STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, December 10, 2010

Sam wa Ukweli kuwasindikiza Mapacha Watatu J'3



MSANII anayekuja juu kwenye muziki wa kizazi kipya, Salum Mohammed 'Sam wa Ukweli', anayetamba na kibao cha 'Sina Raha' anatarajia kulisindikiza kundi la muziki wa danis la 'Mapacha Watatu' katika onyesho la 'Usiku wa Sauti ya Kizazi Kipya cha Dansi' linalofanyika keshokutwa.
Onyesho hilo litakalofanyika kwenye ukumbi wa Stereo Bar, Kinondoni jijini Dar es Salaam na Sam wa Ukweli, atakuwepo kulipamba onyesho hilo kwa vibao vyake murua kikiwemo cha 'Sina Raha' kinachotamba kwa sasa nchini.
Akizungumza na MICHARAZO, mratibu wa onyesho hilo, Sauda Mwilima, alisema onyesho hilo ni maalum kwa ajili ya kuwapa burudani mashabiki wa muziki wa dansi kupitia kundi hilo la Mapacha Watatu linaloundwa na waimbaji nyota watatu toka bendi za Africana Stars na Fm Academia.
Waimbaji hao wanaouunda kundi hilo linalotamba na albamu yao ya 'Jasho la Mtu' ni Khalid Chokoraa na Kalala Junior wa Twanga Pepeta pamoja na Jose Mara toka FM Academia.
"Katika kuwapa raha mashabiki wa muziki wanaojiandaa kuuaga mwaka 2010 na kuukaribisha 2011, nimeandaa Usiku wa Sauti ya Kizazi Kipya cha Dansi utakaofanyika Jumatatu ya Desemba 13, ambapo utapambwa na burudani toka kundi la Mapacha Watatu watakaosindikizwa na nyota wa muziki wa kizazi kipya, Sam wa Ukweli," alisema.
Sauda, alisema maandalizi ya onyesho lao yamekamilika kwa asilimia zote na kuwataka mashabiki kukaa mkao wa kula kupata burudani kabambe toka kwa wakali hao.

Munishi aja kuchangia yatima Bongo



MUIMBAJI nyota na mkongwe wa muziki wa Injili, Faustin Munishi anayeishi Kenya, anatarajia kutua nchini wiki ijayo kwa ajili ya kuja kutumbuiza kwenye tamasha maalum la muziki wa Injili la kuchangisha fedha kwa ajili ya yatima na watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu.
Tamasha hiloi litakalofanyika kwenye viwanja vya Posta, Kijitonyama siku ya Desemba 26, limeandaliwa na asasi ya Keep a Child Alive, ambapo wasanii mbalimbali wa muziki wa injili wa ndani ya nje ya nchi wamealikwa kuja kulipamba.
Mratibu wa tamasha hilo, Godfrey Katunzi, aliiambia MICHARAZO kuwa, kati ya wasanii wa muziki wa Injili watakaotumbuiza siku hiyo ya 'Boxing Day' ni muimbaji mkongwe, Mtanzania Faustin Munishi, ambaye kwa miaka mingi anafanya shughuli zake nchini Kenya.
Katunzi, alisema mbali na Munishi anayetamba na vibao kama Chini ya Mwamba, Paulo na Sila, Amua Mwenyewe, Nimuogope Nani na nyingine, wengine watakaotumbuiza siku siku hiyo ni Dk Aaron, Jane Misso, Beatrice Muone na kwaya mbalimbali za jijini Dar es Salaam.
Mratibu huyo ambaye ni Katibu wa asasi hiyo ya Keep a Child Alive, alizitaja baadhi ya kwaya hizo ni ile ya New Life Church wanaotamba na albamu yao ya 'Sipati Picha', Tabata Menonite maarufu kama Wakunyatanyata na nyinginezo.
Katunzi alisema, lengo la tamasha hilo la injili ni kuchangisha fedha kwa ajili ya kusaidia yatima na watoto hao wa mitaani walipiwe ada na kununuliwa vifaa na sare za shule pamoja na kutatua matatizo mbalimbali waliyonayo.
Aliwaomba watu binafsi na makampuni yenye uwezo kujitokeza kuwapiga tafu katika tamasha hilo, ili kutimiza malengo la kuwaonyesha upendo watoto hao, akidai jukumu la kusaidia na kulea yatima ni la watu wote bila kujali, dini, rangi, kabila au jinsia.

Levent kurekodi tatu mpya

BAADA ya ukimya mrefu tangu ilipofyatua albamu yao ya pili ya Mama Kabibi, bendi ya muziki wa dansi ya Levent Musica ya mjini Morogoro wiki ijayo itaingia studio kurekodi nyimbo tatu kwa ajili ya maandalizi ya albamu yao ijayo mpya.
Kiongozi wa bendi hiyo, Seleman Ramadhani 'Suzuki Sauti ya Malaika', aliiambia MICHARAZO jana kuwa nyimbo zitakazorekodiwa ni 'Pongezi Baba Madinda' na 'Mapenzi Maradhi' alizotunga yeye (Suzuki) na 'Mapenzi Sio Pesa' wa Steve Dokta.
Suzuki, alisema nyimbo hizo ni katyi ya nyimbo sita mpya za bendi hiyo zilizopangwa kurekodiwa kwa ajili ya albamu yao mpya na ya tatu ambayo wamepanga kuitoa mapema mwakani.
"Tupo katika maandalizi ya kwenda kurekodi nyimbo mpya tatu, tukiwa tunajiandaa kupakua albamu yetu ya tatu, kwa kweli kwa sasa Levent tupo kamili na tumepania," alisema Suzuki.
Mtunzi na muimbaji huyo, aliyerejea katika bendi hiyo baada ya kuikimbia kwa muda na kujiunga na Extra Bongo, alisema nyimbo nyingine tatu zimeshaanza kufanyiwa mazoezi na mara baada ya kumaliza kurekodi hizo za awali watarejea tena studio kukamilisha nyimbo hizo.
Kuhusu kikosi chao, Suzuki alisemakipo kamili, kila idara kuanzia safu ya unenguaji, wapiga ala na waimbaji ambao mbali na yeye yupo pia Steve Dokta na Salum Mzalamo 'Baba Mapacha'.
Bendi hiyo ya Levent ilianzishwa mwaka 2004 na imewahi kufyatua albamu mbili tu hadi sasa ambazo ni Rafiki ya 2006 na ile ya Mama Kabibi ya mwaka 2008 wakati bendi ikiwa chini ya Richard Malifa, alioyewahi kung';ara na bendi mbalimbali hapa nchini.

Msondo yamuombea Gurumo



WAKATI hali yake ikizidi kuwa tete, uongozi wa bendi ya Msondo Ngoma umemuombea dua njema na kuwataka Watanzania kuzidi kumuombea kiongozi wao na muimbaji mkongwe wa muziki wa dansi nchini, Maalim Muhidin Gurumo aliyelazwa hospitalini kwa matatizo ya mapafu.
Msemaji wa bendi hiyo, Rajabu Mhamila 'Super D', alisema wanamuziki na uongozi mzima wa Msondo umekuwa ukiendesha dua maalum kila siku kumtakia kila la heri na afueni, Gurumo ili aweze kurejea tena jukwaani.
Super D, alisema Msondo bado inamhitaji mno Gurumo kutokana na umahiri wake katika muziki na uongozi kwa ujumla na kuwaomba mashabiki wao na wadau wa muziki wa ujumla kuzidi kumuombea mwanamuziki huyo mkongwe awe kupona haraka.
"Kwa kweli tunamuombea sana mwenzetu aweze kupona na tunawasihi watanzania bila kujali dini, rangi au kabila na ushabiki wa muziki, wamuombee kamanda Gurumo, Mwenyezi Mungu amfanyie tahafif apone haraka," alisema Super D.
Super D, alisema pamoja na kumuombea kiongozi wao huyo, bendi yao bado inaendelea na maonyesho yao kama kawaida pamoja na kufanya maandalizi ya kufyatua albamu yao mpya.
Alisema kwa leo Jumamosi bendi yao itakuwa kwenye bonanza lao kwenye viwanja vya Sigara, TCC- Changombe na kesho Jumapili watawachezesha wapenzi wa muziki miondoko yao ya Msondo kwenye onyesho litakalofanyika Max Bar, Bungoni Ilala jijini Dar es Salaam.
"Hatuwezi kuacha maonyesho, tunaendelea na shoo huku tukizidi kumuombea mwenzetu, leo (jana) Ijumaa tutakuwa Postal Club, Jumamosi tunaendelea na bonanza letu pale TCC-Chang'ombe na tutamalizia wikiendi yetu kwenye ukumbi wa Maxi Bar, Ilala," alisema.
Msondo inayotamba na albamu ya HUna Shukrani iliyotoka mwaka jana, ipo katika maandalizi ya kutoa albamu mpya ambapo hadi sasa tayari imeshaachia nyimbo tatu ambazo ni Dawa ya Deni, Lipi Jema na Mjomba.

Ally Choki awafunda wanamuziki wenzake



NYOTA wa muziki wa dansi nchini, Ally Choki amewafunda wanamuziki wenzake akiwataka wajenge tabia ya kuwa na shukrani wakikumbuka mazuri wanayofanyiwa na bendi wanazozihama badala ya kuziponda na kutaja mabaya tu.
Choki alisema tabia ya wanamuziki wanaohama bendi kuponda na kukashfu kule watokapo sio tu zinavunja umoja, ila inajenga uhasama miongoni mwa wasanii na wamiliki na mwisho wa siku ni kudidimiza muziki ambao umekuwa ukisaidia vijana wengi kupata ajira zao.
Akizungumza na MICHARAZO, Choki, alisema yeye binafsi pamoja na kutamba kimuziki nchini, katu hawezi kusahau fadhila na mazuri aliyofanyiwa na Asha Baraka, kitu alichotaka hata wasanii wengine wawe na moyo wa namna hiyo wa kukumbuka fadhila.
Choki alisema amelazimika kusema hayo kutokana na baadhi ya wasanii walioihama bendi yake kusambaza maneno ya kashfa juu yake na bendi yake, wakati kabla ya kuhama walikuwa wakifanyiwa fadhila zilizowafanya wamuone kama 'Mungu-Mtu'.
"Siwalazimishi, lakini nawaasa wanamuziki wenzake na wasanii kwa ujumla kuwa na shukrani kwa mazuri wanayofanyiwa na makundi yao, kuhama hakukatazwi, lakini sio kwa kukashfu au kuponda tu, kwani ndiko kunakodumaza muziki," alisema Choki.
Aliongeza kama sio kuwa na moyo wa kutaka muziki wa dansi usonge mbele na kusaidia vijana wengine wenye vipaji kupata riziki kupitia ajira ya sanaa hiyo, asingeanzisha na kuendesha bendi ya Extra Bongo na badala yake angekuwa mwanamuziki wa kujitegemea ili ale kuku kwa raha.
"Kwa jina na umaarufu nilionao ndani na nje ya nchi naweza kuendesha shughuli zangu za muziki kama solo artist, lakini naguswa na kupenda kusaidia wengine kutokana, ili kulifanya jina langu liendelee kutajwa katika mchango wa muziki huu," alisema.
Choki, alisema hata leo Mbaraka Mwinshehe na Marijab Rajab pamoja na kufa wanatajwa kwa sababu waliwasaidia wengi kupitia bendi zao hali ambayo anatamani naye iwe hivyo milele.

Dance Music Competition laiva

USAILI wa wasanii chipukizi wa muziki wa dansi watakaoshiriki shindano la kusaka nyota wapya wa muziki huo nchini, kupitia shindano la 'Dance Music Competation' unatarajiwa kuanza rasmi Desemba 20-21 kwenye ukumbi wa Afri Center, Ilala jijini Dar es Salaam.
Mratibu wa shindano hilo, Seleman Mathew alisema maandalizi ya mchakato huo umeshaanza kwa kuanza kutoa fomu za ushiriki kwa wanaopenda kushiriki mchuano huo kuzichangamkia kabla ya usaili huo utakaoendeshwa na majaji wanne.
Mathew aliwataja majaji hao kuwa ni wanamuziki wakongwe wa muziki huo nchini, Ally Choki wa Extra Bongo, Tshamanga Kalala Assosa wa Bana Marquiz, Nyota Waziri wa Kilimanjaro Band 'Wana Njenje' na Abdul Salvador 'Father Kidevu' wa Hisia Kali Band.
'Mchujo wa kusaka vijana kwa ajili ya shindano letu na nyota wapya wa muziki wa dansi utaanza rasmi Desemba 20-21 kwenye ukumbi wa Afri Center Ilala kuanzia saa 2 asubuhi hadi saa 11 jioni, na watakaopenya wataingia kwenye kinyang'anyiro hicho," alisema Mathew.
Alisema kinyang'anyiro cha shindano hilo kitaanza Januari 16 kwa washiriki kuingia kambini na kupigiwa kura hadi atakapopatikana mshindi katika fainali zitakazofanyika Machi 6 mwakani.
Mathew, beki za zamani wa timu za Simba, Yanga, Plisner na Ndovu-Arusha, alisema lenye lengo la shindano hilo ni kuibua wanamuziki wapya wa dansi na kuendeleza muziki huo nchini kuwabadili vijana wengi kuona hakuna muziki mwingine zaidi ya Bongofleva tu.
Alisema washiriki wanaotaka kushiriki wanapaswa kuwa katika kundi la kuanzia wasanii watano hadi saba wenye uwezo wa kuimba nyimbo za muziki wa dansi na kuongeza kwa wale ambao hawana makundi pia wanaruhusiwa muhimu wawe na uwezo katika muziki huo.
Alisema fomu za ushiriki wa shindano hilo zinapatikana kwenye ukumbi wa Afri Center kwa gharama ya Sh 3,000 na kuwataka wenye vipaji hivyo kuchangamkia nafasi hiyo, huku akiwataka wadhamini kujitokeza kuwapiga tafu kufanikisha shindano hilo la kwanza nchini kwa muziki huo.

Kanumba, apania uzinduzi wa Off Side DR Congo



NYOTA wa filamu nchini, Stephen Kanumba, ametamba kuwa uzinduzi wa kazi mpya aliyotoa pamoja na Vincent Kigosi 'Ray' iitwayo 'Off Side' utakaofanyika wiki ijayo nchini DR Kongo, utakuwa wa aina yake kutokana na jinsi walivyojiandaa kuwapa raha mashabiki wao nchini humo.
Uzinduzi wa filamu hiyo iliyowarejesha tena wawili hao pamoja tangu walipotoa Ophra miaka miwili iliyopita, unatarajiwa kufanyika kati ya Desemba 15-20 katika miji miwili ya nchi hiyo ya Goma na Bukavu.
Akizungumzia uzinduzi huo, Kanumba, alisema wamepania kufanya kweli ili kusuuza nyoyo za mashabiki wao lukuki waliopo katika nchini hiyo na Ukanda mzima wa Afrika Mashariki na Kati na pia kutaka kujitengenezea majina yao katika anga la kimataifa.
"Hii ni nafasi ambayo haipaswi kuichezea na ndio maana tunaenda kamili kuwapa raha mashabiki wetu wakati wa uzinduzi huo, ili kujitangaza kimataifa," alisema Kanumba.
Kanumba, atakayeambatana na washiriki vinara wa filamu hiyo, Ray, Irene Owoya, Aunty Ezekiel na mtoto Jennifa aliyecheza filamu za This is It na Uncle JJ, alisema maandalizi yao ya kwenda kufanya uzinduzi huo yamekamilika na kwamba wakati wowote wiki ijayo watatua nchini humo kufanya mambo.
"Tunaendelea vema na maandalizi ya shughuli hiyo na tunawasihi wakazi wa Kongo wakae mkao wa kula kupata klitu roho inapenda kqwani tutafanya onyesho la jukwaani la dakika kama 30 ili kukonga nyoyo zao," alisema.
Katika filamu hiyo ya kimapenzi, Kanumba amecheza kama kijana maskini anayelazimishwa mapenzi na mke wa tajiri kitu ambacho kinamletea kizaazaa cha aina yake.
Kanumba alisema mara baada ya uzinduzi huo wa Kongo wataenda Burundi kabla ya kurejea nchini kwa ajili ya kuitoa hadharani kupitia kampuni ya Steps Entertainment ambayo ndiyo yenye kibali cha kuisambaza kazi hiyo.

Huba wana Bangkok Deal

BAADA ya kutamba na filamu ya Hazina, kampuni ya Huba, ipo mbioni kufyatua kazi mpya iitwayo Bangkok Deal ambayo imeshirikisha nyota kadhaa wa fani hiyo nchini.
Mkurugenzi wa kampuni hiyo, Husseni Ramadhan 'Swagger' aliiambia NIPASHE jana kuwa, wapo hatua ya mwisho ya upigaji wa picha za filamu hiyo ambayo ameshirikishwa mkali Charles Magali.
Swagger alisema ndani ya filamu hiyo mbali na Mzee Magali, pia kuna wachina walioshirikishwa katika kuipa ladha kulingana na simulizi ya kazi hiyo aliyodai italeta mapinduzi ya fani hiyo nchini.
"Walioishuhudia Hazina na kazi nyingine tulizofyatua kupitia kampuni hii ni chamtoto tu, Bangkok Deal ni kazi isiyo na maelezo, tuombe tumalize na kuiingiza sokoni mashabiki ndio watakaijaji," alisema.
Swagger, alisema pamoja na kuendelea kurekodi filamu hiyo, pia kampuni hiyo tayari imeshaanza maandalizi ya kazi nyingine itayofahamika kwa jina la Hofu Tupu, aliyopanga kuitoa mapema mwakani.
Swagger aliyekuwa msanii wa muziki wa kizazi kipya kupitia makundi ya 2 Wise Boy na The Crime Busters, alisema ndani ya filamu hizo wasanii wakali na wanaotamba katika fani hiyo wameshirikishwa.