STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, January 16, 2013

Azam kwenda Kenya kujifua zaidi

 
BAADA ya kutwaa Kombe la Mapinduzi mwishoni mwa wiki visiwani Zanzibar, Azam FC inatarajiwa kuondoka nchini Alhamisi kwenda Nairobi, Kenya kwa ziara ya wiki moja ya michezo ya kirafiki, kujiandaa na mzunguko wa pili wa Ligi Kuu na Kombe la Shirikisho.
Katibu Mkuu wa Azam FC, Nassor Idrisa ameiambia BIN ZUBEIRY leo kwamba katika ziara hiyo watacheza mechi tatu za kujipima nguvu dhidi ya timu za Sofapaka, AFC Leopards na Gor Mahia kabla ya kurejea nchini Januari 23.
Nassor alisema ziara hiyo ni maalum kwa ajili ya kuiweka sawa timu yao kabla ya kuanza kwa mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Bara na Kombe la Shirikisho Afrika.
Nassor amesema anaamini timu za Kenya ni nzuri na zitawapa changamoto nzuri kabla ya kuanza kwa mzunguko wa pili wa Ligi Kuu na kuingia kwenye Kombe la Shirikisho.
“Tumekuwa katika programu ndefu ya maandalizi tangu Desemba, tukianzia Kongo (DRC) ambako tulicheza mashindano na kuchukua Kombe, tumetoka tumeingia kwenye Kombe la Mapinduzi tumeshiriki na kuchukua Kombe, na sasa tunakwenda Kenya,”alisema Nassor.
Katibu huyo alisema kikosi kizima cha Azam kitakwenda Kenya kwenye ziara hiyo na baada ya hapo timu itarejea tayari kwa mzunguko wa pili wa Ligi Kuu.
 

IMEHAMISHWA: BIN ZUBEIRY

Emmanuel Okwi aiacha Simba solemba atua Etoile du Sahel


Emmanuel Okwi

MSHAMBULIAJI wa kimataifa wa Uganda, Emmanuel Okwi wa Simba anadaiwa kujiunga na klabu ya Etoile du Sahel ya Ligi Kuu ya Tunisia kwa dola za Kimarekani 300,000 (Sh. milioni 472).
Taarifa zilizopatikana jana jijini zinadai kwamba Okwi amekamilisha vipimo vya afya na kila kitu na tayari amesaini mkataba na klabu hiyo na atakuwa analipwa mshahara wa dola za Marekani 15,000 (Sh. milioni 24) kwa mwezi. Hata hivyo, haikuelezwa ni mkataba wa muda gani.
Taarifa hizo zinasema kuwa tayari Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage ameshatua nchini humo kwa ajili ya kuweka mambo sawa na kwamba sehemu za fungu hilo la usajili wa mchezaji huo zitagawanywa pia kwa klabu ya SC Villa kulingana na mkataba.
Okwi aliyekuwa akipiga chenga kuripoti kambini Simba na ameachwa katika safari ya Oman ambako mabingwa hao wa Tanzania Bara wameweka kambi kujiandaa na mzunguko wa pili wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.
Baada ya kumaliza mkataba wake wa awali na Simba Desemba mwaka jana, Okwi aliongeza mkataba wa miaka miwili na ‘Wekundu wa Msimbazi’ ambao kabla hajaanza kuutumikia, ameamua kuhamia Sahel.
Okwi akiitumikia timu ya taifa lake la Uganda


Mbio za uchaguzi wa TFF zapambamoto

Michael Wambura



ALIYEKUWA Katibu Mkuu wa Chama cha Soka Tanzania (FAT sasa TFF), Michael Wambura na kiongozi wa zamani wa klabu iliyokuwa Ligi Kuu ya Moro United ‘Chelsea ya Bongo’, Muhsin Balhabou ni miongoni mwa wadau wa soka walichukua fomu jana kuwania nafasi mbalimbali za uongozi ndani ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).
Wambura amechukua fomu kuwania umakamu wa rais huku Balhabou akiwania nafasi ya ujumbe katika kamati ya uchaguzi ya TFF. Uchaguzi huo utafanyika Februari 24 jijini Dar es Salaam
Tayari wagombea wengine wawili, Makamu wa Pili wa Rais anayemaliza muda wake, Ramadhan Nassib na Mjumbe wa Kamati ya Utendaji inayomaliza muda, Wallace Karia wameshachukua fomu za kuwania nafasi anayoiwania Wambura.
Wanamichezo wengine waliochukua fomu jana ni pamoja na Mbasha Matutu, Salum Chama, Titus Osoro na Zafarani Damoder ambao wote wanawania pia nafasi za ujumbe wa kamati ya utendaji ya TFF.
Wagombea wengine waliojitokeza kuchukua fomu za kuwania ujumbe ni Salum Chama anayewania kupitia Kanda ya Kagera na Geita, Mugisha Galibona, Samuel Nyalla, Titus Osoro na Vedastus Lufano (Mara na Mwanza), Epaphra Swai na Mbasha Matutu (Shinyanga na Simiyu), Charles Mugondo, Elly Mbise na Twahili Njoki (Arusha na Manyara) huku Yusuph Kitumbo (Kigoma na Tabora).
Ayubu Nyaulingo, Nazarius Kilungeja na Selemani Kameya (Katavi na Rukwa) na James Mhagama (Njombe na Ruvuma), Athuman Kambi (Lindi na Mtwara), Hussein Mwamba na Stewart Masima (Dodoma na Singida), Farid Nahdi (Morogoro na Pwani), Khalid Mohamed (Kilimanjaro na Tanga) na Muhsin Balhabou, Shaffih Dauda na Zafarani Damoder (Dar es Salaam).
Taarifa iliyotolewa jana na Afisa Habarin wa TFF, Boniface Wambura, imeeleza kuwa jumla ya waliochukua fomu hadi sasa ni watu 26, lakini idadi hiyo ni ya wale wanaochukua fomu hizo katika ofisi za TFF. Fomu hizo huchukuliwa pia kupitia tovuti ya TFF (www.tff.or.tz) na mwisho wa kuchukua na kuzirejesha ni keshokutwa Ijumaa, saa 10:00 jioni.
Mwaka 2004, Wambura pamoja na aliyekuwa Mwenyekiti wa FAT, Muhiddin Ndolanga, waliangushwa na Tenga lakini mwaka 2008, Wambura alijitosa tena katika nafasi ya Makamu wa Kwanza wa Rais lakini jina lake lilienguliwa kwa maelezo kwamba hakuwa na sifa ya uadilifu.
Hata hivyo, mwaka jana Wambura akiwa anawania nafasi ya uenyekiti wa Chama cha Soka cha Mkoa wa Mara (FAM), jina lake lilienguliwa na baada ya kukata rufaa lilirejeshwa lakini muda wa uchaguzi ulikuwa umeshamalizika na hivyo alishindwa kuwania cheo hicho kama alivyodhamiria.
Juzi, Tenga alitangaza wazi kwamba hatawania tena cheo hicho na hivyo kuwapunguzia 'presha' wale waliokuwa wakihofia kutwaa fomu za kuwania uenyekiti wa shirikisho hilo kwa sababu yake.
Katika hatua nyingine, Said Mohamed amechukua fomu ya kuwania umakamu mwenyekiti wa Bodi ya Ligi Kuu (TPL Board).

Mkina, Ochieng waiponza Simba

Mkenya Pascal Ochieng

WACHEZAJI Pascal Ochieng na Shija Mkina wameiponza klabu ya Simba baada ya uongozi wa mabingwa hao wa soka Tanzania Bara kutakiwa kufika mbele ya Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) kutoa maelezo kuhusiana na madai mbalimbali ya wachezaji hayo.
Mkenya Ochieng aliwasilisha barua katika ofisi za (TFF) Desemba 19 mwaka jana akiliomba shirikisho hilo kumsaidia kupata haki zake zikiwamo fedha zake za usajili, Sh. milioni sita na mashahara wake wa mwezi mmoja (Novemba 2012), ambao hata hivyo hakuwa tayari kutaja ni kiasi gani kwa madai kuwa ni siri yake na Simba.
Ochieng, ambaye alilazimika kuununua mkataba wake wa miezi sita na klabu ya AFC Leopards ya Kenya ili ajiunge na Simba, alinukuliwa akisema kuwa anaidai Simba dola za Marekani 8,000 (Sh. milioni 12.6) na kwamba hajapatiwa barua ya kuvunjwa kwa mkataba wake na klabu hiyo, hivyo anaamini kuwa bado yeye ni mwajiriwa wa ‘Wekundu wa Msimbazi’.
Kwa upande wake, Mkina ambaye hivi sasa anaichezea kwa mkopo klabu ya ligi kuu Bara ya Kagera Sugar (akitokea Simba), anadai Simba haijamlipa Sh. milioni sita zilizokuwa zimebaki baada ya kusaini mkataba nao kwa makubaliano ya Sh. milioni 10 na kwamba walimlipa fedha ya utangulizi Sh. milioni nne mwaka 2010.
Mkina pia anadai kuwa uongozi wa Simba umekuwa ukimzungusha katika malipo ya fedha zilizobaki na kwamba anawadai pia fedha za mshahara wake wa miezi mitatu (Septemba – Novemba, 2012).
Akizungumza jana jijini Dar es Salaam jana, Afisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alisema kuwa Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ili ilikutana jijini Dar es Salaam Jumamosi kupitia masuala mbalimbali yakiwamo madai ya wachezaji hao.
Wambura alisema kuwa baada ya kamati hiyo kupitia madai ya Ochieng na Mkina, iliamua kuzikutanisha pande zote (Simba na wachezaji wanaolalamika) ili iwahoji kwa pamoja Jumamosi ya Januari 19.
“Ni kweli tulipata barua za wachezaji hao. Kamati ya Sheria, Maadili na Hadhi za Wachezaji ilikaa Jumamosi iliyopita ikaamua kuwaita viongozi wa Simba na wachezaji wanaolalamika ili wahojiwe kwa pamoja Jumamosi,” alisema Wambura.
Baada ya kumalizika kwa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara Novemba mwaka jana huku timu yao ikifanya vibaya na kuangukia katika nafasi ya tatu katika msimamo wa ligi hiyo, viongozi wa Simba waliamua kusitisha mikataba ya baadhi ya wachezaji wao wakiwamo beki Ochieng na mshambuliaji Daniel Akuffor wa Ghana.

Zahoro Pazi aenda kujaribiwa Afrika Kusini

Zahoro Pazi akiwa kando ya 'mkoko' wake hivi karibuni mitaa ya Temeke Maduka Mawili

MSHAMBULIAJI wa zamani wa timu za Mtibwa na Azam aliyekuwa ametua JKT Ruvu kwa mkopo, Zahoro Pazi, ameondoka nchini juzi usiku kuelekea Afrika Kusini kufanya majaribio ya kucheza soka la kulipwa katika klabu ya Ligi Kuu ya Bloemfotein Celtic.
Akizungumza na MICHARAZO muda mchache kabla ya kupaa kuelekea nchini humo, Pazi alisema kuwa safari yake imefanywa na wakala wake ambaye hakupenda kumtaja jina na kwamba mipango hiyo ilikuwepo tangu mwishoni mwa mwaka jana.
Pazi, alisema kwamba klabu hiyo ya Bloemfotein Celtic inayoshiriki Ligi Kuu ya Afrika Kusini, ilivutiwa naye kupitia michuano ya Kombe la Kagame pamoja na kutuma maskauti wao walipoenda DR Congo kushiriki michuano ya Kombe la Hisani.
"Ndoto zangu za kucheza soka la kulipwa baada ya kukwama mara mbili Ujerumani na Umangani naona zinaelekea kuwa kweli kwani nimeitwa na klabu ya Bloemfotein Celtic kwa ajili ya kufanyiwa majaribio," alisema Pazi.
Pazi, mtoto wa kipa nyota wa zamani wa kimataifa wa Tanzania aliyewahi kutamba na timu za Pilsner, Simba, Taifa Stars na El Merreikh ya Sudan, Idd Pazi 'Father' alisema ana imani kubwa ya kufanya vema majaribio yake.
"Sina hofu yoyote na safari yangu hii, kama niliweza kuivutia Kaiserslautern ya Ujerumani sidhani kama nitashindwa Afrika Kusini muhimu niombeeni dua Mungu anifanyie wepesi," alisema Pazi.
Kinda hilo lililozaliwa Julai 4, 1989 akiwa mtoto wa mwisho kati  ya watoto wawili wa Idd Pazi, alisema majaribiuo yake amedokezwa yatakuwa ya wiki moja na kama kutakuwa na lolote la ziada atalifahamisha NIPASHE akiwa nchini humo.
***