipaji kujiingiza kwenye sanaa kwa hofu ya kuharibikiwa.

KIPAJI
Maria ambaye ni shabiki mkubwa wa Simba anayependa kula ugali kwa mlenda, anasema kipaji cha sanaa alianza kukidhihirisha tangu akiwa shule ya msingi.
Anasema alikuwa akiimba na kucheza ngoma, kuimba kwaya na kuigiza, lakini alikuja kujikita kwenye unenguaji kwa kuvutiwa na Lilian Internet na Aisha Madinda aliwahi kufanya nao kazi Twanga Pepeta.
"Hawa ndiyo waliochochea mimi kujikita kwenye unenguaji, ndipo mwaka 2006 nilipoingia kwenye shindano la Manywele na kuanzisha safari ndefu mpaka hapa nilipo," anasema.
Anasema kiu yake kubwa ni kufika mbali kisanii na hasa kuja kuwa muimbaji akidai ameanza kujifunza taratibu ndani ya bendi yake ya Extra Bongo.
Maria, anayewashukuru watu wote waliomsaidia kufika alipo anasema muziki wa Tanzania unazidi kupiga hatua kubwa, jambo bado kuna tatizo la kukosekana ubunifu unaoweza kuutrangaza kimataifa.
"Lazima wasanii na wanamuziki wawe wabunifu zaidi ili kuhimili ushindani wa soko la kimataifa," anasema.
Pia anavitaka vyombo vya habari kutoa nafasi sawa kwa miondoko yote ya muziki badala ya kuegemea kwenye muziki wa kizazi kipya tu na taarab na kuutupa mkono dansi na muziki asilia.
Kadhalika aliiomba serikali kusaidia kuwapigania wasanii kuepukana na unyonyaji na wizi wanaofanyiwa na baadhi ya watu waliohodhi soko la sanaa nchini ili wasanii waweze kunufaika na jasho lao.
===============

Magaidi wailipua tena Kenya, sita wafa

 

MILIPUKO mitatu katika mji mkuu wa Kenya wa Nairobi imesababisha vifo vya watu 6 na karibu darzeni mbili kujeruhiwa jumatatu usiku katika mtaa mkubwa wenye wakazi wengi wa asili ya Kisomali wa Eastleigh.     

Mkuu wa polisi wa County ya Nairobi Benson Kibue anasema milipuko hiyo ilitokea takriban saa moja na nusu usiku  na kwa karibu wakati mmoja katika migahawa ya Sheraton Café na The New Kwa muzairua Grill.


Kufuatana na mmiliki wa Sheraton Café Bw. Patrick Gakuyu watu walikuwa wanatizama taarifa ya habari ya saa moja kwenye televisheni wakati aliposikia milipuko miwili na umeme kuzimika na kuwa katika kiza. Anasema anadhani ni grunetti mbili zilizorushwa ndani ya mgahawa wake.


Jumapili usiku karibu na mtaa huo mtu anayedhaniwa ni gaidi aliuwawa alipokuwa anatengeneza milipuko yake pamoja na wenzake watatu. Na gruneti moja ilipatikana siku hiyo hiyo ya jumapili katika mji wa pwani wa Lamu ndani ya kanisa moja.


Usalama umeimarishwa katika miji mikuu ya Kenya na hadi hivi sasa haijulikani aliyehusika na mashambulio ya jumatatu.
Voa