STRIKA

STRIKA

USILIKOSE

USILIKOSE

Wednesday, May 8, 2013

Unamkumbuka mcharaza gitaa huyu Alain Dekula Kahanga 'Vumbi?

 
Mwanamuziki nyota aliyewahi kutamba na bendi kadhaa nchini ikiwamo Orchestra Marquiz Original 'Wana Sendema' akiwa ni mtunzi, muimbaji na mcharaza gitaa la solo unajua kafanya nini nchini Sweden anakoendelea na fani yake ya muziki? Fuatilia Blog hii ya MICHARAZO MITUPU upate majibu ya kitu gani amekifanya ughaibuni.

MWALIMU AUAWA BAADA YA KUZINI NA MKE WA ASKOFU


Kakamega, Kenya
KUNDI la watu wenye hasira huko Kakamega  lilimpiga hadi kumwua mwalimu ambaye alibambwa akifanya mapenzi na mke wa askofu.


Askofu huyo alikuwa akiendesha ibada ya mazishi kijijini Tomboo, Jimbo la Malava.

Mkuu wa Wilaya ya Kakamega Kaskazini,  Gideon Ombongi , alisema mwalimu huyo na mke wa askofu walitoroka kwenye mazishi na kuingia nyumbani kwa askofu huyo ambapo ni mita chache tu kutoka mazishini.

Baada ya kukamilisha ibada ya mazishi, askofu aliingiwa wasiwasi na kuamua kumtafuta mkewe alipokwenda. Alipofika nyumbani kwake aliwakuta wawili hao wakifanya mapenzi jikoni.

Mapigano yalitokea kati ya askofu na mwalimu huyo ambapo mwanamke alikimbia.

Mkuu wa Polisi wa Kakamega Kaskazini, Justus Kitetu, alisema mapigano hayo yalivutia watu ambao walijaa kwenye nyumba ya askofu.

“Askofu aliwaambia wanakijiji kilichokuwa kimetokea nao wakampiga mwalimu na kumwua,” alisema na kuongeza kwamba askofu amekatwa kwa uchunguzi.  Mke wa askofu naye alikamatwa lakini aliachiliwa.

Chanzo:Mpekuzi Huru

Simba yaipumulia Azam, Chanongo apeleka furaha Msimbazi


Mfungaji wa bao pekee la Simba leo, Haruna Chanongo (kushoto)
BAO pekee lililotumbukizwa wavuni na mshambuliaji anayezidi kuja juu nchini, chipukizi Haruna Chanongo limeiwezesha Simba kuibuka kidedea mbele ya Mgambo JKT ya Tanga katika pambano lililochezwa kwenye uwanja wa Taifa, jijini Dar es salaam jioni ya leo.
Ushindi huo ambao ni wa tatu mfululizo kwa Simba tangu walipojipanga upya wakizima 'mgogoro' uliokuwa ukifukuta chinichini klabuni kwao, imeifanya ifikishe pointi 45 na kutishia usalama wa Azam waliopo nafasi ya pili kwa muda mrefu katika msimamo wa Ligi Kuu Tanzania Bara.
Azam ambayo imesaliwa na michezo miwili mkononi yenye ina pointi 48, tatu pungufu na ilizonazo Simba japo yenye imesaliwa na mechi mbili mkononi kabla ya kuhitimisha msimu wa 2012-2013.
Haruna Chanongo alifunga bao hilo pekee katika kipindi cha kwanza katika dakika ya 8 tu ya mchezo huo baada ya kuwafungisha tela mabeki wa Mgambo kabla ya kufunga bao tamu lililoihakikishia Simba kukalia nafasi ya tatu na ikiinyemelea nafasi ya pili ya uwakilishi wa michuano ya kimataia mwakani iwapo itaifunga Yanga na Azam iteleze kwenye mechi zake ilizosaliwa nazo.
Kwa kipigo hicho cha leo, Mgambo imeendelea kupumulia mashine na kuziipa afueni Toto Africans na Polisi Moro katika hatari ya kushuka daraja, kwani maafande hao wanahitaji pointi moja tu kutoka baraka kwa wapinzani wao hao wawili waliopo nao mkiani kuteremka daraja wakiunga na Africana Lyon.
Timu hiyo itashuka dimbani Jumamosi jijini Dar es Salaam kuvaana na Azam katika mechi nyingine inayotabiwa kuwa ngumu kwao, ambako siku hiyo pia kwenye uwanja wa Kaitaba mjini Bukoba, wenyeji Kagera Sugar watawakaribisha Ruvu Shooting.
Katika pambano la leo vikosi vya timu hizo vilikuwa kama ifuatavyo:
Simba: Juma Kaseja, Nassor Masoud 'Chollo', Haruna Shamte, Miraji Adam, Hassan Khatib, Jonas Mkude, Edward Christopher, William Lucian, Amri Kiemba, Ramadhan Chanongo 'Messi' na Haruna Chanongo.
Mgambo JKT; Godson Mmassa, Salum Mlima, Ramadhan Kambwili, Bashiru Chanacha, Bakari Mtama, Salum Kipanga, Chande Magoja, Peter Mwalyanzi, Issa Kandulu, Fully Maganga na Nassor Gumbo.

Victor Ambrose ndiye aliyerusha bomu kanisani


DEREVA wa pikipiki maarufu kama bodaboda, Victor Ambrose, anatuhumiwa kurusha bomu katika Kanisa Katoliki la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi, Parokia ya Olasiti jijini Arusha, lililosababisha vifo vya watu wawili na wengine karibu 70 kujeruhiwa.

Ambrose mwenye umri wa miaka 20 na mkazi wa Kwa Mrombo, Arusha, anashikiliwa pamoja na watuhumiwa wengine tisa, wakiwemo raia wanne wa Saudi Arabia kwa mahojiano zaidi ya kuhusika na tukio hilo.

Taarifa zilizopatikana jana jioni, zilieleza kuwa raia hao wa Saudi Arabia, waliingia nchini Jumamosi usiku kwa ndege kupitia Uwanja wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA), na baada ya tukio Jumapili, waliondoka nchini kupitia mpaka wa Tanzania na Kenya, Namanga.

Serikali kupitia kwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Dk Emmanuel Nchimbi, ilitoa taarifa hiyo jana bungeni na kueleza namna uhalifu huo ulivyotendeka kanisani hapo juzi, muda mfupi baada ya ibada kuanza.

Kwa mujibu wa Waziri Nchimbi, uchunguzi wa awali unaonesha kuwa mlipuko huo ni bomu. Hata hivyo uchunguzi wa kubaini aina ya bomu lililotumika, unaendelea kufanywa na Polisi na wataalamu wa Jeshi la Ulinzi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ).

“Hadi sasa watuhumiwa sita wanashikiliwa na Jeshi la Polisi. Miongoni mwao ni Victor Ambrose mwenye umri wa miaka 20 dereva wa bodaboda...ambaye anatuhumiwa kurusha bomu hilo. “Watuhumiwa wengine watano waliokamatwa ni raia wa kigeni na Mtanzania mmoja ambao wanashikiliwa kwa mahojiano,” alisema Dk Nchimbi.

Waziri alitaja waliokufa katika tukio hilo kuwa ni mtoto mwenye umri wa miaka 16, James Gabriel, aliyefariki usiku wa jana na Regina Kurusei (45), mkazi wa Olasiti aliyefariki siku ya tukio wakati akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Mount Meru.

Hata hivyo, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Magesa Mulongo, alisema waliokamatwa wamefikia 10, na raia hao wa nje ni wa Saudi Arabia.

Alisema pia mtu wa tatu alifariki lakini hakumtaja jina. Kaimu Mganga Mkuu wa Hospitali ya Mount Meru, Dk Mariam Murktadha, alifafanua kuwa kijana Gabriel, alifia Uwanja wa Ndege wa Arusha, akiwa njiani kupelekwa Hospitali ya Taifa ya Muhimbili kwa matibabu zaidi.

Aliongeza kuwa majeruhi walikuwa 66 na hivi sasa wamebaki 34 na wengine wameruhusiwa.

Kwa mujibu wa Dk Nchimbi, majeruhi walikimbizwa Hospitali ya Mount Meru, wengine Hospitali ya St Elizabeth kwa Father Babu, Hospitali ya Selian na mwingine alipelekwa katika Hospitali ya Dk Wanjara, Mianzini.

Bomu lilivyorushwa

Akielezea tukio hilo, Waziri Nchimbi alisema lilirushwa wakati mgeni rasmi, Balozi wa Vatican nchini na Mjumbe wa Baba Mtakatifu, Askofu Fransisco Padilla, akiwa ametoka nje ya kanisa akijiandaa kukata utepe kama ishara ya uzinduzi.

Alisema mtu huyo alirusha kitu chenye ukubwa wa ngumi, kwenda eneo kulipokuwa na mkusanyiko wa watu na baada ya kutua, kulitokea kishindo na mlipuko mkubwa. Inakadiriwa uzinduzi huo wa Kanisa, ulihudhuriwa na watu zaidi ya 2,000.

Alisema viongozi wa dini na Serikali waliohudhuria ibada hiyo, hawakupata madhara yoyote kutokana mlipuko huo.  Amewasihi Watanzania kuwa watulivu wakati vyombo vya dola vikiwasaka walihusika na shambulio hilo.

Aidha ametaka kila mwenye taarifa za kuwezesha kukamatwa wahalifu hao azitoe Polisi. Kwa mujibu wa Waziri Nchimbi, siku za hivi karibuni kumekuwepo jitihada kubwa za watu wachache wasioitakia mema nchi, kutaka kupandikiza chuki za kidini miongoni mwa Watanzania na kuleta mapigano na mauaji.

“Sina shaka kuwa shambulio la Arusha ni sehemu ya mikakati hiyo miovu,” alisema bungeni na kusisitiza kwamba Serikali itachukua hatua kali kwa mtu yeyote bila kujali hadhi na nafasi yake katika jamii.

Wanasiasa waonywa

Wakati huo huo, Waziri Nchimbi amekemea wanasiasa wanaotafuta umaarufu wa kisiasa kupitia tukio hilo, akisisitiza kwamba Serikali isilaumiwe kwa hatua kali za kisheria itakazochukua dhidi ya viongozi wa aina hiyo.

“Kokote duniani tukio la kushitukiza linalosikitisha na kuhuzunisha kama hili linapotokea, wananchi wote huungana na kuwa wamoja kama taifa na kulaani wahusika na kuwafariji waathirika wa tukio hilo,” alisema Dk Nchimbi.

Akikemea wanasiasa wanaotumia matukio kujinufaisha, huku akitoa mfano wa Marekani na kusema mgombea mmoja wa urais wakati wa uchaguzi mkuu wa mwaka 2012, aliishutumu Serikali kutokana na kulipuliwa kwa ubalozi wa Marekani nchini Libya.

“Ni wazi kuwa mgombea huyo alichukua tatizo lile kama ajenda ya kisiasa. Hata hivyo alishutumiwa vikali na Wamarekani wenzake kwa kuelezwa kuwa ni mtu mwenye kukosa kabisa misingi ya uaminifu na uzalendo kwa taifa lake.”

“Serikali inasikitishwa sana na wanasiasa wa aina hii, ambao wanajitokeza nchini na kutafuta umaarufu wa kisiasa kwa gharama za maisha ya Watanzania…Serikali isilaumiwe kwa hatua kali za kisheria itakazochukua dhidi ya viongozi wa aina hii, ambao maslahi yao ni muhimu kuliko maisha ya Watanzania,” alisema.

Dk Nchimbi alilaani waliohusika kufanya uhalifu huo na kusema Serikali kwa nguvu zote itahakikisha watuhumiwa wote waliohusika na kushiriki kwa namna yoyote katika tukio hilo, wanasakwa popote walipo na kufikishwa katika vyombo vya sheria.

“Tunawataka viongozi wa kisiasa, kidini na wananchi wote kwa ujumla kila mmoja kwa nafasi yake kuwajibika, ili kuhakikisha kuwa nchi yetu inaendelea kuwa kisiwa cha amani na utulivu,” alisema.

Imeandikwa na Stella Nyemenohi, Dodoma na Veronica Mheta, Arusha.

Source: Habari leo

REDD'S MISS KIGAMBONI KWA MWAKA 2013 KUFANYIKA JUNI 7

Miss Kigamboni 2012, Eda Sylvester (katikati) kushoto ni mshindi wa pili Agness Godluck (kulia) ni mshindi wa tatu Elizabeth Boniface, walipotangazwa washindi mwaka jana.

SHINDANO la kumtafuta mrembo wa kitongoji cha Kigamboni mwaka huu "Redd's Miss Kigamboni 2013" linatarajiwa kufanyika Ijumaa Juni 7 kwenye ukumbi wa Navy Beach kuanzia saa 2:00 usiku hapa jijini Dar es Salaam.
Tayari warembo wameshaanza mazoezi kwa ajili ya kujiandaa na shindano hilo ambapo wanajifua kwenye ukumbi wa Break Point (VIP) uliopo Posta hapa jijini.

  Mratibu wa shindano hilo, Somoe Ng'itu, alisema kuwa maandalizi ya shindano hilo yako katika hatua za mwisho na bado wanakaribisha warembo wenye sifa za kushiriki shindano hilo kufika mazoezini kutoka sehemu mbalimbali hapa nchini.

Mratibu huyo alisema kwamba lengo la kuweka wazi na kuwahamasisha warembo ni kutaka kutoa nafasi kwa wasichana wengi zaidi kujiandikisha na hatimaye kupata mshindi atakayekiwakilisha vyema kitongoji hicho katika mashindano ya ngazi ya Kanda yatakayofanyika baadaye mwezi ujao.

"Tumeshaanza maandalizi na tunawaomba wadau wa sanaa ya urembo wa hapa nchini kujiandaa kusubiri Kigamboni kutoa mrembo wa taifa mwaka huu, tunawashiriki wenye mvuto na sifa za ushindani," alisema Somoe.

Aliongeza kwamba fomu kwa ajili ya kushiriki shindano hilo zinapatikana bure na warembo wanafanya mazoezi chini ya Blessing Ngowi, ambaye mwaka juzi alishiriki fainali za taifa za Redd's Miss Tanzania na alitwaa taji la Kanda ya Elimu ya Juu.

Alisema pia makampuni na taasisi mbalimbali zinakaribishwa kudhamini shindano hilo ambalo mwaka jana lilitoa mshindi katika kinyang'anyiro cha Kanda ya Temeke ambaye ni Edda Sylivester.

Edda alifanikiwa kushika nafasi ya tatu kwenye fainali za taifa huku mshindi wa taifa ni Brigitte Alfred ambaye mwaka huu ataenda kupeperusha bendera ya nchi katika mashindano ya dunia.

HATIMAYE MAHAKAMA YAFUTIA LWAKATARE KESI YA UGAIDI


LWAKATARE

MAHAKAMA Kuu ya Tanzania leo imetangaza kuyafuta mashtaka yote ya ugaidi yaliyokuwa yanamkabili Mkurugenzi wa Ulinzi na Usalama wa CHADEMA Wilfed Lwakatare.
Taarifa kutoka Mahakama Kuu zinasema Mahakama Kuu imebakiza shitaka moja tu, la utekaji ambalo kimsingi ni Jinai na lina dhamana.
Taarifa zilizoufikia mtandao huu zinasema kuwa baada ya kufutwa kwa kesi hiyo, ziliripuka shangwe na nderemo kutoka kwa wafuasi wa Chadema waliofika mahakamani hapo kwa ajili ya kusikiliza kesi hiyo.
Katika kesi hiyo, Lwakatare alikuwa akiwakilishwa na Jopo la mawakili nguli watano ambao ni Mabere Marando,Tundu Lissu,Professor Abdallah Safari, Peter Kibatala na Naronyo Kicheere. (33).

Sir Alex Ferguson abwaga manyanya Man Uneted

Kocha wa Man United, Sir Alex Ferguson

LONDON, England
KLABU ya Manchester United imethibitisha leo Jumatano kuwa Kocha Sir Alex Ferguson atastaafu kuinoa timu hiyo mwishoni mwa msimu huu.

Ferguson atastaafu Man United akihitimisha zaidi ya robo karne ya kufanya kazi Old Trafford, akisaidia kuipa mataji 20 ya Ligi Kuu ya England hivi  karibuni. 
Fergie, 71 ameiongoza klabu kwa mafanikio ndani na nje ya uwanja, akiingiza klabu hiyo katika soko la hisa la New York Stock Exchange, huku ikikusanya maaamilioni ya mashabiki duniani kote kuanzia mwaka 1986 aliposhika hatamu.
Katika miaka yake 26 ya kuinoa Man United, Ferguson raia wa Scotland ametwaa zaidi ya mataji 30, yakiwamo 13 ya Ligi Kuu ya England – pamoja na huu iliotwaa msimu huu.
Ferguson anatarajia kuaga mashabiki wa klabu hiyo baada ya mechi ya mwisho ya Ligi Kuu msimu huu, ugenini dhidi ya West Bromwich Albion, itakayopigwa Mei 19, taarifa ya klabu ya Manchester United ilisema.
The Sun

Mikoa yatakiwa kuchezesha Coca Coca Cola wilayani


Na Boniface Wambura
Vyama vya Mpira wa Miguu vya mikoa vinatakiwa kuendelea na mashindano ya Copa Coca-Cola yanayoshirikisha watoto wenye umri chini ya miaka 15 katika ngazi ya wilaya wakati vikisubiriwa vifaa na fedha za uendeshaji kutoka kwa mdhamini.

Kwa mujibu wa kalenda ya mashindano (roadmap), mashindano ya Copa Coca-Cola ngazi ya wilaya yanatakiwa kufanyika na kukamilika ndani ya mwezi Mei mwaka huu ili baadaye kuendelea na hatua inayofuata.

Hivyo, Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF) linawataka wanachama wake (vyama vya mpira wa miguu vya mikoa) ambao wamejipanga kuendelea na mashindano wakati suala la vifaa na fedha likiendelea kufuatiliwa kwa mdhamini wa mashindano.

Vifaa na fedha zitapatikana wakati wowote baada ya taratibu husika kukamilika. Vifaa kwa ajili ya mashindano hayo vimeagizwa kutoka nje ya Tanzania.

Ni matumaini yetu kuwa tutakuwa na mashindano mazuri mwaka huu kulinganisha na msimu uliopita. Kampuni ya Coca Cola ilianza kudhamini mashindano hayo mwaka 2007, na tangu mwaka huo yamekuwa yakifanyika kila mwaka.


Simba, Mgambo hapatoshi leo Taifa


Mgambo JKT

Kikosi cha Simba
SIMBA yenye ari, nguvu na kasi mpya jioni ya leo inatarajiwa kuwakaribisha maafande wa Mgambo JKT toka Tanga pambano pambano pekee la Ligi Kuu TanzaniaBara litakalochezwa kwenye uwanja wa Taifa.
Mgambo ambao wameshatua jijini tangu majuzi imeshatangaza 'kiama' kwa 'Mnyama' kwamba wasitarajie mteremeko kama ilivyopata kwa Polisi Moro na Ruvu Shooting waliochezea vichapo na kuirejesha Simba katika nafasi ya tatu.
Kocha wa kikosi hicho cha Mgambo kilichoibania Yanga katika mechi yao ya mwisho iliyochezwa Mkwakwani, Mohammed Kampira ametamba kwamba wanachosaka leo ni pointi za kuwavusha kwenye janga la kushuka daraja.
Mgambo ina pointi 25 na inahitaji pointi moja tu ili kujihakikisha kusalia katika ligi hiyo wanayoicheza msimu huu kwa mara ya kwanza baada ya kupanda toka Ligi Daraja la Kwanza msimu uliopita.
Hata hivyo Simba imesisitiza kuwa dhamira yao ni kuhakikisha wanataka kushinda mechi zao zilizosalia kwa nia ya kulinda heshima yao baada ya kunyang'anywa ubingwa na Yanga kabla ligi haijamalizika.
Simba ambayo haina hata nafasi ya kuiwakilisha nchi mwakani katika michuano ya kimataifa, ipo nafasi ya tayu baada ya kufikisha pointi 42 na kuwaengua Kagera Sugar walioikalia nafasi hiyo kwa kipindi kirefu kidogo pale Simba ilipokuwa ikitetereka kabla ya kuamka na kurejea kwenye makali yake.
Maandalizi ya pambano hilo yamekamilika na TFF imesema mchezo huo utaanza majira ya saa 10.30 jioni na kuhimiza mashabiki kujitokeza kwa wingi kushuhudia mtanange huo wa aina yake.

Askofu Pengo awatuliza Wakatoliki mlipuko wa bomu, vifo vyaongezeka







Askofu Pengo

Baadhi ya Majeruhi wa tukio hilo akihudumiwa

WATANZANIA wametakiwa kuwa watulivu na kuachana na hisia za kunyoosheana kidole kwamba wahusika wa shambulizi la kigaidi dhidi Kanisa Katoliki la Mtakatifu Josefu Mfanyakazi, Parokia ya Olasiti, jijini Arusha Jumapili iliyopita kuwa ni Waislamu kwa kuwa watuhumiwa waliokwisha kukamatwa pia kuna Wakristo.

Kauli hiyo ilitolewa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, alipokuwa akizungumza kupitia kituo cha televisheni cha  Tumaini.

Askofu Pengo aliwataka wananchi kuacha hisia badala yake waache uchunguzi wa kubaini waliohusika uendelee ili kupata matokeo mazuri.
“Siamini kama waliofanya tukio hili baya ni Waislamu kwa kuwa watuhumiwa wanaoshikiliwa mpaka sasa wamo Wakristo, ni bora kuacha kuhisi,” alisema  Askofu Pengo.

Hii ni mara ya kwanza kwa Kardinali Pengo kuzungumzia shambulizi hilo baya la bomu ambalo limeibua hisia kali miongoni mwa jamii kwani ni kwa mara ya kwanza kanisa linapigwa bomu kwa mbinu zinazodhihirisha kuwa ni harakati za kigaidi.

WASAUDI WALIINGIA NCHINI MEI 4
Pengo akiweka msimamo huo, NIPASHE imefahamishwa kuwa raia wanne wa Saudi Arabia waliokamatwa kwa tuhuma za kuhusika ugaidi dhidi ya Parokia ya Olasiti, walilala katika hoteli moja iliyopo jirani na stendi kuu ya mabasi ya kwenda na kutoka mikoani.

Uchunguzi wa NIPASHE umebaini kuwa watuhumiwa hao waliingia nchini kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Kilimanjaro (KIA) Mei 4, mwaka huu, na baada ya tukio la mlipuko wa bomu hilo walianza safari ya kutoroka nchini kupitia mpaka wa Tanzania na Kenya wa Namanga.

Habari zinasema kuwa watuhumiwa hao walikamatwa na vyombo vya usalama karibu na maeneo ya mzunguko wa Forida katika barabara itokayo Mianzini kwenda katikati ya jiji.

VIFO VYAFIKA WATU WANNE
Katika hatua nyingine, majeruhi mwingine wa mlipuko huo, Isabela Michael (19), amefariki dunia katika Hospitali ya Mtakatifu Elizabeth, maarufu kama ‘kwa babu’ jana.

Taarifa  hizo zilizotolewa na Mganga Mkuu wa Hospitali ya St. Elizabeth, Goodluck Kwayu mbele ya Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu jana.

Kifo cha Isabela ambaye mama yake mzazi naye yupo mahututi hospitalini hapo, kinafanya idadi ya watu waliokufa kutokana na shambulizi kufikia wanne.

Juzi waliotajwa kufariki dunia ni Regina Longino Kurusei (45) na James Gabriel (16) pamoja na majeruhi mwingine ambaye jina lake halikutajwa.

Katika tukio hilo, zaidi ya watu 66 walijeruhiwa na kulazwa katika Hospitali ya Mkoa wa Arusha ya Mount Meru, Hospitali binafsi ya Selian na St. Elizabeth.

Akizungumza katika Hospitali ya Mount Meru baada ya kuwatembelea majeruhi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar, Balozi Seif Ali Idd, alilaani tukio hilo na akawataka Watanzania kuwa tukio hilo lisiwagawe Wakristo na Waislamu.

Alisema Wakristo na Waislamu kwa miaka mingi wamekuwa wakishirikiana kama ndugu, hivyo ni vyema ushirikiano huo ukaendelea.

“Tukio hili lisitugawe Wakristo na Waislamu, tuna historia ya muda mrefu ya kushirikiana vizuri,” alisema.

Balozi Idd aliwataka Watanzani kuwa watulivu wakati vyombo vya ulinzi na usalama vikifanya kazi ya uchunguzi wa tukio hilo na kuwanasa wahusika.

MAALIM SEIF: TUMESIKITISHWA
Naye Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif Sharrif Hamad, ambaye aliwatembelea majeruhi hao, alisema Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) na Chama cha Wananchi (CUF) wanalaani vikali tukio hilo.

“SMZ na CUF tumesikitishwa na kulaani tukio hilo la uhalifu na ugaidi wa hali ya juu kufanyika hapa nchini,” alisema.

Aliwaomba Watanzania kuwa watulivu na akawaomba wananchi ambao wana taarifa kuhusiana na watu waliohusika kwenye tukio hilo kutoa taarifa hizo kwa vyombo vya dola.

TAARIFA YA PINDA BUNGENI
Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, amesema tukio hilo si jambo la kushabikiwa kisiasa.
Alitoa kauli hiyo jana bungeni mara baada ya kurejea kutoka Arusha alikokwenda kutembelea eneo la tukio, baada ya Spika wa Bunge, Anne Makinda, kumpa nafasi ya kutoa taarifa fupi ya safari yake.

Alisema kwa bahati mbaya wapo baadhi ya viongozi wachache wanapitapita eneo la tukio na badala ya kutumia wananchi kuzungumza nao wanaingiza visiasaisa. “Naomba sana jambo hili tusilitumie kwa namna hiyo.”

Pinda alisema uchunguzi bado unaendelea, wamekamatwa watu wanane, wanne ni watu wenye asili ya kutoka Uarabuni, watatu ni Watanzania ambao wameanza kuhojiwa katika vuguvugu la jambo hilo.

Alisema raia wanne wa Kenya ambao walikamatwa ni kwa sababu tu ya kutaka kujiridhisha kwa kuwa wako Arusha siku moja kabla na siku ya tukio ndipo walipoanza safari ya kwenda Nairobi.

“Kwa sababu barabara zile zilikuwa zimeshafungwa, isingewezekana wao kupita kiurahisi bila kuhojiwa kwa maana ya kujiridhisha. Ni matumaini yetu kuwa pengine taarifa itatoka mapema leo (jana) au kesho (leo) kwa sababu wameanza tangu jana kuzungumza nao kama wanahusika kwa namna moja au nyingine.

Wengine bado uchunguzi na mahojiano yanaendelea.” Alisema alipofika Arusha alikuta wananchi wameshatulia na eneo la tukio palikuwa na utulivu, ingawa watu walihamaki, lakini wamefarijika na hatua za serikali za kufanya uchunguzi mara moja.

Alisema hospitalini katika majeruhi 66, walioruhusiwa ni 24 waliobaki wanaendelea kuuguzwa katika hospitali mbalimbali, wengi wao wapo Mount Meru.

Alisema sehemu kubwa ya wale walioathirika wameshafanyiwa upasuaji kwa ajili ya kutoa vipande vya vyuma vilivyokuwa vimewaathiri.

“Wengi tumewakuta wako katika hali nzuri, wengine leo (jana) watapelekwa katika chumba cha upasuaji na wengine inawezekana kesho (leo).”

Alisema wamewaomba madaktari vile vipande vya vyuma vikipatikana wasivitupe wakabidhi kwa vyombo vya dola ili waweze kubaini kama bomu lile la mkono limetengenezwa kienyeji au lililotengenezwa viwandani na kwa hiyo ni bomu linalotokana na jeshi. “Tutaweza kubaini chimbuko la bomu hilo ni nini.”

Wakati uchunguzi ukiendelea, Waziri Mkuu alisema wamewaomba wakazi wa Arusha yeyote mwenye taarifa ambazo zinaweza kusaidia za kubaini kwa uhakika juu ya nani kafanya jambo hilo na kwanini ajitokeze.

WABUNGE:  AMANI KWA GHARAMA YOYOTE
Baadhi ya wabunge wamewataka Watanzania kuungana, kuepuka tofauti zao za kiitikadi, dini na viongozi kunyoosheana vidole ili amani ilindwe kwa gharama yoyote.

Wakichangia mjadala wa hotuba ya Bajeti ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi jana, wabunge wengi waliochangia mjadala huo walisema  tukio la Arusha limeishtua nchi na dunia na  kilichotokea huko si utamaduni, desturi na jambo lililozoeleka kwa Watanzania.

Waliwaomba Watanzania wajikumbushe yaliyotokea Rwanda kwani mgogoro ule kwa kiasi kikubwa ulisababishwa na kauli. Mbunge wa Kuteuliwa, James Mbatia (NCCR-Mageuzi), alisema ni mambo ya kusikitisha kwa kuwa taifa ni la Watanzania.

Alisema janga likitokea inabidi Watanzania wote bila kujali imani, dini wala itikadi wawe wamoja.

“Amani inabidi ilindwe kwa gharama yoyote ile. Chochoko zilizozama miongoni mwa Watanzania kwa kauli za baadhi ya viongozi na Watanzania,” alisema.

Alisema Serikali haina dini na kila mtu ana imani yake ya dini, lakini leo unaweza kumpigia kiongozi wa serikali, hata askari simu mlio wake ni wa nyimbo za dini.

“Ningeomba kuanzia leo milio ya simu ya dini tuiondoe inasambaratisha Watanzania. Tuko wapi na tunaipeleka wapi. Naomba kwa moyo wa dhati mihadhara ya kidini iliyodumu kwa zaidi ya miaka 20 tuseme basi imetosha,” alisema.

Alihoji serikali inashindwaje kufanya maamuzi huku akinukuu maneno ya falsafa yanayosema ukiona maovu yanatokea, kemea, zuia. Alisema ukumbi wa Bunge ni baraza, lakini limefanywa la matusi.

Alishauri Watanzania wawe na utulivu na watafakari pamoja.

“Watanzania, viongozi wa dini tusiwe wepesi kuonyesheana vidole, mauaji ya padre, viongozi wamekata tamaa, wamesema sasa tumechoka.

Tusiwaruhusu viongozi wetu watupeleke huko,” alisema na kuongeza: “Ndimi zetu kauli zetu zitaliangamiza taifa la Tanzania. Tumefika mahali Tanzania tuseme basi.”

Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Shamsa Vuai Nahodha, akichangia mjadala huo alisema, ni kawaida kwa viongozi kulaumiana na kumtafuta mchawi.

Alisema viongozi wenye busara kama hawa hawapaswi kulaumu watu linapotokea tatizo kama hilo. Alisema ajenda iliyopo mbele ni tatizo la kuvurugika kwa amani.

“Huu si wakati wa kulaumiana ni wakati kujenga mshikamano wa kuwatafuta waliohusika na tukio hili.”

Alisema sifa ya uongozi ni kukubali ukweli hata kwa mambo ambayo hawayapendi. “Kuna mahali sisi viongozi tumekosea. Unaposikiliza mijadala ya wabunge, wakati mwingine kauli zetu haziashirii mema. Na hatuwezi kushangaa haya yanayotokea,” alisema.

Aliongeza kuwa kiongozi anaposema jambo ni lazima apime kwani Tanzania ni nchi changa ina miaka 50 tu na kutokana na kiwango cha elimu na uwezo wa kuchanganua mambo ni mdogo.

“Tujikumbushe yaliyotokea Rwanda. Mgogoro ule kwa kiasi kikubwa ulisababishwa na kauli.

Waswahili husema watu makini na wenye busara hujifunza. Najua ni ngumu sana mwanadamu kubadilika na kuacha mambo ambayo ameyazoea,” alisema.

Mbunge wa Rombo, Joseph Selasini (Chadema), alisema tukio la Arusha limeishtua nchi na kilichotokea Arusha siyo utamaduni, desturi na halijazoeleka kwa Watanzania.

“Nitoe wito kwa wabunge na Watanzania wote kuwa huu si wakati wa kutupiana lawama.

Katika jambo hili lazima tuhakikishe kwamba tunashirikiana kurejesha utulivu katika jiji la Arusha. Lazima tuchunge ndimi zetu, viongozi pamoja na sisi wananchi.

Tuanzie hapa bungeni. Hakuna sababu ya kuanza kunyoosheana vidole, kwamba jambo hili ni la kisiasa au la kidini. Mwenye kuhisi hivyo ashirikiane na tume ya uchunguzi kuwabaini,” alisema.

Alisema sheria zimetungwa na zipo, lakini kuna woga wa kuzitumia. Mtu mwenye uhakika kwamba ni la kidini au la kisiasa kwa nini asitoe ushahidi?”

Aliongeza kuwa jambo hili linafundisha kuwa nchi haiko salama, Watanzania wamegawanyika kwa sababu hiyo ni rahisi kutumiwa na maadui.

“Baadhi yetu tunasema jambo hilo limesababishwa na kundi fulani. Hatuko salama. Hakuna mashehe au maaskofu wanaotengeneza makundi kutukana wenzao.

Lakini naamini kuna kundi la wahuni wanaofanya hivyo. Sababu gani hawakamatwi, tunawaogopa nini. Nyinyi polisi ndiyo mnatoa vibali vya mikutano ya kutukana watu. Kwa nini watu hawa hawakamatwi?” alihoji.

Alisema watu wamefikia hatua ya kusimama hadharani na kushambulia kuwa chama hiki ni cha Waislamu, chama hichi ni cha Wakristo. Serikali ionyeshe ipo na weledi wake.
Aidha, alitaka Serikali itunge sheria ya kudhibiti lugha za uchochezi kwenye mikutano na majukwaa.

Mbunge wa Sumve (CCM), Richard Ndassa, alisema kutokana na matukio yanayotokea hivi sasa kuna haja ya kuimarisha ulinzi kwenye eneo la jengo la Bunge.

Alimwambia Spika wa Bunge kuwa asije kushangaa siku moja Bunge lake tukufu linavamiwa na wahuni.

“Arusha kusingekuwa na ulinzi wa kutosha hata wale waliohusika wasingekamatwa.
Kuanzia sasa huku nyuma (bungeni) mtu akirusha kitu kitafika ndani.

Watu kule nje wanatuona tunavyozungumza na tunavyosigana humu ndani. Lazima ulinzi uimarishwe,” alisema na kuongeza: “Tuzime moto kabla moto haujalipuka, anayechokozwa,  huchokozeka.”

Aidha, alipendekeza makomandoo wa Jeshi la Polisi, waongezewe muda wa kustaafu ili kutoa uzoefu kwa vijana.

Mbunge wa Viti Maalumu (Chadema), Chiku Abwao , alihoji kuhusu uchunguzi wa kutekwa kwa Mwenyekiti wa Jumuiya ya Madaktari Tanzania, Dk. Stephen Ulimboka na Mwenyekiti wa Jukwaa la Wahariri Tanzania (TEF), Absalom Kibanda, na kwamba serikali imefikia wapi kuhusiana na suala hilo.

Hamad Ali Hamad (CUF-Magogoni), alisema chama chake kimewagharimu muda mwingi kuwaambia Watanzania kuwa si chama cha kidini, lakini ilikuwa ikitumiwa kama propaganda ya kukiua.
Naibu Waziri wa Serikali za Mitaa, Tawala za Mikoa (Tamisemi), Aggrey Mwanry, alisema adui anaigawa Tanzania.

Alisema Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere, aliposema nchi hii haina dini watu hawakumuelewa.

“Taifa hili likienda likateketea, sisi hatutaacha kulaumiwa. Hapa imezungumzwa habari za dola, hiki ni chombo cha kundi ni chombo kinachoangalia tabaka. Dola ni chombo cha mabavu, akifika anabamiza. Kiwango cha mabavu kinategemea na kiwango kitakachokutwa sehemu ya tukio,” alisema.

Alisema ikifika mahali kwamba nchi haitawaliki maana yake unafika kwenye shamba la mtu unavuna mahindi unaondoka, unaenda sokoni unachukua samaki wa watu unaondoka bila kulipa, hapo ndipo utasema nchi haitawaliki.

Waziri wa Nchi, Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano) Samia Hassan Suluhu, alisema vitabu vyote vya dini havina maamrisho ya kuvuruga imani ya mwenzie.  “Kinachozungumzwa ndani ya ukumbi wa Bunge ni kizuri, lakini kinachotokea nje kinasababishwa na sisi wenyewe,” alisema.

Alisema amani ni kama uzi wa hariri, hivyo Watanzania wasiukate, ukikatika vinginevyo watashindwa kuunga.

Waziri Nchi Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika, alitaka polisi kuchapa kazi yao kwani hata nje ya nchi wanasifiwa. Alisema baadhi ya wanasiasa wanafanya kazi ya polisi kuwa ngumu.

“Kauli zetu wanasiasa tuchunge maslahi ya nchi hii, anayesema mtu huyu ni mhalifu tunamtia hatiani ni kazi ya mahakama,” alisisitiza.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Uratibu na Bunge), William Lukuvi, alisema Jeshi la Polisi litatimiza wajibu wake pamoja na kufanyakazi katika mazingira magumu.
Alisema ukiona mtu anaichukia polisi, lazima ujiulize ana nini.


CHANZO:NIPASHE