STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Monday, April 25, 2011

Tamasha la ngumi laanzishwa Dar

MABONDIA mbalimbali wakiwemo wakongwe na chipukizi wanatarajia kujumuika pamoja katika tamasha maalum la ngumi linaloanza rasmi kesho kwenye Manispaa ya Ilala, jijini Dar es Salaam.
Tamasha hilo lililoandaliwa na Taasisi ya Kinyogoli Foundation inayomilikiwa na bondia wa kimataifa wa zamani ambaye ni kocha kwa sasa, Habib Kinyogoli, awali lilipangwa kufanyika leo Jumatatu ya Pasaka, kwenye ukumbi wa Panandipanandi.
Akizungumza na MICHARAZO, mmoja wa waratibu wa tamasha hilo, Rajabu Mhamila 'Super D' alisema katika tamasha hilo, mabondia mbalimbali wakongwe na chipukizi watachuana na lengo ni kuwapa nafasi chipukizi ya kujifunza mbinu kutoka kwa mabondia hao wazoefu.
Super D ambaye pia ni bondia wa zamani na kocha wa klabu ya Ashanti, alisema yeye na Kinyogoli, wameamua kushirikiana kuandaa tamasha hilo ili kuhakikisha mchezo wa ngumi nchini unarejesha heshima yake baada ya kudorora kwa muda mrefu.
"Katika kurejesha hadhi ya ngumi nchini, tumeamua kuandaa tamasha la ngumi ambalo litakuwa likifanyika kila wiki kwenye ukumbi wa Panandi Panandi ambapo wakongwe na mabondia wanachipukia watashirikiana kupigana katika kutoa burudani," alisema Super D.
Aliongeza kuwa, mbali na michezo kadhaa ya ngumi, ikiwahusisha baadhi ya nyota wa mchezo huo kama mabondia wa ukoo wa Matumla, pia tamasha hilo litapambwa na burudani kemkem za muziki kutoka kwa wasanii ambao watakakuwa wakipokeza kwenda kutumbuiza kama njia ya kuwahamasisha watu kuhudhuria kwa wingi.

Sikinde wana mbili mpya



BENDI ya Mlimani Park 'Sikinde' imekamilisha vibao viwili ikiwa ni moja ya mikakati yake ya kujipanga upya baada ya kuondokewa na mwanamuziki wake, Shaaban Dede aliyejiunga na mahasimu wao, Msondo Ngoma.
Katibu wa bendi hiyo, Hamis Milambo, alisema kuwa bendi yao ambayo kwa wiki mbili mfululizo imekuwa kambini ikijifua, ambapo imekamilisha nyimbo mbili zilizotungwa na muimbaji wao mkongwe, Hassani Bitchuka.
"Tumeanza kujipanga upya kwa ajili ya kupakua albamu mpya na tayari tupo kambini kwa wiki ya pili sasa, ambapo tumeshakamilisha nyimbo mbili mpya zilizotungwa na Bitchuka," alisema.
Katibu huyo alisema nyimbo hizo zinazoendelea kufanyiwa mazoezi, hazijapewa majina hadi sasa na zitatambulishwa kwa mashabiki wao katika maonyesho yao ya Sikukuu ya Pasaka.
"Tutazitambulisha kwenye maonyesho yetu ya Pasaka, na hapo ndipo zitakapofahamika majina yake, ila ni kati ya nyimbo zitakazothibitisha kuwa Sikinde ni mabingwa wa muziki wa dansi nchini," alisema Milambo.
Milambo alisema baada ya maonyesho ya Pasaka, bendi yao itarejea kambini kwa ajili ya kumalizia kuzifanyia mazoezi nyimbo nyingine mpya ambazo zimeshaandikwa mashairi na waimbaji wao, Abdallah Hemba na Hassani Kunyata tayari kukamilisha idadiu ya nyimbo zinazotakiwa kwa albamu yao ijayo.
Tangu mwaka juzi, Sikinde ilipotoa albamu yao ya Supu Imetiwa Nazi, bendi hiyo haijaachia albamu nyingine zaidi ya vibao viwili vya Wanawake Wanaweza na Tunu ya Upendo vilivyotungwa na Dede maarufu kwa sasa kama 'Mzee wa Loliondo' ambaye ameenda Msondo Ngoma.

Kitabu cha Assosa chatinga mitaani





KITABU cha mwanamuziki nguli wa muziki wa dansi, Tshimanga Kalala Assosa, kiitwacho 'Jifunze Lingala' kimeingia mitaani, huku mwenyewe akijiandaa kutoa toleo la pili la kitabu hicho kinachofundisha lugha ya Kilingala na Kiswahili.
Akizungumza na MICHARAZO, Assosa, alisema kitabu hicho ambacho mbali na kufunza watu Kilingala, pia kina tafsiri ya nyimbo za wanamuziki maarufu wa Kongo na kiliingia sokoni tangu juzi huku kikigombewa kama njugu.
Assosa, alisema tangu akiingize sokoni kitabu hicho kimeshauza kopi zaidi ya 1000, huku akipokea oda kedekede toka kila pembe ya nchi kwa watu wanaokiulizia.
"Aisee kile kitabu changu nimeshakiingiza sokoni, na huwezi kuamini kimekuwa kikinukuliwa kama njugu tofauti na matarajio yangu, hali inayonifariji mno," alisema Assosa.
Mkongwe huyo aliyewahi kuzipigia bendi za Negro Succes, Orchestre Lipualipua, Fukafuka, Le Kamalee, Marquiz du Zaire, Marquiz Original, Mambo Bado, Legho Stars na sasa Bana Marquiz, alisema hakutaraji kama kingegombewa.
Alisema hakuwa na tumaini la kugombewa kwa kitabu chake kutokana na ukweli ndicho cha kwanza kwake kukitoa tangu aamue kujikita kwenye uandikaji wa vitabu, nje ya shughuli zake za muziki anaoendelea nao hadi sasa.
Aliongeza kuwa, hali hiyo unamfanya afikirie kuongeza idadi ya nakala zake, ili kukidhi mahitaji ya mashabiki wanaokiulizia ambacho ndani yake pia kina picha za wasanii wakongwe wa Kongo pamoja na yeye na familia yake.
"Kama watakuwa wanavihitaji pia wanaweza kwenda pale Shule ya Sekondari Benjamin Mkapa, kuna wakala anaviuza pale, au wanaweza kunipigia simu namba 0713-240735, watakipata." alisema Assosa.

Rapa wa Levent atua TOT-Plus

BENDI ya TOT-Plus ambayo sasa inaendelea na kambi yake ya mazoezi, Mwananyamala, jijini Dar es Salaam, imempata rapa mpya Dokta Steve 'Sauti ya Ng'ombe' kutoka bendi ya Levent Musica ya mjini Morogoro.
Kiongozi wa TOT-Plus, Badi Bakule, alisema rapa huyo alijiunga na tangu wiki iliyopita na anaendelea
na mazoezi kama kawaida akisubiri kutambulishwa rasmi.
"Tumemchukua rapa huyu ili kuziba nafasi ilioachwa na Jua Kali ambaye ameachana na TOT-Plus na kwenda kufanya kazi kwingine, Dokta Steve ameonyesha uwezo mkubwa hivyo anatufaa," alisema Bakule.
Bakule alisema bendi hiyo ambayo imekuwa na mazoezi kwa zaidi ya mwezi mmoja, inatarajia kutoka kambini Ijumaa Aprili 29 na kisha itajitambulisha rasmi Mei Mosi.
Alisema, rapa huyo kwa sasa amekuwa akijifua katika mazoezi makali kwenye kambi ya bendi hiyo iliopo eneo la Ujiji Mwananymala, jijini Dar es Salaam ili kuhakikisha kwamba anaibuka na vitu vipya.
"Pia tunataka azijue nyimbo zote mpya ambazo tayari tumezikalimisha na hata zile za zamani ambazo wanamuziki karibu wote wamezifanyia mazoezi kabla rapa huyu mpya hajajiunga na bendi yetu," alisema.
Kiongozi huyo alizitaja nyimbo hizo mpya kuwa ni 'Kilio cha Linda', 'Zai' 'Maisha Duni', Liwalo na Liwe','Dakika Tisa' na 'Riziki na Zengwe' ambazo baadhi yake tayari zimesharekodiwa.
Aliongeza kuwa 'Sauti ya Ng'ombe' atatoka kambini akiwa pia amemaliza kuzifanyia mazoezi baadhi ya nyimbo za zamani zilizochangia kuiweka TOT-Plus kwenye matawi ya juu.
"Kuna nyimbo kama Masimango, Mtaji wa Masikini, Elimu ya Mjinga, Mtoto Yatima, Mnyonge Mnyongeni na nyingine nyingi ambazo anatakiwa azifahamu vizuri kabla hatujatoka kambini," alisema.
Tangu imalize kampeni za Uchaguzi Mkuu mwishoni mwa mwaka jana, bendi hiyo bado haijafanya maonyesho na badala yake imeingia kambini ili kujipanga vizuri kwa ajili ya kuibuka kwa kishindo.

Stone Mayiyasika wanasa watano

BENDI ya Stone Mayiyasika 'Vijana wa Kazi' imeimarisha safu ya ushambuliaji wa jukwaa kwa kunasa wanenguaji watano akiwemo mnenguaji mahiri aliyewahi kutamba na bendi ya Twanga Pepeta, Juma Mohamed (Super Danger).
Mratibu wa bendi hiyo, Pascal Mahollelo, alisema wanenguaji hao watano wameanza mazoezi na katika maonyesho yao yote ya kusheherekea sikukuu ya Pasaka wataanza kuwatambulisha kwa mashabiki.
Alisema, mbali ya Super Danger ambaye ni mkongwe, wanenguaji wengine wapya ni wa kike na kwamba ni chipukizi ambao wameonyesha uwezo mkubwa wa kazi.
Aliwataja wanenguaji hao wa kike kuwa ni Zawadi Seif, Joselina Ngatunga (Happy), Shania Malimba na Mwanahamisi Ramadhan.
"Sisi hatuhitaji kugombana na watu ndiyo maana tumeona tuwatengeneze wetu wenyewe na nina imani mashabiki watawakubali kutokana na umahiri wao jukwaani" , alisema Mahollelo.
Alisema, utambulisho wa wanenguaji hao ungeanza kwenye maonyesho yao Sikukuu ya Pasaka.

Cloud atambia Basilisa




MSANII nyota wa filamu nchini, Issa Mussa 'Cloud', amedai filamu yake mpya ya 'Basilisa' ni funika bovu, miongoni mwa kazi zake alizowahi kuzitoa kwa hivi karibuni.
Cloud, alisema filamu hiyo iliowashirikisha wasanii kadhaa mahiri nchini, akiwemo mrembo Wema Sepetu na Ummy Wenslaunce 'Dokii', inaweza kuwa kazi bomba kwa mwaka huu wa 2011 kwa jinsi ilivyoandaliwa kwa ustadi mkubwa.
Mkali huyo aliyetamba na michezo ya kuigiza kupitia runinga kabla ya kuibukia filamu, alisema 'Basilisa' ambayo itasambazwa na kampuni ya Steps Entertainment ni bora kati ya zote alizowahi kuzitoa tangu aiingie kwenye fani hiyo.
Alisema kinachomfanya aamini hivyo ni kwa jinsi hadhithi yake ilivyo, namna alivyoshiriki na umahiri ulioonyeshwa na wasanii wenzake, acha upigaji picha wa kiwango cha hali juu na mandhari iliyotumika kurekodiwa kazi hiyo.
"Sio vibaya mtu kujisifia kwa jinsi anavyofanya kazi yake, nami naiona 'Basilisa' ni moja ya kati niliyoumiza kichwa na kushiriki kwa kiwango kikubwa, nadhani itakuwa miongoni mwa kazi bora kwa mwaka," alisema Cloud.
Msanii huyo, ambaye hushirikishwa kazi mbalimbali, alisema ndani ya filamu hiyo ameigiza katika nafasi tatu tofauti kama alivyowahi kufanya muigizaji wa Kimarekani, Eddy Murphy katika filamu yake ya 'Nutty Professor'.
Tofauti na Murphy aliyeigiza kikomedi zaidi, Cloud ndani ya filamu yake ameigiza 'siriazi' akiwa kama chizi, kiumbe wa kutisha na hali yake ya kawaida, kiasi ni vigumu kubaini kama nafasi hizo tatu tofauti zimechezwa na mtu mmoja.
Mbali na yeye (Cloud) wengine walioshiriki filamu hiyo itakayoingia sokoni mwezi ujao ni Adam Kuambiana, Dokii, Wema Sepetu, Selemani Barafu 'Mzee wa Land Rover', Single Mtambalike 'Richie', Kajala Masanja na wengineo.