STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Sunday, September 21, 2014

Simba yashindwa kulipa kisasi kwa Coastal Taifa

simba
MASHABIKI wa klabu ya Simba wametoka uwanja wa Taifa wakiwa hawana furaha baada ya kikosi cha timu yao kushindwa kulinda mabao mawili waliyoyafunga kipindi cha kwanza na kuwaachia Coastal Union warejeshe kipindi cha pili na kufanya mchezo huo kumalizika kwa sare ya mabao 2-2 katika Ligi Kuu.
Mabao mawili ya Shaaban Kisiga na Amissi Tambwe yaliwafanya vijana wa Msimbazi kuwa na furaha na kuamini wangepata nafasi ya kuwacheka wapinzani wao Yanga waliozabuliwa mabao 2-0 na Mtibwa Sugar jana mjini Morogoro baada ya kwenda mapumziko wakiwa mbele.
Hata hivyo kipindi cha pili kilipoanza Coastal waliingia kivingine na kucharuka na kurejesha bao moja baada ya jingine kupitia wa Lutimba Yayo na Ramadhani Salim kufungwa kwa faulo na kuifanya matokeo kusomeka mabao 2-2 na kuwafanya mashabiki wa Simba kuwa wanyonge, licha ya timu ya kupata pointi moja.
MSIMAMO LIGI KUU TANZANIA BARA 2014-2015
                                          P  W  D  L  F  A  Pts
1. Ndanda Fc                    1   1    0   0  4   1    3
2. Azam                             1   1    0   0  3   1   3
3. Mtibwa Sugar                1   1    0   0  2    0  3
4. Prisons                           1   1   0   0   2   0   3
5. Mgambo JKT                1    1   0   0   1   0   3
6. JKT Ruvu                      1    0   1   0   0   0   1
7. Coastal Union                1    0   1   0   2   2   1
8. Simba                            1    0   1   0   2   2   1
9.Mbeya City                     1    0   1    0   0  0  1
10. Kagera Sugar               1    0   0   1    0   1   0
11. Ruvu Shooting              1    0   0   1    0   2  0
12.Yanga                            1    0   0   1    0   2  0
13. Polisi Moro                  1    0   0   1    1    3  0
14.Stand Utd                     1    0   0   1    1    4  0

Manchester United bado sana, yagongwa 5, Spurs yafa nyumbani

Emmanuel Adebayor
Adebayor akipaparika kuisaidia Spurs isife nyumbani bila mafanikio
Esteban Cambiasso
Hivi ndivyo Mashetani Wekundu walivyonyonyolewa leo ugenini na Leicester City
Etienne Capoue (left) and Stephane SessegnonHALI bado tete kwa klabu ya Manchester United baada ya jioni hii kubamizwa mabao 5-3 na klabu iliyorejea kwenye ligi kuu ya England, Leicester City katika pambano la ugenini, huku Tottenham Hotspur ikifa nyumbani mbele ya West Bromwich Albion kwa bao 1-0.
Manchester iliyofanya 'mauaji' ya kutisha wiki iliyopita kwa kuifumua timu kibonde ya QPR kwa mabao 4-0 ilionekana kama ingeendeleza ushindi kwa Leicester City baada ya kutangulia kupata mabao mawili ya haraka.
Mabao hayo yaliyofungwa na Robin van Persie katika dakika ya 13 ya mchezaji akimalizia kazi nzuri ya Radamel Falcao na Angel di Maria kuongeza la pili dakika tatu baada ya kumegewa pande na Wayne Rooney.
Hata hivyo hilo la pili halikudumu kwani dakika moja baadaye Ulloa aliifungua wenyeji bao na kufanya matokeo kuwa 2-1  hadi wakati wa mapumziko.
Kipindi cha pili Mashetani Wekundu ambao wana pengo katika nafasi ya ulinzi tangu walipowauza Rio Ferdinand na Namanja Vidic, waliongeza bao la tatu dakika ya 57 na kiungo Ander Herrera kwa kazi nzuri ya Di Maria.
Wenyeji walicharuka na kurejesha bao la pili dakika ya 62 kwa mkwaju wa penati kupitia Nugent kabla ya Cambiasso kusawazisha bao dakika mbili baadaye, huku pia Mashetani Wekundu wakimpoteza beki wao Blackett kwa kadi nyekundu.
Magoli yaliyoizamisha vijana wa Louis Van Gaal, yalitumbukizwa wavuni katika dakika ya 79 na Vardy na Ulloa akahitimisha kwa mkwaju wa penati katika dakika ya 83.
Katika mechi nyingine iliyochezwa mapema sambamba na pambano hilo, Spurs ikiwa nyumbani iliendeleza uteja baada ya kulazwa bao 1-0 na wageni wao West Brom.
Bao lililoiua Spurs lilifungwa na James Morrison katika dakika ya 74, licha ya wenyeji kucharuka kutaka kuondokana na aibu ya kulala nyumbani.
Ligi inaendelea kwa mechi mbili kati ya Crystal Palace dhidi ya Everton na Manchester City dhidi ya Chelsea.

Simba, Coastal hapatoshi leo, Ndanda Kuchele!

Simba watapona kwa Coastal
Yusuf Chippo, Kocha wa Coastal Union (mwenye kofia) ataendeleza ubabe kwa vijana wake dhidi ya Simba leo Taifa?
https://blogger.googleusercontent.com/img/b/R29vZ2xl/AVvXsEgSvHwYqtPQMuzPoWUu4QCWVjjgvVwLySqdBYExhW-LxDkl-tjqI3X__y-_vwNzmO6A72piQEbxsK79AqJ8vub5o2bTvjx1VL8FqSFT_-uMryVYDTOmZZVv18G_WiMV4YrQE_D_be0p_aWy/s1600/20140913_160438.jpg
Ndanda Fc waliokaa kileleni baada ya ushindi wake wa kishindo jana dhidi ya Stand Utd
WAKATI mabingwa wa zamani wa soka nchini, Simba na Coastal Union zikishuka dimbani leo katika mechi ya kisasi baina ya 'wanandugu' hao, wageni wa Ligi Kuu Tanzania Bara, Ndanda wameanza na mguu mzuri kwa kukaa kileleni mwa msimamo wa ligi.
Ushindi wa mabao 4-1 iliyopata ugenini dhidi ya Stand United ya Shinyanga imeiweka Ndanda kileleni ikiwazxidi mabingwa watetezi Azam kwa uwiano wa bao moja la kufunga.
Azam wanakamata nafasi ya pili na kufuatiwa na Mtibwa Sugar waliowatoa nishai Yanga na Marcio Maximo wao pamoja na Jaja, kisha Prisons waliowakong'ota maafande wa Ruvu Shooting wakifuatia mbele ya Mgambo JKT walioshinda jana nyumbani mjini Tanga.
Ingawa ni mapema mno kuijadili ligi kwa sasa, lakini kwa kuwa asubuhi njema huonekana asubuhi, Ndanda, Azam, Mtibwa na Prisons zimesafisha 'nyota' kwa ushindi katika mechi zao za ufunguzi, huku Mbeya City na JKT Ruvu wenyewe wakikusanya pointi moja moja.
Raundi ya kwanza ya mechi hizo za ufunguzi itakamilika leo wakati Simba na Coastal Union zitakazpovaana kwenye dimba la Taifa, huku Simba ikitaka kulipa kisasi na Coastal wakitafuta rekodi ya kuendeleza ubabe kwa vijana wa Msimbazi.
Katika mechi ya mwisho ya msimu uliopita baina ya timu hizo, Simba ilikubali kipigo cha bao 1-0, goli lililofungwa na beki kinda wa Coastal Hamad Juma dakika chache kabla ya mapumziko na kulizamisha jahazi la Wekundu wa Msimbazi waliokuwa chini ya Kocha Zdravkov Logarusic ambaye kwa sasa hayupo na timu hiyo.
Simba itawakabili Coastal wakiwa chini ya Mzambia Patrick Phiri na ikiundwa na kikosi imara, hali inayofanya pambano hilo kuwa la kusubiriwa kwa hamu kwani hata Coastal nao siyo ya kubezwa kwa usajili iliyofanywa chini ya kocha Mkenya, Yusuf Chippo.
Je ni Simba itakayolipa kisasi au Coastal itakayoendeleza ubabe katika mechi ya leo? Jibu ni baada ya dakika 90 ya mchezo huo. Tusubiri tuone.

TP Mazembe yafa ugenini kwa ES Setif

http://www.groupelavenir.org/IMG/arton1718.jpg
TP Mazembe
KLABU ya TP Mazembe ya DR Congo imepewa kipigo cha mabao 2-1 ugenini na ES Setif ya Algeria, lakini bao la kujifunga ,a wenyeji limewasaidia kuwaweka katika nafasi nzuri ya kusonga mbele kama itashinda angalao bao 1-o nyumbani wiki ijayo.
Said Aroussi alijifunga kattika dakika 52 kwenye harakati za kuokoa mpira wa krosi uliopigwa na Rainford Kalaba na kuwapa uongozi TP Mazembe.
Hata hivyo wenyeji walirudisha bao hilo dakika chache baadaye kupitia kwa Younes akimalizia krosi pasi huku waamuzi wa poambano hilo wakijichanganya, refga wa kati akisema goli wakati msaidizi wake akionyesha kibendera cha kuotea cha mpiga krosi.
Refa Neant Alioum alikubali goli hilo baada ya kuzongwa na wachezaji wa ES Setif wakipinga maamuzi ya mshika kibendera, japo TP Mazembe waliamua kucheza soka.
Dakika chache kabla ya kumalizika kwa pambano hilo wenyeji walipata bao la ushindi kupitia kwa Abdulmalek Ziaya aliyemtungua kipa mwenye mbwembwe Robert Kidiaba.

Tevez aiangamiza AC Milan Italia

Carlos Tevez
Carlos Tevez akitupia kitu nyavuni na kuwaacha kipa na mabeki wa Milan wakiwa katika simanzi
BAO pekee lililofungwa na Muargentina, Carlos Tevez katika dakika ya 71 akimalizia kazi ya Paul Pogba lilitosha kuwapa ushindi mujarabu mabingwa watetezi wa Ligi Kuu ya Italia, Seria A Juventus dhidi ya AC Milan katika pambano lililochezwa uwanja wa San Sirro, mjini Milan.
Kipigo hicho kimeishusha Milan mpaka nafasi ya tatu ikisaliwa na pointi zake 6 na kuwapisha Juventus kukaa kileleni ikiwa na pointi 9 na mabao manne ya kufungwa ikiwa haijafungwa bao lolote mpaka sasa.
AS Roma waliokuwa nafasi ya tatu wamepanda hadi nafasi ya pili katika msimamo wa ligi hiyo kwa uwiano wa mabao ya kufunga na kufungwa dhidi yake na Milan ambao wamefunga mabao nane na kuruhusu mabao sita.
Ligi hiyo inatarajiwa kuendelea leo kwa michezo mbalimbali ambapo mapame saa saba mchana huu, Chievo Verona itakuwa nyumbani kuialika Parma, Genoa itaialika Lazio na AS Roma watakuwa nyumbani kuikaribisha Cagliari.
Mechi nyingine za leo ni kati ya Sassuolo dhidi ya Sampdoria, Atalanta itaikaribisha Fiorentina, Udinese itaialika Napoli, Palermo itakuwa wenyeji wa Inter Milan na Hellas Verona watakuwa wageni wa Torino.