STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Saturday, December 1, 2012

Shamsa Ford, Mayasa warejea 'After Death'

Shamsa Ford


Mayasa Mrisho 'Maya' katika pozi kabambe

BAADA ya kitambo kirefu cha mapumziko ya uzazi, msanii Shamsa Ford amerejea upya kwa kasi katika fani ya uigizaji akitarajiwa kuonekana kwenye filamu ya 'After Death' akishirikiana na wazoefu Mayasa Mrisho, Ruth Suka 'Mainda' na Jacklyne Wolper.
Shamsa aliyekuwa mmoja wa waigizaji waliofanya kazi kwa karibu na marehemu Steven Kanumba ameshiriki filamu hiyo iliyotayarishwa na Jacklyne Wolper kama njia ya kumuenzi Kanumba aliyefariki Aprili 6 mwaka huu.
Muongozaji wa filamu hiyo inayotarajiwa kuzinduliwa mapema mwakani. Leah Richard 'Lamata' alisema filamu hiyo mpya imemrejesha upya Shamsa na kukumbushia 'umoja' wa wasanii hao waliokuwa wakishiriki kazi na marehemu Kanumba.
"Ndani ya filamu yetu ya 'After Death' ambaye ni maalum kwa ajili ya kumuenzi Kanumba imemrejesha upya Shamsa Ford, aliyeigiza na akina Mayasa Mrisho 'Maya', Mainda, Irene Paul, Wolper, Patcho Mwamba na Uncle D aliyeigiza kama Kanumba."
Lamata, mmoja wa waongozaji wachache wa filamu wa kike nchini, mbali na wakongwe hao pia filamu hiyo imewashirikisha 'watoto wa Kanumba' Jenifer na Patrick na wanajipanga kwa ajili ya uzinduzi wake mapema mwakani.
"Tunapanga kuzindua mwakani katika ukumbi utakaotangazwa ambao siku hiyo itatumika pia kumkumbuka marehemu Steve Kanumba," alisema Lamata.
Lamata alisema mipango kwa ujumla juu ya uzinduzi huo utawekwa bayana kadri siku zitakavyokuwa zikisogea, ila alisisitiza utafanyikia jijini Dar es Salaam.

BASATA yawalilia akina Sharo Milionea

Sharo Milionea enzi za uhai wake





BARAZA la Sanaa la Taifa, BASATA, limetuma salamu za rambirambi na kueleza kusikitishwa na vifo vya wasanii wa watatu wa filamu na muziki nchini vilivyotokea mfululizo wiki iliyopita.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotiwa saini na Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego baraza hilo limesema limepokea kwa masikitiko makubwa misiba ya wasanii hao ambao ni Khaleed Mohammed 'Mlopelo', John Maganga na Hussein Mkiety 'Sharo Milionea'.
BASATA limedai kuwa vifo vya wasanii hao ni pigo kubwa kwa familia, ndugu, jamaa na wadau wote wa tasnia nzima ya sanaa nchini kwa kusema inaungana na wote walioguswa na msiba huo.
“Baraza limestushwa na kuhuzunishwa sana kutokana na taarifa ya vifo hivi vya wasanii hawa John Mganga, Mlopelo na Hussein Mkeity a.k.a Sharo Milionea ambao mchango wao unahitajika sana katika tasnia ya sanaa, pengo waliloliacha ni kubwa kwani ubunifu wao bado unahitajika katika tasnia hii.” Sehemu ya taarifa hiyo inasomeka hivyo.
Taarifa hiyo ikaongeza kuwa; " Baraza linatoa pole kwa familia za marehemu na wasanii wote nchini, aidha linawatakia moyo wa subira katika wakati huu wa majonzi ya kuondokewa na wapendwa wetu. Tunaomba mwenyezi Mungu azipumzishe mahala pema peponi roho za marehemu.
BASATA likaongeza kuwa wapo pamoja na familia za marehemu katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo, tutambue kuwa haya ni mapenzi ya Mungu.
Salamu hizo zimekuja wakati watanzania wakiendelea kuomboleza vifo vya wasanii hao pamoja na kile cha muimbaji wa taarab wa kundi la TOT -Plus, Mariam Khamis 'Paka Mapepe' kilichotokea wiki tatu zilizopita wakati akijifungua mwanae wa pili.
Katibu Mtendaji wa BASATA, Ghonche Materego


Man Bizo: 'Mvunja mbavu' anayetaka jamii iwathamini walemavu

Man Bizo akiwa kwenye kiti chake cha magurudu

Man Bizo akiwa na 'swahiba' zake, Mama Shotii na Kazi




KWA mashabiki wa filamu hasa za vichekesho ama wafuatiliaji wa kipindi cha 'vituko show', jina la Man Bizo huenda sio geni masikioni mwao kwa jinsi wanavyosuuzwa roho na umahiri wa msanii huyo mwenye ulemavu.
Man Bizo ambaye majina yake kamili ni Ally Boffu, amejizolea umaarufu mkubwa kwa namna ya uigizaji wake na umbile lake analolitumia vema katika kazi mbalimbali alizoshiriki pamoja na wasanii wenzake.
Msanii huyo amekuwa akikitendea haki kipaji chake cha sanaa sambamba na kile alichodai kutaka kuwaonyesha mfano walemavu wengine kwamba hali walizonazo sio mwisho wa kila kitu katika maisha yao.
Anasema walemavu wakiamua, kuthubutu na kujituma kama anavyofanya yeye ni wazi wanaweza kufika mbali kimaisha na kuepuka utegemezi.
Man Bizo anasema kama asingezingatia mambo hayo huenda kipaji chake kingepotea hivi hivi.
"Kujiamini, kuthubutu na kutaka kuonyesha mfano kwa wengine, ndiko kulikonifikisha hapa," anasema.
Anasema licha ya kukutana na changamoto nyingi, hajakata tamaa kwa vile  anatamani kufika mbele zaidi katika fani hiyo na kubwa kuja kuanzisha asasi ya kuwasaidia walemavu wenzake.
Man Bizo anayefahamika pia kama Kapeto, Jini Mahaba na Kipwinto, anasema tangu utotoni na hata alipokuwa shuleni alipenda kuchekesha watu, lakini hakuota kuja kuwa muigizaji nyota.
"Sikuota kuja kuwa muigizaji mkali kwa mazingira niliyokulia, ila kuvutiwa na msanii aitwae Zimwi na kujiamini kulinifanya nijitose rasmi mwaka 2007 na ninashukuru yapo mafanikio ya kujivunia" anasema.
Anasema licha ya umaarufu, sanaa pia imemwezesha apate ajira katika kampuni ya Al Riyamy na kumiliki maktaba ya kuuzia na kukodia kanda za filamu (video library) inayomuingizia pato la ziada.
"Nashukuru Mungu tangu nijitose kwenye sanaa, nimepata umaarufu, kupata ajira na kumiliki 'video library' na nina kila kitu katika nyumba yangu," anasema.

MUZIKI
Man Bizo anayependa kula ugali kwa mboga za majani na kunywa kinywa juisi,  ni mshabiki wa klabu ya Simba akiwazimia manahodha, Juma Kaseja na Haruna Moshi 'Boban'.
"Huniambii kitu kwa Simba, naipenda mno klabu hii na navutiwa na Kaseja na Boban, ila kimataifa mie ni mnazi wa Manchester United," anasema.
Msanii huyo anasema mbali na uigizaji, pia ni mahiri katika muziki akiwa mbioni kwa sasa kupakua albamu akitanguliza kwanza nyimbo tatu mpya.
Anasema nyimbo hizo tatu ameziimba akishirikiana na wasanii wakali kama Karapina, Dully Sykes na Prince Amigo na kudai kuwa kujitosa kwake kwenye fani hiyosio kwa kubahatisha bali ni kipaji alichonacho.
"Nilipokuwa nasoma Shule ya Jeshi la Wokovu, nilikuwa naimba hivyo kuibukia kwangu kwenye muziki sio kwa kubahatisha ila najua ninachokifanya," anasema.
Muigizaji huyo mwenye matumaini ya kuja kutamba zaidi ndani na nje ya nchi katika fani zote za muziki na uigizaji, anasema hakuna tukio la furaha kwake kama siku alipokabidhiwa nyumba ya urithi wa baba yake.

MTOTO
Man Bizo anasema hakuna tukio la huzuni linalomuuma mpaka leo kama lile la kukataliwa na kunyang'anywa mtoto  kwa kile alichodai hali yake ya ulemavu.
Anasimuliwa kuwa, alikuwa na mahusiano na msichana mmoja aliyekataa kumtaja jina la kumpa ujauzito aliokuja kujifungua mwaka 2009 mtoto wa kike ambaye alimtaja kwa jina la Lilian, ambaye ana umri wa miaka mitatu kwa sasa.
Anasema hata hivyo familia ya msichana huyo ilionyeshwa kuchukizwa na kitendo cha msichana huyo kuzaa naye na hivyo kumkana na kumnyima mtoto huyo anayedai anampenda kupita maelezo.
Hata hivyo Man Bizo anasema kwa sasa familia hiyo imemkubali kwa shingo upande na mama watoto wake wamekuwa wakimpeleka mwanae kwake kumuona, kitu kinachomfariji ingawa bado hajasahau tukio alilofanyiwa siku za nyuma.
"Lilian ni mwanangu na ninampenda mno, kwa sasa mie najipanga kufunga ndoa ili niweze kumtunza vema," anasema.
Akaongeza kuwa, suala la unyanyapaa dhidi ya walemavu ndani ya jamii ni kitu  kinachokatisha tamaa na kuonyesha namna gani baadhi ya watu wanashindwa  kuitambua uwepo wa Mungu na fani yake ya uumbaji.
"Nadhani jamii inapaswa kubadilika na kuwaona walemavu kama watu wengine licha ya kasoro za maumbile," anasema.

MAN BIZO
Ally Boffu 'Man Bizo' alizaliwa Julai 7, 1984 jijini Dar es Salaam akiwa mtoto wa mwisho kati ya watoto wa nne wa familia yao na Elimu ya Msingi aliisoma katika Shule ya Jeshi la Wokovu alipohitimu darasa la saba.
Alijitosa kwenye sanaa mwaka 2007 katika kundi la MCAP, na filamu yake ya kwanza ikiwa ni 'Olopong', kabla ya kushiriki 'Kiroba' na 'Vyumba Vimejaa' anayodai ndiyo iliyomtangaza zaidi na kumpa nafasi ya kucheza filamu nyingine zinazokaribia 50.
Baadhi ya kazi aliocheza msanii huyo anayeiomba serikali kuisaidia fani ya sanaa nchini kutoa tija kwa wasanii na kuondoka na unyonyaji wanaofanyiwa na baadhi ya watu wachache ni pamoja na 'Kitimtim', 'Hekaheka', 'Mishemishe', 'Kichefuchefu', 'Jazba' na 'Koziman'.
Man Bizo, anayewashukuru bosi wake, Khalfan Abdallah, Madhila Piana na wasanii wenzake wote anasema kubahatika kuigiza na wasanii wakubwa na wenye majina kama King Majuto, Kitale, Mzee Jangala, Sharo Milionea na wengine kwake ni fahari kubwa.
Juu ya ugonjwa wa Ukimwi, Man Bizo anasema kila mtu ndani ya jamii anapaswa kupambana nao kwa sababu umekuwa na madhara na kukatisha ndoto za watu wengi.
Msanii huyo anasema kitu cha muhimu watu ni kuwa waaminifu katika ndoa zao, kumcha Mungu na kuepuka anasa zinazoweza kuywapelekea kuangukia katika mapenzi yasiyo salama.
Man Bizo (aliyekaa kulia) akiwa na wasanii wenzake wa 'Vituko Show'



Man Bizo (kulia) akiwa na 'swahiba' yake Seleman Kazi

Sare tu kuivusha Kilimanjaro Stars ribi fainali

Kikosi cha Kilimanjaro Stars


Na Somoe Ng'itu, Kampala

Kilimanjaro Stars leo inahitaji angalau sare dhidi ya Somalia katika mchezo wa mwisho wa Kundi B la Kombe la Chalenji mjini hapa ili kukata tiketi ya kucheza robo-fainali.
Endapo itapata sare, Stars yenye pointi tatu sawa na Sudan katika kundi hilo inaweza kufuzu kama moja ya 'best liza' wawili katika mchezo utakaoanzia saa 8:00 kwenye Uwanja wa Lugogo jijini hapa, baada ya ushindi wa Kenya dhidi ya Somalia jana kumaanisha mshindi wa tatu wa Kundi A ana pointi tatu tu.
Kocha Mkuu wa Kilimanjaro Stars, Kim Poulsen, alisema jana kuwa ameiona Somalia katika mechi zake mbili zilizopita hivyo hatawadharau kwa sababu ni timu inayoimarika kadri inavyocheza mechi.
Poulsen alisema amejipanga kupata ushindi, hata hivyo, ili kujiweka kwenye nafasi nzuri katika kundi hilo baada ya kupoteza mechi yake ya pili dhidi ya Burundi iliyofanyika Jumatano kwenye uwanja wa Namboole ambao ulijaa maji na matope kufuatia mvua zinazonyesha mfululizo jijini  hapa.
"Wapinzani wetu wanaimarika kila siku zinavyokwenda, tutaingia uwanjani ili kusaka ushindi na si kuwadharau," alisema kwa sababu "timu zote zimekuja kupambana na ndio maana hakuna anayekata tamaa hata  kama amefungwa mechi zote."
Poulsen alisema hali ya beki wake, Shomary Kapombe na kiungo, Mwinyi Kazimoto zinaendelea vyema na watakuwepo kwenye kikosi kitakachoshuka dimbani kuivaa Somalia.
Naye Kocha Mkuu wa Somalia, Sam Ssimbwa, aliliambia gazeti hili juzi kwamba wamekuja Kampala kupambana ingawa wachezaji wake hawana uzoefu wa mechi za kimataifa ukilinganisha na wapinzani wao.
Ssimbwa ambaye alikuwa akiifundisha Sofapaka ya Kenya alisema hana majeruhi kwenye timu yake na amejiandaa kucheza kwenye hali yoyote kwa sababu mazingira ya viwanja vya Afrika yanajulikana.
Mbali na mechi hiyo, leo pia saa nane mchana Burundi na Sudan zilizoko kundi B zitashuka kwenye uwanja wa Wankulukuku na baadaye Malawi itakutana na Zanzibar wakati Rwanda itaikaribisha Eritrea kuanzia saa 10:00 jioni kwenye uwanja huo.
Mabingwa watetezi na wenyeji Uganda Cranes, Zanzibar na Burundi tayari wameshakata tiketi ya kucheza robo fainali ya mashindano hayo ya kila mwaka.

Nguo alizovuliwa Sharo Milionea zakamatwa



Na Steven William, Muheza
Polisi ya Tanga imekamata mali kadhaa za marehemu msanii wa filamu na muziki wa bongofleva Sharo Milionea, ikiwemo suruali ya jeans na fulana alizokuwa amevaa, vilivyoibwa baada ya kupata ajali ya gari na kufariki papo hapo katikati ya wiki wilayani hapa.
Msako wa nyumba hadi nyumba uliofanywa na polisi kwa ushirikano na wananchi ulifanikisha kupatikana kwa tairi la akiba la gari alilokuwa akiendesha, radio ya gari na betri ya gari.
Vitu vingine vilivyopatikana ni simu yake ya mkononi, saa ya mkononi, suruali aina ya jeans na fulana ambavyo marehemu alivuliwa na kuachwa na chupi tu.
Akizungumza na Nipashe juzi usiku, mkuu wa wilaya ya Muheza Subira Mgalu alisema watu kadhaa waliokutwa na mali hizo za marehemu kwenye kijiji cha Maguzoni wanashikiliwa na polisi.
Sharo Milionea alifariki baada ya gari alililokuwa akiendesha aina ya 'Toyota Harrier' kupasuka tairi la mbele akiwa katika mwendo kasi na kupinduka mara kadhaa wakati akitoka Dar es Salaam.
Mgalu alisema msako huo wa nguvu uliohusisha jeshi la polisi na raia wema wa kijiji cha Maguzoni ulifanyika usiku kwa kupita nyumba hadi nyumba.
Mgalu alisema msako huo bado unaendelea, na jeshi la polisi linaongozwa na Kamanda wa Wilaya ya Muheza Endrew Satta.
Juzi mkuu huyo wa wilaya alitoa siku mbili vitu hivyo viwe vimerudishwa vinginevyo msako mkali wa nyumba hadi nyumba ungefanyika kijijini hapo.
Milionea alipata umaarufu mkubwa kwa kuigiza kama mchekeshaji msafi tofauti na wengi ambao huamini mchekeshaji ni lazima avae vinyago, kikatuni ama ajipake masizi.
Misemo yake ya "kamata mwizi meen", "umebugi meen!" na "ohh mamma!" ilimpa mashabiki wengi; hasa watoto.

Chanzo:NIPASHE JUMAMOSI

GUNDU LAKUMBA UZINDUZI WA MASHUJAA, KISA UMEME

Kiiipe Yayooo...! Mwanamuziki JB Mpiana na bendi yake wakifanya vitu vyao baada ya kupanda stejini kwenye viwanja vya Leaders Club, Kionondoni jijini Dar es Salaam  usiku wa kuamkia leo. Hapa ilikuwa ni mida ya saa 9:00 baada ya gwiji huyu kusubiri sana kutokana na mizinguo ya umeme wa TANESCO na pia wa jenereta kubwa lililotegemewa mahala hapo kuzalishia nishati hiyo usiku wa kuamkia leo (Desemba 1, 2012).
Litapona kweli...? Watu wakiwa wamelizunguka jenereta lililokuwa linawazingua wakati wa uzinduzi uliofeli wa albamu ya pili ya mashujaa kwenye viwanja vya Leaders Club, Kinondoni jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia leo Jumamosi (Desemba 1, 2012). (Picha: Zote kwa Hisani ya issamichuzi.com)
Gundu la aina yake limeikumba bendi ya Mashujaa inayoundwa na wanamuziki kadhaanyota akiwamo Chaz Baba baada ya uzinduzi wake kukwama usiku wa kuamkia leo kutokana na kukatika hovyo kwa umeme wa TANESCO na pia 'mizinguo' ya kuwaka na kuzima kila mara kwa jenereta kubwa liliotarajiwa kutoa huduma ya nishati hiyo kwenye viwanja vya Leaders, Kinondoni jijini Dar es Salaam.

Inadaiwa kuwa mizinguo hiyo ya umeme ilimchanganya kuliko kawaida mmiliki wa bendi ya Mashujaa, Mamaa Sakina, ambaye inasemekana alianguka na kupoteza fahamu kiasi cha kukimbiziwa hospitali akiwa hoi.

Tatizo hilo lilidumu kwa masaa kibao na kuwafanya mafundi kuihangaikia jenereta huku na huko huku mwanamuziki wa kimataifa kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo aliyealikwa kusindikiza uzinduzi wa albamu hiyo, JB Mpiana akilazimika kusubiri sana --  hadi mishale ya saa 9:00 usiku -- ndipo alipopata nafasi ya kupanda jukwaani na kundi lake kufanya kazi iliyowapa fursa ya kutua nchini kwa mbwembwe.

Hata hivyo, baadhi ya mashabiki walishakereka mida hiyo na kutimkia zao, hivyo kukosa uhondo uliotarajiwa katika onyesho hilo ambalo awali lilikuwa na ratiba 'tamu' sana kwa wapenzi wa burudani.

Hakukuwa na taarifa za kina kuhusiana na hali ya kiafya ya Mamaa Sakina hadi kufikia leo asubuhi ya leo (Jumamosi Desemba 1, 2012); kwa mujibu wa chanzo chetu.