STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, April 8, 2015

YANGA NJIA NYEUPEE, YAMZIBA MDOMO JULIO KWA 8-0

https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEinj8FsP_aDKXr8JLCGkYb7oGiMFKfaPcj8820SGepcKAM55k0Uq2GxQrLCnguU3GwSrYripfOY8Ta3XUFVzdVLqv_dEEqHfLLmZvc13ggQClezx2G2o24dgIxNCG46MD36j1TlFROkrZ4/s1600/DSC_7835.JPGNJIA nyeupe kwa Yanga kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu baada ya jioni hii kugawa dozi ya maana kwa Coastal Union, huku watetezi Azam wakilazimishwa na Mbeya City.
Yanga ikiwa kwenye uwanja wa Taifa Dar es Salaam imemfunga mdomo kocha anayechinga sana, Jamhuri Kihwelu 'Julio' baada ya kupata ushindi wa mabao 8-0, huku Amissi Tambwe akifunga mabao manne na kurejea rekodi aliyoiweka msimu uliopita wakati akiwa Simba. Kipigo hicho kimekuja katika Ligi Kuu tangu Yanga ilipoifanyia Kagera Sugar mwaka 1998 ambapo Edibily Lunyamila alifunga pekee yake mabao matano.


Mabao mengi ya Yanga katika mchezo huo yalifungwa na Simon Msuva aliyefunga mawili, Salum Telela na Kpah Sherman aliyefunga bao lake la kwanza akiwa na Yanga tangu ajiunge nayo miezi minne iliyopita.
Kwa ushindi huo Yanga imefikisha jumla ya pointi 43 na mabao 36 ya kufunga na kuwaacha Azam kwa pointi sita baada ya watetezi hao kulazimishwa sare ya 1-1 na Mbeya City kwenye uwanja wa Chamazi.
Kwa kufunga mabao manne, Tambwe amefikisha mabao 9 msimu huu katika Ligi Kuu wakati Msuva amezidi kumuacha mbali Didier Kavumbagu wa Azam kwa kufikisha mabao 13 dhidi ya 10 ya mpinzani wake huyo ambaye leo hakushuka dimbani katika pambano la Mbeya City.

Liverpool yamnyatia Alexandre Lecazette

http://cdn.sports.fr/images/media/football/ligue-1/scans/lyon-domine-lille-grace-a-un-triple-de-lacazette/alexandre-lacazette/12966789-1-fre-FR/Alexandre-Lacazette.jpgKLABU ya Liverpool iko tayari kuungana na vilabu vingine vya Ligi Kuu kumfukuzia nyota wa Lyon ya Ufaransa Alexandre Lacazette katika kipindi cha majira ya kiangazi. 
Wakongwe wa Ujerumani Burussia Dortmund pia wamekuwa wakifuatilia mwenendo wake wakati Manchester City nao wamekuwa wakimkodolea macho nyota huyo mwenye umri wa miaka 23 toka Novemba mwaka jana. Klabu za Chelsea, Arsenal na Tottenham Hotspurs nazo pia zimeshatuma maskauti wao kuangalia mwenendo wa mchezaji huo huku Newcastle wakiendelea kumfuatilia pamoja na kushindwa kumsajili hapo nyuma. 
Safari hii Liverpool wamejipanga kuimarisha safu yao ya ushambuliaji mapema yasije kuwakuta kama walivyomuuza Luis Suarez kwenda Barcelona na kulazimika kumnunua Mario Balotelli ambaye hata hivyo amekuwa hana msaada sana msimu huu. Baada ya Balotelli kushindwa kung’aa na Daniel Sturridge akiendelea kusumbuliwa na majeruhi huku kukiwa hakuna uhakika wa kuendelea kuwa na Raheem Sterling msimu ujao, Brendan Rodgers anahitaji kupata chaguo zaidi katika kikosi chake.

AFCON 2017 KAZI KWELI, STARS WAPEWA MISRI, NIGERIA

http://www.fullshangweblog.com/wp-content/uploads/2014/07/TAIFA1.jpg
Taifa Stars
Kombe la AFCON
SAFARI ya Taifa Stars ya Tanzania katika mchakato wa kufuzu Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (Afcon) zitakazofanyika nchini Gabon mwaka 2017, inaonekana kuwa ngumu. Hii ni baada ya  Shirikisho la Soka Afrika (Caf) kuipanga kundi moja la G pamoja na vigogo.
Kwa mujibu wa droo iliyofanyika jana jijini Cairo, Misri, Tanzania imepangwa kundi moja na mabingwa wa kihistoria wa michuano hiyo, Misri, pia wakipewa mabingwa wa mwaka jana, Nigeria na Chad. Huku Morocco, Tunisia zilizokuwa zimefungiwa na CAF nazo zikijumuishwa katika droo hiyo.
Timu 16 zitakazopenya katika hatua hiyo ya makundi ndiyo watakaoenda Gabon kusaka ubingwa ambao kwa sasa unashikiliwa na Ivory Coast waliotwaa mapema mwaka huu kwa kuilaza Ghana.
Tanzania kwa mara ya kwanza na mwisho kufuzu fainali hizo ilikuwa mwaka 1980 wakati michuano hiyo ilipofanyika nchini Nigeria na kwa miaka zaidi ya 30 imekuwa ikisota kusaka nafasi ya kushiriki tena bila mafanikio.
Makundi ya michuano hiyo ambayo awali ilikuwa iandaliwe na Libya kabla ya hali ya machafuko ya kisiasa kuifanya ijitoe ni kama yafuatavyo;
Kundi A: Tunisia, Togo, Liberia, Djibouti
Kundi B: Madagascar, DRC, Angola, CAR
Kundi C: Mali, Equatorial Guinea, Benin, South Sudan
Kundi D: Burkina Faso, Uganda, Botswana, Comoros
Kundi E: Zambia, Congo, Kenya, Guinea Bissau
Kundi F: Cape Verde, Morocco, Libya, Sao Tome
Kundi G: Nigeria, Egypt, Tanzania, Chad
Kundi H: Ghana, Mozambique, Rwanda, Mauritius
Kundi I: Cote d'Ivoire, Sudan, Sierra Leone, Gabon
Kundi J: Algeria, Ethiopia, Lesotho, Seychelles
Kundi K: Senegal, Niger, Nambia, Burundi
Kundi L: Guinea, Malawi, Zimbabwe, Swaziland
Kundi M: Cameroon, South Africa, Gambia, Mauritania

Ally Choki, Super Nyamwela warudi Twanga Pepeta

Luiza Mbutu akiwatambulisha Ally Choki na Super Nyamwela leo jijini juu ya kurudi kwao Twanga pepeta
MUIMBAJI nyota wa muziki wa dansi nchini, Ally Choki ametangazwa kurudi African Stars 'Twanga Pepeta' ikiwa ni miezi michache tangu bendi yake ya Extra Bongo kusambaratika.
Kiongozi wa bendi hiyo, Luiza Mbutu alimtangaza Choki na Super Nyamwela kurudi tena Twanga leo mbele ya wanahabari ikiwa ni miaka michache tangu alipoihama bendi hiyo kwenda kuanzisha bend iliyokufa ya Extra Bongo.
"Tumeamua kuiboresha bendi yetu ya mama ya Twanga Pepeta na huu ni uamuzi wangu binafsi sikushurutishwa na mtu yeyote ieleweke hivyo," alisema Choki katika utambulisho huo uliofanyika Kinondoni jijini Dar es Salaam.
“Twanga ni bendi yangu, hakuna ubishi ni bendi ambayo nimeitumikia kwa miaka mingi sana hivyo kwa kuanzia nitatoka na kibao kiitwacho ‘Kichwa Chini’ ambacho nitaimba na Luiza ukitoa somo kwa wanaume,” alisema Choki .
Aliongeza tayari kuna nyimbo mbili zilizo tayari kufyatuliwa na kuzitaja kuwa ni ‘Usiyaogope  Maisha’ na ‘No Discuss’.
Choki alidokeza pia kuwa hana mpango wa kuasisi tena bendi kwa sababu hataki ‘stress’ kwani kumiliki bendi ni pasua kichwa.
Naye Nyamwela alisema amerudi nyumbani na yupo tayari kwa ajili ya kuchapa kazi na Kiongozi wa Twanga Pepeta, Luiza Mbutu alisema wanatarajia kuandaa onyesho maalum la utambulisho wa wakali hao Aprili 18, jijini Dar es Salaam

TFF yampongeza Tenga, kuziona Twiga, Shepolopolo buku 2

http://shaffihdauda.co.tz/wp-content/uploads/2015/04/malinzi1.jpg
Rais wa TFF, Jamal Malinzi
RAIS wa Shirikisho la Mpira wa Miguu nchini TFF Jamal Malinzi, amempongeza Bw Leodgar Tenga kwa kuchaguliwa kuendelea kuwa mjumbe wa Kamati ya Utendaji ya Shirikisho la Mpira wa Miguu barani Afrika (CAF).
Aidha Rais Malinzi ametuma salamu za pongezi kwa wajumbe  waliochaguliwa kuwa wajumbe wapya wa Shirikisho la Mpira wa Miguu baranai Afrika (CAF) na Shirikisho la Mpira wa Miguu Duniani FIFA.
Katika salamu hizo na nakala zake kutumwa kwa Rais wa CAF Bw. Issa Haytou na Rais wa FIFA Bw. Blatter, Malinzi amewatakia kila la kheri katika majukumu hayo mapya,na  kwa ajili ya maendeleo ya mpira wa miguu duniani.
Tenga amechaguliwa nafasi hiyo baada ya kuwa mgombea pekee kutoka kanda ya Afrika Mashariki aliyejitokeza kuwania nafasi hiyo na kuungwa mkono na nchi zote wanachama wa CECAFA.

Wakati huo huo kiingilio cha kuziona timu za Twiga Stars dhidi ya Wazambia ni Sh 2000 katika pambano la marudiano ya kuwania Fainali za Soka za Wanawake Afrika. Mechi inatarajiwa kuchezwa wikiendi hii.