STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, March 12, 2013

Kim Poulsen kuanika silaha za kuivaa Morocco

Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Kim Poulsen
Na Boniface Wambura
KOCHA Mkuu wa timu ya Taifa ya Tanzania (Taifa Stars), Kim Poulsen kesho anatarajia kuanika kikosi cha timu yake kitakachovaana na Morroco katika pambano la kuwania kufuzu Fainali za Kombe la Dunia za mwaka 2014.
Kim atazungumza na wanahabari kesho majira ya saa 5 asubuhi kwenye ofisi za Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF).
Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager itacheza na Morocco kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam, Machi 24 mwaka huu katika mechi ya kundi C ikiwa sambamba na Ivory Coast na Gambia.
Mpaka sasa Stars inashika nafasi ya pili katika msimamo wa kundi lake ikiwa na pointi 3 moja nyuma ya ilizonazo Ivory Coast wanaoongoza msimamo na ambao wikiendi hii nao watashuka dimbani kucheza na Gambia.
Stars inahitaji ushindi katika mechi hiyo ili kuweka hai matumaini yta kufuzu fainali hizo za Kombe la Dunia ambazo zitafanyika mwakani nchini Brazili.
Msimamo wa kundi walilo Stars ni kama ifuatavyo:

                                   P  W  D  L   F  A  GD PTS
1. Ivory Coast             2   1   1   0   4   2    2   4
2. Tanzania                  2   1   0   1   2   3   -1   3
3. Morocco                 2   0   2   0   3   3    0   2
4. Gambia                    2   0   1   1   2   3  -1   1

Pambano la Simba, Coastal laingiza Mil 37



Na Boniface Wambura
PAMBANO la Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya mabingwa watetezi, Simba dhidi ya Coastal Union iliyochezwa juzi Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam imeingiza sh. 36,820,000 kutoka na watazamaji 6,284.

Viingilio katika mechi hiyo namba 138 iliyomalizika kwa Simba kuibuka na ushindi wa mabao 2-1 vilikuwa sh. 5,000, sh. 8,000, sh. 15,000 na sh. 20,000 huku kila klabu ikipata mgawo wa sh. 8,265,752.45 wakati Kodi ya Ongezeko la Thamani (VAT) iliyolipwa ni sh. 5,616,610.17.

Mgawo mwingine wa mapato hayo ni asilimia 15 ya uwanja sh. 4,202,924.97, tiketi sh. 3,183,890, gharama za mechi sh. 2,521,754.98, Kamati ya Ligi sh. 2,521,754.98, Mfuko wa Maendeleo ya Mpira wa Miguu (FDF) sh. 1,260,877.49 na Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA) sh. 980,682.49.

Uchaguzi TAFCA kufanyika Morogoro



Na Boniface Wambura

UCHAGUZI Mkuu wa viongozi wa Chama cha Makocha wa Mpira wa Miguu Tanzania (TAFCA) utafanyika Jumamosi (Machi 16 mwaka huu) mjini Dodoma ambapo wajumbe wanatakiwa kuripoti siku moja kabla ya uchaguzi.

Wagombea waliopitishwa kuwania uongozi na Kamati ya Uchaguzi ya TAFCA chini ya uenyekiti wa Ramadhan Mambosasa ni Oscar Don Koroso (Mwenyekiti), Lister Manyara (Makamu Mwenyekiti) na Katibu (Michael Bundala).

Wengine ni Gabriel Gunda (Katibu Msaidizi), Mjumbe wa Mkutano Mkuu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania- TFF (Wilfred Kidao) wakati wagombea ujumbe wa Kamati ya Utendaji ni Jemedali Saidi, George Komba na Magoma Rugora.

Kivumbi cha Ligi Kuu kuendelea J'mosi, Yanga kunusa ubingwa?



Wachezaji wa Yanga wakifurahia moja ya mabao yao ya Ligi kuu

Na Boniface Wambura

KIVUMBI cha Ligi Kuu Tanzania Bara (VPL) kinatarajiwa kuendelea tena Jumamosi kwa mechi tatu kupigwa viwanja vya mikoa mitatu tofauti ya Mwanza, Dar es Salaam na Morogoro.
Timu inayopigana kuepuka kushuka daraja, Toto Africans itakuwa dimba la nyumbani la CCM Kirumba jijini Mwanza kuvaana na Mgambo JKT katika moja ya pambano linalosubiriwa kwa hamu wikiendi hii.
Toto walio nafasi ya pili kutoka mkiani wakiwa na pointi 15 na ikiuguza kipigo cha 'kaka' zao Yanga itakuwa na kiu ya kupata ushindi ili kuweza kujinasua mkiani na kujiweka katika nafasi za kuepuka kushuka daraja.
Pambano jingine la mwishoni mwa wiki ni kati ya vinara wa ligi hiyo, Yanga watakaokuwa dimba la Taifa jijini Dar es Salaam kuwakaribisha maafande wa Ruvu Shooting, mechi ambayo itatoa taswira ya mbio za ubingwa kwa Yanga ambao msimu huu wameonekana wapo tofauti wakiwa na kiu ya kutwaa taji.
Mpaka sasa Yanga inaoongoza msimamo wa Ligi ikiwa na pointi 45 kutokana na mechi 19 ilizocheza ikifuatiwa na Azam waliopo nafasi ya pili na pointi zao 37 kisha Simba wanaokamata nafasi ya tatu wakiwa na pointi 34 wote pia wakiwa wamecheza mechi 19 kila mmoja.
Mtanange mwingine wa Jumamosi utazikutanisha timu zinazolingana pointi na kutofautiana uwiano wa mabo ya kufunga na kufungwa, Coastal Union ya Tanga watakaokuwa wageni wa Mtibwa Sugar kwenye uwanja wa Manungu, Morogoro.
Mshindi yoyote wa mechi hiyo wataweza kufikisha pointi 34 na hivyo kuwakamata mabingwa watetezi ambao wenyewe watashuka dimbani siku ya Jumapili.

DRFA yaunda kamati mbalimbali wakongwe waula


 
KAMATI ya Utendaji ya Chama Cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam kwa mamlaka iliyonayo imeteua kamati mbali mbali zitakazoshirikiana na Kamati ya Utendaji katika kukabiliana na changamoto mbali mbali za mpira wa miguu katika Mkoa wake ili kuweza kufikia malengo yake waliyojiwekea. Wafuatao ni watu na kamati mbali mbali walioteuliwa/zilizoteuliwa na Kamati ya Utendaji ya Chama Cha Soka Mkoa wa Dar es Salaam:
 
Bw. Joseph Kanakamfumo                     Mkurugenzi wa Ufundi
Bw. Saidi Pambalelo                              Afisa Tawala
Bw. Mohamedi Muharizo                       Afisa Habari
Bw. Hashim Abdallah                             Afisa Usalama
 
KAMATI YA FEDHA NA MIPANGO
1.       Bw. Meba Ramadhani               Mwenyekiti
2.       Bw. Iddi Msonga                       Makamu Mwenyekiti
3.       Bw. Ali Hassani                                                  
4.       Bw. Ramadhani Kilemile
5.       Bw. Isack Mazwile
 
KAMATI YA UFUNDI NA MASHINDANO
1.       Bw. Kenny Mwaisabula              Mwenyekiti
2.       Bw. Shabani Mohamedi              Makamu Mwenyekiti
3.       Bw. Hugo Seseme
4.       Bw. Daudi Kanuti
5.       Bw. Kassim Mustapha
6.       Bw. Abeid Mziba
7.       Bw. Bakari Mtumwa
 
KAMATI YA MAENDELEO YA SOKA LA VIJANA NA WANAWAKE
1.       Bw. Benny Kisaka                     Mwenyekiti
2.       Bw. Muhsin Balhabou                Makamu Mwenyekiti
3.       Dr. Sesy Makafu
4.       Bw. Emmanuel Kazimoto
5.       Dr.  Maneno Tamba
6.       Bw. Edwin Mloka
7.       Bw. Sande Mwanahewa
8.       Bw. Richard Shayo
 
KAMATI YA WAAMUZI
1.       Bw. Jovin Ndimbo                     Mwenyekiti
2.       Bw. Sijali Mzeru                        Makamu Mwenyekiti
3.       Bw. Saidi Mbwana
4.       Bw. Benny Mtula
5.       Bw. Abdallah Mitole
 
KAMATI YA NIDHAMU NA USULUHISHI
1.       Mheshimiwa Roman Masumbuko            Mwenyekiti
2.       Bw. Fahadi Faraji Kayuga                       Makamu Mwenyekiti
3.       Bw. Mohamedi Mpili
4.       Bw. Peter Nkwera
5.       Bw. Jimmy Mhango
 
KAMATI YA RUFAA
1.       Mheshimiwa Salehe Njaa                       Mwenyekiti
2.       Bw. Saidi Engo                                      Makamu Mwenyekiti
3.       Bw. Abasi Kuka
4.       Bw. Yusuph Macho
5.       Bw. Boi Risasi
 
Pia Kamati ya Utendaji ya Chama Cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam inapenda kuwafahamisha wanachama wake, wadau na mashabiki wa mpira wa miguu Tanzania dhamira yao ya kuendeleza mpira wa miguu katika Mkoa wa Dar es Salaam na Tanzania kwa ujumla.
 
Kwa kuanzia Chama cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam kipo kwenye mchakato wa kukamilisha DRFA Strategic Plan 2013 - 2016 (Mpango Mkakati Kazi) kwa kipindi cha miaka minne pamoja na kuboresha Financial Regulations zake ili kiweze kuwa na dira ya kuwahudumia wadau wake kwa ufanisi na uwazi zaidi. Lakini pia Kamati ya Utendaji imeona haja ya Chama Cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam kuwa na Website yake kwa ajili ya kuwapa habari wadau wake na Watanzania kwa ujumla.
 
Mwisho Kamati ya Utendaji ya Chama Cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam kinaomba ushirikiano na wadau wote wa mpira hususani Serikali, TFF, Vyama vya Mikoa, Walimu, Waamuzi, Madaktari, Vilabu, Makampuni na Waandishi wa habari na Vyombo vya habari katika kuendeleza mpira wa miguu katika mkoa wa Dar es Salaam na hatimaye mikoa yote ya Tanzania. “Kwani Pamoja Tunaweza”
 
Ahsanteni,
 
Almasi Kasongo
Mwenyekiti wa Chama Cha Mpira wa Miguu Mkoa wa Dar es Salaam (DRFA)

Arteta aitaka bodi Arsena ivunje benki kujiimarisha

Kiungo wa Arsenal, Mikel Arteta


KIUNGO nyota wa Arsenal, Mikel Arteta anaamini kwamba umefika wakati wa Arsenal kuwekeza vya kutosha kuimarisha timu iwapo inahitaji kurejesha heshima yake katika soka la Ulaya.
Mchezaji huyo ametoa maoni yake hayo baada ya kuishuhudia timu yake iking'olewa kwenye michuano ya nyumbani na timu za Bradford City na Blackburn Rovers, huku ikiwa imepoteza mechi ya mkondo wa kwanza wa 16 Bora Ligi ya Mabingwa Ulaya kwa mabao 3-1 dhidi ya Bayern Munich.
Arsenal kwa miaka nane sasa haijawahi kutwaa taji lolote, hali inayompa hofu mchezaji huyo hasa akiangalia pengo lililopo baina yao na wanaoongoza Ligi Kuu ya Engalnd, Mancester United.
Arteta alisema kuwa pamoja na misingi mzuri ya kukuza vipaji vya wachezaji ndani ya Arsenal na falsafa iliyopo na wachezaji iliyonayo, lazima klabu ifanye manunuzi wa wachezaji wakali zaidi iwapo inapata mafanikio zaidi.
Alisema kusalia kwao kwenye Ligi ya Mabingwa Ulaya kunahitaji miujiza, sawa na kukata tamaa ya kutwaa ubingwa wa Ligi ya England.
Hata hivyo alisema ni vema Arsenal ikaanza kujipanga kwa msimu ujao kwa kununua nyota watakaoweza kuijenga upya timu hiyo kuweza kukata kiu ya misimu karibu nane bila taji lolote.
"Tunatakwa kuwa bora na msimu ujao tuhahitaji kupata pointi nyingi zaidi kwa maana ya kutaka kushinda kila mchezo. Nadhani bodi inajua hili na tumaini letu msimu ujao watafanya kila jambo ili kufikia malengo hayo," alinukuliwa kiungo.
Kiungo alieleza pia sababu yake yua kuihama Everton na kutua Arsenal lengo likiwa ni kucheza Ligi ya Mabingwa na kwake ilikuwa na maana kubwa.
Juu ya pambano lao la kesho la Ligi ya Mabingwa Ulaya, Arteta alikiri ni kazi kutokana ukweli wapinzani wao Bayern Munich kuwa wazuri msimu huu na walionyesha hivyo hata katika mechi ya mkondo wa kwanza walipoibuka na ushindi wa mabao 3-1.

Mwandi yahimiza wachezaji kuchangamkia African Youth

Moja ya timu za vijana ya Yosso United ya Arusha
WACHEZAJI wa Ligi Kuu ya Soka Tanzania Bara na Zanzibar wenye umri kati ya miaka 18 na 21 wametakiwa kuchangamkia fursa ya kufanya majaribio ya kucheza soka la kulipwa Barani Ulaya, Asia na Afrika wakiwa nyumbani Tanzania.

Akizungumza na waandishi wa habari, Mkurugenzi wa Kampuni ya Tanzania Mwandi, Teonas Aswile, waandaaji wa Michuano ya African Youth Football Tournament amesema kuwa katika michuano hiyo wachezaji 11 bora watatafutiwa timu moja kwa moja katika mataifa nane barani Ulaya (Ufaransa, Ureno, Uholanzi, Denmark, Norway, Sweden, Ubelgiji na Switzerland), Asia na Afrika.

Bwana Teonas Aswile amesema kuwa wachezaji wa Tanzania bado hawajaonesha muamko mkubwa licha ya kiwango cha chini cha kushiriki ambacho wamewekewa ikilinganishwa na wachezaji wa kigeni, ambao licha ya kuwekewa USD 500 bado wamezidi kumiminika.

“Mpaka sasa kuna mawakala wawili ambao tumezungumza nao na wamethibitisha kuleta wachezaji wao zaidi ya 20 kushiriki kwenye michuano.”

“Hii ni mbali ya wachezaji mmoja mmoja ambao tunaowasiliana nao ambao wanataka kuja, wakiwa zaidi ya watano. Kwahiyo wachezaji wetu waamke na kuitumia fursa hii ambayo haipo katika nchi nyingine ya Afrika kwa wachezaji kufanya majaribio nchini mwao.”

Aidha Aswile ameviomba vilabu mbalimbali ambavyo vinaweza kuwalipia wachezaji wake ada ya shilingi laki tatu (Tsh 300, 000) ambayo inahitajika kwa mchezaji ili aweze kushiriki kwenye michuano ya African Youth Football Tournament kufanya hivyo kwani mchezaji huyo atakapouzwa klabu husika ndiyo itakayokubaliana na klabu itakayomchukua na si Kampuni ya Tanzania Mwandi.

“Sisi tunachokifanya ni kumuwezesha mchezaji aone njia za kufikia malengo yake. Kwa hiyo akishafanikiwa na amepata timu ya kuchezea iwe Ulaya, Asia au Afrika, klabu yake ndio itakayokubaliana na timu ya huko sisi hatutachukua chochote”, Teonas alisema.

Mkurugenzi huyo akitaja idadi ya wachezaji wa Tanzania ambao tayari wamethibitisha kushiriki amesema kuwa ni wachezaji watatu jambo ambalo bado linaonyesha mwamko umekuwa mdogo.

Michuano ya African Youth Football Tournament itafanyika Tanzania katika uwanja wa Karume jijini Dar es Salaam kuanzia tarehe 10 hadi 14 mwezi wa sita mwaka huu na kuwashirikisha wachezaji wenye umri wa miaka 18 hadi 21 ambapo watafundishwa na makocha watatu kutoka nje ya nchi na wawili wa Tanzania.

Pia michuano hiyo itashirikisha mawakala kutoka nchi nane za barani Ulaya, Asia na Afrika ambao wanahitaji wachezaji kwaajili ya klabu wanazoziwakilisha kati yao wakiwa ni Budak Johan, Cabrera Oliver, Dag Larsson, Phillip Mwakikosa na Dahlin Martin huku wakala wa kimataifa wa Tanzania Dr Damas Ndumbaro akiwa miongoni mwa mawakala wa Tanzania watakaoshiriki katika michuano kusaka vipaji kwaajili ya klabu mbalimbali.

“Tuna maombi ya mawakala wawili ambao wanataka wachezaji mabeki, washambuliaji na viungo kwaajili ya klabu zao Kuwait, Qatar, Libya na sehemu nyingine kwa hiyo hii ndio fursa ya wachezaji wetu kwenda kucheza soka la kulipwa na lenye maslahi zaidi kwao.”

Yanga yaipigia hesabu Ruvu Shooting

 
VINARA wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Yanga inaendelea kujifua kwa mazoezi makali kwa ajili ya pambano lake lijalo dhidi ya maafande wa Ruvu Shooting litakalochezwa Jumamosi kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar.
Yanga inayoongoza msimamo wa ligi ikiwa na pointi 45 na mabao 36 ya kufunga na mabao 12 ya kufunga, inahitaji ushindi katika mechi hiyo ijayo ili kuzidi kujiweka katika mazingira mazuri ya kutwaa ubingwa amnbao unashikiliwa kwa sasa na Siumba iliyopo nafasi ya tatu ikiwa  na pointi 34, tatu nyuma ya Azam.
Baada ya kupata ushindi wa nne mfululizo kwa kuilaza Toto Africans, vijana hao wa Ernest Brandts wapo katika mazoezi makali katika uwanja wa Mabatini Kijitonyama ikiwa maandilizi ya mechi hiyo ya Jumamosi.
Katika mazoezi ya jana kikosi hicho kiliwakosa nyota wake Kelvin Yondani na Said Bahanuzi ambao ni majeruhi.
Yondani anasumbulia na maumivu ya dole gumba aliloumia kwenye mchezo dhidi ya Toto Africans na Bahanuzi alishtua msuli wa kisigino na kwa mujibu wa daktari wa timu Dk Nassoro Matuzya wachezaji hao wanaendelea vizuri na huenda leo wakajumuika na wenzao kuendelea na mazoezi.
Pia Dk Matuzya alisema mchezaji Ladislaus Mbogo anatazamiwa kufanyiwa upasuaji wa uvimbe (shavuni) leo.
Mbogo atafanyiwa upasuaji huyo baada ya klabu ya Yanga kuridhia kufuatia  uchunguzi uliofanywa na madaktari juu ya uvimbe huo na kwa maana hiyo mchezaji huyo atakosa mechi kadhaa za timu yake.

Golden Bush Fc yazidi kugawa dozi Ligi ya TFF-Kinondoni



LICHA ya kushiriki michuano ya Ligi kwa mara ya kwanza, timu ya soka ya Golden Bush Fc ya Sinza imeendelea kugawa 'dozi' wa wapinzani wao, baada ya juzi kuifumua Makumbusho Talents kwa mabao 3-1 katika mfululizo wa Ligi Daraja la Nne Wilaya ya Kinondoni.
Vijana hao wanaonolewa na nyota wa zamani wa timu za Kagera Sugar na Moro United, Shija Katina huyo ni ushindi wao wa pili mfululizo kwani katika mechi yao ya fungua dimba la michuano hiyo, iliifanyia 'mauaji ya sharubella' timu ya Victoria ya Kijitonyama kwa kuinyuka mabao 6-1.
Ushindi huo umewapa faraja viongozi wa timu hiyo wakiamini ni mwanzo mwema wa ndoto zao za kuwa kufika mbali katika soka la Tanzania wakitamani kufuata nyayo za Azam Fc inayotamba Ligi Kuu Tanzania Bara ikiqwa timu inayomilikiwa na mtu binafsi kuzitetemesha Simba na Yanga na kung'ara kimataifa.