STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, July 27, 2011

Banka aishtaki Simba kwa TFF




KIUNGO Mohammed Banka ameishtaki klabu yake ya Simba kwa Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, juu ya sakata lake la kutaka kupelekwa kucheza kwa mkopo katika timu ya Villa Squad bila ridhaa yake.
Banka, aliyeichezea Simba kwa mafanikio tangu ilipomsajili baada ya kutemwa na Yanga, msimu wa 2008-2009, alisema ameamua kuchukua maamuzi huo kutokana na kuona viongozi wa Simba wanamzungusha kuhusu suala la uhamisho wake.
Mwanasheria aliyepewa kazi ya kumpigania Banka, John Mallya, aliiambia MICHARAZO jana kuwa, wameandika barua Shirikisho la Soka Tanzania, TFF, ili kuingilia kazi suala la mteja wao kabla ya hatua zingine za kisheria kufuata.
Mallya, alisema wameamua kuandika barua hiyo, TFF kutokana na kuona viongozi wa Simba wanakwepa kukutana kulimaliza suala la Banka, kutokana na wenyewe kukiuka mkabata baina yao na mchezaji huyo kama sheria zinavyoelekeza.
Alisema walikuwa katika mazungumzo mazuri na viongozi wa klabu hiyo, lakini juzi walipopanga kukutana ili kulimaliza suala hilo, wenzao walishindwa kutokea na kuona ni vema waombe msaada TFF, kabla ya kuangalia cha kufanya kumsaidia mteja wao.
Afisa Habari wa TFF, Boniface Wambura alikiri kupokewa kwa barua hiyo ya ombi la Banka kutaka shirikisho lao kuingilia kati na kudai itapelekwa kunakohusika kufanyiwa kazi.
"Ni kweli barua hiyo imefika kwetu, Banka akiomba TFF iingilie kati sakata lake la Simba," alisema Wambura.
Naye Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, alikiri kuwepo kwa mazungumzo yaliyokuwa yakiendelea baina ya pande hizo mbili, ingawa alisema alikuwa hajaipata nakala ya barua hiyo ya malalamiko ya Banka iliyopelekwa TFF.
"Hilo la kushtakiwa TFF, silijui kwani sijapata barua, pia siwezi kuliongelea kwa undani kwa vile lilikuwa linashughulikiwa na viongozi wa juu, ambao kwa bahati karibu wote wameenda Uturuki kushughulikia suala la ujenzi wa uwanja," alisema.
Banka, amekuwa akisisitiza kuwa kama Simba haimhitaji ni bora mlipe chake aangalie ustaarabu wake kuliko kumlazimisha kwenda Villa Sqaud iliyorejea ligi kuu msimu huu.

Mwisho

Bingwa wa Kick Boxing Kenya atua Bongo kuzipiga




BINGWA wa Kick Boxing kutoka Kenya, Rukia Kaselete ametua nchini tayari kwa ajili ya pambano lake dhidi ya Mtanzania Jamhuri Said, watakaosindikiza pambano la nani mkali kati ya Amour Zungu wa Zanzibar na Mchumia Tumbo wa Tanzania Bara.
Michezo hiyo iliyoandaliwa na Bingwa wa Dunia wa Kick Boxing anayeshikilia mikanda ya WKL na WKC, Japhet Kaseba inatarajiwa kucheza siku ya Jumamosi kwenye ukumbi wa DDC Keko, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na MICHARAZO jana, Kaseba, alisema maandalizi ya michezo hiyo kwa wastani inaendelea vema ikiwemo mabondia wote kuwasili jijini akiwemo mkenya huyo atakayepigana na Jamhuri kusindikiza pambano la Zungu na mwenzake.
Kaseba alisema mabondia wote watakaoshiriki michezo hiyo ya Kick Boxing na Ngumi za Kulipwa wanatarajiwa kupimwa afya zao siku ya Ijumaa kwenye gym yake, iliyopo eneo la Mwananyamala jijini Dar es Salaam.
"Kwa kweli kila kitu kinaenda vema ikiwemo mabondia wote kuwasili Dar tayari kwa ajili ya michezo hiyo ya Jumamosi, ambapo Amour Zungu atazipiga na Mchumia Tumbo katika pambano la kusaka mkali kati yao," alisema Kaseba.
Kaseba alisema mbali na pamoja ya pambano la Kaseleta na Jamhuri, siku hiyo pia kutakuwa na michezo mingine ya utangulizi ambapo wanadada Asha Abubakar wa Kisarawe na Fadhila Adam wa Dar wataonyeshana kazi kwenye kick boxing.
"Wengine watakaopigana siku hiyo ni kati ya Dragon Kaizum dhisi ya Faza Boy, Idd na Dragon Boy na Lion Heart ataonyeshana kazi na Begeje," alisema.
Aliongeza pambano la ngumi za kulipwa zitawakutanisha wakongwe wa mchezo huo, Ernest Bujiku dhidi ya Maneno Osward 'Mtambo wa Gongo'.

Mwisho

Viongozi Simba waenda kumalizana na Waturuki



VIONGOZI wa klabu ya soka ya Simba wameondoka nchini juzi kuelekea Uturuki kwa ajili ya kwenda kumalizia taratibu za ujenzi wa uwanja wao mpya wa kisasa utakaojengwa eneo la Bunju, nje kidogo ya jijini la Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa Afisa Habari wa klabu hiyo, Ezekiel Kamwaga, viongozi walioondoka ni Mwenyekiti Ismail Aden Rage na Katibu wake, Evodius Mtawala.
Kamwaga alisema Rage na Mtawala waliondoka juzi kuelekea nchini humo kufanya mazungumzo ya mwisho na uongozi wa kampuni ya Petroland, ambayo ndiyo itakayoujenga uwanja huo utakaoingiza watazamaji wasiopungua 60,000.
"Viongozi wetu wawili wa juu wameondoka nchini jana, kwenda Uturuki kwa ajili ya kumalizana na watakaotujengea uwanja wetu wa kisasa utakaokuwa eneo la Bunju," alisema Kamwaga.
Afisa Habari huyo, alisema viongozi wao wameenda kuweka mambo sawa kabla ya wakandarasi hao kuja kuanza kazi yao na kuifanya Simba kufuata nyayo za klabu kubwa barani Afrika kama ASEC Memosa au Kaizer Chief zenye viwanja vikubwa vya kisasa.
Uwanja huo utakaokuwa wa kisasa na mkubwa kama ule wa Taifa, utaigharimu Simba kiasi cha Shilingi Bilioni 75 hadi utakapomalizika ukihusisha uwanja wa kuchezea, maduka, kumbi za mikutano na burudani, mbali na hoteli na kituo cha michezo.
Kwa hapa nchini ukiondoa Yanga yenye kuumiliki uwanja wa Kaunda, klabu nyingine yenye uwanja wake mwenyewe ni Azam iliyoujenga eneo la Chamanzi, Mbande nje kidogo ya jijini la Dar es Salaam ambao utaanza kutumika msimu mpya wa Ligi Kuu.

Mwisho

Simba yawaita DCMP Da kumjadili Mgosi




UONGOZI wa klabu ya soka ya Simba, umeutaka uongozi wa timu ya DC Motema Pembe ya DR Congo, kuja jijini Dar es Salaam kuzungumza nao ili waachiwe kiungo mshambuliaji, Mussa Hassani Mgosi vinginevyo imsahau kumpata.
Motema Pembe imeonyesha nia ya kumsajili Mgosi, isipokuwa inamtaka kama mchezaji huru, kitu kinachopingwa na uongozi wa Simba wenye mkataba bao ikidai kama ina ya dhati ya kumnasa mchezaji huyo wake wazungumze mezani waafikiane.
Akizungumza na MICHARAZO jana, Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, alisema klabu yao ipo tayari kumuacha Mgosi aende DCMP, ila kama uongozi wa klabu hiyo utakuja kuzungumza nao ili kumhamisha kwani ni mchezaji wao halali.
Kamwaga alisema Simba haina nia ya kumbania Mgosi, ila kwa hali ilivyo ni vigumu kwao kumtoa winga huyo bure wakati wana mkataba naye.
Kamwaga, alisema Simba itaona raha iwapo mchezaji huyo atajiunga na DCMP kama ilivyokuwa kwa akina Mbwana Samatta na Patrick Ochan walisajiliwa TP Mazembe, ila wenzake wanamtaka bure kitu kinachowafanya wamzuie hadi kieleweke.
"Kama kweli wana nia na Mgosi waje wazungumze nasi, Mgosi ana mkataba Simba na hivyo hatuwezi kumuachia bure," alisema.
Kamwaga, alisema tayari wameshaifahamisha TFF juu ya msimamo wao na wanasubiri kuona uongozi wa DCMP utafanya nini kuamua hatma ya Mgosi, ambaye jina lake lipo kwenye orodha ya usajili wa klabu ya Simba kwa msimu ujao wa ligi kuu Tanzania Bara.
Alisema kama mipango yake ya kwenda Congo itakwama, Mgosi ataendelea kuichezea timu yao kwa msimu ujao hadi atakapomaliza mkataba utakaoisha mwakani.
Katika hatua nyingine, Kamwaga alisema klabu yao inatarajiwa kuianika timu watakaocheza nao kwenye Tamasha la Siku ya Simba 'Simba Day' litakalofanyika Agosti 8 mwaka huu.
Kamwaga alisema klabu yao ilipeleka maombi kwa klabu tatu za nje ya nchi na leo wanatarajia kutangaza timu watakayocheza nao katika tamasha hilo
"Timu itakayotusindikiza kwenye Simba Day tutaitangaza kesho (leo) pia tutaanika kila kitu juu ya maandalizi ya tamasha hilo," alisema Kamwaga.

Mwisho

Talent Band kutambulisha mpya Sinza

BENDI ya muziki wa dansi ya Talent 'Wazee wa Kuchechemea' inatarajiwa kuvamia kitongoji cha Sinza ili kuitambulisha albamu yao mpya ya 'Shoka la Bucha'.
Mkurugenzi wa bendi hiyo, Husseni Jumbe, aliambia MICHARAZO jana kuwa, onyesho hilo litafanyika kesho kwenye ukumbi wa Nouvel Social Centre (zamani Rufita) ambapo watatambulisha nyimbo zote zilizopo kwenye albamu hiyo mpya.
Jumbe, alisema onyesho hilo limeratibiwa na Mkurugenzi wa ukumbi huyo aliyemtaja kwa jina la Mamaa Joyce.
"Baada ya kuikamilisha albamu yetu mpya ya Shoka la Bucha, Talent Band, inatarajiwa kuitambulisha albamu hiyo katika onyesho maalum litakaloofanyika siku ya Alhamis kwenye ukumbi wa Nouvel Social Centre," alisema Jumbe.
Jumbe alizitaja nyimbo zitakazotambulishwa kwenye onyesho hilo kuwa ni Shoka la Bucha, Kiapo Mara Tatu, Kilio cha Swahiba na zile za albamu yao ya kwanza ya Subiri Kidogo.
Naye mratibu wa onyesho hilo, Joyce alisema kila kitu kipo sawa na wanachosubiri ni kupata burudani toka kwa Talent.

Mwisho

Tamasha kubwa la sanaa kufanyika Moro

WASANII zaidi ya 100 wa mkoani Morogoro wanatarajia kufanya tamasha kubwa litakaloshirikisha sanaa za aina mbalimbali.
Mratibu wa tamasha hilo lililopewa jina la 'Wakali Concert', Athuman Mswagala 'Mahita' aliiambia Micharazokwa njia ya simu kutoka Morogoro kuwa tamasha hilo litafanyika Julai 30 katika ukumbi wa Vijana Social ulioko mjini hapa.
Mswagala, alisema lengo la tamasha hilo litakalowahusisha wasanii wa mkoa huo wa fani mbalimbali ni kufahamiana na kuibua vipaji vipya.
Alisema maandalizi kwa ajili ya tamasha hilo yanakwenda vizuri na kwamba kinachosubiriwa ni kufanyika kwa tamasha hilo.
Alisema katika tamasha hilo litakalokuwa likifanyika kila mwaka, wasanii watakaofanya vizuri watazawadiwa zawadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na fedha taslimu.
"Kimsingi, maandaalizi yanakwenda vizuri na wasanii wengi wamethibitisha kushiriki hali ambayo naamini itakuwa burudani tosha kwa wakazi wa Morogoro" alisema.
Naye, mkurugenzi wa kampuni ya Katundu, wanaodhamini tamasha hilo, Mohamed Katundu, alisema kampuni yake imeamua kudhamini tamasha hilo kwa lengo la kusapoti wasanii wa Morogoro.
Katundu alisema hiyo ni moja ya mipango ya kampuni yake kuhakikisha wasanii mkoani hapa wanapata mafanikio makubwa kupitia sanaa mbalimbali.