STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, September 5, 2010

Dk Kikwete akiri watumishi wake wengi ni wezi



MGOMBEA wa Urais wa Chama cha Mapinduzi, CCM, Dk Jakaya Kikwete, amekiri wazi kuwa, watumishi wengi wa Halmashauri ni wezi na ndio wanaokwamisha miradi mingi ya maendeleo.
Aidha mgombea huyo amesema kuwa watanzania wengi wanajitakia kupata maambukizo ya ugonjwa wa Ukimwi kwa kuendekeza starehe na 'kiherehere' cha kupapia mapenzi yasiyo salama licha ya hamasa mbalimbali zinazotokea juu ya kujikinga na maradhi hayo.
Dk Kikwete aliyasema hayo jana katika mkutano wake wa kuomba kura katika uchaguzi mkuu ujao na kuwanadi wagombea wa nafasi za udiwani na ubunge wa wilaya ya Kilosa, mkoani Morogoro.
Alisema kuwa, pamoja na juhudi za serikali chini ya CCM kutaka kuleta maendeleo kwa wananchi, wapoo baadhi yawatumishi wa Halmashauri ambao ni wezi na wanaoangalia masilahi yao kwa kuzifuja fedha za miradi katika maeneo yao.
"Watumishi wengi wa Halmashauri ni wezi na wanaokwamisha miradi ya maendeleo kwa kuzitumia vibaya fedha wanazopelekewa na serikali kwa ajili ya kuwainua wananchi katika sekta mbalimbali jambo ambalo ni baya," alisema Dk Kikwete.
Katika kukaribia na hilo, mgombea huyo alisema akipata nafasi ya kuchaguliwa tena atahakikisha anapambana nao kwa ari zaidi, nguvu zaidi na kasi zaidi kama ilivyo kauli mbiu yao kwa kuwa kufanya hivyo kutaondoa kikwazo cha kuwapelekea wananchi maendeleo.
Akizungumza suala la maambukizi ya Ukimwi, mgombea huyo wa CCM, alisema anaamini kuwa, ugonjwa huo unakingika na kuepukika iwapo wananchi wataamua kuzingatia mahubiri na makatazo ya viongozi wa kidini juu ya suala la zinaa.
Dk Kikwete alisema maambukizi mengi yaliyopo nchini ni kama wananchi wanajitakia wenyewe kwa kutawaliwa na kuendekeza starehe na kiherehere cha kukimbilia mapenzi yasiyo salama.
"Kama sio kiherehere ni vipi mwanafunzi badala ya kushughulika na masomo shuleni yeye anakimbilia mapenzi?" alihoji Dk Kikwete.
Alitoa ushauri kwa wananchi juu ya kuwa makini na ugonjwa huo kwa kuoa, kujizuia kuwa waaminifu au kutumia kinga.
Kwani kwa kutokufanya hivyo maambukizi yatazidi kuongezeka na taifa kupoteza nguvu kazi ilihali Tanzania Bila Ukimwi Inawezekana!
Alizungumzia dawa za kurefusha maisha ya waathirika, Dk Kikwete serikali yake inatoa dawa hizo bure na kudai kama kuna wanananchi wanaouziwa basi watakuwa wanaibiwa na wanapaswa kutoa taarifa ili wahusika washuighulikiwe.
Juu ya malaria, aliyodai seikali yake inaumia kuona wananchi wanakufa kwa ugonjwa huo kuliko hata Ukimwi na kudai wameweka mikakati ya kupambana nao kwa kuongeza ugawaji wa vyandarua, kupuliza dawa katika kila nyumba nchi nzima na kuhakikisha wanaua mbu wanaoambukiza ugonjwa huo.

Mwisho

Chagueni CCM Tanzania istawi-Dk Kikwete





MGOMBEA wa Urais wa kiteki ya CCM, Dk Jakaya Kikwete, amewataka wananchi kukichagua chama chake kwa mara nyingine ili kuistawisha nchi, kwa maelezo kwamba vyama vya upinzani vilivyopo ni vya msimu na havina uwezo wa kuongoza.
Dk Kikwete ambaye pia ni Rais wa Jamhuri ya Muungano aliyasema hayo leo alipokuwa akiwatuhubia wakazi wa wilaya ya Kilosa katika mkutano wa kampeni uliofanyika eneo la Wahanga wa Mafuriko lililopo njia panda ya Ilonga na Kimamba, mkoani Morogoro.
Rais Kikwete alisema kuwa, pamoja na kwamba wapinzani wamekuwa wakitoa kejeli dhidi ya utendaji wa CCM, ukweli ni kwamba vyama hivyo havina uwezo wa kuongoza na hivyo ni vema wananchi wakaichagua tena CCM kustawisha maendeleo yaliyopo.
Alisema pamoja na utitiri wa vyama vya upinzani, vingi vyake ni vya msimu tu, ambapo huibuka wakati wa uchaguzi na hasa wanapofanikiwa kuwapata wanaohama toka CCM.
"Wananchi wa Kilosa na Watanzania kwa ujumla nawaombeni muichague CCM kwa mara nyingine kwa kuwa ndio chama pekee bora kinachoweza kustawisha maendeleo ya nchi yaliyopo pamoja na kudumisha amani na utulivu, vyama vingi vya upinzani ni vya msimu tu na hasa vinapofanikiwa kuwanasa wanaohama toka CCM pale wanapogombea na kutochaguliwa," alisema Dk Kikwete.
Dk Kikwete alisema CCM imfanikiwa kutekeleza ilani ya uchaguzi ya mwaka 2005 kwa asilimia kubwa katika nyanja na sekta za Afya, Elimu, Maji, Miundo Mbinu, Kilimo na Ufugaji na ikipewa nafasi tena itamalizia sehemu zilizobakia.
Alitoa mfano suala la elimu kwa wilaya ya Kilosa, imefanikiwa kuongeza majengo ya shule kuanzia chekechea hadi sekondari, ambapo alisema kwa mfanoi mwaka 2005 idadi ya wanafunzi katika sekondari ilikuwa ni 6969 ambapo kwa sasa idadi hiyo imefikia 17666 ikiwa ni ongezeko la zaidi ya wanafunzi 10,000.
Pia alisema juhudi hizo za kuboresha sekta hiyo zinaendana na kuongeza idadi ya walimu ambapop alisema mwaka 2005 idadi ya wahitimu wa ualimu nchi nzima ilikuwa ni 600 tu, lakini awamu ya nne imejitahidi na kufanya idadi hiyo kufikia 16,000.
Alisema, anafahamu idadi hiyo bado haikidhi hivyo serikali yake kupitia CCM inafanya mipango ya kuongeza walimu zaidi kupitia vyuo vyake na vile vya watu binafsi ili kufikia lengo sambamba na kuwezesha kupatikana kwa vitabu, maabara na nyumba za walimu.
Kuhusiana na vitabu,Dk Kikwete alisema tayari jitihada zimeshafanywa kwa kuomba msaada toka kwa nchi marafiki ikiwemo Marekani ambayo imejitolea kutoa jumla ya vitabu 800,000 vya masomo mbalimbali ya sekondari na mapema mwakani itapokea vitabu vingine zaidi ya Mil 2.4.
Alisema hayo na mengine ambayo yamekuwa yakifanywa na CCM tangu iwe madarakani hayawezi kufanywa na vyama vya upinzani na kuwataka wapiga kura kutofanya makosa Oktoba 31 watakapochagua viongozi kwa ajili ya miaka mitano ijayo.
Katika hatua nyingine, mgombea huyo alizungumzia suala la wahanga wa mafuriko yaliyoikumba wilaya hiyo mnamo Desemba mwaka jana, kuwa serikali ipo katika mpango wa kuwajengea nyumba za kudumu wahanga hao wanaishi kambini kwa sasa.
Dk Kikwete alisema kazi ya ujenzi wa nyumba hizo utafanywa na Jeshi la Kujenga Taifa, JKT, kwa lengo la kuwarejesha maisha ya amani na utulivu wakazi hao ambao kwa sasa wanaishi katika nyumba za mabati.
Pia alisema, serikali imetenga fedha kwa ajili ya ujenzi wa bwawa jipya la Kidete pamoja na kujenga tuta jipya la kudhibiti maji ya Mto Mkondoa ambao aliutaja kuwa ndio tatizo lililosababisha mafuriko hayo yaliyoleta maafa makubwa.
Katika ziara yake ya kampeni wilayani humo, mgombea huyo wa CCM alikuwa akisimamishwa yeye na msafara wake na wananchi mbalimbali wa vijiji kwa ajili ya kumueleza kero zao.
Alipofika kata ya Dumila wananchi wa eneo hilo kupitia Mwenyekiti wa serikali ya Mtaa wa Dumila, Douglas Mwaigumila, walimueleza mgombea huyo juu ya kero zinazowakabili ambapo walizitaja ni huduma ya maji, afya, umeme na uporwaji wa ardhi yao ipatayo ekta 400 shutuma alizozipeleka kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya wilaya yao.
Dk Kikwete aliwajibu wananchi hao kuwa serikali yao inayatambua kero hizo na tayari ilishaanza kuzitekeleza kwa awamu, huku akishangaa kusikia tukio la uporwaji huyo wa ardhi na kuahidi kulifuatilia.