STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Friday, July 19, 2013

Mpigania haki za Mashoga auwawa kikatili


MPIGANIA  Haki za mashoga nchini Cameroon amekutwa amekufa nyumbani kwake Yaounde baada ya kuteswa, Wapigania Haki za Binadamu wamesema.
Mwili wa Eric Lembembe ulikutwa kwenye jiji hilo mnamo siku ya Jumatatu huku ukionekana alikuwa ameteswa vibaya sana, kundi hilo lilisema kwenye maelezo yao siku ya Jumanne.
 
Marafiki wa Lembembe waliukuta mwili wake mnamo siku ya Jumatatu jioni. Kwa mujibu wa rafiki zake shingo yake ilivunjwa na uso wake, mikono na miguu viliunguzwa moto kwa kutumia pasi, taarifa ilisema.
 
Shirika hilo limeelezea kitendo hicho kama ni cha “mauaji”na kuzitaka mamlaka husika kuendelea kufanya uchunguzi wa kina.

Denti wa Tegeta Sec ajinyonga hadi kufa kisa...!


Mwanafunzi  wa kidato cha kwanza katika Shule ya Sekondari Tegeta jijini Dar es Salaam, Bertha Amir (14), pichani, amejinyonga hadi kufa akipinga kulazimishwa na mama yake mzazi kusoma.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kinondoni, Camilius Wambura, alisema mwanafunzi huyo alijinyonga juzi  saa 11:00 jioni, maeneo ya Tegeta Namanga, jijini Dar es Salaam.
Alisema marehemu alikutwa amejinyonga chumbani kwa kutumia mtandio ulioning’inizwa juu ya dari.
Kamanda Wambura alisema sababu za mwanafunzi huyo kujinyonga bado hazijafahamika, lakini akasema inasadikika kuwa wakati wa enzi za uhai wake, siku moja kabla ya kifo chake, alikuwa ameongea na mama yake, Angelina Maiko Mshami (30), ambaye alimtaka achukue fedha kwa ajili ya kujiandaa kwenda shule.
Alisema mtoto huyo alimjibu mama yake kuwa hahitaji kusoma, bali anataka kufanya kazi.

Kamanda alisema kuwa mwili wa mwanafunzi huyo umehifadhiwa katika Hospitali ya Mwananyamala kwa uchunguzi na kwamba, polisi wanaendelea na upelelezi kuhusiana na kifo chake.
 Mama wa mtoto huyo, Angelina Mshami, alisema alishangazwa na kitendo cha mtoto wake kuamua kukataa shule ghafla wakati alikuwa ana uwezo mzuri darasani.

Alisema kuwa mtoto wake alikuwa na akili darasani akishika nafasi ya kwanza ama ya pili wakati akisoma shule ya msingi na hivyo kumfanya afaulu kujiunga  kidato cha kwanza.

Hata hivyo, alisema kabla ya kifo chake, binti yake alimweleza kuwa hataki shule bali anataka kufanya kazi.

Alisema alipomuuliza kazi gani anataka kuifanya, hakuitaja bali alisisitiza kuwa anaifahamu mwenyewe.

Betha ambaye ni mtoto wa kwanza kati ya watoto wawili katika familia yao, alizaliwa mwaka 1999, Wilaya ya Lushoto mkoani Tanga.

Alianza  darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Malindi mkoani Tanga na kufanikiwa kujiunga na Shule ya Sekondari Mtumbi na baadaye kuhamishiwa katika Shule ya Sekondari Tegeta.

Aidha, baadhi ya majirani waliokuwapo msibani hapo, walielezea masikitiko yao na huzuni kuhusiana na kifo cha msichana huyo.

Marehemu anatarajiwa kusafirishwa leo kuelekea mkoani Tanga kwa mazishi yatakayofanyika kesho kijijini Malindi

CREDIT:swahili tz.

Deo Lyatto atoa Shukrani kwa wadau wa soka nchini

Deo Lyatto, alipokuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF
HAPO chini ni Maelezo ya Shurani ya Mwenyekiti Aliyemaliza muda wake wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF, Deo Lyatto kwa wadau wa soka nchini.

1. Kama wote tunavyofahamu jana uongozi wangu wa Kamati ya Uchaguzi ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) ulifikia tamati kama mlivyotangaziwa na Rais wa TFF. Kwa heshima kubwa naomba kutumia fursa hii kuwashukuru viongozi na wadau wa soka kwa ushirikiano mkubwa nilioupata kutoka kwao wakati nikitekeleza majukumu mbalimbali ya TFF.

2.  Kwa kushirikiana na viongozi wa mpira wa miguu katika TFF na mikoa yote Tanzania Bara, pamoja na wadau wa soka, nimepata fursa kulitumikia soka la nchi yetu kwa nafasi mbalimbali. Kwa pamoja tumetekeleza majukumu ya ujenzi wa misingi ya uongozi bora katika TFF na wanachama wake.

3.  Naishukuru Kamati ya Utendaji ya TFF:

(i)kwa kuniteua kuwa mjumbe wa Kamati ya Nidhamu ya TFF, (Jan 2005 - Jan 2007). Nawashukuru pia wajumbe wa Kamati hiyo chini ya Mhe. Said El-Maamry kwa kunichagua kuwa Katibu wa Kamati hiyo. Ushirikiano mlionipatia ulioniwezesha kulitumikia taifa katika soka na kwa pamoja kurejesha nidhamu kwa kiwango kikubwa.

(ii)kwa kuniteua kuwa mjumbe wa Kamati Maalumu, iliyochunguza mkasa wa timu yetu ya Taifa ya wachezaji wa umri chini ya miaka 17 (Serengeti Boys) mwezi Juni 2005. Nawashukuru wajumbe wa kamati  hiyo chini ya Dr. Hamad Ndee Mkuu wa Idara ya Michezo ya Chuo kikuu cha Dar es salaam, kwa kunichagua kuwa Katibu wa kamati hiyo iliyoandaa taratibu za mashindano ya vijana  ambazo ni msingi  wa mashindano ya vijana wa umri chini ya miaka 17  hapa nchini.

(iii)kwa kuniteua kuwa Mjumbe wa Kamati Maalumu iliyotayarisha Programu ya kuendeleza Timu ya Taifa kwa kipindi cha miezi 15 (April 2006 hadi Juni 2007). Progamu iliyochangia Tanzania kiinua kiwango cha ubora wa soka kutoka nafasi ya 165 duniani mwezi Februari 2006 hadi nafasi ya 89 mwezi Desemba 2007.

(iv)kwa kunipa fursa ya kuwa mjumbe wa Kamati Maalumu ya kuboresha mapato ya TFF mwaka 2009. Nikiwa mjumbe na Katibu wa Kamati hiyo nilipata ushurikiano mkubwa kutoka kwa wadau wa soka nchini  na nje ya nchi.  Nina imani kuwa TFF itakamilisha utekelezaji wa mapendekezo ya Kamati na ya wadau wa soka ikiwa ni pamoja na kuanza kutumia tiketi za elektroniki.

(v)kwa kuniteua kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF  kwa  vipindi viwili; Februari 2009 - Machi 2011 na kuniteua tena kuiongoza Kamati hiyo kwa kipindi cha pili Machi 2011 hadi jana tarehe 18 Julai 2013. Naishukuru Kamati ya Utendaji ya TFF kwa imani kubwa iliyoonyesha kwangu na wanakamati wenzangu.
4.  Nawashukuru wajumbe wote wa wa Mkutano Mkuu wa TFF, kwa ushirikiano mkubwa mliotoa kwangu na Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa kushiriki kwa amani na utulivu na kuzingatia Katiba za vyama vyenu, Katiba ya TFF na Kanuni za Uchaguzi na hivyo kufanikisha zoezi la chaguzi za viongozi katika wilaya zote na Mikoa yote ya Tanzania Bara na hivyo kuwezesha kuwa na wajumbe wa Mkutano Mkuu, ambao  katika kikao chake cha kwanza baada ya chaguzi hizo kimefanya jambo la kihistoria kuweka nguzo za  Mwenendo, Maadili  na Miiko ya uongozi wa soka la nchi yetu. Nilifarijika kuwa sehemu ya Mkutano Mkuu huo nikiwa mwalikwa.

5. Nawashukuru viongozi na wafanyakazi wote wa Sekretarieti ya TFF, wajumbe wa Kamati zote za TFF, Wajumbe wa Kamati zote za Uchaguzi za wanachama wa TFF na wanachama wao, kwa ushirikiano mkubwa na wa dhati uliowezesha kuwatumikia wadau wa soka kwa kuzingatia taratibu zilizowekwa.

6. Nawashukuru sana wajumbe wa Kamati ya Uchaguzi ya TFF kwa ushirikiano niliopata kutoka kwao kwa muda tuliofanya kazi pamoja. Si jambo rahisi kusimamia chaguzi za mikoa yote na klabu zenye wanachama za Ligi Kuu, hata hivyo kwa kushirikiana na wadau mbalimali wa soka ambao nachukua fursa hii kuwashukuru, kwa pamoja tumeweza kutimiza jukumu hilo kikamilifu.  

7. Nawashukuru sana Waandishi na Wahariri wa habari za michezo na pia Wahariri Watendaji wa vyombo vya habari, kwa ushirikiano mzuri nanyi, ushirikiano na uhusiano wa uwazi ambao haukuwa na mikwaruzo ya aina yoyote kwa kipindi chote (Jan 2005-Jul 2013) tulichoshirikiana kwa pamoja kulitumikia soka la nchi yetu.

8. Namshukuru sana Rais wa TFF Ndg. Leodegar Tenga kwa imani kubwa aliyonayo kwangu na kwa wanakamati niliokuwa nao katika kutekeleza majukumu ya umma. Miaka ishirini na tisa (29) iliyopita nilipata fursa ya kufanya kazi ya mpira miguu kwa mara ya kwanza na Ndg. Tenga, nikiwa nahodha wa Timu ya Mpira wa Miguu ya Chuo kikuu cha Dar es salaam, Desemba 1984, wakati Ndg. Tenga alipojitolea kuifundisha timu ya Chuo Kikuu cha DSM. Tangu wakati huo hadi sasa imani  na  ushirikiano katika utekelezaji wa majukumu ya umma niliopata kutoka kwa Ndg. Tenga haujawai kutetereka hata kwa siku moja. Ni faraja kubwa kwangu kufanya kazi hizi za umma chini ya kiongozi anayeheshimika na kuaminika na wadau wa soka hapa nchini, Afrika Mashariki na Kati, Afrika na familia ya soka Duniani kwa ujumla.

9. Mwisho, kwa viongozi na wadau wote wa mpira wa miguu, nawashukuru na nawatakia kheri, baraka  na mafanikio katika Uchaguzi Mkuu wa TFF na  ujenzi wa  soka la nchi yetu..

Asanteni.
 
Deogratias J. Lyatto
19 Julai 2013, Dar es salaam, Tanzania.

Yanga wamegeuzia kibao Kiiza, kisa...!

Na Dina Ismail
BAADA ya kuipiga danadana kwa muda mrefu, hatimaye klabu ya soka ya Yanga imemgeuzia kibao aliyekuwa kiungo mshambuliaji wake wa kimataifa,Hamis Kiiza. 
Hivi karibuni nyota huyo kutoka nchini Uganda, amekuwa katika mvutano na uongozi wa klabu hiyo juu ya kusaini mkataba mpya wa kuendelea kutumikia klabu hiyo. 
Kwamba, Kiiza alitaka kuongezwa ofa ya aliyopewa na uongozi kutoka dola 35,000 hadi dola 50, 000 ambazo amesisitiza kupewa na baadaye kumuongeza hadi dola 40,000. 
Hata hivyo, habari kutoka ndani ya uongozi wa Yanga zinaeleza kwamba wameamua kuachana kwanza na suala la Kiiza kutokana na nafasi yake kutokuwa na umuhimu katika kikosi hicho. 
Kiongozi mmoja aliliambia gazeti hili kwamba kwa sasa Yanga inahitaji mshambuliaji halisi mmoja ambaye atashirikiana na mshambuliaji aliyepo sasa, Didier Kavumbagu. 
“Kwa sasa suala la Kiiza tumeliweka kando kwani nafasi yake haina umuhimu katika kikosi chetu, tunatafuta mshambuliaji halisi, ila tukikosa ndo tutarudi kwake,”alisema 
Akienda mbali zaidi, kiongozi huyo alisema kwamba mshambuliaji huyo anafahamu kila kitu juu ya mustakabali wake ndani ya klabu hiyo na hata hilo suala la kumpa fedha anayoitaka yeye halipo. 
Aliongeza kuwa baada ya kumleta mshambuliaji kutoka Nigeria Ogbu Brendan  kwa ajili ya majaribio, hivi karibuni tena wanataleta washambuliaji wengine kuja kujaribiwa. 
Katika hatua nyingine, kikosi cha Yanga kimeendelea na mazoezi yake ya kujiandaa na ligi kuu soka Tanzania Bara ambapo keshokutwa itacheza mechi ya kirafiki na URA ya Uganda. 

Mchezo huo utakaopigwa kwenye dimba la Taifa jijini Dar es Salaam ikiwa ni sehemu ya kukipima kikosi hicho.

Mtwara kumekucha! Lori lenye shehena ya mabomba lashambuliwa mawe dereva hoi


Habari zilizotufikia kutoka mjini Mtwara zinasema kuwa Gari lililokuwa limebeba Shehena ya Mabomba ya Kusafirishia gesi kutoka Mjini Mtwara kuelekea Dar limeshambuliwa na mawe na kupelekea dereva wa lori hilo Kujeruhiwa Vibaya. 
Lori hilo lilianza kushambuliwa mara baada ya kuingia katika eneo la Mikindani Manispaa ya Mtwara Mjini na sababu ya kushambulia gari hilo ni katika kile kinachodhihirisha kuwa wana Mtwara bado hawajakubaliana na hoja ya Serikali ya kutaka Kusafirisha Gesi hiyo kwa ajili ya Manufaa ya Nchi. Lori hilo kwa sasa lipo kituo kikubwa cha polisi  Mtwara.
Tukio hilo linatokea ikiwa ni wiki moja tu imepita tokea watu kadhaa kukamatwa na jeshi la polisi mkoani Mtwara kwa kile kinachodaiwa kusambaza waraka wa kuhujumu miundombinu yote ya gesi mara tu serikali itakapoanza utekelezaji wake wa ujenzi wa bomba hilo kupeleka Dar.

Source: Jamii Forum

Miili ya wanajeshi waliouwawa Darfur kurejeshwa nchini kesho

http://www.raiamwema.co.tz/sites/default/files/styles/slideshow/public/field/image/307_jwtz.jpg?itok=8L3GOhTM
Miili ya wanajeshi hao ilipokuwa ikiagwa na askari wenzao nchini Sudan

MIILI ya wanajeshi waliouwawa katika mji wa Darfur, nchini Sudan inatarajiwa kuwasili nchini kesho kuanzia majira ya saa 4 asubuhi kwa ajili ya mazishi yake.
Wanajeshi hao waliokuwa kwenye jeshi la kulinda amani la Umoja wa Mataifa, walishambuliwa asubuhi ya Jumamosi iliyopita na waasi wanaopigana na serikali ya Sudan katika jimbo hilo la Darfur wakati wakisindikiza msafara ambaopo askari wengine akiwemo Polisi wa Tanzania walijeruhiwa.
Taarifa zinasema miili hiyo itapokelewa kesho kwa heshima zote kabla ya kufanyiwa taratibu za kuagwa kitaifa kisha kuzikwa kwa kushirikiana na familia zao.

Wenger amkatia tamaa Fabregas

http://gossip.ladyarse.com/wp-content/uploads/2012/07/wenger-arsene.jpg
Kocha Arsene Wenger

KOCHA wa Arsenal, Arsene Wenger amesema kwamba kuwa hatarajii kumsajili Cesc Fabregas katika kipindi hiki cha usajili wa majira ya kiangazi kwani kiungo huyo wa timu ya taifa ya Hispania ameamua kubaki kwa "mwaka mmoja zaidi " kwenye klabu yake ya Barcelona.
Arsenal wamesisitiza kuwapo kwa kipengele kinachowaruhusu kumnunua tena Fabregas kwa paundi za England milioni 25 ambacho kiliwekwa wakati wa mkataba wao wa kumuuza Mhispania huyo kwa Barca miaka miwili iliyopita.
Hata hivyo, licha ya Manchester United kujaribu kumtwaa kwa kuwasilisha ofa ya euro milioni 30 Jumatatu iliyopita, Mfaransa Wenger anaamini kwamba wao hawahitaji kutuma ofa yoyote kwa nia ya kumzuia nahodha wao huyo wa zamani kwenda Man U.
Iliripotiwa mwishoni mwa mwezi uliopita kuwa Wenger amekuwa akiwasiliana kila mara na nahodha wake huyo wa zamani, na sasa amedai kuwa anafahamu msimamo wa Mhispania huyo kuhusiana na hatma yake msimu ujao.
"Hivi sasa, Fabregas ameamua kubaki Barcelona kwa mwaka mmoja zaidi," Wenger aliwaambia waandishi wa habari.
Nahodha huyo wa zamani wa Arsenal amekuwa akihaha kupata nafasi ya uhakika katika kikosi cha kwanza tangu arejee katika timu yake ya utotoni lakini kuondoka kwa Thiago Alcantara kwenda Bayern Munich kunamaanisha kuwa sasa ana nafasi kubwa ya kucheza katika kiungo cha kocha Tito Vilanova.
Vilanova alisisitiza mwanzoni mwa wiki hii kwamba kiungo huyo mwenye miaka 26 anataka kubaki Barca na kuigania namba.
Alisema: "Natambua kwamba tumepokea ofa kadhaa kutoka klabu nyingine. Nilizungumza naye na ameniambia anataka kubaki.
"Cesc hafikirii kuhamia katika klabu nyingine. Anajua kwamba ushindani hapa ni mkubwa. Ndoto zake ni kuona anafanikiwa akiwa hapa."
Katika hatua nyingine kocha huyo amesema klabu yake inamudu mshahara wa kumlipa mshambuliaji wa Manchester United, Wayne Rooney anayetajwa kutaka kuhama Old Trafford licha ya klabu kudai HAUZWI.
Wenger alisema kama mchezaji huyo ataamua kukubali kutua kwao hawatakuwa na tabu ya kumlipa mshahara ambao kwa wiki hulipwa pauni 250,000.
"Rooney ana mkataba na amebakisha miaka miwili uishe, hivyo ni Man U wenye maamuzi. Lakini hatutakuwa na shida kulipa mshahara wa Rooney." alinukuliwa kocha huyo kutoka Ufaransa.

Mama atelekeza kichanga kisa wivu wa mapenzi

http://www.varbak.com/images/photos-of-black-babies-nb17527.jpg
Picha hii haihusiani na tukio hilo la kutelekezwa mtoto mjini Tanga
MWANAMKE mmoja mkazi wa eneo la Mtakuja jijini Tanga, aliyetajwa kwa jina la Asha Muhidini, amedaiwa kumtekeleza mtoto wake mchanga wa miezi miwili na kutokomea kusikojulikana kutokana na kile kilichoelezwa kuwa ni wivu wa mapenzi dhidi ya mumewe.
Mtonyaji wa habari hizi, Mariam Victor aliyejitambulisha kama mpwa wa mume wa mwanamke huyo, aliiambia MICHARAZO kuwa, mama huyo amekuwa na mzozo kwa muda mrefu na mumewe aliyetajwa kwa jina la Muhidini Mohammed baada ya mwanaume kuzaa nje ya ndoa mtoto mwenye miaka mitano.
Mariam alisema mwanamke huyo alimtelekeza kichanga hicho kwa kumfungia ndani ya chumba wanachoishi na mumewe tangu saa 1 usiku na walikuja kushtuka saa 5 usiku mtoto akilia na mjomba aliporejea kazini.

Aliongeza kuwa Asha amekuwa akipinga mtoto huyo aliyezaliwa kuja kuishi katia familia yao, lakini mumewe alikuwa akipinga akidai hawezi kuiacha damu yake kwa msimamo wa mkewe huyo.
"Mzozo uliosababisha hili jambo ni mtoto aliyezaliwa nje ya ndoa na Mjomba ambapo kwa muda mrefu amekuwa akipinga na mkazamjomba (Asha) na jana alikuja kumtembelea baba yake na mke akapinga lakini mjomba alishikilia msimamo wake," alidokeza Mariam.
Alisema hawakujua kinachoendelea mpaka walipobaini kuwa mtoto kaachwa pekee yake na mama wa mtoto katoweka na kuanza kumsaka asubuhi hii bila ya mafanikio na kukimbilia ofisi ya serikali ya mtaa wao kuripoti ambapo wameombwa kuwa na subira kuona kama mwanamke huyo atarudi au la.
"Mwenyekiti katuambia tuvute subira na tumlishe mtoto maziwa na ng'ombe wakati tunasubiri mama yake arejee na kama vipi tuangalie ustaarabu mwingine ikiwemo kuripoti Polisi au kuendelea kumtunza mtoto kwa sababu pia hasumbui zaidi ya anapotaka kunyonya tu," alisema Mariam.
Juu ya mjomba wake na tukio hilo alilofanyiwa na mkewe, Mariam alidai hana la kusema kwa vile ni mpole kupita maelezo na kwamba amekubali kilichotokea kwa sababu kichanga hicho ni mwanae na ana wajibu wa kumtunza hasa ikizingatiwa wanapoishi ni nyuma ya familia hivyo kichanga kitaangaliwa.

Salha atua King's Modern Taarab


MUIMBAJI wa zamani wa kundi la Dar Modern Salha Abdallah 'Salha wa Hammer' aliyetimuliwa katika kundi hilo kwa kutoa wimbo binafsi na mumewe, amejiunga na la King's Modern Taarab na ameanza kuijifua kwa ajili ya maonyesho ya sikukuu ya Idd el Fitri.
Salha aliyetamba na vibao kadhaa akiwa na Dar Modern ukiwamo utunzi wake uliobeba jina la albamu ya 'Nauvua Ushoga' amelamba ajira King's Modern Julai 4 mwaka huu na anaendelea kujifua nao kwa ajili shoo za Idd na maandalizi ya albamu mpya ya kundi hilo.
Akizungumza na MICHARAZO, Salha alisema amesaini mkataba wa kulifanyia kazi kundi hilo linalotamba na kibwagizo cha 'Kijoka chazima taa' na hakuona sababu ya kuvunga huku akiwa ameshatimuliwa katika kundi lake la zamani.
"Baada ya kutemeshwa mzigo Dar Modern hivi karibuni, kundi la King's Modern limenifuata na kuniomba kujiunga nalo na kwa sasa mimi ni muimbaji wa kundi hilo, tunajiandaa kwa shoo za sikukuu ya Idd," alisema Salha.
Alisema hana cha kuahidi kwa mashabiki wa kundi hilo lakini wajiandae kupata burudani kabambe akishirikiana na wanamuziki wenzake ambao wamempokea kwa mikono miwili.
Uongozi wa Dar Modern unadaiwa kumtimua Salha baada ya muimbaji huyo na mumewe kutoa wimbo wa 'Mapenzi Matamu' (Wapendanao) kinyume na utaratibu uliopo ndani ya kundi hilo, japo Salha alilia kwamba hakutendewa haki kwa vile aliyeimba naye katika kazi hiyo ni mumewe na siyo kundi au msanii mwingine wa nje.

JAJI KORTI YA RUFANI KUONGOZA KAMATI TFF

Na Boniface Wambura
SHIRIKISHO la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) limemteua Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Bernard Luanda kuongoza Kamati ya Rufani ya Uchaguzi kufuatia mabadiliko ya Katiba yaliyofanywa Jumamosi (Julai 13 mwaka huu) na kuingiza kamati nyingine mpya.

Rais wa TFF, Leodegar Tenga ametangaza wajumbe wa kamati hizo jana (Julai 18 mwaka huu) mara baada ya kikao cha Kamati ya Utendaji ya TFF kilichofanyika jijini Dar es Salaam.

Amesema uteuzi wa wajumbe hao umezingatia maoni ya wajumbe wa Mkutano Mkuu wa TFF, lakini vilevile amewashukuru wajumbe walioteuliwa kwa kukubali kutoa mchango wao katika maendeleo ya mpira wa miguu nchini.

Mbali ya Jaji Luanda ambaye ni Mwenyekiti wa kamati hiyo, wajumbe ni Francis Kiwanga (Makamu Mwenyekiti), Anney Semu, Yohane Masalla na Allen Kasamala. Kamati ya Uchaguzi inaongozwa na Hamidu Mbwezeleni, Moses Kaluwa (Makamu Mwenyekiti), Mustafa Siyani, Hassan Dyamwale na Kitwana Manara.

Mwenyekiti Kamati ya Rufani ya Maadili ni Jaji Steven Ihema, Bi. Victoria Makani (Makamu Mwenyekiti), Mheshimiwa Mohamed Missanga, Henry Tandau na Mheshimiwa Murtaza Mangungu. Kamati ya Maadili inaundwa na Bi. Jesse Mguto (Mwenyekiti), Francis Kabwe (Makamu Mwenyekiti), Profesa Mtambo Madundo, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Mohamed Mpinga na Evod Mmanda.

Profesa Mgongo Fimbo anaongoza Kamati ya Rufani ya Nidhamu wakati Makamu wake ni Ong’wanuhama Kibuta na wajumbe ni Kanali Mstaafu Idd Kipingu, Dk. Mshindo Msolla na Kamishna Msaidizi Mwandamizi wa Polisi (SACP) Mstaafu Jamal Rwambow. Kamati ya Nidhamu inaongozwa na Kamishna wa Polisi (CP) Mstaafu Alfred Tibaigana, Mustafa Kambona (Makamu Mwenyekiti), Mheshimiwa Azzan Zungu, Yusuf Nzowa na Mohamed Msomali.
Pia Kamati ya Utendaji imefanya mabadiliko katika Kamati ya Waamuzi ambapo Said Nassoro na Charles Ndagala kutoka Chama cha Waamuzi wanachukua nafasi za Joan Minja na Riziki Majala. Kamati hiyo inaendelea kuongozwa na Kapteni Mstaafu Stanley Lugenge, Omar Kasinde (Makamu Mwenyekiti) wakati mjumbe mwingine ni Mohamed Nyama.

Kamati ya Tiba inaongozwa na Dk. Paul Marealle wakati nafasi ya Makamu Mwenyekiti itajazwa baadaye na Rais Tenga. Wajumbe ni Mwanandi Mwankemwa, Anthony Ngome, Frank Mhonda, Kapteni Joakim Mshanga na Helen Semu.

Rais Tenga alisema mabadiliko mengine yamefanyika kutokana na waliokuwa wajumbe kuomba kupumzika. Wajumbe walioomba kupumzika ni Dk. Sylvester Faya, Idd Mtiginjola na Deo Lyatto