STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, June 29, 2011

Hapa na pale za Micharazo



Villa Squad yaangukia wadau

UONGOZI mpya wa klabu ya soka ya Villa Squad, umekiri una kazi ngumu katika kuiongoza klabu hiyo kutokana na hali mbaya kiuchumi iliyonayo na kuwaangukia wadau wa soka wa wilaya ya Kinondoni kujitokeza kuisaidia kwa hali na mali.
Villa iliyorejea Ligi Kuu Tanzania Bara baada ya kushuka daraja mwaka 2008, ilipata viongozi wake mwishoni mwa wiki katika uchaguzi mkuu uliohusisha nafasi za makamu mwenyekiti na wajumbe wa kamati ya utendaji tu.
Makamu Mwenyekiti, Ramadhani Uledi, alisema kwa jinsi hali ilivyo mbaya kiuchumi katika klabu hiyo wanalazimika kuwaomba viongozi, wanasiasa na wakazi wa wilaya yao kuisaidia kwa hali na mali klabu yao ili kuhimili vishindo vya ligi hiyo wasirudie makosa ya mwaka 2008.
Uledi, alisema Villa kwa sasa ni kama 'jicho' kwa wakazi wa Kinondoni kutokana na kuwa timu pekee kushiriki Ligi Kuu baada ya awali kuteremka daraja na hivyo ipewe sapoti ikisaidiwa ili irudi 'mchangani'.
"Pamoja na kuwashukuru wanachama kutuchagua kuiongoza Villa, tulikuwa tunaomba tupewe sapoti ya kutosha kwa wadau wa soka na wakazi wa Kinondoni kuiunga mkono kwa kuisaidia kwa hali na mali ili imudu mikikimikiki ya ligi kuu na tusirejee makosa ya 2008 tuliposhuka daraja," alisema Uledi.
Aliongeza uongozi wao ulitarajiwa kupanga siku ya kukutana kwa ajili ya kujadili mambo mbalimbali pamoja na kuteua kamati za kuusaidia uongozi wao katika maandalizi ya ushiriki wao wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu ujao inayotarajiwa kuanza Agosti 20 mwaka huu.
***

Yanga waituliza Ruvu Shooting


BAADA ya Ruvu Shooting kuitemea cheche Yanga kwa kumchukua beki wao Oscar Joshua bila kufuata taratibu, uongozi wa Yanga umewatuliza ukisema watamalizana nao tu.
Yanga imeipoza Ruvu kwa kusema isubiri mapesa ya mchezaji huyo kwani hata wao wanajua kuwa ametokea kwao.
Msemaji wa Yanga Louis Sendeu amesema, uongozi wao unafahamu kuwa Joshua hajaokotwa jalalani ila kuna timu ametoka, hivyo haiwezi kumsajili bila kufuata taratibu.
"Hili ni suala la muda tu, sisi tutakutana na viongozi wa Ruvu Shooting na tutamalizana tu, hala hakuna tatizo," alisema Sendeu.
Yanga imeamua kupoza makali hayo, baada ya Ruvu kuwa mbogo na kusema kuwa itapinga sehemu yoyote yule mchezaji wao huyo kwenda Yanga kwa sababu hawakumchukua kihalali.
Viongozi wa Ruvu waliripotiwa kwenye vyombo mbalimbali vya habari, walisema kuwa mchezaji huyo ana mkataba na timu yao.
Kabla hata Yanga haijamalizana na Ruvu, tayari mchezaji huyo ameanza kuitumikia timu hiyo kwenye michuano ya Kagame.
Mchezaji huyo mwenye uwezo wa kucheza beki na kiungo amejiunga na Yanga akitokea Ruvu Shooting ambako nako alichukuliwa kutoka Toto African ya Mwanza.
***

Mcuba kuwasaka 10 Bora ngumi taifa


MABONDIA wa timu ya taifa ya ngumi waliopo kambi ya mazoezi jijini Dar es Salaam wanatarajiwa kuchuana wenyewe kwa wenyewe ili kuchujwa na kupatikana mabondia 10 watakaoiwakilisha nchi kwenye michuano ya 'All African Games'.
Michuano hiyo ya Afrika inatarajiwa kufanyika kati ya Septemba 3-18 mjini Maputo Msumbiji.
Mchujo wa mabondia wa Tanzania unatarajiwa kufanywa na Kocha Mkuu wa timu hiyo, Mcuba Pimintel Hutardo ambaye anatarajia kuwashindanisha wachezaji wake kusaka wakali 10.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Ngumi za Ridhaa Tanzania, BFT, Makore Mashaga, alisema kocha Hutardo atawachuja mabondia hao katika michezo itakayofanyika kwenye kumbi mbalimbali za jijini Dar es Salaam ukihusisha mapambano 20.
Mashanga alisema baada ya mchujo huo mabondia 10 watakaosalia wataendelea kujifua pamoja na kwenda kucheza mechi za majaribio katika nchi kadhaa ambazo Tanzania imapata mialiko na kuzitaja ku ni pamoja na England, India, Scotland na Mauritius.
Katibu huyo alisema sababu ya kocha kuendesha zoezi hilo la mchujo kwa kushindanisha mabondia hao wenyewe ni kupata wachezaji wenye uwezo wa kuisaidia Tanzania kwenye michuano hiyo ya Afrika ambayo inatarajiwa kushirikisha karibu nchi 55.
***

Kinondoni yaapa Pool Taifa


MABINGWA watetezi wa michuano ya taifa ya Pool ya 'Safari Lager National Pool Championship 2011' yaliyoanza kutimua vumbi Juni 30, wametamba kutetea vema ubingwa huo waliouchukuwa mwaka jana mkoani Arusha.
Katibu mkuu wa chama cha pool cha Kinondoni (KIPA), Zaharo Ligalu aliwaambia makatibu wakuu juzi wa klabu 10 zitakazoshiriki mashindano hayo kuwa wamejipanga vema kuhakikisha hawapotezi ubingwa huo.
Ligalu aliyasema hayo wakati wa upangaji wa ratiba ya mashindano hayo kwenye ukumbi wa Meeda Club uliopo Sinza Jijini Dar es salaam.
Alisema kuwa licha ya ushindani mkubwa ambao wanategemea kuupata kutoka kwa mikoa mingine lakini hakuna sababu ya kuchukuwa tena ubingwa huo kutokana na Kinondoni kusheheni vipaji vya wachezaji wa mchezo huo.
"Makatibu wenzangu wa klabu naomba niwambie kuwa tumejipanga kuhakikisha ubingwa unarudi tena Kinondoni, hivyo endeleeni kuwaandaa wachezaji wenu vizuri ambao nina imani ndiyo watakaosaidia Kinondoni kutetea vema ubingwa wetu,"alisema Ligalu.
Alisema kuwa kikubwa ambacho kitafanikisha kutetea ubingwa huo ni ushirikiano wa pamoja wa wadau wote wa mchezo huo wa Kinondoni.
Klabu zinazoshiriki mashindano hayo ngazi ya mikoa kwa upande wa Kinondoni ni Shoko, Topland, Meeda, 4 wayz, Madrid, Mkwajuni, Ubungo Terminal, Jaba, Bahama mama na Mlalakuwa.
Fainali za taifa ambazo Kinondoni itatetea taji lake zitafanyikia kwenye ukumbi wa Kilimani mkoani Dodoma.

===========
Akudo, Mapacha Wa3 uso kwa uso


BENDI za muziki wa dansi za Akudo Impact na Mapacha Watatu, zinatarajia kufanya onyesho la pamoja linalolenga kudumisha urafiki baina ya wanamuziki wa bendi hizo mbili.
Mratibu wa onyesho hilo, Mkurugenzi wa kampuni ya Biggy One Entertainment, Abubakar Mwanamboka, alisema bendi hizo zitaonyeshana kazi kesho kwenye ukumbi wa Vatican, Dar.
"Lengo letu ni kutaka kuonyesha kwamba bendi za muziki wa dansi zinaweza kushirikiana na kuondoa mawazo yaliyojengeka miongoni mwa baadhi ya watu kuwa wanamuziki wa bendi mbili hawawezi kushirikiana," alisema.
Alisema, majigambo kati ya bendi moja na nyingine siyo ugomvi bali ni njia ya kuvuta mashabiki na kwamba kampuni yake imeandaa onyesho hilo ili kudhihirisha kuwa wanamuziki wanaweza kushirikiana katika kazi yao.
Mratibu huyo alisema, mbali na bendi hizo mbili kutoa burudani kwenye onyesho hilo, piaatakuwepo msanii wa muziki wa kizazi kipya H. Baba ambaye naye atafanya vitu vyake.
Aliongeza onyesho hilo la Akudo na Mapacha ni la kwanza kuratibiwa na kampuni yake.
Akudo Impact imekuwa ikitamba na albamu ya kwanza ya 'Impact' wakati Mapacha Watatu nayo ikitamba na albamu ya kwanza ya 'Jasho la Mtu' na sasa bendi hizo kila moja iko kwenye maandalizi ya albamu ya pili.


Mwisho