STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, April 8, 2014

TFF yaridhia maamuzi ya Kamati ya Maadili

http://www.ippmedia.com/media/picture/large/mweigwachequetbl.jpg
Katibu Mkuu wa TFF, Celestine Mwesigwa
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF) imekubaliana na uamuzi uliofanywa na Kamati ya Maadili katika malalamiko mawili ambayo iliyawasilisha mbele yake, hivyo haitakata rufani. Katibu Mkuu wa TFF, Celestine Mwesigwa aliwasilisha mashauri mawili mbele ya Kamati hiyo iliyoongozwa na William Erio. Malalamiko ya kwanza yalikuwa dhidi ya waamuzi wenye beji za Shirikisho la Kimataifa la Mpira wa Miguu (FIFA), Oden Mbaga na Samwel Mpenzu na wakufunzi wa waamuzi Riziki Majala na Mchungaji Army Sentimea. Wote aliwalalamikia kwa kuwafanyisha mitihani (wakufunzi), na waamuzi kufanya mitihani hiyo kinyume na utaratibu pamoja na kughushi matokeo. Kamati katika uamuzi wake iliiagiza waamuzi hao kufanya upya mtihani huo katika robo inayofuata ambapo wakifaulu waendelee kuchezesha mechi. Waamuzi wa FIFA hufanya mitihani hiyo mara nne kwa mwaka. Kwa upande wa shauri dhidi ya Ofisa Takwimu wa TFF, Sabri Mtulla ambaye alilalamikiwa kwa kuidanganya Kamati ya Sheria na Hadhi za Wachezaji kuwa hakukuwa na pingamizi dhidi ya mchezaji Emmanuel Okwi, Kamati iliagiza suala hilo liwasilishwe upya pamoja na ushahidi wa kuthibitisha malalamiko hayo.

Vitu Vizito kuendesha harambee kusaka fedha za kwenda Botswana

Baadhi ya viongozi wa TAWA akiwemo Katibu Mkuu Magnus Simon (aliyeshika dambeli) wakiwa na baadhi ya wachezaji katika ukumbi wa Mayfair Plaza
Baadhi ya viongozi wa TAWA wakiwa na wachezaji wa mchezo huo wa kunyanyua vitu vizito
Rais wa Shirikisho la Wanyanyua Vitru Vizito Mr Kyler toka Marekani ( wa pili toka kulia) akiwa na baadhi ya wachezaji wa Tanzania alipotembelea hapa nchini hivi karibuni.
Wachezaji wa timu ya taifa wa mchezo huo wakionyesha umwamba mbele ya viongozi wa TAWA
Tupo fiti kinoma...tupelekeni Botswana tukalete medali
Titus Joseph akijiandaa kunyanyua chuma mbele ya wenzake
Katibu Msaidizi wa TAWA, Hillary Kahinji (wa kwanza kushoto mbele) akifanya mazoezi na wachezaji wa timu ya mchezo huo kwenye ukumbi wa Mayfair Plaza
Mkurugenzi wa Idara ya Michezo nchini, Leonard Thadeo ( wa pili toka kushoto) akiwa na viongozi wa TAWA mara baada ya kuchaguana mwezi uliopita.
 CHAMA cha Wanyanyua Vitu Vizito Tanzania (TAWA) kimeandaa hafla maalum itakayotumika kuendesha harambee ya kusaka fedha za kuiwezesha Timu ya Taifa ya mchezo huo kwa Vijana kwenda kwenye michuano ya Afrika itakayofanyika nchini Botswana mwezi ujao.
Katibu Mkuu wa TAWA, Magnus Simon, aliiambia MICHARAZO kuwa, hafla itakayoambatana na uzinduzi wa chama hicho kilichofufuliwa upya itafanyika siku ya Mei 3 mwaka huu kwenye ukumbi wa Mikocheni Resort, ambapo wanatarajiwa wageni mbalimbali na wadau wa mchezo huo watahudhuria.
Simon alisema wamekusudia kukusanya si chini ya Sh. Milioni 20 zinazoweza kuwasaidia kupeleka kikosi cha wachezaji watano katika michuano hiyo ya Vijana ya Afrika itakayofanyika Botswana kati ya Mei 22-26.
"Baada ya kukwama kutuma timu katika michuano ya Afrika kuwania kucheza michezo ya Olmpiki kwa vijana nchini Cameroon, tunapigana angalau tuweze kutuma timu Botswana na tumeandaa hafla itakayoambatana na harambee ya kuchangisha fedha kwa ajili ya jambo hilo," alisema Simon.
Simon, alisema hafla hiyo mbali na kuendeshwa kwa harambee pia itapambwa na mazoezi na shindano ndogo la wanyanyua vitu vizito na wale ambao watafanya vyema watazawadiwa pamoja na kuongezwa kwenye kikosi cha timu ya taifa, kinachoendelea kujifua kwenye ukumbi wa Mayfair Plaza.
Katibu alisema wachezaji hao wa taifa ndiyo pia watakaokuwa sehemu ya watakaoiwakilisha Tanzania kwenye michuano ya kimataifa baadaye nchini China na Uganda.
Simon alisema mpaka sasa TAWA imefanikiwa kupata wadhamini wachache ambao ni Akbar Jaffer wa Mayfair Plaza,  Mikocheni Resort Centre (MRC), Saada Beauty Para na blogu hii (MICHARAZO MITUPU)ambao wamekuwa bega kwa bega na uongozi waop katika kukirejesha chama chao katika uhai baada ya kuwa kimya kwa miaka 9 na kuwaomba wengine wajitokeze kwa ajili ya kufanikisha hafla hiyo ya Mei 3.
"Tunayaomba makampuni, asasi na watu binafsi watusaidie tufanikishe hili, ili Tanzania tukashiriki michuano hiyo na kurejesha heshima katika anga la kimataifa baada ye soka na michezo mingine kukwama kusuuza nyoyo za mashabiki," alisema Simon.

Thomas Mashali, Karama Nyilawila kuwania ubingwa wa UBO-Mabara Dar

Thomas Mashali 'Simba Asiyefugika'
https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEjJPGulwWfuBf6qU9wozguZwayMgHptdhsmYHyZc9wFEWZozMHE2d6nf9VE5hAje14ScS1QW5Vq1efAJNar_tBcC2Xielx2Lv9MQn5_9zvT9E1BXSzwW15Kj4sp5jhXYaWnpmNdubvh974/s640/DSC_1840.JPG
Karama Nyilawila 'Captain'
BINGWA wa UBO-Afrika uzito wa kati, Thomas Mashali 'Simba Asiyefugika' anatarajiwa kuvaana na bingwa wa zamani wa Dunia wa WBF, Karama Nyilawila 'Captain' siku ya Mei Mosi kuwania ubingwa wa Mabara wa UBO.
Rais wa Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPBO-Limited), Yasin Abdallah 'Ustaadh' aliiambia MICHARAZO mapema leo kuwa, pambano hilo la uzito wa kati litafanyika kwenye ukumbi wa PTA Dar es Salaam.
Ustaadh alisema pambano hilo limeandaliwa na Promota Ally Mwazoa kutoka Tanga na TPBO-Limited watalisimamia kama chama wenyeji.
"Baada ya kufanikiwa kumchapa Japhet Kaseba na kutwaa ubingwa wa UBO Afrika, bondia Thomas Mashali ana nafasi nyingine ya kutwaa taji jingine atakapopanda ulingoni Mei Mosi kupigana na Karama Nyilawila," alisema.
Ustaadh alisema mabondia hao walisaini mkataba huo jana na kwamba wanaanza maandalizi kwa ajili ya mchezo huo utakaokuwa wa raundi 12 uzito wa Super Middle utakaosindikizwa na michezo kadhaa ya utangulizi.
Rais huyo wa TPBO-LImited, alisema anaamini ni nafasi kwa mabondia wote wawili kumaliza ubishi baina yaoe baada ya hivi karibuni Mashali kuwakejeli Nyilawila na Mada Maugo akiwafananisha na midoli na kudai hakuna wa kumweza.
Mashali aliyepigana mara 13 na kushinda michezo 10 akipigwa miwili na kutoka sare mchezo mmoja, alimtwanga Kaseba kwa pointi katika pambano lililofanyika mwishoni mwa mwezi uliopita na kutwaa taji la UBO Afrika lililokuwa wazi.

Yanga, Azam hapatoshi kesho VPL

Mabingwa watetezi Yanga watakaovaana na Kagera Sugar
Vinara wa VPL, Azam watakaoitembelea Ruvu Shooting Mabatini
Ruvu itavuna nini dimba lake la nyumbani dhidi ya  Azam kesho
Baada ya kuidindia Simba uwanja wa Kaitaba na kutoka sare ya 1-1, Kagera ya jackson Mayanja itavuna nini kwa Yanga kesho Taifa?
KIVUMBI cha Ligi Kuu ya ya Vodacom Tanzania Bara inaendelea kesho (Aprili 9 mwaka huu) huku timu za Azam na Yanga ambazo zipo nafasi mbili za juu zikiendelea kuchuana. Azam itakuwa mgeni wa Ruvu Shooting katika mechi itakayochezwa kwenye Uwanja wa Mabatini uliopo Mlandizi mkoani Pwani. Nayo Yanga itakuwa mwenyeji wa Kagera Sugar katika Uwanja wa Taifa jijini.
Joto la mechi hiyo lilianza mapema kwa Azam kuomba kuahirishiwa kutoka Jumapili hadi kesho, huku wapinzani wao wakiwasimamisha nyota wake watatu waliodaiwa kutoweka kinyemela kambini.
Wachezaji hao ambao hawatakuwepo katika mechi hiyo ya Mabatini ni Ibrahim Susan 'Chogo', Juma Seif 'Kijiko' na Cosmas Lewis. Watetezi Yanga, vinara wa ligi hiyo Azam, Ruvu Shooting na Kagera Sugar zote zimeshinda mechi zao za raundi ya 23 wakati mechi za kesho zitakuwa kwa ajili ya kukamilisha raundi ya 24 ya ligi hiyo ambayo inatarajia kukamilika Aprili 19 mwaka huu. Ligi hiyo itaingia raundi ya 25 Aprili 12 na 13 mwaka huu ambapo timu zote 14 zitakuwa viwanjani. Aprili 12 mwaka huu itakuwa Mtibwa Sugar vs Ruvu Shooting (Manungu, Morogoro), Coastal Union vs JKT Ruvu (Mkwakwani, Tanga), na Tanzania Prisons vs Rhino Rangers (Sokoine, Mbeya).
Aprili 13 mwaka huu ni Mgambo Shooting vs Kagera Sugar (Mkwakwani, Tanga), Simba vs Ashanti United (Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam), Mbeya City vs Azam (Sokoine, Mbeya) na Oljoro vs Yanga (Sheikh Kaluta Amri Abeid, Arusha).
Azam inaongoza msimamo ikiwa na pointi 53 wakati Yanga wenyewe wana pointi 49 na Kagera Sugar wana 34 huku Ruvu Shooting wakiwa na 32 hali inayoonyesha upinzani ulivyo kwa timu zote nne na matokeo yoyote yanaweza kubadilisha msimamo hasa baina ya Ruvu na Kagera Sugar wanaochuana na Simba kuwania nafasi ya nne.

TFF yazithibitisha zilizopanda Ligi Kuu 2014-2015

http://www.eatv.tv/sites/default/files/styles/detailpageimg/public/ndanda%20uwiiiiiiiiiiiii.jpg?itok=eDereNWK
Timu ya Ndanda FC iliyopanda Ligi Kuu msimu ujao
https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEiaJ14FtkVg1y8zrjK8LdjzREEGxgzh8IN3GKVznVp2K0mMuy8ZF2EeEY2Fgm5LWFXYO6O2VDZQeN1wUHd3SAl4fu0kdvqgHu-50NZqtOhZ4J9zg7f2-xJa8bAXhgn1m-g1DrMLkC7FZ7bl/s1600/KIKOSI+POLISI.jpg
Polisi Moro iliyorejea Ligi Kuu kwa mara nyingine tena
SHIRIKISHO la Soka Tanzania (TFF), limezithibitisha timu za Ndanda SC ya Mtwara, Polisi ya Morogoro na Stand United ya Shinyanga kupanda daraja kutoka la Kwanza, kwenda Ligi Kuu ya Vodacom msimu ujao.
Taarifa ya TFF leo, imesema timu tatu za Ligi Daraja la Kwanza zitacheza Ligi ya Mkoa katika mikoa yao msimu ujao baada ya kushika nafasi za mwisho katika makundi yao, hivyo kushuka daraja.
Transit Camp imeshika nafasi ya mwisho katika A wakati Mkamba Rangers imeshuka daraja kwa kukamata mkia katika kundi B. Nayo Pamba SC imerudi kucheza Ligi ya Mkoa wa Mwanza baada ya kuwa ya mwisho kwenye kundi C.
Timu zilizopanda daraja kutoka FDL kwenda Ligi Kuu ya Vodacom (VPL) msimu ujao ni Ndanda SC ya Mtwara kutoka kundi A, Polisi Morogoro ya kundi B na Stand United ya Shinyanga iliyoibuka kinara katika kundi C.

Chelsea kikaangoni leo, Ronaldo fit kuwakabili Dortmund

Ronaldo aliyerejea tena dimbani
Chelsea watakaokuwa na kibarua kigumu mjini London mbele ya PSG
WINGA nyota wa Real Madrid, Cristiano Ronaldo yupo fiti tayari kuwakabili Wajeruman, Borussia Dortmund katika pambano la leo la marudiano la Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya, licha ya kudaiwa kulalamika kusumbuliwa na goti baada ya kuumia wakati Real Madrid ikishinda 3-0 kwenye mechi ya awali.
Wakati Real wakichekelea, Chelsea watakuwa na kazi ngumu ya kubadili matokeo ya kipigo cha mabao 3-1 dhidi ya PSG, licha ya kiungo wake kutamba kuwa hilo litawezekana leo Stanford Bridge.
Kocha wa Real, Carlo Ancelotti alimpumzisha Ronaldo katika mechi ya La Liga Jumamosi ambayo waliibuka na ushindi wa mabao 4-0 uliowasaidia kupunguza wigo wa pointi dhidi ya vinara Atletico Madrid na mabingwa watetezi Barcelona wanaoshika nafasi ya pili.
Nahodha huyo wa Ureno, ambaye wiki iliyopita aliweka rekodi kwa kufikisha mabao 14 msimu huu kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya, alikuwa alilalamika kutojisikia vizuri katika goti la mguu wa kushoto lakini Ancelotti alisema atakuwapo uwanjani katika mechi ya marudiano leo nchini Ujerumani baada ya kupata matibabu na mapumziko.
Ronaldo alifikisha mechi 100 za Ligi ya Mabingwa Ulaya katika mchezo wa awali Bernabeu na mabao yake 14 yalimfanya kuifikia rekodi ya Lionel Messi aliyoiweka katika msimu mmoja wa 2011/12.
Kwa ujumla Ronaldo amefunga mabao 64 kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya, matatu nyuma ya nyota wa Barcelona, Messi, na anayo 54 katika mechi 44 zilizopita za Real na Ureno ikiwa ni pamoja na 'hat-trick' tano.
Real ina hofu ya kumkosa mchezaji ghali zaidi duniani Gareth Bale baada ya Jumamosi kupata majeraha katika goti lake la kulia wakati wakicheza huko San Sebastian.
Winga huyo wa Kimataifa wa Wales, ambaye alifumania nyavu na kuifanya Real kuwa mbele kwa mabao 2-0, alihitaji kushonwa nyuzi mbili, taarifa za ndani zilieleza.
Hata hivyo, Ancelotti hakuongea lolotekatika mkutano na waandishi wa habari kuhusu majeraha ya winga huyo.
"Ushindi huu umetuimarisha na pia tumeepuka kuwa na mejeruhi na tulikuwa imara," Muitalia huyo alisema. "Tumecheza vizuri sana, kwa akili. Tulianza kwa kasi na tulikuwa imara sana katika kipindi cha pili.
"Kila mmoja alikuwa katika nafasi nzuri kimchezo ninafurahi kwa kuwa haikuwa rahisi. Ninajisikia furaha kuiongoza timu hii. Ninao wachezaji ambao wanapenda kupigana, tutaendelea kupigana hadi mechi ya mwisho."
Msimu uliopita katika michuano hiyo Dortmund ilipeperusha ndoto za Real baada ya kuitoa kwenye hatua ya nusu fainali.
Dortmund, pia ilijiweka katika nafasi ya kufanya vizuri katika mechi ya leo baada ya Jumamosi kutoka nyuma na kushinda 2-1 dhidi ya VfL Wolfsburg kwenye mechi ya Bunsdesliga, hivyo kushika nafasi ya pili katika kinyang'anyiro hicho ambacho Bayern Munich imeshaibuka mabingwa.
"Ushindi huu ni mzuri kwetu," alisema Kocha wa Dortmund, Juergen Klopp. "Kama tungepoteza tungekuwa tumenyosha mikono juu kutokana na presha ya mchezo. Ilikuwa ni muhimu kushinda na kuelekea mechi ya Jumanne tukiwa tunajisikia vizuri.
"Hatuwezi kuachia chochote bure. Jumanne (leo) tunahitaji kuwa na nusu ya pili nzuri na baada ya hapo tutaona nini kinatokea."
Klopp atakuwa na kinara wake wa kucheka na nyavu Robert Lewandowski baada ya mechi iliyopita kuwa nje akitumikia adhabu.
Lewandowski alifumania nyavu dhidi ya Wolfsburg Jumamosi, hivyo uwezo wake wa kucheka na nyavu utakuwa muhimu leo kama Wajerumani hao wanataka kusonga mbele.
Kocha Jose Mourinho amekuwa akilalamika kuwa kikosi chake hakina mshambuliaji, lakini vyovyote itakavyokuwa, Chelsea bado inayo nguvu ya kuwafunga mabingwa wa Ufaransa Paris St Germain na kutinga nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya leo.
PSG, bila nyota wake Zlatan Ibrahimovic ambaye ni majeruhi, haitahitaji kufunga bao Uwanja wa Stamford Bridge leo ili kuitoa Chelsea, kwani tayari ina faida ya mabao 3-1 kwenye mechi ya awali jijini Paris.
Ni wazi hautakuwa rahisi, hasa ikifahamika kuwa ushindi wa 2-0 unatosha kwa Chelsea kusonga mbele kwa faida ya bao la ugenini.
Hata kama washambuliaji wake watashindwa kufumvutia Mourinho, Chelsea ina viungo wanaojua kuteleza na kuibeba miamba hiyo ya Magharibi mwa London.
Hata hivyo, Chelsea katika Uwanja wa Stamford Bridge ni habari tofauti kwa timu ambayo imepoteza mechi tatu za nje katika michuano yote msimu huu.
Jumamosi iliitandika Stoke City 3-0 katika Ligi Kuu England huku mabao yote yakifungwa na viungo: Mohamed Salah, Willian na Frank Lampard, ambaye mpaka sasa ameshafumania nyavu mara 250 tangu akiwa West Ham United, Swansea City na sasa Chelsea. Pia ana mabao mengine 29 kwa timu ya Taifa ya England.
Mechi hiyo pia ilikuwa ya 77 bila kufungwa kwa Mourinho katika vipindi vyake viwili kwenye klabu hiyo, jambo ambalo atahitaji kuonyesha ubora wake tena Ulaya.
"Tunajua haitakuwa rahisi nyumbani, lakini tutabadili matokeo," kiungo Eden Hazard, ambaye alifunga kwa penalti katika mechi ya awali alisema.
"Tulithibitisha tunaweza kufanya hivyo kabla, na tunaweza kufanya hivyo tena wiki hii (leo)."

Anelka amfuata Ronadinho Brazil

Nicolas Anelka
MSHAMBULIAJI wa zamani wa timu ya taifa ya Ufaransa, Nicolas Anelka amejiunga na Atletico Mineiro na kuungana na nyota wa zamani wa klabu mbalimbali za Ulaya, Ronaldinho, kwa mujibu wa rais wa klabu hiyo ya Brazil, Alexandre Kalil.
Anelka (35) hana klabu tangu alipotimuliwa na West Brom mwezi uliopita baada ya kushangilia goli alilofunga katika sare ya 3-3 dhidi ya West Ham Desemba mwaka jana kwa staili ya saluti ya Hitler.
Chama cha soka England (FA) kilimfungia mechi tano na kumtoza faini ya paundi 80,000 kwa kosa hilo.