STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, May 27, 2014

AC Milan kumtema Seedorf, Pipo kumrithi

Clarence Seedorf
KLABU ya AC Milan imedaiwa inajiandaa kumtimua kazi Kocha wake wa sasa Clarence Seedorf na nafasi yake huenda ikachukuliwa na kocha wa timu ya vijana na nyota wa zamani wa klabu hiyo na timu ya taifa ya Italia (Azzurri) Filippo Inzaghi.
Kwa mujibu wa taarifa kutuka Italia zinasema kuwa, Seedorf aliyeinoa timu hiyo kwa muda wa miezi minne tu kati ya mkataba wake wa miaka miwili na nusu atafungashiwa virago kwa nia ya kuimarisha klabu hiyo imekuwa na msimu mbaya siku za karibuni kabla ya Mholanzi huyo kuisaidia kuindoa maeneo ya mkiani mwa Ligi Kuu ya nchi hiyo, Seria A.
Seedorf, 38, aliyeitumikia klabu hiyo kwa miaka 10 alipewa jukumu la kuinoa timu hiyo Januari mwaka huu kuchukua nafasi ya Massimiliano Allegri aliyefurushwa baada ya mkataba wake kusitishwa kutokana na mwenendo mbaya wa timu katika michuano iliyokuwa ikishiriki.
Pamoja na klutokuwa kocha mzoefu Mholanzi huyo aliiwezesha timu hiyo kushinda mechi 11 kati ya 19 ilizocheza Milan na kumaliza kwenye nafasi ya nane, tofauti na mtangulizi wake aliyeshinda mechi tano tu kati ya 19 za duru la kwanza.
Hata hivyo timu hiyo inayomilikiwa na Waziri Mkuu wa zamani wa Italia, Silvio Berluscoini imekwama kushiriki hata michuano ya Ligi Ndogo ya Ulaya kutokana na kuangushwa na pointi moja tu, hali iliyowafanya wamiliki wake kutaka kuipanga upya mabingwa hao wa zamani wa Ulaya kurejesha hadhi yake msimu ujao.
.

Mbeya City wateleza Sudan, Wakenya waongoza kundi lao


WAWAKILISHI wa Tanzania katika michuano ya CECAFA Nile Basin Cup,Mbeya City chini ya kocha mkuu Juma Mwambusi wamefungwa mabao 2-1 na AFC Leopard ya Kenya katika mchezo uliopigwa usiku wa jana mjini Khartoum.
Bao la Mbeya City lilifungwa na kiungo mshambuliaji,Deus Kaseke, huku washindi wakitangulia kufunga mabao yao .
Ushindi huo unawafanya AFC Leopard wajikite kileleni mwa kundi B baada ya kufikisha pointi 6.

Stars, Malawi kupepetana leo Taifa, kiingilio buku 5

TIMU ya soka ya taifa, Taifa Stars jioni ya leo inatarajiwa kushuka dimbani kurudiana na The Flames ya Malawi katika mechi ya kirafiki ya kimataifa itakayochezwa Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam kuanzia saa 11 kamili jioni.


Stars na Malawi zinavaana leo ikiwa ni wiki moja na ushei tangu zilipoppetana mjini Mbeya na kushindwa kutambiana zikijiandaa na mechi zao za kuwania kufuzu Fainali za Afrika za mwaka 2015 zitakazofanyika nchini Morocco.
Stars iliyopiga kambi yake Tukuyu mkoani Mbeya imewasili jijini Dar es Salaam  saa 4 asubuhi kwa ndege ya Air Tanzania tayari kwa mechi hiyo kujiandaa na mechi yao ya marudiano dhidi ya Zimbambwe itakayochezwa wikiendi hii mjini Harare.


Kiingilio katika mechi hiyo kitakuwa sh. 5,000 kwa viti vya rangi ya chungwa, bluu na kijani. Kwa upande wa VIP B na C kiingilio kitakuwa sh. 10,000 wakati kwa VIP A itakuwa ni sh. 20,000.


Hiyo itakuwa ni mechi ya mwisho ya majaribio kwa Taifa Stars inayodhaminiwa na Kilimanjaro Premium Lager kabla ya kwenda jijini Harare kwa ajili ya mechi ya marudiano ya michuano ya Afrika dhidi ya Zimbabwe (Mighty Warriors).


Malawi (Flames) inayonolewa na mchezaji wake wa zamani Young Chidmozi nayo itakuwa inacheza mechi ya mwisho ya majaribio kabla ya kwenda N’djamena kuikabili Chad.

Video ya Shaa yakamilika

VIDEO ya staa wa zamani wa kundi la WAKILISHA, Sarah Kais 'Shaa' iitwayo 'Subira' imekamilika na wakati wowote itaanza kurushwa hewani.
Meneja wa msanii huyo, Said Fella alisema video hiyo iliyorekodiwa na kampuni ya Visual Lab, chini ya Adam Juma imekamilika na kwa sasa wapo katika hatua ya mwisho ya kuanza kuisambaza tayari kwa kurushwa hewani.
Alisema video hiyo imepigwa katika maeneo mbalimbali ya jijini Dar es Salaam na haitofautiani sana na ile ya 'Sugua Gaga' ambayho imemweka matawi ya juu msanii huyo.
"Video imekamilika kupigwa picha kwa sasa inarekebishwa kidogo kabla ya kuanza kusambazwa na mashabiki wa Shaa wajiandae kupata burudani zaidi na ile ya 'Sugua Gaga'," alisema.
Aliongeza, kukamilika kwa video ya wimbo huo ni mwanzo wa maandalizi ya kazi nyingine mpya za msanii huyo aliyekuwa mmoja wa washiriki na mshindi wa shindano la Coca Cola Pop Star lililofanyika mwanzoni mwa miaka ya 2000 na yeye Witness na Langa Kileo (marehemu) waliibuka kidedea kwa Tanzania na kwenda kuchuana na wasanii wenzao wa makundi ya nchi za Kenya na Uganda.

Sikinde kutambulisha mpya TZF Kigogo

Waimbaji wa Sikinde, Abdallah Hemba, Hassan Bitchuka
Bitrchuka (kushoto) akiimba huku Adolph Mbinga akicharaza gitaa
BENDI kongwe ya muziki wa dansi ya Mlimani Park 'Wana Sikinde' keshokutwa inatarajiwa kutambulisha nyimbo mpya kwa mashabiki wa  Kigogo ikiwa ni kwa mara ya kwanza ndani ya mwaka huu.
Katibu wa bendi hiyo, Hamis Milambo aliliambia gazeti hili kuwa, Sikinde itatambulisha nyimbo hizo zitakazokuwa katika albamu yao ijayo na zile za  zamani.
Milambo alisema mashabiki wa muziki wa dansi wamekuwa wakituma maombi ya kupelekewa burudani na wao wameitikia na watafanya hivyo Jumatano.
"Sikinde inatarajiwa kufanya onyesho maalum la kutambulisha nyimbo mpya za albamu yetu ijayo pamoja na kukumbushia vibao vya zamani kwa mashabiki wetu wa Kigogo walioililia bendi yao kwa muda mrefu," alisema.
Milambo alitaja nyimbo zitakazotambulishwa kuwa ni 'Jinamizi la Talaka', 'Kibogoyo', 'Tabasamu Tamu', 'Deni Nitalipa', 'Za Mkwezi' na Nundule' ambazo zinamaliziwa kurekodiwa albamu mpya ya bendi hiyo iliyotoa albamu ya mwisho mwaka 2011.
Nyimbo za zamani zitakazopigwa katika onyesho hilo kwa mujibu wa Milambo ni 'Kassim', 'Selina', 'Salam kwa Wazazi', 'Mv Mapenzi', 'Supu Imetiwa Nazi', 'Maisha Mapambano', 'Edita', 'Naomi' na 'Clara'.
"Yaani itakuwa bandika bandua kwa nia ya kusuuza nyoyo za mashabiki wetu ambao walitukosa kwa muda mrefu," alisema.

Utata pambano la Nyilawila, Mbelwa kuamuliwa na jopo

Said Mbelwa na Karama Nyilawila wakichuana Jumamosi kabla ya kutibua pambano lao
WAKATI hatma ya mshindi wa pambano la kimataifa kuwania mkanda wa UBO ikitarajiwa kuamuliwa chini ya jopo la mashirikisho ya ngumi Tanzania na UBO, Oganaizesheni ya Ngumi za Kulipwa Tanzania (TPB)-Limited) imelaani kitendo kilichofanywa na bondia Said Mbelwa kumpiga Karama Nyilawila nje ya ulingo.
Mbelwa alimsukuma na kutupa nje ya ulingo mpinzani wake kabla ya kumrukia miguu miwili wakati wa pambano lao lililochezwa kwenye ukumbi wa Friends Corner, Manzese kwa kilichodaiwa kukerwa kupigwa kichwa na mpinzani wake.
Kitendo hicho kilipelekea pambano hilo kuvunjika katika raundi ya 8 kati ya 10 zilizokuwa zichezwe na mpaka sasa wasimamizi wa pambano hilo wameshindwa kumtangaza mshindi.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Ngumi za Kulipwa Tanzania (PST), Anthony Rutta aliiambia MICHARAZO kwa njia ya simu jana kuwa wameshindwa kutangaza mshindi mpaka jopo la wadau wa ngumi wakutane kujadili tukio hilo kwa kina.
"Tunamsubiri  Rais wa PST, Emmanuel Mlundwea ambaye ni Mwakilishi wa UBO-Afrika, arejee toka Thailand na kuitisha kikao cha jopo la wadau wa ngumi ikihusisha vyama vya PST, TBBO na TPBC kujadili kilichotokea na kutoa maamuzi kwa sasa nahofia kusema lolote," alisema Rutta.
Alipoulizwa juu ya kanuni na sheria kwa bondia anayeanzisha fujo kwenye ulingoni kwa namna yoyote na kuvuruga pambano adhabu yake huwa ni nini, Rutta alisema huwa si chini ya kifungo cha miezi 6 cha kutocheza ngumi.
"Atalkayebainika anaweza kufungiwa kati ya miezisita na miaka miwili na mpinzani wake kupewa ushindi kulingana na itakavyobainika nani mkosa," alisema.
Hata hivyo, Rais wa TPBO-Limited, Yasin Abdallah 'Ustaadh' waliosimamia pambano ya utangulizi siku ya pambano hilo la Nyilawila na Mbelwa alilaani tukio hilo na kuelekeza lawama zake kwa Mbelwa kuwa hakufanya uungwana.
"TPBO tunalaani kilichofanywa na Mbelwa, kwani siyo uungwana hata kama mwamuzi na mpinzani wake hawakumtendea haki kwenye ulingoni, mambo haya ndiyo yanayovuruga mchezo wetu na kuonekana wa kihuni," alisema.
Ustaadh alisema pia anashangazwa mtandao wa UBO kutoa taarifa mechi hiyo haina mshindi wakati mwakilishi wake, Emmanuel Mlundwa yupo nje ya nchi na hakuwepo kwenye pambano hilo.
"Sidhani kama ni sahihi, Mlundwa hakuwepo ukumbini, ila mtandao wao umetoa ripoti kuwa mchezo hauna mshindi, nani aliyetoa taarifa hizo wakati mwakilishi yupo Thailand," alisema Ustaadh na kuoingeza;
"Kama ingekuwa ni  sisi TPBO moja kwa moja trungemtangaza Nyilawila kuwa mshindi kwa sasa kilichofaywa na mpinzani wake kipo nje ya kanuni na sheria ya ngumi na TPBO tunalaani kwai inatuvurugia sana ngumi zetu," alisema.

Wakazi King'ongo wachimbwa mkwara, kisa michango ya Ulinzi

Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa King'ongo, Demetrius Mapesi
UONGOZI wa Serikali ya Mtaa wa Kimara-King'ongo, kata ya Saranga wilaya ya Kinondoni umewachimba mkwara wakazi wake ambao watashindwa kulipa Sh 3,000 kwa ajili ya Ulinzi Shirikishi ukisema ni suala muhimu kwa taifa.
Mkwara huo umetolewa na Mwenyekiti wa mtaa huo, Demetrius Mapesi katika mkutano uliowahusisha wajumbe wa nyumba 10 na baadhi ya wakazi wa mtaa huo uliohudhuriwa na Mkuu wa Kituo cha polisi Kimara Mwisho, Mfaume Msuya.
Mapesi alisema suala la ulinzi shirikishi ni la lazima kwa kila mkazi wa eneo hilo na wale wasioweza  kushiriki kulinda watalazimika kulipa kiasi hicho cha fedha kitakachohusisha kila kaya kwa ajili ya  kuwalipa walinzi watakaoshiriki kufanya doria usiku.
Mwenyekiti huyo alisema kumekuwa na kusuasua kwa zoezi hilo kutokana na wakazi wengi kutolipa  fedha hizo kwa kisingizio cha kuwa na walinzi wao katika maduka na nyumba zao, kitu alichodai hata wao wanalazimika kulipa fedha hizo la sivyo watachukuliwa hatua kali za kisheria.
Alisema moja ya hatua ni kuwafikisha polisi kabla ya kuburuzwa mahakama ya Jiji ambako watakutana na na adhabu ya kifungo pamoja na fidia kisichopungua Sh 50,000.
"Wenyewe mmesikia ripoti ya kamati ya ulinzi ambayo kati ya walinzi 20 waliokuwa wakilinda awali  wamesalia wanne tu kutokana na kusuasua kupatikana kwa malipo ya kuwalipa posho, sasa  tunaweka wazi kwamba suala hili siyo hiari, ni  lazima na atakayekiuka atachukuliwa hatua," alisema.
Alisema kuwa, ulinzi huo umekuwa ukisaidia kuweka mtaa wao salama dhidi ya wahalifu na kuwataka  wananchi kuuunga mkono uongozi wao, kwani ni kwa faida yao kwani uhalifu ukipungua inawapa  nafasi ya kufanya shughuli zao kwa ufanisi na kwa amani.
Hata hivyo Mwenyekiti huyo aliwakanganya wananchi kwa kueleza kila kichwa kitalazimika kulipa kiasi hicho cha fedha wakiwamo wapangaji na wenye nyumba wanaoishi katika mtaa huo.
Katika kusisitizia mkwara huo, Mkuu wa Kituo cha Kimara, Mfaume Msuya alisema kituo chake  kimejenga eneo kubwa la kuweza kuwasweka wale watakaofikishwa hapo kwa ajili ya kosa hilo la  kutolipa fedha hizo za ulinzi shirikishi.
"Wasiolipa waleteni kwangu, nitawahifadhi kabla ya kuwafikisha mahakamani na ninashukuru kwa sasa  eneo la Kimara uhalifu umepungua kwa sababu ya ulinzi shirikishi kwa sasa kesi nyingi ni za fumanizi  na masuala ya mapenzi, kwa nini tuwachekee wanaokwamisha ulinzi huo," alisema Afande Msuya na  kufafanua kuwa sheria namba 82 ya ulinzi ndiyo itakayowashughulikia wakwepaji hao.

Masai ya Wapi anayejitoa kundini?!

Masai katika pozi
Masai Nyota Mbof

WAKATI akiwa mbioni kuachia video ya wimbo wake mpya uitwao 'Masai ya Wapi' alioimba na Christian Bella, mchekeshaji maarufu nchini, Gilliad Severine 'Masai Nyota Mbofu' ametangaza kujiengua Al Riyami Production.
Akizungumza na MICHARAZO, Masai anayetamba na nyimbo za 'Rungu na Mukuki' na 'Yero Masai' aliouachia hivi karibuni, alisema ameamua kujiengua Al Riyami inayoendesha vichekesho vya 'Vituko Show' kutokana na kutoridhishwa na hali ya mambo na sasa atajitegemea hadi atakapotua kundi au kampuni nyingine ya uigizaji.
Masai alisema kuondoka kwake hakuna maana kama kuna ugomvi na yeyote ila ameamua kubadilisha upepo na kujikita zaidi kwenye  muziki, japo ataendelea kucheza filamu kwa yeyote atakayemhitaji.
Kuondoka kwa Masai kumezidi kulidhoofisha kundi hilo kwani kabla ya hapo wakali kama akina KItale, Mzee Majuto, Kingwendu, Ringo na Gondo Msambaa nao walijeingua kwa nyakati tofauti, huku wasanii wengine wakipunguzwa kundini humo kwa sababu mbalimbali.
Kuhusu kazi yake mpya, Masai alisema kwa sasa anajiandaa kuitoa hadharani video ya wimbo wa 'Masai ya Wapi'.
Alisema amepanga kutoa video tu wa wimbo huo bila 'audio' yake kwa sababu zake na kwamba kazi hiyo mpya ameimba kwa kushirikiana na Christian Bella.
"Wakati video ya wimbo wangu wa 'Yero Masai' ikianza kubamba katika runinga, nipo katika maandalizi ya mwisho ya kukamilisha na kuiachia video nyingine ya wimbo wa 'Masai ya Wapi', huu sitatoa 'audio' yake," alisema Masai.

10 kuwania taji la Miss B'moyo 2014, Mapacha Wa3 kunogesha

Washindi wa Miss Bagamoyo kwa mwaka jana wakiwa katika pozi
BENDI ya muziki wa dansi ya Mapacha Watatu wanatarajiwa kuwasindikiza warembo 10 watakaokuwa wakiwania taji la urembo la wilaya ya Bagamoyo 'Miss Bagamoyo 2014' katika shindano litakalofanyika siku ya Jumamosi wilayani humo.
Mratibu wa shindano hilo, Awetu Salim, Mkuregenzi wa Asilia Decoration, aliliambia MICHARAZO
kuwa, shindano hilo litafanyika kwenye ukumbi wa hoteli Palme Tree Village wilayani humo na maandalizi yote yamekamilika na warembo wanaendelea na kambi yao mjini humo kujiandaa na mchuano huo.
Awetu alisema warembo hao watakaosindikizwa na burudani toka bendi ya Mapacha Watatu chini ya Khaleed Chuma 'Chokoraa' na Jose Mara watachuana kurithi taji hilo linaloshikiliwa kwa sasa na Elizabeth Pertty aliyetwaa katika shindano la mwaka jana (2013).
Mratibu huyo aliwataja warembo watakaochuana hiyo Jumamosi kwa jina moja moja kuwa ni; Faith, Dora, Glory, Susan, Khadija, Princess, Nkyali, Manka, Amina na Zena.
"Shindano la Miss Bagamoyo 2014 litafanyika siku ya Jumamosi ya Mei 31 jumla ya warembo 10 watachuana kuwania taji hilo na nafasi za ushiriki wa michuano ya Miss Pwani 2014, tayari tumefanikiwa kupata wadhamini kadhaa baadhi ni Chama cha Wavuvi wilaya ya Ukerewe, Duran Sound, Palme Tree Village, D'z Restaurant and Take Away," alisema Awetu.
Awetu alisema warembo watatu wa kwanza licha ya kupata zawadi, lakini wataingia kwenye kinyang'anyiro cha kushiriki shindano la Miss Pwani litakalofanyika baadaye mwaka huu.

Simanzi tena:Rachel 'Recho' Haule wa Bongo Movie afariki

MUIGIZAJI aliyekuwa anazidi kuja juu katika Bongo Movie, Rachel Haule 'Recho' afariki asubuhi hii Muhimbili Hosp, Dar es Salaam baada ya kujifungua kwa upasuaji, ambapo mtoto alifariki tangu jana.
Kwa mujibu wa taarifa zilizothibitishwa na muigizaji mwenzake, Zuwena Mohammed 'Shilole', Recho alikumbwa na mauti hayo na kwa sasa wanajipanga kukutana Leaders kwa ajili ya kujua taratibu za mazishi za msanii mwenzao ambaye alikuwa katika hali mbaya tangu alipofanyiwa upasuaji kiasi cha kukimbizwa ICU kabla ya kukumbwa na mauti asubuhi hii.
Kifo cha Recho kimekuja ndani ya wiki moja baada ya kufariki kwa msanii mwingine wa Bongo Movie Adam Kuambiana , huku pia fani ya sanaa ikishuhudiwa ikimpoteza mwanamuziki Amina Ngaluma 'Japanese' aliyefariki nchini Thailand aliyezikwa siku ya Jumamosu.
MICHARAZO inatoa pole kwa ndugu, jamaa na familia ya marehemu Recho na Bongo Movie kwa ujumla kwa kuwataka kuwa na subiora katika kipindi hiki kigumu kwa kutambua kuwa kila Nafsi itaonja Mauti, yeye katangulia sisi tu nyuma yake.