STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Tuesday, May 27, 2014

Wakazi King'ongo wachimbwa mkwara, kisa michango ya Ulinzi

Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa wa King'ongo, Demetrius Mapesi
UONGOZI wa Serikali ya Mtaa wa Kimara-King'ongo, kata ya Saranga wilaya ya Kinondoni umewachimba mkwara wakazi wake ambao watashindwa kulipa Sh 3,000 kwa ajili ya Ulinzi Shirikishi ukisema ni suala muhimu kwa taifa.
Mkwara huo umetolewa na Mwenyekiti wa mtaa huo, Demetrius Mapesi katika mkutano uliowahusisha wajumbe wa nyumba 10 na baadhi ya wakazi wa mtaa huo uliohudhuriwa na Mkuu wa Kituo cha polisi Kimara Mwisho, Mfaume Msuya.
Mapesi alisema suala la ulinzi shirikishi ni la lazima kwa kila mkazi wa eneo hilo na wale wasioweza  kushiriki kulinda watalazimika kulipa kiasi hicho cha fedha kitakachohusisha kila kaya kwa ajili ya  kuwalipa walinzi watakaoshiriki kufanya doria usiku.
Mwenyekiti huyo alisema kumekuwa na kusuasua kwa zoezi hilo kutokana na wakazi wengi kutolipa  fedha hizo kwa kisingizio cha kuwa na walinzi wao katika maduka na nyumba zao, kitu alichodai hata wao wanalazimika kulipa fedha hizo la sivyo watachukuliwa hatua kali za kisheria.
Alisema moja ya hatua ni kuwafikisha polisi kabla ya kuburuzwa mahakama ya Jiji ambako watakutana na na adhabu ya kifungo pamoja na fidia kisichopungua Sh 50,000.
"Wenyewe mmesikia ripoti ya kamati ya ulinzi ambayo kati ya walinzi 20 waliokuwa wakilinda awali  wamesalia wanne tu kutokana na kusuasua kupatikana kwa malipo ya kuwalipa posho, sasa  tunaweka wazi kwamba suala hili siyo hiari, ni  lazima na atakayekiuka atachukuliwa hatua," alisema.
Alisema kuwa, ulinzi huo umekuwa ukisaidia kuweka mtaa wao salama dhidi ya wahalifu na kuwataka  wananchi kuuunga mkono uongozi wao, kwani ni kwa faida yao kwani uhalifu ukipungua inawapa  nafasi ya kufanya shughuli zao kwa ufanisi na kwa amani.
Hata hivyo Mwenyekiti huyo aliwakanganya wananchi kwa kueleza kila kichwa kitalazimika kulipa kiasi hicho cha fedha wakiwamo wapangaji na wenye nyumba wanaoishi katika mtaa huo.
Katika kusisitizia mkwara huo, Mkuu wa Kituo cha Kimara, Mfaume Msuya alisema kituo chake  kimejenga eneo kubwa la kuweza kuwasweka wale watakaofikishwa hapo kwa ajili ya kosa hilo la  kutolipa fedha hizo za ulinzi shirikishi.
"Wasiolipa waleteni kwangu, nitawahifadhi kabla ya kuwafikisha mahakamani na ninashukuru kwa sasa  eneo la Kimara uhalifu umepungua kwa sababu ya ulinzi shirikishi kwa sasa kesi nyingi ni za fumanizi  na masuala ya mapenzi, kwa nini tuwachekee wanaokwamisha ulinzi huo," alisema Afande Msuya na  kufafanua kuwa sheria namba 82 ya ulinzi ndiyo itakayowashughulikia wakwepaji hao.

No comments:

Post a Comment