STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, June 26, 2011

Jumbe ahidi Talent kufanya makubwa Kilwa Masoko

MWANAMUZIKI nyota wa bendi ya Talent 'Wazee wa Kuchechemea', Husseni Jumbe, amejigamba kuwa atafanya makamuzi ya haja kwenye onyesho la bendi yake litakalofanyika Jumatano ijayo mji wa Kilwa Masoko, mkoani Lindi.
Jumbe na bendi yake wanatarajia kwenda kutambulisha albamu yao mpya na ya pili iliyokamilika hivi karibuni katika onyesho litakalofanyika Jumatano ijayo (Juni 29) kwenye ukumbi wa Kilwa PM Resort.
Akizungumza na MICHARAZO, Jumbe, alisema wamepania kwenda kuwapa burudani wakazi wa mji huo kutokana na kwamba hiyo itakuwa ni mara yao ya kwanza kwenda mjini Kilwa.
Alisema katika onyesho hilo Talent itatambulisha albamu yao ya awali ya 'Subiri Kidogo' na ile moya iitwayo 'Shoka la Bucha' ambayo imekamilika hivi karibuni ikiandaliwa kupakuliwa video zake.
"Tumejiandaa vya kutosha kuwapa burudani wakazi wa Kilwa katika onyesho letu la Juni 29, tunaamini tutakidhi kiu ya muda mrefu ya mashabiki wa muziki wa eneo hilo," alisema Jumbe.
Jumbe, alizitaja nyimbo watakazozitambulisha katika onyesho hilo lililoratibiwa na mmiliki wa ukumbi huo, Yohana Miwa, kuwa ni 'Shoka la Bucha', 'Usiku Haulaliki', 'Kiapo Mara Tatu', 'Kilio cha Swahiba' na zile za albamu yao iliyopita ya 'Subiri Kidogo' iliyozinduliwa Novemba, 2010.
Mkongwe wa dansi alisema pia katika onyesho hilo watawapigia mashabiki watakaohudhuria nyimbo za albamu zake binafsi za 'Mapenzi ya Siri' na 'Kwetu ni Wapi', pamoja na vibao alivyowahi kung'ara navyo akiwa na bendi za DDC Mlimani Park na Msondo Ngoma.

No comments:

Post a Comment