STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, April 2, 2013

Wacomoro kuwahukumu Azam, Barrack YCII

 
Na Boniface Wambura
Shrikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF) limeteua waamuzi watakaochezesha mechi ya marudiano ya Kombe la Shirikisho kati ya Azam na Barrack Young Controllers II ya Liberia itakayochezwa Jumamosi, Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Mwamuzi wa kati ni Adelaide Ali, mwamuzi msaidizi namba moja ni Amaldine Soulaimane wakati Ibrahim Mohame atakuwa mwamuzi msaidizi namba mbili. Mwamuzi wa mezani (fourth official) ni Ansudane Soulaimane.

Kamishna wa mechi hiyo itakayoanza saa 10.30 jioni atakuwa Abdelhamid Radwan kutoka Misri. Maofisa hao wa mechi hiyo watafikia kwenye hoteli ya Holiday Inn.

Wakati huo huo, Barrack Young Controllers II imewasili nchini leo (Aprili 2 mwaka huu) saa 3.35 asubuhi kwa ndege ya PrecisionAir ikitokea Nairobi, Kenya inapounganisha safari hiyo inayoanzia Monrovia kupitia Accra, Ghana.

Timu hiyo iliyofia hoteli ya Sapphire Court itafanya mazoezi leo jioni kwenye Uwanja wa Kumbukumbu ya Karume ikiwa ni sehemu ya maandalizi yake kwa ajili ya mechi hiyo huku wapinzani wao Azam wakiendelea kujinoa kwenye uwanja wao wa Azam Complex.

Mengi yaibuka sakata la aliyemuua mtoto wake na kumzika sebuleni

Marehemu Debora Riziki miaka 3 enzi za uhai wake
Riziki Mwangoka kulia anaetuhumiwa kumzika mtoto wake akiwa hai

Hapa maiti ya mtoto Debora ikiwa imetolewa nnje mara baada ya kufukuliwa ndani ya nyumba ya baba yake mzazi 
TUNAOMBA RADHI KWA PICHA HIZI TUNAZOZIONYESHA

Mwili wa marehemu Debora  ukionyeshwa kwa mzazi na kudhibitisha kuwa ndiye mwenyewe aliyemfukia 
Mwili wa mtoto Debora ukiandaliwa kwa kuzikwa kwa heshima zote
Mwili wa Debora tayari kwa kuzikwa
Hatimae sasa Debora anazikwa
Mara tu baada ya mazishi baba mzazi wa Debora anapelewa kituo cha polisi Tukuyu

Mama mzazi wa marehemu Debora asimulia kisa chote
 Mama mzazi wa Marehemu, Esther Mwambenja, alisema kabla ya tukio hilo kutokea kulikuwa na viashiria vingi vya mumewe kufanya ukatili
Bibi wa marehemu Debora 
Tukiwa na baadhi ya waandishi wenzangu tukiendelea kupata historia fupi ya marehemu Debora toka kwa mama yake mzazi
 Novemba 15 mwaka 2012 serikali ya kijiji chini ya Mwenyekiti, Lutengano Mwakyoma na mashahidi watano wakiwemo wazazi na ndugu zake, walinikabidhi barua ya kuridhia kuondoka na mwanangu, huku ikimuonya mume wangu kutorudia kosa hili la kumuiba mtoto hadi hapo atakafikisha miaka saba.
 Dada wa marehemu Debora, Neema Stevini(5) kulia ambaye ni mtoto wa kufikia wa baba mzazi wa marehemu, akisimulia jinsi mdogo wake alivyoibwa , alisema kuwa anakumbuka mara ya mwisho ilikuwa jioni majira ya saa 12 jioni.
“Nilitaka kwenda nao, lakini baba Debora akaniambia nirudi kuchochea moto ndani na niliporudi nikakuta wameondoka na nilipokimbilia sana siku waona” alisema kwa masikitiko Neema.
Mwandishi Mkuu wa Mbeya yetu Joseph Mwaisango akiwaanasindikizwa na dogo Asajile huku akielezwa ni jinsi gani walimfahamu mtoto mwenzao Debora kwakweli watoto hawa wamesema hawaamini kabisa kama Debora hawata mwona tena





MKASA wa baba kumuua mwanae kwa kumzika akiwa hai kutokana na mgogoro wa ndoa, umezidi kuibua mapya, baada ya mama mzazi wa marehemu ,Debora Riziki (3), kusimulia mkasa mzima .
Akizungumza kwa hisia kali, katika mahojiano maalumu  na Mbeya yetu kijijini kwake Ibula, katika kata ya Kiwira, wilayani Rungwe, Mama mzazi wa Marehemu, Esther Mwambenja, alisema kabla ya tukio hilo kutokea kulikuwa na viashiria vingi vya mumewe kufanya ukatili.
Alisema  tukio la mzazi mwenza huyo kumwiba mtoto  na kwenda kumfanyia  ukatili huo wa kinyama lilikuwa la pili, baada ya awali kumuiba akiwa na miaka miwili na miezi mine na alimrudisha kwa maandishi ya serikali ya kijiji.
Alisema katika tukio la kwanza la mtalaka wake huyo kumuiba mtoto wao huyo, lilitokea Septemba mwaka 2012, baada ya wiki chache za kumfukuza katika nyumba waliyokuwa wakiishi katika kitongoji cha Iponjola, kijiji cha Asenga, nyumba iliyotumika kuzikwa mtoto huyo.
Alitaja sababu za yeye kufukuzwa ni ugomvi uliotokana na yeye kuhoji  sababu za kuficha fedha kiasi cha sh. 120,000 zilizotokana na wao  kwa pamoja kufanya  kazi ya kibarua katika mashamba kijijini hapo na baada ya malipo kutolewa mtalaka wake huyo alionesha kiasi kidogo cha sh.80,000.
Alisema ugomvi huo ndio ulisababisha  yeye arudishwe kwa wazazi wake, lakini baada ya muda mfupi mwanaume huyo  alimfuata na kumbembeleza ili warudiane na alipogoma aling’ang’ania aondoke na mtoto .
“Nakumbuka ilikuwa Novemba mwaka jana baada ya mimi kuondoka nyumbani kwake na kurudi kuishi hapa nyumbani, siku hiyo tukiwa shambani huyo bwana alikuja hapa nyumbani na kumkuta mwanangu wa kwanza (Neema Steven ) niliyezaa na mwanaume mwingine” alisema Mwambenja.
Alisema baada ya kufika eneo hilo majira ya saa mbili asubuhi alitumia ujanja na kufanikiwa kumuiba mtoto na kisha kutokomea naye kijijini kwao Asenga, hali ambayo ilisababisha kutoa taarifa kituo cha polisi Kiwira.
“Unajua kuwa baada ya kwenda kutoa taarifa polisi walitusaidia kufika kijijini kwao ambapo serikali ya kijiji ilikubali nimchukue mwanangu kwa kuwekeana mkataba wa kisheria kwa mujibu wa sheria, kwani alikuwa chini ya miaka saba”.
Aliongeza kuwa  Novemba 15 mwaka 2012 serikali ya kijiji chini ya Mwenyekiti, Lutengano Mwakyoma na mashahidi watano wakiwemo wazazi na ndugu zake, walinikabidhi barua ya kuridhia kuondoka na mwanangu, huku ikimuonya mume wangu kutorudia kosa hili la kumuiba mtoto hadi hapo atakafikisha miaka saba.
  
Tukio la pili la kuiba mtoto.
Alisema tukio hilo lilitokea Novemba 29 mwaka jana 2012, ambapo alifika nyumbani kwao majira ya saa 12 :00 na kumkuta dada wa marehemu kumchukua mtoto akimdanga kuwa anaenda kusenya kuni eneo la jirani.
Aliongeza kuwa baada ya kuona dada wa marehemu anang’ang’ania kwenda wote alimuamuru arudi nyumbani kuchochea moto kwa kuwa kulikuwa kumeinjikwa mboga na kukubali kurudi.
“kwa mujibu wa maelezo ya mwanangu huyu wa kwanza alisema baada kurudi toka ndani, alikuta baba yake huyo ameondoka na mtoto na tuliporudi na kupokea taarifa hizo tulichanganyikiwa na kuanza kuhangaika hovyo” alisema mama wa marehemu.
Mwambenja alisema kuwa baada ya kucha siku ya pili asubuhi yake walienda kutoa taarifa kituo cha polisi cha Kiwira ili waweze kupata msaada wa kumtafuta, huku wakionesha barua ya makubaliano ya awali ya yeye kuwa na haki ya kisheria ya kusimamia malezi ya mwanao hadi afikishe miaka saba.
Alisema baada ya kutoa taarifa hizo kituoni hapo, askari aliyekuwa zamu siku hiyo alimtaka kutoa kiasi cha shilingi 50,000 ili fedha hizo wapewe askari mgambo wa kwenda  kijijini kwa mzazi mwenzake huyo, kwani tayari walikuwa na taarifa kuwa alikuwa amekimbilia huko.
 “Kutokana na hali ngumu ya maisha tulikosa kiasi hicho cha fedha  hivyo suala hilo kubaki bila msaada wa  polisi na pia hatukuweza kwenda kwa kijijini kwao”.
Aliongeza “sababu ya mimi kuwa mzito kuendelea kumfuatilia kijijini kwao kwa mara ya pili ili kujua kama yupo huko na mtoto ilitokana na hofu niliyoijenga, kwani awali tukiwa kwenye ugomvi alitamka maneno ya vitisho kuwa endapo nitaendelea kung’ang’ania kumchukua mtoto pale anapomchukua atakuja kumuua ili tukose wote”.
Hata hivyo mama huyo mzazi wa Debora, alisema kuwa baada ya kuona hali hiyo, aliendelea kuwasiliana na wifi yake , Bupe Mwangoka,ambaye ni dada mkubwa wa mume wake  anayeishi eneo la Isanga  Jijini mbeya, ambaye ndiye alisaidia kwa kiasi kikubwa kubainika kwa  unyama aliofanya.
  
Maisha kabla ya tukio.
Akielezea maisha yao kabla ya kutengana na baadae kuamua kufanya ukatili huo, alisema aliwahi kumtamkia maneno makali wakati akiwa na ujauzito wa miezi nane .
Alisema baada ya kuibuka ugomvi katika kipindi hicho, mwanaume huyo alimtaka kwenda kuiuza mimba ile kwa mwanaume mwingine yeyote atakayempenda ili asije akazaa mtoto ambaye atachanganya damu ya koo hizo mbili.
“Maneno yale katika kipindi hicho sikuyatilia maanani kwani nilifikiri zilikuwa ni hasira, lakini leo hii ndio najua maana ya ile kauli ” alisisitiza Mwambenja.
Hata hivyo alisema inashangaza kwani  kuna wakati tukiwa katika maisha ya kawaida kabla ya yeye kufanya tukio hilo, mara kadhaa alijutia na kuonya juu ya matukio machafu yaliyojitokeza na kusikika ya watu kuuawa au kuondolewa baadhi ya viungo vya miili yao.
Aidha, alieleza mkasa mwingine wa mume wake huyo ni ule wa wao kufukuzwa katika mji wa Kiwira walikokuwa wakiishi awali kwa kufanya shughuli za umachinga.
Alisema walitimuliwa na serikali ya mtaa katika mji huo kutokana na mumewe huyo kutuhumiwa kuiba simu ya mkononi ambapo alipokea kipigo kikali na baadae kufukuzwa.
Kutokana na hali hiyo, mama wa marehemu Debora alisema yote yaliyotokea amemwachia mungu na kwamba kama ingekuwa uwezo wake angeamuru naye anyongwe, hivyo mamlaka husika zitajua cha kufanya.
Kwa upande wake dada wa marehemu Debora, Neema Stevini(5) ambaye ni mtoto wa kufikia wa baba mzazi wa marehemu, akisimulia jinsi mdogo wake alivyoibwa , alisema kuwa anakumbaka mara ya mwisho ilikuwa jioni majira ya saa 12 jioni.
“Nilitaka kwenda nao, lakini baba Debora akaniambia nirudi kuchochea moto ndani na niliporudi nikakuta wameondoka na nilipokimbilia sana siku waona” alisema kwa masikitiko Neema.
Hata hivyo uchunguzi wa Mbeya yetu umebaini kuwa marehemu Debora alifariki dunia siku hiyo ya Novemba 29 mwaka jana, majira ya saa nne usiku baada ya baba yake kufanikiwa kumuiba kutoka nyumbani kwa mama yake.
Inadaiwa kuwa baada ya kufanikiwa kumtorosha baba huyo wa marehemu alitembea kwa mguu umbali wa kilomita 50 kutoka kijiji cha Ibula alikomuiba hadi nyumbani kwake kijiji cha Isange katika kata ya Isange.
Imeelezwa kuwa baada ya kufika nyumbani kwake, baba huyo mzazi wa marehemu alichimba shimo katikati ya sebule na kumchukua mtoto wake huyo akiwa usingizini na kisha kumfukia akiwa hai.
“Mwanaume Yule alikuwa katili sana, kwani baada ya kumfukia alichukua meza ya chakula na kuiweka juu yake huku akiipamba kwa magazeti jambo ambalo lilifanya ndugu zake wasigundue kirahisi” alisema mpasha habari.
Chanzo hicho kilisema baada ya kufanya hivyo aliishi kwa wiki moja na baadae kukimbilia Jijini Mbeya ili watu wasibaini juu kitendo alichofanya na kwamba kila alipohojiwa na ndugu zake alisema mwanae huyo alimuweka kwa rafiki yake Jijini Mbeya.
Hata hivyo baada ya danadana za muda mrefu ndipo dada wa mtuhumiwa huyo aliamua kutoa taarifa jeshi la polisi na kufanikiwa kumkamata akiwa katika harakati za kutorokea wilayani Chunya na alipobanwa alifichua siri ya alipo mwanae kwa kueleza kuwa alimuua na kumfukia ndani kwake.

Imehamishwa Mbeya Yetu

Aden Rage asema hang'oki Simba ng'o

Mwenyekiti wa Simba, Ismail Aden Rage
MWENYEKITI wa klabu ya Simba ya jijini Dar es Salaam, Ismail Aden Rage, amesema kuwa licha ya timu yake kufanya vibaya katika mechi za Ligi Kuu ya Tanzania Bara inayoendelea nchini, hataachia ngazi hadi muda wake wa kukaa madarakani utakapomalizika mwezi Mei mwakani.
Katibu huyo wa zamani wa chama cha soka nchini (FAT sasa TFF) alisema pia anashangazwa kusikia kwamba anang'ang'ania madarakani kwa sababu anasubiria fedha (Dola 300,000 ambazo ni sawa na Sh. milioni 473) za mauzo ya aliyekuwa mshambuliaji wa timu hiyo Mganda Emmanuel Okwi zitue ili ashiriki katika mgawo wa matumizi yake.                 
Rage na viongozi wenzake waliingia madarakani mwezi Mei mwaka 2010 na kwa mujibu wa katiba, watafikia ukomo wa miaka minne ifikapo mwezi Mei mwakani.
Akizungumza na NIPASHE jana, Rage alisema kuwa kinachomfanya yeye 'apigiwe' kelele za kujiuzulu ni jinsi alivyoshiriki kudhibiti mali za klabu hiyo na kukabidhi nguvu za kisheria kwa baraza la wadhamini kama katiba yao inavyosema.
Rage alisema kuwa anafahamu kwamba suala la timu kufanya vibaya linachukuliwa kama sababu kuu lakini kilichoko nyuma ya 'pazia' ndani ya klabu hiyo ni namna baadhi ya wanachama wachache wa Simba waliokuwa wanafaidika kupitia mali za klabu kudhibitiwa na ndiyo wanaoshawishi kuwapo kwa migogoro hiyo inayoendelea chini kwa chini hivi sasa.
"Sina makosa yoyote, nilichokifanya mimi ni kurejesha heshima ya wadhamini ambao haikuwapo Simba kwa zaidi ya miaka 20 iliyopita, Rage siwezi kusaini mkataba wowote na hali hiyo nimeijenga ili hata nikiondoka watakaokuja waheshimu katiba ya Simba," alisema Rage.
Kuhusiana na fedha za Okwi aliyesajiliwa katika klabu ya Etoile du Sahel ya Tunisia, Rage alieleza kwamba siku hizi mitandao inaonyesha na kama fedha hizo zingekuwa zimeshapokelewa na kuliwa hakuna ambaye asingejua na anasikitika kuonekana kwamba yeye ndiye ana njama ya kuzitumia kwa maslahi yake binafsi.
"Tunisia kwa sasa hakuna serikali, huwezi kuhamisha fedha nje ya nchi mpaka mambo yatakapotulia, na hao wanaopia kelele wengine si wanachama na wengine hawana msaada kwa timu na hawajawahi kuichangia, ninachowaambia tuheshimu katiba," alisema kiongozi huyo ambaye ni Mbunge wa Tabora Mjini.
Kuhusiana na madeni mbalimbali yanayoikabili Simba hivi sasa, Rage alisema hakuna taasisi kubwa kama klabu ya Simba ambayo haidaiwi duniani na kusema pia hata wao (Simba) kuna kampuni na taasisi wanazofanyakazi nazo wanazidai lakini busara na heshima ndiyo inatumika katika kusubiri malipo yafanyike.
Alisema pia leo jioni Kamati ya Utendaji ya klabu hiyo itakutana kujadili mambo mbalimbali, kubwa likiwa ni ripoti ya ufundi ya timu yao inayoshika nafasi ya nne katika msimamo wa ligi ya Bara.


CHANZO:NIPASHE.