STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, February 26, 2014

Tanzia! Nyota wa zamani Coastal afariki, kuzikwa leo Tanga

KWA niaba ya uongozi wa Coastal Union, tunatangaza msiba wa mchezaji wa zamani wa timu hii Bakari Jeki, pichani, aliefariki usiku wa kuamkia jana katika hospitali ya rufaa Bombo.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka kwa kaka wa marehemu ndugu Ally Jeki, ndugu yetu aliugua kwa muda mfupi ambapo alilazwa katika hospitali ya Bombo wiki iliyopita mpaka mauti yalipomfika siku tatu baada ya kuanza kuugua.
Mwandisi wetu alizungumza na mchezaji wa zamani wa Coastal Union, ambae alipata bahati kumuona Bakari Jeki akiitumikia Coastal Union, Razak Yusuf ‘Careca’ ambae alibainisha kuwa marehemu alikuwa na mchango mkubwa katika timu.

“Coastal Union imekosa mtu muhimu katika soka ambae alikuwa msaada mkubwa akitoa mawazo, vilevile alikuwa hakosi katika mechi na mazoezi ya timu,” Careca.
Aidha beki namba tano wa zamani Coastal Union, Mzee Salim Amir ambae alicheza na marehemu katika michuano ya UFUMA, iliyoandaliwa na Chama Cha Soka nchini (FAT), ambao ulikuwa ni ushauri wa Rais wa kwanza wa Tanzania, Julius Nyerere.

Nyerere alitoa ushauri huo ili kuisaidia FAT iliyokuwa chini ya Said El Maamry, kuondokana na madeni. Michuano hiyo ikapewa jina la Operesheni Futa Madeni (OFUMA).
Ilishirikisha timu nne ambazo ni Simba (Dar es Salaam), Nyota (Mtwara), Coastal Union (Tanga) na Nyota Afrika (Morogoro), Coastal Union waliibuka mabingwa marehemu Bakari Jeki akiwa beki mbili na langoni alikuwa mdogo wake Said Jeki ambae pia alikuwa golikipa wa Taifa Stars.

Baadhi ya wachezaji waliokuwa katika kikosi kilichotwaa kombe la OFUMA, ambalo lilichezwa mara moja tu na kutoendelea tena ni Zacharia Kinanda, Mohammed Makunda, Bakari Rashid, Kuzu Mbwana, Salim Amir, Mohammed Salim, Zaharan Makame, Said Jeki na Mguruko.
“Alikuwa ni beki mzuri, Coastal Union ilinufaika na uchezaji wake kwani alicheza kwa moyo wote beki mbili ambayo ilipanda na kushuka bila kuchoka. Mbali na hayo aliishi vizuri na wenzake hakuwa mtu wa matatizo muda mwingi alipenda utani.

“Alinikuta mwaka1976 nikitokea Misri na timu ya Taifa, tukashiriki kombe la OFUMA tukiwa pamoja katika safu ya ulinzi lakini baadae nilistaafu baada ya kuumia, yeye aliendelea mpaka mwanzoni mwa miaka ya 1980 ndipo akaachana na soka, lakini hakuacha kuwa karibu na Coastal Union, muda mwingi alijitokeza kutoa ushauri na kila alipohitajika hakusita kuitikia mwito, huyo ndie Bakari Jeki ninaemfahamu,” alisema Salim Amiri.

Marehemu, alianza kucheza Coastal Union mwaka 1976 akitokea timu ya Magunia Moshi, alipotua Coastal Union alicheza kwa moyo wake wote mpaka alipostaafu soka, mpaka mauti yanamfika alikuwa kocha wa timu za mchangani mjini tanga na mshauri mkubwa wa benchi la ufundi Coastal Union.

Vilevile marehemu alitoka katika familia yenye vipaji vya soka kwani walikuwa ndugu watatu wa baba mmoja na mama mmoja ambapo Said Jeki alikuwa golikipa wa Coastal Union na timu ya Taifa, mwingine ni Hassan Jeki ambae alikuwa akichezea Reli Morogoro, lakini kwa sasa wote watatu ni marehemu.

Mwili wa Marehemu utatolewa Hospitali ya Rufaa Bombo mjini Tanga kuelekea nyumbani kwa kaka yake Ally Jeki maeneo ya Majengo, ifikapo saa tisa alasiri mwili wa marehemu utasaliwa katika msikiti wa Majengo kabla ya kupelekwa kijijini kwa Masuguru Wilayani Muheza Mkoani Tanga saa kumi alasiri.
Kaka wa marehemu hakuweka wazi kuhusu familia ya marehemu hasa upande wa mke ama watoto lakini alibainisha kuwa marehemu alizaliwa mwaka 1953 wilayani Muheza, Tanga. 
KWETU HANDENI

Yanga wapo kamili kuiua Al Ahly Jumamosi

Tegemeo la Tanzania michuano ya Afrika kwa sasa, Yanga
WAWAKILISHI pekee  wa Tanzania kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika, Yanga imeingia kambini katika hotel ya Laico Ledger iliyopo eneo la Bahari Bahari Beach Kunduchi  tayari kwa ajili ya pambano la Jumamosi dhidi ya ya Al Ahly kutoka Misri.
Mchezo huo wa Yanga dhidi ya Al Ahly utachezwa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam kuanzia saa 10 kamili jioni.
Akizungumza na waandishi wa habari jana Ofisa Habari wa Yanga Baraka Kizuguto alisema kikosi cha Yanga  chenye wachezaji 25 pamoja na benchi la Ufundi kilianza mazoezi juzi jioni katika Uwanja wa Kaunda Makao Makuu ya Klabu na jana asubuhi kimeendelea kujinoa katika Uwanja wa Boko Beach.
“Wachezaji wote wapo katika hali nzuri, mpaka sasa hakuna mchezaji majeruhi kuelekea mchezo huo,”alisema.

Alisema  Kocha  anatambua mchezo huo utakua ni mgumu, kwani Al Ahly wana uzoefu na michezo ya kimataifa lakini na wao wana malengo na zaidi  ni kufanya mapinduzi kwa kushinda
“Kwa vile Kocha anawafahamu Al Ahly  vizuri hakuna kitakachoshindikana kwasababu tayari tumepata  mbinu zao kutoka kwa  Kocha Msaidizi Boniface Mkwasa, kilichobaki ni kuwaandaa wachezaji kiakili,”alisema.

Katika mchezo huo, Mshambuliaji wa Kimataifa Emanuel Okwi atakuwa ni miongoni mwa wachezaji tegemeo katika kikosi kitakachotua dimbani siku hiyo. Kizuguto alithibitisha ushiriki huo kwa kuonyesha leseni yake iliyotoka Shirikisho la Soka Afrika(CAF) .



Al Ahly imewasili leo alfajiri saa 12 kasorobo kwa Shirika la Ndege la Misri Egypt Air kikiwa na watu 35 wakiwemo wachezaji 22, bechi la Ufundi 8 pamoja na viongozi 5 na wamefikia katika Hotel ya Hyatt Kempsinki ambapo ndio itakuwa ikiweka kambi.

Siku ya Jumatano na Alhamisi  jioni watafanya mazoezi katika Uwanja wa IST uliopo Upanga, na Ijumaa jioni watapata fursa ya kufanya mazoezi katika Uwanja wa Taifa jijini Dar es salaam tayari kwa mchezo huo wa Jumamosi.


Tiketi zitauzwa kwenye vituo mbalimbali kuanzia Ijumaa ambapo kiingilio cha juu ni  Shs 35,000,  25,000,  13,000 na cha chini kwa viti vya kijani na bluu ni Sh. 7000.

Rekodi ya Al Ahly:
Wana mataji 19 moja zaidi ya mataji 18 ya Ac Milan
Imeshinda mara 8 kombe la mabingwa barani Afrika, mwaka 1982,1987,2001,2005,2006, 2008, 2012, na 2013. Makombe 4 ni ubingwa wa Kombe la washindi 1984,1985,1986, 1993.

Mara sita imetwaa kombe la CAF Super Cup 2002, 2006,2007,2009, 2013, na 2014 na mmoja likiwa la Afro-Asian Cup mwaka 1988.

Shepolopolo kutua kesho kuivaa Twiga Stars Ijumaa


Timu ya Taifa ya Zambia (Shepolopolo) inatua nchini kesho mchana (Februari 27 mwaka huu) kwa ajili ya mechi ya marudiano ya michuano ya Afrika kwa Wanawake (AWC) dhidi ya Tanzania (Twiga Stars) itakayochezwa keshokutwa (Februari 28 mwaka huu).

Shepolopolo yenye msafara wa watu 29 itawasili kwa ndege ya Fastjet ikitokea Lusaka na itafikia kwenye hoteli ya Accomondia kwa ajili ya mechi hiyo itakayochezwa Uwanja wa Azam Complex ulioko Chamazi kuanzia saa 10 kamili jioni.

Waamuzi wa mechi hiyo kutoka Burundi wakiongozwa na Ines Niyosaba wamewasili nchini leo asubuhi wakati Kamishna Fran Hilton-Smith kutoka Afrika Kusini atawasili kesho (Februari 27 mwaka huu) saa 8 kamili mchana kwa ndege ya South African Airways.
Katika hatua nyingine Rais wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Jamal Malinzi atakuwa na mkutano na waandishi wa habari juu ya benchi la ufundi la timu ya Taifa ya wakubwa (Taifa Stars).

Mkutano huo utafanyika kesho (Februari 27 mwaka huu) saa 4 asubuhi kwenye ofisi za TFF zilizopo ghorofa ya 3 katika Jengo la PPF Tower, mtaa wa Garden na Ohio.

Symbion kusaidia programu za vijana za TFF


SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) na Symbion Power Tanzania Limited zimesaini makubaliano ambapo kampuni hiyo itasaidia kwenye maeneo matatu ya mpira wa miguu wa vijana.
Makubaliano hayo yametiwa saini leo (Februari 26 mwaka huu) kwenye ofisi za TFF jijini Dar es Salaam. Rais wa TFF, Jamal Malinzi amesaini kwa niaba ya shirikisho wakati upande wa Symbion aliyesaini ni Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni hiyo Peter Gathercoles.
Maeneo ambayo Symbion itasaidia ni ujenzi wa vituo viwili vya kuendeleza vipaji vitakavyojengwa Kidongo Chekundu na Kinondoni mkoani Dar es Salaam, mashindano ya Taifa ya wachezaji wenye umri wa chini ya miaka 12 (U12) yatakayofanyika mwaka huu na kuisaidia timu ya U17 ya Tanzania (Serengeti Boys).
Serengeti Boys itacheza na Afrika Kusini, Julai mwaka huu katika mechi za mchujo kuwania tiketi ya kucheza Fainali za Afrika kwa wachezaji wa umri huo zitakazofanyika mwakani nchini Niger.
Hivyo Symbion imetoa dola 60,000 (zaidi ya sh. milioni 96) kwa ajili ya mashindano ya U12, na dola 50,000 (zaidi ya sh. milioni 80) kwa ajili ya maandalizi ya Serengeti Boys kwa mechi dhidi ya Afrika Kusini.
Rais Malinzi ameishukuru Symbion kwa kukubali kushirikiana na TFF katika mpira wa miguu wa vijana, lakini vilevile amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Jakaya Kikwete kwani ndiye chachu ya kampuni hiyo kuamua kujishirikisha na mpira wa miguu wa vijana.

Ushawahi kula Kuku mwenye ngozi nyeusi tii?!


Kuku weusi
Aina kadhaa za kuku weusi  hupatikana barani Asia, lakini  kuku au ndege aina ya Silkie wa huko China, ndiyo maarufu zaidi.  Ndege hao, kama majina yao yalivyo, huwa wana manyoya yanayofanana na hariri.
Hata hivyo, chini ya uzuri wote huo, ndege hao wana ngozi nyeusi tii!  Ndege hao huuzwa katika nchi za magharibi kama mapambo, ambapo nchini China ni kitoweo cha hali ya juu kwani nyama yake  hupendwa sana.  Pia ndege hao huchukuliwa kama ‘mama wema’ kwani wanaweza kuatamia mayai ya ndege wengine bila kinyongo.
Black-Chicken
Wachina huwaelezea ndege hao kama “kuku wenye mifupa myeusi” au  “wu gu ji” na wamekuwa wakiwala kwa kuamini nyama yao ina tiba tangu karne ya saba au ya nane ambapo wanawake huila kwa ajili ya kuimarisha afya zao baada ya kujifungua. 
 Pia nyama hiyo inaaminika kuimarisha mapafu, tumbo na damu ikiliwa.  Wachina huitumia nyama ya ndege hao kwa kutengeneza supu yake na kuichanganya na viungo na matunda mbalimbali kwa ajili ya tiba.

Utafiti uliofanywa na kuchapishwa mwaka 2011 ulionyesha kwamba hali hiyo ya kipekee ya ndege hao aina ya Silkie ambayo inajulikana kama ‘fibromelanosis’ inatokana na mabadiliko katika jeni.  Mabadiliko hayo kisayansi  huenda sambamba na kuongezeka kwa chembechembe za  rangi ambazo huzifanya sehemu za ndani (mwilini) na mifupa kuwa nyeusi.

Ndege hao pia wana chembechembe za aina ya ‘carnosine’ ambazo huongeza nguvu mwilini.  Watu wenye kutaka kuongeza ukubwa wa misuli huwatumia kwa wingi kwa nia hiyo na kama chakula chenye kuleta nguvu.  Pia hutumika katika kupambana na ugonjwa wa akili wa watoto (autism), kisukari na kupambana na matatizo yanayotokana na uzee.
 
Kwa jumla ndege hao hutumiwa kama tiba ya maumivu ya viungo na kuzuia ugonjwa wa akili ujulikanao kama Alzheimer.
 
Kwa mujibu wa  utafiti wa kisayansi kuhusu kuku nchini Uingereza, mayai ya kuku weusi  ni bora kwa afya hasa yakitumika katika kupika keki.  Yakilinganishwa na mayai mengine, mayai ya kuku weusi yana kiwango kidogo cha tindikali  katika mafuta yake. 
 
 Kwa waliowahi kuila nyama yake, wanasema ina ladha kama ya kuku wa kawaida, lakini baadhi hudai ni tamu zaidi.  Je, ungependa kula nyama ya Silkie ili ufahamu utamu.
Credit:KALUNDE

Ivo Mapunda apatwa pigo zito, afiwa na baba

KIPA namba moja Tanzania, Ivon Philip Mapunda amefiwa na baba yake mzazi Mzee Philip Mapunda jana jioni na anatarajiwa kuzikwa kesho kijijini kwao, Tukuyu Mbeya.
Kipa huyo wa Simba SC, Ivo ameiambia BIN ZUBEIRY leo asubuhi kwamba, Mzee Mapunda aliyekuwa ana umri wa miaka 86 amefariki akiwa katika hospitali ya Ikonda, iliyopo Njombe ambako alikuwa amelazwa kwa takriban miezi miwili na nusu.
Pole mpiganaji; Ivo Mapunda amefiwa na baba yake mzazi jana 

Ivo alisema Mzee Mapunda alikuwa anasumbuliwa na maradhi ya kibofu cha mkojo, sukari na vidonda vya tumbo. 
Ivo aliyekuwa akizungumza akiwa njiani kuelekea Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), Dar es Salaam, amesema mwili wa marehemu kwa sasa upo kijijini Tukuyu tangu usiku wa jana. Pole Ivo na famili yake. Mungu ampumzishe kwa amani Mzee Mapunda.
BIN ZUBEIRY

Jahazi la Manchester Utd lazama Ugiriki, Chelsea kazi leo Uturuki

50/50: Olympiacos' Leadro Salino (left) fights with United's Ashley Young
Manchester Utd walipokuwa wakihenyeshwa uwanjani jana
Nowhere to be seen: United were outplayed in every area in Greece on Wednesday night
Wachezaji wa Manchester United wakiwa hawaamini kilichjowakuta Ugiriki jana
JAHAZI la Manchester United bado linaendelea klukumbwa na dhoruba baada ya usiku wa jana kukubali kipigo cha mabao 2-0 ugenini dhidi ya Olympiacous ambayo ipo kwenye kiwango cha juu.
Kipigo hicho ni cha kwanza kwa Mashetani Wekundu kwa timu hiyo ya Ugiriki katika miaka minne iliyopita kwani Olympiacous ilikuwa haijawahi kuifunga Manchester Utd katika michuano ya kimataifa.
Vijana wa David Moyes,  walishindwa kuhimili vishindo vya vinara hao wa Ligi Kuu ya Ugiriki, kwa kufungwa mabao hayo moja kila kipindi na kupata kibarua kigumu cha kushinda nyumbani kwao kwa mabao 3-0.
Mabao yaliyoiangamiza Manchester Utd na kutimiza tambo za kocha wa timu hiyo ya Ugiriki kwamba wangeshinda mchezo huo, yalifungwa na Alejandro Dominguez aliyefunga dakika ya 38 kabla ya nyota wa Arsenal anayecheza kwa mkopo Olympiacos, Joel Campbell kumaliza udhia katika dakika ya 55.
Kipigo cha Mashetani Wekundu imekuwa kama muendelezo wa aibu kwa timu za England katika hatua hiyo ya 16 baada ya wiki iliyopita Arsenal na Manchester City kufungwa idadi kama hiyo nyumbani na timu za Bayern Munich na Barcelona.
Timu nyingine ya England Chelsea leo itajaribu bahati yake kwa kuvaana na Galatasaray uwanja wa ugenini nchini Uturuki, huku mechi nyingine ya leo ni ile ya Schalke 04 itakayoikaribisha Real Madrid.
Katika mechi nyingine ya mapema jana,  wenyeji Zenit ya Urusi ilifumuliwa mabao 4-2 na wanafainali wa mwaka jana Borussia Dotmund ya Ujerumani ambapo hadi mapumziko walikuwa nyuma 2-0.
Mabao yaliyoiweka Dotmund katika nafasi ya kutinga robo fainali ya Ligi ya Mabingwa ya mwaka huu yalifungwa na Mkhitaryan, Reus kabla ya Robert Lewandowski kufunga mawili na wenyeji yaliwekwa kimiani na Shatov na Hulk.

Azam, Ashanti United hapatoshi leo Chamazi

Ashanti United

Azam Fc
LIGI Kuu ya Vodacom Tanzania Bara inaendelea leo kwa pamoja moja tu kati ya Azam itakayoumana na Ashanti United kwenye Uwanja wa Azam Complex uliopo Chamazi jijini Dar es Salaam.
Azam yenye pointi 37 itakutana na Ashanti yenye pointi 14 ikiwa na kumbukumbu ya kulazimishwa sare ya 2-2 na Prisons na kushindwa kurejea kwenye kilele cha msimamo wa ligi hiyo inayoongozwa kwa sasa na Yanga yenye pointi 38.
Ushindi wowote itakayoupata leo itairejesha Azam katika kiti cha uongozi, japo Ashanti siyo timu ya kubeza kwani katika mechi yao ya mkondo wa kwanza walitoshana nguvu ya kutoka sare ya 1-1.
Katika mechi iliyopita Ashanti inayonolewa na King KIbadeni ilifumuliwa mabao 2-1 na Mtibwa Sugar na pia ipo kwenye nafasi mbaya ya kushuka daraja ikiwa nafasi ya 13 juu ya Rhino Rangers inayoburuza mkia.
Bila shaka pambano hilo litakuwa kali kwa kila timu kutaka kupata ushindi ili kujiweka pazuri katika nafasi walizopo Azam kukwea kileleni, Ashanti kuondoka mkiani.
Wakati huo huo Shirikisho la Soka Tanzania (TFF) limewaagiza wanachama wake- vyama vya mpira wa miguu vya mikoa kuwapatia orodha ya klabu zote za mpira wa miguu zilizosajiliwa katika mikoa yao.
Orodha hiyo inatakiwa kujumuisha namba ya usajili wa klabu, viongozi waliopo madarakani kwa sasa pamoja na mawasiliano yao (namba za simu na anuani za email) na eneo yalipo makao ya klabu husika.
Kwa utaratibu huo, vyama vya mikoa vitakusanya taarifa za klabu zinazocheza ligi ya mikoa, lakini wakati huo vinatakiwa kuwasiliana na wanachama wake (vyama vya wilaya) kupata taarifa za klabu zinazocheza ligi za wilaya na baadaye kuziwasilisha TFF.
Klabu ambazo taarifa zake zitakuwa hazijawasilishwa TFF hadi Agosti mwaka huu hazitaruhusiwa kushiriki ligi ya msimu wa 2014/2015 katika ngazi yoyote ile.
Naye Rais wa TFF, Jamal Malinzi atakuwa na mkutano na waandishi wa habari juu ya programu ya mpira wa miguu kwa vijana.
Mkutano huo utafanyika kesho (Februari 26 mwaka huu) saa 5 asubuhi kwenye ofisi za TFF zilizopo ghorofa ya 3 katika Jengo la PPF Tower, mtaa wa Garden na Ohio.

Kaseja atemwa Taifa Stars, 22 waitwa kuivaa Namibia

SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) limetangaza kikosi cha wachezaji 22 kwa ajili ya mechi ya kirafiki ya kalenda ya FIFA dhidi ya Namibia (Brave Warriors) itakayochezwa Machi 5 mwaka huu jijini Windhoek, Namibia, ndani yake wakiwemo wachezaji sita wa Yanga SC.
Hata hivyo kipa tegemeo na nahodha wa zamani wa timu hiyo, Juma Kaseja akiwa ameachwa nje.
Kikosi hicho kilichotangazwa na TFF badala ya kocha mkuu wa timu hiyo, Kim Poulsen na kuashiria kupewa 'mkono wa kwaheri' kwa kocha huyo kutoka Denmark na kitakachoingia kambini Machi Mosi na kuondoka nchini Machi 3 kwenda kuivaa wenyeji wao ni pamoja na makipa watatu ambao ni  Deogratius Munishi (Yanga), Ivo Mapunda (Simba) na Mwadini Ally (Azam). 
Wengine waliotajwa ni mabeki wa pembeni ni Edward Charles (JKT Ruvu), Erasto Nyoni (Azam), Hassan Mwasapili (Mbeya City) na Michael Aidan (Ruvu Shooting).
Mabeki wa kati ni Aggrey Morris (Azam) na Kelvin Yondani (Yanga) wakati viungo ni Amri Kiemba (Simba), Athuman Idd (Yanga), David Luhende (Yanga), Frank Domayo (Yanga), Jonas Mkude (Simba) na Mwinyi Kazimoto (Markhiya Sports Club, Qatar).
Washambuliaji ni Athanas Mdamu (Alliance Mwanza), Haruna Chanongo (Simba), Khamis Mcha (Azam), Mbwana Samata (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC), Mrisho Ngasa (Yanga), Ramadhan Singano (Simba) na Thomas Ulimwengu (TP Mazembe, Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo- DRC).
Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itaingia kambini Machi 1 mwaka huu, kwenye hoteli ya Accommondia inatarajiwa kuondoka Machi 3 mwaka huu kwenda Windhoek.
TFF imesema wachezaji ambao timu zao zinacheza mechi za mashindano ya kimataifa na ligi wikiendi hii wataripoti kambini mara baada ya mechi zao kumalizika.

Kuziona Yanga na Al Ahly Buku 7 tu

http://gatemedia.ahram.org.eg/english/News/2012/10/29/2012-634871100531794113-179.jpg
Al Ahly ya Misri
Yanga ya Tanzania
WAKATI Al Ahly wakitua nchini leo, viingilio vya pambano mkondo wa kwanza raundi ya kwanza ya Ligi ya Mabingwa Afrika kati ya watetezi hao kutoka Misri na Yanga litakalofanyika Jumamosi hii uwanja wa Taifa, Dar es Salaam huku kile cha chini kabisa kitakuwa ni Sh. 7,000.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na klabu ya Yanga ni kwamba watu watakaoketi jukwaa la viti vya rangi ya Chungwa, wakati VIP A tiketi moja itauzwa kwa Sh. 35,000 na kwa viti vya VIP B na C Sh. 25,000.
Na kwamba wapinzani wa yaani Al Ahly wanatarajiwa kuwasili asubuhi hii na watafikia katika hoteli ya Hyatt Regency, Kempinsky au Kilimanjaro Hotel, iliyopo maeneo ya Kivukoni.
Waarabu hao wanaweza kufanya mazoezi kwenye Uwanja wa Gymkhana, uliopo kando ya bahari ya Hindi na kikosi wanachotarajiwa kuja nacho Dar es Salaam ni makipa; Sherif Ekramy, Ahmed Adel Abdel-Monem na Mahmoud Abou El-Sooud.
Mabeki ni; Wael Gomaa, Sherif Abdel-Fadil, Ahmed Fathi, Mohamed Naguib, Saad El-Din Samir, Sayed Moawad na Ahmed Shedid Qenawy.
Viungo ni; Hossam Ashour, Shehab El-Den Ahmed, Ahmed Nabil Manga, Ahmed Shokry, Mahmoud ‘Trezeguet’, Rami Rabia, Walid Soliman, Abdullah El-Said na Mohamed Abou-Treika na washambuliaji El-Sayed Hamdy, Dominique  Da Silva, Emad Meteb na Amr Gamal ambaye ndiye tegemeo la mabao la timu hiyo kwa sasa.