STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, January 9, 2013

Chipolopolo aanza kusuka kundi lake

Chipolopolo katika pozi

MUIMBAJI wa zamani wa kundi la King's Modern Taarab, Mwanahawa Ally 'Mwanahawa Chipolopolo', ameanza kulisuka kundi lake la miondoko hiyo aliloliunda hivi karibuni baada ya kupata mfadhili aliyempa vyombo vya muziki.
Pia msanii huyo amekanusha kumnyakua wasanii waliodaiwa kujiengua katika kundi lake la zamani wa King's Modern, kwa kile alichodai hataki ugomvi na 'bosi' wake wa zamani wala kutaka wasanii wenye majina makubwa.
Akizungumza na MICHARAZO jana, alisema kundi lake linaloendelea kujifua kabla ya kutoa burudani, linaundwa na wasanii kadhaa wasio na majina makubwa lakini wenye vipaji vya hali ya juu katika muziki.
Msanii huyo aliwataja baadhi ya wasanii wanaounda kundi lake hilo lenye maskani yake Keko kuwa ni Haruna Hassani 'Bonge la Bwana', Kuruthumu Akida, Mwajuma Abdalla na Rehema 'Mtu Mzima Dawa ambao ni waimbaji.
Msanii huyo aliongeza hata taarifa kwamba wamewanyakua baadhi ya wasanii wenzake wa zamani wa Kings Modern waliodaiwa kulihama kundi hilo, sio za kweli kwa sababu hana mpango wa kunyakua msanii yeyote mwenye jina kubwa.
"Hakuna msanii hata mmoja mwenye jina aliyetua kwangu, wala sijamnyakua msanii aliyetoka Kings Modern au kokote kule kunakotajwa kuna wasanii wakali," alisema.






Dogo Muu ‘Siwezi Kushukuru’

Dogo Muu (kulia) akiwa na Dogo Aslay


MSANII chipukizi kutoka kituo cha Mkubwa na Wanae, Muharami Kajonjo 'Dogo Muu' anatarajiwa kuachia kazi mbili tofauti, moja ikiwa 'audio' ya wimbo wake mpya wa 'Nashukuru' na video ya kibao chake kiitwacho 'Siwezi'.
Meneja wa msanii huyo, Said Fella, aliiambia MICHARAZO kuwa wameamua kutoa 'audio' na video kwa lengo la kuwapa burudani mashabiki wa msanii huyo ambaye wanajiopanga ili kumtambulisha rasmi katika ulimwengu wa muziki.
Fella, alisema katika wimbo wa 'Nashukuru'. Dogo Muu ameimba pamoja na msanii nyota aliyetoka kuwania tuzo za Kora Africa, Dogo Aslay.
"Tupo katika maandalizi ya kutoa kazi za msanii wetu mpya, Dogo Muu, tutatoa nyimbo zake mbili katika mfumo wa 'audio' na video, lakini zikiwa tofauti," alisema Fella.
Aliongeza wakati Dogo Muu akijiandaa kujitambulisha kwa mashabiki wa muziki na kazi hizo, kundi la TMK Wanaume Family, nalo limefyatua vibao viwili vipya kimoja kiifahamika kwa jina la 'Tutaonekanaje?
Katika hatua nyingine, alisema pamoja na Dogo Aslay kushindwa katika tuzo za muziki za Kora, lakini fursa ya kuteuliwa kuwania tuzo hiyo kama Msanii Bora Chipukizi, imeonyesha ni namna gani kijana huyo alivyo na kipaji.
"Tunajivunia uteuzi wake, hata kama hatafanikiwa kushinda ikizangatiwa ndio kwanza ameingia kwenye sanaa hii baada ya kukitambua kipaji chake," alisema Fella.

Simba, Azam hapatoshi Mapinduzi Cup Z’bar leo

Simba na Azam katika mechi yao ya Ligi Kuu duru lililopita

Na Mwinyi Sadallah, Zanzibar
MABINGWA  watetezi wa Kombe la Mapinduzi, klabu ya Azam wanashuka dimbani kucheza dhidi ya mabingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara, Simba katika mechi yao ya nusu fainali ya Kombe la Mapinduzi 2012 kwenye Uwanja wa Amaan mjini Zanzibar leo.
Mechi hiyo itaanza saa 2:00 usiku, ikitanguliwa na nusu fainali nyingine itakayochezwa jioni kati ya mabingwa wa Ligi Kuu ya Kenya, Tusker na Miembeni ya mjini visiwani hapa.
Tusker wamefanikiwa kuingia fainali wakiwa na pointi 7 na kuongoza katika kundi lao la A baada ya kushinda pia katika mechi yao ya mwisho kwa bao 1-0 dhidi ya Jamhuri ya Pemba.
 Simba ambao wamekuwa wakionyesha kiwango kizuri kadri mashindano hayo yanavyosonga mbele, walitinga nusu fainali wakiwa pointi tano baada ya kutoka sare ya 1-1 katika mechi yao ya mwisho ya hatua ya makundi dhidi ya Bandari.
Azam pia waliingia hatua ya leo wakiwa na pointi tano baada ya juzi kutoka sare na Mtibwa Sugar na hivyo kuongoza katika kundi lao la B, huku Miembeni wakiingia nusu fainali wakiwa na pointi nne baada ya kutoka sare ya 0-0 na Coastal Union ya Tanga.
Kocha wa Simba, Jamhuri Kihwelu alisema kwamba lengo la timu yake ni kutwaa ubingwa baada ya wachezaji wake kuonyesha kiwango kizuri tangu kuanza kwa mashindano hayo.
“Nia tunayo na uwezo wa kutwaa Kombe la Mapinduzi mwaka huu tunao…  wachezaji wetu wameonyesha kiwango kizuri na hivyo naamini kesho (leo) tutashinda tu,” alisema Kihwelu.
Kocha wa Tusker, Robert Matano, alisema kwamba pamoja na timu yake kushiriki kwa mara ya kwanza mashindano hayo, wachezaji wake wameonyesha kiwango kizuri na kufanikiwa kuongoza katika kundi A, hivyo ni imani yake kwamba watashinda pia leo na kutinga fainali.
Hata hivyo, alisema kwamba timu zote zilizofanikiwa kuingia nusu fainali ni nzuri na mafanikio yao yatatokana na juhudi na maarifa ya wachezaji watakocheza leo.
Katibu wa Kamati ya Kombe la Mapinduzi, Abdallah Said, alisema bingwa wa mashindano ya mwaka huu atazawadiwa Sh. milioni 10, mshindi wa pili Sh. milioni tano na mfungaji bora atazawadiwa Sh. 300,000.
Aliongeza kuwa mwamuzi bora wa mashindano hayo na mwanahabari bora pia watapata zawadi ya Sh. 200,000 kila mmoja.
Fainali ya mashindano hayo zitafanyika Jumamosi ambayo ni siku ya kilele cha maadhimisho ya Mapinduzi ya Zanzibar na utachezwa pia kwenye Uwanja wa Amaan na kuhudhuriwa na mgeni rasmi,  Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi.


CHANZO:NIPASHE

SUGU AFUNGUA INTERNET CAFE YA IZZO B MJINI MBEYA


Mbunge wa Mbeya mjini Mh Joseph Mbilinyi (Sugu) ndiye aliye fanya ufunguzi wa biashara mpya ya msanii Izzo B "INTERNETE CAFE" iliyoko katika chuo cha Teku jijini Mbeya.
Huu utakua ni uwekezaji wa pili wa msanii Izzo B baada ya kufungua duka la nguo hapo mjini mbeya ambapo ndipo anapotoka.

NJEMBA APEWA KIPONDO BAADA YA KUIBA 'KITIMOTO' NA BIA



 Kijana mmojaambaye jina lake halikuweza kupatikana mara moja akilia kwa uchungu mara baada ya kupokea kichapo kutoka kwa wananchi wenye hasira kali mara baada ya kudaiwa ameiba nyama ya Nguruwe (Kitimoto) pamoja na Bia katika glosali jijini Dar es Salaam.
Mmoja ya wasamalia wema akimtetea kijana huyo ambaye alipokea kichapo.
Akijitetea.
Akisaidiwa na wasamalia wema.

Mrisho Ngassa, John Bocco wainogesha Stars

Ngassa na Bocco wakipongezana


 
WASHAMBULIAJI Mrisho Ngassa wa Simba na John Bocco ‘Adebayor’ wa Azam ni miongoni mwa nyota zaidi walioripoti katika kambi ya timu ya taifa ya Tanzania (Taifa Stars) itakayosafiri leo jioni  kwenda jijini Addis Ababa, Ethiopia kucheza mechi ya kimataifa ya kirafiki dhidi ya wenyeji keshokutwa Ijumaa.
Awali, Bocco, Ngassa, kipa Juma Kaseja na wachezaji wengine kadhaa walioitwa Stars kutoka katika klabu za Simba na Azam walishindwa kuripoti katika kambi ya timu hiyo kwavile walikuwa na klabu zao kwenye michuano inayoendelea visiwani Zanzibar ya Kombe la Mapinduzi.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Afisa Habari wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Boniface Wambura, alisema kuwa nyota kutoka Simba, Azam na Mtibwa wameungana na wenzao na kwamba sasa Stars itasafiri leo ikiwa na kikosi chenye wachezaji wengi zaidi miongoni mwa wale walioutwa na kocha wao Mdenmark, Kim Poulsen.
Mbali na Bocco, Ngassa na Kaseja, wachezaji wengine walioitwa Stars kutoka Simba, Azam na Mtibwa ni Shomari Kapombe, Amri Kiemba, Amir Maftaha, Mwinyi Kazimoto, Salum Aboubakar 'Sure Boy', Mwadini Ali, Mcha Khamis, Aggrey Morris,  Erasto Nyoni, Aishi Manula na nyota Issa Rashid ‘Baba Ubaya’ na Shabani Nditi kutoka Mtibwa Sugar,
"Stars inaondoka leo huku ikiwa kamili baada ya nyota wengi kuripoti kambini," alisema Wambura.
Alisema timu hiyo itarejea jijini Dar es Salaam baada ya kumalizika kwa mechi dhidi ya Ethiopia na kuendelea na kambi yao kujiandaa kwa mechi nyingine mbili za kirafiki, zote zikiwa ni sehemu ya maandalizi kabla ya mechi ya kuwania kufuzu kwa fainali zijazo za Kombe la Dunia dhidi ya Morocco itakayochezwa Machi.

MTANGAZAJI ALIYEPOTEA AKUTWA PORINI AMEKUFA HANA SEHEMU NYETI

Bw. Issa Ngumba.

Mwandishi wa habari wa Radio Kwizera anayefanyia kazi wilayani Kakonko mkoani Kigoma,Bw. Issa Ngumba aliyepotea katika mazingira ya kutatanisha amekutwa amekufa huku akiwa kanyofolewa  sehemu zake za  siri.
 

Taarifa  kutoka Kigoma ambazo mtandao huu  MICHARAZO umezipata jana kuwa, mwili wa mwanahabari  huyo umekutwa nje  kidogo na mkoa  wa Kigoma.
Kamanda  wa  polisi  wa mkoa wa Kigoma Frasser Kishai, amethibitisha  juu ya kutokea kwa  tukio  hilo na kwamba  bado jeshi la polisi linaendelea kufanya uchunguzi.
Mbunge wa  jimbo la Kigoma Zitto Kabwe amenukuliwa kusikitishwa na kifo cha mwandishi huyo na kulitaka jeshi hilo kufanya uchunguzi wa kina juu ya kifo chake.
Kabwe  ameeleza  jinsi  mwanahabari  huyo  alivyokuwa akiifanya kazi yake kwa jamii ya Kigoma kwa ufanisi zaidi na kuwa wakati mwingine yeye kama mbunge alikuwa akizunguka na mwanahabari huyo katika jimbo lake.
" Kweli  nimeguswa   sana na kifo  cha kusikitisha cha mwanahabari huyo nilimfahamu  vema kwa  utendaji kazi wake  ila nawapa  pole sana  waandishi  wote nchini kwa  msiba huu mkubwa .....na zaidi nitapata  kueleza mengi mara baada ya  uchunguzi"
Taarifa za awali  zilizotolewa na  Jeshi la Polisi wilayani Kakonko baada ya  kupotea kwa mwanahabari huyo zilisema kuwa Bw Ngumba alipotea  tangu January 05 mwaka huu majira ya saa 11 jioni ambapo alimuaga mke wake Bi. Rukia Yunus kuwa anakwenda Muhange senta wilayani Kakonko na kwamba hajarudi nyumbani hadi sasa.
Kufuatia tukio hilo jeshi la polisi kwa kushirikiana na wananchi wa Kijiji cha Muhange wanaendelea kumtafuta katika mapori ya kijiji hicho baada ya rafiki zake kueleza kuwa aliwaanga kuwa anakwenda kutafuta dawa msituni.
Bw. Issa Ngumba.
Aidha jeshi la polisi Wilayani Kibondo liliomba kampuni za mitandao ya simu anayotumia Bw Ngumba kusaidia kutambua simu zake zilipotumika kwa mara ya mwisho ili kurahisisha upatikanaji wake.
Akizungumza kwa njia ya simu, Mke wa Bw Issa Ngumba, Bi Rukia Yunus amesema kuwa wananchi walio wengi ambao walikuwa wakimtafuta maporini wamerudi kijiji hapo baada ya kumkosa.

CHANZO:FRANCIS Godwin

OMARI OMARI KUZIKWA LEO TEMEKE


MSANII nyota wa miondoko ya Mchiriku, Omari Omari, aliyefariki jana alfajiri anatarajiwa kuzikwa leo saa 7 mchana kwenye makaburi yaliyopo eneo la Temeke Mikoroshini, jijini Dar es Salaam.
Kwa mujibu wa rafiki ya karibu wa marehemu huyo aliyekuwa akitajwa kama mfalme wa Mnanda King Sapeto, alisema mipango ya mazishi yanaendelea vema na kwamba Omar Omar atazikwa leo mchana.
Sapeto, alisema ndugu na jamaa wa marehemu wanategemea kupata ujumbe mzito kutoka kwa viongozi wa Serikali watakaopishana kwenda kutoa mkono wa faraja kwenye nyumba ya msiba.
Kwa siku za hivi karibuni viongozi wa serikali na vyama mbali mbali vya siasa wamekuwa mstari wa mbele kwa kushiriki bega kwa bega kwenye misiba ya wasanii, hivyo watu wa karibu na Omari Omari wanategemea hali hiyo pia itatokea kwa ndugu yao kipenzi. 
"Hatutegemi ubaguzi wa misiba" anaeleza mmoja wa ndugu wa marehemu.
Omari Omari aliyetamba na wimbo “Kupata Majaaliwa”, alifariki katika hospitali kuu ya Temeke baada ya kuugua ugonjwa wa kifua kikuu.
Msiba wake umekuja siku chache baada ya watanzania kumzika nyota wa filamu, Juma Kilowoko 'Sajuki' aliyefarikia Januari 2, katika hospitali ya Muhimbili alipokuwa amelazwa kwa matatizo ya kiafya.
 
Mwisho