STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, August 11, 2013

HILI NDILO TAMKO LA JESHI LA POLISI KUHUSU SHEIKH PONDA ISSA PONDA



1.  MNAMO TAREHE 10, AGOSTI ,2013 MAJIRA YA SAA 8 MCHANA, MAENEO YA SHULE YA MSINGI KIWANJA CHA NDEGE MANISPAA YA MOROGORO,  KULIFANYIKA KONGAMANO LA BARAZA LA EID LILILOANDALIWA NA UMOJA WA WAHADHILI MKOANI MOROGORO. DAKIKA KUMI KABLA YA KONGAMANO HILO KUMALIZIKA  ALIFIKA SHEKHE PONDA ISSA PONDA AMBAYE ALIZUNGUMZA KWA MUDA MFUPI.
 
2. KONGAMANO HILO LILIFUNGWA  MAJIRA YA SAA 12:05 JIONI AMBAPO WATU WALIANZA KUTAWANYIKA, BAADHI YAO WAKIWA WAMEZINGIRA GARI DOGO ALILOKUWA AMEPANDA SHEKHE PONDA. BAADA YA KUTOKA KATIKA  ENEO HILO, ASKARI WA JESHI LA POLISI WALIZUIA GARI HILO KWA MBELE KWA NIA YA KUTAKA KUMKAMATA SHEKHE PONDA AMBAYE MPAKA SASA  ANATUHUMIWA KWA KOSA LA KUTOA MANENO YA UCHOCHEZI SEHEMU MBALIMBALI HAPA NCHINI YENYE MLENGO WA KUSABABISHA UVUNJIVU WA AMANI.
 
3. BAAADA YA ASKARI KUTAKA KUMKAMATA, WAFUASI WAKE WALIZUIA UKAMATAJI HUO KWA KUWARUSHIA  MAWE ASKARI.  KUFUATIA PURUKUSHANI  HIYO, ASKARI WALIPIGA RISASI HEWANI KAMA ONYO LA KUWATAWANYA.
 
4. KATIKA VURUGU HIZO, WAFUASI HAO WALIFANIKIWA KUMTOROSHA  MTUHUMIWA. HIVI SASA IMETHIBITIKA KUWA SHEKHE PONDA YUKO KATIKA HOSPITALI YA TAIFA YA MUHIMBILI AKITIBIWA JERAHA KATIKA BEGA LA MKONO WA KULIA LINALODAIWA ALILIPATA KATIKA PURUKUSHANI HIZO.
 
5. KUFUATIA TUKIO HILO, TIMU INAYOSHIRIKISHA WAJUMBE KUTOKA JUKWAA LA HAKI JINAI IKIONGOZWA NA KAMISHINA WA JESHI LA POLISI  CP ISSAYA MNGULU IMEANZA KUFANYA UCHUNGUZI WA TUKIO HILO.
 
6. AIDHA, JESHI LA POLISI LINATOA  WITO KWA  WANANCHI KUWA WATULIVU WAKATI SUALA HILI LINASHUGHULIKIWA KISHERIA.
 
Imetolewa na:-
Advera Senso- SSP
Msemaji wa Jeshi la Polisi.

TPBO Limited 'yamfungia' bondia kwa udanganyifu

Bondia Ramadhani Kido aliyefungiwa na TPBO
OGANAIZESHENI ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBO-Limited) imemfungia kwa muda usiojulikana bondia machachari, Ramadhani Kido kwa madai ya kufanya udanganyifu katika pambano lake dhidi ya Chupaki Chipindi na kusababisha kutokea vurugu ukumbini.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Rais wa TPBO-Limited, Yassin 'Ustaadh' Abdallah', Kido alifanya udanganyifu kwa kujiangusha ulingoni sekundu chache baada ya pambano lake na Chipindi kufanyika kwenye ukumbi wa Dar Live na kusababisha usumbufu mkubwa.
Ustaadh, alisema Kido alijiangusha na kugoma kuendelea na mchezo wakati mpinzani wake alipomrushia konde ambalo hata hivyo alikumpata na kufanya mashabiki waliofurika ukumbini kurusha chupoa za maji na kutukana kitu ambacho alisema TPBO haikikubali.
Alisema kilichofanyika ni udanganyifu kama aliowahi kuufanya Francis Cheka kwa kukataa kucheza na Japhet Kaseba na wao kumfungia kwa muda kabla ya kumasamehe, hivyo hata kwa Kido hali itakuwa hivyo kwa vile ameonyesha siyo wanamichezo.
Ustaadh alisema mara baada ya kumalizwa kwa pambano hilo kwa Kido kupigwa kwa KO ya sekunde 23, alimhoji sababu ya kufanya uhuni ule na kwa maelezo yake alimwambia kuwa mpinzani wake alipanda na 'jini' ulingoni lililomdhibiti kitendo alichodai ni kuingiza ushirikina katika michezo.
"Vitendo kama hivi huwa hatukubaliani navyo, tunaamini kabisa bondia huyu hakutaka kupigana ila aliingia mkataba na waratibu ambao ni Global Publishers, hivyo mbali na kumfungia pia tunamtaka arudishe fedha alizochukua kwa pambano hilo," alisema Ustaadh.
MICHARAZO halikubahatika kumpata Kido kusikia maoni yake juu ya tuhuma hizo na adhabu aliyopewa na TPBO, ingawa mashuhuda wa pambano hilo ambalo lilifuatiwa na pigano kali kati ya Francis Miyeyusho aliyemnyuka Mzambia Fidelis Lupapa, ni kwamba Kido alijiangusha.
"Sijawahi kuona bondia anaanguka na kugoma kucheza bila hata kuguswa na ngumi, huu ni uhuni na tumeibiwa fedha zetu. Mambo haya ndiyo yanayofanya ngumi za Tanzania zisiendelee kwa vile zinakatisha tamaa waaandaaji na mashabiki," alisema Ally Kisa 'Kingkong' mmoja wa mashuhuda wa michezo hiyo ya Eid Mosi aliyezungumza na MICHARAZO mapema leo.

Benchi la Ufundi linachekaaaaaa!


BENCHI la ufundi la klabu ya Yanga limeusifia usajili wao iliyofanya safari hii na kutamba kuwa hawaoni cha kuwazuia kutetea tena taji lao la Ligi Kuu Tanzania Bara.
Kocha Msaidizi wa Yanga, Fred Felix Minziro, aliiambia MICHARAZO kuwa, kwa namna usajili wao ulivyofanywa kwa umakini mkubwa na hasa safu yao ya mbele kunawapa nafasi ya kuwa ya kutetea taji lao na kufanya vyema kwenye mechi za kimataifa ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Minziro alisema, msimu wa 2013-2014 unaoatarajiwa kuanza wiki mbili zijazo utakuwa wao kwa kuringia wachezaji iliyonayo na namna wanavyojiandaa, huku wakiionya mapema Azam kwamba wajiandae na kipigo Jumamosi katika mechi ya Ngao ya Hisani.
Yanga na Azam zitaumana katika uwanja wa Taifa Dar es Salaam kuashiria kuanza kwa msimu mpya, ambapo wana lamabalamba wenyewe walijichimbia Afrika Kusini na wanatarajiwa kuwasili kesho baada ya kambi ya wiki moja ugenini.
"Kikosi kipo imara na vijana wanatuma matumaini makubwa ya kufanya vyema msimu huu kuliko ilivyokuwa msimu uliopita. Kifupi tunaamini tutatetea taji letu kwa sababu hatuoni kitu cha kutuzuia kuanzia kikosi tulichonacho hadi maandalizi tuliyofanya," alisema.
Minziro aliongeza kushika kwa wepesi kwa maelekezo ya makocha kwa wachezaji wageni kikosini kunawafariji na kuwapa fursa ya benchi lao kumtumia mchezaji yeyote wakati wowote katika mechi yoyote bila tatizo.
"Wachezaji wageni wameshika haraka maelekezo kitu ambacho kimeturahisishia kazi na ndiyo maana tunaamini kwa silaha hizi tulizonazo sijui kama kuna timu itakayofua dafu mbele yetu," alisema Minziro beki wa zamani wa kimataifa wa Yanga na Taifa Stars.
Yanga inatarajiwa kukata utepe wa Ligi Kuu kwa kuumana na Ashanti United ambayo imejichimbia Kigoma na mwishoni mwa wiki wanatarajiwa kucheza mechi mbili na timu za nchini Burundi walikozifuata ili kujiweka fiti kabla ya kuwavaa watetezi hao wa ligi.
Jioni ya leo iliendeleza ubabe katika mechi zake za kirafiki za kujipima nguvu kwa kuilaza SC Villa ya Uganda kwa mabao 4-1 ikiwa ni ushindi wa tatu mfululizo baada ya awali kuilaza Mtibwa Sugar 3-1 kisha kuikamua kiduchu 3 Pillars ya Nigeria kwa bao 1-0.

Cheka abadilishiwa bondia pambano la WBF

Francis Cheka

Bondia Phil Williams ndiye atakayepigana na Cheka,

WAKATI akiendeleza rekodi yake ya kutopigwa katika ardhi ya Tanzania kwa karibu miaka 10 sasa, bondia Francis Cheka 'SMG' amebadilishiwa mpinzani atakayepigana naye Agosti 30 kuwania ubingwa wa WBF ulio wazi kwa sasa kutoka Findley Derrick hadi Phil Williams.
Mabondia wote hao wawili waliobadilioshana ili kupigana na Cheka anayeshikilia ubingwa wa IBF Afrika na mikanda minginje inayotambuliwa kimataifa wanatokea Marekani.
Rais wa Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBO-Limited), linalosimamia pambano hilo la kimataifa litakalochezwa kwenye ukumbi wa Dimaond Jubilee,  Yassin Abdallah 'Ustaadh' alisema Derrick ameondolewa kwa kukosa sifa za kupigana a Cheka.
Ustaadh alisema baada ya kupitiwa kwa rekodi za mabondia wote ilionekana Cheka amemuacha mbali Derrick na hivyo WBF ikamteua Williams anayeshikilia nafasi ya 45 duniani kati ya mabondia zaidi ya 900 wa uzito wa Super Middle kupigana na Mtanzania huyo.
Cheka yeye yupo nafasi ya 34 duniani katika uzito huo tofauti na ilivyokuwa kwa Derrick anayeshikilia nafasi ya 95 kati ya mabondia 1220 wa uzani wa kati, kitu ambacho kingempa nafasi nzuri Cheka kumshinda kirahisi mpinzani wake kwa wasifu na vigezo hiovyo.
Rais huyo wa TPBO-Limied alisema kutokana na hali hiyo ndiyo ikaamuliwa Derrick aenguliwee na nafasi yake kupewa Williams ambapoa tayari Cheka ameshataarifiwa juu ya mabadiliko hayo na anapaswa kujiandaa vyema ili kuipeperusha vizuri bendera ya Tanzania.
"Haya ni mabadiliko ya kawaida, hivyo kila kitu kinaendelea vyema juu ya maandalizi ya mchezo huo ambao ufasindikizwa na  mingine kadhaa ukiwamo wa kuwania ubingwa wa Afrika wa WBF kati ya Thomas Mashali na Mada Maugo," alisema Ustaadh.
Wakati akibadilishiwa mpinzani, Cheka juzi alimfumua Mmalawi Chiotcha Chimwemwe kwa pointi na kuendeleza rekodi ya kutipigwa katika ardhi ya Tanzania tangu Agosti 2013.
Cheka alimshinda Mmalawi huyo katika pambano lisilo la ubingwa lililofanyika kwenye uwanja wa Jamhuri Morogoro lililokuwa la raundi nane, ingawa baadhi ya mashabiki wanaamini kuwa Mtanzania huyo alibebwa mbele ya Chiotcha.
Hiyo ni mara ya pili kwa Cheka kumpiga Mmalawi huyo na kuibua hisia hizo baada ya awali kufanya hivyo Desemba 24 jijini Arusha walipokuwa wakiumana kuwania taji la IBF Afrika, ambapo Cheka alishinda na kutetea taji hilo kwa pointi huku akiachiwa majeraha makubwa.

Ajali nyingine ya basi, safari hii basi la Meridian

MATUKIO ya ajali za barabarani kwa mabasi ya abiria yameendelea baada ya leo tena basi la kampuni ya Meridian kupata ajali mbaya katika  eneo la Mbwewe, mjini Bagamoyo.
BASI la Meridian linalofanya safari zake Dar es Salaam na Rombo limepata ajali mbaya eneo la Mbwewe Bagamoyo
mkoani Pwani likiwa safarini kuelekea jijini Dar es Salaam likitokea Rombo.
Abiria kadhaa wamepoteza maisha katika ajali hiyo japo idadi kamili bado haijafahamika.

Chanzo: Jamii Forum
Baadhi y abiria walinusurika wakisaka mizigo yao baada ya ajali hiyo iliyopoteza uhai wa watu kadhaa

Hatimaye yathibitika Sheikh Ponda kujeruhiwa kwa risasi angalia picha zake

Jeraha la Sheikh Ponda linavyoonekana kwa karibu

Sheikh Ponda akiwa hospitalini


Sheika Ponda akiwa wodini Muhimbili

BAADA ya danadana ya Polisi kukwepa ukweli juu ya tukio la kupigwa risasi na kujeruhiwa kwa Sheikh Ponda Issa Ponda, ukweli sasa upo hadharani baada ya kiongozi huyo wa Umma wa Kiislam kuonesha jeraha hilo hadharani akiwa kalazwa Muhimbili.
Awali Polisi mkoa wa Morogoro kupitia Kamanda wake Faustin Shilogile lilikuwa likidai halijui lolote kuhusu tukio hilo, licha ya kukiri kwamba ilitaka kumkamata kiongozi huyo kipenzi wa waislam walio wengi.
Tangu jana vyombo vya habari vikitumia vyanzo vyake vya habari kutoka mjini humo ikiwemo MICHARAZO viliripoti juu ya tukio hilo ambalo lilitokea jioni mara baada ya Sheikh huyo kuhutubia kwenye Kongamano la Kiislam, lakini Polisi ikawa inavunga kuwa haujui lolote.
Hatimaye sheikh huyo alitua jijini mchana kwa matibabu katika hospitali ya Muhimbili na 'kuwaumbua' wale waliokuwa wakikanusha taarifa hizo kwamba hakuna kilichotokea juu ya kujeruhiwa kwake.
Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba amezungumza jijini Dar leo na kumtaka Rais Jakaya Kikwete na IGP Saida Mwema kuangalia namna ya kuthibiti jeshi la Polisi juu ya matumizi ya risasi za moto kwa raia wasio na silaha yoyote.
Matukio ya polisi kuwatwanga risasi raia kwa sasa imekuwa kama fasheni, kitu ambacho kinawatia hofu raia juu ya umakini wa askari wa jeshi hilo ambalo ni la usalama wa raia na mali zao.

Yanga kama Simba, Ngassa atupia moja wakiiua Sc Villa 4-1

Na Prince Akbar YANGA SC imetuma salamu Johannesrbug, Afrika Kusini ambako Azam FC wameweka kambi kujiandaa na msimu mpya- kufuatia ushindi wa mabao 5-1 leo katika mchezo wa kirafiki dhidi SC Villa ya Uganda, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam. Yanga na Azam zitamenyana Jumamosi ijayo Uwanja wa Taifa, katika mechi ya kuwania Ngao ya Jamii, kuashiria ujio wa msimu mpya wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara. Azam imeweka kambi Afrika Kusini kujiandaa na mechi hiyo ya kufungua msimu na Yanga wanaendelea na maandalizi yao Dar es Salaam, wakitarajiwa kuingia kambini baada ya mechi ya leo kisiwani Pemba, au Bagamoyo, Pwani.
Akaunti mpya; Ngassa amefungua akaunti
mpya ya mabao Yanga leo
Katika mchezo wa leo, hadi mapumziko, tayari Yanga SC walikuwa mbele kwa 3-1, mabao yake yakifungwa na Mrisho Ngassa dakika ya saba, Nadir Haroub ‘Cannavaro’ dakika ya 27 na Didier Kavumbangu dakika ya 30, wakati la nne lilifungwa kipindi cha pili na Haruna Niyonzima dakika ya 62. Bao la kufutia machozi la Villa ambayo jana ilifungwa 4-1 pia na Simba Uwanja huo huo wa Taifa, lilifungwa na Moses Ndaula dakika ya 18.    Katika mechi zake za awali za kujiandaa na msimu, Yanga SC ilitoa sare ya 2-2 na URA ya Uganda kabla ya kuzifunga 3-1 Mtibwa Sugar na 3Pillars ya Nigeria 1-0.  Azam nayo imekwishacheza mechi tatu za kujipima nguvu Afrika Kusini, imeshinda moja tu dhidi ya Mamelodi Sundwons 1-0, imefungwa mbili, 3-0 na Kaizer Chiefs na 2-1 na Orlando Pirates na kesho itacheza mechi ya mwisho na Moroka Swallows kabla ya kurejea nyumbani keshokutwa. Kikosi cha Yanga SC leo kilikuwa; Ally Mustafa ‘Barthez’, Juma Abdul, David Luhende/Oscar Joshua, Nadir Haroub ‘Cannavaro’, Kevin Yondan/Rajab Zahir, Athumani Iddi ‘Chuji’/Bakari Masoud, Mrisho Ngassa, Salum Telela, Didier Kavumbangu, Jerry Tegete/Hussein Javu na Haruna Niyonzima/Said Bahanuzi. 

SEMINA YA MAKAMISHNA YAANZA DAR, MWANZA


Na Boniface Wambura
SEMINA kwa ajili ya makamishna wa Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) na Ligi Daraja la Kwanza (FDL) pamoja na mtihani wa utimamu wa mwili (physical fitness test) kwa  waamuzi wote wa daraja la kwanza (Class I) wanaotaka kuchezesha VPL msimu wa 2013/2014 vinaanza kesho (Agosti 12 mwaka huu) katika vituo vya Dar es Salaam na Mwanza.

Mafunzo hayo yatakayomalizika Agosti 14 mwaka huu yatakuwa chini ya wakufunzi Leslie Liunda, Joan Minja na Riziki Majara kwa kituo cha Dar es Salaam wakati kituo cha Mwanza kitakuwa na Alfred Rwiza na Omari Kasinde.

Kwa Dar es Salaam mafunzo yatafanyika Uwanja wa Taifa wakati Mwanza itakuwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba.

Kituo cha Mwanza kitakuwa na makamishna na waamuzi kutoka mikoa ya Geita, Kagera, Katavi, Kigoma, Manyara, Mara, Mwanza, Shinyanga, Simiyu, Singida na Tabora.

Kituo cha Dar es Salaam kitahusisha waamuzi na makamishna kutoka mikoa ya Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Iringa, Kilimanjaro, Lindi, Mbeya, Morogoro, Mtwara, Njombe, Pwani, Ruvuma na Tanga.

Washiriki wote wanakumbushwa kuwa ni lazima wafuate utaratibu huo wa vituo, na si vinginevyo.

Kagera Sugar yatakata Uganda, kesho kuivaa URA

Kikosi cha Kagera Sugar

KAGERA Sugar iliyosafiri mpaka Uganda jioni ya leo imeanza vyema michezo yao ya kujiandaa na Ligi kuu Tanzania Bara baada ya kuikwanyua Bunawaya Fc kwa bao 1-0 katika pambano la kirafiki la kimataifa lililochezwa jijini Kampala.
Kocha Msaidizi wa Kagera, Mrage Kabange wimba wa zamani wa Simba na Taifa Stars, alisema kikosi chao kilionyesha soka la kuvutia katika pambano hilo licha ya ugeni na kujipatia bao katika kipindi cha kwanza lililofungwa na Juma Mpola.
Timu hiyo itashukla tena dimbani kesho kuumana na URA katika pambano jingine kabla ya kuangalia mechi nyingine na kurejea Kagera tayari kujiandaa na mechi yao ya fungua dimba ya ligi kuu msimu wa 2013-2014 dhidi ya 'wageni'  Mbeya City mechi itakayochezwa uwanja wa Sokoine, Agosti 24.

MAKOCHA 32 KUSHIRIKI KOZI YA FIFA COPA COCA-COLA

 
Na Boniface Wambura
MAKOCHA 32 kutoka mikoa ya Tanzania Bara na Visiwani wanashiriki kozi ya Copa Coca-Cola inayoanza kesho (Agosti 12 mwaka huu) jijini Dar es Salaam chini ya Mkufunzi kutoka Shirikisho la Kimataifa la Vyama vya Mpira wa Miguu (FIFA).

Kozi hiyo itakayomalizika Agosti 17 mwaka huu itafunguliwa saa 3 kamili asubuhi kwenye ukumbi wa Msimbazi Centre na washiriki wote tayari wameshawasili Dar es Salaam. Mkufunzi wa kozi hiyo ni Govinder Thondoo kutoka Mauritius.

Washiriki wa kozi hiyo ni Ahazi Ibrahim Kasegese (Mbeya), Aloyce Mayombo (Pwani), Andrew Zoma (Tabora), Asuri Msakamali (Simiyu), Bakari Khamis Kilambo (Kaskazini Pemba), Chacha Sambulo (Mara), Charles Rwezaura (Kagera), Daniel Sambala (Njombe), Dudu Haruni (Iringa) na Emmanuel Kapurata (Rukwa).

Faki Makame Haji (Kaskazini Unguja), Fatawi Khamis Sheha (Kusini Pemba), Hamisi Omary Mabo (Kigoma), Hussein Maulid (Morogoro), Issa Lugaza (Kilimanjaro), James Gaspar (Shinyanga), James Wambura (Arusha), Jomo Jackson Puccey (Lindi), Joseph Sihaba (Dodoma), Kelvin Haule (Ruvuma) na Kessy Juma Abdallah (Tanga).

Kessy Mziray (Mwanza), Menswi Mchwampaka (Kinondoni), Mohamed Abdallah Kweka (Singida), Nurdin Gogola (Temeke),  Pius Kamande (Rukwa), Ramadhan Abrahman Ramadhan (Mjini Magharibi), Ramadhan Salum Mnyoti (Manyara), Raphael Ngeleja (Geita), Samuel Edgar Maokola (Ilala), Shaweji Nawanda (Mtwara) na Vuai Abdul Haji (Kusini Unguja).

Fainali za U15 Copa Coca-Cola ngazi ya Taifa zitafanyika Septemba mwaka huu jijini Dar es Salaam.

Sheikh Ponda aletwa Muhimbili? Ukweli kuweka hadharani Alasiri Msikiti wa Mtambani

 
HABARI zilizotufikia hivi punde zinasema Sheikh Ponda Issa Ponda ameletwa Dar na kukimbizwa Hospitali ya Muhimbili kwa ajili ya matibabu na tayari kuna habari kwamba Polisi wakiwa kwenye madifenda yao wameshatimba hospitalini hapo.
MICHARAZO inafuatilia taarifa hizo zilizopenyezwa hivi punde kujua ukweli na ikiwezekana kuwatupia na picha kama ni kweli Sheikh huyo machachari na kiongozi wa umma wa waislam walio wengi amepelekwa hospitalini hapo.
Pia taarifa rasmi kuhusu hali ya Sheikh Ponda inatarajiwa kutolewa Alasiri hii katika Msikiti wa Mtambani na Amir wa Shura ya Maimamu Tanzania, Sheikh Mussa Kundecha baada ya kuwepo kwa mkanganyiko juu ya hali ya kiongozi huyo wa umma wa waislam Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda juu ya tukio la kujeruhiwa kwa risasi begani na Polisi wakati alipotaka kukamatwa, japo Polisi wanaendelea kukomaa kwamba hawajui lolote.

Yanga, Sc Villa hapatoshi leo taifa, Javu kuendeleza dozi?

Kikosi cha Yanga
TIMU ya soka ya Yanga, inatarajiwa kushuka dimbani jioni ya leo kuvaana na SC Villa ya Ugannda huku mashabiki wakielekeza macho yao kwa Hussein Javu kuona atawafanyizia vipi wageni hao katika mechi hiyo ya leo.

Javu aliyetua Jangwani hivi karibu akitokea Mtibwa Sugar, ameanza na moto kwa kufunga katika mechi zake mbili za awali akiisiaidia Yanga kuisulubu Mtibwa kwa mabao 3-1 na kuizamisha 3 Pillars ya Nigeria kwa bao pekee katika mechi iliyoichezwa katikati ya wiki.

Villa iliyochezea kichapo cha aibu jana toka kwa Simba, itaikabili Yanga itakayotumia mchezo huo kujiweka vyema kabla ya pambano lake la Ngao ya Hisani dhidi ya Azam litakalofanyika siku ya Jumamosi.

Ofisa Habari wa Yanga, Baraka Kizuguto, alisema jana kuwa maandalizi ya mechi hiyo yamekamilika na kila mchezaji yu tayari kuonesha uwezo wake.

Kwa upande wa Yanga, si tu itaitumia mechi hiyo kujiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu itakayoanza Agosti 24, pia kunoa makali ya kuikabili Azam FC katika mechi ya Ngao ya Hisani itakayochezwa Agosti 17.

Mechi ya Ngao ya Hisani ambayo ni ishara ya ufunguzi wa Ligi Kuu, itachezwa ikiwa ni siku nne tangu Azam warejee nchini wakitokea nchini Afrika Kusini walikokwenda kusaka makali kwa ajili ya msimu mpya tangu Agosti 3, wakicheza mechi za kirafiki.

Wakati Azam wakitokea Afrika Kusini, Yanga wao tofauti na msimu uliopita ambapo walikwenda kujinoa nchini Uturuki kabla ya kuanza kwa ligi hiyo, safari hii wameamua kujifua nyumbani.

Kwa mujibu wa tovuti ya Yanga, Kocha Mkuu wake, Ernie Brandts, amefurahia kwisha salama kwa mazoezi ya nyota wake hadi jana asubuhi, huku akisema hakuna majeruhi hata mmoja kuelekea mechi ya leo.

“Mechi ya kesho (leo) dhidi ya Villa, itakuwa kipimo kizuri kwetu kwani itakuwa ya mwisho kabla ya kuikabili Azam katika mechi ya Ngao ya Hisani na kuanza kwa Ligi Kuu ya Vodacom,” alisema Brandts.

Kwa mujibu wa tovuti ya Yanga, viingilio vya mechi ya leo ni sh 20,000 kwa jukwaa la VIP A; sh 15,000 kwa VIP B; sh 10,000 kwa VIP C na sh 5,000 kwa viti vya rangi ya machungwa, bluu na kijani.

Wapenzi wa soka na mashabiki wa klabu ya Yanga wameombwa kujitokeza kwa wingi kujionea uwezo wa timu yao kuelekea vita ya kutetea ubingwa wake wa Ligi Kuu ya Vodacom ambao iliutwaa msimu uliopita.

Wakati Yanga iliyoanzishwa mwaka 1935 ikimaliza msimu uliopita na ubingwa ukiwa wa 24 tangu mwaka 1965, Villa ni mabingwa mara 16 tangu ianzishwe mwaka 1975, ambapo mara ya mwisho kuonja ubingwa wa Uganda ni mwaka 2004.

Azam yaanza kuingiwa mchecheto kwa Yanga

Na Mahmoud Zubeiry, Johannesburg, Afrika Kusini, IMEWEKWA AGOSTI 11, 2013 SAA 5:05 ASUBUHI
KOCHA Muingereza wa Azam FC, Stewart John Hall ameridhishwa na maandalizi ya timu yake katika kambi ya kujiandaa na msimu hapa Afrika Kusini, lakini kuelekea mchezo dhidi ya Yanga SC Jumamosi ijayo kuwania Ngao ya Jamii, mwalimu huyo anahofia sana juu ya marefa.
Stewart ameiambia BIN ZUBEIRY leo mjini hapa kwamba ana imani na timu yake imenufaika mno na kambi ya Afrika Kusini na inaweza kwenda kuwapa burudani nzuri wapenzi wa soka Tanzania baada ya hapa.
Marefa watende haki; Kocha Stewart Hall kulia akiwa na Msaidizi wake, Kali Ongala. Amemba marefa watende haki Agosti 17 Taifa dhidi ya Yanga.

Hata hivyo, Stewart amesema mchezo wa kufungua pazi la Ligi Kuu dhidi ya Yanga, Agosti 17, wasiwasi mkubwa ni marefa kuwabeba wapinzani wao siku hiyo.
“Nina wasiwasi na marefa, tena sana. Mara ya mwisho tulipocheza na Yanga, walitufunga 1-0, lakini refa alitunyima penalti na akakataa bao letu lililofungwa na John Bocco,”.
“Imekuwa kawaida unapocheza na Simba SC au Yanga, marefa wanakuwa upande mwingine. Sasa kama na kwenye mechi ya Ngao itajirudia hivyo, itakuwa mbaya. Naomba marefa watakaopangwa wachezeshe kwa haki,”alisema Stewart.
Azam ipo hapa tangu Agosti 3, kwa ajili ya kujiandaa na msimu- ambapo wataanza na mechi ya kuwania Ngao ya Jamii dhidi ya Yanga SC, Agosti 17, mwaka huu, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mwaka jana, Azam FC ilifungwa 3-2 na Simba SC katika mechi ya kuwania Ngao, licha ya kuongoza kwa mabao 2-0 hadi mapumziko, lakini kocha Stewert amepania kubeba ‘Ubao’ safari hii.  
Kikosi kazi; Kikosi cha Azam katika moja ya mechi zake hapa Afrika Kusini

Tangu iwasili hapa, Azam, ambayo imekuwa ikijifua katika viwanja vizuri vya Chuo Kikuu cha Wits, ikitokea kwenye hoteli ya nyota tano, Rundburg Towers, imekwishacheza mechi tatu na kufungwa mbili, ikishinda moja.
Ilifungwa 3-0 katika mchezo wa kwanza na Kazier Chiefs, ikashinda 1-0 katika mchezo uliofuata na Mamelodi kabla ya kufungwa 2-1 na Orlando Pirates, wakati kesho itacheza mechi ya mwisho na Moroka Swallows kabla ya Jumanne kurejea Dar es Salaam.

Yathibitika Sheikh Ponda yu hai na kisa cha kupigwa risasi hiki hapa!



KATIBU wa Jumuiya ya Kiislamu nchini , Shekhe Ponda Issa Ponda, alijikuta katika wakati mgumu baada ya kuumizwa na kitu kinachodhaniwa kuwa ni risasi kwenye bega lake la kulia wakati akiekelea katika Msikiti wa Mungu Mmoja Dini Moja wa Mjini Morogoro baada ya kumalizika kwa kongamano ya Dini ya Kiislamu.

Mkasa huyo ulitokea jana Jumamosi Augosti 10, mwaka huu majira ya saa 12: 15 za jioni eneo la barabara ya Tumbaku karibu na Fire, mara baada ya kumaliza kwa Kongamano la Kiislamu lililofanyika kwenye uwanja wa Shule ya Msingi Kiwanja Cha Ndege, Kata ya Saba Saba , Manispaa ya Morogoro.
 

Shekhe  Ponda alishiriki katika Kongamano hilo lililoandaliwa na Umoja wa Wahadhiri wa Dini ya Kiislamu Mkoani Morogoro na kufanyika siku ya Idd Pili kuanza saa nane mchana hadi kumi na mbili jioni ya siku hiyo. 
 

Kongamano hilo lilipata baraka zote na Jeshi la Polisi Mkoani Morogoro, ambalo lilitoa  masharti kadhaa ya kuzingatiwa na wazungumzaji ikiwa ni kutokashifu dini nyingine wala viongozi wa serikali. 
 

Sakata la kutaka kutiwa mbaroni kwa Shekhe Ponda lilikuja baada ya yeye kudaiwa kukiuka masharti ya Mahakama aliyopewa baada ya kuhukumiwa kifungo cha mwaka mmoja nje wa  kutakiwa asitende kosa lolote la jinai anapotumikia adhabu hiyo. 

Mwenyekiti wa Kamati ya Maadalizi ya Kongamano hilo, Ustaadh Idd Msema, alidai kuwa Shekhe Ponda baada ya kutoka ndani ya gari eneo la Uwanja wa Shule ya Msingi Kiwanja Cha Ndege aliofika mita chache katika barabara ya Tumbaku aliteremka na wakati akitaka kuingia garini ilifyatuliwa risasi iliyompiga begani. 
 

Ustaadh Msema alidai kuwa baada ya kupigwa risasi begani waumini waliokuwa wameambatana naye walimchukua na kumpakiza kwenye Piki Piki hadi Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro ili kupatiwa matibabu. 
 

Kwa mujibu wa Mwenyekiti huyo, baada ya kufika hospitali, waliona anacheleweshwa kupatiwa matibabu na ndipo walipoamua kumwondoa na kumpekea kwenye Hospitali binafsi ambayo hakupenda kuitaja. 
 

Akizungumzia kwa kina hali ya Shekhe Ponda baada ya kujeruhiwa huko, alisema kuwa yu hai licha ya kuumia vibaya begani na kwamba wanatarajia kumpekela eneo jingine hususani Jijini Dar es Salaam kupata matibabu zaidi.
 

Alisema viongozi wa Umoja huo hauwezi kuweka wazi sehemu anakotibiwa kwa kuwa jambo hilo ni la kiusalama zaidi hasa wakati huu ambapo kumekuwa na sinto fahamu.
 

Baadhi ya walinzi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro waliozungumza juu ya tukio hilo , walikiri kuwa Shekhe Ponda aliletwa hapo kwa usafiri wa Piki piki zikiambatana na nyingine zaidi ya 50 na kuishia getini. 
 

Walisema walimwingiza hadi mapokezi na kwamba walipoona umati mkubwa upo getini waliamua kutoa taarifa Polisi kuwa wamevamiwa na watu ambapo muda si mrefu Polisi wa FFU waliwasili na gari lao Hospitalini hapo.  
 
Hata hivyo walinzi hao walisema, baada ya kuona Askari wamefika Hospitalini hapo, baadhi ya wafuasi wa Shekh Ponda waliamua kumnyanyua na kumbeba mabegani na kutoka naye mlango mwingine wakimlazimisha mlinzi kuwafungulia mlango na baadaye wakatokomea naye kwa usafiri wa Pikipiki kusikojulikana. 

Kufikishwa kwa Sheikh Ponda katika Hosipitali ya Rufaa kulithibishiwa pia na Mwenyekiti huyo ambaye alidai  kuwa waliamua kumwondoa baada ya kuchekewa  kupatiwa huduma. 
 

Baada ya tukio hilo, uvumi ulisambaa maeneo mbalimbali nchini ukidai kuwa Sheikh Ponda amepigwa risasi na Polisi na kufariki dunia. 

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Morogoro, Feustine Shilongine akizungumza na Mwandishi wa Habari hizi majira ya saa tatu usiku wa Augosti 10, baada ya kutokea kwa tukio hilo, alisema kuwa hapakuwa na taarifa juu ya kutokea kifo cha Shekhe Ponda. 
 

“ Nimepigiwa simu zaidi ya 50 , zikiulizia jambo hili...kuwa Ponda amefariki dunia ...Binafsi nami ninazisikia , ujumbe umesambazwa kwenye simu za watu mbalimbali...tumezunguka kila mahali hakuna kifo wala maiti yake ...na vijana wangu wanaendelea kulifuatilia suala hili” alisema Kamanda huyo. 

Juhudi za kufuatilia sakata la uvumi kifo cha Sheikh Ponda uliendelea kufanyiwa kazi na Ripota wetu huyu na usiku wa saa tano Mwenyekiti wa Kamati huyo aliweka wazi kwa kusema kuwa Sheikh huyo machachari yu hai isipokuwa ameumia vibaya sehemu ya bega . 
 

 “ Nipo katika eneo ambalo Shekhe Ponda anapatiwa matibabu...sehemu ambayo hatuwezi kupataja kiusalama , isipo kuwa ameumia vibaya kwenye bega lake.

 "Lakini yu hai wala hajafa” alisema Msema.

 Askari wa FFU wakijisogeza kati kati ya uwanja mara baada ya muda wa kongamano kumalizika.

 Kutambulishwa jukwaani Shekh Ponda.

 Kikosi cha FFU uwanjani

 Shekh Ponda akikaribishwa kwenye jukwaa kuu baada ya kuwasili kwenye viwanja vya shule ya Msingi Kiwanja Cha Ndege , mjini Morogoro

 Shekh Ponda akisalimiana na Mhadhiri wa Mihadhara nchini, Ustaadhi Abubakari

 Shekh Ponda akisisistiza jambo mbele ya waumini wa Dini ya Kiislamu kwenye Kongamano , Augosti 10, mwaka huu mjini Morogoro

 Shekh Ponda akiteta jambo na baadhi ya Viongozi wa umoja wa Wahadhiri wa Dini ya Kiislamu Mkoa wa Morogoro

 Shekhe Ponda akiwa meza kuu kwenye kongamano hilo

 Shekhe Ponda akiwa amezingirwa na waumini

 Umati wa waumini wa Kiislamu wakimsikiliza Shekh Pond




Waumini wa Dini ya Kiislamu wa mjini Morogoro wakimsikiliza Shekh Ponda


Waumini wa Kiislamu wakitawanyika uwanjani baada ya muda wa kongamano kufikia tamati


The Choice

Huyu alijeruhiwa vurugu za msikitini Kyela Mbeya

HUYU ni mmoja ya watu waliojeruhiwa katika vurugu wakati wa sala ya Idd zilizotokea jana katika msikiti wa Kyela mkoani Mbeya. Anatambuliwa kwa  jina la  Khamis Hussein na alijeruhiwa na kitu chenye ncha kali na kushonwa nyuzi tatu.

Pichani akiwa hospitali mara ya kupewa matibabu.

Kiza kinene chatanda sakata la kupigwa risasi Sheikh Ponda

Katibu wa Kamati ya Kutetea Haki za Waislam Tanzania, Sheikh Ponda Issa Ponda.
MPAKA muda huu bado hatujaweza kupata taarifa nyingine zozote kuhusu tukio la kupigwa kwa risasi kwa Sheikh Ponda Issa Ponda lililotokea mjini Morogoro.
Juhudi zetu zimeishia kupata taarifa kama tulizowafahamisha mapema, huku jeshi la Polisi likisisitiza kutohusika na kitendo hicho, licha ya mashuhuda kueleza kwamba Polisi walifyatua mabomu ya machozi na risasi za moto ambayo moja ilimpata Ponda begani.
Kadhalika hakuna ukweli wowote kwamba Sheikh Ponda amefariki dunia kama baadhi ya watu wanavyovumisha, kwa sababu mpaka tunapoandika taarifa hii kwenu tumefahamishwa kuwa sheikh huyo alikuwa kajeruhiwa na hakukuwa na yeyote kati ya vyanzo vya habari au hata Polisi wenyewe kuthibitisha juu ya Ponda kuaga dunia.
Hivyo wasomaji wa MICHARAZO, endeleeni kuvuta subira kupata ukweli wa kinachoendelea badala ya kupandwa presha kwamba Kiongozi huyo wa Umma wa Kiislam anayependwa kila kona ya nchi kwa harakati zake za kupigania haki za waislam walio wanyonge huenda amefariki.
Pia kama ni kweli Sheikh Ponda atakuwa amefariki basi ni mipango ya Mungu kwa vile kila nafsi itaonja mauti, ila ukweli ulivyo ni kwamba hakuna taarifa za kupoteza kwake maisha zaidi ya hizo za kujeruhiwa na pia haifahamiki kwa sasa yupo wapi, kitu ambacho hata Polisi kimesema na kutangaza kumsaka na kutaka wenye taarifa juu ya alipojichimbia Sheikh huyo watoe taarifa haraka. Vuteni subira.

Cheka aendeleza ubabe katika Masumbwi amtwanga Mmalawi mjini Morogoro

Francis Cheka 'SMG'

BINGWA wa IBF Afrika, Francis Cheka ameendeleza ubabe mbele ya mabondia wenzake baada ya usiku huu kumshinda kwa pointi Mmalawi Chiotcha Chimwemwe katika pambano lisilo la ubingwa lililochezwa kwenye Uwanja wa Jamhuri Morogoro.
Cheka amepata ushindi huo katika pambano hilo la raundi 8 japo baadhi ya mashabiki wamedai Mtanzania huyo amebebwa tena kama ilivyokuwa mjini Arusha alipomtwanga Chimwemwe na kutetea taji lake la IBF Desemba mwaka jana.
Ushindi huo umeendeleza rekodi ya Cheka ya kutopigwa katika ardhi ya Tanzania tangu Agosti, 2003 na kwa sasa atakuwa akijiandaa na mchezo wake mwingine lakini wa kimataifa kuwania mkanda wa WBF dhidi ya Mmarekani, Phil Williams atakayepigana naye Agosti 30 katika ukumbi wa Diamond Jubilee.
Pia ushindi huo wa Cheka umekuja saa chache baada ya Mtanzania mwingine na bingwa wa UBO Afrika, Francis Miyeyusho kumtwanga Mzambia Fidelis Lupapa katika pambano lisilo la ubingwa lililofanyika jana kwenye ukumbi wa Dar Live, Mbagala Dar es Salaam.
Miyeyusho alimtwanga Mzambia huyo kwa KO ya raundi ya 8 kati ya 10 zilizopangwa zichezwe katika kusindikiza sherehe za sikukuu ya Eid el Fitri.