STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, April 29, 2014

UEFA yazitia hatiani Man City, PSG

KLABU za Manchester City ya Uingereza na Paris Saint-Germain ya Ufaransa watakabiliwa na adhabu baada ya kukiuka maadili ya sheria ya matumizi ya fedha ya Shirikisho la Soka barani Ulaya-UEFA. 
Mbali na hao vilabu vingine vipatavyo 20 vinaaminika kukutwa na hatia ya kuvunja sheria hiyo. 
UEFA itatoa ofa maalumu kwa vilabu hivyo vilivyokiuka sheria hiyo kuelekea katika mkutano wao utakaofanyika Alhamisi. 
Adhabu kubwa ambayo ni timu husika kuenguliwa katika michuano ya Ulaya haitarajiwi kuwepo ingawa pia hawakuweka wazi ni adhabu zipi zitaazotolewa kwa timu hizo.

Rais wa Brazil amuunga mkono Dani Alves Hispania

Dani Alves aliebaguliwa Hispania na shabiki wa Villarreal
Rais wa Brazil  Dilma akiwa na Rais wa FIFA
RAIS Dilma Rousseff, amesifu kitendo cha mchezaji wa kimataifa wa Brazil, na Barcelona Dani Alves kutokana na tukio la ubaguzi wa rangi wakati wa mechi ya ligi kuu ya Uhispania, La Liga kati ya Barcelona na Villareal .
Mchezaji huyo wa Barcelona aliokota ndizi aliyokuwa ametupiwa na kuila kabla ya kuitupa na kuendelea na mchezo.
Bi Rousseff aliandika katika mtandao wake wa twitter kuwa Dani Alves alionyesha ujasiri wa kukabiliana na ubaguzi wa rangi katika kandanda na kuwa ni tukio la kuigwa .
Klabu ya Villarreal inasema kuwa imempiga marufuku mwanaume ambaye alitupa ndizi hiyo uwanjani na kuwa hatohudhuria mechi zote za nyumbani za klabu hiyo maishani.
Mamia ya watu na wachezaji maarufu duniani wameonyesha upendo wao kwa mchezaji huyo kwa kuweka picha zao kwenye mitandao wa kijamii wakila ndizi.
Mchezaji wa Manchester City Sergio Aguero alipachika picha akila ndizi sawa na nyota ya soka ya wanawake Marta .
Wengine ni Luiz Suarez wa Liverpool,Oscar, David Luiz na Willian wote wa Chelsea .
Rais wa Fifa sepp Blatter ameongezea sauti yake katika tukio la hivi punde akisema ni vibaya kwa dhulma hizo kuendelea katika karne hii.
BBC

Elias Maguli ajinadi Simba, Yanga, Azam

Elias Maguli
MSHAMBULIAJI nyota wa Ruvu Shooting, Elias Maguli amesema yupo tayari kutua klabu yoyote kati ya Simba, Yanga au Azam, iwapo ataridhishwa na dau atakalowekewa mezani na klabu hizo.
Maguli aliyeshika nafasi ya pili kwa ufungaji sambamba na Kipre Tchjetche na Mrisho Ngassa, wakiwa nyuma ya Amissi Tambwe aliyeibuka Mfungaji Bora, alisema haoni tatizo kuihama Ruvu Shooting kama kuna klabu inayomhitaji.
Alisema, ingawa mpaka sasa hakuna timu yoyote iliyomfuata kumshawishi kujiunga nayo kwa msimu ujao, lakini amekuwa akisoma na kusikia tetesi tu kuwa Simba inamnyemelea na kusema milango i wazi kwao kama wanamtaka.
Maguli, alisema siyo Simba tu bali hata kama ni Yanga, Azam au Mbeya City inamhitaji yupo tayari kujiunga nayo mradi taratibu zifuatwe na masilahi yawe ya kuridhisha kwa sababu maisha yake yanategemea soka kama ajira.
"Nisiwe muongo zijafuatwa na klabu yoyote mpaka sasa, lakini nasikia tu tetesi za kuhitaji na moja ya klabu kubwa nchini, ila mimi nategemea soka klabu yoyote iliyoridhishwa nami milango i wazi waje tuzungumze," alisema.
Kuhusu kushindwa kuendelea na kasi ya ufungaji kama ilivyokuwa kwenye msimu wa kwanza, Maguli alisema matatizo aliyokuwa nayo kwenye duru la pili ikiwamo kuuguliwa na mama yake na sakata lake la kutimka umangani kusaka soka la kulipwa lilichangia kumfanya aachwe mbali na Tambwe.
Maguli aliyekuwa akishika nafasi ya pili nyuma ya Tambwe katika duru la kwanza wakitofautiana bao moja, Tambwe akiwa na 10 yeye akiwa na 9 alijikuta akiachwa mbali na mpinzani wake huyo aliyefunga bao 19 huku yeye na wenzake wawili wakimaliza msimu na mabao 13 tu.
Aidha Maguli amesema anamshukuru Mungu kwa kuweza kuitwa kwenye kikosi cha timu ya taifa, chini ya kocha mpya kutoka Uholanzi, Mart Nooij, akidai ni furaha kwake na kuahidi kutomuangusha.
"Namshukuru Mungu, nilikuwa likizo nyumbani Mara na sasa naelekea Mbeya kwenye kambi, nimefurahi sana kocha mpya kunijumuisha kikosini.

Muumin & Double M Sound kujitambulisha Kigoma

Muumin
BAADA ya kukonga nyoyo za mashabiki wa mikoa ya Shinyanga na Kagera wakati wa sikukuu ya Pasaka, bendi iliyorejeshwa upya ya Double M Sound mwezi ujao inatarajiwa kwenda kujitambulisha kwa wakazi wa Kigoma.
Mkurugenzi wa bendi hiyo, Prince Mwinjuma Muumini aliiambia MICHARAZO kuwa, wanatarajia kwenda kuitambulisha bendi yao katika miji ya Kibondo na Kasulu iliyopo mkoani Kigoma.
Muumin alisema onyesho la kwanza mkoani humo watalifanya Mei 9 mjini Kibondo kabla ya siku inayofuata watahamia Kasulu kabla ya kurejea maskani kwao Kahama-Shinyanga kwa ajili ya kufanya mazoezi za uzinduzi rasmi.
"Tunashukuru tumerejea salama kutoka kwenye maonyesho yetu wakati wa sikukuu ya Pasaka kwa kutambulisha bendi eneo la Kakola, Ushirombo, Ruzewe, Ngara na Katoro. Kwa sasa tupo kambini mjini Kahama kujiandaa na ziara ya mkoani Kigoma mapema mwezi ujao," alisema Muumin.
Muumin aliongeza kuwa uongozi wao unajipanga kufanya uzinduzi na onyesho la kwanza kuitambulisha na kuizindua Double M Sound mjini Kahama mwishoni mwa mwezi ujao.
"Pamoja na watu kujua Double M Sound ipo Kahama, lakini hawajawahi kuiona hadharani kwa sababu tunapanga kuizindua rasmi mwishoni mwa Mei na kisha ndipo tuanze kuifanya maonyesho mjini hapa," alisema Muumin.
Double M Sound iliyowahi kutamba na nyimbo mbalimbali ilisambaratika mara baada ya uzinduzi wa albamu yao ya Titanic mwaka 2004 na Muumin ameamua kuifufua upya na kujichimbia Kahama kama maskani yake kwa sasa.

Kamanda Kova afunguka vifo vya watoto Bwawa la Kuogolea Dar

Picha haihusiani na habari, ila watoto wakifurahia kuoga kwenye bwawa la kuogolea kama wanavyuoonekana
KAMANDA wa Polisi Kanda Maalum  Suleiman Kova amefafanua juu ya taarifa ya vifo vya watoto watatu
waliofariki wakati wakiongolea kwenye bwawa la hoteli.
Kamanda Kova alisema April 27  kulitokea vifo vya watoto 3 ambao walikua na birthday party nyumbani lakini baada ya kukamilika kwa taratibu za party ya nyumbani waliamua kuimalizia party hiyo hotel ya Landmark,walipofika walienda kuogelea kwenye swimming pool ya watoto lakini baadae watoto hao walitoka kwenye pool ile ya watoto wakaingia kwenye pool ya wakubwa na kwa bahati mbaya waliingia sehemu yenye kina kirefu.
Watoto wenzao walipoona wenzao wanazama walianza kuwavuta kuwatoa nje lakini hali zao tayari zilikua mbaya, mmoja wapo hali yake ilikua kidogo afadhari lakini kwa bahati mbaya nayeye alifia hospital wakati akipatiwa matibabu katika hospitali ya Masana na kufanya Idadi ya watoto waliofariki kuwa 3 majina yao ni Janet Zacharia, Eva na Ndimbuni.
Kamanda Kova amesema; "’Kusema kweli sio mara ya kwanza kutokea, mara nyingi vifo vya watoto vinatokana na uangalifu au uzembe kutoka kwa wale wanaotakiwa kuwaangalia hao watoto wao, hizi hotel zote zenye swimming pool lile eneo la kuogelewa basi wasiruhusiwe watoto wadogo kuogelea au kuwe na mtu ambaye anajua kuogelea au kuokoa ambaye yupo pale’
‘Unajua watoto wana tabia ya kuigana mmoja akiingia akiogelea pengine anafahamu kidogo wengine wote wanafata mkumbo wanaona wanaweza,sisi kama jeshi la Polisi tumeamua hili kosa la uzembe kusababaisha kifo kisheria mtu anaweza kushtakiwa kwa kuzembea kwa kutochukua tahadhari mpaka watoto kama wale ambao hawana hatia uwezo wao mdogo wa kufikiri au kuijiokoa’
‘Tunafatilia kwa umakini lakini jukumu la kufatilia maisha ya watoto ni la wazazi mia kwa mia wasipofanya hivi wakiwa hawapo makini matokeo yake ni haya watoto 3 wamefariki,tunaendelea na uchunguzi na baadae tutatoa taarifa kamili’.

Ubingwa mweupe kwa Juventus, yaifumua Sassuolo 3-1

Wachezaji wa tatu wa Juve (jezi za njano) wakiwania mpiura na beki wa Sassuolo walipoikandika timu hiyo mabao 3-1 ugenini
JUVENTUS imebakisha mechi moja tu kutangazwa tena kuwa mabingwa wa Italia baada ya usiku wa kuamkia leo kupata ushindi mnono wa mabao 3-1 ugenini dhidi ya Sassuolo katika mfululizo wa Ligi Kuu ya nchini hiyo Seria A.
Mabingwa hao watetezi ambao Alhamis hii watakuwa nyumbani kwao kuwakaribisha Benfica ya Ureno kwenye mechi ya marudiano ya Nusu Fainali ya Ligi Ndoigo ya Ulaya (UEFA Europa League) ili kujaribu kupindua matokeo ya kipigo cha mabao 2-1, ilishtukiza kwa bao la mapema la dakika 9 la wenyeji liliwekwa kimiani na Simone Zaza.
Hata hivyo wakati wakitafakari jinsi ya kulirudisha bao hilo wenyeji hao waliwasaidia  kulisawazisha wenyewe baada ya Alessandro
Longhi kujifunga dakika ya 34.
Juventus maarufu kama kibibi kizee cha turin, iliongeza bao la pili katika dakika ya     58 kupitia Claudio Marchisio kabla ya Llorente kufunga bao la tatu katika dakika ya 76 na kuifanya timu hiyo kufikisha pointi 93, nane zaidi na ilizonazo wanaoshikilia nafasi ya pili Roma wenye pointi 85 na kila timu ikiwa imesaliwa na mechi tatu kabla ya kufunga msimu huu.

Arsenal yapumua, yaifumua Newcastle United 3-0

KLABU ya soka ya Arsenal imefufua matumaini yake ya kuwepo kwenye Top 4 na kushiriki moja kwa moja Ligi ya Mabingwa ya Ulaya bada ya usiku wa kuamkia kuitandika Newcastle United kwa mabao 3-0 kwenye uwanja wa wa Emirates, mjini London.
Mabao ya Laurent Koscielny katika dakika ya 26, Mesut Ozil aliyefunga dakika ya 42 na jingine la Olivier Giroud yaliweka Arsenal pazuri ikiwa imepata ushindi wa tatu mfululizo na kuzidi kuikimbia Everton wanaoifukuzia nafasi yao.
Arsenal waliokuwa vinara wa ligi ya England kwa muda mrefu kabla ya kuporomoka, itasubiri kujua hatma yake ya kutwaa nafasi ya nne baada ya pambano la Everton na Manchester City mwishoni mwa wiki, kama Everton itateleza kama ilivyofanya katika mechi zake zilizopita basi vijana wa Gunners watakuwa wamejihakikisha kutwaa nafasi hiyo na kucheza ligi ya mabingwa moja kwa moja.
Vijana hao wa Arsene Wenger wamekusanya jumla ya pointi 73 nne zaidi na iliyonazo Everton waliopo nyuma yao na pointi 69.

Ajali tena! Zaidi ya 15 wafariki ajalini usiku wa kuamkia leo Singida

Picha haihusiani na habari hii, lakini ni miongoni mwa mabasi ya Sumry lililowahi kupata ajali siku za nyuma.
WATU 13 akiwemo askari wa kikosi cha usalama barabarani (Trafiki) wamepoteza maisha baada ya kugongwa na basi la kampuni ya Sumry lililokuwa likitoka Kigoma kwenda Dar katika kijiji cha Ikungi mkoani Singida usiku wa kuamkia leo.
Ajali hiyo ilitokea baada ya ajali ya kwanza iliyolihusisha lori lililomgonga mwendesha baiskeli aliyepoteza maisha papo hapo na wakati wananchi wakiwa wamekusanyika eneo hilo la ajali huku trafiki akiendelea kupima ajali hiyo, lilitokea basi la kampuni ya Sumry na kuwagonga watu hao pamoja na trafiki na kupelekea jumla ya watu 14 kupoteza maisha eneo hilo.
Basi hilo lililokuwa likitokea Kigoma kwenda Dar halikuweza kusimama eneo hilo mpaka dereva wake alipokwenda kujisalimisha kituo cha polisi Ikungi, Singida. 
Miili 14 ya waliopoteza maisha katika ajali hiyo imehifadhiwa katika Hospitali ya Rufaa mkoani Singida pamoja na majeruhi wawili waliopelekwa hospitalini hapo.
MUNGU AZILAZE ROHO ZA MAREHEMU MAHALI PEMA PEPONI. AMEN!

Ronaldo, Bale, Benzama kuanza pamoja 'kuiua' Bayern, Klopp atabiri

Bale na Ronaldo
WAKATI kocha hasimu wa Bayern Munich, Jurgen Klopp wa Borussia Dortmund akiwapa nafasi kubwa mabingwa watetezi hao kutinga fainali za Ligi ya Mabingwa Ulaya, miamba wa soka wa Hispania, Real Madrid timu yenye mafanikio zaidi katika historia ya michuani hiyo  wakitwaa taji hilo mara tisa wamepania safari hii kuondokana na mzimu wa kulikosa kila mara kwa miaka 12  sasa.
Madrid imeangukia katika hatua ya nusu fainali katika michuano yote mitatu iliyopita, mara mbili ikitolewa dhidi ya timu za Ujerumani.
Borussia Dortmund waliwafunga jumla ya magoli 4-3 katika nusu fainali ya mwaka jana wakati Bayern waliwatoa kwa 'matuta' katika nusu fainali ya msimu wa 2011-12 lakini wanaingia katika mechi ya leo ya marudiano kwenye Uwanja wa Allianz Arena kwa ushindi wa 1-0, kufuatia kiwango cha juu walichoonyesha katika mechi yao ya awali mjini Madrid.
Karim Benzema alifunga goli pekee la mechi hiyo, kuipa timu ya kocha Carlo Ancelotti uongozi, lakini, licha ya hilo, watatakiwa kuwachunga Bayern ambao wamekuwa na mafanikio chini ya kocha wa zamani wa Barcelona, Pep Guardiola.
Mabingwa hao wa Bundesliga wanafukuzia kutwaa makombe matano chini Guardiola baada ya kutwaa Uefa Super Cup na Kombe la Dunia la Klabu, huku pia wakiwasubiri Borussia Dortmund katika fainali ya Kombe la 'FA' la Ujerumani la DFB-Pokal.
Bayern wamepoteza mechi nne tu nyumbani tangu mwanzo wa msimu huu, huku Manchester City na Arsenal zikiwa ni timu pekee za Ligi ya Klabu Bingwa Ulaya zilizoonja mafanikio kwenye Uwanja wa Allianz Arena katika kipindi hicho, lakini Ancelotti amesisitiza timu yake itakwenda kwenye mechi hiyo ikijiamini wakati wakidhamiria kutwaa makombe matatu katika msimu wa kwanza chini ya kocha huyo Muitalia.
"Nina imani na wachezaji na nadhani kila mmoja anapaswa kuwa hivyo pia," aliuambia mkutano na waandishi wa habari wa Hispania. "Mpango wetu mjini Munich ni kufunga, kuliko kujilinda."
Ancelotti alibainisha kuwa washambuliaji watatu wa Madrid, Benzema, Cristiano Ronaldo na Gareth Bale, wote wataanza mjini Munich.
Alvaro Arbeloa, Jese Rodriguez na Sami Khedira (wote goti) ndiyo wachezaji pekee watakaokosa Real.
Beki Rafinha amerejea kwa Bayern baada ya kutumikia adhabu ya kadi katika mechi ya ligi wikiendi lakini, wakati Thiago amerejea mazoezini, Holger Badstuber (goti), Xherdan Shaqiri (paja) na Tom Starke (kiwiko) wote bado wako nje ya uwanja.
Bayern wamekuwa wakitajwa kama timu inayopewa nafasi kubwa zaidi ya kutwaa taji hilo kwa muda wote wa michuano na Guardiola anaamini kwamba mabingwa hara tano wa Ulaya wanaweza kupindua matokeo ya mechi yao ya awali.
"Ninaiamini kwa asilimia 100 timu yangu," Mcatalunya huyo aliiambia tovuti rasmi ya klabu hiyo ya mjini Munich. "Tunaweza kama tutafanya kazi pamoja."
Mshambuliaji wa Bayern, Mario Mandzukic na nyota wa Madrid, Sergio Ramos, Xabi Alonso na Asier Illarramendi watakosa fainali kama watapigwa kadi za njano katika mechi hiyo ya leo.
Licha ya kuwa bado na nafasi ya kutwaa taji hilo, staili ya uchezaji inayofundishwa na Guardiola imezidi kupoteza umaarufu na haiwavutii wakosoaji wa Bayern.
"Kumiliki mpira hakuna maana yoyote pale mpinzani wako anapotengeneza nafasi bora zaidi yako. Tuna bahati walifunga goli moja tu," alisema rais wa heshima wa Bayern, Franz Beckenbauer katika ukosoaji wake mpya alioutoa karibuni dhidi ya staili ya kucheza ya Guadiola ya tiki-taka la Kijerumani.
Katika hatua nyingine meneja wa klabu ya Borussia Dortmund, Jurgen Klopp ameipa nafasi Bayern Munich kugeuza matokeo ya kufungwa bao 1-0 na Real Madrid katika mchezo wa kwanza wa nusu fainali ya michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.
Bao la Karim Benzema lilitenganisha timu hizo mbili katika mchezo huo uliofanyika wiki iliyopita katika Uwanja wa Santiago Bernabeu baada ya Madrid kucheza mchezo wa tahadhari kubwa.
Hata hivyo, Klopp ambaye timu yake ilienguliwa na Madrid katika mzunguko wa mwisho anaamini mahasimu wao Bayern watashinda mchezo huo.
Klopp amesema bado anashawishika kuamini kuwa Bayern wanaweza kushinda hususani kwa mchezo maridadi waliouonyesha mara ya kwanza pamoja na kufungwa. Bayern na Madrid zinatarajiwa kukwaana kesho katika mchezo wa marudiano kutafuta nafasi ya kucheza fainali ya michuano hiyo itakayofanyika jijini Lisbon, Ureno.

Chelsea ilipaki mabasi mawili Anfield, kocha Liver alia

Makocha wanaofukuzana kwenye mbio za ubingwa wa Ligi Kuu ya England
MENEJA wa klabu ya Liverpool, Brendan Rodgers amemtuhumu meneja wa Chelsea Jose Mourinho kwa kupaki mabasi mawili na kuipa ushindi wa mabao 2-0 katika Uwanja wa Anfield. 
Katika mchezo huo mabao ya Chelsea yalifungwa na Demba Ba aliyetumia vyema makosa ya nahodha Steven Gerrard kipindi cha kwanza na lingine la Willian katika majeruhi. 
Kocha Rodgers amesema wapinzani wao walipaki mabasi mawili langoni mwao akimaanisha walikuwa wakizuia kipindi chote cha mchezo huo hivyo kuwapa wakati mgumu kupenya ngome yao ingawa walijitahidi kujaribu. 
Rodgers amesema walijitahidi kushinda mchezo huo lakini walishindwa kupenya ngome ya wapinzani wao ambayo ilikuwa ikilindwa vizuri. 
Pamoja na ushindi huyo Mourinho bado ameendelea kudai kuwa hawana nafasi ya kunyakuwa ubingwa wa Ligi Kuu na kudai kuwa mbio hizo wamewaachia Manchester City na Liverpool. 
Mreno huyo amesema kitu cha msingi alichokuwa akihitaji ni kupata alama tatu hizo muhimu ambazo zitawasaidia kujihakikishia nafasi tatu katika msimamo wa ligi hivyo kufuzu moja kwa moja bila kucheza mechi za mtoano katika michuano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya msimu ujao.
Timu hiyo ya Mourinho kesho itakuwa na kibarua kizito mbele ya Atletico Madrid katika mechi ya marudiano ya Ligi ya Mabingwa Ulaya hatua ya nusu fainali.
Katika mchezo wa kwanza timu hizo zilitoka suluhu bila kufungana mjini Madrid na hivyo Chelsea inapatakiwa kuhakisha inapata ushindi au sare isiyokuwa na mabao iwapo inataka kufuzu hata kwa mikwaju ya penati.

Neymar akemea ubaguzi wa rangi Hispania

MSHAMBULIAJI wa Barcelona, Neymar amesema atapambana na ubaguzi wa rangi baada ya mchezaji mwenzake Dani Alves kurushiwa ndizi wakati wa mechi yao waliyoshinda 3-2 ugenini dhidi ya Villarreal juzi.
"Sisi sote tuko sawa, sisi sote ni nyani, sema hapana kwa ubaguzi wa rangi," Neymar aliandika katika ukurasa wa mtandao wake wa kijamii, akiweka 'hashtag' #SisiSoteNiNyani.
"Ni aibu kwamba hadi mwaka 2014 bado kuna matendo kama haya. Ni wakati sasa wa watu kuinua sauti zao kukemea. Njia yangu ya kusapoti ni kufanya alichofanya Dani Alves.
"Kama nawe unasapoti kampeni hii, jipige picha ukila ndizi nakisha tutaitumia katika kupinga ubaguzi huu."

Del Piero atundika daluga zake

MCHEZAJI mkongwe Alessandro Del Piero ameamua kutundika daruga kuitumikia klabu ya Sydney FC lakini anaweza kurejea kwa shughuli nyingine. 
Mshambuliaji huyo wa zamani wa Juventus amekuwa akihusishwa na tetesi za kuwa kocha katika klabu hiyo inayoshiriki Ligi Kuu nchini Australia baada ya Frank Farina kutimuliwa. 
Del Piero, 39 na klabu hiyo wanataka kuendelea na mahusiano lakini haijabainika wazi ni uhusiano wa namna gani. 
Akiwa amefunga jumla ya mabao 24 yakimfanya kuwa mfungaji bora wa klabu katika misimu yote miwili aliyoitumikia, mkali huyo aliandika ujumbe kushukuru na kuaga kupitia mtandao wake. 
Del Piero amesema katika ujumbe huo ule wakati umewadia safari yake akiwa na Sydney FC inakaribia ukingoni ingawa inasikitisha lakini amekuwa na muda mzuri katika kipindi chote alichoitumikia.

Haya ndiyo makundi ya AFCON 2015

Kocha Steven Keshi akiwa amebebwa baada ya kuipa Nigeria taji la AFCON 2013 nchini Afrika Kusini

WAKATI Tanzania itaanzia katika hatua ya awali ya michuano ya kufuzu kwa fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON) 2015, mabingwa watetezi Nigeria watawakabili Afrika Kusini na Sudan katika kundi lao la kuwania kutinga katika fainali hizo zitakazofanyika Morocco.
Kikosi cha kocha Stephen Keshi kilitwaa kombe hilo kwa mara ya tatu mwaka 2013 kwa ushindi wa 1-0 dhidi ya Burkina Faso na watakutana na wenyeji wa mwaka huo, Afrika Kusini, katika kuwania kufuzu kwa fainali za 2015.
Timu hizo mbili zinaungana na Sudan katika Kundi A, wakati timu nafasi moja ya mwisho ya kufuzu kuingia katika kundi hilo kutokea katika hatua ya awali itagombewa na timu za Namibia, Congo, Libya au Rwanda.
Burkina Faso watakabiliana na Angola na Gabon katika Kundi C, na nafasi moja ya mwisho itagombewa na timu za Liberia, Lesotho, Kenya na Comoro.
Ivory Coast na Cameroon, ambao wataungana na Nigeria katika fainali za Kombe la Dunia nchini Brazil, wamepangwa pamoja katika Kundi D la kuwania kufuzu pamoja na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo.
Ghana - taifa jingine litakaloenda kwenye Kombe la Dunia - litakabiliana na mahasimu wao wa Afrika Magharibi, Togo katika Kundi  E, wakati Algeria, wawakilishi wengine wa Afrika nchini Brazil, watakuwa na mechi dhidi ya Mali na Ethiopia katika Kundi B.
Mabingwa mara saba Misri watawavaa Tunisia na Senegal katikaKundi G.

Makundi yote ya kufuzu kwa fainali za Mataifa ya Afrika 2015 kwa ujumla:

Kundi A: Nigeria, Afrika Kusini, Sudan na moja kati ya Namibia, Congo, Libya na Rwanda

Kundi B: Mali, Algeria, Ethiopia na moja kati ya Sao Tome na Principe, Benin, Malawi na Chad

Kundi C: Burkina Faso, Angola, Gabon na moja kati ya Liberia, Lesotho, Kenya na Comoros

Kundi D: Ivory Coast, Cameroon, DR Congo na moja kati ya Swaziland, Sierra Leone, Gambia na Shelisheli

Kundi E: Ghana, Togo, Guinea na moja kati ya Madagascar, Uganda, Mauritania na Equatorial Guinea

Kundi F: Zambia, Cape Verde, Niger na moja kati ya Tanzania, Zimbabwe, Msumbiji na Sudan Kusini

Kundi G: Tunisia, Misri, Senegal na moja kati ya Burundi, Botswana, Jamhuri ya Afrika ya Kati na Guinea Bissau.