STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, June 26, 2011

MCHANYATO WA MICHARAZO

Tisa wamwagwa Mtibwa Sugar

KLABU ya soka ya Mtibwa Sugar, imetangaza kuwatema wachezaji wake 9 akiwemo mkongwe Faustine Lukoo na kipa Soud Slim waliomaliza mkataba wa kuichezea klabu hiyo.
Kwa mujibu wa Msemaji wa klabu hiyo, Thobias Kifaru, baadhi ya wachezaji wengine waliopewa mkono wa kwaheri katika mashamba ya Manungu, Morogoro ni winga Julius Mrope aliyeenda Yanga na Obadia Mungusa aliyesajiliwa na Simba.
Kifaru, aliwataja wachezaji wengine ni Yusuph Mgwao, Yona Ndabila anayeenda kucheza soka la kulipwa nje ya nchi, Mganda Boban Zilintusa waliyeshindwa kumtumia kwa kukosa ITC, ambaye walimsajili na kushindwa kumtumia kwa kukosa ITC, na Lameck Dayton.
"Tumeacha jumla ya wachezaji tisa, akiwemo mkongwe Faustine Lukoo baada ya kumaliza mikataba ya kuitumikia klabu yetu na wengine kuhamia klabu zingine za Ligi Kuu, ila Ndabila aliyekuwa na mkataba aliomba kusitisha kwa vile anataka kwenda kucheza soka nje," alisema.
Hata hivyo Kifaru hakuweka bayana juu ya wachezaji Salum Machaku na kipa Shaaban Kado ambao wametajwa kutua kwa watani wa jadi wa soka la Tanzania, Simba na Yanga kwa msimu ujao wa ligi kuu.
Machaku anayeichezea pia timu ya taifa, Taifa Stars imedaiwa amesajiliwa Simba na Kado anayechezea timu za vijana U20 na ile ya wakubwa tayari imethibitishwa amenyakuliwa na Yanga kwa ajili ya msimu ujao utakaoanza Agosti 20 mwaka huu.
***

Fainali Pool Taifa zaiva


FAINALI za taifa za mchezo wa pool za 'Safari Lager National Pool Champioship 2011' zinatarajia kuanza mwezi ujao.
Kwa mujibu wa Meneja wa bia ya Safari Lager, Oscar Shelukindo, fainali hizo zitafanyika kati ya Julai 27-30 kwenye ukumbi wa Kilimani mkoani Dodoma.
Shelukindo alisema, fainali hizo zitatanguliwa na mashindano ya ngazi za mikoa yatakayoanza Juni 30 hadi Julai 17, ikishirikisha mikoa 14 ya Tanzania Bara.
Alisema mara baada ya mashindano hayo kukamilika katika ngazi za mikoa kila mkoa utaunda kombaini ya wachezaji kwa ajili ya kuwakilisha kila mkoa katika ngazi ya fainali hizo za taifa.
Shelukindo alisema bingwa wa fainali hizo atanyakulia Sh.mil. 5, mshindi wa pili ataondoka na mil. 3, mshindi wa tatu Mil. 2 na mshindi wa nne Mil 1.
Aliongeza fainali hizo ambazo zitahusisha na wachezaji mmoja mmoja wanaume na wanawake, bingwa kwa upande wa wanaume atazawadiwa Sh.Sh.500,000, mshindi wa pili Sh.250,000, mshindi wa tatu Sh.200,000 na mshindi wa nne Sh.100,000
Kwa upande wa wanawake bingwa atapewa Sh.350,000, mshindi wa pili Sh.200,000, mshindi wa tatu Sh.150,000 na mshindi wa nne Sh.50,000.
Aliongeza kwa kuzitaja zawadi kwa upande wa ngazi ya mikoa kuwa bingwa atajinyakulia Sh. 700,000, mshindi wa pili ataondoka na Sh.350,000, mshindi wa tatu atazawadiwa Sh.200,000 na mshindi wa nne Sh150,000.
Kwa upande wa mchezaji mmoja mmoja ngazi ya mikoa (wanaume) bingwa atajinyakulia Sh.350,000, mshindi wa pili Sh.200,000, mshindi wa tatu Sh.150,000 na mshindi wa nne Sh.100,000,
Kwa upande wa wanawake bingwa atapewa Sh.250,000, mshindi wa pili Sh.150,000, mshindi wa tatu Sh.100,000 na mshindi wa nne Sh.50,000.
Mikoa itakayoshiriki ni mabingwa watetezi Kinondoni, Ilala na Temeke, Shinyanga, Mwanza, Kagera Mbeya, Tanga, Arusha, Kilimanjaro, Dodoma, Iringa, Manyara na Morogoro.
***

Toto Afrika yazionya Kagera, Mtibwa Sugar


KLABU ya soka ya Toto Afrika ya Mwanza imezitaka klabu zinazotaka kuwasajili nyota wao kutotumia mlango wa nyuma na badala yake zionane nao na kufanya mazungumzo.
Uongozi wa Toto, umesema umelazimika kutoa tahadhari hiyo kutokana na kuwepo kwa taarifa zinazoripotiwa na vyombo vya habari juu ya timu za Kagera Sugar na Mtibwa Sugar kuwanyakua wachezaji wao wawili nyota bila ya wenyewe kujua lolote.
Wachezaji walioufanya uongozi huo kucharuka mapema ni mshambuliaji, Husseni Sued anayedaiwa kutua Kagera Sugar na kiungo Mohammed Soud aliyevumishwa kunyakuliwa na klabu ya Mtibwa ya Morogoro.
Katibu wa klabu hiyo, Salum Kaguna, alinukuliwa hivi karibuni akisema kuwa, hawana taarifa zozote za wachezaji hao kunyakuliwa na timu hizo kwa vile hakuna mazungumzo yoyote yaliyofanywa hadi ssa baina yao na klabu hizo.
Kaguna, alisema ni vema klabu zinazowataka wachezaji ziende mezani kuzungumza kwa sababu nyota hao wana mikataba na hivyo hawatakuwa radhi waondoke kienyeji.
"Hatuzuii wachezaji wetu kuondoka kama wamepata timu, muhimu ni taratibu zifuatwe, mfano Soud anayetajwa kutua Mtibwa, yeye ana mkataba wa miaka mitatu ya Toto akiwa ametumikia miaka miwili na kubakisha mmoja utakaoisha mwakani," alisema Kaguna.
Viongozi wa Mtibwa na Kagera hawakupatikana kuweka bayana kinachoendelea juu ya harakari zao za kuwanyakua wachezaji hao na onyo hilo la uongozi wa Toto Afrika ambayo imekuwa ikijinadi imepania kufanya kweli msimu ujao katika Ligi Kuu Tanzania Bara.
***

TAVA yapongezwa, yashauriwa


CHAMA cha Mpira wa Wavu nchini, TAVA, umepewa 'kifyagio' kwa kujitahidi kurejesha hadhi ya mchezo huo, lakini kikashauriwa kuwekeza nguvu zao ngazi za chini hususani katika mashule ili kuzalisha nyota wa baadaye watakaoisaidia Tanzania kimataifa.
Kifyagio na ushauri huo umetolewa na mchezaji nyota wa zamani wa klabu ya Jeshi Stars, Ibrahim Christopher 'Michael Power' alipozungumza na MICHARAZO na kusema uongozi wa TAVA umekuwa ukijitahidi katika hali ya mazingira magumu kuinua tena mchezo huo nchini.
Christopher, alisema kukosekana kwa wadhamini ni tatizo lililochangia kuufanya mchezo wa wavu kudodora, lakini jitihada za viongozi wa chama chao umesaidia kuendesha michuano ya kitaifa na kimataifa jambo la kupongezwa.
Alisema hata hivyo bado TAVA inapaswa kuelekeza nguvu zao katika ngazi za chini kusaka nyota wa baadae ikiwezekana kuendesha michuano katika shule za msingi na sekondari ili kuwapa morali vijana kujitosa kwenye mchezo huo.
"Kwa kweli TAVA inafanya kazi katika mazingira magumu kwa kutokuwa na wafadhili wala wadhamini, lakini bado naiomba waelekeza nguvu zao kwa vijana toka ngazi za chini ili waje kuchukua nafasi zetu kuendelea mchezo huu," alisema.
Nyota huyo aliyeisadia Mzinga ya Morogoro kutwaa taji la Ligi ya Muungano lililofanyika mjinio Tanga, alisema kadhalika wachezaji na viongozi wa zamani wa mchezo huo wanapaswa kujitokeza kuusaidia uongozi wa sasa katika kuhakikisha wavu inarejesha makali yake.
"Viongozi na wachezaji wa zamani wamejiweka kando, wanapaswa kutoka mafichoni kusaidiana na TAVA kurejesha makali ya mchezo huo," alisema.
***


'Wazee wa Kizigo' wapata meneja


BENDI ya Extra Bongo 'Wazee wa Kizigo', imepata meneja ambaye atabeba jukumu la kusimamia shughuli zote za bendi hiyo ili isonge mbele kufikia malengo ya kuwa matawi ya juu.
Kiongozi wa bendi hiyo Rogert Hegga, alimtaja meneja huyo mpya kuwa ni Mujibu Hamis aliyewahi kuifanya kazi katika bendi za FM Acdeamia na Mashujaa Musica.
Hegga alisema, kwa vile Mujibu ni mzoefu wa kazi hiyo kwa muda mrefu, ana uhakika mchango wake utakuwa mkubwa ndani ya Extra Bongo ambayo inazidi kupanda chati kila kukicha.
"Fitina za muziki anazijua sana na sisi tunaamini kwamba tukiwa naye kwenye bendi yetu ya Extra Bongo tutaendelea kupiga hatua zaidi ili kufikia malengo ambayo tumejiwekea," alisema Hegga.
Alisema, Extra Bongo haikuwa na meneja hali ambayo ilikuwa inachangia baadhi ya shughuli za bendi kukwama na kwamba sasa amempata Mujibu ambaye atatumia uzoefu wake kusimamisha maendeleo ya Extra Bongo.
Katika hatua nyingine kiongozi huyo alisema, Extra Bongo imeanzisha ushirikiano wa maonyesho ya pamoja na vikundi mbalimbali vya burudani ili kujenga urafiki kati ya wanamuziki wake na wasanii wa vikundi hivyo.
Alisema ushirikiano huo ulianza wiki iliyopita kwa kufanya onyesho la pamoja na vikundi vya Baikoko, Kiti Tigo, Werawera na Khanga Moja ambavyo vina umaarufu miongoni mwa mashabiki wa burudani.

Sikinde yabakisha mbili albamu mpya





BENDI kongwe ya muziki wa dansi ya Mlimani Park 'Sikinde' imebakisha nyimbo mbili kabla ya kukamilisha albamu mpya itakayokuwa na nyimbo sita.
Katibu wa bendi hiyo, Hamis Milambo, alisema hadi sasa bendi yao imekamilisha nyimbo nne ambazo zilitarajiwa kutambulishwa jana kwa mashabiki wao katika onyesho maalum la uzinduzi wa vyombo vyao.
Milambo alizitaja nyimbo hizo nne zilizokamilika kuwa ni 'Jinamizi la Talaka', 'Mihangaiko ya Kazi', 'Kinyonga' na 'Deni Nitalipa'.
"Tumekamilisha nyimbo nne ambazo tutazitambulisha kwa mashabiki wetu na mbili za mwisho tayari zimeshaandikwa mashairi ingawa hazijapewa majina yake," alisema Milambo.
Alisema nyimbo hizo za awali zimetungwa na waimbaji wao mahiri akiwemo mkongwe, Hassani Rehani Bitchuka na wengineo.
Tangu ilipopakua albamu ya 'Supu Imetiwa Nazi', Sikinde haijapakua albamu nyingine tena mpya na hivi karibuni iliondokewa na mtunzi na muimbaji wake nguli, Shaaban Dede aliyetua kwa mahasimu wao, Msondo Ngoma ambapo ameshaibuka na nyimbo mbili mpya.
Nyimbo hizo ni 'Suluhu' uliowekwa kwenye albamu mpya ya Msondo na kingine cha 'Vita Dhidi ya Dawa za Kulevya' uliowekwa kiporo kwa albamu ijayo ya bendi hiyo.

Jumbe ahidi Talent kufanya makubwa Kilwa Masoko

MWANAMUZIKI nyota wa bendi ya Talent 'Wazee wa Kuchechemea', Husseni Jumbe, amejigamba kuwa atafanya makamuzi ya haja kwenye onyesho la bendi yake litakalofanyika Jumatano ijayo mji wa Kilwa Masoko, mkoani Lindi.
Jumbe na bendi yake wanatarajia kwenda kutambulisha albamu yao mpya na ya pili iliyokamilika hivi karibuni katika onyesho litakalofanyika Jumatano ijayo (Juni 29) kwenye ukumbi wa Kilwa PM Resort.
Akizungumza na MICHARAZO, Jumbe, alisema wamepania kwenda kuwapa burudani wakazi wa mji huo kutokana na kwamba hiyo itakuwa ni mara yao ya kwanza kwenda mjini Kilwa.
Alisema katika onyesho hilo Talent itatambulisha albamu yao ya awali ya 'Subiri Kidogo' na ile moya iitwayo 'Shoka la Bucha' ambayo imekamilika hivi karibuni ikiandaliwa kupakuliwa video zake.
"Tumejiandaa vya kutosha kuwapa burudani wakazi wa Kilwa katika onyesho letu la Juni 29, tunaamini tutakidhi kiu ya muda mrefu ya mashabiki wa muziki wa eneo hilo," alisema Jumbe.
Jumbe, alizitaja nyimbo watakazozitambulisha katika onyesho hilo lililoratibiwa na mmiliki wa ukumbi huo, Yohana Miwa, kuwa ni 'Shoka la Bucha', 'Usiku Haulaliki', 'Kiapo Mara Tatu', 'Kilio cha Swahiba' na zile za albamu yao iliyopita ya 'Subiri Kidogo' iliyozinduliwa Novemba, 2010.
Mkongwe wa dansi alisema pia katika onyesho hilo watawapigia mashabiki watakaohudhuria nyimbo za albamu zake binafsi za 'Mapenzi ya Siri' na 'Kwetu ni Wapi', pamoja na vibao alivyowahi kung'ara navyo akiwa na bendi za DDC Mlimani Park na Msondo Ngoma.

Extra Bongo kujitambulisha Morogoro



BAADA ya ziara ya mafanikio kwenye mikoa ya Lindi, Mtwara na Pwani, bendi ya Extra Bongo 'Next Level', inatarajia kuzuru mkoani Morogoro kwa maonyesho maalum matatu ya kuinadi nyimbo mpya ikiwemo 'Watu na Falsafa' uliotungwa na Ramadhan Masanja 'Banzastone' katika miji ya Kilombero, Ifakara na Kilosa.
Ikiwa mkoani Lindi Extra Bongo ilitumbuiza katika ukumbi wa Lindi Oceanic Hoteli, Mtwara katika ukumbi mpya wa Safari Pub na Pwani katika ukumbi wa Maendeleo mjini Utete ambapo maonyesha hayo yalipata wapenzi wengi.
Akizungumza na MICHARAZO, mkurugenzi wa bendi hiyo, Ally Choki alisema kufuatia mafanikio waliopata kwenye mikoa hiyo ya kusini mwa Tanzania, wapenzi wa mkoa wa Morogoro wameitaka bendi ikatumbuize huko.
Alisema, Julai Mosi Extra Bongo itatumbuiza katika ukumbi wa Jamos Centre uliopo Ifakara kabla ya kwenda Kilombero katika ukumbi wa K2 Centre na kisha mjini Kilosa ambako itakuwa katika ukumbi wa Babilon Luxury Centre.
"Tunakwenda Morogoro baada ya kupata mafanikio katika ziara yetu mikoa ya kusini, tunaamini ziara hii inaweza kupanua milango zaidi ya Extra Bongo kupata mialiko ndani na nje ya Dar ili kusaidia wanamuziki kunufaika," alisema.
Chuki alisema hii ni mara ya pili kwa Extra kufanya ziara mkoani Morogoro, lakini alisema awali ilitumbuiza katika ukumbi uliopo mjini na kwamba hatua ya kwenda hadi wilayani ni mwanzo wa bendi yake kutembelea nchi nzima.
Wakati hayo yakiendelea, Choki alisema kabla ya kwenda Morogoro, leo bendi hiyo itafanya vitu vyake katika ukumbi wa Rufika, Tabata Segerea.

Msondo Ngoma wasaka jina la albamu yao



LICHA ya kukamilisha nyimbo zote sita zitakazokuwepo kwenye albamu yao mpya ijayo, uongozi wa bendi ya Msondo Ngoma 'Baba ya Muziki', bado haujajua albamu hiyo mpya iitwe kwa jina gani.
Msondo ambayo leo inatarajiwa kuendelea na makamuzi yao kwenye ukumbi wa TCC-Chang'ombe, Temeke, imesema inaendelea kutafakari waipe jina gani albamu hiyo ijayo.
Msemaji wa bendi hiyo, Rajabu Mhamila 'Super D', alisema wanamuziki wao wanaendelea kuumiza vichwa kutafuta jina litakalobeba albamu hiyo itakayochukua nafasi ya ile ya mwaka juzi ya Huna Shukrani'.
Super D, alisema hata hivyo siku si nyingi mashabiki wao wao watafahamu jina la albamu hiyo ambayo baadhi ya nyimbo zimekuwa zikitambulishwa kwenye maonyesho yao ndani na nje ya jijini la Dar es Salaam.
"Albamu yetu ijayo bado haijafahamika itaitwaje kwa vile wanamuziki wanaendelea kuumiza vichwa kutafuta jina lake, ila nyimbo zote sita zimeshakamilika na kuanza kutambulishwa kwa mashabiki wetu," alisema.
Alizitaja nyimbo za albamu hizo na watunzi wake kwenye mabano kuwa ni 'Lipi Jema' na 'Baba Kibebe' (Eddo Sanga), 'Dawa ya Deni (Isi'haka Katima), 'Suluhu' (Shaaban Dede), 'Nadhiri ya Mapenzi' (Juma Katundu) na 'Kwa Mjomba Hakuna Urithi (Huruka Uvuruge).

Mapacha Wa3 wajikomboa zaidi




BENDI mpya ya muziki wa dansi ya Mapacha Watatu 'Wazee wa Kuchakachua', imendelea kujikwamua kwa kufanikiwa kupata vyombo vipya vya muziki vyenye thamani ya shilingi milioni 36.
Mmoja wa Wakurugenzi wa bendi hiyo, Khalid Chokoraa alisema wamefanikiwa kununua vyombo kwa juhudi zao wenyewe na kuungwa mkono na baadhi ya mashabiki wao.
Chokora alisema, sasa bendi hiyo inatarajia kuzindua vyombo hivyo leo Jumapili katika ukumbi wa Mzalendo Pub, Kijitonyama, jijini Dar es Salaam ambapo wamealikwa watu mbalimbali akiwemo Asha Baraka.
"Tutazindua vyombo vyetu Jumapili ambapo tumewaalika Wakurugenzi wa bendi mbalimbali na wadau wa muziki wa dansi akiwemo Asha Baraka, Ally Choki, Martin Kasyanju, Mama Sakina na wengine wengi," alisema.
Mkurugenzi huyo alisema vyombo hivyo vitaanza kutumika rasmi kwenye onyesho la pamoja na bendi ya Akudo Impact ambalo linatarajiwa kufanyika Julai 2 katika ukumbi wa Vatican Sinza, jijini Dar es Salaam.
Mapacha Watatu ina albamu ya kwanza ya 'Jasho la Mtu' na sasa iko kwenye maandalizi ya albamu ya pili ikiwa imekamilisha nyimbo za 'Tangulia Shambani', 'Sumu ya Mapenzi remix', 'Mtoto wa Paka' na 'Usia wa Babu'.
Bendi hiyo ilianza kama kundi likiwa na vijana watatu ambao ni Khalid Chokoraa, Jose Mara na Kalala Junior lakini wamepiga hatua kwa kuanzisha bendi ambayo ina wanamuziki ya 10.
Baadhi ya wanamuziki hao ni Allen Kisso (solo), Jimmy London (besi), Sele Tumba (tumba), Erasto Mashine (kinanda), Mariam Bessie, Mariam Zidane, Juddy Chakachua, Mariam na Sabrina Pazi ambao wote ni wanenguaji.

Dede alia na uvivu wa mawazo katika dansi



MWANAMUZIKI mkongwe nchini, Shaaban Dede 'Mzee wa Loliondo' amewaasa wanamuziki wenzake wa dansi kutobweteka na mafanikio machache waliyonayo katika sanaa zao na badala yake waumize vichwa kubuni mambo mapya kama wanavyofanya wale wa muziki wa taarab.
Dede, alisema anawafagilia wanamuziki wa taarab kwa kubuni kitu kilichouinua muziki huo nchini toka taarab asilia hadi kuwa ya kisasa ikichezeka na kupendwa na mashabiki wengi.
Alisema kuwekwa kwa rhumba na rapu katika muziki wa taarab kumeupandisha chati na kuonyesha jinsi gani wanamuziki wa dansi walivyo na changamoto ya kuumiza vichwa kuhimili ushindani wanaoupata toka kwa miondoko hiyo ya mwambao na muziki wa kizazi kipya.
"Lazima wanamuziki waumize vichwa, wasibweteke kwa kuona muziki wetu unakubalika na watu wengi, hilo linaweza kutufanya tubaki tulipo wakati wenzetu wakisonga mbele kama ambavyo taarab walivyofanya," alisema Dede.
Dede anayeifanyia kazi Msondo Ngoma, alisema kwa kuwa wanamuziki wanaojiandaa kuwarithi wakongwe katika muziki wa dansi wanapaswa kuacha kulemaa na kasumba ya kuiga kazi za nje na badala yake wakajikita katika kutafuta vyao kama ambavyo miaka ya nyuma bendi zilivyotofautiana kimipigo na kuzoa mashabiki lukuki.
Alisema tabia ya bendi kuwa na ladha yake ya kimuziki na kujitofautisha na wengine ndio iliyozifanya Sikinde na Msondo hadi leo kuwa na mashabiki wao binafsi, kitu ambacho bendi zingine za kisasa zinapaswa kufuata mkumbo huo.

Rufita yamnasa Kibugila



BENDI ya muziki wa dansi ya Rufita Connection 'Wana Shika Hapa Acha Hapa', imepata mcharaza solo mpya ikiwa ni wiki chache baada ya Seleman Shaibu Mumba kukimbilia Twanga Pepeta.
Kwa mujibu wa rais wa bendi hiyo, Chai Jaba, mpiga solo huyo ni Abdalah Kibugila ambaye amewahi kuwa bendi mbalimbali ambapo kwa mara ya mwisho alikuwa Bwagamoyo International ya Mwinjuma Muumin.
"Seleman alikuwa mpiga solo wetu lakini ameshahama, lakini tayari tumeshapata aliyeziba nafasi yake, kazi inaendelea kama kawaida kutokana na ukweli kwamba Kibugila ni mwanamuziki siku nyingi ana uzoefu wa kutosha," alisema.
Alisema Kibugila anashiriki maonyesho ya bendi hiyo huku akizifanyia mazoezi nyimbo za bendi hiyo zikiwemo za 'Mapenzi Yanaua', 'Nilinde Nikulinde', 'Anasa', 'Shida ya Mapenzi', 'Usia', 'Acha Pupa','Mkosi Gani' na 'Mazi'.
Akielezea zaidi mipango ya bendi hiyo, Chai Jaba inajiandaa kumalizia kazi ya kurekodi nyimbo zote na kisha kuanza kushuti video na kisha zitafuatia taratibu za kuzindua albamu.
"Nina uhakika yatakwenda vizuri na inawezekana tukakamilisha kazi ya kurekodi nyimbo zetu mwezi ujao kabla ya kuendelea na kazi ya kushuti video ili tujitambulishe zaidi kwa mashabiki wa muziki wa dansi," alisema.
Aidha, alisema bendi hiyo inajiandaa kuleta wanenguaji wapya wanne kutoka Congo (DR) watakaokuja kuungana na wenzao waliopo kwa sasa ili kuongeza nguvu kwenye safu ya ushambuliaji wa jukwaa.

Gilla alia na Phiri kumzibia riziki Simba



MSHAMBULIAJI chipukizi wa Simba Salim Aziz Gilla aliyetangazwa kutafutiwa timu ya kucheza kwa mkopo msimu ujao amemlaumu aliyekuwa kocha mkuu wa klabu hiyo Patrick Phiri kuwa alichangia kufifisha nyota yake kisoka.
Gilla aliyenyakuliwa na Simba kwa mkataba wa miaka mitatu mwaka 2009 baada ya kung'ara kwenye michuano ya Kombe la Taifa, alisema kutoaminiwa na Phiri kulikopelekea kushindwa kuitumikia vema Simba ndiko kulikomfanya asifurukute.
Akizungumza na MICHARAZO, Gilla alisema hata kushindwa kuitwa kwake kwenye timu za taifa, zikiwemo za vijana, inatokana na kukalishwa benchi na Phiri.
Phiri aliondoka Simba mara baada ya kumalizika kwa ligi kuu ya Bara msimu uliopita.
"Kushindwa kuaminiwa na Phiri na kunipa nafasi ya kuonyesha uwezo wangu katika kufumania nyavu umenisababishia haya yote yanayonikuta ndani ya Simba na kukosa kuitwa hata katika timu za vijana ambazo huenda ningezisaidia," alisema Gilla.
Gilla, anayekaribia umri wa miaka 21, alisema misimu miwili aliyokuwa Simba hakuwahi kupata nafasi ya kucheza dakika 90 za mchezo wowote, kitu alichodai sio kimemvuruga akili, bali kimemnyima fursa ya kuonekana kama alivyong'ara kenye Kombe la Taifa akiwa na timu ya mkoa wa Tanga.
Katika michuano hiyo, Gilla aliibuka Mchezaji Bora, huku akiteuliwa mara mbili kuwa 'nyota' wa mchezo ukiwemo ule wa kusaka mshindi wa tatu ambapo Tanga waliilaza Mwanza mabao 2-0.
Alisema hajakata tamaa kutamba kisoka, hatahivyo.
Alisema anaamini alichokutana nacho Simba ni mtihani hivyo anajipanga ili kuendeleza kipaji chake kilichomfanya aichezee Polisi Dodoma chini ya Sekilojo Chambua kabla ya kutua Simba.

Simba yaanza kwa kusuasua Kagame, Ocean View safi



MABINGWA wa kihistoria wa michuano ya Klabu Bingwa kwa nchi za Afrika Mashariki na Kati, 'Kagame Cup' Simba ya Tanzania jana ilianza kwa kusuasua michuano hiyo baada ya kulazimishwa suluhu na Vital'O ya Burundi, katika pambano la lililofanyika kwenye Uwanja wa Taifa.
Simba inayopewa nafasi kubwa ya kutwaa ubingwa kutokana na kucheza nyumba na rekodi yake nzuri michuano hiyo inapofanyika Tanzania, imebakiza mechi dhidi ya Zanzibar Ocean View, Etincelles ya Rwanda na wawakilishi wa Eritrea -- Red Sea.
Nafasi nzuri zaidi ya kupata bao kwa Simba ambayo ilianza mchezo na wachezaji wanne wapya ilikuja mwishoni mwa kipindi cha kwanza wakati Haruna Moshi 'Boban' alipopiga mpira wa kwa tik tak uliogonga mwamba wa mabingwa wa Burundi hao kabla ya kuokolewa na mabeki.
Shuti la 'Boban' ambaye hajacheza kwa miaka miwili kutokana na mzozo wa mkataba kati yake na Gefle IF ya Sweden lilikuja kutokana na krosi ya Ulimboka Mwakingwe ambaye kama mpigaji huyo amerudi kikosini baada ya kuachwa msimu uliopita.
Mwakingwe aliuwahi mpira mikononi mwa mlinda mlango wa Vital'O kufuatia shambulizi kali kwenye lango la wapinzani wa Simba hao, pembeni mwa eneo la hatari kabla ya kupiga krosi.
Kikosi cha Simba yenye pointi moja sawa na Vital'O na ambayo bado ina matumaini ya kusonga mbele kutokana na kundi lake kuwa na nafasi tatu za kucheza robo-fainali, kilikuwa pia na mchezaji wa zamani Said Nassoro 'Cholo' na Walulya Derick.
Kocha wa Simba MOses Basena alisema ameshangazwa na matokeo ya kutofungana wakati Simba ilitengeneza nafasi nyingi katika mchezo huo. Na kweli.
Wakati Vital'O ilicheza kwa kujihami zaidi na kushambulia kwa kushitukiza mara nyingi, Simba ilikuwa na mlolongo wa mashambulizi langoni mwa warundi hao.
Kocha wa Vital'O Younde Kagabo alisema ameridhika na sare hiyo kutokana na timu yake kuwa na wachezaji 10 wapya uwanjani.
Katika mchezo wa kwanza mabingwa wa Zanzibar, Zanzibar Ocean View walianza kwa kishindo michuano hiyo baada ya kuilaza Etincelles ya Rwanda kwa mabao 3-2 na hivyo kuongoza kundi hilo la A linalohusisha timu tano.
Michuano hiyo inatarajiwa kuendelea tena leo kwa mechi za kundi B ambapo mabingwa wa soka nchini Tanzania, Simba itakwaruzana na El Merreikh ya Sudan iliyokuja kwenye michuano hiyo baada ya mabingwa wa nchi yao, Al Hilal kujitoa ili ijiandae vema na Ligi ya Mabingwa Afrika hatua ya makundi inayotarajiwa kuanza mwezi ujao.
Mechi ya Yanga na Wasudan hao ambao inakumbusha fainali za michuano hiyo za mwaka 1986 ambapo Yanga ilikomboa mabao mawili dakika mbili za mwisho wa mchezo kupitia Abubakar Salum 'Sure Boy' kabla ya kulazwa kwa mikwaju ya penati na kuliacha kombe liondoke Tanzania, itachezwa kwenye uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Pambano jingine la leo ni la kundi C michezo inayochezwa uwanja wa Jamhuri, Morogoro kwa mabingwa watetezi wa michuano hiyo, APR ya Rwanda kuumana na Ports Authority ya Djibout.