STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, March 8, 2011

Msamba 'ajitoa' Villa Squad *Ni baada ya kuirejesha Ligi Kuu

KOCHA aliyeipandisha daraja klabu ya Villa Squad hadi Ligi Kuu Tanzania Bara, Abdallah Msamba, ametangaza 'kuitema' timu hiyo akiutaka uongozi usake kocha mwingine wa kuiongoza kwenye ligi hiyo msimu wa 2011-2012.
Akizungumza na Micharazo, Msamba, alisema baada ya kutimiza jukumu la kuirejesha Ligi Kuu, Villa Squad anaona ni vema kupisha kocha mwingine wa kuendelea kuinoa timu hiyo katika ligi hiyo msimu ujao.
Msamba, alisema kujiondoa kwake kuinoa timu hiyo haina maana kuwa kajitoa kabisa Villa Squad, ila alisema kwa hadhi ya ligi ilivyo inapaswa timu iwe na mtu mwingine kukabiliana na mshikemshike wake.
"Nimeashautaarifu uongozi utafute kocha mwingine wa kuiandaa timu kwa ligi kuu ijayo, mie naishia hapa baada ya kuipandisha daraja, ila nitakuwa kocha msaidizi au mshauri kwa lengo la kuona Villa inafanya vema," alisema.
Winga huyo wa zamani wa Sigara, Simba na Kajumulo World Soccer, alisema ili kuweza kufanya vema kwenye ligi hiyo, Villa inahitaji kufanya marekebisho kidogo katika kikosi chake, chini ya kocha mwenye hadhi stahiki.
Alisema ana imani kama marekebisho hayo yatafanyika mapema na timu kuandaliwa mapema ikipata michezo mingi ya kujipima nguvu inaweza kutisha katika ligi hiyo iliyowahi kuicheza kabla ya kushuka msimu wa 2008-2009.
Villa Squad ni miongoni mwa timu nne zilizopanda Ligi Kuu msimu ujao baada ya kufanya vema kwenye Ligi Daraja la Kwanza iliyochezwa mjini Tanga.
Timu zingine zilizoungana na klabu hiyo yenye maskani yake Magomeni Mapipa ni JKT Oljoro waliokuwa mabingwa wa ligi hiyo ya daraja la kwanza, Coasta Union na Moro United zinazorejea tena kwenye Ligi Kuu ya Tanzania.

Mwisho

Mtambo wa Gongo, kuzigonga na Cobra Machi 12

BONDIA mkongwe wa ngumi za kulipwa nchini, Maneno Osward 'Mtambo wa Gongo' anatarajiwa kuvaana na Robert Mrossy 'Cobra' katika pambano la Middleweight, litakalofanyika Machi 20 mwaka huu.
Osward mwenye miaka 41 atapigana na Cobra katika pambano lililoandaliwa na Rais wa Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania, TPBO, Yassin Abdalla 'Ustaadh' litafanyika kwenye ukumbi wa Amana Club, Ilala jijini Dar.
Ustaadh aliiambia Micharazo kuwa, pambano hilo lisilo la ubingwa la raundi 12 ni maalum kwa ajili ya kupima viwango vya mabondia husika, pia kutoa fursa kwa mabondia wa mikoani kujitangaza kwenye mchezo huo.
Rais huyo wa TPBO, alisema Cobra ni bondia kutoka Arusha na hivyo kupata fursa ya kupigana na mkongwe Osward, kutampa nafasi ya kujitangaza katiuka mchezo huo.
Ustaadh alisema awali pambano hilo lilipangwa kufanyika Jumapili ijayo, ila kutokana na kuahirishwa kwa lingine la ngumi hizo za kulipwa kati ya Ashraf Suleiman na Awadh Tamim kutoka Machi 5 hadi Machi 12 imewafanya walisogeze mbele hadi Machi 20.
"Tumeona isingekuwa vema pambano letu lifanyika kama tulivyopanga Machi 13, wakati siku moja kungekuwa na pigano jingine la Ashraf na Tamim ambalo awali lilipangwa kufanyika Machi 5, lakini likasogezwa hadi Machi 12," alisema Rais huyo wa TPBO.

Kaseba, Maugo kutambulishwa rasmi leo

MABONDIA Mada Maugo na Japhet Kaseba wanaotarajiwa kupigana Aprili 16, pamoja na watakaowasindikiza pambano hilo wanatarajiwa kutambulishwa rasmi leo mbele ya waandishi wa habari.
Mratibu wa pambano hilo, Kaike Siraju aliiambia Micharazo jana kuwa leo watafanya mkutano na vyombo vya habari kulitambulisha rasmi pambano hilo ambalo litafanyika kwenye ukumbi wa PTA, jijini Dar es Salaam.
"Nitawatambulisha rasmi mabondia wote watakaopigana Aprili 16 katika mkutano na vyombo vya habari utakaofanyika kesho (leo) kwenye ukumbi wa Habari-Maelezo majira ya saa 5," alisema Siraju.
Alisema katika mkutano huo, Maugo na Kaseba kila mmoja atapata fursa ya kuongea machache kuhusiana na pambano lao hilo la raundi nane uzito wa kilo 72 litakalokuwa la kusaka mkali baina yao wa kuzipiga na Francis Cheka.
Ingawa Siraju amekuwa akificha majina ya mabondia watakaoshindikiza pambano hilo, lakini uchunguzi wa Micharazo umebaini kuwa nahodha wa zamani wa timu ya taifa ya ngumi ya ridhaa, Joseph Martin ni miongoni mwao.
Martin aliyeachana na ngumi za ridhaa na kuingia za kulipwa atapigana na Sweet Kalulu, pia Francis Miyeyusho na Afande Juma nao watakuwepo katika usindikizaji.
Kwa mujibu wa Siraju, mgeni rasmi wa pambano hilo anatarajiwa kuwa Kamanda wa Polisi wa Kanda Maalum ya Dar es Salaam, Suleiman Kova ambaye atamualika IGP Said Mwema kuhudhuria kwenye ngumi hizo.