STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, December 31, 2012

Majeraha yamzuia Cheka kurudiana na Mmalawi

Bondia Francis Cheka 'SMG'


BINGWA anayeshikilia mataji manne tofauti likiwemo la IBF, bondia Francis Cheka 'SMG' hataweza kupambana kwa mara nyingine tena na Mmalawi, Chiotra Chimwemwe kutokana na kuumia katika pambano lao la kwanza lililochezwa jijini Arusha wiki iliyopita.
Cheka na Chimwemwe walitarajiwa kuvaana mjini Addis Ababa, Ethiopia katika pambano maalum la kusindikiza mkutano wa Viongozi Wakuu wa nchi za Afrika, Januari 26.
Mabondia hao wangepigana kuzindikiza pambano la kimataifa kati ya Oliver McCall wa Marekani dhidi ya Sammy Retta wa Ethiopia kuwania ubingwa wa uzito wa juu IBF (IBF AMEPG).
Rais wa IBF/USBA, Onesmo Ngowi, alisema nafasi ya Cheka imechukuliwa na mkali mwingine nwa ngumi za kulipwa nchini katika uzito wa juu, Alphonce Mchumiatumbo, ingawa haijafahamika atapigana na nani.

Ngowi alisema mapambano mengine siku hiyo ya Januari 26 ni pamoja na lile la Mkenya, Daniel Wanyonyi dhidi ya Issac Hlatswayo wa Afrika Kusini watakaowania ubingwa wa IBF AMEPG uzito wa Welterweight
Pambano jingine litawakutanisha Manzur Ali wa Misri dhidi ya Harry Simon wa Namibia watakaowania taji la IBF AMEPG uzito wa Light heavyweight.

Minziro atamba Yanga moto ule ule

Fred Minziro (kulia) katika moja ya majukumu yake uwanjani

KOCHA Msaidizi wa klabu ya Yanga, Fred Felix Minziro, ametamba kwamba moto waliomalizia nao kwenye duru la kwanza la Ligi Kuu Tanzania Bara, ndiyo watakaoanza nao katika duru lijalo, huku akisisitiza lazima Yanga iwe bingwa 2012-2013.
Aidha kocha huyo ametamba kwamba timu yao imejipanga ili kuhakikisha wanatetea taji lao la Kombe la Kagame katika michuano itakayofanyika hivi karibuni nchini Rwanda.
Akizungumza na MICHARAZO kabla ya kupaa na timu kwenda Uturuki, Minziro, beki wa kimataifa wa zamani wa Yanga na Taifa Stars, alisema ubora wa kikosi alichonacho na namna  wanavyojiandaa, inampa imani ya kuamini kwamba Yanga itawavua ubingwa wa ligi watani zao, Simba msimu huu.
Minziro, alisema Yanga itaendeleza moto ule ule waliomalizia nao duru la kwanza la ligi hiyo iliyowatoa nafasi za kati mpaka kileleni ikiwaengua waliokuwa vinara Simba na Azam, ili mwisho wa msimu klabu yao iwe mabingwa wapya wa Tanzania.
"Hatudhani kama tutaanza kinyonge kama ilivyokuwa katika duru la kwanza, tupo katika maandalizi kabambe ili kuhakikisha tunaendeleza moto na kasi yetu ili kurejesha taji tuliloporwa na watanbi zetu, Simba," alisema Minziro.
Minziro, alisema japo anatambua duru lijalo litakuwa lenye ushindani mkubwa, lakini wao wamejiandaa vya kutosha kuhakikisha wanafanya vema, huku akisisitiza kuwa maandalizi yao yanalenga pia kwenda kutetea taji lao la Kombe la Kagame njini KIgali.
"Macho na akili zetu zote tumezielekeza kwenye duru la pili la ligi pamoja na michuano ya Kagame, tungependa kwenda kutetea taji ugenini, tunajiamini na wachezaji wana ari kubwa ya kufanya hivyo," alisema Minziro.
Yanga inayoongoza msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara ikiwa na pointi 29, tano zaidi ya Azam waliopo nafasi ya pili na sita zaidi ya watani zao Simba wanaoshika nafasi ya tatu, ilitwaa taji hilo la Kagame Julai, 2012 kwa kuilaza Azam mabao 2-0 katika mchezo fainali zilizochezwa kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es Salaam.

Mtanzania kuwania taji la Jumuiya ya Madola


BONDIA machachari wa ngumi za kulipwa nchini, Fadhili Majia ameteuliwa na Bodi ya Wakurugenzi ya Baraza la Ngumi la Jumuiya ya Madola (CBC) kupigana na Isaac Quaye wa Ghana kuwania nafasi ya kupigana na bingwa Kevin Satchell wa Uingereza.
Mabondia hao wanatarajia kupigana katika pambano hilo la uzani wa Fly Februari 22 mwakani kwenye mji wa Accra, Ghana ambapo mshindi wa mechi hiyo ya mchujo atapata fursa ya kupigana na Satchell anayeshikilia taji hilo la Jumuiya ya Madola.
Rais wa Kamisheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBC) Onesmo Ngowi ambaye ni mmoja wa wakurugenzi wa CBC, alisema wajumbe wa bodi hiyo walimpigia kura Majia baada ya yeye kulipendekeza na hiyo kuibuka kidedea.
Ngowi, alisema hiyo itakuwa ni mara ya kwanaa kwa Majia kuwania mkanda huo wa Jumuiya ya Madola ambao huziunganisha nchi zote zilizotawaliwa na Uingereza.
"Bondia Mtanzania Fadhil Majia amepeta fursa ya kuteuliwa kucheza mechi ya mchujo dhidi ya Mghana, Isaac Quaye Februari 22, 2013 ili kuwania nafasi ya kupigana na bingwa wanayeshikilia taji la CBC, Kevin Satchell wa Uingereza," alisema Ngowi.
Katika hatua nyingine, Ngomi alisema CBC, imepitisha azimio la kuruhusu ubingwa wa baraza hilo katika Bara la Afrika.
Ubingwa huo utakuwa unajukikana kama 'CBC Africa Zone' na tayari wapo mabondia kadhaa wa nchi za Afrika ya Magharibi ambao wameshandaa mapambano mwakani.
"Napenda kuwahamasisha mapromota wa Tanzania kuchangamkia fursa hizi adimu na kuandaa mapambano ya ubingwa wa 'CBC Africa Zone' kwa manufaa ya mabondia wetu," alisema Ngowi ambaye pia ni Rais wa IBF Afrika/USBA.
***

Julio afichua siri Msimbazi


KOCHA msaidizi wa timu ya vijana chini ya miaka 17 Serengeti Boys, Jamhuri Kihwelo 'Julio', aliyerejeshwa Msimbazi kama kocha msaidizi, amefichua siri ya wachezaji wa Simba akidai wengi wao wana matatizo ya kutokuwa na pumzi na stamina ya kutosha.
Julio, alisema kutokana na kupewa jukumu la kuwanoa vijana hao kama kocha wa viungo wa Simba atarekebisha tatizo, ili timu yao iweze kufanya vema katika duru lijalo la ligi kuu pamoja na uwakilishi wa nchi kwenye michuano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Beki huyo wa zamani wa Simba na Taifa Stars, alisema pamoja na mambo mengine yaliyoiponza Simba kwenye duru lililopita, amegundua tatizo kubwa kwa kikosi hicho ni kukosekana kwa stamina na pumzi za kutosha kwa nyota wa timu hiyo.
Alisema kutokana na kubaini tatizo hilo, amejipanga kuwanoa wachezaji hao ili wawe 'ngangari'.
Julio alisema anadhani tatizo hilo ndilo lililoigharimu Simba kwenye duru la kwanza kwa wachezaji wake kushindwa kumudu dakika zote 90 za mchezao badala yake kuonekana tishio dakika 45 za kwanza na kuwa 'urojo' dakika 45 za pili na kupata matokeo mabaya.
"Nimegundua wachezaji wengi wa Simba wana tatizo la pumzi na stamina, hivyo nitajitahidi kurekebisha tatizo kabla ya kuanza kwa duru la pili la ligi ili vijana wawe ng'ang'ari," alisema.
Julio amerejeshwa Msimbazi sambamba na aliyekuwa kocha mkuu wa zamani wa timu hiyo, Moses Basena ili kumsaidia kocha mpya wa klabu hiyo, Patrick Liewig  anayechukua nafasi ya Mserbia , Circokiv Milovan aliyetupiwa virango Simba.
Kwa sasa Julio na vijana wake wanaendelea kujifua kwa mazoezi ya ufukweni wakati wakisubiri kuanza kufanya mazoezi ya uwanjani mara atakapowasilia kwa Mfaransa Liewig, aliyepewa mkataba wa muda mrefu ili 'kupimwa' kiwango chake.

Kocha wa Simba sasa kutua leo Yanga wafika salama Uturuki


UONGOZI wa Simba umedai kuwa kocha mpya wa timu yao, Mfaransa Patrick Lieweg atawasili kwenye Uwanja wa Kiamataifa wa Ndege wa Julius Nyerere (JNIA) leo saa 7:15 mchana akitokea mjini Baho, Ufaransa.
Ujio wa kocha huyo umekuwa wa danadana tangu ilipotangazwa awali angetua Desemba 27, lakini safari hii uongozi umethibitisha kuwa atatua leo mchana bila kupepesa macho.
Akizungumza na MICHARAZO jana, Mwenyekiti wa Simba, Aden Rage alisema kuwa kocha huyo atatua kurithi mikoba ya aliyekuwa kocha wao, Mserbia Milovan Cirkovic, ambaye wamelazimika kumfungashia virago baada ya kumalizika kwa mzunguko wa kwanza wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara.
“Kulikuwa na tatizo la usafiri wa ndege katika nchinnyingi za Ulaya kipindi hiki cha bararidi kali barani humo ndiyo maana alikuwa anakosa ndege za kumleta Tanzania,” alisema Rage.
Simba, ambao ni mabingwa watetezi wa Ligi hiyo, walilazimika kuvunja mkataba na Cirkovic kutokana na kilichodaiwa na uongozi wa klabu hiyo kuwa kocha huyo alikuwa ‘anaikamua’ kiasi kikubwa mno cha fedha.
Hata hivyo, baada ya kuvunja mkataba na kocha huyo aliyewapa ubingwa msimu uliopita, ‘Wekundu wa Msimbazi’ tayari wameingia mkataba na makocha wawili wapya, Jamhuri Kihwelo ‘Julio’ na Mganda Mosses Basena.
Kwa mujibu wa Afisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga, baada ya kutua kwa Lieweg, uongozi wa klabu hiyo utatangaza mfumo mpya wa benchi la ufundi la timu yao.
Katika hatua nyingine msafara wa mabingwa wa Kombe la Kagame, Yanga umefika salama nchini Uturuki na unatarajiwa kuanza programu zao nchini humo.
Kwa mujibu wa taarifa za mtandao wa klabu hiyo, kikosi hicho kilifika salama jana asubuhi na leo kilitarajiwa kuanza kujifua kabla ya kuanza kucheza mechi kadhaa za kirafiki na wenyeji wao zikiwa maalum kwa ajili ya duru la pili la Ligi Kuu Tanzania Bara na utetezi wao wa Kombe la Kagame litakalofanyika nchini Rwanda.

Golden Bush, Wahenga kuuaga mwaka Tp Afrika


TIMU ya soka ya Golden Bush jioni ya leo inatarajiwa kushuka dimbani kumenyana na Wahenga Fc katika pambano maalum la kuuaga mwaka 2012 na kuukaribisha mwaka mpya wa 2013.
Pambano la timu hizo mbili zinazoundwa na wachezaji nyota wa zamani nchini, litafanyika kwenye uwanja wa TP Afrika, Sinza Dar es Salaam kuanzia majira ya jioni.
Timu hizo zitakutana katika pambano hilo huku zikiwa na kumbukumbu ya kukutana hivi karibuni kwenye dimba la uwanja huo.
Wahenga wanakumbuka kipigo cha mabao 4-2 ilichopewa na wapinzani wao siku chache baada ya kutoka sare ya bao 1-1 katika michezo iliyochezwa hivi karibuni.
Golden Bush inayomilikiwa na mmoja wa wanachama wa zamani wa Friends of Simba, Onesmo Wazir 'Ticotico', itashuka dimbani leo ikiwa na kumbukumbu ya ushindi wa mabao 3-2 iliyopata siku ya Jumamosi dhidi ya vijana nwa Chuo Kikuu.
Ticotico aliyeshindwa kuonyesha makeke yake katika pambano la Jumamosi kutokana na kuumia dakika 9 tu baada ya pambano hilo kuanza, alisema anaamini leo akijaliwa atashuka dimbani kuwaongoza wenzake kuendeleza 'dozi' yao ya mabao manne iliyokuwa inaitoa kabla ya kutibuliwa na vijana hao wa Chuo Kikuu.
"Nilikamia mechi ya Jumamosi, lakini nikashindwa kwa kuumia mapema, ila Jumatatu (leo) naweza kushuka dimbani kuwavaa wahenga," alisema Ticotico.
Katika mechi yao ya Jumamosi, Golden Bush ilipata mabao yake kupitia nyota wa zamani wa Yanga, Moro United na Prisons Mbeya, Herry Morris na Omar Msangi na inatarajiwa kushuka dimbani leo ikiwa na nyota wake kama Steven Marashi, Yahya Issa, Salum Swedi 'Kussi', Said Swedi 'Panucci', Herry Morris, Athuman Machuppa, Machotta, Majaliwa, Omar Msangi, Ticotico, Katina Shija na wakali wengine.
Wahenga wenyewe inatarajiwa kuwa chini ya nyota wa zamani wa Majimaji, Simba na Taifa Stars, Madaraka Seleman 'Mzee wa Kiminyio'.


Lampard aipaisha Chelsea


Frank Lampard akishangilia moja ya mabao yake aliyofunga jana


LONDON, England
FRANK Lampard alionyesha thamani yake kwa  Chelsea baada ya kufunga magoli mawili ‘makali’ yaliyoipa ushindi wa ugenini wa mabao 2-1 dhidi ya Everton jana na kukwea hadi katika nafasi yake ya tatu kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya England.
Huku kukiwa na uvumi mwingi kuhusiana na hatma yake ndani ya Chelsea, alionyesha kiwango cha juu na kufunga mabao yote huku goli la Everton likifungwa na Steven Pienaar.
Ushindi wan ne mfululizo wa Chelsea chini ya kocha Rafael Benitez umeiinua hadi kubakiza pointi nne tu kabla ya kuifikia Manchester City inayoshika nafasi ya pili, huku Chelsea ikiwa na mechi moja mkononi.
-----

Mhasibu Simba aporwa mamilioni ya fedha Sinza

Mwenyekiti wa klabu ya Simba, Ismail Aden Rage


ZAIDI ya Sh. milioni 10 za klabu ya Simba zimeporwa baada ya Mhasibu wa klabu hiyo, Erick Sekiete (28) kudai kuvamiwa na majambazi sita katika mtaa wa Sinza kwa Remmy na kuporwa kiasi hicho cha pesa juzi saa 3:20 usiku.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kipolisi Kinondoni, Charles Kenyela alisema kuwa Sh. milioni 7.59 na dola za Marekani 2,000 ambazo Simba walizipata baada ya makato ya mapato ya mechi yao dhidi ya Tusker FC ya Kenya iliyomalizika kwa wenyeji Simba kuchapwa 3-0 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
“Simba ilipata mgawo wa Sh. milioni 10.6 na dola za Marekani 2,000 (Sh. milioni tatu) kutokana na mapato ya kiingilio cha mechi yao dhidi ya Tusker. Baada ya makato, walibakiwa na Sh. milioni 7.59 ambazo Sekiete alikabidhiwa,” alisema Kamanda Kenyela.
Alisema kuwa baada ya kukabidhiwa fedha hizo, Sekiete na mwenzake Stanley Phillipo (23) ambaye alidaiwa kuwa ni mwanafunzi, walipanda kwenye gari aina ya Toyota Premio yenye namba za usajili T869 BKS lililokuwa likiendeshwa na Said Pamba na kwamba walipofika eneo hilo, dereva aliwashusha na kwamba wakaanza kutafuta teksi.
Aliendelea kueleza kuwa muda mfupi baada ya kushushwa, Sekiete na Philipo waliamua kuvuka upande wa pili wa barabara ya iendayo Kijitonyama ili wachukue teksi lakini ghafla  walilitekwa na watu sita walioshuka kutoka kwenye pikipiki tatu.
“Mmoja wa watu walioshuka kwenye pikipiki alikuwa na bastola... alifyatua risasi hewani wakati wenzake wakipora begi lenye fedha kutoka kwa mhasibu,” alisema Kenyela.
Aliendelea kufafanua kuwa wakati watu hao wakimnyang’anya begi Sekiete walikuwa wakitamka maneno ya kejeli kwa uongozi wa Simba.
Aliyanukuu maneno hayo kwa kusema; “Mnafungwa halafu mnazingua, na kwa kuwa viongozi wenu wanakula pesa za klabu, nasi hizi tunaziiba.”
Kamanda Kenyela alisema kuwa baada ya watu hao kupora fedha hizo, walitokomea kusikojulikana na hadi sasa, Jeshi la Polisi linawashikilia watu watatu akiwamo Sekiete kuhusiana na tukio hilo.
Watu wengine wanaoshikiliwa na jeshi hilo katika Kituo cha Polisi Magomeni ni Pamba na Philipo ambao walikuwa pamoja na Sekiete kwenye gari.
“Sisi (Jeshi la Polisi) tulishaonya watu kusafirisha kiasi kikubwa cha fedha bila ulinzi, tunawashikilia watu hawa watatu kwa sababu huenda walipanga kuiba fedha hizo,” aliongeza.
“Mazingira ya kuporwa kwa fedha hizo yanatia shaka huenda kuna kitu kilikuwa kimepangwa ili fedha hizo ziibwe. Iweje mtu akahifadhi nyumbani kwake kiasi kikubwa cha fedha kama hicho?” alihoji Kamanda Kenyela.
“Kwa sasa mtu yeyote atakayeripoti kuporwa fedha kiasi kikubwa kama hiki na alikuwa akisafirisha pasipo na ulinzi, tutaanza naye.
“Tunawashikilia wawa watatu kwa uchunguzi zaidi kuhusiana na tukio hilo. Tunaomba ushirikiano kutoka watu wenye taarifa juu ya waliohusika na tukio hili.”
Mwenyekiti wa Simba, Aden Rage alinukuliwa jana akidai amesikitishwa na taarifa za kuporwa kwa fedha za klabu yao.
“Mhasibu wetu anaishi Sinza. Alizichukua zile fedha za klabu akazihifadhi nyumbani kwake ili leo (jana) azipeleke benki,” alisema Rage.


Masawe Mtata ana Love position

MCHEKESHAJI mahiri wa kipindi cha 'Ze Comedy Show', Rogers Richard a.k.a. Masawe Mtata, amefyatua filamu mpya iitwayo 'Love Position', akijiandaa pia kupakua nyimbo mpya kwa ajili ya albamu yake ijayo.
Msanii huyo anayefahamika pia kwa jina la Dokta Kicheko, alisema tayari filamu hiyo ya kimapenzi ipo mtaani baada ya kuitoa wiki iliyopita akiwa ameigiza na wasanii kadhaa wenye majina na chipukizi.
Masawe Mtata, alisema filamu hiyo ya 'komedi' imekuja wakati akiwa katika harakati zake za kupakua albamu mpya ya muziki wa kizazi kipya baada ya kutamba na nyimbo kadhaa ukiwemo wa 'Siwezi Kulala'.
"Nimekamilisha na kuiachia filamu yangu mpya iitwayo 'Love Position', huku nikiwa mbioni kukamilisha albamu yangu ya tatu itakayokuwa na nyimbo nane," alisema.
Msanii huyo alisema albamu hiyo inakuja baada ya awali kutamba na albamu za 'Say Ye' au 'Unanipenda Mimi' na 'Mirinda Nyeusi' iliyofahamika pia kama 'Kicheko.com'.
Mchekeshaji huyo, alisema wakati filamu yake hiyo mpya ikiendelea kupokelewa na mashabiki wake, pia anajipanga kuandaa kazi nyingine mpya ili iwe kama 'funguo' kwa mwaka 2013 alioutabiri utakuwa na ushindani mkubwa kisanii nchini.